Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 45. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 45.

Jack akiwa ofisini kwake akaambiwa anamgeni anahitaji kumuona. Akatoka mpaka mapokezi. Akakutana na mtu mtanashati. “Nikusaidie nini?” “Nimekuja kutafuta amani.” Jack akakunja uso. “Tunaweza kukaa kidogo?” Jack akatafuta sehemu wakakaa. “Mimi ni mwakilishi wa bwana Maximilian Kundi na mkewe.” Jack akacheka na kutulia. “Nimekuja kuomba amani na kuomba kumaliza mambo bila kufikishana kwenye vyombo vya sheria.” “Nafikiri hilo tumeshachelewa.” Jack akajibu. “Basi labda niseme, tusiende mbali.” “Nilimwambia Tino, ambaye alishawishiwa na huyo unayemwakilisha ili aje anifanyie mimi fujo, labda hakukwambia wewe au Max. Ila nitarudia kwa manufaa yako na wewe.” Yule wakili akakaa sawa kusikiliza.

“Hakuna umbali nitakao shindwa kwenda ambako kutanisaidia kulinda familia yangu. Nitafanya lolote na chochote kulinda familia yangu. Sijui walikushirikisha nini na kwa umbali gani, lakini hao uliowataja, wametishia familia yangu, na siwezi kufumbia macho. Ushahidi ninao. Na ninakutuma kwao, waambie chochote kitakachompata mke wangu, watoto wangu, mimi mwenyewe na familia ya Msindai, wao watakuwa watuhumiwa wa kwanza. Wakili wetu anao ushahidi wote na wengineo wanao ushahidi pia, ili chochote kikimtokea hata huyo wakili wetu, kuwepo na ushahidi mwingine.” “Lakini nafikiri tunaweza kuzungumza tu.” “Si ndio tunazungumza hapa! Ulitaka kusikia nini? Au kuna ujumbe mwingine ambao hujaufikisha kwangu?” Jack akawaka. Ujasiri uliongezeka kwa kuwa aliwawahi kwa ushahidi. Kwa mara ya kwanza Max akafikishwa magotini.

“Kama hakuna ujumbe mwingine, naomba nirudi kwenye kuwajibika.” “Samahani kwa kuwa najua upo kazini. Lakini naomba niombe msamaha na nikuhakikishie kabisa, hiyo familia itakaa mbali kabisa na familia ya Msindai. Naweza hata kuweka kwenye maandishi ili tu kufanya haya mambo yasiende mbali.” “Nakwambia haya mambo yapo mbali zaidi ya hivi tunavyozungumza. Vitisho vyao vimenaswa na vyombo vya Usalama wa taifa! Hawakukwambia hilo!?” Jack akauliza na kuendelea bila kusubiri jibu. “Kunifuata mimi mtu mdogo sana, muhasibu wa serikali tu, tena mkoani Singida, ukiwa umemtishia waziri wa hii nchi, unafikiri itabadili kitu? Au kusaidia kweli!?” Jack akazidi kumtisha.

“Nafikiri unataka kunipotezea muda ambao nalipwa na serikali  kuwajibika.” “Naweza kukufuata tena baada ya kazi.” Jack akakunja uso. “Nipo hapa na wewe. Nimekupa nafasi ya kuzungumza. Tena kwa kutumia muda wa mwajiri wangu. Halafu unataka tena nikupe na muda wa familia! Ni nini ungetaka kusikia kutoka kwangu?” “Natafuta amani kati yako na kina Kundi.” Jack akashangaa sana. “Mnamfanya nani mtoto mdogo hapa!? Upo leo kutafuta amani kwakuwa wamekamatwa. Wamekwambia lakini ni nini walipanga dhidi yangu na familia yangu?” Kimya kwa kuwa Jack alishapandwa sana na hasira.

“Nakuuliza? Unajua mipango mibaya waliyokuwa wamepanga kwa siri huyo Max na mkewe kumtenda kaka yangu ambaye hakuwa na hatia?” Kimya. “Walikusudia kumuharibia kazi kwa kumzulia kashifa nzito! Kwa ajili ya Max kujinufaisha tu yeye mwenyewe kifedha na ajira. Mtu kama huyo aachwe na kazi yenye nguvu sana kwenye jamaii, unafikiri ataangamiza wangapi? Na wewe unajiharibia kuja hapa kutetea uovu wao, si inamaana unahalalisha uovu wao?” “Hata kidogo.” “Basi acha sheria ichukue mkondo wake. Kama na wewe unalipwa ili kuwatetea, basi simama kisheria ujipange kuwatetea siku watu wa Usalama watakapokamilisha uchunguzi wao. Nakutakia siku njema.” Jack akasimama  na kuondoka.

