Sabrina
akaona Pendo ameingiwa hofu, asijue mama yake mkwe ndio zaidi. Akamfariji Pendo
bila hila. “Tutaomba dada. Usitie shaka. Bibilia inasema, ‘hakuna silaha itakayoinuka juu yetu ikafanikiwa!”
“Ndio maana nampenda Sabrina wangu. Sasa na wewe toka hapo ili ukanisimamie
harusi bwana!” Wote wakaanza kucheka upya.
“Naona
hatutoki hapa bwana! Kaka mwenyewe ana kazi ya kula tu hapa! Wala simuoni
mwenye tatizo la mapafu mimi! Akija mzee Msindai, naomba mama Msindai muwekee
msisitizo kesho tuondokeni hapa.” Wote wakacheka lakini si mama Msindai akawa
kama amepotea kabisa pale kimawazo. Kimya. “Hata mimi nishachoka dada. Namisi
vile vicheko vya wale kina dada, kesho lazima tutoke hapa.” “Na mabusu.”
Akaongeza mama K. “Maana na mimi mwenyewe nikipita kuwaangalia na bibi yao,
nagawiwa mabusu na kupigiwa makofi.” Akaongeza mama K. Wakacheka, hawana habari.
“Na Jack naye ana kazi ya kwenda kuyafuata, na kuja kuniringishia hapa. Mimi
naona nitoke tu hapa, nikalee wanangu wanne.” Wakacheka zaidi. “Unamaanisha wa
nne na Jack?” “Yeye ndio zaidi. Naona huyu Brayan atakuwa na nafuu kuliko hiyo
timu ya watu watatu!” Sabrina akawafanya waendelee kucheka lakini akaaanza
kugundua ukimya wa gafla wa mama Msindai, akashindwa kuelewa ila stori
zikaendelea.
Siku ya Kuruhusiwa
Hospitalini.
Jumatano.
K |
wa juhudi
alizozionyesha mama Msindai hapo hospitalini, kila mtu alijua Sabrina akitoka
hapo anakwenda nyumbani kwake. Alikuwepo hapo hospitalini na Sabrina bila
kuchoka wala hakuona aibu kana kwamba ndio mtoto wao wa kwanza. Alijaa hapo
akiongoza mambo, ilimradi kila mtu ajue yeye ndio muhusika. “Chumba
kilishaandaliwa kabisa. Eti baba! Msindai mwenyewe wewe! Ushaandaliwa mji
wako!” Sabrina akamwangalia Jack, Jack akatabasamu tu. Lakini Sabrina alijua ni
jambo analolihitaji sana Jack. Wawepo nyumbani kwao kwa muda huo. “Sasa
ugeni huu mbona anatajwa mtoto mmoja tu! Wale mabinti zangu je!?”
Akajiuliza Sabrina wakati akimtizama mama Msindai na mjukuu wake. Na alikuwa
akimvalisha nguo zake yeye tu. Kila kitu alichovaa huyo mjukuu, kilitoka kwa
bibi yake. Sabrina akatulia tu akijitizamia.
Tayari zilishapita siku tatu tokea
afanyiwe upasuaji. Na kwakuwa alijua Pendo naye anamsubiria, ikabidi kujikaza
kuweza kutembea vizuri. Walikuwa wakizunguka na Pendo muda wote kufanya mazoezi
ya kutembea huku wakizungumza mambo yao yasiyoisha. Walishajikuta wameshikana
haswa kana kwamba wapo rika moja na ni marafiki wa muda mrefu.
Siku hiyo ya nne mama Msindai akaweka
msisitizo kwa mumewe mpaka wakaruhusiwa. Sabrina kimya akitaka kujua
kitakachoendelea ila hakuwa na furaha kabisa kwenda kwa mama Msindai. Kwanza
alimuogopa sana huyo mama alimuona ni kama hajamfungulia moyo wake ila
kujitahidi tu tena mbele za watu si wanapokuwa peke yao. Na alishaonyesha wazi
mtoto aliyeandaliwa chumba ni huyo Brayan tu. Sabrina akabaki akiwaza wale
wazungu wake, na fujo zao huko ukweni!
