Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 47. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 47.

Wakati wanaongea hao kina Msindai hapo, kina mama Sabina na Sabina wakisikiliza, Willy akimpapasa mkewe taratibu kama kumtuliza, Sabrina akatolewa chumba cha upasuaji akiwa na usingizi wa madawa. “Pole Sabrina.” “Pole mama.” “Mmemuona mtoto?” Sabrina akauliza akiwa anarudishwa chumbani. “Mwanao mzima. Ana nguvu.” “Anafanana na Jack?” Wakacheka. “Labda baadaye lakini sasa hivi amefanana sana na babu yake.” Akatulia, wakamuona anakunja uso. “Vipi? Ni maumivu?” Mama Msindai akauliza kwa upole. “Nasikia maumivu. Jack hajaja?” “Bado lakini yupo njiani.” “Wakamuona anajifuta machozi.” Wakaendelea kumfuata kwa nyuma. Wauguzi wakamuweka vizuri kitandani na kumchoma sindano ya maumivu ndipo wakawaruhusu waingie.

“Inabidi aachwe apumzike.” Nesi akashauri. “Naombeni kuzungumza na Jack. Atakuwa na wasiwasi sana.” Sabrina akaongea kwa upole. “Ni kweli. Pengine akikuona hivyo atatulia na yeye. Pole sana Sabrina.” “Asante shem. Nawashukuruni sana.” “Usijali, tupo pamoja.” Wakampigia video Jack. “Mkeo anataka kuzungumza na wewe.” “Ameshatoka!?” “Kila kitu kilienda sawa. Ila anatakiwa kupumzika. Mkizungumza tu, na sisi tutamuacha alale.” “Nawashukuruni sana kuwa naye.” Jack akasikika akianza kulia. Mama yake kimya. Jacinta akapokea simu. “Baba wewe mimi unanishangaza! Mwanao huku analia, na baba huko unalia!” Angalau wakacheka.    

“Mbwembwe zote zile za ubaba za asubuhi, zimekwisha kabisa!” “Nilitamani niwepo bwana!” “Sasa haupo sisi ndio tupo huku. Usiwe na wasiwasi bwana. Tunashukuru Mungu kaka amekuja salama, mzima, na mama yake huyu hapa nakupa, yupo salama. Mkeo amejikaza sana mpaka amekufikishia dume lako, umshukuru sana sio kuendeleza wasiwasi. Hapa ni furaha tu.” “Nashukuru.” Kidogo Jack akasikika ametilia.

Wakampa Sabrina simu. Jack akamuona mkewe. “Pole.” “Ni hongera bwana! Namshukuru Mungu kila kitu kilienda sawa. Ila sijamuona mtoto. Na wamesema sitamuona leo.” “Kwa nini tena!?” Jack akashituka sana. “Amewekwa kwenye mashine. Wanasema ni kwa uangalizi tusiwe na wasiwasi.” Jack akanyamaza. “Usiwe na wasiwasi Jack, baba yuko naye huko. Na hata ungekuwepo wasingekuruhusu kwa sasa kwa kuwa ndio kama wanaanza matibabu yake. Hata kunyonyesha nimewaulizia hawa waliokuwa wananihudumia hapa baada ya upasuaji, wamesema siwezi kumnyonyesha sasa hivi mpaka baada ya masaa 48.”  Sabrina ndio akawa sasa faraja kwa mumewe kila mtu akisikiliza, hayo hata wao walikuwa hawajui.

“Kwa nini tena jamani!” Jack akaendelea kulalamika. Wote wakamgeukia mama Msindai. “Sasa nini? Lazima awe na wasiwasi.” Mama yake akamtetea Jackson. Wote wakacheka kwa masikitiko. Na Sabrina akacheka na kushika tumbo. “Acha bwana wasiwasi Jack. Wanasema ni kwa ajili yakutochosha mapafu yake. Wanataka atulie kabisa. Mengine utamuuliza daktari mwenyewe ukija.” “Afadhali.” Wote wakaitika kwa pamoja na kucheka. Jena akachukua simu na kumueleza jinsi inavyokuwa kwa mtoto anayezaliwa na fetal distress. Angalau wote sasa wakaelewa. “Kwa hiyo ni utaratibu mzuri kwa ajili ya mtoto lakini sio kwamba yupo kwenye hatari.” Jena akamalizia. “Hapo sawa sasa.” “Nakurudisha kwa mkeo.” Akampa simu Sabrina. “Nasinzia Jack.” “Basi pumzika. Nitakuona karibuni. Pole.” “Asante. Lakini usiwe na wasiwasi kila kitu kipo sawa.” “Umewasiliana na mama huko nyumbani na watoto?” “Mama yuko hapa.” Sabrina akajibu taratibu akiwa anasinzia. “Tena! Sasa watoto wangu wameachwa na nani!?” “Naomba utulie Jack. Nakupa mama akwambie habari zao. Wazima, hawana tatizo. Na amewaacha wamelala.” Sabrina akampa simu mama yake.