Kwa Sabrina.

J

ack akaingia ndani na kumpigia simu Sabrina. “Upo mzima baba watoto?” Akaanza Sabrina. “Mzima. Mbona kimya?” “Nilikuwa nimesinzia hapa sakafuni,  hivi umepiga ndio nimeamka. Makinda yako sijui yametawanyikia wapi! Ngoja nianze kusaka.” Sabrina akakaa Jack akacheka. “Walikuwa wanaongea hapa huku wanarukaruka tumboni, nikaishia kuloa mate, nikaona nilale tu maana sielewi.” “Mlango wa mbele wa hapo sebuleni umefungwa lakini?” Sabrina akashituka kidogo akasimama. “Umefungwa, watakuwa.. Jeiline!” “Muite Keiline kwanza ndio atakuja kwa haraka.” “Na kweli.” Sabrina akaanza kuwasaka huku akimuita Keiline, akamuona anatokea chumbani. Akacheka. “Kama ulijua. Keiline ndio katoka. Walikuwa chumbani kwao.” Sabrina akainama na kumbusu.

“Mtoto mzuri wewe! Mlikuwa mnaharibu nini chumbani?” Akaanza kucheka. “Muone!” “Weka kwenye video nimuone.” “Naona hiyo shuguli niifanye nikiwa nimejilaza kabisa chini sakafuni hapo chumbani kwao. Haya twende Keiline.” Kuingia chumbani, wamevuruga kuliko kawaida. “Hapa chumbani kwao ni kama kumepigwa bomu!” Jack akacheka. “Nalala hapa hapa. Haya, njooni watoto wa Jack, mumuone baba yenu, mimi nilale.” Sabrina akaweka video akajilaza chini, wote waliposikia sauti ya Jack akiwaita wakatambaa mpaka kwenye simu, wakaanza kupiga makofi, kila mtu akiongea lake. Jack moyo safi, amejishindia vibinti viwili. Tena vinaafya nzuri. Jack aliporidhika wote wapo salama, akarudi kuendelea na kazi.

Sabrina na watoto jijini Dar.

S

iku zilipokaribia za harusi ya Pendo na Willy, ikabidi Sabrina atangulie na watoto Dar amuache Jack kazini ili kutunza siku za likizo. Akashukia nyumbani kwa Pendo kwa makubaliano baada ya harusi atahamia ukweni. Ukweli ni kwamba Sabrina alijua maisha yake na hao watoto wakizungu huko ukweni bila Jack, itakuwa shida tupu. Hapatakuwa na uhuru na watoto hao wanaofika kila mahali kama si kwa kutambaa, basi kwa kutumia vigari vyao wakisuma mpaka watakapo. Sabrina akamwambia Jack, atajifungua kabla ya siku kwa wasiwasi. Ndipo Jack akamwambia mama yake kuwa Sabrina atakuwepo Dar lakini nyumbani kwa Pendo kwa ajili ya kumsaidia maandalizi ya harusi, ila harusi ikiisha atahamia kwa mama Msindai. Yote hayo Sabrina alijua mumewe atakuwa yupo naye jijini. Wakaelewa.

Alifika Dar na wanae akiwa ameshatafutiwa daktari wa wakina mama, baba mkwe wake akamwambia lazima aanze mara moja ili ikitokea anajifungua mapema, basi huyo daktari ajue anamsaidia mama wa namna gani na mtoto. Pendo alimsindikiza kliniki kwa mara ya kwanza hapo jijini Dar. Sabrina alimuomba mama yake aje akae nao hapo kwa muda akimsaidia swala la watoto ili msichana wa kazi, wa Pendo asilemewe. Kwa hiyo siku wanafika na mama yake naye akaletwa na Sabina. Kwahiyo wakati anakwenda kliniki na Pendo, aliwaacha watoto wake na mama yake akiwa hana wasiwasi.

Walitoka na Pendo wakiwa wamejawa furaha, moja kwa moja mpaka kliniki. Sabrina akaanza upya kwa huyo daktari kama hajawahi kuhudhuria kliniki kabla. Akafanyiwa vipimo vyote na ultrasound. Akaambiwa mtoto alishageuka kabisa. Siku zilikuwa zimekaribia. Daktari alimwambia kila kitu kipo sawa. Wakatoka hapo akamtaarifu Jack na kumtumia picha za ultrasound. ‘Mwanao huyo! Mzima, wanasema yupo tayari kuja kukuona dady.’ Jack akafurahia na kumpigia simu baada yakuona picha. Wakazungumza. “Binti zangu?” “Wako na bibi yao, amesema leo atawalisha ugali. Kama nawaona watakavyolala!” Jack akacheka. Akamsalimia na Pendo wakaagana baada ya kuwaambia watakwenda sehemu wakae na kula ili kupata muda wao.

