Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 46. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 46.

 

Kitu cha kwanza akachukuliwa vipimo vya mapigo ya moyo, pressure ikaonekana ipo juu sana. Sabrina akapewa huduma ya kwanza hapo hapo na kupandishwa kwenye gari kuwahishwa hospitalini ili kumsaidia yeye kwanza na mtoto asidhurike. Tena akiwa hakuwa mgonjwa wala hakuwa na tatizo lolote ila pressure ilikuwa juu kidogo tu, daktari akamwambia asiwe na wasiwasi, ni kawaida tu kwa kuwa ni mjamzito, sasahivi imekwenda juu mpaka kumuweka hatarini!

Jack alikuwa na wasiwasi, hakutaka baba yake akate simu. “Nitakutaarifu tukifika hospitalini Jackson. Lakini usiwe na wasiwasi, wataweza kuishusha tu.” “Tafadhali usikate simu baba.” “Sasa nitawasiliana vipi na madaktari wengine ili kumsaidia mkeo, Jackson?” “Weka comference call.” Baba yake akajua amepaniki. “Nisikilize Jackson. Haitasaidia ila utaongeza hali ya wasiwasi hapa. Madaktari wote wataongea lugha za kidaktari hata ukiwa kwenye simu hutaelewa. Naomba utulie, tutakuta...” Mzee Msindai akaona simu imekatwa. Kabla hajamwambia mkewe, akaona simu ya mkewe inaita. “Mwanao huyu hapa, amehamia kwangu!” Mama Msindai akaongea akiitizama simu yake. “Sasa leo hakuna kitakachofanyika ila kumtuliza yeye!” “Wewe mwambie atulie, bwana Jackson! Mkewe na mtoto watakuwa sawa!” Baba yake akaanza kupiga simu kuomba msaada wa haraka kwa madaktari aliojuwa ni wazuri na hawapo kazini.

“Mama!” “Jackson, baba yako anahangaika kutafuta madaktari wa kukutana na Sabrina huko hospitalini. Ameondoka hapa na gari ya wagonjwa ya usalama, anapelekwa usalama wa taifa ambako atakuwa ni yeye tu na madaktari. Ameshawekewa dripu, nina uhakika mpaka tunafika hospitalini Sabrina atakuwa yupo sawa. Ni pressure ndiyo ipo juu baba.” Mama yake akajaribu kumtuliza. “Wewe usikate simu. Mimi narudi nyumbani kujiandaa. Naomba niombee kwa kaka, tiketi ya ndege yakuondoka leo huku.” “Nisikilize Jack. Umepaniki, na sidhani kama ni sawa kuendesha hata kurudi nyumbani.” “Mama! HUU SIO WAKATI WAKUNIFIKIRIA MIMI ILA HALI YA MTOTO WANGU NA SABRINA. NAONDOKA SASA HIVI.” Jack akagomba mpaka mama yake akaweka simu pembeni akawa anasikiliza simu akiwa ameishika mkononi wala si sikioni. “Mama!” “Nimeelewa baba. Nampigia simu sasa hivi Junior akutafutie usafiri wa kukuleta leo Dar. Ila naomba taratibu huko njiani Jack.” Simu ikakatwa. “Leo kazi ipo.” Akaongea mama Msindai.

Akimpigi simu Junior. “Junior baba, naomba msaidie Jack afike Dar leo. Lasivyo hakuna kitakachofanyika leo ila kujibu simu zake tu.” “Na simu yake hiyo inaingia hapa kwangu. Ananipigia sasa hivi.” “Kila la kheri! Anawasiwasi sana.” “Na mimi nipo njiani nakuja huko hospitalini, Jacinta ameniambia.” Wakaagana, ili apokee simu ya Jack. Jacinta ndiye aliyekuwa ni mfanyakazi wa usalama wa taifa, tena kiongozi aliyeshika wadhifa wa juu sana, na Mzee Msindai ambaye alikuwa daktari hapo kwa muda mrefu akihudumia watoto na hospitali kuu ya Muhimbili pia, mpaka akastaafu na kufungua hospitali yake mwenyewe.

Sabrina Hospitalini.