Jena
alipoingia hapo wodini, chumba alichokuwepo amelazwa Sabrina, alisema anapita
tu siku hiyo hatakaa sana, yupo kazini. Alimkuta Pendo, mama Msindai, Sabrina
na mtoto. Kwa kuwa Jena na yeye ni daktari wa watoto, akataka kumtizama tena
mtoto kabla hajaondoka. “Namvua nguo zote. Ili kumtizama vizuri.” “Kama ndio
hivyo namuandalia maji kabisa ili nimuogeshe. Baba yake akimaliza kulipia,
tunaondoka tu.” Akajibu mama Msindai kwa shangwe zote. Sabrina akaona yeye na
Pendo wakatembee kupata mazoezi wakati wao wakiendelea na mtoto. Wakatoka hapo
na kuwaacha wao wawili na mtoto. Watu wote walijua Jena na mama yake wapo
karibu.
~~~~~~~~~~~~~~~~
“Mtakuwa
kwa mkweo kwa muda gani?” Pendo akauliza walipofika mbali kidogo. “Hata sijui
dada. Lakini namuona Jack amefurahi kweli! Sitaki kuanza kumuuliza maswali
yakuondoka wakati hata bado sijafika!” “Wewe usiwe na wasiwasi. Una Jacinta na
Junior upande wako, tena wote hao wanasikilizwa sana kwao, wa kali na
wanamsimamo, utakuwa sawa tu.” “Tatizo ni pale nitakapotakiwa kubaki na huyo
mama peke yetu, siku nzima! Hayupo hivyo unavyomuona hapo tukiwa tunabaki
wawili tu. Sina jinsi yakumuelezea, lakini moyo wake si mzuri kwangu.” “Jack si
yupo! Na mimi nitakuwa nikija kila siku asubuhi. Nalala hapo mpaka Willy akija
kunichukua jioni. Hamtakuwa peke yenu kwa muda mrefu.”
“Kweli dada?!” “Kabisa. Na hivi sina
tatizo lolote!” Wakacheka. “Kweli Mungu mkubwa Sabrina! Vimbe zimesalimu
amri!” “Wewe usifanye mchezo na Mungu anapotaka kujipatia utukufu! Mbona
anagawanya bahari mbele ya kila jicho ili wamjue kama yeye yupo! Sasa amefanya
njia humo tumboni ili mapacha wake wapite, watoke watu washuhudie ukuu
wake! Usifanye mchezo wewe!” Wakafurahia kwa pamoja, wakati wakizunguka
kwa mara ya mwisho wakati Jack
akimalizia kulipia hapo hospitalini. Wakazunguka kidogo, wakaamua kurudi.
Moyo Wa Mtu Msitu.
W |
alipokaribia
chumbani wakasikia wakicheka kwa sauti ya chini. “Mama!” “Hakika! Asiniletee
upuuzi mimi!” Jena akasikika tena akicheka kama asiyetaka kusikika. “Sasa
unawachukua na wale watoto wakizungu?” Wakasikia Jena akiuliza tena. Sabrina
akamfanyia ishara Pendo anyamaze wasikilize kwanza. “Yaani hapa nawapigia
mahesabu jinsi yakuwakwepa.” Sabrina alishituka nusura akae chini. Akasikia
maumivu makali yamepita chini kabisa ya tumbo. Akajishika.
“Wewe
niambie mwenyewe nawatolea maelezo gani wale watoto jumamosi jioni watu wakija
kwenye hiyo babyshower?!” Jena akacheka kishabiki. “Baba na mama weusi pamoja
na mtoto huyu mmoja, wakike wakizungu!” “Hebu niambie! Jack kaenda kulitafuta
balaa mpaka kalipata! Na nitalikomesha tu. Wewe subiri.” “Weza kukuta
yaliyompata Ngoi na yeye yamempata mama! Watu wanabisha tu.” Pendo akaumia
sana. Akamtizama Sabrina.
“Mbona
hilo nimelithibitisha Jena! Nimefikiria vile Ngoi alivyokuwa mbishi na msimamo
kwenye mambo yake, leo aje ayumbishwe tu na kasichana!” “Eti mama! Yaani mkewe
mwenyewe alikuwa akimshindwa, eti gafla Ngoi kawa mjinga kwa mapenzi!” “Sasa
mfikirie Jack na mzee Ngoi hali zao, niambie zinatofauti gani?” “Kweli hakuna
mama.” Jena akamuunga mkono mama yake. “Sasa na mimi nishaanza mikakati ya
kumtoa mwanangu. Wasinichezee akili! Jackson amekuwa kama mjinga jamani!