Sabrina akamtumia na mama mkwe wake hizo picha za mtoto za ultrasound. Kisha akampigia kumshukuru kwa kumtafutia daktari mzuri. “Walikuangalia kila kitu lakini?” “Kila kitu mama. Utafikiri ndio mara ya kwanza ninaanza kliniki!” Mama Msindai akacheka. “Nilimwambia huyo daktari aweke umakini maana mimi huyo daktari wenu mliyekuwa mkimuona huko Singida hata sijamuelewa vizuri.” Sabrina akacheka tu akimjua mama Msindai. Jambo lake yeye ndio huwa linaeleweka. Akaulizia wajukuu zake. “Wapo na bibi yao. Amesema leo atawalisha ugali.” Wakacheka. “Watakubali sasa?” “Tunashangaa sisi huwa tukiwalisha wanatukatalia, lakini bibi yao akiwalisha huwa wanakula bila shida! Na huwa wanalala mpaka mnasahau.” Wakacheka tena. Na yeye akamsalimia Pendo na kutaka kujua anaendeleaje na watoto wake. Akawatania. “Bibi harusi na msimamizi wote mnashindana matumbo!” Wakacheka na kuagana.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakafika kwenye hoteli nzuri wawili hao stori zikaanza. Sabrina akamwambia muhudumu kile kilichopo tayari kwa haraka kiletwe aanze kula ndipo ataagiza anachotaka. Pendo akaanza kucheka. “Huogopi kunenepa?” “Hata sina hilo wazo na wasiwasi. Mwili wenyewe naona umegoma!” “Kwa hiyo hapo unakula kila kitu!?” Pendo akauliza kwa mshangao. “Nakwambia kila kitu, tena sana. Mpaka uji wa ulezi nakunywa kama wale watoto wa Jack.” Pendo akacheka sana. “Ukinikuta nakula ugali, utafikiri nimetoka shamba.” “Sasa mbona hunenepi?” “Mama anasema nimechukua mwili mkavu kama shangazi zetu. Halafu chakushangaza, ni mimi tu nyumbani ndio sina mwili.” “Namuona Sabina na ndugu zako wengine.” “Basi. Mama alikuwa akinilisha nilipokuwa nanyonyesha, niliongezeka kidogo tu, tukadhani mwili utasogea lakini ulipoishia ndio ikawa basi.” Pendo akacheka. “Basi mimi nikila hivyo, nafumuka kama nyumba.” “Na hupendi?” Sabrina akaendelea huku akinywa juisi ya embe ambayo walishaletewa.

“We Sabrina! Si nitatisha?” “Ulivyo na umbile zuri hivyo Pendo, dada yangu! Utapendeza kama mama yako.” “Sasa ndio ninachokwepa na sitaki kinitokee.” Wakacheka sana kwani ni kweli Pendo alifanana na mama yake. “Hongereni kwa nyumba nzuri, tulipita na Willy juzi.” “Kweli ile nyumba nzuri! Mpaka nahisi wanaweza kubadili mawazo na kuja kutudai!” Wakazidi kucheka. “Jack anamuharakisha kaka yake amsaidie iwe kwa majina yetu haraka kabla hawajaabadilika hao ndugu.” “Mtahamia sasa au mnakodisha?” Pendo akauliza. “Mmmh! Mimi nahisi kuna ambalo linaendelea, Jack anasita kuniambia.” “Kwa nini?” “Maana na mimi nilimuuliza swali hilo hilo. Tunaanza kutafuta mteja lini na wapi?” “Akajibu tusubiri kidogo, tunaweza tusiikodishe. Sasa nikamshangaa kidogo, kwamba pale Joy alisema tukikodisha tutapata pesa nyingi, na yeye akalifurahia hilo, ni nini kimegeuka gafla!” Sabrina akaendelea kula kwanza.