S

abrina alifikishwa hospitalini matibabu ya kaanza. Hapakuwa na kitu kigeni sana na chakutisha ila ni kweli pressure ilikuwa juu. Mzee Msindai alishaomba vipimo alivyofanyiwa kutoka hospitali ya Muhimbili siku hiyo asubuhi vitumwe hapo ili anayemuhudumia hapo ajue anamshugulikia mama mjamzito wa namna gani. Akaja huyu akafanya kile ilimradi Sabrina alikuwa kwenye mikono salama na sahihi.

Hali ya mtoto ikaonekana sio nzuri, wakaombwa wote watoke nje akabaki mzee Msindai tu na madaktari wengine ndani ya chumba alichokuwa akihudumiwa Sabrina, kina Mama Msindai, Jacinta na Pendo wakatoka nje wakisubiria Sabrina ahudumiwe. Wasiwasi sasa ukawaingia wote baada ya daktari aliyekuwa akiangalia mapigo ya mtoto kutopata vizuri. Jacinta akaanza. “Huyu Sabrina mbona nilisikia habari zake masaa machache yaliyopita kutoka kwa mumewe akanitumia na picha za mtoto wao kuwa ni mzima kabisa! Na Jack akasema daktari alimwambia Sabrina mtoto ni mzima hata amegeuka! Jack akawa ananiringishia kuwa dume lake linataka kuwahi kutoka kumuona! Imekuaje sasa hivi nasikia madaktari wananong’ona tena kuwa hawasikii vizuri mapigo ya mtoto?” Jacinta akauliza. Pendo kimya.

“Eti Pendo, kulitokea nini hapo katikati maana na mimi Sabrina alinitumia picha za mjukuu, nikampigia akase...” “Na mimi nilikuwepo mama wakati mkizungumza. Si unakumbuka ulitutania tunashindana matumbo?” Pendo akaongea akionekana ameingiwa na yeye na wasiwasi. “Hakika Jackson atachanganyikiwa chochote kikitokea kwa huyo mtoto. Mimi mwenyewe nahisi nita...” “Mama tulia bwana. Akija hapa Jack na kuona wewe umepaniki ndio atapaniki mara mbili.” “Junior amempatia usafiri?” “Niliona kuna ndege Dodoma. Kuna mkubwa anarudi huku jioni hii. Junior amemwambia apitie Dodoma, watakuja naye.” “Sasa atapata ndege yakumtoa Singida mpaka Dodoma kweli?” “Junior ameshugulikia kila kitu mama. Na mimi nikisaidia kwa kadiri ya uwezo wangu. Naomba utulie, Jack atakuwepo hapa kabla ya saa 11 jioni.” “Na hizo foleni za uwanja wa ndege mpaka hapa!” Mama Msindai akaendelea kuweka wasiwasi. “Mama Msindai! Nimekwambia ninashugulikia Jackson awepo hapa kabla ya saa 11 jioni. Naomba utulie mama.” Jacinta akamtuliza. Akanyamaza.

Pendo naye alikuwa kimya. “Eti Pendo? Au alianguka huyu Sabrina?” “Hapana dada. Tena vile kukutwa sakafuni ni yeye mwenyewe aliwahi ili asije kuanguka. Nafikiri alipandisha hasira baada ya mazungumzo yake na mtu aliyekuwa akimtaja kama Max.” Jacinta akashituka sana. “Subiri kwanza Pendo. Maximilian Kundi!?” “Sijui dada, ila yeye alikuwa akimtaja kama Max tu.” “Kwani wewe Jacinta unamjua huyo Maximilian Kundi kama nani kwa Sabrina?”  Akauliza mama yake. Jacinta hakujibu akamsogelea karibu Pendo.

“Walikuwa wakizungumza kwa simu au alimfuata?” “Huyo Max alitukuta tunakula pale akakaa akisema anataka kuzungumza na Sabrina akisema anataka kuomba amani. Lakini Sabrina akaanza kulia sana akimshutumu Max. Sikuelewa ni nini anaongelea, kwa kuwa ndio na mimi kwa mara ya kwanza namsikia na kumuona huyo Max ila ni kama nakumbuka Sabrina akimsema pale kama ni mwanasheria.” “Ni yeye. Ngoja nimtaarifu Junior.” “Kuna nini!?”  Akauliza mama Msindai na wasiwasi akiona amepitwa.