Sabrina! Sabrina! Ukimtizama huyo Sabrina hata mkononi hajai!” “Eti mama
jamani! Jack kakataa wanawake wazuri eti sababu yake! Hakika kuna jambo.” “Sasa
watanijua kama mimi ndiye niliyebeba miezi 9 au mganga wao. Nimeanza
taratibu tena na huyohuyo Junior wanayemuona Mungu mtu! Najua nikimuweka sawa
Junior mshauri wao, watafuata tu. Sasa subiri!” Mama Msindai akasikika kupania
kwa uchungu.
“Namuona!
Pendo amebadilika ameku..” “Subiri kwanza mama. Unakumbuka siku ile ya birthday
ya wale watoto wao wakizungu na kuchumbiwa tena kwa Pendo?” “Nakumbuka sana.”
“Eti Pendo anasema bila Sabrina asingeshika mimba!” “Nilimsikia na
wakakumbatiana!” “Mimi nikajiuliza, hivi huyu Pendo anasahau vipi shida
nilizopata naye kwa madaktari mpaka kuacha kazi zangu kuwa naye! Unakumbuka
mama mpaka ukaniambia niwe mwangalifu nisije nikashika la mimba ya mwenzangu tu
na kazi ikanishinda?” “Nakumbuka. Sasa leo eti ni Sabrina!” “Nakwambia huyu
msichana ana kitu, mama. Si bure. Sijui utafanyaje mama yangu!” “Nakwambia
nimeshaanza mikakati yangu. Wewe subiri tu.” Mama Msindai akasikika.
“Nasikia kichomi dada, acha
nikajipumzishe kidogo.” Pendo alibadilika mpaka rangi. Ndani wakanyamaza ghafla
walipomsikia Sabrina akilalamikia vichomi wasijue walikuwa hapo nje ya mlango
kwa muda wakutosha tu. Pendo na Sabrina wakaingia. “Vichomi tena! Au umetembea
sana! Pole.” Mama Msindai akamuwahi kwa upendo mara tu walipoingia, kama si
yeye. “Nahisi hivyo. Hata hivyo nahisi nimechafuka sana. Acha niingie bafuni
nijisafi kidogo. Dada Pendo nisindikize.” Wakapitiliza bafuni. “Pole Sabrina.
Pole sana mdogo wangu.” Pendo akanong’ona. Sabrina akabaki amesimama akiwaza.
“Badili basi.” Pendo akawa kama anamkumbusha kilichowaingiza hapo upande wa
bafuni. Sabrina akajisafisha na kubadili.
Majembe Yamegongana.
Wakati
wanataka kutoka chooni mara wakamsikia
Jack amerudi hapo chumbani. “Niambie muheshimiwa wa Bunge la Afrika
Mashariki! Mzee wa dola.” “Mshabiki wewe!” Akamsikia Jack akijibu hivyo na
kushituka sana. Sabrina akakunja uso na kumwangalia Pendo kama akimuuliza.
“Sijui Sabrina!” Sabrina akatoka.
“Tokea lini wewe Jack ni mbunge wa
Afrika Mashariki?” Sabrina akauliza taratibu tu akiwa anapanda kitandani.
“Kumbe upo! Nilijua bado mnatembea.” Jack akauliza akionekana kushituka kidogo.
“Mumeo yupo kwenye kinyang’anyiro cha ubunge wa Afrika ya Mashariki, usahili
ushakaribia. Na hivi alivyo maarufu sasa hivi, hata Junior anaamini atapata
tu.” Jena akadakia na kuongeza swali kwa Sabrina. “Kwani wewe hujui kama siku
zimeshafika!?” Sabrina akashangaa sana.
Akamwangalia
Jack. “Sina taarifa hizo! Sijui siku wala huo Ubunge!” “Mama wewe naona safari
hii umepitwa! Wenzio mpaka mavazi ya shughuli yakuapishwa akipata huo
ubunge, tunayo!” Jena akaongea kishabiki kama kumuumiza Sabrina. “Na kweli
naona nimepitwa! Mimi bado nipo na mambo ya Singida kumbe...” “Mambo
yanabadilika bwana! Tena nilimshauri Jack baada ya kuzungumza na wakubwa
wengi tu. Kwa kuwa ameshajitengenezea jina, kwa asilimia kubwa sana atapata.
Anazo sifa zote. Huko Singida ni kutuma tu lori na kuwachukulia mizigo yenu,
mrudi mjini. Kilichompeleka huko Jack kishakamilika. Inatosha.” Akaongea mama Msindai
macho kwa mjukuu wake akimuweka sawa ili amnyanyue hapo alipokuwa akimvalisha.
“Eti Pendo mwanangu, utakuwa ukiwaleta
wajukuu kila siku asubuhi pale kwangu ili wawe wanakuwa na kaka yao? Wakue
pamoja sio mbalimbali.” Sabrina akaumia kama Pendo. “Wala usiwe na wasiwasi.
Jackson huyu ndio atakuwa na hiyo kazi ya kukuletea huyu kaka kila utakapomuhitaji.”
Sabrina akajibu kwa haraka akiwa ameshakasirika. “Mbona sielewi!? Nani natakiwa
kumpeleka wapi!?” “Brayan kwa bibi yake.” Akajibu Sabrina huku akitoka tena
kitandani, akavaa viatu.
“Sijaelewa!” Jack akawa kweli
hajaelewa. “Sasa si Brayan atakuwa na bibi yake!?” Akadaki Jena kwa kuhamaki.
“Popote nilipo mimi, ndipo watakapokuwepo watoto wangu wote watatu,
bila kuachwa wala kufichwa hata mmoja wao, kwa kuwa wote watatu
ni watoto niliozaa mimi Sabrina. Ni wangu. Kwa hiyo wakati nikisubiria
harusi ya Pendo, nitakuwa na watoto wangu wote pale kwa Pendo,
kama mama alivyoshauri hapa, ili WAKUE pamoja. Mkimtaka Brayan, muda na
wakati wowote mtampata. Jack, tunaweza kuzungumza hapo nje kidogo?” Sabrina
akaanza kutoka.
“Jamani na mimi nitarudi baada ya muda
mfupi kidogo.” Pendo akatoka kwa haraka na kumpita hata Sabrina ambaye
alishaanza kuongoza njia. “Hakika haiwezekani! Nilivyojiandaa hivyo!” Mama Msindai
akasikika akiongea kwa mshangao mkubwa, Sabrina hakujibu. Akatoka. “Kwani kuna
nini!?” Jack akauliza. “Muulize huyo mkeo anayekuwa kigeugeu wakati
alishakubali na mama akaingia gharama kubwa za matayarisho. Jack akakunja uso
akatoka akiwa na mshangao usoni.
Hakumkuta Sabrina hapo nje, akajua
amekwenda upande mwingine. Akaongeza mwendo kumfuata. Akamkuta anaendelea
kwenda. “Vipi tena Brina!? Mbona sielewi?” Sabrina akaendelea kutembea bila
hata kugeuka nyuma mpaka alipojiridhisha amefika mbali kabisa, hakuna
atakayewasikia. Jack akamkimbilia.
SABRINA AWEKA MSIMAMO WAKE
KWA JACK.
“Nini kinaendelea?! Halafu mbona ni
kama upo na maumivu?” “Nimekuomba tuzungumze, lakini nikutaka unisikilize
Jackson.” Jack akatulia akimtizama maana kuitwa jina lake zima na Sabrina, si
alivyozoea. Akajua amekasirika. Alionekana amejawa hasira na maumivu.
“Uliponikuta Moshi kipindi kile, sikuwa pale kwa bahati mbaya. Tuliweka mipango
na Tino, tena mipango mizuri tu, yakueleweka. Katikati ya mipango yetu,
akatokea Max na mipango mingine kwa Tino. Tino alipopima, akaona ya Max ndio
inamanufaa kwake, akaamua kufutilia mbali mipango tuliyokuwa tumeweka pamoja.”
Jack Kimya.
“Hakuniacha tu. Lakini alihakikisha
ananiuzia mipango yake mipya na kutaka na mimi niendane nayo. Nikamwambia
haiwezi kuwa kwa haraka kiasi hicho, nahitaji muda wa kufikiria kama yeye ili
niweze kufikia maamuzi, kama yeye.” Sabrina alikuwa amejawa hasira Jack aliweza
kumuona jinsi anavyo tetemeka. “Nilipofikiria, sikuafikiana naye, ndipo
akaondoka na kuniacha pale uliponikuta, yeye akarudi huku Dar, akafanya
alichoona au alichoshauriwa ni chema kwake, na kweli akafanikiwa kukipata.”
“Kweli leo unanifananisha mimi na Tino kwa sababu ya Ubu..” “Tafadhali
nimekuomba kuzunngumza, usiniingilie Jackson. Mimi ndiye niliyekuita hapa.”
Jack akapoa.
“Ni nini nataka kukwambia juu ya
haya?” Sabrina akaendelea. “Kwa sababu yeyote ile utakayokuwa umekubaliana
na ushauri wa mama yako, juwa ni kati yenu nyinyi wawili, usifanye maamuzi
kwa familia nzima. Kama nilivyomwambia Tino, na kwambia na wewe pia.
Wewe ulishauriwa, ukapata muda wa kutafakari, ukakubali na kuchukua
hatua. Ni wewe. Mimi kama Sabrina, nikiwakilisha vichwa vya Jeiline, Keiline na
Brayan, peke yangu lakini nikisimama kwa niaba ya hao watu watatu.
Namaanisha ninapozungumza na wewe, nawakilisha hao watu watatu, hufanyi
maamuzi kwa niaba yetu.” Jack akashituka sana moyoni.
“Wewe unapofanya maamuzi, popote
ulipo, muda wowote, jua unafanya maamuzi kwa niaba yako wewe peke yako.
Ila mimi ninapofanya maamuzi, nafanya maamuzi kwa niaba ya watu wanne mpaka hao
watu watatu watakapofikisha umri wa kujitegemea! Kwa maana ambayo nataka uelewe
leo, jua hivi, endapo tunakaa mimi na wewe tukaamua jambo, hapo ujue ndipo tunapofanya
maamuzi ya familia nzima, si vinginevyo.” Ikabidi Jackson aweke mikono
mfukoni na kumtizama Sabrina vizuri.
“Sasa basi, wakati mama yako
anapokwenda kufuata mizigo Singida, hakikisha unamwambia achukue ya
kwako tu. Yangu na watoto wangu ibakie Singida, kwa kuwa mimi bado sijamalizana
na Singida.” “Mpaka lini?” “Mpaka MUNGU atakaponiambia vinginevyo.”
Sabrina akamjibu na kumtizama machoni. Wakatulia kidogo wakitizamana,
kisha Sabrina akaendelea.
“Uliponikuta Moshi, na si kwingineko,
ni kwa kuwa Mungu wangu alitaka niwepo pale. Huna utakaponipeleka hata kama ni
Ulaya, kama Mungu hayupo na mimi.” “Umekasirika tu Brina, kwa kuwa sikukwambia
maswala ya Ubunge wa Afrika Mashariki, lakini ulikuwa tayari kuhamia Dar! Na
sikukwambia kwa sababu...” “Nakwenda kuishi kwa Pendo. Nikisema
nakwenda, ninamaanisha kama nilivyokwambia, mimi na watoto wangu wote,
mpaka harusi ya Pendo itakavyoisha nitakuwa nikirejea Singida. Mkimtaka Brayan,
muda na wakati wowote mnaweza kumfuata. Kwa hiyo, kwa kuwa mama yako hajui jibu
la hapana, nashauri safari hii tafuta hekima ya kuzungumza naye. Ila naondoka
sasa hivi na PENDO.” “Mbona kama unazungumza kwa kufunga mjadala hunipi
hata nafasi ya mimi kutoa maamuzi yangu!? Wale watoto wote watatu ni wangu
pia!” “Tafadhali naomba usisahau jambo la msingi. Vitu vyangu na wanangu visiondolewe
Singida. Nisipovikuta Singida, nitajua natakiwa kuanza upya. SITASUBIRI.”
Sabrina akamalizia na kugeuka na kuanza kuondoka.
“Sabrina!?” Sabrina akamgeukia.
“Tafadhali usinifuate Jack. Niache kwa muda.” “Mpaka lini na kwa nini!? Mbona
kama unakuza mambo bila sababu!? Unakuwa kama mtu uliyekuwa ukinitafutia sababu
tu!” Sabrina akaondoka bila yakujibu. “Kuna dawa za kutuliza maumivu. Rudi
ndani unywe.” Sabrina hakugeuka kabisa, akaendelea kutembea kwenda upande
mwingine kabisa wa hiyo hospitali.
Pendo kwa
Willy.
Huku
kwa Pendo yeye alitoka hapo na kuanza kulia. Akalia Pendo kwa uchungu kisha
akampigia simu Willy ambaye alikuwa ofisini. Akalia hapo kwenye simu mwishoe
akamsimulia kila kitu Willy. “Haiwezekani Pendo! Jack amegairi
Ubunge wa Singida bila kuzungumza na mwezie wakati anajua mwezie alihangaika
sana!” “Kazi ya mama yake kama nilivyokwambia.” “Hapana Pendo. Hawa kina mama
tunawasingizia tu na kuwapa nafasi kubwa sana kwenye maisha yetu ambayo hata
Mungu aliamuru tuwaache, tukaungane na wake zetu. Sisi wenyewe tunatakiwa
kufikiria na kuondokana kwa wazazi kuwa mwili mmoja na wake zetu. Jackson
ataharibu nyumba yake vibaya sana. Anitizame mimi!” Pendo akamcheka
moyoni akajua yamempata, imekuwa fundisho.
“Ila nimeumia sana aisee!” “Juu ya Jena kukusimanga?”
Willy akauliza. “Vyote Willy! Nahisi pia wameamua
kumkataa kabisa Sabrina bila yakumpa nafasi jamani! Wanampangia mabaya bila
sababu! Na safari hii naona wamefanikiwa kwa Jack.” “Sawa. Sisi tutakuwa
watizamaji. Ila nakuomba Pendo utulie bwana. Sitaki mambo ya Pressure tena.”
“Acha nikamtafute Sabrina wangu, amesema ataondoka na mimi.” “Huogopi kugombana
na mama Msindai?” “Baada ya kumsikia leo kumbe walikuwa wakinisema na mwanae,
sijali tena Willy. Wanadamu hata ufanye nini huwezi kuwaridhisha, heri Sabrina
huwa anasimama na mimi.” “Ni kweli. Uwe mwangalifu mpenzi wangu.” “Sawa. Kazi
njema.” “Ukinihitaji tu, nipigie.” Pendo akacheka na kukata. Akaanza
kurudi wodini.
MAMA MKWE NA WIFI
VITA YAKISOMI.
P |
endo alifika
kwenye chumba alichokuwa amelazwa Sabrina akakuta tena wakimsema vibaya sana
Sabrina. “Najua hayanihusu, lakini mimi naomba nizungumze jamani.” Pendo
akaingilia maneno kati ya Jena na mama yake waliyokuwa wakimrushia Jack kama
kumsemelea Sabrina. “Sabrina si kigeugeu!” “Na wewe si utamtetea tu.” “Hapana Jena.
Wewe umebeba chuki na Sabrina na umeshindwa kumfungulia mlango moyoni mwako
ndio maana unamsema vibaya sana.” “Nimemsema nini na wewe kama sio unafiki tu?”
Jack kimya kama asiyeelewa tena.
“Mimi
niite vyovyote vile Jena, lakini Mungu wa Sabrina mnayekazana kumuita ni
mchawi, anawaweka kweupe! Ila naumia kuona ni kwa
nini anaruhusu kuwasikia jamani! Kila mkimsema vibaya, mwenyewe anawasikia.
Jamani acheni nyinyi! Mnamtafuta Mungu wa yule bint..” “Subiri kwanza
Pendo. Acha kulia tafadhali. Usije ukapandisha pressure, mumeo akatulaumu. Kuna
nini tena?” Jack akasimama. “Analia nini sasa na yeye kama si...” “Naomba
nyamaza Jena.” Jack akawa mkali. “Anataka kuzusha mambo ya ajabu hapa!”
“Unaniuma Jena wewe, basi tu! Kwa nini nyinyi mnashindwa kujifunza kwa
yaliyotupata mimi na Willy jamani!” “Ndio tunajifunza na kuchukua hatua.” Mama Msindai
akajibu kwa jazba. “Basi Sabrina amewasikia yote.” “Amesikia nini tena?” Jack
akauliza.
“Nakuonya
Pendo acha uchonganishi wewe mtoto! Kama yalishindikana kwako, uache kwetu.”
Mama Msindai akawa kama anamtisha asiseme. “Acha maneno ya uchonganishi na
uzushi kwenye familia zisizokuhusu. Angalia ya kwako ambayo hata hayajakaa
sawa, unarukia ya kina Msindai, utayaweza wapi!” “Sawa mama Msindai. Mimi nanyamaza ila ujue Sabrina
amewasikia na ndio maana amegairi kuja kwako wala si kigeugeu maana
alipanga sana kuja kuishi kwako bila shida.” “Juu ya nini?!” Jack akazidi
kuuliza. “Anaumia huyo mkeo kuona amepitwa kwa habari za Ubunge. Sisi wote
tunajua, yeye hajui ndio ametuziria! Yeye alitegemea...” Sabrina
akaingia. Wakanyamaza.
“Dada,
naomba twende nikapumzike.” “Na usisahau hata huyo Pendo ni sisi tumekutambulisha.”
Sabrina akamgeukia Jena. “Unasema nini Jena? Samahani sijakusikia.” “Nakwambia
hivyo unavyokataa kwenda kwa mama unakimbilia nyumbani kwa Pendo kana kwamba na
sisi Pendo hatuhusu!” Sabrina akabaki akimtizama na kukunja uso. “Sijaelewa.”
“Kwamba isingekuwa sisi, na huyo Pendo usingemfahamu.” “Ni kweli kabisa.”
Sabrina akajibu hivyo na kuendelea kufuata vitu vyake.
“Nisaidie
kubeba hili kapu dada. Mimi nitabeba mtoto.” “Tunaweza kuzungumza Sabrina?”
“Naomba isiwe sasa hivi tafadhali. Nina maumivu, naomba dada Pendo anipeleke
nyumbani kwa wanangu, nikapumzike.” “Ungekunywa dawa.” Sabrina hakumjibu Jack
akamsogelea mama Msindai. “Namuomba mtoto, mama.” Sabrina akaongea kwa upole
tu. “Hivi unajua nina uwezo wa kukukatalia huyu mtoto na kumwambia Pendo asikukaribishe
nyumbani kwake?” Mama Msindai akamuuliza kibabe. “Hapana. Sikuwa nikijua
hivyo.” Sabrina akamjibu taratibu tu. “Umeona dharau zake?” Pendo akatoka na
kapu bila kujibu lakini kama kumwambia mama Msindai yeye ameamua kumchukua
Sabrina hata akipinga.
“Jena,
naomba nyamaza tafadhali. Mwache Sabrina. Acha kujibishana naye na kumtupia
maneno.” Jack akaingilia. “Anadharau sasa hivi kwa sababu marafiki wa mama wote
amewageuza mioyo.” “Unaongea nini wewe!?” Jack akashangaa kidogo, kabla Jena
hajajibu akamgeukia Sabrina. “Tangulia kwenye gari nitakuletea mtoto.” Sabrina
akatoka kimyakimya. “Ni nini kiliendelea wakati mimi nilipotoka kwenda kulipia?
Wewe Jena umezungumza nini tena? Kwanza mimi nilijua tunafuata ushauri wa mama.
Mpaka nikichukua fomu na mambo yakikaa sawa ndipo tuwaambie watu ili kupunguza
ushindani au vikwazo. Tukishakuwa na chaguzi mbili ndipo kuwaambia watu! Sasa
mbona na wewe unazungumza hata kabla mambo yenyewe hayajawa tayari! Nini
kinaendelea tena?!” “Weee! Niache kabisa usiniingize kwenye mambo ya ajabu.
Mkeo mwenyewe kisirani kakasirika kupitwa kwenye hili. Anataka muendelee
kumficha mama mambo yenu, awe anajua yeye tu ili akutawale. Amekasirika
ndio maana anaonyesha jeuri yake waziwazi kwetu kwa sababu sasa hivi anafahamiana
na watu wakubwa! Hana shukurani hata kidogo. Mama amemuuguza hapa bila kuchoka,
yeye...” Sabrina alikuwa akisikiliza nje ya mlango. Akaona aondoke tu.
Asijiumize roho yake zaidi maana ni kama Jena alikuwa akificha ukweli kwa
kuongea maneno mengi kumchanganya Jack. Akamuacha Jack na ndugu zake.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Katikati Ya Furaha Ya Kupata Mtoto Mwingine tena
kwenye familia, Mtoto Anatolewa Hospitalini Akiwa Mzima, Mama Yake Akiwa Hai,
Hawana Tatizo Lolote, Mungu Mtenda Miujiza Ameshakamilisha Yake, Na Shetani
Naye Amepenyeza Agenda Yake.
Ni Nini Kitaendelea?
Kama Kwa Tino Tu Mizani Iliemea Kwa Max, Tena
Kirahisiii, Kwa Jack Na Mama Yake Kipenzi, Je?
Inaendelea….
0 Comments:
Post a Comment