     “Siku ananijibu hivyo nilikuwa na usingizi, nikaona nifanye yawe mafupi, nilale.” Pendo akacheka. “Sasa wakati nakuja huku nikamkumbusha tena, akaniambia kuna kitu anataka tuzungumze kwanza ndipo atakuwa na uwezo wa kunijibu maswala ya nyumba. Sasa namsubiria aje huku tuzungumze.” “Au anataka auze tena?” “Hawezi. Amesema hiyo ndio itakuwa nyumba za hao binti zake. Wakisumbuliwa na waume zao, wawe na pakurudi.” Pendo akacheka sana. “Jeiline na Keiline?” “Hao hao wawili ndio wanampeleka kichwa resi. Na ndio maana alimwambia kaka yake hati iwe na jina langu na lake, ili isiwahi kutokea mtu ananipokonya.” “Hongera Sabrina.” “Dada! Ni Mungu. Hakika ni Mungu. Mimi mwenyewe namshangaa huyo Mungu.” “Naye Mungu ana mambo yake Sabrina wewe! Sasa hivi kila nikikaa, ndio naelewa mambo mengine.” Wakaendelea kuzungumza hili na like, huku wakiendelea kula.

Max aharibu zaidi.

M

ara Sabrina akashangaa Max anawasogelea. Kitu kikampanda Sabrina, akashikwa na hasira ya ajabu sana baada yakumuona Max. Pendo akamuona ametulia akimtizama anapowasogelea. “Unamfahamu?” “Sana.” Akajibu Sabrina macho kwa Max. “Hujambo Sabrina?” “Sijambo kabisa, namshukuru Mungu.” Akajibu Sabrina macho kwa Max bila tabasamu. “Familia haijambo?” Max akauliza tena kama anayebabaika hajui chakuzungumza. “Unataka nini kwangu Max!? Ni nini unataka?” Sabrina akauliza. “Naweza kukaa kidogo, nina shida yakuzungumza na wewe.” Sabrina akakunja uso. “Sitakuchukulia muda mrefu.” Max akavuta kiti na kukaa.

“Tunafahamiana vizuri kwa muda mrefu sasa ndio maana nimeona nikufuate tuzungumze.” Sabrina kimya akimtizama kwa hasira. “Najua unaelewa kinachoendelea kati yetu na kina Msindai. Nimekosa Sabrina. Hata nimemtuma mtu kwa mumeo kuniombea msamaha ili haya mambo yaishe, kuwe na amani. Nipo tayari hata kuweka kwenye maandishi kuwahakikishia kuwa sitawaingilia tena familia ya Msindai. Tafadhali nisaidie.” Sabrina akakunja uso tena akimwangalia Max kwa mshangao. “Ni hivyo tu Sabrina. Najua nilizungumza maneno ambayo sikutakiwa. Nahisi nikutokana na hasira tu siku ile. Nikampigia simu Tino nikiwa na hasira, nikaongea maneno mabaya. Lakini wote tunajua sina uwezo wa kuwadhuru nyinyi.” Sabrina akazidi kukasirika.

“Kweli.” “Umemaliza Max?” Sabrina akauliza. “Ni hilo tu.” Max akajibu wazi alionekana yupo kwenye hali mbaya. Midomo ilikuwa imemkauka kama siye Max aliyekuwa akinukia vizuri na shati jeupe haswa kila wakati mpaka usiku. “Cha kwanza mimi na wewe hatufahamiani kabisa. Unafahamiana na Sabrina yule mliyekuwa mkimuona dhaifu ambaye angekukwamisha kwanza wewe kupata pesa baada yakushinda kesi ambayo, pili sasa, Tino alikuwa akihangaika kujinufaisha dhidi ya Lela. Ukazungumza naye na kumshawishi aondoe kikwazo ambaye ni mimi, si kwa manufaa yake tu, ila yako pia. Ushinde kesi, ulipwe na Tino, na Tino apate nyumba.” Max akataka kukataa. “Usikatae Max. Kwa kuwa mimi nilikuwa na Tino Moshi nilikuwa nikisikia na kujua njama zako ulizokuwa ukipanga kwa kumfundisha Tino, dhidi yangu.” Max akapoa.

“Kutoka mlipotuaga wewe na mkeo, mimi na Tino kututaka tujipange vizuri, ukarudi kinyumenyume na kumwambia Tino kwa siri kuwa mimi ndio tatizo pekee litakalomfanya asifanikiwe kwenye kesi uliyokuwa ukiitengeneza dhidi ya Lela na mengine mengi unayoyajua wewe, yaliyombadilisha kabisa Tino. Bisha Max.” Kimya. “Mkaanza mipango ya kutonihusisha. Kila ukipiga simu swali lako la kwanza si hata kujua ninaendeleaje mimi niliyekuwa nikimtunza mtu unayetaka pesa yake, unamtaka atoke au awe mbali na mimi ili mzungumze. Na mimi kwa kutaka kujua kinachoendelea, mimi ndio nikawa nikiondoka kumpa Tino nafasi ya mazungumzo, lakini nikiacha simu yangu alipo Tino, iwarikodi mazungumzo yenu yote. Baadaye nilipokuwa nakuwa peke yangu, nilikuwa nikisikiliza kila kitu.” Max kimya na kuzidi kuamini mambo yamemgeukia haswa na hila yake ipo mwangani.

