Wakati
wapo njiani kila mmoja akiwaza lake, Pendo akapata wazo. “Nashauri majibu ya
hii DNA tukayafungulie kwa mchungaji Swai na kuweka naye mipango yote ili kila
mmoja atoke hapo akiwa ameridhika, au unaonaje Zelda?” Willy akamtizama Pendo
na kurudisha macho barabarani. “Mimi nakushukuru sana dada yangu, maana
ingekuwa mtu mwingine kwa tulichokutendea, usingesamehe. Nilikuwa na mahusiano
na mumeo, nika...” “Hukuwa kwenye mahusiano na mimi.” Willy akapinga kwa jazba.
“Mimi
sijui wewe unaitaje! Naomba nisamehe. Lakini mimi namaanisha ile tu kulala na
wewe tena zaidi ya mara mbili na yeye kujua na kusamehe! Binafsi namshukuru.”
Pendo akanyamaza kimya na kugeukia dirishani. Willy akajua kimemuumiza.
“Chochote utakachonishauri dada yangu nitakusikiliza.” Zelda akaongeza kwa
unyenyekevu, Pendo akabaki kimya. Akarudisha mawazo kwa watoto wake, akaendelea
kujisugua taratibu tumbo lake. Pakatulia.
“Hongera
dada, naona na wewe Mungu amekujalia.” Zelda akavunja ukimya. Pendo akatamani
asijibu lakini akaona awe muungwana. “Asante.” Akajibu Pendo taratibu tu, Willy
akitamani amwambie asizungumze chochote huko nyuma alipokuwa amekaa. “Mungu
mkubwa, ndio maana mimi nimemgeukia. Nimeshajua maisha, nimeamua kutulia
kabisa.” Akaendelea Zelda taratibu tu. Kimya kwa Pendo na Willy wanasikiliza.
“Maana mama Ngoi alikuwa akinihakikishia kuwa nisiwe na wasiwasi kumbembea
mimba mumeo maana huna kizazi na wala hutakuja kuzaa.” Willy alitamani
kuchanganyikiwa, akafunga macho na kutingisha kichwa wakiwa wamesimama kwenye
mataa. Pendo kimya.
“Hata
wifi Stella na..” “Tafadhali nyamaza Zelda. Tafadhali sana.” Willy akamkatisha.
“Kwani nimeongea baya gani mimi! Nimemtukuza Mungu kwa kile alichokifanya!
Amemuabisha shetani na kazi zake. Sasa mimi nimekosea wapi!?” Zelda akauliza
taratibu tu. “Maana kuna kazi za Mungu. Akifanya jambo lake utajua tu, ana...”
“Nimekwambia nyamaza Zelda. Wewe ni mtu gani huwezi kusikia na kutii!?
Utapungua wapi ukinyamaza? Nimekwambia nyamaza, tafadhali nyamaza. Upo ndani ya
gari yangu mimi, nimekwambia nyamaza. Kamtukuze huyo Mungu wako sehemu nyingine
lakini si hapa. Umenisikia na kuelewa?” Willy akaongea kwa kugomba, Pendo macho
nje ya gari ametulia kimya. “Sawa. Na samahani kama nimewaudhi. Nia..” “Basi.
Nyamaza na usizungumze tena. Usiombe msamaha wala usieleze chochote. Sitaki
kukusikia hapa. Tukafanye kinachotupeleka hospitalini, basi.” Willy akamkatisha
kwa haraka sana tena kwa ukali. Zelda akanyamaza.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Walifika
hospitalini gafla Pendo akawa anajisikia kochoka kabisa kama asiyetaka kuwepo pale.
Akawa ametulia kabisa, amejishikilia tumbo lake. “Kwa kuwa leo ni jumapili,
sidhani kama tutachukua muda mrefu.” Willy akamwambia kwa upendo, Pendo kimya
akitembea kuelekea mapokezi. Wakaandikisha na kupelekwa kumuona daktari na
kufanyiwa vipimo, Willy akitumia kadi yake ya hospitalini. Waliambiwa vipimo
vitachukua siku tatu mpaka saba, Willy atapigiwa simu yakiwa tayari. Akaomba
hayo majibu yafungwe ili waje wayafungue pamoja. Kisha Pendo akawa muungwana.
Akahakikisha Zelda anapata daktari wa watoto. Akalipia matibabu yote, akampa na
pesa ya taksii yakumrudisha nyumbani kwake.
“Lakini
kabla hatujaachana, naomba nisaidie simu yako mara moja.” Willy na Zelda wakawa
hawajaelewa, lakini kwa pesa aliyopewa na msaada, Zelda akamkabidhi. Wakamuona
anapekua hiyo simu na kufuta namba ya simu ya Willy. Akatafuta kama kuna jumbe,
akafuta kila kitu mpaka mawasiliano na jumbe za zamani bila kusoma.
Aliporidhika hakuna alichobakisha cha Willy kwenye ile simu, akamrudishia.
“Majibu yakitoka, nitakupigia ili tukutane kwa mchungaji tuwekane sawa. Sijui
una swali?” “Naomba usimuulize hivyo Pendo. Wewe umeshahakikisha mtoto
ameangaliwa, hana tatizo. Umempa pesa zaidi ya nauli yakumrudisha tulipomtoa,
inatosha. Naomba tuachane kwa sasa.” Pendo akanyamaza. “Asante dada.” Akawa
kama amemkasirikia Willy, Zelda akaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Wakarudi
kwenye gari Willy akifikiria chakuzungumza. Pendo alikuwa ametulia kimya.
“Asante kusimamia hili na kuhakikisha linakamilika.” “Bado halijakamilika.”
Pendo akajibu. “Lakini hata ulichofanya mpaka sasa ni kikubwa na wazo la
kumalizana kwa mchungaji nimelipenda. Ni la busara na litatusaidia kuuwa ndege
wawili kwa jiwe moja.” Pendo akajua anajaribu kujirudi. Lakini alishakuwa
amechafuka moyoni kupita kiasi. Zelda alimtibua kupitiliza. Hakujua aseme nini
tena. Mpaka hapo hamu ya hiyo ndoa ilishamuisha. Akanyamaza bila ya kujibu.
“Nakupenda
Pendo. Nakupenda sana mpenzi wangu.” “Lakini haibadilishi kuwa umenisaliti
Willy!” Machozi yakaanza kumtoka Pendo. “Tena
uliniacha kwa sababu ya matatizo niliyokuwa nayo wakati tuliahidiana tutasimama
pamoja kwenye maisha yetu yote Willy! Uliniahidi tokea chuo kuwa utakuwa na
mimi katika maradhi na furaha, lakini ukanikimbia! Moyo wangu unauma sana na
nashindwa kupinga wazo la kuwa upo na mimi hapa sababu ilishindikana kwa Zelda.
Inamaana kama Zelda angekukubalia mkaanze maisha na wewe, kwa hakika usingekuwa
na mimi sasa hivi Willy. Najisikia mimi ndio chaguo la pili kwa kuwa huko
kulishindikana.” “Najua ni hasira tu Pendo, lakini nina uhakika sivyo
moyo wako unavyokwambia. Unazungumza kwa kupitia hisia zilizoumizwa. Lakini
moyoni unajua kwa hakika sina mwanamke ninayempenda hapa duniani isipokuwa
wewe. Najua hilo unalijua kwa hakika.” Willy akaongea kwa uhakika kabisa. Pendo
akanyamaza nakuendelea kujifuta machozi.
Jumapili
hiyo ikataka kuisha tofauti na walivyotarajia Pendo na Willy. Waliianza kwa
furaha hata wazazi wa Pendo wakijua wanakwenda kuandikisha ndoa. Lakini wawili
hawa wanarudi nyumbani hawaongeleshani! Walipofika nyumbani Willy akamfungulia
mlango wa gari, akashuka na pochi yake. “Asante.” Akashukuru Pendo kwa sauti ya
kinyonge, akaingia ndani moja kwa moja jikoni. Akajiwekea chakula chake na
Willy mezani, akaanza kula chake. Willy akaja, na yeye akaanza kula kimya
kimya. Pendo akamaliza yeye wa kwanza. “Nakwenda kuoga nijipumzishe mpaka
asubuhi. Usiku mwema.” Akaaga na kuondoka. Hawakuwa wakilala chumba kimoja
bado. “Asante na wewe.” Willy akajibu wakati Pendo akielekea kwenye chumba
kilichokuwa chao wote wawili.
Willy na yeye akaoga, akakaa chumbani
kwake akijiuliza hili na lile. Kwa hakika alimuhitaji Pendo, msichana
waliyekuwa wote miaka yote. Anampenda Pendo. Pendo amempokea na kumpa sehemu ya
kuishi bila shida. Willy hakutaka apoteze tena ile hali ya utulivu pale.
Akatoka na kumfuata chumbani kwake, akamkuta amelala. Amezima taa kubwa ya juu,
amebakisha ndogo ya mezani. Akapanda kitandani akajilaza akijua wazi hajalala.
“Samahani
nimekusaliti, nilitoka nje ya ndoa na kukuacha kipindi ukinihitaji Pendo.
Nisamehe nilikosa sana.” Kimya. “Kwa sababu yeyote inayokujia sasa hivi.
Unayosikia kutoka kwa watu, naomba ujue ni kweli nimekwama huko nje, lakini
nimekurudia wewe kimbilio langu. Najua ni kwako tu ndipo nitakuwa salama Pendo.
Ningeweza kujificha popote na aibu yangu, lakini nakujua utanisitiri aibu
yangu, utasimama na mimi kwa kuwa ndivyo ulivyokuwa ukifanya wakati wote.”
Willy akaendelea taratibu akimbembeleza.
“Katika
ahadi zetu tuliahidiana kuwa pamoja kwenye shida na raha. Nimerudi kwako nikiwa
nipo kwenye shida. Naomba usinitupe.” “Sikutupi Willy, ila nimekasirika.”
“Naomba nikukumbatie vizuri na kukubusu, pengine hasira itapungua.” Willy
alimjua Pendo, mpenda kubembelezwa. “Pendo?” Kimya. “Au umenichukia kiasi
hutaki nikuguse kabisa?” “Nataka Willy.” Pendo akajibu kwa kudeka, Willy
akajisogeza kwa haraka, akamkumbatia na kuanza kumpapasa taratibu. “Nisamehe
Pendo. Nataka tubaki pamoja.” “Na mimi nataka tubaki wote Willy, lakini bado
nina maumivu. Nipe muda naamini nitakuwa sawa.” “Ilimradi tupo wote, sina
tatizo. Nitakusubiri mpaka utakapokuwa tayari. Ila mipango ya harusi si
inaendelea kama kawaida?” Akamuona amenyamaza.
Akamnyanyua uso na kuanza kumbusu
midomoni kwa muda kidogo, kisha akamuachia. “Usibadilike bwana!” Akambembeleza.
“Labda tusubiri hili lipite Willy. Tusijichanganye.” “Naomba yote yatupite
tukiwa ndani ya ndoa. Nilikuomba Pendo. Naomba hasira isitutenganishe na
kusahau tulichonacho. Mwenzio nilizidiwa nguvu na kina mama. Lakini unajua
nakupenda Pendo. Nilisimama na wewe wakati wote! Tokea chuo mimi nilikuwa mtu
wako nikikuuguza ukiumwa tumbo. Usinisahau tafadhali.” “Siwezi kusahau.” “Basi
tufunge ndoa. Usibadili mawazo. Niangalie.” Pendo akanyanyua uso akamwangalia.
“Tuambiane
chochote kitakachotokea baada ya hapa, tutasimama pamoja kama Willy na Pendo
wale wa zamani. Ulisema hiki chumba hakijawahi kukosa kutupa majibu ya mambo
magumu. Naomba kisianzie kwangu. Nakuhitaji Pendo. Niahidi utaendelea kusimama
na mimi hata katika hili.” Akasindikiza na busu la muda mrefu, mikono ikasambaa
kila mahali kwenye mwili wa Pendo. Akamvutia kwake zaidi, hali ya Pendo
ikabadilika, akamkumbatia Willy kwa nguvu kama anayetaka amshike kwa nguvu
zaidi. Willy akaendelea kumpapasa kila alipofikia na kumbusu hiyo midomo kwa
utulivu. Midomo ikahamia kwenye shingo ya Pendo akaendelea na romance Pendo
akifurahia.
Gafla
Pendo akashangaa anamwachia. “Willy bwana! Ndio nini!?” “Safari hii honey moon
tunakwenda wapi?” “Bwana Willy! Malizia ulichoanza.” Willy akacheka na
kumfunika vizuri. “Honeymoon wapi?”
Willy akaendelea kuuliza. “Sijui. Lakini hatuwezi kusafiri. Na ninaomba
uondoke hapa. Unanitesa tu.” Willy akacheka na kusimama. “Ushanihakikishia
ndoa, kaa mkao wakusubiri.” “Kwani sasa hivi kuna nini?” “Uridhike sasa hivi,
ukose sababu yakusubiri? Nguvu hiyohiyo uitunze kule kwa mchungaji usimamie kwa
hekima zote atufungishe ndoa. Halafu ukafaidi honeymoon.” Pendo akamwangalia,
Willy akacheka na kutoka.
Jumatatu.
Jackson Msindai Afanya kweli
Kwa Max na Tino.
Kwa Max.
W |
akati Max
ndio amerudi tu nyumbani akizungumza na mkewe ambaye naye pia, ndio alikuwa
amerudi nyumbani kutoka kazini, mlinzi akawagongea kuwa wanamgeni na amesema
nilazima aonane na Max mwenyewe. Max akamwambia amkaribishe baada ya kuuliza
maswali na kujiridhisha ni mtu mzuri. Akafika mlangoni na kumuomba asaini kuwa
amepokea barua aliyokuwa ameshika mkononi. Max akiwa na mshangao akaipokea na
kusaini baada ya kujiridhisha ni yake kwa jina lililokuwa limeandikwa juu ya
bahasha. ‘Maximilliun Kundi.’ Mjumbe akaondoka,
Max akiwa amekunja uso akarudi ndani.
“Ni
nani na anataka nini?” Akauliza mkewe. “Ameleta hii barua.” Akajibu akiifungua.
Moja kwa moja akaenda kwenye kichwa cha habari. ‘SHITAKA.’
Max akashituka sana mpaka mkewe akamuona. “Vipi?” Akauliza mkewe lakini safari hii hakupata
jibu. Barua ilieleza dhumuni lakutaka kushitakiwa na Jackson Msindai kwa kosa
la kumpiga picha yeye akiwa na watoto wake bila idhini ya Jackson mwenyewe, na
kisha kuzisambaza kwa uchochezi. Nyuma yake ziliambatanishwa karatasi zenye
hizo picha zikuwa na siku, pamoja na muda alipomtumia Tino hizo picha. Na
ikaandikwa kuwa mazungumzo kati yake na Tino akimpa ushawishi akimtaka Tino
arudi nchini kwa haraka kuwadai watoto wa Jackson na Sabrina Msindai, huku Tino
akimthibitishia kuwa watoto si wake ila wa Sabrina. Ila yeye bwana Max aliendelea kumshawishi
kichochezi bwana Tino, aliambiwa mazungumzo hayo yapo yalinaswa.
Barua
ikaendelea kusema, hata mazungumzo kati yake na mkewe pia yalinaswa wakiwa
wanaweka mipango hatari tena yakutisha kwa familia ya Msindai, wakimlenga moja
kwa moja waziri wa Jamuhuri ya Muungano wa nchi ya Tanzania. Mwanasheria huyo
aliyemwandikia hiyo barua kwa niaba ya Msindai, alimthibitishia mazungumzo hayo
yapo na yalinaswa na watu wa Usalama wa Taifa. Ndugu Maximilian Kundi
akatajwa kama mchochezi, muharibu amani, na mtu hatarishi.
Max
alihisi kizunguzungu akakaa kwenye kochi la karibu. Mkewe akasimama na
kumpokonya zile barua. Akasoma. “Mungu wangu Max umeniponza wewe!” Mama Kundi
akashika kichwa. “Nilikuonya Max. Nilikuonya kabla hujaanza hii vita na kina Msindai,
mume wangu! Ni nini umefanya?” “Nilituma na kuzungumza nikiwa kwenye hasira!”
Max akajitetea akiwa ameishiwa nguvu kabisa. “Lakini pia nilikuonya siku ile
Max. Unakumbuka lakini? Kwa nini kujiingiza kwenye mambo yasiyokuhusu?” Mama
huyo akaendelea kulalamika huku akirudia ile barua akitamani hiki na kile
kisingeandikwa na kujitoa kabisa kwenye mpango mzima na kumtupia lawama mumewe.
Kwa Tino!
Kilichompata
Max ndicho kikampata Tino. Ni kama kuna mtu alikuwa akisubiria warudi majumbani
kwao. Akahakikisha Tino anapokea na kuweka saini ndipo akaondoka. Yake ilikuwa ‘Restrain order’ na barua kutoka kwa mwanasheria wa
Jackson Msindai akimtaka akae mbali na familia ya Jackson Msindai, kwa vitisho
alivyofanya siku iliyopita, ya jumapili, kwa familia hiyo. Barua hiyo ikaeza
kuwa vyombo vya usalama vimenyaka mazungumzo kati yake na Max akimshawishi
arudi nchini kudai watoto wa Jackson na Sabrina Msindai. Barua ikaeleza majibu
yake kwa Max, baada yakuona picha zilizoambatanishwa nyuma ya waraka huo,
yalisikika Tino mwenyewe akijibu ‘watoto si wangu ni wa
Sabrina’, aliambiwa yapo na sauti zao wote wawili zikiwa zimenaswa
vizuri bila shida.
Waraka
huo ukaendelea kueleza kushangazwa na hofu iliyowapata familia ya Jackson
Msindai kurudi kudai tena watoto baada ya ukiri wake yeye mwenyewe kwa Max, alipomthibitishia
kuwa watoto si wake, lakini jana yake aliwafuata na kudai watoto wa Jackson na
Sabrina huku akitoa vitisho. Mwanasheria huyo akaeleza, kwa alichokifanya jana
baada ya kukataa yeye mwenyewe kuwa watoto si wake, na uthibitisho wa kuwa ni
kweli watoto wa Jackson si wake kwani alishaua watoto wake yeye mwenyewe na
uthibitisho wa mauaji wa watoto wake upo, inaashiria kuwa amekubali
kushawishiwa na mwanasheria wake na amekusudia kufanya fujo kwa familia hiyo ya
Msindai.
Kwa
mshituko mkubwa sana Tino akaangalia karatasi ya nyuma. Ilikuwa na zile picha
alizotumiwa na Max zikionyesha muda na siku sahihi zilipotumwa. Akaambiwa
mazungumzo yapo yamenyakwa. Alionywa na kutakiwa kukaa mbali na familia hiyo au
atachukuliwa hatua kali za kisheria na kushitakiwa kwa kosa la mauaji, na
vitisho kwa familia hiyo ya Jackson Msindai. Tino hakuamini akabaki ameduaa,
hajui kama ni hofu au ni mshituko ndio unamsababishia baridi. Akakaa na yeye
kwenye kochi la karibu. Akaamini kuwa Jack hakuwa akimtania na amewawahi
kuwashitaki na kweli anao ushahidi. Tino akabaki ametulia.
Picha
za binti zake, vile walivyo wazuri ikamjia. Akakumbuka vile walivyombusu Jack
kwa pamoja na kupiga makofi. Jack akarudisha mabusu kwa watoto wake. Akakumbuka
vile walivyokuwa wamejilaza begani kwa Jack. Kisha akakumbuka jinsi Jack
alivyokuwa amewashika mkono na kutembea nao baada yakumlilia asiwaache. Jack
akarudi akawachukua. Akakumbuka jinsi walivyokuwa wamemganda Jack hata
mchangani kule baharini. Na mabusu ya hapa na pale. Akaumia sana Tino na kujuta
mno moyoni. Akumchukia Max kwa ushauri
wake. Akaitazama ile nyumba. Jumba zuri sana. Kweli ameshinda kesi, lakini yupo
peke yake! Akazidi kuumia na kumchukia Max kuliko kawaida. Tino akabaki
akiwaza.
Jumatano.
Zelda, Willy & Pendo
Mbele Ya Mchungaji Tena.
W |
illy
alishampigia simu mchungaji na kumuomba kikao siku hiyo ya jumatano. Akamwambia
atakuwa na Zelda. Lakini hakumwambia maswala ya DNA. Mida ya saa nne asubuhi
Willy alikwenda kuchukua majibu hospitalini, akabaki nayo mpaka jioni. Akaenda
kumfuata Pendo nyumbani ndipo wakaelekea kanisani. Walimkuta Zelda ameshafika
kanisani na mtoto wake akisubiria. Mchungaji alikuwa na watu wengine ofisini,
wakabaki nje ya ofisi wakisubiri. Pendo akamuona Willy anawasiwasi sana.
Anasugua mikono bila kutulia. Akajua anawasiwasi na majibu hayo ya DNA. Gafla
Willy akawa hataki tena mtoto kutoka kwa Zelda aliyemkimbilia kwa kutupa ndoa
ya kanisani. Pendo akamuacha kabisa wala hakumtuliza. Akahangaika kwa hili na
lile akijituliza, mwishoe Pendo akamuona anamshika mkono. “Nakupenda Pendo.”
“Najua Willy.” Zelda akabaki kimya akiwasikiliza.
Willy
akambusu Pendo kwenye mkono aliokuwa ameushika, midomo ikitetemeka, macho
mekundu, mishipa ya kichwa imesimama. Pendo akamuhurumia. Alikuwa amepatwa hofu
ya kupitiliza. “Naamini tutakuwa sawa Willy.” “Kweli?” Willy akataka uhakika.
Pendo akaelewa ni ombi kwamba hata mtoto akiwa wake, basi asimuache. “Naamini
hivyo.” Pendo akajibu taratibu. Willy akabaki akimwangalia. “Itakuwa sawa Willy.”
Hapo Willy akaridhika. “Nashukuru Pendo. Na nina uhakika tutakuwa na wakati
mzuri honeymoon.” Pendo akacheka taratibu. Alikuwa amependeza vilivyo na mimba
yake ya mapacha. Na vile alivyo mtulivu, kila alichoweka mwilini mwake
kilitulia. “Si hata wewe unasubiria honeymoon kwa hamu?” Willy akauliza
akibembeleza. Pendo akamwangalia
akacheka. Mlango wa mchungaji ukafunguliwa, waliopo ndani wakatoka, mchungaji
akawaita ndani.
Baada
ya salamu, Willy akaanza. “Tulipotoka hapa siku ya jumapili, tulikwenda
nyumbani kwa Zelda. Tukazungumza naye kwa urefu na undani. Lakini tukagundua
katika mazungumzo kati yenu, kuna mambo mengi sana hakukushirikisha. Tukamuomba
kama leo anaweza kuja hapa, tuzungumze kwa pamoja ili ujue ukweli wote.”
Mchungaji akamkaribisha Zelda. Akaanza Zelda kuongea kuanzia mwanzo mpaka
mwisho bila mtu yeyote kumwingilia.
“Na
mimi si mvunja ndoa za watu. Kama mama Ngoi asingeniambia kama mke wa Willy
hazai, mimi nisingekubali tokea mwanzo. Mama Ngoi ndiye aliyeniingiza
matatizoni mchungaji. Nimebaki njia panda kwa mipango yake!” Zelda akaanza
kulia. “Alinihakikishia ndoa na malezi ya mtoto!
Amenitoa kwenye maisha yangu ambayo hayakuwa ya juu sana, lakini nilikuwa
najitosheleza. Ona sasa hivi nahangaika na mtoto na sina kazi ya maana wakati
kila mtu ananilaumu mimi! Nimebaki peke yangu nikiteseka, wakati niliahidiwa
mengi tu. Yule mama amekufa na kuniacha nahangaika, hakuna asiyemtaka huyu
mtoto!” Zelda akaendelea kulia.
“Naomba
kuzungumza na mimi.” Pendo akaingilia. Alikuwa kimya muda wote. “Karibu Pendo.”
“Asante. Labda nirudie nilichomwambia Zelda, ili ajue sikuwa nikimdanganya.
Tumefanya vipimo kujua kama mtoto ni wa Willy au la, ili kuwa na uhakika.”
“Mmefanya vizuri sana maana ndicho nilichotaka kuwashauri.” “Majibu ninayo
tayari, tulitaka uje utusaidie wewe kusoma ili kuondoa utata.” Willy akaweka
ile bahasha mezani.
“Endelea
Pendo.” Willy akamtaka Pendo aendelee. “Nilimwambia Zelda, kama mtoto ni wa
Willy, nina uhakika bado Willy anamtaka mtoto wake. Si ndio Willy?” Hapo Willy
akapoa. Kimya. “Najua wamepitia kwenye ugumu na Zelda, lakini mimi kama mpenzi
wa Willy na ninayekusudia kuwa na Willy, kama mtoto ni wa Willy, nakuhakikishia
mchungaji huyo mtoto atatunzwa vizuri tu. Sitakuwa na amani kuona Willy yuko na
sisi, halafu mtoto wake anateseka huko na mama yake. Itakuwa ni laana hata kwa
watoto wetu. Atatunzwa na kusomeshwa kadiri atakavyoweza huyu mtoto aliyezaliwa
na Zelda, kwa kuwa yeye hana hatia. Lakini kama ni wa Willy. Ila kama si wa
Willy, basi hapo hainihusu tena. Itanihusu tu, pale atakapokuwa ni mtoto wa
Willy.” “Nashukuru dada. Na ninaomba usinilewe
vibaya. Mama Ngoi na wale watoto wake wa kike ndio walio nisukumia kwa mmeo.”
Akaongea Zelda kwa unyenyekevu. Willy kimya akisugua mikono.
“Mimi
naona huko tulishapita. Naomba mchungaji tusaidie tuendelee mbele. Mama hayupo,
tuliobaki ni sisi. Na hatuwezi kukwama kwa jambo lililokwisha tokea. Tusimfanye
huyu mtoto ni laana wakati Zelda umepewa na Mungu kwa upendo tu. Mimi nimehangaika
miaka na miaka kutafuta mtoto. Wewe umepewa, naomba uchukue ni kama zawadi ya
thamani sana. Usije mchukia mtoto kwa mazingira uliyoyasababisha wewe mwenyewe.”
“Sio mimi dada!” Zelda akabisha. “Usikatae kuwajibika Zelda. Mtu wa kawaida
hawezi kulala na baba na mtoto wake kwa wakati mmoja! Hata kama mama Ngoi
alikushawishi yeye na watoto wake hao wakike, pamoja na mumewe na hata Willy
mwenyewe, bado ulikuwa na nafasi ya kukataa. Lakini ulikubali wewe mwenyewe.
Usimfanye mtoto wako akawajibika kwa maamuzi yako machafu.” Pendo akawa mkali.
“Lakini
Mzee Ngoi alisema anataka kumsaidia kijana wake pia.” Zelda akaendelea
kujitetea. “Zelda! Huna jinsi ukajitoa katika hili. Yule mzee hakuanzia kwako.
Alianza na mimi pia.” Mchungaji na Zelda wakashangaa sana. “Mahusiano
uliyoyakubali kuwa nayo na mzee Ngoi mpaka kukimbia naye kwenye mahoteli,
kumfungia kwako tena mkewe akiwa hai, hayakuwa ya kulazimishwa wala yakutafuta
huyu mtoto. Ulitaka mahusiano na yule baba, ukakataa kuwa na Willy kwa kuwa
ulitaka kunufaika na mzee Ngoi, ila mwenzio amekuzidi akili.” Pendo na sauti
yake ya upole akawa mkali.
“Na
usifikiri nia ya mzee Ngoi ni kumsaidia Willy, aliona umejirahisisha kwake na
yeye akajinufaisha akijua mwisho wa siku utaondoka na Willy, yeye maisha yake
yaendelee kama kawaida. Ngoi hana shida na watoto. Kama ameweza kuwafukuza
watoto wake aliolea na mkewe, ulifikiri atashindwa nini kwa mtoto wako?
Tena ukawatoa watu wawili muhimu kwenye maisha yako! Stella na Prisca
waliokuingiza kwenye familia. Ulitegemea nini!? Kweli wewe ulidhani mzee Ngoi
na umri ule aanze kulea mtoto na wewe! Kwa nini Zelda? Kwa kipi? Alikuwa
akifurahia kampani yako tu. Mzunguke naye kwenye biashara zake, basi. Hakuanza
na wewe na wala hataishia kwa Chonge. Alianza kwangu akiniomba mahusiano nikiwa
mke wa Willy tena akiniambia sababu kama yako. Kumsaidia kijana wake.” Wote
wakashangaa.
“Kwamba
na wewe alikutongoza!?” Akauliza Zelda kama asiyeamini. “Ulifikiri kwako ni
mapenzi Zelda!? Samahani nazungumza hivi kwa baba yake Willy, lakini yule Mzee
hajatulia Zelda! Ni vile wewe humfahamu. Hata wanae wanamjua baba yao.
Alihangaika sana na mimi mpaka nikamtisha kuwa nitamwambia baba yangu na kuja
kumtisha pia kuja kumwambia Willy ndipo akaniacha kwa kuwa anamuogopa sana
Willy kuliko watoto wake wote. Anajua Willy anauwezo wakusimami jambo na
akashinda. Sio tegemezi wala hana shida na mali zake kama watoto wake wengine.
Willy alianza kujitegemea akiwa bado mdogo sana. Wewe ndio uliyefungua mwanya
wa yule mzee kumtukana Willy, lakini hata yeye anajua Willy hana shida na mali
zake. Kwa kifupi anajua hana kitu anaweza kumtisha nacho Willy kama watoto wake
wengine waliozoea kumkopa pesa mara kwa mara na ndio maana anawanyanyasa kila
wakati na kuwadhalilisha. Kwa mara ya kwanza, wewe Zelda, ndiye
uliyefungua mlango mzee Ngoi akapata jambo la kumtukania Willy. Ila anamjua
Willy si mjinga wala hajashindwa maisha. Na anajua kwa hakika Willy wangu
sio muhuni.” Hapo Willy akajisikia vizuri na kuanza kutulia.
“Si
mzee Ngoi wala mkewe, wote wanajua Willy sio muhuni. Na pia usifikiri wewe
ndiye mwanamke wa kwanza kushawishiwa pale nyumbani kuwa na Willy. Ila wenzio
walikuwa na akili. Waliokuja kujaribu walipogundua mapenzi ya Willy kwangu,
walikataa kabisa na kuondoka. Wewe mwenyewe tokea mwanzo ulisema Willy
alikwambia atazaa tu na wewe. Si ndivyo?” Zelda kimya. “Sasa ulitegemea nini
kama si kulea huyo mtoto peke yako?” Kimya.
“Hakuna
uchawi uliofanyika Zelda. Wewe ndio ulishindwa kucheza karata zako vizuri,
umeshindwa. Hamuwezi nyinyi kumloga mzee Ngoi. Anaakili sana yule mzee wewe
hujui na nafikiri hata Chonge hajui. Anapoteza pesa zake bure huko kwa waganga.
Utakuja kuniambia na yeye akishika mimba, kama hatakalia hicho kiti ulichokaa
hapo akimlilia mchungaji hapa. Mzee Ngoi ana watoto wa kike na wa kiume. Tena
amesomesha wote, na amewaweka mkononi wote kasoro Willy. Wanafanya kile
anachotaka yeye. Sasa unafikiri kwa nini atake mtoto mwingine?” Kimya.
“Samahani
nimezungumza sana mchungaji.” “Lakini ni heri umeweza kutufungua macho na
kuelewa ukweli mzima kwa undani. Pengine niende kwenye jambo hili la msingi
litakalotupa dira nyingine kuanzia sasa.” Akafungua ile bahasha. Akaisoma
kwanza yeye mwenyewe. Wakamuona anavuta pumzi. Wote wakabakia na hali ya
wasiwasi usoni. Uso wa mchungaji ukapooza kabisa. Akasoma tena, na tena. “Hivi
vipimo mlifanyia wapi?” Willy akajibu. “Inamaana basi ni vya kweli.” Wote kimya
wakimtizama. Akabaki ametulia.
“Niambie
tu mchungaji nijue moja. Nishamjua Ngoi alivyo, nishamjua Willy na mkewe.
Nataka kujua hayo majibu ili nijipange upya.” Zelda akaongea kinyonge.
Mchungaji akasoma tena na kujibu, “Huyo ni binti wa Ngoi.” “Asante Mungu
wangu.” Willy akashukuru kwa sauti na kusimama kabisa akiwa amenyanyua mikono
juu. “Willy wewe!” Pendo akashangaa, na kumvuta arudi kukaa. Zelda akaanza
kulia. “Nitafanyaje sasa?” Zelda akauliza
akilia. “Naomba nisaidie kuzungumza na Mzee Ngoi, dada.” “Najua ulisikia
malalamiko ya wifi na mama Ngoi kuwa sipendi kwenda nyumbani kwao? Si ndio?”
“Waliniambia unakimbia majukumu ya ugonjwa.” Zelda akajibu. “Sawa sawa. Lakini
si hivyo. Ni nilikuwa nikimkwepa mzee Ngoi. Mimi na yule baba tuliacha
kuzungumza muda mrefu sana na huwezi hata kutukuta tumekaa sehemu moja peke
yetu. Kwa sababu ya kutaka kunibaka, na kunishika shika kimapenzi.” Wote
wakazidi kushangaa, Willy kimya.
“Na
ujue wazi kabisa, ndipo ugomvi wangu na mama Ngoi ulipoanzia. Alijua mimi
natembea na mumewe kwa kuwa alishatukuta mimi na mzee Ngoi kwenye kile chumba
mama alikuwa akiwekea vitu vyake vya thamani na vipya. Alitukuta mumewe akiwa
na hali mbaya, na mimi nipo hapo. Akadhani kuna kilichokuwa kikiendelea hapo
chumbani ametufumania, kumbe yule baba alikuwa amenifungia hapo,
tunakimbizana anikamate, lakini sikupiga kelele. Hiyo ni mara ingine, ingine
nahisi yule mama aliniona wakati mumewe akinishika makalio, tena aliingiza
mkono ndani ya gauni, tukiwa nje, yule mama akiwa ndani na unajua nyumba yao
inamadirisha ya vioo. Hakusikia tulichokuwa tukizungumza ila kushuhudia kitendo
cha mumewe kuingiza mkono ndani ya gauni na kunishika makali.”
“Hatukuwahi
kuwa marafiki na yule mama tena, na akaacha kunikaribisha nyumbani kwake, na
akaweka mazingira ya mimi hataki nifike nyumbani kwake, japo kwa wengine
hakusema moja kwa moja, ila mimi mwenyewe aliniambia kwa kinywa chake mwenyewe.
Ndio maana usingeniona mimi nakwenda kwa yule mama kama sipo na Willy.
Ninachotaka kukwambia ni kwamba, kwa yule mzee sitaweza kukusaidia, labda
mchungaji.” Mchungaji akacheka kwa kusikitika.
“Mimi
mwenyewe ndio maana nimeumia sana nilipogundua ni mtoto wa Ngoi. Namjua Ngoi
tokea kina Willy ni watoto wadogo kabisa. Ni mkorofi asiyebadilika. Na
akisimamia jambo lake, kumbadili ni neema. Mwanzoni alihangaika sana mkewe,
mpaka akakubali kuishi naye vile alivyo. Mtu pekee anayeweza kumsikiliza kwenye
maisha yake ni yeye mwenyewe.” Hapo Zelda akazidi kulia. “Natamani
angekuwa mtu mwingine, lakini si Ngoi.” Wote wakanyamaza kwa muda Zelda
akisikika akilia.
“Na Willy
je?” Akauliza Zelda huku akilia. “Unanitania wewe!?” Willy akashangaa
sana. “Si ulikuwa naye siku akitufukuza pale nyumbani tena ukimsaidia kwa
maneno machafu sana kwangu na dada zangu! Au umesahau?” Willy akamuuliza tena
kwa ukali sana. “Willy!” Pendo akaita kwa upole. “Hapana Pendo. Anajidai analia
hapa, ni muongo. Hakuna anayemjua Zelda wa ukweli ila mimi. Ni mbaya huyu,
kuliko hivi anavyoonekana na kusikika. Ana maneno machungu, hujawahi kuona.
Mkatili asiye na hata chembe ya ubinadamu. Ana matusi yale ya nguoni. Mazito
ambayo mdomo wake umeshindwa au haujui kuyachuja. Zelda akikutukana, hapepesi
jicho.” Willy akaongea kwa jaza akitetemeka.
“Ninafuraha
si kwa kuwa mtoto si wangu. Nataka sana mtoto. Lakini nilikuwa nikiwaza kuwa na
mtoto na wewe! Natamani leo iwe mwisho wa sisi kukutana, ili usinipatie sababu
hata yakunisalimia.” “Willy naomba utulie.” Pendo akamshika. “Nikwambie kabisa
mchungaji Swai, kwake huyu labda kanisa limsaidie, lakini si ndugu. Yeye ni
shahidi wa hiki ninachokwambia. Sisi kama watoto, hawa wawili, yeye na baba,
walivyotufukuza vibaya vile, tulitafuta wazee wa ukoo. Watu ambao wanaweza
kumkalisha mzee Ngoi wakazungumza. Mzee alitukaribisha nao nyumbani, lakini
muulize Zelda kama atakuwa mkweli, fujo, matusi na dharau
alizoonyesha mbele ya wale wazee na sisi.” Kimya.
“Ilikuwa
inatisha mpaka aibu. Ikabidi tuondoke. Zelda alitukana waziwazi mbele ya wale
wazee. Akanikashifu mimi akisema ndio maana hashangai ni kwa nini mke wangu
hakushika mimba, sijui mapenzi, nipo
kama mwanamke.” Pendo na mchungaji wakashangaa na kushituka kwa sauti. “Haaa!”
“Mungu wangu nishahidi. Alisema huyu mbele za wale wazee na ndugu zangu. Tena
akasisitiza hata shuguli yenyewe siiwezi, sina nguvu za kiume zakutosha, hata
dakika 5 sifikishi!” “Mungu wangu!” Pendo akashangaa sana. “Kama mimi naongopa,
akanushe hapa. Mama mmoja akamuomba atulie, atumie tafsida kwani pale kuna
wazee. Lakini Zelda akamjibu vibaya yule mama, tena kama shangazi yetu, japo si
tumbo moja na baba lakini sisi tumekua tukimuita shangazi. Akasema yeye pale
haoni mtoto mdogo ambaye hafanyi mapenzi.” “Haiwezekani Willy!” “Si huyu hapa
muulize. Muulizeni.” Willy akaweka msisitizo.
“Sasa
huyu leo anarudia mlango upi na kwa nani wakati alitufukuza pale kwa mzee? Sisi
na wale wazee wote.” “Siku ile sikuwafukuza.” Zelda akajitetea. “Kilichopungua
ni neno ondokeni. Lakini ulitukana mpaka yule mama akasema hawezi kuendelea
kusikiliza ukitutukana, yeye yupo na mumewe pale, na sisi ni kama watoto
aliotuzaa kwani alitulea. Hakukwambia hivyo yule mama na kuondoka na mumewe,
ndio baba akasema na sisi tuondoke haraka?” Kimya.
“Tafadhali
mchungaji, mimi nataka kuoa. Nataka kumuoa Pendo mpenzi wangu. Naamini tatizo
au kipingamizi kilikuwa Zelda tu. Sina mwanamke nimelala naye, hata kuwa na
mahusiano naye tokea nianzane na Pendo isipokuwa huyu Zelda. Na Pendo wangu
hivyo hivyo. Mimba ya Pendo ni yangu mimi. Mpenzi wangu alitulia hata
tulipoachana hakuwa na mahusiano. Tatizo lilikuwa mimi kwa huyu Zelda. Umeshapata
ukweli juu ya Zelda. Naomba akutafute kwa wakati wake, sisi tumalize yetu.
Naomba Pendo, uumpe nauli aondoke.” “Nilimrushia pesa ya nauli yakuja na
kurudi. Labda nimuongeze tu.” “Hapana. Naomba atupishe tafadhali. Hiki ni kikao
chetu.” “Mimi naomba nikusubirie hapo nje
mchungaji. Lasivyo sitakubali kushindwa kirahisi hivi.” Zelda
akaongea wasimuelewe anamaanisha nini. “Sawa. Bila shida unaweza kunisbiria tu.”
Zelda akatoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~
·
Zelda Atakubali Kuachwa Njia Panda?
·
Pendo Na Willy Safari Hii
Watafanikiwa?
·
Mama Kundi Amejua Amesikiwa
Na Bosi Wake. Na Yeye Anakabiliwa Na Lipi?
·
Tino & Max?
Itaendelea.
0 Comments:
Post a Comment