“Samahani mama yangu, sikujua kama wameachwa peke yao.” “Hawapo peke yao baba.” Mama Sabrina akajibu akicheka. “Huna utakachomwambia huyo sasa hivi mkaelewana.” Sabrina akaongea taratibu. Wakacheka. “Lakini naona kama kuachwa na mtu baki asiyewawezea, watateseka sana!” Jack akaendelea kulalamika. “Watoto wenu wanashida na wanakataa watu nyinyi wenyewe mkiwepo. Lakini wale watoto wanamkubali kila mtu. Mchana Sifa alinisaidia kuwaogesha baada ya kula ugali wakawa wanambusu tu na kumpigia makofi.” “Ndio kazi yao hiyo. Hawana jingine wawezalo na cheko lao.” Sabrina akaongeza akiwa amefunga macho. Wakacheka.

“Hawana shida kabisa. Bora washibe na wawe wasafi. Usiwe na wasiwasi baba. Na nimewaachia chakula chakutosha, wala hawatapata shida.” Mama Sabina akaendelea kumtuliza. “Nimemtuma na mama awapitie pale kuwaangalia kabla hajaja hapa. Usiwe na wasiwasi Jack.” Pendo akaongeza. “Nashukuruni sana. Labda tu na kupiga simu sasa hivi kujua wanaendeleaje! Inawezekana walionekana sawa kwa kuwa walikuwa na wewe mama ambaye wanakufahamu. Sasa wakija kuamka wajikute na watu wote wageni! Watakuwa, watashituka sana na..” Wote wakacheka.

“Niliwaambia mimi. Jack hawezi kuridhika hata mumwambie nini! Ni mpaka yeye mwenyewe awepo hapa. Naomba mumtumie tu namba ya simu ya Sifa tafadhali. Ili apige na kuwaona sura zao, hapo ndipo atatulia. Lasivyo hakuna lugha mtamwambia mkaelewana.” “Naona kweli.” Jacinta akaongeza. “Nakutumia Jack. Ila nilimwambia Sifa hata wakianza kulia tu, anipigie. Na mimi narudi huko sasa hivi kwenda kumtengenezea Sabrina supu. Nikifika pia nitakupigia mzungumze.” “Nakushukuru Pendo. Asante sana.” Wakaagana, pakatulia.

~~~~~~~~~~~~~~~~

J

ackson mpaka anafika Arusha, ilishakuwa usiku, akakosa nafasi ya ndege. Sabrina anaamka jioni walipomletea supu, swali la kwanza baada ya uchovu na madawa ya usingizi sasa kuisha akafungua macho kuangaza, Jackson mumewe hayupo, kila mtu yupo. “Jack yuko wapi?” Wakaangaliana. Jacinta ambaye yuko karibu nao hao wawili kwa upande wa Msindai akasogea hapo kitandani. “Jack amekosa ndege leo anakuja na ndege ya kwanza kesho asubuhi.” Hapo hapo Sabrina akajifunika. Hakujua hasira ilipotokea, akaanza kulia hapo wakwe zake wakimtizama. Alilia Sabrina kama aliyefiwa. “Labda mumpigie Jack azungumze naye.” Sabrina akapandisha mabega kukataa. Akaendelea kulia.