“Nilijua ushauri wako wote wa kikatili uliokuwa ukimshauri Tino kuwa aachane na mimi ila anilipe ili nisije mgeuka baadaye. Ukamsisitiza aweke ushahidi wote wa pesa atakayonilipa mimi ili ikitokea nina madai yeyote yale, muwe na ushahidi. Bisha Max. Nakukaribisha ukanushe haya ninayozungumza.” Kimya. Sabrina akazidi kupandisha hasira. “Ulimpanga Tino vizuri, akawa akitembea na kufanya kila unachomshauri wewe. Na kwa kuwa na yeye roho yake ni mbaya sana, amejawa na ubaya moyoni mwake, akatekeleza yote uliyokuwa ukimtaka anifanyie bila shida, tena akaenda umbali mrefu tu kukufanikishia kila kitu. Ukampongeza. Si ni kweli?” Kimya.

“Upo hapa leo, kwa kuwa umekamatwa kwenye uovu wako, na mipango yako mibaya uliyokuwa ukiipanga dhidi yetu. Na aliyekukamata ni Mungu aliye hai Max. Wala si kina Msindai. Ni Mungu. Na ubaya wako umekufuata, unatakiwa kulipa ndio maana unahangaika kila mahali.” Kimya, Pendo akisikiliza. “Mungu amekuweka kweupe kabisa Max. Hakika amekuweka pabaya. Yale uliyokuwa ukiyafanya kwa siri dhidi yangu nikiwa sijakutendea kosa wewe ambaye ulikuwa ukinufaika na pesa mnazotengeneza kesi na Tino ambaye nilimtoa katika hali ya kufa, mkanitenda ubaya, Mungu ameamua kukuweka mwangani na kukulipiza. Visa vyako na ubaya wako wote, ndivyo vipo mlangoni vikikulilia Max. Wala si Sabrina na mumewe.” Sabrina akaendelea.

“Huu msamaha unaoutafuta kwangu na Jack, nashauri uanze kwa Mungu mwenye nguvu na uweza mkubwa sana Max. Yeye pekee atakutoa kwenye shimo kubwa ulilopo sasa hivi, na hakika nakuhakikishia, hutatoka isipokuwa kwa msaada wa Mungu,  endapo atakurehemu. Kwa kuwa hila yako imechukua sura kubwa zaidi ya unavyodhani Max. Hila yako, uchochezi wako, na njama ulizokuwa ukitaka kumuangusha kiongozi mzuri sana ambaye anasifiwa hata na raisi, imebebwa na usalama wa taifa, wala si mimi. Nilimwambia hivi Tino.” Sabrina akamgeukia Max vizuri.

“Nilimwambia, sijui ni kwa nini Mungu alinikutanisha na yeye akiwa kwenye ile hali ambayo Mungu alitaka kunitumia kumtoa pale. Nikamwambia, nilitoka kwenye maombi ya karibia mwezi. Hivi unaelewa Max? Mwezi mzima mimi nakula mara moja tu kwa siku, tena nikiwa nafanya kazi ngumu sana, nikimuomba Mungu anisaidie anitoe kwenye ile hali. Halafu eti Mungu ananitoa kwenye kutunza ngombe, kusafisha mavi ya ng’ombe na kutibu madonda yao, majibu ya Mungu ananipeleka kwa Tino aliyekuwa amejawa madonda na kinyesi mwili mzima! Sijui kama unanielewa Max?” Sabrina akauliza kwa ukali.

“Yule ambaye ulikuwa ukimfundisha anikimbie, na kumwambia endapo nitafanya madai kwake, utamtengenezea kesi na kunishinda. Yule uliyekuwa ukijinufaisha na pesa yake bila kumjali yeye mwenyewe, na kutumia uovu wa moyo wake vizuri sana, ukimpandikizia chuki dhidi yangu, nilimtoa kwenye mauti. Au nisema Mungu alinitumia kumtoa kwenye mauti. Alijawa nywele mwili mzima kama mnyama wa porini! Alijawa kinyesi kilichogandana na madonda, mikojo! Hata mkewe alinizuia nisiingie kwenye chumba chake. Lakini mimi nikamtii Roho wa Mungu. Nikaingia chumbani kwake, nikamsaidia Tino. Sikuwahi kukusikia wewe wala mkeo mkija pale kumsalimia wakati mlijua ni mgonjwa. Ukasubiri nilipomrudisha tena kwenye uhai, mkaanza kumtumia tena ili kujinufaisha.” Sabrina alijawa jazba. Akawa mkali, mpaka Max akaogopa.

“Basi Sabrina. Mimi nilitaka...” “Nakuamuru ukae Max, unisikilize mpaka nimalize. Lasivyo nitahakikisha unarudishwa kwangu unisikilize kwa lazima. Usinitanie. Umekuja hapa mwenyewe tena bila kukuruhusu kukaa, umekaa. Sasa nakuamuru ukae mpaka nimalize ndipo nitakuruhusu. Usinifanye mimi mjinga. Nilinyamaza nikiwa nakujua sana kuwa wewe ni mbaya Max.” Max akarudi kukaa, kwani alitaka kuondoka watu walipoanza kuwageukia.

“Hivi unajua nilikuwa silali?” Sabrina akaanza tena. “Mchana na usiku nilikuwa silali nikimuhudumia ‘chanzo chako cha pesa’, aliyekuwa hawezi hata kushika kijiko! Mimi nilihangaika naye kutafuta jinsi ya yeye kujisaidia bila kinyesi na mkojo kumshika mwilini. Nikamtibu madonda na kumsafisha kutoka kwenye hali aliyokuwa nayo kama mnyama wa porini, mpaka akarudi kuwa Tino aliyekuwa akikulipa wewe mapesa mengi, mimi sinufaiki naye mpaka mwisho wakati unamshauri jinsi ya kuniacha! Mikono hii miwili, bila pesa, kwa kutumia akili na uwezo wa Mungu, vilimfufua Tino. Na ndipo nirudi kwa kile nilichomwambia Tino mwanzoni kabisa wakati nikimfariji na kumtia moyo mpaka pressure yake ikapona. Nilimwambia hivi, sijui ni kwa nini Mungu amenipeleka pale wakati nilikuwa nafanya kama kile anachotaka tena nikifanye. Tena nikiwa nimeomba kwa muda mrefu sana, lakini, nikamwambia Tino sasa, nitafanya kwa uaminifu bila kuchoka, bila kumfanyia yeye ubaya, kama nafanya kwa Mungu mwenyewe.” Sabrina akatulia.

“Unanielewa Max?” Kimya. “Nilimwambia na ndivyo nilivyofanya kwake, kwa uaminifu wote, kwa kuwa Tino hakuwa hata akiweza kuzungumza. Sikuwa namjua hata sura kwa kuwa kama nilivyokwambia, alijawa nywele kama mnyama. Usingeweza kumsogelea wewe Max. Nina uhakika kabisa. Alikuwa anatisha mno. Tino anapona, ndipo nakuja kugundua kumbe anao uzuri wa kibinadamu! Sikuwa nikijua namtunza mtu wa namna gani! Lakini Max, nilinyenyekea kwa yule kiumbe, vile alivyo kama namuhudumia Mungu mwenyewe. Mchana, usiku bila kuchoka wala kunung’unika ila mkewe kunishauri kumuacha. Na mkewe alipoona simuachi, naye akanikimbia akiwa ameniachia mgonjwa mahututi. Lakini nilimwambia Tino, nitamdai Mungu wala si yeye.” Sabrina akacheka.

“Paliponishangaza zaidi vile njia za Mungu zilivyo za ajabu, eti Tino ananiacha hospitalini mimi mgonjwa na dripu inanining’inia! Ananiacha hospitalini na kunidai vitu vyake!” “Hiyo mimi sikujua Sabrina?” “Acha unafiki Max! Wewe ulimshauri Tino ahakikishe wakati anaondoka akiniachia gari lake anirikodi nikiwa nakiri kuwa gari lake ninalo na anirikodi nikiwa nakubali kumpa mtu atakayemtuma kuja kulichukua. Kanusha Max.” Max akashituka sana. “Nakwambia hivi, nilikuwa nikijua na kufuatilia kila mazungumzo yenu Max. Mpaka nikawa namuuliza Mungu, ni kwa nini anaruhusu hata tu ile kujua ubaya mnaopanga dhidi yangu wakati sijawatendea ubaya ila wema!” “Lakini mimi sikumwambia akupokonye ukiwa mgonjwa.” Max akajaribu kujitetea.

“Unabisha nini Max wewe!? Tino aliniacha kama ulivyomshauri wewe. Tena bila kujali nitakwenda wapi wakati alinipeleka mji wa ugenini kwa ajili ya kumuhudumia yeye mwenyewe! Aliniacha nikiwa sijui pakwenda na wala sijui chakufanya! Kama mwanadamu nikaumia sana. Roho wa Mungu akanikumbusha ninayemdai si Tino wala wewe, ni Mungu. Ndipo nikasamehe, na kumgeukia sasa kumdai mdeni wangu. Nilimlilia Mungu, Max! Mchana na usiku nikimwita bila kuchoka kwa kuwa kwanza nilikuwa siwezi kulala tena kwa hofu. Kazi ikabakia kumuita Mungu anitetee. Bila kula wala kunywa maji, nilimuita Mungu wangu mpaka akanitumia Jack.” Sabrina akakaa vizuri.

“Huyu Jack uliyetaka kumdhuru huyu, ni Mungu wangu hapa duniani. Mungu anamtumia kunilipa hapa duniani. Pengine hujaelewa kama mimi mwanzoni. Ninapomuona Jack mume wangu na yale anayoyafanya kwangu, namuona Mungu akinilipa Max. Umbali ule niliokwenda kwa Tino na kukunufaisha wewe, ndio anakwenda Jack mpaka mimi naogopa! Jack ni Mungu aliyepo kazini. Huna utakalopanga dhidi ya Jack ukafanikiwa Max. Nakuhakikishia na ninakwambia, umecheza na Mungu, na wala hatakuacha kwa kuwa unajaribu kusimama kwenye kusudi la Mungu, ndio maana wakati wote umekosa, hujalipwa kama safari hii.” Sabrina akaongea kijasiri.

“Kama unafikiri upo matatizoni, umekosea Max. Bado. Ulikuwa ukitayarishwa tu, na kutambulishwa kuwa, umecheza na moto. Wewe si ni mzuri wa kutengeneza kesi, nakushauri jipange. Huna utakapokimbia au utakapojificha, usionekane. Hata hapa ulipo sasa hivi, unajulikana upo hapa. Nina uhakika barua yako ya restrain kama aliyopewa Tino, inakuja.” Max akazidi kuingiwa hofu zaidi. “Hiki ulichokifanya hapa, ni kosa ambalo Jack alikuonya uwanja wa ndege siku ile, ukakasirika na kwenda kupiga simu za uchochezi dhidi yetu. Kwa kuwa wewe ni mkorofi, umekiuka alichokuagiza mume wangu, akikuonya ukae mbali na mimi, umemdharau.” “Hapana Sabrina. Nimekuja kwa amani kabisa. Mungu wangu ni shahidi.” Sabrina akazidi kukasirika.

“Amani ipi Max!? Unatafuta amani baada ya kukamatwa! Ubaya wote ule uliokusudia kuufanya dhidi yetu kama usingekamatwa si ungetenda tena kama ulivyonitenda mimi nilipokuwa Moshi?” Max kimya. “Upo hapa kwa kuwa umekamatwa. Halafu najiuliza Max, hata kama unapenda pesa kiasi hicho jamani! Kwa nini umenuia kuniangamiza mimi kwa kiasi hicho!? Nilikukosea nini Max wewe isipokuwa kukuheshimu wewe na mkeo?” Sabrina akaanza kulia. “Ulipanga mipango mibaya sana, ya hila ili Tino aniache. Sikulalamika kwako wala kukuuliza. Nikakuachia Tino. Ukaenda umbali wakumwambia ahakikishe haniachi hata na ujauzito. Ukamtafutia mpaka daktari wa kunitoa mimba. Ukahangaika mpaka ukafanikiwa na hilo. Tena unarudi tena kuja kumtaka Tino anifanyie fujo! Unataka nini kwangu Max?” “Naomba utulie Sabrina.” Pendo akajaribu kumtuliza.

“Hapana dada. Hujui huyu mtu kitu alichonipokonya. Wala si kwa Tino, ila sasa hivi amevunja familia yangu dada. Nilitaka familia moja, ya baba mmoja tu ambaye atajulikana kote mpaka kifo, kuwa ni Jack. Lakini huyu mwanaume amenipokonya dada! Kulikuwa na amani, yeye amevuruga tena. Kila nikitulia sehemu, ananifuata kunitenda ubaya mkubwa sana. Hayupo hapa kutafuta amani, yupo hapa kwa kuwa safari hii uovu wake umefika mbele ya kiti cha enzi cha Mungu wangu, amekamatwa ndio unamuona hapa. Ni muuaji huyu dada. Simaanishi muuaji wa maneno, namaanisha mmwaga damu kabisa wa vitendo. Hawezi kuniona nimetulia mahali nina amani, akatulia. Lazima avuruge kwa manufaa yake. Sasa hivi mambo yamekuwa makubwa mno! Mambo yaliyokuwa yametulia. Ameyachokonoa chokonoa mpaka yamekuwa makubwa! Tena ni yeye mwenyewe aliyaanzisha tukiwa Moshi, nikaamua kumuachia Mungu tu. Unarudi tena nyuma nyuma kuvuruga!? Ni nini unataka kwangu wewe mtu? Kwa nini unaumia kuniona nimetulia!” Sabrina akazidi kulia.

“Hakika Mungu akulipe Max mpaka ujue ni Mungu anashugulika na wewe. Umenionea vyakutosha. Ubaya wako, uovu wako na dhuluma mlizokuwa mkifanya na Tino mkijinufaisha moja kwa moja kupitia mimi, Mungu anashugulika na wewe. Ubaya uliotaka kunifanyia mimi, mume wangu na watoto wetu, unakurudia wewe na familia yako. Hutatoka hapo, kwa kuwa kila siku inayokwenda kwa Mungu, unapikwa, ukishamalizwa kwenye vyombo vya usalama, ulimwengu utakutambua, na utakuwa fundisho Max.” Sabrina akaongea kwa hasira na uchungu sana. Akajifuta machozi.

“Hakika hutasimama Max. Na Jack alimwambia Tino, atawashugulikia nyinyi wawili, mpaka anamalizana na wewe, hutakaa ukawa na uwezo wa kumdhuru au kutumia usomi wako kumuangamiza mtu mwingine tena na wala ukawa na uwezo wakusimamia kesi ya mtu hapa mjini ila kubeba jembe na kurudi migombani. Akamuhakikishia Tino ambaye amekimbia.” Max akashangaa mpaka usoni akaonyesha. “Hajakuaga eeh!” Sabrina akamkejeli. “Mwenzio alipopata tu ujumbe wake kuwa ushahidi wake wote upo, na atashugulikiwa kikamilifu. Jack akamwambia mpaka anamalizana naye, atajua Sabrina si tambaa lakufutia matapishi kila akihitaji. Aliposikia hivyo,  akasalimu amri. Sasa bado wewe mchochezi, unayejinufaisha kwa kupitia machozi ya watu, hukumu yako inakuja Max. Damu uliyokusudia kuimwaga bila hatia kule Moshi, yale mauti uliyoita kwangu kule Moshi, inakuwinda wewe na familia yako. Imekusimamia mlangoni, ikikutaka kukumaliza wewe na familia yako kama ulivyofanya kwangu na Tino. Mungu anakulipa. Nimemaliza, naomba utupishe na siku nyingine, usirudie kunivizia kwenye mahoteli.” Max akasimama na kuondoka kimyakimya.

Hakuna Msiba Usiokuwa Na Mwenzie!

S

abrina akiwa na hasira vilevile akageukia chakula chake ili ale, hata hakumeza chakula alichoweka mdomoni, akaanza kujisikia vibaya. Jasho likaanza kumtoka. Najisikia vibaya da Pendo. Moyo unaenda mbio mpaka naona shida kufungua macho!” Pendo akaingiwa hofu, akamuita muhudumu. “Naomba...” Kabla hajamaliza, Sabrina akakaa chini kabisa sakafuni. “Sabrina!” “Najisikia vibaya dada. Sitaki nianguke nimuumize mtoto wangu. Usigope, ila naomba mpigie simu Jack.” “Nikupeleke hospitalini?” “Jack kwanza dada.” Sabrina akasisitiza. Pendo akampigia simu Jack kwa haraka.

“Sabrina anajisikia vibaya, lakini amesema nikupigie kwanza wewe simu.” “Nipe nizungumze naye.” Pendo akamkabidhi simu Sabrina. “Vipi Brina, mama!?” Jack akaanza kwa wasiwasi. “Najisikia vibaya sana Jack. Mapigo ya moyo yanakwenda mbio, hii hali haijawahi kunipata. Na ninapatwa kizunguzungu!” “Ngoja nimpigie simu baba watume gari. Usikate.” Ndani ya nusu saa gari ya wagonjwa ya usalama wa taifa na mama Msindai, Mzee Msindai na Jacinta wakawa wameshafika hapo Masaki walipokuwa wamekaa wakila.

~~~~~~~~~~~~~~~~

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment