“Mungu
amekurudishia na zaidi. Si Willy tu, na watoto.” Pendo akacheka na kujifuta
machozi. “Wakati ule ilikuwa hata haileti maana!”
Pendo akaongea na kushika tumbo lake, akajifuta machozi. “Mambo ya Mungu huwa
hayaelewiki kwa akili za kibinadamu.” Pendo akanyamaza. “Ulisema kuna kitu
ulitaka kuzungumza.” Pendo akavuta pumzi kwa nguvu na kucheka kidogo. “Majuzi nilipata muda wakufikiria sana. Nikakumbuka
mwanzo wangu na Willy. Najua alikosa, lakini Willy amenibeba jamani!” Machozi
yakaanza kumtoka tena Pendo. “Alinibeba mpaka nikawa nashangaa! Alisimama na
mimi akinitetea kwa ndugu zake hata kwa mama yake bila kuchoka. Na wala Zelda
hakuwa msichana wa kwanza mama yake kumtafutia Willy. Walitafutwa wazuri na
warembo tu, lakini Willy alikuwa na msimamo akisimamia agano alilonipa si siku
ya ndoa, zamani sana tukianza mahusiano tukiwa
chuoni.” Pendo akaendelea taratibu.
“Tokea
chuo, mimi ni shahidi wa Willy, wasichana walikuwa wakimtongoza kwa siri,
lakini Willy alibakia kuwa mwaminifu kwangu. Hata tulipojua mwenye tatizo
linalosababisha tusipate watoto ni mimi, bado Willy alisimama na mimi. Aliniambia
hivi, sijui kama atakumbuka! Kuwa ni bora abaki na
mimi mpaka kifo, kuliko watoto bila mimi.” Willy akabaki ameinama. “Na ndivyo ilivyokuwa kwa Willy. Yeye hakuwa na wasiwasi
kama mimi. Aliridhika, ila pressure ya familia ndio nahisi ilimzidi. Willy ni
mwaminifu sana na ananipenda bila kujitahidi. Hilo sina shaka nalo.”
Pendo akacheka na kujifuta machozi.
“Ninachotaka
kusema ni hivi mchungaji, unatujua sisi. Kile ulichokuwa ukikiona hapa kanisani
ndicho kilichokuwa nyumbani. Hatukuwa na matatizo ya siri. Na hata alipoanza
mahusiano na Zelda...” “Hayakuwa mahusiano Pendo!” Willy akakanusha. “Basi
niseme hata ulivyoanza kulala na Zel..” “Haina nafuu Pendo.” Willy akamkatisha
tena kumsihi aache tu. “Basi niseme hata Zelda alipoingia kwenye picha,
hapakuwa na utofauti nyumbani. Willy alijua Zelda amebeba mtoto wake, lakini
bado aliendelea kuwa mtulivu nyumbani, japo niliona mabadiliko, ila nakiri
kulikuwa na heshima kubwa tu. Willy ananiheshimu. Sijui kitakachotokea mbeleni
kati yetu, lakini...” “Hakuna kingine kitatokea mbele yetu Pendo.” “Usiseme
hivyo Willy. Sisi ni binadamu.” “Labda kifo au wewe unigeuke. Mimi nimejifunza
kutokana na kosa.” Pendo akamwangalia, akaamua aendelee.
“Anyway,
ninachotaka kusema ni kuwa, najua wapo wanandoa wanatoka nje ya ndoa na
kuumizana sana kipindi hicho wakiwa na mahusiano ya nje. Najua pia ndoa
zinachangamoto zake nyingi, lakini nilipenda ndoa yangu. Nampenda Willy. Kama
Mungu akitusaidia tukarudi kwenye ndoa ya namna ileile, nitashukuru. Ningependa
watoto wangu wazaliwe na kukua kwenye mazingira ambayo Willy yupo kwenye maisha
yangu. Waone na kuonja ule upendo alionao. Tabia ya uadilifu na kujituma katika
mambo. Kwa hiyo nilikuwa naomba utusaidie ikiwezekana wanangu wazaliwe tukiwa
ndani ya ndoa.” Pendo akaongea kwa upole. Akawa amemaliza.
Mchungaji
akavuta pumzi kwa nguvu na kujiweka sawa kitini. “Na mimi naahidi hutakaa
ukafungisha tena ndoa yangu na Pendo. Hii ni mara ya pili na ya mwisho kwa kuwa
haitakaa ikavunjika tena.” Mchungaji akacheka akimtizama Willy. “Unauhakika
Willium?” Mchungaji akamuuliza. “Kwa asilimia 100.” “Labda nikuulize Willy.
Nijibu tu bila kuuliza au kwenda mbali na swali.” “Sawa.” Willy akakubali.
“Watoto
aliobeba Pendo ni wa miujiza haswa. Hilo kila mtu anajua mpaka madaktari wake
kama sikosei, si ndio?” Pendo akatingisha kichwa kukubali. “Siombei kitu
kitokee. Lakini hawa watoto ni wa Mungu na nyinyi mmepewa tu dhamana. Sasa je,
mwenye nao akiamua kuwachukua?” “Inamaana mimba itoke na watoto wafe?” Kama
kawaida ya Willy akaenda kulitengeneza swali na kuliweka wazi kabisa. “Ndiyo.”
Ikabidi mchungaji akubali tu. Pendo kimya. “Nakujibu jibu ambalo nilimjibu
Pendo mwenyewe na ndugu zake. Sijarudi kwa Pendo sababu ya watoto. Nimerudi kwa
Pendo kwa sababu amenipokea. Angenifukuza Pendo, na akaniambia watoto alionao
ni wangu, ningewatunza bila shida na yeye angeendelea na maisha yake na mimi
hivyo hivyo. Mimi bado nikijana mchungaji. Kama mzee Ngoi mpaka leo anaweza
kuoa, nashindwaje mimi!?” Hapo Willy akawa ameongea uhalisia.
“Kwa
hivi nilivyo, ninauhakika ningeweza kutafuta mwanamke mwingine yeyote nikaoa na
nikaanzisha familia bila shida. Lakini Pendo ni Soulmate wangu. Hakuna
jinsi nikawa nafuraha na mwanamke mwingine, nikijua Pendo wangu yupo! Narudia
tena, labda ingekuwa Pendo amenikataa. Kwa hiyo nipo hapa mbele yako si kwa
sababu ya watoto aliobeba Pendo, ni kwa sababu ya Pendo wangu. Nampenda
Pendo. Japo sitaona haya kusema nimefurahia kumkuta Pendo na watoto. Hilo
sitadanganya kwa kuwa najua litampa utulivu Pendo mwenyewe aliyekuwa akiwataka
hao watoto mchana na usiku. Muulize Pendo kama mimi nilikuwa namsumbua kwa
swala la ujauzito!” “Amekiri mwenyewe.” Akajibu mchungaji.
“Na
ni kweli. Na penda watoto, lakini si kama Pendo. Nilifikia hatua mimi
nikamwambia Pendo, tena kwa kumuomba Pendo tuachane na maswala ya watoto, maana
niliona namkosa na Pendo mwenyewe! Kulia kila wakati, na kila nikiwa naye
anachozungumzia ni watoto tu! Nikamuomba tuache kabisa. Akalikubali hilo,
tukatulia. Nikaenda umbali wa kuonya kila mtu nyumbani, asizungumzie lolote na
mke wangu juu ya watoto. Wakakubali japo ilikuwa kwa shida na kubishana sana,
lakini wakaliheshimu hilo, angalau tukatulia. Muulize Pendo kama kuna hata mtu
alimsumbua tena juu ya watoto.” Pendo kimya.
“Nikashangaa
wakati Zelda ni mjamzito, akaanza tena kitu ambacho tulishafunga mjadala.
Akaanza tena habari za watoto wakati mpaka nilimwapisha asizungumzie tena swala
la watoto isipokuwa mapenzi yetu sisi tu wenyewe. Tukakubaliana wakija sawa,
wasipokuja pia ni sawa. Na kweli Pendo akatulia kabisa, na kurudia hali yake ya
zamani kabisa. Kwani maswala ya watoto yalianza kumfanya azeeke, mpaka usoni
alikuwa kama amechoka! Kwa mara ya kwanza alipolirudisha hilo la watoto nikawa
mkali kwake japo yeye anafikiri ilikuwa sababu ya Zelda. Lakini ni kwakuwa
nilijua itaanza tena shida ileile. Mahangaiko yaleyale wakati tulisharidhika.
Kumbe mwenzangu alikuwa akitembea kwenye imani kwa maombi aliyofanyiwa na
Sabrina! Ndiye aliyemrudishia tumaini la hawa watoto. Kwa hiyo naomba
nikuhakikishie mchungaji, mimi nitatulia. Na Mungu anisaidie.” “Hapo umeongea.”
Mchungaji akamalizia.
“Nataka
Sabrina anisimamie harusi. Ndiye aliyesimama na mimi kipindi nimeachika, na
ndiye aliyerudisha imani ndani yangu mpaka nikapata hawa watoto. Amekuwa
akiniombea kuanzia mwanzo mpaka sasa. Ni mtu wangu anayesimama na mimi mchana
na usiku. Ila anajifungua mwezi ujao. Nilitaka harusi kabla hajajifungua. Haitakuwa
kubwa, ndogo tu, lakini lazima Sabrina awepo.” Mchungaji akacheka. “Kisheria
nilazima tutangaze. Tupange tarehe ya harusi, na tuanze matangozo angalau hata
mara mbili tu kuweka nafasi kwa uma.” “Sawa.” Wakazungumza hapo ofisini kwa
mchungaji na kuweka tarehe ya harusi kabisa, wakatoka wakiwa wameridhika.
Wakampita Zelda hapo nje ya ofisi, wakaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Wakarudi
nyumbani wakiwa wamejawa furaha. Kwani hata walipokuwa kwa mchungaji waliombana
tena msamaha, wakasameheana. Mchungaji alizungumza nao kwa kina tu, na
kuwaombea. Wakatoka hapo wapo ukurasa mmoja, wamejawa amani wanazungumzia ndoa
tu. Pendo alipofika tu kitandani kwake, akaanza kupiga simu akitangaza tarehe
yao ya harusi. Pendo akataarifu ndugu zake wote akiwa amejawa furaha, akisema
haamini kama Mungu amemrudishia Willy wake. Alijawa vicheko na kilio kwa
furaha. Wakati Pendo anaongea na watu wake, Willy akatoka hapo chumbani.
Willy
akaanza kufikiria amtaarifu nani kwenye familia yake. Hawakutaka kualika watu
wengi, ni watu wa karibu tu na wenyewe mahusiano ya mara kwa mara sio ndugu
wakutafutana mara moja kwa mwaka! Hao walikubaliana wawaache. Hawakutaka kitu
kikubwa na wala hawakutaka kutumia pesa nyingi kulisha watu. Walitamani hata
wasizidi 30. Willy alikaa pale akifikiria ndugu zake, akaanza kuwachuja mmoja
baada ya mwingine. Ubaya waliomtendea yeye tokea alipokuwa na Pendo mpaka kuja
kumuuzia mbuzi kwenye gunia! Zelda! Wote akaona asiwarudishe tena kwenye maisha
ya Pendo kwa wakati ule anao tarajia watoto, na afya yake haijakaa sawa. Akaona
upande wake yeye asialike yeyote hata marafiki. Bado kazini alikuwa mgeni
hakuwa na rafiki wa karibu wa kiasi hicho. Akaamua atulie tu.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Na
huku kwa Sabrina na Jack walipopata tarehe ya harusi ya kina Pendo, ilikuwa
karibu kabisa na Sabrina kujifungua. Kama week hiyo hiyo. Ikabidi Jack kuweka
mipango ya kueleweka ya yeye na familia yake kuwepo Dar kwa muda wakutosha
mpaka Sabrina na mtoto huyo atakayezaliwa watakapokuwa tayari kwa safari ya
kurudi tena Singida. Wakawekeza nguvu kwenye kukamilisha nyumba. Na kwa jinsi
walivyoiona, haikuhitaji marekebisho mengi. Akamuomba shemeji yake amsaidie
kutafuta watu watakayoisafisha vizuri. Ndani na nje. Maswala ya maji na umeme
kuhakikisha pako sawa. Wakatuma kiasi cha pesa walichonacho na wanachotaka
kitumike kwenye hiyo nyumba. Joy akawaambia atawasaidia. Huo mpango ukakaa
sawa.
Kina
Jacinta, Nancy na Jena pamoja na wazazi wakawasaidia kuandaa hiyo harusi.
Kuanzia Pendo mwenyewe, mavazi na maswala ya saluni. Hawakutaka wasimamizi wa
watoto, lakini Joy na Junior wakabembeleza mpaka wakakubaliwa mtoto wao
asimamie. Kwa hiyo wakagaramia mtoto na maua. Wakati huo Willy anatafuta sehemu
ya fungate.
Hakuna Msiba Usiokuwa na
Mwenzie.
W |
akati
ofisi za serikali zinahamia Dodoma mji mkuu wa Tanzania, mama Kundi na baadhi
ya wenzake wakabahatika kubakishwa Dar. Likawa jambo la furaha kwa kuwa
hawakujua ingekuaje kwa familia kutengana. Lakini wakiwa kwenye hofu ya
Msindai, na bosi wake akipita na kuendelea na shuguli zake bila kuonyesha kuna
tatizo lolote lile, siku ya alhamisi mama Kundi akapokea barua ya uhamisho.
Barua ilimtaka akaripoti katika kituo kipya cha kazi kwenye ofisi zao jijini
Dodoma, jumatatu inayofuata. Alishituka karibu kuchanganyikiwa. Akatamani
kumpigia simu Max, lakini akaogopa tena mawasiliano yao yasije kamatwa.
Akaamua
kwenda kulalamika kwa meneja wake. Meneja akamwambia ni agizo lililokuwa
limetolewa kutoka zamani kuwa serikali ihamie Dodoma, ila wao walikuwa
wakitekeleza kwa awamu. Zamu yake imefika, anatakiwa akaripoti kazini.
Akamshauri kama anayo malalamiko yeyote yale, aandike barua kupinga agizo la
kuhamia Dodoma. Mama Kundi alikuwa kwenye hali mbaya kwani biashara zake zote
zilikuwa jijini Dar. Anaondokaje kuacha biashara zake, mume na watoto
wanaosoma! Nani atasimamia nyumba yake! Lakini alitakiwa aondoke, au aache
kazi. Kuacha kazi napo ikawa ngumu kwani alishatumikia serikalini kwa miaka
mingi sana. Kuacha kazi kwa kukataa kazi ni kupoteza haki zake nyingi sana ambazo
angepewa kama angesubiri mpaka kustaafu kwake!
Kwa
Tino.
Alibakiwa
na ile hali mpaka alipotoka kazini bila kumtaarifu yeyote kwa simu kwa hofu ya
kusikilizwa mazungumzo yao. Hofu ilizidi kuwaangia walipofika wote nyumbani na
kuzungumzia hiyo hali na kinachowakabali. Hapo ndipo wakajua maji yamezidi
unga. Waliotangulia wametangulia, na kina Msindai wanacheza mchezo wa kiutu uzima,
kihalali kabisa. Wakajua wao wameshika kwenye makali, wanaumia. Mama Kundi na
mumewe ikabidi sasa kumfuata Tino wazungumze na wajipange.
Wanafika
kwa Tino, wakagundua na Tino naye alishapewa barua kutoka kwa mwanasheria wa
Msindai. “Kwa nini hukuniambia!?” Max akalalamika akishangaa. “Hapa
nimechanganyikiwa, nilikuwa nikifikiria jinsi yakujipanga upya.” Ndipo wakaomba
kusoma barua yake. Baada ya kuwazungusha kwa hili na ile akishindwa kuwaonyesha
barua yake, Max akahisi lipo jambo.
“Nini
kinaendelea Tino?” “Mimi nilikuwa Cliff kwa mambo yangu ya kikazi. Ndipo
nikawaona wanangu na Jack. Hakika ile ni damu yangu. Ilikuwa ni birthday yao
yakutimiza mwaka! Nikaumia! Nahisi ni kupaniki, nikatafuta muda ambao
wametoka katikati ya kundi ambalo walikuwa wamekusanyika kwa ajili hiyo, mimi
nikawafuata. Mambo hayakuwa mazuri, nikapaniki na kuongea hata
ambayo sikuwa nimekusudia. Nikawatisha nikitumia ushawishi wako kwangu
kuwa nirudi huku nchini, tuwadai hata kisheria wale watoto ni haki yangu
na mimi. Hapo ndipo nafikiri yule jamaa akakasirika sana. Kaka yake akaja,
akanikuta nimesimama nao pale tunaongea.” “Kaka yao waziri Msindai!?” Wakauliza
kwa pamoja. “Ndiyo.” “Basi wewe ndio umeharibu Tino.” Wakaanza kumlaumu Tino
kwa kumshambulia.
“Hebu
subirini kwanza!” Tino akawakatisha kwa kuwashangaa sana tena kwa ukali. “Mbona
mnataka kunichanganya sasa hivi? Maswala kama nina watoto huku nchini niliyatoa
wapi kama sio wewe Max kunipigia mwenyewe!?” Tino akauliza kwa
ukali. “Tena ulinipigia simu kwa
ushawishi mkubwa sana ukitaka nirudi kudai watoto wangu na ukaniambia unayo
mipango mizuri tu. Ulinishawishi na kuniambia ninahaki kisheria kudai watoto
wangu! Nimekutana na kina Jack na Sabrina. Nikaeleza nia yangu juu ya watoto
wangu. Kaka yao alikuja mwisho kabisa tumemaliza mazungumzo. Akauliza kama ni
kwema, mimi nikaondoka bila hata yakujibu. Sasa kosa langu lipi!?” Tino
akawashangaa kwa ukali.
“Wale ni ndugu Tino! Unafikiri
hawatazungumza?” Akauliza mama Kundi
akiwa amepoa sio jazba tena ila akilaumu. “Halafu na mazungumzo yetu tulimtaja
huyo waziri, kama watu wa usalama walinyaka hayo mazungumzo na kumpa Jack,
unafikiri watashindwa vipi kumfikishia waziri mwenyewe!” “Subiri kwanza Max.
Msitake kunichanganya mimi!” Tino akawakatiza tena. “Unazungumzia nini!? Mimi
na wewe hatukuzungumzia swala lolote juu ya waziri, isipokuwa watoto wangu.
Maswala ya waziri mimi sipo kabisa na sifahamu ni nini mnazungumzia!” “Ni mimi
na mke wangu.” Max akajibu akiwa amepoa kama aliyeishiwa ujasiri. “Hapo sasa
sijui! Huko sipo. Mimi nimedai wanangu kama ulivyonishauri, basi. Sikutishia
familia ya Msindai.” “Kwa nini hutaki tuone barua yako Tino?” Akauliza mama
Kundi. “Nahisi haiwahusu.” Wakashangaa sana.
“Tokea
lini mambo yako hayatuhusu wewe Tino?” Akashangaa sana mama Kundi. “Isingekuwa
kukuthamini, wala usingekuwa hapa leo! Max alikufanyia uungwa kukutaarifu swala
la watoto, leo unamkana!” “Hapana. Alifanya kwa ridhaa yake na sababu zake
anazozijua yeye mwenyewe. Mimi nilishamwambia watoto ni wa Sabrina! Kwa
nini yeye aliendelea kuning’ang’ania, akinitafuta hata nilipomkatia simu!?” Hapo ukalipuka ugomvi haswa. Kukanana
kukaendelea. Mama Kundi akilia na kutukana wote wawili. Max mumewe, na Tino
ambaye alimuita hana shukurani na ndio maana Lela alimtenda. Wakagombana haswa!
“Subiri
kwanza mama Kundi. Naona unakwenda kusiko kweli.” Hapo Tino akaamua kuvua
uvivu na kuzungumza. “Mimi sijui huwa mumeo anakwambia nini au alikushirikisha
nini juu ya kesi yangu, lakini nipo hapa, hivi unavyoniona peke yangu kwenye
hili jumba, sababu ya ushauri ambao najutia sana kuusikiliza na
kuutendea kazi, kutoka kwa mumeo.” Tino akaendelea akiwa anatetemeka kwa
hasira. Max akataka kukana, akamkatisha. “Kwanza nilikushangaa sana
uliponipigia simu na ndio maana nikakukatia simu. Ni kama unayetaka
kunichanganya tu.” “Kivipi wakati mimi ndiye niliyekusaidia?” Max akahamaki.
“Katika
lipi na sasa hivi unataka nini?” Tino akauliza kwa ukali. “Ni wewe mwenyewe
uliniambia niachane na Sabrina.” Mkewe akashangaa sana. “Haiwezekani Tino! Wewe
ni muongo. Mpaka leo Max hajui kilichotokea kati yako na Sabrina!” Tino
akashangaa sana. “Unanitania mama Kundi!? Ndivyo anavyokudanganya mumeo?” Mama
Kundi akatulia kidogo na kumwangalia mumewe.
“Sikumleta
kwenu Sabrina na kuwaambia nimepata mwanamke anayenipenda na kunijali?” Tino
akauliza na kuendelea. “Umesahau mama Kundi tulitoka kwenu tukiwa tunakwenda
kuanza upya?” “Mpaka nikawapa na ushauri!” “Basi mumeo alikuja kubadilika
kabisa na kunishauri tofauti na hivyo. Akanishawishi na kunichanganya kabisa.
Yaani simu yake ya mwisho akinishawishi nirudi kudai watoto kuna sehemu kidogo alijichanganya
ndipo ikabidi kuanza kujipa muda kwa upya na kukumbuka neno moja hadi jingine
juu Sabrina, kwangu. Mumeo, anaakili sana. Yaani nikitafakari sasa hivi, huwa
nashangaa mpaka mapigo ya moyo yanabadilika! Najiuliza, hivi ilikuaje!
Hakika sijapata jibu mama Kundi! Kutoka kwenye kumpenda Sabrina, alihakikisha
anatembea na mimi hatua kwa hatua, akinipa shutuma chungu sana za Sabrina,
mpaka akanifikisha sehemu nikamgeuka Sabrina na kumuacha Sabrina kabisa.
Tena vibaya sana.” “Haiwezekani!” Mama Kundi akapinga akimtetea mumewe.
Tino
akacheka kwa masikitiko akaendelea kama anayejaribu kukumbuka hila za Max.
“Hakika wewe ni kiboko Max! Mimi ni mjinga kwa kukusikiliza ushauri wako wa
kinyama, lakini wewe ni katili aisee! Yaani alikuwa ananikaba, sihemi,
akisema nihakikishe sifanyi kosa la kumuacha Sabrina na mimba yangu.” “Kwa nini
aseme hivyo!?” Mama Kundi akauliza kwa kushangaa sana. “Wakati huu nimetulia
ndio naamini kile alichoniambia juu ya Sabrina hakikuwa cha kweli, japo sina
uthibitisho, ila kwa jinsi ambavyo nimeanza kuujua moyo wa mumeo kwangu kuwa ni
pesa tu wala si kunijali mimi, nahisi nia yake ilikuwa ni ashinde ile
kesi ili nimlipe ile pesa niliyomlipa. Alikuwa masikioni mwangu
masaa yote akiniambia maneno mengi ya kumchafua Sabrina kwangu akisema ni uchunguzi
ameufanya. Ila kila nikikumbuka ushawishi wake kwangu juu ya Sabrina,
hakika ni kosa langu mwenyewe kwa kuwa ni mimi mwenyewe nilishindwa tu kumsikia
vizuri kwa wakati ule. Nilichagua cha kusikia na kuamini.
Maana alikuwa akisisitiza sana akisema kama nishafanya kosa la kumpa Sabrina
mimba basi nirekebishe haraka kabla kesi kutajwa ili Lela asije nizidi
kwenye MALI, ikaonekana mimi ndiye nimetoka nje ya ndoa sio yeye.”
“Kwamba urekebishe kwa kutoa mimba!?” Mama Kundi akawa ameelewa ila anapingana
na ukweli. “Abishe Max sasa hivi.” Mkewe akamgeukia Max akitamani akanushe.
“Max?”
Mkewe akaita kwa ukali. “Haikuwa hivyo moja kwa moja.” “Acha kumdanganya mkeo
Max. Swala la kuwa Lela alikujia ofisini akiwa si mjamzito kama ilivyokuwa
imesemekana, kwa hiyo na mimi niwe makini kabisa tena nisirudi na
Sabrina Dar, lilitoka wapi?” “Haiwezekani Max!” Mkewe akasikika akiwa ameumia
sana. “Mama Kundi, mumeo ndiye aliyenishawishi na kusimamia
kumtoa mimba Sabrina. Sikuwa napumzika! Mchana, asubuhi na usiku yupo kwenye
masikio yangu akitaka nimsafishe kabisa Sabrina, asibakiwe na mimba
yangu ili tushinde kesi, huku akisema tuhuma nyingi za Sabrina ikiwepo
ya uchawi kwamba kwao ni wachawi pamoja na shutuma za Sabrina na dada
yake kunilia njama ili wampindue Lela, niwe na yeye Sabrina anufaike
na pesa yangu. Akanithibitishia Sabrina ni tapeli hana mapenzi ya kweli
kwangu, kama ilivyokuwa ikionekana. Sasa ili kumzibiti ni kumtoa mimba asije
rudi na watoto na kunidai mali!” “Mungu wangu Max!” Yule mama akazidi kuumia.
“Na
hakutulia Max mpaka alipohakikisha nimemfikisha Sabrina hospitalini kwa daktari
wa kutoa mimba ambaye ni yeye mwenyewe Max alinisaidia kumtafuta. Sijui
alimpata wapi, lakini alinipa jina na namba za simu. Wakakubaliana na
huyo daktari mpaka kiwango cha pesa cha mimi kumlipa huyo daktari kwa
kazi ya kumtoa mimba Sabrina. Sijui Sabrina alifanya mchezo gani! Hakika mpaka
leo nimeshindwa kuelewa. Lakini mimi nilifanya kama Max, mumeo,
alivyoagiza. Kumpeleka Sabrina mpaka kwa huyo daktari wake wa kuua watoto wangu,
na nilimuacha Sabrina hospitalini akiwa amewekewa dripu kama mgonjwa kabisa
aliyetolewa mimba. Nikamuacha hapo maana Max aliniambia na hilo, nihakikishe
sirudi naye Dar. Kwa kuwa Lela anamsaka sana Sabrina kama shahidi wake. Akaniambia
nisije onekana na Sabrina popote pale. Basi nikamuacha Sabrina
hospitalini, akiwa kama mgonjwa na nikashuhudia ana dripu kabisa amewekewa ile
sindano ya mkononi.”
“Mpaka
leo nashindwa kujisamehe kumuacha Sabrina hospitalini wakati yeye aliniuguza
mkiwa nyinyi wooote, mmenisusa. Mkaja kurudi na ushauri wenu mlipojua
nipo hai, bado pesa yangu itawasaidia. Alichofanya Max mumeo ni kuhama tu
upande. Kutoka kula pesa yangu kwa kupitia Lela aliyekuwa akimsaidia madai
yangu wakati mimi nipo mahututi kitandani, na kuhamia upande wangu mimi
mwenyewe alipoona nimerudisha uhai, nachukua pesa yangu kwa Lela, na yeye
atakuwa upande wa Lela, usio na masilahi.”
“Anyways,
aliponifanya mumeo, nianze kufikira kwa makini sasa, ni ile simu yake ya
kurudi nchini nije kudai watoto, na kuendelea kunitafuta japo nilimkatia simu. Ikabidi nianze
kujiuliza kwa upya. Hivi huyu Max aliyehangaikia mpaka tiketi yangu kuhakikisha
narudi Dar bila Sabrina, baada ya kuua watoto wangu mwenyewe, inakuaje
tena mtu huyuhuyu aliyenishauri na kusimamia kuua wanangu hatua kwa
hatua, bila aibu wala huruma, iweje leo anarudi tena kuniambia nikadai
tena watoto walewale aliosema tuwauwe ili wasije rudi kudai MALI!
Hapo nikabaki kujiuliza bila jibu. Lakini nikajiuliza tena au huyu Max,
mwenzangu pengine kwa kuwa yeye watoto wake hakuna aliyemshauri awauwe na anaye
mke wake, ametulia kwake, ni kwamba amesahau au la! Lakini. LAKINI. Nikaja
kukumbuka tena pale aliponipigia tena simu ya kurudi kudai watoto wangu,
alibadilika tena pale nilipomwambia watoto si wangu ni wa Sabrina,
akanishauri tena tumtengenezee tena Sabrina kesi, tuseme wakati ule
nafanya yote yale sikuwa kwenye akili timamu, nilikuwa mgonjwa.” “Mungu
wangu!” Mama Kundi mikono kichwani.
“Yaani
tena mumgeuke tena sabrina huyohuyo!?” “Yeap! Tena si kumgeuka tu
Sabrina, hapo ukituliza mawazo na kufikiria, ni kwamba hata mimi ananigeuka.
Ananiambia yote yaliyotokea Moshi, yeye hausiki ni mimi tu.” Tino
akamjibu mkewe macho kwa Max. “Huo ndio ushauri kutoka kwa mumeo, huyo hapo
mpaka mimi mwenyewe nikamkatia simu. Na ndio maana mmeona nimerudi lakini
nimeshindwa hata kuwatafuta.”
“Namtafakari
mumeo sipati jibu! Najilaumi ni kwa nini nilimruhusu anifanye mimi kama mjinga!
Tena mjinga wa kiasi hiki! Hakika namuwaza Max mpaka silali kwa hofu. Na hofu
kubwa niliyonayo nahisi ni yale maovu yangu mimi mwenyewe. Halafu
kuja kuona hao watoto nilioshauriwa na mumeo niwauwe! Hakika
nimeshindwa kulala. Nakunywa madawa ya usingizi ili niweze kulala.” Tino
akazungumza kwa uchungu sana.
“Na
ndio maana hata nilipopata hii barua kutoka kwa kina Msindai, nilibaki kimya.
Kila nikiwaza, najuta na kubakia nikijiambia tatizo kubwa na aliyenifikisha
hapa mpweke hivi ni Max.” “Ni kweli ni Max!” Mkewe akaongea kwa uchungu sana.
“Max amenitenda kwa faida yake yeye wala si ya mtu mwingine. Amenishindia
hii nyumba lakini amenipokonya Sabrina ambaye nilimwambia wazi kuwa ni
mwanamke pekee aliyenipenda kwa dhati. Lakini Max alihakikisha
anamtoa kwangu vibaya sana na kuua watoto wangu! Leo anakuja nyumbani kwangu
anataka kujua kinachoendelea tena kwenye maisha yangu! Hakika ondokeni kabla
sijamuita mlinzi. Kama ulifikiri utatengeneza pesa nyingine kupitia kesi yangu,
hapana. Acha kwa mara ya kwanza, na mimi nifikirie kwa akili zangu
nikiwafikiria binti zangu na Sabrina ambaye ulinifanya nimtelekeze
vibaya sana.” Tino akasimama na kufungua mlango. Akamuita mlinzi. Mama Kundi
alipoona hivyo akasimama kwa haraka na kutoka. Max akafuata kimya kimya akijua
hata nyumbani kumeharibika.
~~~~~~~~~~~~~~~~
0 Comments:
Post a Comment