“Wewe mama angalia mambo ya mjukuu, mengine yaache.” “Wewe unajua sitaacha na sasahivi nitajua. Aidha kutoka kwako, au kwa Junior, au kwa Jackson mwenyewe au nitapiga simu sasa hivi habari zinifikie hapahapa tukiwa tumesimama hapahapa.” “Kuna mambo mengine mama Msindai jifunze kuyaacha yakupite. Junior na Jack wameomba kabisa na kunisihi usiambiwe.” Jacinta akamsihi mama yake. “Sasa hapo ndipo nitakapotaka kujua, tena sasa hivi. Jambo linalotaka kuhatarisha maisha ya watu wanaonihusu! Mjukuu ambaye nimekuwa nikisumbiria! Huna utakaloniambia Jacinta, nikanyamaza. Na unanijua mimi, nitafanya makubwa, patanguruma hapa au nitaagiza niletewe huyo Max mwenyewe ajieleze yeye ni nani na anataka nini.” Jacinta akabaki akimtizama mama yake, na yeye akamtizama.

“We Jacinta?” “Basi naomba Junior aje azungumze na wewe, mama. Yupo njiani anakuja.” “Sawa.” Akakubali mama Msindai na kutulia kidogo. “Au...” “Hapana mama. Umeshakubali kusubiri, naomba subiri tafadhali.” “Kwani yanamuhusu nani?” Jacinta akatingisha kichwa na kutaka kuondoka. “Unanipuuza mimi Jacinta!?” Jacinta akageuka. “Umekubali kusubiri mama yangu. Ni nini!?” “Nataka sasa kujua yanamuhusu nani. Naona kusubiria hilo jibu sitaweza na sitaki kuzungumza na mtu asiye sahihi.” “Yanamuhusu mwanao Jack na familia yake. Tena yeye ndio amenisihi haswa usiambiwe mama. Tafadhali acha.” “Sasa Junior ameingiaje?” Akaendelea kudadisi. Jacinta akavuta pumzi kwa nguvu, akainama kama anayefikiria.

“We Jacinta? Au unataka nikamtoe Msindai ndani anisaidie kunitafutia habari kamili kwa kinachoendelea kati ya huyo Maximilian Kundi na familia ya Msindai au unaniambia?” “Umeshamshika jina lake kamili, mama jamani! Mbona unataka kunigombanisha na kina Junior walioniamini, na...” “Kwa hiyo na Junior anahusika?” Jacinta akanyamaza. “Au yeye ndio mama yenu siku hizi, anayeambiwa mambo yenu, mimi sina maana tena?” “Mama Msindai usiende mbali. Yanamuhusu Junior pia.” Mama Msindai akakunja uso.

“Jambo gani linalomuhusu Jackson na familia yake, halafu tena limuhusu na Junior?!” Akafikiria kwa sauti. “Yanamuhusu kama Junior Msindai au kama Waziri?” Akauliza kwa sauti akimtizama Jacinta. “Naenda kupiga simu mama, naomba tulia na usimtoe baba ndani, acha amuhudumie mtoto wa Jack, usije ukazua jingine.” “Ninao watu wa Usalama wengi tu. Wala si wewe na baba yako ndio ninaowafahamu huko Usalama wa Taifa. Ulinikuta nikifahamiana nao. Nyinyi kina Msindai msinibabaishe. Mnajidai mnanificha mimi mnafikiri sifahamiani na watu! Nawajua watu wakubwa kuliko nyinyi kina Msindai.” “Sawa mama.” Jacinta akaondoka pale wala hakutaka kubishana naye tena. Alijua akibaki pale, atamtoa ukweli wote na kujikuta akimwambia kila kitu.

Jacinta & Junior.