“Mimi naona nitoke hapa, niende nikamuulize dokta hukusu huku kuvimba kwake.” Wote wakamgeukia Jena kwa mshangao. “Kwani ilikuwa lazima utangaze mpaka umtie hofu!?” Mama Msindai akamuuliza binti yake huyo daktari kwa mshangao sana. Sabrina akajifunua kutoka kwenye shuka, akajiangalia vizuri mikono. Kweli alikuwa amevimba, akazidi kulia. “Nitakufa hata sijamuona Jack, jamani!” Kilio kikaongezeka. “Umefurahi sasa?” Mama Msindai akamuuliza tena Jena kwa hasira. “Jamani mama! Mimi nilitaka kusaidia tu.” “Sasa mbona bado umesimama hapo?” Mama Msindai akamuuliza kwa ukali zaidi, Jena akaona atoke bila kuongeza neno.

“Mama!” Mzee Msindai akamsogelea Sabrina. “Usilie kabisa, wala hutakufa kwa hili. Ni kawaida ya hayo madawa waliyokupa huko chumba cha upasuaji. Wengine inakuwa hivyo. Mwili wako utarudi kama kawaida. Wamekuwekea maji hayo yanasafisha mwili wako kutoa sumu yote. Usiogope.” Mzee Msindai akaongea kumtuliza Sabrina aliyekuwa akilia huko ndani ya shuka. “Hata mimi ilinitokea nilipojifungua Cleo, Sabrina. Usiogope huwa inatokea. Junior si unakumbuka?” “Nakumbuka. Na labda kumuhakikishia Sabrina, mumewe atakuwa amefika hapa kwenye mida ya saa nne asubuhi. Una maumivu yeyote?” Sabrina akaendelea kulia.

“Mtoto sijamuona! Jack mwenyewe simuoni, nimebakiwa na maumivu tu.” “Umetoka kufanyiwa upasuaji leo mama. Ukiendelea hivyo vizuri, kesho wakatoa hiyo catherter ukiweza kutembea, utakwenda kumuona mtoto wako. Wamempa maziwa, ametulia kabisa hana shida.” Hapo Sabrina akajifuta machozi. “Sasa wanampa maziwa gani?” Wakacheka kidogo. “Hivi sivyo tulivyopanga na Jack jamani!” “Kwani nyinyi mlipanga nini?” Ikabidi aulizwe. “Tulipanga tuwe wote wakati najifungua halafu tukate keki siku hiyo hiyo!” Wote wakaelewa sasa. “Yaani tulipanga kuwe mpaka na mchukua video ili kupata ukumbusho wa Brayan. Mimi ndio nilitaka niwe mtu wa kwanza kumnyonyesha Brayan sio maziwa ya kina mama ng’ombe! Ona sasa hivi tulivyvosambaratika! Mipango yote imebadilika! Angalau hata Jack angekuwepo!” Sabrina akaendelea kulalamika huku akilia.

“Pole sana Sabrina. Lakini katika yote, naomba tumshukuru Mungu. Mpo mbali mbali lakini wote mpo salama. Willy amechukua video ya kila kitu tokea Brayan anatoka chumba cha upasuliwaji.” “Nilianzia wakati yeye mwenyewe anapelekwa.” Willy akaongeza. “Umeona sasa. Wewe ulipotoka. Na sasa hivi pia kabla hatujaja hapa tulikwenda kumuona Brayan. Tumeshindwa tu kumshika, kwa kuwa hatukuruhusiwa. Lakini amemchukua video vizuri, mwanao amelala, safi. Ukiacha kulia tutakuonyesha.” “Na bado hakuna kilichoharibika. Akitolewa kwenye hiyo mashine, tutakata keki hapahapa baba yake, na dada zake wakiwepo. Wapige makofi mpaka wachoke.” Mama Msindai akaongeza kwa Pendo, angalau Sabrina akatabasamu. Wengine wakacheka.

“Naomba mnisamehe jamani! Nashukuru kwa kuwa hapa, lakini nilitegemea Jack angekuwa ameshafika. Natamani angekuwepo hapa.” Sabrina akaongea kwa upole na kujifuta machozi. “Ni sawa kabisa Sabrina na ni haki yako mumeo kuwepo hapa. Hata yeye anatamani angekuwepo hapa. Lakini imetokea gafla, ni mipango ya Mungu. Na uzuri Mungu amekusaidia wewe na mtoto, mengine yaendelee hivyo hivyo taratibu.” “Halafu mipango yetu si ya Mungu, Sabrina. Pole.” Sabina akaongeza.

“Mama naye yuko wapi?” Wote wakacheka. “Mumeo ameomba kwa kubembeleza arudi nyumbani, akakae na watoto. Naona haamini yeyote na wale wanae.” “Mmh! Yaani Jack jamani! Naomba tu umsamehe da Pendo. Na ubaya wa Jack hajuagi kunyamazia jambo.” Wote wakacheka. “Na alikazana huko nyumbani, mpaka ikabidi nimuombe Willy aje amchukue hapa mama.” “Jamani Jack! Kwamba na wewe ulikuwepo pia pale nyumbani?” Sabrina akauliza kwa kushangaa. “Si tuliondoka hapa karibu wote kasoro mama yako na mama Msindai. Ili upumzike. Wengine wakarudi makazini, mimi nikarudi nyumbani kukupikia. Mumeo akaanza. Mbona hawaamki? Nikamwambia bibi yao amesema huwa wakila ugali huwa wanalala sana. Akataka awaangalie hivyo walivyolala.” Watu wakazidi kucheka.

“Nikaenda na simu mpaka chumbani, ikaanza sasa kazi ya kuwapanga. Mara aseme Jeiline awekwe hivi, mdogo wake vile.” Sabrina akaanza kucheka. “Ndivyo alivyo Jack kama hajalaza yeye watoto! Pole dada.” “Sasa kwani hao watoto huwa hawageuki!?” Mama Msindai akauliza. “Wewe mama hutamuweza Jack.” Sabrina akamalizia. Pendo akaendelea. “Mimi sikubisha kwani ulishaniambia habari za Jack za kuamka usiku pia kupanga watoto chumbani kwao.” Wakacheka. “Na nyumbani pia!?” “Hivyo hivyo. Kila siku usiku lazima aamke akawaangalie. Sasa mimi huwa namwambia wakiamka, asirudi nao pale chumbani maana huwa wakimuona tu, wanachangamka. Wanataka waanze kucheza, wakati mimi mwenzie nimeshinda nao siku nzima nataka kumpumzika. Kwa hiyo namwambia awaache, na kama anaona hawezi akiwaamsha akae nao huko huko. Lakini kwani utalala! Kunakuwa kama ndio kumekuchwa.” “Na hapo ndio ikawa hiyo kazi.” Pendo akaendelea.

“Mara ya kwanza akaridhika. Tukaagana. Niko katikati yakupika, akapiga tena anaomba nikawatizame tena. Nikakuta watoto wapo vilevile wamelala. Nikajua hajaridhika. Ila nikaona nimwache nipike. Akapiga mara ya tatu anawaulizia kama hawajaamka pengine wamepatwa na tatizo. Nikamwambia naenda kuamsha wanae ili wote tutulie.” Wote wakacheka. “Na yeye akacheka lakini akakubali niwaamshe. Sifa akabeba mmoja mmoja mpaka sebuleni. Akaanza tena, hawajachangamka!” “Jamani! Watoto waliotoka kulala!” Sabina akashangaa. “Wewe hujamjua Jack. Anaweza akakupigia simu mchana, yeye yupo kazini, labda ndio umejipumzisha tu, anakupigia umelala mchana, anakuamsha ukaangalie watoto wanaocheza. Na yeye awaone.” “Basi kazi ipo, wanakuwa watatu!” “Mbona yeye ndio watatu, wanne ndio Brayan.” Sabrina akaongeza wote wakamwangalia mama Msindai. Akacheka.

“Sasa ndio kazi yakumtaka bibi yao ikaanza. Akaanza fujo sasa. Mwenzie napika, yeye analalamika. Eti watoto wake huwa hawazubai muda mrefu hivyo, lazima wameingiwa na hofu. Kwa muda huo wangekuwa wameshanifuata pale jikoni, wamechangamka. Ule sio uzubaifu wao.” Kila mtu alikuwa akicheka wakati Pendo akisimulia. “Kila nililokuwa nikimwambia anajibu lake. Akaona simuelewi, akaenda moja kwa moja kwenye shida yake. Yeye anataka bibi yao ndio awe nao pale.” Kila mtu akacheka. “Namwambia yupo na Sabrina kule hospitalini, anasema yeye anamjua mkewe, atakuwa sawa tu na sisi, ila wanae watateseka ugenini. Anaomba bibi yao arudi hapo. Nikamwambia namtuma Willy atoke ofisini amfuate bibi yao hapa, amrudishe nyumbani ili watu wote tutulie.” “Hapa napo alishampigia simu bibi yao akajieleza weee. Mimi nikamnong’oneza hapa huyo bibi yao, nikamwambia maneno hayo yooote juu ya wanae, anamtaka arudi tu nyumbani, yeye ndio awe nao.” Mama Msindai akafanya wote wacheke zaidi. Angalau stori zikaendelea, Sabrina akatulia.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Asubuhi na mapema Sabrina akatolewa kila kitu na kuambiwa anaweza hata kutembea kidogo. Mama Msindai alirudi kulala naye. Ndugu walipopita asubuhi wakiwa wanawahi makazini, wakamkuta mama Msindai anampeleka chooni. “Anatembea!” “Naona mwenyewe ametaka aanze kutembea ili akamuone mtoto wake.” Mama Msindai akajibu. “Vipi maumivu?” “Naona ni kawaida yale ya kufanyiwa upasuaji. Yapo lakini sio sana.” Wakasalimia wote asubuhi hiyo kila mtu akawahi majukumu yake. Akabakiwa na mama Msindai tena peke yao. “Nipeleke nikamuone mwanangu mama.” “Wewe Sabrina! Sio tungojee kidogo!” “Nitafika mama. Sijui mwanangu hata anafananaje jamani! Wanampa vitu ambavyo hata sivijui! Baba yake hayupo na mimi pia nishindwe kwenda kumuona! Acha niende mama.” “Basi usilie. Twende taratibu tu, naamini tutafika. Na mumeo ameshaondoka Arusha, anakuja. Mtakuwa pamoja hivi karibu. Na Msindai atakuja tena baadaye atupe picha kamili ya Brayan.” “Nashukuru mama. Asante.” Wakaanza safari ya kumfuata mtoto.

Wakatembea mpaka alipokuwa amewekwa huyo mtoto na vitoto vingine. Sabrina akafurahi sana kumuona mwanae. “Brayan amezaliwa mkubwa kuliko dada zake! Niombee nimshike kidogo mama.” Mama Msindai akacheka. Akazungumza na wale manesi, wakamfunika vizuri mtoto na Sabrina mwenyewe, akamshika Sabrina akafurahi sana, akatafuta mahali akakaa. Akamshukuru sana Mungu wake huku amemshika. Mama Msindai kimya akimtizama. Akambusu wee, na kumfunua kidogo. “Kweli anafanana na babu yake!” Wakacheka. “Msindai amefurahi huyo. Namwambia watoto wanabadilika aache kuniringishia, ananiambia lakini kwa sasa amemfanana sana.” Wakacheka. “Amekuja kukaa naye hapa usiku akimwangalia, mpaka tukamwambia akapumzike, sisi tutakuwa naye.” Muuguzi mmoja akaongeza, wakacheka.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Ilipofika kwenye majira ya saa tano na nusu asubuhi, Jack na dada yake Jacinta wakaingia hapo hospitalini. Sabrina hakujua kama ni furaha au uchungu, akaanza kulia tena. Akalia hapo mumewe akiwa amemkumbatia mpaka akatulia. “Mbona umevimba sasa?” “Wamesema nitakuwa sawa tu. Nimefurahi Jack! Pole.” “Pole na wewe. Nilikuwa nakuhurumia upo peke yako!” “We Jack?” Mama yake akamuita kwa ukali, akihamaki. Wakacheka. “Kwani sisi sio watu hapa?” Akauliza mama Msindai. “Mwenzio kalala uwanja wa ndege huyo.” Jacinta akaongeza. “Jack!” “Sikutaka niende hotelini, halafu nipitiwe na usingizi, niachwe na ndege ya asubuhi!” “Pole. Ila nimefurahi!” Wakacheka na Jack akambusu mkewe. “Hongera Brina. Ila kwa jinsi baba alivyonionyesha picha zake Brayan, heri ulimzaa kwa upasuaji! Mkubwa sana.” Wakacheka kwa furaha. “Twende wote tukamwangalie.” “Nashauri uoge kwanza Jack. Umekuwa na safari ndefu, na mtoto bado yupo kwenye uangalizi.” Mama yake akamuwahi. “Kweli.” Jack akakimbilia hapo bafuni kuoga ili kwenda kumwangalia mtoto wao.

Atafutaye Hachoki,

Jumanne!

K

atika hekaheka hizo za hospitalini, maandalizi ya harusi yao, Pendo na William kama marafiki wa karibu wa Sabrina na Jack, hawakuwa wakikosa hospitalini pia. Siku ya tatu ambayo mtoto alionyesha nafuu kubwa na ahadi ya kutolewa siku inayofuata, endapo mambo yasipobadilika kwa mtoto, kwani alishaweza kunyonya bila shida. Willy na wengine wakiwa ndani ya hicho chumba stori na vicheko vimekolea mida hiyo ya jioni wafanyakazi wakiwa wametoka kazini na kujikuta wote hapo hospitalini kumuona Sabrina na mtoto, mzee Ngoi akampigia simu Willy. Willy akakunja uso na kumtizama Pendo. “Nani?” “Mzee Ngoi huyu! Sijui anataka nini kwangu!?” Willy akaongea akiitizama simu yake kama aikate tu.

          “Msikilize.” Pendo akashauri kwa utulivu. Willy akamtizama na kupokea. “Shikamoo.” “Marahaba Willy. Hujambo?” Mpaka Willy akashangaa. “Kuna nini baba!? Maana hapa nipo hospitalini.” “Ni salamu tu na kukutaka wewe na Pendo mfike nyumbani kuna habari njema.” “Kama nilivyokwambia, nipo na mgonjwa na maandalizi ya harusi yangu. Tafadhali niambie tu.” “Nani tena mgonjwa?” Mzee Ngoi akauliza swali lililomshangaza zaidi Willy. “Ni nini kinaendelea baba?!” “Nataka kujua tu! Kwani kuna ubaya gani?” “Kwani wewe unamfahamu rafiki yangu yupi? Kwa nini usiniambie ulichonipigia?” Pendo akamshika kidogo kama kutaka kumtuliza. “Mimi sielewi!” Willy akamlalamikia Pendo, simu sikioni. “Taratibu.” Pendo akamsihi.

          “Ni habari njema tu. Si kutaka kukuudhi. Najua hatukuwa kwenye mahusiano mazuri, lakini naona mama yenu mdogo anaona ni vizuri tuwe na mahusiano kama familia.” “Subiri kwanza baba. ‘Mama yetu mdogo’ ndio nani!?” Hilo swali la Willy likavuta masikio ya watu wote pale chumbani ila akasikika mzee Ngoi akicheka kidogo. “Ndio habari njema nilitaka ukija hapa na wenzio niwaambie. Ila kwa kuwa upo na mgonjwa na mambo hayo ya harusi kama alivyoniambia mchungaji, acha tu nikwambie.” Willy kimya akisikiliza.

          “Nimeamua kutekeleza ushauri wa mama yenu. Alinipa baraka zote kumuoa Zelda, naona nitekeleze.” Willy alishituka nusura kuangusha simu. “Subiri kwanza baba.” Ikabidi Willy atoke nje maana alivuta masikio ya wote mle ndani, akahisi atawasumbua. “Ni jambo alilolitaka mama yenu, ila Chonge naona aliniyumbisha kidogo kwa ushirikina. Naona yamemrudia yeye mwenyewe, amegeuka mwendawazimu kabisa yule wakuvua nguo mbele za watu.” “Mungu wangu!” Willy akashituka sana. “Kabisa. Huwezi kucheza na mipango ya Mungu. Yule msichana alitaka nitelekeze damu yangu, ili niwe naye! Mabaya yote aliyomfanyia mama yenu mdogo, yamemrud...” “Tafadhali mwite Zelda tu.” Willy akamkatisha akiwa amejawa mshituko, hasira na hofu.

          “Sasa tulirudi kwa mchungaji kumuomba atufungishe ndoa kwa  haraka hata kabla yenu ili unapoa uwe na wazazi wote.” “Zelda sio mama yangu na hatakaa akawa mama yangu. Kwanza sitaki mtu yeyote yule kwenye harusi yangu. Mnataka...” Willy alikuwa akiongea kwa sauti ya juu akigomba mpaka ndani wanasikia. “Samahanini jamani. Acha nikamtulize.” Pendo akasimama na tumbo lake akatoka taratibu akijivuta. “Naiomba hiyo simu Willy.” Wakamsikia Pendo na sauti yake ya chini na ya taratibu. “Nakaribia kuitupa mimi!” “Sasa kabla hujaitupa, naiomba mimi.” Akamkabidhi Pendo kwa hasira.

          “Hellow.” Wakamsikia Pendo. “Ni mimi Pendo. Naomba Willy akupigie baadaye tukitoka hospitalini.” “Kumbe na wewe upo? Tena Zelda anakushukuru sana kwa kumsaidia kipindi akiwa kwenye shida. Ameomba usikose kwenye harusi.” “Naomba tuzungumze baadaye, tafadhali.” Wakamsikia Pendo ametulia. Wakajua anasikiliza. “Siwezi kuahidi kwa kuwa sijui itakuwa lini na mimi najiandaa...” “Naomba mumuache Pendo, tafadhali.” Willy akagomba kwa sauti ya juu na kuchukua simu kutoka kwa Pendo.

          “Ni nini jamani!? Kwa nini mnalazimishia?” “Sitaki mpitwe na kitu cha muhimu kama hiki na itakuwa kumuenzi mama yenu.” Willy akafunga macho. “Sasa kwa kuwa kanisani wanaka kutangaza kwanza, tumeona tukafungie tu mahakamani siku ya ijumaa kisha tutakwenda kubariki kanisani wakiwa tayari na sisi.” “Haraka ya nini jamani!? Mnaharaka gani nyinyi mnaoshindwa kusubiri kanisani?” Willy akauliza. “Hatutaki kuendelea kuishi dhambini.” “Kwamba Zelda amesharudi hapo nyumbani!?” “Kabisa, pamoja na mdogo wenu.” “Hakika natupa hii simu.” “Nipe mimi Willy.” Pendo akasikika tena.

          Willy akampa na kuondoka kabisa pale. “Ni mimi Pendo, tena. Tunashukuru kwa mwaliko.” “Ni ijumaa ya kabla ya harusi yenu hiyo jumamosi.” Akaongeza mzee Ngoi na kuendelea. “Ndio maana tuliona mfike leo jumanne, tupate upatanisho kwa familia nzima, ndipo tuanze upya. Hatukuachana vizuri. Hawa ni ndugu, damu moja. Hakuna jinsi mdogo wao akakua bila ndugu zake.” “Nashukuru sana. Asante kwa mualiko. Willy atakupigia baadaye. Lakini kwa binafsi yangu sitaweza. Kama ulivyosikia harusi yetu ni siku ya jumamosi, yaani siku inayofuata baada ya harusi yenu.” “Na Zelda ameshauri tufanye harusi yetu siku hiyo makusudi kabla yenu ili siku ya harusi yenu kuwepo na wazazi wakueleweka. Hatutachukua michango. Nitagharamia harusi yetu, mimi mwenyewe.” Pendo akachoka kabisa baada ya kusikia mzee Ngoi akizungumza hivyo.

“Lakini mimi nimeshauriwa na daktari nipumzike. Sitaweza shughuli mfululizo. Harusi yenu na yangu! Sitaweza kwa kweli. Ingekuwa siku zimepishana, angalau kwa juma moja hapo ingekuwa afadhali ningeweza kuhudhuria harusi yenu. Lakini hivyo sitaweza. Naomba niwatakie maandalizi mema, mfanikiwe.” “Nashukuru sana Pendo na umetoa sababu ya msingi sana. Inaeleweka kabisa.” Pendo akakata  na kubaki ameduaa.

~~~~~~~~~~~~~~~~

“Haya njoo Pendo utujuze ya ukweni.” “Nancy! Acha bwana. Unataka kumliza bure.” Baba yake akamuwahi. “Hawezi. Eti Pendo, mdogo wangu? Maana tumesikia kila kitu ila si kwa undani.” Wote wakaanza kucheka. Pendo akaingia akicheka taratibu. “Jack naomba kanitafutie Willy wangu. Asije akaenda kujirusha baharini bure!” Jack akacheka na kutoka. “Haya! Nimesikia umepata mama mkwe mwingine!?” Wote wakacheka. “Nancy umekazana!” “Dada Jacinta kila familia ina vijimambo, lakini ya Ngoi ni kiboko! Hutakaa ukaipatia mwenzie. Tangia Pendo ameolewa huko, tunajionea mambo. Inageuka aina ya viroja kila kukicha! Si misibani si kwenye masherehe, lazima washangaze uma.” Nancy akaongeza na kufanya wacheke tena.

          “Pendo mdogo wangu?” Nancy akaendelea kusihi akitaka kujua zaidi, watu wakacheka vile anavyobembeleza. Pendo akacheka kidogo kama anayefikiria. “Ila kwa nilivyomsikia mzee Ngoi! Mmmh!” “Nini?” “Hayupo sawa bwana. Amekuwa kama sio yule Ngoi mkorofi! Sijawahi muona Ngoi huyu! Mnyenyekevu na mvumilivu mpaka akamaliza ujumbe wake kama aliyesimamiwa lazima aseme! Sasa najiuliza, Ngoi ni wakulazimishwa kusema jambo kweli!” “Mkewe mwenyewe alikuwa anamshindwa!” “Sawasawa Nancy. Huyu baba ameshindikana kila mahali! Mchungaji mwenyewe alituambia walimnyanyulia mikono hata pale kanisani! Walimshindwa yule! Halafu alimfukuza vibaya sana Zelda. Ghafla Zelda amerudi na ndoa juu! Tena ya haraka hivyo, na mwenzie aliyekuwa aolewe na Ngoi kawa kichaa jamani!” “Haaa!”  Hapo kila mmoja akahamaki nakutaka kujua zaidi.

          “Kweli! Yaani Chonge alifanikiwa kuteka moyo wa Ngoi mpaka kumfukuza Zelda na mtoto kabisa!” “Kisa nini?” “Mmmh! Yaani mama Msindai, ndio utachoka kabisa. Mambo ya ushirikina.” Pendo akawasilimulia kwa ufupi, wote wakajua lipo jambo kwa hakika. “Basi safari hii uchawi umempata. Atulie na yeye yule mzee! Khaa!” “Nashauri Nancy na wewe utulie.” Wote wakacheka. “Sawa baba. Maana ni baba yake mkwe Pendo?” Nancy akamuuliza baba yake kishabiki. “Wameambiwa na mama mdogo anakuja.” Wote wakacheka. “Mama K na wewe kumbe umo! Umetulia hapo kimya kumbe unasikiliza! Haya baba, mama naye kasikia.” Nancy akafanya wazidi kucheka lakini kumbe wameamsha wasiwasi na hofu kubwa kwa mama Msindai, wasijue.

“Ila naona Willy hataki tena!” Nancy akaongeza, Pendo akacheka mpaka machozi. Wote wakaanza kucheka tena kwa sauti ya kimyakimya ili Willy mwenyewe asije kuwasikia. “Nancy mshabiki wewe! Mwache mpenzi wangu!” Pendo akaendelea kucheka. “Sasa wewe nawe umkazanie maombi. Maana hao watu wanaonekana sio wazuri. Umesikia Pendo?” “Kweli mama!” “Haya! Wewe cheka tu. Kama wamemuweza Ngoi, ujue...” “Bwana mama!” “Mimi nakutahadharisha. Vita imeanza.”

~~~~~~~~~~~~~~~~

  • v     Zelda Amerudi Enzini, Akitaka Undugu Na Watoto Wa Ngoi. Nani Atakuwa Upande Wake Nani Atakua Kinyume Naye? Na Je, Atakayekuwa Kinyume Naye Kama Chonge, Ambaye Amegeuka Mwendawizimu, Kitampata Kipi? Nini Kilitokea Na Nini Kitaendelea Kwa Familia Hiyo Ya Ngoi Iliyoachwa Na Mama Ngoi Mikononi Mwa Zelda?
  • v Kile Alichodhania Amefanyiwa Mwanae, Jack, Wanakithibitisha Kwa Mzee Ngoi Na Kuinua Wasiwasi Mkubwa Na Hofu Kwa Mama Msindai. Nini Kitatokea Katikati Ya Furaha Kubwa Hivyo?

v  Bado Shetani Yupo Kazini.

o   Usikose Muendelezo….

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment