Walitoka
hapo kimya kimya wakaingia garini bila hata kusemeshana. Willy akaondoa gari hapo
kanisani.
Pendo akashangaa Willy anasimamisha gari pembeni ya barabara.
Akamgeukia. “Si unanipenda?” Pendo akashangaa. “Nataka kujua Pendo.” “Wewe
unajua nakupenda. Kwa nini?” “Na wewe unajua kama nakupenda na nimekusudia kuwa
na wewe?” “Najua Willy ila sijui kwa umbali gani?” “Kwa kila umbali unaoweza
kufikiria na unaokuogopesha sasa hivi, maana na mimi nimeingiwa hofu. Naomba tu
uniahidi kwa chochote tutakachokutana nacho kuanzia sasa, hakitatutenganisha.
Tutasimama pamoja.” Pendo akavuta pumzi kwa nguvu. “Nikwambie ukweli Willy?”
Pendo akauliza huku akipapasa tumbo lake, kama aliyepata nafuu.
“Nini?”
“Nilishaingiwa hofu yakupitiliza nikijua kibao ndio kinanigeukia. Hayo maneno
nilitamani nikwambie wewe, lakini nikaishiwa ujasiri.” “Kuwa chochote
tutakachokutana nacho kuanzia sasa, hakitatutenganisha?” Willy akamuuliza.
“Ndiyo, lakini nikaona nitakuwa mbinafsi endapo ukimpata Zelda, ukagundua mtoto
alikuwa wako, ukamtelekeza kwa ajili yangu ambaye hata watoto hawajazaliwa!” “Kwa
hiyo bado huamini kama nimerudi kwako kwa ajili yako ila watoto?” Willy
akauliza kwa kuumia. “Nipo njia panda Willy. Upande mmoja unaamini, upande
mwingine nakuwa na wasiwasi hata naogopa chochote kisije kutokea kwa hawa
watoto, nikakupoteza.” Willy akavuta pumzi kwa nguvu akajirudisha nyuma ya gari
akaegemeza kichwa na kugeukia nje. Pendo naye akanyamaza kimya.
Mtaka Cha Uvunguni, Sharti
Ainame.
A |
kamuona
anatoa simu yake na kupiga. Ikaita kwa muda mrefu mpaka ikakata. Akamuona
anapiga tena. “Samahani kwa usumbufu baba. Lakini
nilitaka kuomba namba ya simu ya Zelda, nahitaji kuzungumza naye.” “Sina.”
Akajibu mzee Ngoi kwa jeuri. Pendo akajua kweli Willy amekusudia kuwa naye.
Kumpigia simu mzee Ngoi! Ni jambo la mwisho kabisa angetamani kufanya. Hata mchungaji
alimkatalia. “Pengine unafahamu sehemu anapoishi kwa
sasa?” “Kwa nini unafikiri hivyo?” Mzee Ngoi akauliza kwa jazba. “Nauliza tu baba yangu. Je alipokuwa akiishi zamani
unapakumbuka?” “Keko, karibu na yale magorofa ya National Housing. Kuna nyumba
upande wa nyuma yake, wanalima michicha nje, ndiko alikokuwa akiishi hapo kabla
hajaja kwangu na mke wangu na kuwa tapeli.” “Amekutapeli!?” Willy
akauliza nakuweka spika ili Pendo asikie.
“Sina muda wa kipuuzi na kuzungumza vitu vya kipuuzi.” “Nilitaka tu
kusikia upande wako baba, kabla sijakwenda kuzungumza naye.” “Huna utakachopata
kwa malaya yule, mbwa anayeweza kulala na yeyote na muongo wakupindukia.”
Willy akajua walishageukana. “Unajua alichokuwa
akiniaminisha mimi?” Willy kimya. “Kabla
yakulala na wewe, eti alikuwa akisema anataka mimi nimlale kwanza ili nisije
kula makombo yako na pia akitaka eti mimi niridhike kwanza kwakuwa ananipenda
mimi na anataka mtoto wake wa kwanza awe wangu. Unajua na ahadi yake?”
Willy kimya.
“Msichana yule ni tapeli la mchana kweupe. Alifikiri atanizidi mimi!
Hata kidogo. Anataka kunufaika hapa mjini kwa jasho langu mimi!” “Ni nini
alikuahidi baba?” Willy akamkatiza maana hasira ilizidi
kupanda akataka kusikia ya Zelda zaidi. “Eti hata kama
mama yenu asingefariki pengine angepona, wewe ukaachana na mkeo mkaoana naye,
bado sisi tungeendelea kama kawaida na kuolewa na wewe ndio ingekuwa njia
rahisi yakutufanya tuzidi kuwa karibu kwa kuwa ananipenda sana na mama yenu
ndiye anatutenganisha kumbe muongo tu. Ananiibia akitaka kunufaika kote kote
huku akitumia madawa yakunipumbaza! Nashukuru Mungu huyu msichana tuliyekuwa
naye tokea zamani akitusaidia kazi mimi na mama yenu, ndiye amenifungua macho.”
Willy akajua mapenzi yameshageuka.
“Pole sana baba. Hukufanikiwa kubakisha namba yake?”
Willy akauliza tena kinyenyekevu kama kumtuliza. “Nafikiri
naweza kuwa nayo. Subiri.” Pendo na Willy wakaangaliana. Gafla mzee Ngoi
akasikika ametulia kabisa. Akawatajia hiyo namba, Pendo akawa akiandika. “Nakushukuru sana baba. Asante.” Willy akajishusha
kabisa lakini moyoni alishamchukia huyo baba yake wala hakutaka wala kupanga
kuja kumsikia tena.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Huyu
Mzee ni mtu wa mwisho kabisa ambaye nilitaka kuja kuzungumza naye, zaidi kuja kumuomba
chochote hata maji!” Pendo akamwangalia. “Nafanya hivi kwa ajili yako Pendo.
Nataka kuwa na wewe. Na ndio maana nazungumza na kujishusha kwa hawa wote ambao
sikutaka hata kuja kuwasikia tena.” Pendo akabaki ametulia. “Nakupenda wewe
Pendo, na nimekusudia kutulia na wewe hata iweje.” “Nashukuru Willy.” “Mbona
kama unaongea ukiwa unamashaka!?” Willy akalalamika. “Hapana Willy. Nimeshukuru
ila sijui kinachotukabili mbeleni.” “Hapo sasa unanitia nguvu ukijiweka na
wewe. Angalau unanitia moyo. Naamini tukisimama pamoja kuanzia sasa,
hatutashindwa.” Pendo akatulia. “Si ndio?” “Naamini hivyo Willy. Naamini kuwa
hutabadilika tena.” Willy akajua bado anamashaka. “Basi naomba kuanzia sasa
matendo yazungumze.” Willy akatoa gari hapo.
“Tunakwenda
wapi tena?” “Nataka kutimiza yote, leoleo. Mchungaji amesema nizungumze kwanza
na Zelda ndipo niendelee. Naomba tuongozane mpaka kwake. Na yeye nimsikilize,
niweke kikomo naye. Ni sawa?” “Umeshafikiria kama ikitokea mtoto ni wako!” “Nitajua
mbele ya safari Pendo. Tafadhali tusimame wote.” Pendo akamwangalia na
kunyamaza. “Nini?” “Nafikiria tu.” “Juu ya nini?” “Nasema itakuwa mipango yako
imetimia. Kuzaa na Zelda na kuwa na mimi.” Willy akashindwa hata azungumze nini
tena. Akanyamaza kabisa na kugairi hata kwenda kwa Zelda.
Pendo
akamuona anabadili njia nakurudi nyumbani. “Vipi tena?” “Naona turudi tu
nyumbani Pendo, pengine tujipe muda wakufikiria kujua nini tufanye kuanzia hapa.
Acha mimi niende nikazungumze na Zelda. Kama kuna kufanya DNA, nifaye kabisa
mpaka kieleweke, ndipo nirudi kwako nikupe majibu ili uweze kuamua kuwa na mimi
Willy peke yangu au mimi Willy na huyo mtoto. Nisikubebeshe mizigo
isiyokuhusu.” Pendo akajua amekasirika.
“Umekasirika?”
Akamuuliza taratibu tu. “Hapana, ila sijui natakiwa kufanya nini tena Pendo!
Nahisi akili imefika mwisho. Acha nitembee na kufanya kile ninachoweza.”
“Samahani Willy, naomba usikasirike.” “Hapana Pendo. Nilikosa, acha niwajibike
peke yangu.” “Hapana. Nahisi nimeingiwa na hofu pamoja na wivu tu. Nilifurahi
nilipojua mtoto si wako. Sasa sasahivi kunakuwa na mazingira yote yakuonyesha
mtoto ni wako. Nina hofu ya kukupoteza tena.” “Naomba uniamini hutanipoteza
Pendo. Nimerudi na sitaondoka tena. Hata kama mtoto ni wangu, mimi na wewe
tutafute njia pamoja ya jinsi yakukabiliana na hiyo hali. Nitakusikiliza wewe.”
“Basi twende pamoja.” “Una uhakika?” “Ndiyo. Twende. Sasa hivi ujasiri
umeongezeka.” Akamvuta mkono na kuubusu. “Asante Willy.” Pendo akashukuru na
tabasamu. Willy akajua amefungua moyo. Akageuza gari tena kutafuta Keko.
Kwa Zelda.
“Nashauri
tumpigie simu kwanza.” Pendo akatoa wazo. “Sawa.” Pendo akabonyeza namba kwenye
simu ya Willy, ikaita Zelda akapokea. “Hallo!” Kwa
heshima kubwa sana kama si Zelda. “Unaendeleaje Zelda?”
“Naendelea vizuri, ila mtoto ndiye alikuwa akiumwa.” “Nini?” Willy
akauliza. “Malaria. Akaishiwa maji, tukalazwa kama siku
mbili hivi. Lakini sasa hivi anaendelea vizuri.” “Mnaishi wapi?” “Kule kule
nilikokuwa nikiishi mwanzoni, sikuachia chumba changu. Nilikifungia na vitu
vyangu.” “Unajua mimi sifahamu ulipokuwa ukiishi! Labda unielekeze, nataka kuja.”
Zelda akatulia kidogo. “Zelda.” “Nipo. Nafikiria jinsi
ya kukuelekeza.” “Kwani ni mbali na barabarani?” “Hapana. Gari inafika mpaka
hapa.” Akamuelekeza kwa upendo na ahadi ya kumfuata barabara kubwa, kama
atashindwa kuelewa na kufika kwake. Asijue na Pendo yupo. Wakaagana.
Wakamkuta
barabara kubwa amesimama na mtoto amemfunga mgongoni. Willy akamwambia apande
awaonyeshe njia ya mpaka kwake. Hapakuwa mbali sana na nyumbani kwake. Ilikuwa
nyumba ya wapangaji watatu. Na yeye akawa wanne. Willy aliegesha gari yake nje,
akaenda kumfungulia Pendo mlango, akamsaidia kushuka, baadhi ya wapangaji
wengine, majirani na Zelda wakiwatizama. Wakasalimia waliowakuta hapo nje,
Zelda akawakaribisha ndani. Willy akamtanguliza mkewe, wakawa wanamfuata Zelda
nyuma mpaka chumbani kwake. Kilikuwa chumba kizuri tu kilichokamilika kila
kitu. Makochi mazuri, kitanda safi, kabati kubwa zuri tu na tv yake. Pasafi
kabisa.
“Si
ninaweza kukaa?” Akauliza Pendo. “Karibuni.” Zelda huyu alijawa na heshima kama
Zelda aliyekutanishwa naye Willy mwanzoni kabisa. “Pole na kuuguza.” Akaanza
Willy, Pendo kimya. “Asante. Lakini naona anaendelea vizuri.” “Mara ya mwisho
kuachana pale kwa mzee, mlikuwa mfunge ndoa. Na ukasema mtoto alikuwa ni wa
mzee kwa kuwa ndiye uliyekuwa naye mwanzoni kabla yangu. Swali, kwa nini upo
hapa na mtoto na si kule kwa mzee?” Willy akaenda moja kwa moja kwenye kilichowapeleka.
“Chonge
amenigeuka.” Akaanza Zelda. Willy akakunja uso. Chonge ni msichana wa
kazi wa nyumbani kwao kwa miaka takribani 12. Amekaa na mama yake kwa muda
mrefu sana. “Chonge?!” Willy akataka uhakika. “Ndiyo yule msichana wa kazi. Na
sasa hivi yeye sio msichana wa kazi tena, ndiye mwanamke wake mzee Ngoi,
ameleta ndugu yake kutoka kwao ndiye anayemfanyia kazi.” Pendo akajiweka sawa.
Willy akachoka kabisa. “Muda wote mimi nipo pale kumbe yeye Chonge ananionea
wivu na kunipigia mahesabu yakunitoa pale. Akawa ananung’unika moyoni na kwa
yule kijana wa usafi kuwa kama baba anataka kuoa, yeye ndio alitakiwa arithi
nafasi ya mama sio mimi niliyekuja juzi tu hata simjui baba. Sasa analalamika
hivyo lakini huku kwangu akawa kama ananichekea na kujidai ananiheshimu mimi
kama mama mwenye nyumba wake.” Akaendelea Zelda. Pendo na mumewe wakisikiliza.
“Sasa
nilipojifungua tu, akaanza kunijaza maneno kwamba niwe makini. Watoto wa mzee
Ngoi wanaweza kunichezea kwa kuwa baba amewafukuza pale nyumbani kwa ajili
yangu na pia mkeo wewe hawezi kukubali kwa kuwa nimewavunjia ndoa.” Pendo
akashangaa sana. “Unamaanisha nini ukisema kuchezewa!?” Akauliza Willy akionyesha uso wa hasira
kidogo. “Yaani kuwa mkeo anaweza kuniloga mimi na mtoto wangu kwa kuwa
nimewavunjia ndoa yenu, na yeye hazai. Kwa hiyo akisikia mimi nimezaa,
ataniloga mimi na mwanangu.” Pendo akacheka taratibu kwa kusikitika Zelda
akamwangalia kidogo na kuendelea.
“Eti
na dada zako wanaweza kuniloga mimi na mtoto wangu, sababu baba yenu
aliwafukuza akaniambia niwe makini na niwawahi kwa kuwa hamuwezi kukubali mali
yote nipewe mimi na mwanangu.” Willy akatulia tu akimsikiliza. “Mwezi huo wa
kwanza Ngoi akawa ananijali mimi na mtoto. Ananipa matumizi pale nyumbani na
kunisaidia maswala ya mtoto kwa mapenzi mazito sana. Kumbe Chonge anaumia.
Akawa anasema hajawahi kumuona baba yenu hata akipenda hivyo wajukuu zake! Mimi
nikamwambia mapenzi ya mtoto na wajukuu ni tofauti, mimi sishangai kwa kuwa
yule ni mwanae. Lakini yeye akwa ananing’ang’ania lazima niufunge ule
upendo usije badilika.” Willy akakunja uso. Zelda akaelewa.
“Yaani
niende kwa mganga kumfunga Ngoi ili asije kubadilika.” Willy akapandisha nyusi
zote kwa mshangao. “Ndio mimi nikamwambia siwezi kutoka kwenda kutafuta mganga
wakati nina mtoto mdogo. Akaniambia yeye atanisaidia kwenda kumtafuta. Akaanza
kwenda yeye sasa kwa huyo mganga. Mara ya kwanza akarudi na kuniambia
anachohitaji huyo mganga. Nikampa ili ampelekee.” “Nini?” Willy akauliza bila
kujua. Zelda akasita kidogo. Hapo ndipo Willy akataka kujua zaidi. “Kama
umeamua kuongea, ongea kila kitu, acha kuficha mambo.” Akaongea Willy kwa
ukali. “Ilikuwa nguo yangu ya ndani na ya Ngoi.” Willy akashituka sana. “Kwa
hiyo ukampa zote mbili!?” “Ndivyo alivyoniambia ametumwa na huyo mganga ili
ayafunge hayo mapenzi. Mimi nikakubali nikampa na pesa juu!” Willy akabaki
ameduaa. Zelda akaona aendelee.
“Akarudi
na dawa, akaniambia mganga ameshaanza kazi yake. Hizo dawa nizakumuwekea kwenye
chakula chake. Basi, ikawa rahisi, Chonge akipika, tunamuwekea. Sasa
nikashangaa baada ya muda, Ngoi ni kama anaanza kunibadilikia mimi! Akaanza
ukali hata kwangu, na akawa hana muda na mtoto. Akija nyumbani anakuwa busy na
taarifa ya habari na magazeti kama unavyomjua baba yako kwa magazeti wakati ni
kama mtindo huo alipunguza nilivyokuwa naye. Nikimtaka kimapenzi, ananitolea
sababu. Ikabidi kurudi kwa Chonge na kumwambia mbona zile dawa ni kama
zinambadili Ngoi na kumfanya kinyume nami! Akaniambia labda niende mimi
mwenyewe kwa mganga nikazungumze naye. Atanisindikiza, yeye na mtoto watabaki
kwenye gari.” Wakamuona anaguna kwa kusikitika.
“Jamani
Chonge ni mshenzi yule msichana, msimuone mpole au amenyamaza vile. Mbaya
kuliko shetani!” “Naomba uendelee.” Willy akamkatisha. “Basi, ndio akanichukua
siku hiyo asubuhi kama kwenye saa nne hivi. Akanipeleka mpaka kwa mganga wake.
Akaniambia mimi nishuke, niingie ndani
kwa mganga, nisiwe na wasiwasi alishazungumza naye, yeye atabaki na mtoto
kwenye gari. Mimi nikashuka. Hapo aliniambia nijifunge khanga chini na ingine
nijifunike. Basi, kumbe mimi nashuka, nakwenda kwenye ile nyumba ya mganga,
mpaka naambiwa nikae pale nje nisubiri kama wenzangu. Maana nilikuta kama kina mama
wanne hivi. Nikaambiwa ni kwa foleni, na mimi nikae hapo mpaka zamu yangu
ifike. Nikaka hapo. Kumbe mwenzangu Chonge ananipiga picha tu!” “Anakupiga
picha!?” Akauliza Willy kama ambaye ashapotezwa.
“Ndiyo.
Anatumia simu yake kunipiga mimi picha kila ninachokifanya. Najua anabembeleza
mtoto wangu kumbe ananipiga picha tu. Zamu yangu ikafika, nikaaguliwa na
kubadilishiwa dawa. Nikarudi kwenye gari akawa ananiuliza maswali, kumbe
ananirikodi tu jinsi ninavyomjibu mimi sijui! Nikamsimulia kila kitu
tulichomfanyia Ngoi na huyo mganga, mwenzangu yeye kumbe anajirikodi kama anashangaa
vile, mimi sina habari jinsi anavyoniuliza yale maswali. Najua tupo pamoja!”
Zelda akaendelea.
“Tukarudi
nyumbani tukapika, nikampa zile dawa sasa ili amuwekee. Akapokea na kuniambia
ni heri azifiche yeye huko jikoni, ili iwe rahisi. Nikampa dawa zote. Sasa
nikashangaa Ngoi anazidi kuwa mkali na hali nyumbani. Anagomba mfululizo,
nyumbani ni kama anapakimbia. Hataki nimguse wala nimsogelee. Nikamwambia
Chonge mbona mambo yameharibika zaidi! Akasema labda sikumsikiliza yule mganga
vizuri, nirudi nikamuulize tena labda kuna sharti nimekosea. Mimi nikamwambia
ndio itakuwa mara yangu ya mwisho. Nikirudi havijafaa, dawa zote alizonipa,
nachoma moto. Chonge akaniitikia tu vizuri.” Zelda akacheka tena kwa masikitiko.
“Baada
ya kama siku 5 nilipotoka kwa mganga, Ngoi akaniaga kuwa anasafiri na hajui
atarudi lini. Akaondoka bila maelewano. Hasira zisizo na sababu, tena hapo
alishaniambia nihame chumba kwa kuwa mtoto analia usiku, yeye anashindwa kulala
na kesho anatakiwa kwenye majukumu yake, mimi nina uwezo wakulala mchana.
Nikaona ni sawa. Nikashangaa anaondoka bila kuniachia pesa mimi, eti amemuachia
Chonge! Halafu akaja chumbani nilipokuwa nimelala na mtoto ananiaga na
kuniambia pesa za matumizi amemuachia Chonge! Nikamuuliza kwa nini iwe hivyo na
mimi ndiye mkewe! Akanijibu moja kwa moja, bado hatujafunga ndoa, nisijisahau.
Akaondoka na kufunga mlango kwa nguvu. Jamani nilishituka karibu kuchanganyikiwa.”
Pendo na Willy kimya wakimtizama.
“Nikamfuata
Chonge nikamuuliza ameachiwa kiasi gani na kwa nini iwe yeye si mimi? Akanijibu hata yeye hajui, lakini
akanisisitiza lazima nirudi kwa mganga haraka kabla hajapotelea kwa mwanamke
mwingine huko nje, nishukuru hata akili yake imemtuma kwangu. Na mimi nikaona
ni jambo jema. Ilipofika kwenye saa sita mchana tukarudi kwa mganga. Kama alivyofanya
mwanzo, akabaki kwenye gari na mtoto, mimi nikashuka. Sikukuta watu wengi sana.
Nikakaa kidogo nikaingia. Nimefika naaguliwa, nashangaa Ngoi naye anaingia na
mtoto wangu. Akanikabidhi mtoto wangu pale pale nilipokuwa nimekaa nikiaguliwa,
na kuniambia amepata ushahidi wakutosha, hataki kuniona tena. Akaniambia za
mwizi arobaini. Akanionyesha picha zangu za kwanza na kunisikilizisha
mazungumzo yangu na Chonge yale niliyokuwa nikimwambia Chonge kuwa safari hiyo
nimemfunga kabisa Ngoi. Mganga amenihakikishia ni wangu daima. Ngoi akaondoka
na kuniacha palepale.” Zelda akaanza kulia taratibu.
“Nikatoka nje, sikumkuta Chonge wala gari halikuwepo pale
nilipokuwa nimeegesha. Nikarudi pale kwa mzee Ngoi, mlinzi akaniambia amesema
hataki kuniona tena na niondoke. Basi, mimi nikarudi kwa wazazi maana hata
funguo za hapa zilikuwa pale kwenu. Nikakaa kama siku kumi ili angalau kumpa
nafasi mzee Ngoi atulie ndipo nirudi nijieleze nikiwa na wazazi. Baba na mama
wakanisindikiza nikiwa na mtoto. Bwana nilijuta. Mzee Ngoi alikuwa mkali mno,
heshima hakuna kwa wazazi wangu.” “Ilikuwa
kama siku ile kwetu?” Willy akauliza kwa kejeli.
“Ila sasa mimi Chonge alinigeuka! Akaitwa kutoa ushahidi.
Akaeleza yote ila yeye akajitoa kabisa. Akasema mimi ndiye niliyekuwa
nikimuwekea dawa Ngoi ili kumuharibu akili na akasema nilishamwambia hata huyu
mtoto sio wake Ngoi. Nilimfanyia tu uchawi kumdanganya kuwa mimba ni yake
akakubali. Halafu eti nimemfanyia dawa huyu mtoto, hata akienda hospitalini
kupimwa, ataonekana ni wa Ngoi tu. Kwa hiyo akaniambia hamtaki huyo mtoto tena
na wala nisiwahi kumsogeza pale.” Zelda
akalia kwa uchungu sana.
“Wakatoa ushahidi wote wa picha na sauti yangu nikisema kama
nimemloga Ngoi. Ndio Ngoi akatufukuza na kusema akija kuniona pale tena,
ananipeleka polisi na ushahidi anao. Hataki kuniona mimi wala mtoto wangu. Na
hata nikimshitaki popote, anatoa ushahidi kuwa mimi nimemloga na hamtaki huyu
mtoto kwa kuwa haamini na hatakuja kuamini kama kweli ni wake kwa kuwa nishamloga.
Chonge ndiye mwanamke anayemtakia mema tokea zamani, amekuwa akiwasaidia bila
tamaa. Akasema pale mbele ya wazazi kuwa Chonge ndiye atakayekufa naye, kwa
kuwa wamekuwa naye na ni mwanamke mvumilivu. Akatufukuza pale pale.”
“Mimi nikaomba mizigo yangu, Chonge akasema haniamini tena,
akawa ananisindikiza kila mahali ananisimamia kila ninachofanya huku
akiniharahisha. Akamuita yule kijana anisaidie kubeba vitu vyangu na vya mtoto,
aniachie nje. Tena nguo tu. Vitu kama vitanda vya mtoto akanikatalia nisibebe.”
“Nani sasa?” Willy akauliza. “Si Chonge huyo!
Akaniruhusu kuchukua nguo tu, bila aibu wala huruma! Tukatoka pale na wazazi
nao wakaniambia itabidi nirudi tu kwangu. Nimewatia aibu mno na kuwafedhehesha
kwa tamaa zangu. Nilikuwa na kila kitu, lakini sikuridhika. Wazazi wangu nao
wakaniacha palepale. Wakaondoka. Ndio mimi nikarudi hapa. Lakini namshukuru
Mungu sijatetereka, naishi vizuri tu.” Willy akavuta pumzi kwa nguvu
nakubaki kimya hata hajui aseme nini tena. Akabaki ameinama.
“Willy!”
Pendo akamgusa begani kama kumrudisha pale. “Mmmh! Hata sijui niseme nini
tena!” Willy akabaki kama anafikiria zaidi. “Labda mimi niulize kama
naruhusiwa.” Pendo akaanza taratibu. “Uliza tu. Labda utanisaidia na mimi kujua
chakuongea. Maana nahisi nimeingiwa hofu na hayo mazingaombwe, sijui uchawi!
Sijui lipi la kweli na lipi silo!” “Wewe sijawahi kukuloga. Chonge ndiye
aliyenipeleka.” Zelda akajitetea. “Lakini si ulikubali na kufanya, tena mpaka
kutumia madawa!?” Willy akamuuliza kwa ukali kidogo. Hapo Zelda akashindwa
kujibu.
“Nashindwa hata kuendelea kukuuliza chochote
kwa kuwa unasura nyingi sana Zelda, ambazo kila nikikutana na wewe, zinajifunua!
Zelda niliyetambulishwa na mama, siye niliyekutana naye nilipokwambia tuishi
pamoja, ili tulee mtoto! Hiki unachosema alikufanyia Chonge, nafikiri ndicho
alichokuona ukitufanyia sisi watoto wa baba. Alikuona vile ulivyomudu kugeuza
moyo wa baba, ukawa mkatili kuliko kawaida. Ukafurahia kumuona baba anatufukuza
nyumbani kwetu. Tulipozaliwa na kukulia. Chonge ameiga ulichokifanya Zelda.
Hakikuwa kitu kigeni. Na pengine Chonge hakuwa na hilo wazo ila alilipata
kwako.” Zelda akanyamaza na hapo akashindwa cha kujitetea.
“Ulitaka
kuuliza nini Pendo?” Willy akamgeukia Pendo. “Nilitaka kujua kwa mchungaji
alizungumza nini na kwa nini alikwenda tena kwa mchungaji Swai?” Pendo akabakia
na kile kilichowapeleka pale, hakuyumbishwa na habari nyingi za Zelda. “Swali
zuri sana. Amenichanganya mpaka nimesahau swali la msingi. Ulifuata nini kwa
Mchungaji Swai, na ulimwambia nini?” Willy akarudia swali kwa msisitizo. “Ilikuwa
tufunge ndoa pale kanisani kwa mchungaji Swai. Tulishakwenda tukazungumza naye
mimi na Ngoi kwa pamoja. Akatuuliza maswali na kuzungumza na sisi. Tukaweka
kabisa tarehe yakufunga ndoa. Sasa Ngoi aliponifukuza ndio nikarudi kwa Swai
ili kuzungumza naye.” “Ulizungumza naye kama hivi?” Willy akauliza. Zelda
akababaika sana na kushindwa kutoa jibu la moja kwa moja.
“Usipoteze
muda Zelda. Tafadhali jibu swali.” “Sio kwa undani na uwazi hivi.” Zelda
akajibu kwa kubabaika. “Labda utuambie ni nini ulimwambia, sisi wenyewe tutajua
ni nini uliacha.” “Mimi nilimweleza ule mwanzo kabisa kabla mama hajafa na
makubalino yetu.” “Yapi Zelda?” Willy akauliza kwa ukali. “Yale ya kukubebea
wewe mimba, lakini naweza kulala na Ngoi pia ili kuhakikisha nashika mimba, ili
kukufanya wewe utulie kwangu, umuache mkeo, unioe mimi.” “Hivyo tu ndivyo
ulivyomwambia!?” Akauliza Willy kwa
ukali na mshangao. “Nikamwambia lakini baada ya kifo cha mama, baba
akanibadilikia, sasa hivi yupo na msichana wa kazi, hanitaki mimi na mtoto.”
“We Zelda!?” Willy akashangaa sana.
“Naomba
subiri kwanza Willy.” Pendo akamtuliza ili yeye aongee. “Ukamwambia nini juu ya
Willy?” Pendo akauliza. “Mimi sikuongea mengi juu ya Willy zaidi ya kumwambia
pia nililala na Willy, ila Willy aliondoka sijui alipo.” “Hukumwambia kuwa
mtoto ni wa nani?” Pendo akamuuliza swali la kumtenga tu, lakini akitaka na
yeye jibu. “Ukweli mpaka sasa hivi nimechanganyikiwa.” “Usinitanie Zelda!”
Willy akapaniki. “Naomba utulie Willy. Tafadhali mpenzi. Tupo hapa kwa
mazungumzo. Tulia mimi nizungumze na Zelda.” Willy akatulia.
“Unaposema
umechanganyikiwa, unamaanisha nini?” Pendo akamuuliza kwa sauti yake ya taratibu
bila kuonyesha jazba. “Maana ukumbuke nilikuwa nikilala nao hawa wote wawili.” Pendo
akaumia lakini akajikaza, ila sio Willy. “Sio wewe ulisema mbele ya ndugu zangu
kuwa mtoto ni wa mzee kwa kuwa siku zako za hatari, ulikuwa ukianza na baba?” Kimya.
“Wewe Zelda?” Willy akaita kwa ukali, Zelda akaanza kulia. “Ni muongo huyu
Pendo. Ameona kwa baba ameshindwa, ndio anataka kuniharibia na kwangu kwa
kunikimbilia sasa hivi. Hukumuona siku ananikana.” Pendo akamshika mkono Willy kama kumtuliza.
Willy akanyamza tena.
“Naomba
usilie Zelda. Tulia tuzungumze ili tufikie muafaka. Willy ni mpenzi wangu,
nasitataka atelekeze mtoto kama ni wake. Eti nijidai kama huyu mtoto hayupo
halafu ulee peke yako! Hapana Zelda. Lazima tutamtunza kwa namna yeyote ile.”
Hapo Zelda akaanza kutulia. “Nashukuru dada.”
Zelda akafuta machozi akijua ameshapata ulaji. Pendo akaendelea. “Sasa ili
kusiwe na kurukana na kubadilika tena, haya mambo lazima yaende kwa maandishi.
Kuwepo na kukabidhiana matumizi ya kila mwezi ili usilemewe. Ataingizwa kwenye
matibabu ya kazini kwa Willy ili akiwa anaugua kama hivi, awe anapewa matibabu
mazuri na kuhakikisha anawekewa akiba benki, ya kuja kusoma baadaye.” Mpaka
Willy akamgeukia Pendo kwa mshangao. Pendo akamminya ule mkono aliokuwa
amemshika, Willy akatulia.
“Sijui
kama unanielewa Zelda? Sitakubali Willy akuachie majukumu ya mtoto kama ni
wake.” “Nakushukuru dada. Asante. Mungu na wewe akubariki.” Pendo hakutaka hata
kuitika. “Sasa, itabidi kumpima huyo mtoto na Willy.” Hapo Zelda akashituka
sana. “Haya mambo yanakwenda kisheria Zelda. Leo Willy hawezi kutokezea na jina
tu la mtoto ofisini kwao nakusema naomba kila mwezi kiasi hiki cha pesa kiende
kwa huyu mtoto, na mnipe kadi nyingine ya matibabu kwa ajili ya mtoto wangu! Haitawezekana.
Lakini mtoto akipimwa, akajulikana ni wa Willy, zile karatasi, Willy
atazichukua na kuzipeleka ofisini kwao, kuanzia hapo utaratibu wa matunzo ya
mtoto uanze. Sijui kama umenielewa?” Zelda akanyamaza.
“Au
hutaki msaada, unataka umlee mtoto wako mwenyewe?” “Nataka msaada. Maisha
magumu, halafu ndio nimeanza tu kazi kwenye hiyo shule hata hawalipi vizuri.”
“Basi twende hospitalini hata sasa hivi. Na ndio vizuri mtoto wako atafanyiwa
vipimo zaidi kujua afya yake. Na utakutana na daktari wa watoto akushauri
vizuri.” Hapo Zelda akakubali lakini Willy akawa na wasiwasi.
“Majibu
yakija yakawa kama vile alivyosema baba!” Pendo akamwangalia kama hamuelewi.
“Kama kufanyiwa uchawi sijui mazingaombwe, vipimo vionyeshe ni wangu kumbe si
wangu!” “Ndipo tutakapoomba hayo mazingaombwe yasije kuisha ili abakie kuwa mtoto
wako kama anavyofanya mwenzio Jack. Hajapungua mahali popote. Anahesabu ni
baraka kupata wale watoto. Kwa hiyo usiwe na wasiwasi. Si wewe wala mimi
tutakuwa wa kwanza. Kwanza huyu mtoto mmoja tu atatugarimu nini Willy?” Willy akapoa.
“Hakuna
tutakapopungua kumsaidia mtoto mmoja tu hapa duniani. Akala vizuri, akasoma
vizuri na kukua kwenye mazingira mazuri! Sidhani kama ni jambo baya.” Zelda
akazidi kufurahi, akajitayarisha haraka na kuchukua begi dogo la mwanae,
wakatoka na kukuta watu wengi nje ya mlango kama wamekaa wakifanya shuguli zao,
lakini wakajua walikuwa wakisikiliza. Wakatoka kimya kimya, Zelda akafunga
mlango wake, nakuwafuata kwenye gari. Willy akiomba kikombe alichokwisha nywea
kimuepuke. Kuzaa na Zelda! Willy alijawa na wasiwasi mpaka akaonyesha, ila
Pendo akamuacha tu maana alijiambia aliyafuata yeye mwenyewe huko kwa Zelda!
Apambane na hali yake.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Mtoto Wa Nani? Itajibiwa Sehemu Inayofuata.
Usipitwe.
0 Comments:
Post a Comment