J

acinta alitoka pale na kurudi ofisini kwake, kwenye jengo jingine tu lakini paleplae ndani Usalama wa Taifa, akampigia simu Junior. “Nimetoka kuzungumza na Pendo. Bahati mbaya nilimuuliza nini kilitokea mpaka Sabrina aanguke wakati alikuwa mzima kabisa, lakini mbele ya mama!” “Na mimi nilishangaa. Jack alinitumia picha za mtoto wake akasema ni mzima kabisa. Sasa hivi baba ananipigia simu kuniulizia Jack amefikia wapi, anatakiwa aje atoe maamuzi hali ya mtoto sio nzuri!” “Junior!” “Kweli. Wanasema mapigo yake ya moyo si mazuri kwa sababu ya pressure ya mama yake.” “Jack atachanganyikiwa Junior. Sasa amefikia wapi?” “Sina chakufanya, nilazima asogee mpaka Dodoma kama ulivyosema. Mbaya zaidi hakuna ndege ya sasahivi yakumtoa Singida. Nimemuomba baba wahangaike kwanza, kumtaarifu yeye iwe jambo la mwisho, lakini kwa jinsi nilivyosikia kwenye sauti ya baba, nahisi hali si nzuri.” “Baba huwa sio mtu wa kupaniki au kukata tamaa.” Akaongeza Jacinta. “Ndio hicho sasa, ukimsikia akiwa amepaniki ujue hicho kitu si kizuri.” Wakatulia wakifikiria.

“Ulitaka kusema nini juu ya Pendo na mama?” “Mmmh! Mpaka nilisahau! Nilimuuliza Pendo ni nini kilitokea kutoka Sabrina anatoka hospitalini mpaka pressure kuwa juu kiasi hicho!” Junior kimya akisikiliza. “Akasema Max alimfuata.” “No way!” Junior akahamaki. “Alimfuata wapi!?” “Wakati wanakula baada ya kutoka huko hospitalini kwa kliniki. Anasema Sabrina akagomba na kulia sana kwa Max, mpaka pressure ikapanda.” “Hapana Jacinta. Huyu mtu lazima kumshugulikia sasa hivi. Hatuwezi kuendelea kusubiri.” “Na mimi naona hivyo. Nilitaka kukutaarifu hicho na kukwambia...” “Simu ya mama hiyo!” Jacinta akamsikia kaka yake. “Ndio hicho nilitaka kukwambia. Usipokee kwanza nisikilize.” Jacinta akataka kumpanga kaka yake kwanza.

“Mama anataka nini!?” “Anataka umwambie huyo Max ni nani na anahusika vipi kwako na kwa familia ya Jack.” “Mama angetulia kwanza!” “Hapa nimemkimbia. Ashawaka, hamna utakachomwambia tena akasikia. Amesema yupo radhi akamtoe baba ndani anakomuhudumia Sabrina na mtoto, au apige simu kwa watu wake wengine wa Usalama kuulizia habari za huyo Max.” “Acha nimpigie nimtulize, nimwambie nitakuwepo hapo baada ya muda mfupi sana. Na wewe naomba ukamilishe swala la Max tafadhali, Jacinta. Huyu mtu atatuangamiza kweli!” “Sasa hivi natuma akakamatwe.” Wakaagana.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Bado mapigo ya mtoto yalikuwa chini. Yanapiga na kupotea, na kwa kuwa mtoto alishakomaa, na pressure ya Sabrina ilikuwa imeanza kushuka, daktari akamshauri mzee Msindai watoe mtoto kwa haraka. “Sidhani kama ni sawa kuendelea kusubiri Mzee. Tunajiweka kwenye hatari pasipo sababu.” “Acha nimtaarifu mumewe kwanza.” Mzee Msindai akatoka na kumkuta mkewe hapo nje. “Naomba usipaniki ila unisikilize.” “Sasa hapo ndio unanipanikisha na wewe.” Mama Msindai akawaka kwa mumewe. “Sasa wewe ukiwa juu hivyo, nani atakuwa msaada kwa hawa watoto?” “Wewe niambie Msindai.” “Pressure ya Sabrina imeanza kushuka ni kitu kizuri. Inabidi mtoto atolewe ili kuepuka madhara kwake.” “Mmepata mapigo yake ya moyo?” Mama Msindai akauliza. Willy naye akaja hapo akiongozana na Joy.

“Poleni jamani.” Wote kwa pamoja ndio ikawa salamu yao. “Ndio Msindai anatoa taarifa hapa.” “Naomba tuzungumze na Jack ili atoe baraka zake, mkewe apelekwe chumba cha upasuaji.” “Kupasuliwa tena! Kwa nini?” Mama Msindai akazidi kupaniki, Junior naye akaingia. “Naomba utulie mama. Sauti yako inasikika mpaka huko nje.” Junior akamtuliza. “Mimi sijali maswala ya sauti nataka kujua.” “Naomba nizungumze na Junior hapo pembeni.” Baba yake akamvuta mkono, mama Msindai naye akasimama na kufuata. “Naomba usubiri kwanza, mama J. Hali hiyo tukimpigia simu Jack ndio atapaniki zaidi.” Mumewe akamsihi. “Subiri mama.” Mama Msindai akarudi kukaa.

“Nataka kumpigia simu Jackson na wewe ukiwepo, akubali sasa hivi mkewe afanyiwe upasuaji na pengine azungumze naye. Anatetemeka sana wakati pressure imeanza kushuka, au niseme sio mbaya. Nafikiri ameingiwa na hofu. Lakini tukifanikiwa kumtuliza Jack, akazungumza na mkewe akatulia, hawatapoteza mtoto.” “Ndio tumefikia hapo?!” Junior akaingiwa na wasiwasi. “Yaah! Mapigo ya mtoto sio mazuri amepatwa fetal distress. Na mbaya zaidi mama yake alishaanza tayari uchungu tokea hawajamfikisha hapa. Aliyehusika kumpima kule walikomtoa kabla hawajambemba kwenye gari, anasema alianza kuona dalili za uchungu. Wakajua ni sababu ya hiyo pressure kwenda juu sana, ndio iliyosababisha kuanzwa kwa uchungu. Lakini hata hivyo mtoto amekomaa, amebakisha siku chache sana kuzaliwa, hata 10 zisingefika. Ndio maana wanaona atolewe tu.” “Mungu asaidie. Jack atachanganyikiwa, baba. Acha tumpigie.” Junior akampigia.

“Jack?” “Vipi kaka? Umefika kumuona mke wangu?” Jack akauliza na wasiwasi. “Nipo hapa na baba alikuwa akinipa maendeleo ya mama na mtoto.” Jack akatulia. “Pressure ya Sabrina imeanza kushuka kitu ambacho nikizuri. Na kwa kuwa mtoto amekomaa, wanaona ni heri wamtoe tu.” “Wanamtoaje mtoto, kwani Sabrina ameshaanzwa na uchungu?” Baba yake akapokea simu. “Ndiyo. Lakini wanaepuka asisukume, wanataka kumsaidia ajifungue kwa upasuaji.” “Sijaelewa! Nahisi sijui nimepaniki! Kwa nini upasuaji tena!? Naomba mniambie ukweli kama mke wangu na mtoto wapo matatizoni.” Junior akamtizama baba yake.

“Tukichelewa ndipo watakuwa matatizoni ndio maana tumekupigia ili utoe idhini yako afanyiwe tu.” “Siwezi kufikiria mpaka nimuone Sabrina, baba. Nahisi napaniki sijui niseme nini! Naomba kumuona Sabrina.” Junior akachukua simu. “Sasa mkeo yupo kwenye hali mbaya Jack. Anakuhitaji wewe umtie moyo ili kuweza kupita hapa. Lasivyo mtapoteza mtoto na utamtesa mkeo. Unanisikiliza Jack?” “Nasikia ila naomba unielewe na mimi, nimeingiwa hofu kaka. Nilikuwa kwenye kujiandaa kuja Dar, kumpokea huyo mtoto kwenye hali ya utulivu. Sasa hivi nimekwama huku, mtoto wangu anazaliwa huko! Tena anazaliwa kwa njia ambayo muda mfupi uliopita hata haikuwa ikifikirika!” “Nisikilize Jack na ujikaze uache kulia mbele ya mkeo. Haya mambo yanatokea. Na uzuri kama ipo njia ya kusaidia, ni vizuri utoe ruhusa, mkeo na mtoto  wahudumiwe. Ni sawa?” “Sawa.” “Basi naomba utulie, baba anampelekea mkeo simu umtulize. Anasema ameingiwa na hofu sana.” “Piga kwa video basi nimuone.” Kaka yake akamwangalia baba yao.

“Lazima nimuone na yeye anione ili kumtuliza!” Jack akaweka msisitizo. “Basi tulia Jack ili aweze kuona tumaini kwako.” Junior akakata na kupiga kwa video, akamkabidhi baba yake, akarudi ndani kwa Sabrina. “Mumeo huyu hapa.” Akamkabidhi simu. “Brina?” “Unakuja?” Sabrina akauliza na machozi. “Nipo njiani nakuja. Vipi lakini wewe?” “Naogopa sana Jack. Mapigo ya mtoto hayasikiki vizuri.” “Ingekuwa ni mtu mwingine mwenye huyo mtoto, hata mimi ningeingiwa hofu, lakini kwa kuwa ni wewe, najua utaweza tu.” “Kweli?” “Kabisa. Hata hilo lipo ndani ya uwezo wako. Tulia kabisa na uzuri upo na wataalamu hao, watakusaidia tu.” Sabrina akavuta pumzi kwa nguvu kujaribu kutulia.

“Kwani wewe uko wapi sasa hivi?” “Nakuja Brina. Nipo njiani.” “Bado upo Singida?!” “Niombee nifike salama na mimi nakuombea kila kitu kiende salama.” “Nimesikia wakimwambia baba wanataka kunifanyia upasuji. Sasa itakuaje kama wewe hautakuwepo?” “Kila kitu kitaenda sawa. Baba ameniambia hata ningekuwepo, wasingeniruhusu kuingia.” “Lakini nilitamani ungekuwepo tu nijue upo na tuagane kabla sijaingia. Nisipotoka hai je?” Jack akaingiwa na hofu, na yeye akaanza kulia kama mkewe. “Naogopa Jack. Naogopa sana.” Jack akabaki kimya akilia. Baba yake akachukua simu.

“Naomba nyinyi wawili wote mnisikilize. Hakuna hatari kubwa kwa sasa. Wanachotaka nikumsaidia mtoto. Na kama Sabrina angekuwa na tatizo, ningekwambia Jackson. Mmesikia?” Kimya wakiendelea kulia. “Jack safiri kwa utulivu ukijua unakuja kumkuta mke na mtoto wako, na Sabrina utulie kabisa ili kutuliza hiyo pressure waweze kukusaidia kumtoa mtoto. Hofu yeyote sasahivi haitamsaidia mtoto wenu. Sijui kama mnanielewa?” Hakuna aliyejibu. “Na wameanza kumtaka Sabrina wamwandae kumwingiza chumba cha upasuaji. Usiogope hata kidogo. Hakuna hatari.” Mzee Msindai akawapisha wauguzi waliotaka kumuandaa Sabrina kumpeleka chumba cha upasuaji.

Mipango Ya Mungu Si Ya Mwanadamu.

S

abrina alitolewa akiwa anapelekwa chumba cha upasuaji, analia hakuna anayemsikiliza hapo nje walipokuwa wakimsubiria kumuaga na kumwambia wanamuombea asiwe na wasiwasi. Sabrina alikuwa akilia sana. “Sasa Sabrina mama, watakufanyiaje upasuaji unalia hivyo! Tulia ukijua ukitoka utamkuta mumeo.” Mama Msindai akajaribu kumtuliza wakiwa wanamfuata nyuma akiwa amelazwa kwenye kitanda. “Jack hajatoka hata Singida, mama!” “Lakini anakuja. Naomba utulie na uamini kila kitu kitakwenda sawa.” Sabrina akaendelea kulia wala asimsikilize mtu tena. “Nakuombea Sabrina. Kila kitu kitaenda sawa. Na nimezungumza na mama pamoja na Sabina. Watoto wapo sawa. Nimewaambia wamuachie Sifa watoto, wao waje. Ukitoka utawakuta. Kwa hiyo usiwe na wasiwasi.” Pendo akamuongelesha kwa upole na upendo, Sabrina akatingisha tu kichwa na kuendelea kulia.  “Sasa atafanyiwaje upasuaji analia hivyo!?” Mama Msindai akamuuliza mumewe. “Hatuwezi kumsubiria Jack, lasivyo watapoteza mtoto. Watamchoma sindano, atalala tu. Hakuna jinsi.” Sabrina akaingizwa chumba cha upasuji wengine wote wakasubiri hapo nje.

“Naomba mpigie tena Jack kujua amefikia wapi, Junior mwanangu. Asije akatoka tena, asimkute mumewe.” “Mwanao huyo ameniangusha kabisa! Mimi namwambia azungumze na mwenzie amtulize, na yeye analia bwana!” Mzee Msindai akalalamika. “Anaogopa. Kila mtu ameingiwa na hofu. Msimlaumu mtoto.” Wote wakamgeukia mama Msindai wakimshangaa. “Ndio ni mtoto na ninaomba mumpigie simu sasahivi kujua amefikia wapi.” Junior akatingisha kichwa na kuondoka pale. 

~~~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya muda mama yake na Sabina wakawa wamefika pale. Wakakuta wanasubiria hapo. Willy ndiye aliyekwenda kuwapokea na kuwaleta walipo. Kila mtu alikuwa kimya akisubiria kivyake. Baada ya kama dakika 25 mtoto akatolewa akiwa ameshikwa na daktari wa watoto. Wote wakasimama. “Amefanana na baba huyo!” Wote wakakubaliana na Jacinta. Jacinta akampiga picha kwa haraka, mtoto akatolewa pale. “Inabidi akawekwe kwenye mashine na apewe oxygen kwa haraka, ili kumsaidia upumuaji. Vinginevyo amezaliwa na uzito mzuri tu na amekomaa kama mnavyomuona.” “Asante sana, nashukuru. Naomba tuongozane.” “Bila shaka.” Mzee Msindai akafuata nyuma.

Mama Sabrina akamkimbilia yule daktari kabla hajapotea. “Vipi mama yake huyu?” Akauliza kwa wasiwasi. “Wanamalizia. Atatolewa muda si mrefu. Kila kitu kimekwenda sawa. Usiwe na wasiwasi. Samahani nilikuwa na haraka nimeshindwa kutoa taarifa za mama.” “Asante.” Mama Sabrina akarudi kwenye kundi wengine wakajisuta. Hata walisahau kuuliza habari za Sabrina. “Afadhali umeulizia mama kuliko hivi tulivyokuwa tumebaki hapa na wasiwasi.” Akaongea mama Msindai, mama Sabina akarudi kukaa na kuinama.

Muda ukazidi kwenda. “Jacinta, Jackson amefikia wapi?” Mama Msindai akauliza. Akaona Jacinta na Junior wanaangaliana. “Mnanikera mimi nyinyi wawili na vijisiri visivyoisha! Sasa kama sasa hivi mlitaka kunificha nini?” Akalalamika kwa ukali mama Msindai. “Tulitaka kupunguza wasiwasi mama.” Junior akamtuliza. “Jackson yuko wapi, Junior?” Akauliza tena kwa ukali. “Hajapata ndege yakumtoa Singida. Leo hakuna ndege mama.” Mama Msindai akabaki ameduaa.

“Lakini tumemshauri kama anaweza kusogea hata kwa basi mpaka Dodoma au Arusha, atapata ndege hata ya usiku.” “Yaani nyinyi wawili na akili zenu zote mnashindwa kumfikisha mtoto hapa!? Nimewapa kazi moja tu. Moja! Na imewashinda. Mme..” “Mama, naomba utulie. Jacinta alitafuta ndege na akazungumza na watu wamsubirie Jackson Dodoma, ili waje nae. Wakakubali. Hakuna jinsi nyingine yakufanya kwa kuwa hakuna ndege Singida. Na hawawezi kuendelea kumsubiria Jackson Dodoma wakati hiyo ndege inamleta mkubwa huku Dar.” Junior akajaribu kumtuliza mama yake na kuondoka kuzungumza tena na Jack. Mama Msindai naye akasimama.

“Najua umekasirika mama, ila nakusihi hivyo ulivyo usimpigie simu Jack sasahivi. Nimetoka kuzungumza naye, yupo na hali mbaya kuliko hivi alivyo Sabrina. Imebidi kumsindikiza kwa simu mpaka ameingia kwenye basi.” “Anaelekea wapi sasa?” Mama yake akamuuliza Jacinta. “Amesema Arusha ndio kuna ndege nyingi.” “Sasa si atafika hapa kesho! Mnamshaurije mtoto lakini nyinyi?” “Naomba  tulia mama. Maana ameshaondoka Singida, tumuombee afike hapa salama.” “Kuendesha?” Jena akauliza. “Kuendesha Junior amemkataza. Amepaniki sana.” Jacinta akajibu. Junior ameenda kumpigia tena kumuangalia na kumpa habari za mtoto.

~~~~~~~~~~~~~~~~

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment