Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 41. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 41.

Jack akacheka na kugeuka. “God! I was waiting for you!” Jack akaongea kwa kujiamini kitu kilichomshangaza Sabrina. “Nilikuwa nakusubiri sana. Sasa kama ulifikiri unapambana na Sabrina, jua unapambana na Simba anayelinda familia yake.” Jack akamsogelea. “Nimejiandaa na nakusubiria kwa hamu sana.” Jack akaweka msisitizo na kumtisha hata Tino kidogo. “Najua unazijua habari zangu kwa juu juu. Ila nakuhakikishia na ninauhakika, huko unakozisikia na kuzisoma habari zangu, za ubaba hazijawahi kusomeka wala kusikika. Ni Jackson Msindai mwingine kabisa. Niamini nikikwambia mimi, Jackson Msindai aliye baba, hutaki kumuona akisimamia familia yake, mtu anapotaka kuigusa, tena kwa hila.” Jack akaweka watoto wake vizuri hapo begani.

“Umeshaona ile sinema ya ‘Simba’?” Jack akamuuliza, Tino kimya. “Kaitafute, uitizame. Utaona jinsi lile dume linavyomlinda mtoto wake huyo Simba. Wala si mama ndio mlindaji, ila baba! Kwa hiyo kama mnafikiri mnatengeneza kesi dhidi ya Sabrina, nakusaidia, mnapambana na Jackson Msindai. Baba niliyepewa hicho cheo na Mungu na kukipokea kwa heshima kubwa sana. Nitapambana kwa kila pumzi niliyonayo hapa duniani, na Mungu atanisaidia na kunitetea. Nitapambana kwa uwezo wangu wote kuhakikisha nikimalizana na wewe, unaelewa na kujua, huna ulilobakiza hapa duniani. Kwa hiyo mkajipange sawasawa.” Jack akaongea kwa ujasiri mkubwa sana.

“Na nitahakikisha mpaka namalizana na wewe utakuwa kila ukisikia jina la Sabrina, utajua sio tambaa la deki la kusafishia matapishi kila unapotapika.” Jack akamsogelea zaidi akamkazia macho zaidi. “Utajua, utajuta na nitahakikisha unaelewa kuwa bahati huwa zinakuja mara moja tu. Na kwako ililetwa na Mungu, ukaiua kwa pesa yako mwenyewe. Sikutishi, ila nakuthibitishia, UTAELEWA. Nakukaribisha NIJARIBU.” Jack akatulia kama kumpa nafasi akimtizama. Mapacha wake waliokuwa wamejilaza begani wakatoa uso walipomsikia baba yao ameongeza sauti wakati anasema ‘NIJARIBU’. Wote kwa pamoja wakambusu Jack shavuni na kupiga makofi kama wanaojipongeza kwa walichofanya wenyewe kwa dad wao. Jack akarudisha akili kwao, akawabusu pale pale Tino akiwaangalia. Wakajirudisha begani.

Sabrina akasikika akicheka, kitu kilichomuudhi zaidi Tino mpaka akawa mwekundu. “Kama nilikuwa sijakutambulisha, basi huyo ndio Jack niliyekuwa nikikwambia habari zake. Na ndiye mume wangu.” Sabrina akawa kama amepata ujasiri akajisogeza mbele kidogo ili amuone vizuri Tino usoni. “Na nyinyi mtanitambua. Nikejelini tu, lakini nazijua haki zangu. Na mahakama itanitetea.” “Itakutetea kwenye haki yako. Na ndio kazi ya mahakama, kutoa haki za wananchi. Kama unahisi unahaki yako, hujaipata, au umenyang’anywa, basi kimbilia mahakamani kama ilivyo desturi yako. Maana nasikia wewe ni hodari wakudai hata visivyo halali yako kwa kumtumia mwanasheria wako Max, anayekusaidia kusuka kesi. Sasa safari hii, ujue umekutana na Simba. Nitanguruma, hutakaa ukanisahau wala kusogelea familia yangu tena.” Mpaka Sabrina akashangaa.

“Nimedai nini kisicho changu!?” Akauliza Tino kwa hasira. “Kudai mshahara usiofanyia kazi. Unaishi kwa jasho la watu wanaoamka kila siku asubuhi na kwenda kazini kufanya kazi na kuingizia kampuni faida, wakati wewe unajiliza kama mtoto mdogo kuwa ni mgonjwa. Unafikiri sikufahamu? Nakufahamu sana. Najua ulikuwa nchini Italy ukifanya shuguli zako binafsi, lakini wewe na mwanasheria wako mkidanganya upo kwenye matibabu uendelee kulipwa, wakati unafanya mafunzo ya uchoraji upate leseni ya kimataifa na kujifunza lugha, na ndio umerudi.” Sabrina akazidi kushangaa. Tino akaonekana ameingiwa hofu.

“Nakujua au ninawajua vizuri sana. Na ninazo picha ambazo Max alikutumia za watoto wangu, akikushauri uje uwadai.” “Ni damu yangu na mshahara ninaolipwa ni haki yangu.” Tino akajitetea akionyesha hasira ya waziwazi lakini wazi alionyesha kuishiwa nguvu, anajikaza tu. “Na ndivyo anavyokudanganya Max. Sasa mwambie Max, ninakuja kama moto, nikimalizana na yeye, hatakaa akawa mwanasheria tena hapa nchini. Nitahakikisha anawajibika kwa kosa lakuchukua picha yangu na watoto wangu na kusambaza bila idhini yangu huku akikuchochea wewe uje ufanye fujo kwetu. Mchochezi, mvunja amani na mvunaji asipopanda. Anatumia vifungu vya sheria vibaya, kujinufaisha. Kwa hiyo mwambie Maximilian Kundi, wakati anakutengenezea kesi dhidi yetu, ambayo kwanza kabisa hata kesi yenyewe tu, haipo. Kwa kuwa ulishaua watoto wako na ushahidi wote ninao na ukiri wa video wa daktari aliyeua watoto wako upo. Sasa mwambie ajiandae na kesi yake na yeye. Mwambie ninakuja, na sitamuacha.” Sabrina akashangaa sana na kuogopa. Tino mwenyewe akabaki ametoa macho.

“Ulifikiri nilipokwambia nakusubiria kwa hamu unafikiri nilikuwa nakudanganya? Uliona kimya kwa kuwa nilijua utasimamia ule usemi wako uliomjibu Max na kumkatia simu, alipokupigia simu ukiwa nchini Italy akikushawishi urudi nchini kudai watoto wangu, ili yeye atengeneze pesa zaidi kupitia wewe, ukajibu kwa hakika kabisa, watoto si wako, ni wa Sabrina.” Tino akazidi kuchanganyikiwa. “Nikajua unajielewa na kwa hakika ulikusudia kweli kutokuwa na watoto na mke wangu. Maana ulihatarisha maisha ya mpenzi wangu haswa ili tu  kuwaua watoto! Na hilo nitakuja kukulipiza tu. Ipo hukumu yake juu ya hilo. Endelea kunifuata fuata, nakuhakikishia utalipa ulichomtendea mke wangu.” Sabrina akajisikia vizuri, Jack akaendelea.

“Lakini kwa ule usemi wako uliompa Max kuwa, ‘watoto si wako ila ni wa Sabrina’, hakika nilikuheshimu sana. Nikajua hata kama wewe ni shetani mwenye roho mbaya ya namna gani, lakini unajielewa na unajua unachokitaka. Ndio maana nikakuacha. Sasa leo unakuja kunifanyia fujo mbele ya mke wangu na binti zangu! Hakika umeharibu Tino. Umemfungulia Simba mwenye njaa! Hamtabaki salama.” Junior kaka yake Jackson akaja. “Mmepotelea wapi nyinyi?”  Akauliza na kusogea pale waliposimama. Akakuta ile hali ya tension pale, ila wote kimya. “Vipi Dogo? Kila kitu kipo sawa hapa?” “Oooh yeah! Like never before!” Jack akajibu huku akimtizama Tino kibabe. Tino akaondoka akiwa mwekundu mpaka macho. Wakabaki wakimsindikiza kwa macho mpaka akapotea machoni kwao.

Jack akamgeukia kaka yake. “Naona tumefikia muafaka juu ya nyumba, kaka.” “Kwanza tukushukuru kwa kutufikiria shem. Asante sana.” Sabrina akadakia. “Na nyinyi mnajitahidi. Zaidi wewe Sabrina. Ni mke mzuri. Unamsaidia sana mwenzio. Am so proud of you two. Popote mtakapo kwama, mniambie.” Wakaangaliana. “Nini?” Junior akauliza. “Tunahitaji msaada wa fedha ili kuinunua hiyo nyumba kaka. Tukisema tutoe tu pesa kwenye akiba sasa hivi, wanangu watalala njaa.” Wakacheka.

“Na niwaambie kabisa, nyumba ni hazina ambayo hamtajutia. Hiki mlichoamua ni muhimu sana kwa kuwa hamjui maisha yatawapeleka wapi. Mnaweza kujikuta mnapata kitu kizuri zaidi huku Dar, ikawalazimu kurudi. Hamtaki kurudi mnaanza kuhangaika pakuishi.” “Ni kweli.” Sabrina akakubali. “Na pia mnaweza kufanyia biashara kama mimi na Joy tunavyofanya. Na nashauri kabla yakununua, mkaingalie. Joy aliipenda sana kwa kuwa imekamilika na ipo sehemu nzuri. Mwenye nayo alifariki, alitangulia mke, akaja yeye, ndio ndugu wanauza ili wagawane ndio maana bei ipo nzuri. Kesho nitawapeleka, leo inabidi niondoke. Nimeitwa.” Wakaelewa ni mambo yake ya kikazi. “Ila kesho nitakuwa na nafasi asubuhi kabla hamjaondoka.” “Tunashukuru sana kaka. Tutamshukuru na shem.” “Sawa sawa.” Akawaaga na kuondoka.

Jack Ampe kwa ufupi kilichokuwa kikiendelea kati ya

Max, Mama Kundi, & Tino. Sasa Usalama wa Taifa.

S

abrina akamwangalia Jack. “Nina mengi yakukuuliza, lakini naona tutazungumza vizuri usiku, baada ya kukupongeza vizuri tena kwa kituo.” Jack alicheka sana. “Nahitajika pongezi?” “Kubwa sana. Leo usiku ujiandae, utachoka wewe!” Jack akazidi kucheka. “Najilaumu wewe! Acha tu Jack. Nimejichelewesha mno! Lakini wewe! Hakika wewe ni wangu. The best dad and sweetheart in town.” Jack akajisikia vizuri sana. “Daah!” Sabrina bado hakuamini utetezi alioufanya Jack kwao. Jack alisimama kama dume kweli kweli akitetea familia yake, mpaka akamshangaza Sabrina.

“Turudi kwenye shuguli, wasije ona wametufanikishia ya watoto wetu, tumekimbia kumbe huyu mwendawazimu ndio ametuchelewesha hapa.” Wakaanza kuondoka. “Kwanza amenifanya niongee kitu ambacho nilitaka kuwashitukiza. Kosa la kusambaza picha zangu na wanangu!” “Ulijuaje Jack!?” “Umesahau mimi siku hizi mtu mkubwa sana? Nafikishiwa habari bila kuzitafuta.” Akajisifia kidogo Jack na kumfanya Sabrina acheke huku akimwangalia alivyojivuna. “Lakini Sabrina, acha tu. Niseme ukweli ni Mungu tu. Baada ya kuachana na Max siku ile uwanja wa ndege nikiwa nimemkatalia mawasiliano na wewe, kile kitu kikaendelea kunisumbua. Jinsi alivyokuwa akiwaangalia wanangu na wewe! Nikasumbuka sana moyoni. Nikapuuza kwa muda, lakini nikasema hapana. Lazima nimchunguze Max, kumjua yeye ni mtu wa namna gani. Nikamuomba mtu wa usalama anisaidie kumpeleleza.” Sabrina akajua ni dada yake tu ndiye aliyemuomba ampelelezee, maana Jacinta ni mtu mkubwa sana huko Usalama wa taifa.

“Sikutaka kukwambia ili nisikuogopeshe. Lakini Sabrina!” “Nini?” Sabrina akauliza. “Watu ni wabaya mke wangu. Yaani acha mama! Huyo mtu alipoanza uchunguzi, akakutana nao hao watu wawili pamoja na mkewe Max, yaani yule mtu mwenyewe akaniambia nijiandae kwa vita inayonijia mimi na familia yangu. Yalinaswa mazungumzo yao yote na mipango ya Max, kwa Tino na mkewe pia. Lakini alipoishia ushawishi kwa Tino, Max akiwa ameshamtumia picha za watoto wangu, ni kama aligonga mwamba. Kwa kuwa Tino alimjibu kwa ujasiri kabisa kuwa watoto ni wa Sabrina. Max alipoendelea kumlazimisha, Tino akawa mkali kabisa, akisisitiza kuwa watoto ni wa Sabrina na kumkatia simu kwa kuwa Max aliendelea kumsisitiza arudi watengeneze kesi kudai watoto wake kwani ni wazuri sana.” “Haiwezekani Jack!” Sabrina akashangaa sana kwa kuumia.

“Hakika Brina. Ndio kaka akasema lazima kuongeza umakini na kujipanga.” Sabrina akashituka sana. “Kwani Junior anajua!?” “Ilibidi Sabrina. Haya mambo yamechukua sura nyingine kubwa sana, kwani wamenasa na mazungumzo ya Max na mkewe ambaye anafanya kazi ofisi moja na kaka.” “Nakumbuka Max alisema siku ile.” “Sasa mkewe alionekana kumuonya Max asimshawishi Tino kudai watoto. Si kwa wema, ila kuhofia kazi yake. Sasa utachoka Max alichokusudia kukifanya dhidi ya Junior, kama bosi wa mkewe na waziri. Hapo sasa ikabidi kaka aambiwe na usalama wajulishwe rasimi ili akitekeleza sasa, kaka awe salama.” “Nini Jack!?” Sabrina akazidi kuchanganyikiwa kwani hakutaka kabisa mtu amjue baba wa watoto wake, ibakie tu Jackson Msindai.

“Max alimwambia mkewe, kabla kaka hajamgusa kumuharibia kazi wakati yeye Max anadai watoto wa Tino kwetu kisheria, wamtengenezee kesi kubwa na nzito.” “Junior!?” “Ndiyo. Mbaya eti hata wamtumie yeye mwenyewe mke wa Max. Sasa sijui aseme anamtaka kimapenzi au amembaka ofisini, hawakuweka wazi lakini alisikika Max akimwambia mkewe watamtengenezea kesi nzito dhidi ya huyo mkewe. Ili kwanza atumbuliwe na kumchafua haswa, ili kaka awapishe mjini.” “Jackson Msindai wewe! Max?” “Ni mbaya yule! Mimi mwenyewe sikuamini. Anaonekana anazisaka pesa kwa kila namna na ndio maana amemshikilia sana Tino ili kujinufaisha.” “Na Tino anamsikiliza sana. Yuko kama mjinga kwa Max.” Sabrina akachukia kabisa kila alipokuwa akimkumbuka Max na mazungumzo aliyokuwa akiyasikiliza kwa siri kati ya Max na Tino.

“Sasa kuanzia hapo ndipo ikabidi sasa uchunguzi wa kina uanze ili kujua tunapigana na nani. Ndipo sasa habari zao zikaanza kusakwa kwa kina tena zoote. Kwa kifupi, wanatizamwa kwa karibu mno na kesi yao imechukua sura kubwa zaidi nitakavyokwambia. Uchunguzi ukikamilika, utasikia tu. Lakini ujue Max alikuwa akipanga vita dhidi yetu. Angetushitukiza vibaya sana. Ni Mungu.” “Kweli ni Mungu Jack. Lakini nimeumia sana. Max amenipokonya kitu kikubwa na cha muhimu sana. Sikutaka uma umjue Tino kabisa. Sikutaka habari zake zijulikane na zihusishwe na  familia yangu. Max alimshauri Tino vibaya sana juu yangu. Kama haitoshi, amerudi tena kwenye hiki Mungu alichonibariki! Hakika naumia Jack.” Sabrina akalalamika kwa uchungua sana.

“Nisikilize Sabrina. Labda ni katika kujulikana tu Tino, lakini nitahakikisha hiki tulichonacho, hakuna atakayetupokonya hata Tino mwenyewe na Mungu atatusaidia.” Sabrina akanyamaza. “Hili jambo halipo chini yetu tu. Nakuhakikishia Max hatawahi kuja tena kuwa tatizo kwetu na kwa mtu mwingine. Subiri uone. Na sidhani hata kama atabakishiwa leseni ya uanasheria tena. Kikubwa na cha msingi ni sisi kujipanga na kuwa ukurasa mmoja pale tutakapohitajika kusimama mahakamani endapo Tino atatushitaki. Lakini napo tutamuwahi.” “Sijui Jack! Hakika Mungu aingilie kati. Tino hakutaka hawa watoto kabisa. Na Max alihakikisha anamshawishi Tino akiita ujauzito ni tatizo au niseme kosa. Akamwambia kwa kumsikia mwenyewe, ahakikishe haniachi na ujauzito. Asimamie na ahakikishe ananiacha na pesa tu, tena kwa maandishi. Iweje leo aanze tena kuibua kesi?” “Yeye anataka pesa tu. Wala si kwamba anakusuduia zuri kwa yeyote. Ukisikiliza mazungumzo yake na mkewe, ni pesa tu na umaarufu. Lakini Sabrina, Mungu yupo na sisi, hata hili litapita kwa namna ambayo Mungu atatupigania.” “Ni kweli Jack. Hapo umesema kweli. Mimi nitamlilia Mungu wangu mpaka nibakiwe na haki yangu.” Wakazungumza kidogo na kuamua kurudi walipoacha watu wengine.  

Mama Msindai na Shower ya Briyan.

W

akati wakitembea simu ya Jack ikaanza kuita mfukoni. “Nisaidie kutoa.” Akatoa. “Mama Msindai huyo.” “Pokea.” Sabrina akapokea. “Ni mimi Sabrina, Jack huyu hapa amebeba watoto.” Sabrina akawahi asije akasema neno lisilomuhusu. “Nataka kujua hiyo tarehe ya baby shower. Haitakuwa kubwa kwa kuwa ni mtoto wa tatu. Tunafanyia tu nyumbani.” Sabrina akaanza kucheka. “Mimi sijakupatia mwenzio mama! Ni nini lakini?” Jack akauliza kwa kulalamika. “Nataka nifanye maandalizi mapema. Kwanza nishachelewa kuwapa watu tarehe kamili. Unataka nianze kuonekana mbambaishaji?” “Kwamba ushawaambia watu kuwa kuna baby shower!?” Jack akashangaa sana. “Ndiyo! Hee! Ulitaka sasa nishitukize watu! Wewe mtoto vipi? Wewe niambie tarehe mtakayokuja, nijipange.” Wakamfikia alikuwa amesimama kama mlangoni kutokea upande wa beach. Sabrina akakata simu akicheka, nakuirudisha mfukoni kwa Jack.

“Kwa hiyo hapo ulikuwa ukitufuata?” Jack akamuuliza. “Ndiyo! Naona hatufikii muafaka halafu nasikia kesho mnaondoka, na sijasikia mipango ya kuja nyumbani! Umekuaje Jackson wewe!” “Naomba kabla hujapenyeza agenda ya kuja nyumbani kesho wakati unajua kabisa kilichotuleta hapa ni Pendo, naomba tumalize hilo la shower mama.” Sabrina akazidi kucheka pembeni ya Jack. “Sawa. Kwahiyo mnakuja lini kwa shower na kujifungua? Au mkija mnakuja moja kwa moja?” “Ni nini kinachokufanya ujue kama na kujifungua itakuwa ni huku na Singida?” “Bwana wee! Tushapita huko muda mrefu sana. Naomba nipe tarehe acha kupoteza muda.” Jack akamtizama mama yake asimmalize.

Akamgeukia Sabrina. “Unakuja lini? Mumeo anaweza akakufuata sio lazima ukamsubiria mpaka apate likizo kazini.” “Naomba zungumza na mimi mama.” “Wewe mbishi sana bwana! Jambo dogo tunavutana weee! Niambie Sabrina.” Akamgeukia Sabrina tena. “Tukifika tu Singida, tutakupa tarehe zote mama, wala usijali.” “Ona mambo yalivyo rahisi! Unataka kufanya mipango inakuwa migumuuu!” Akamalizia hivyo mama Msindai na kurudi kwenye kundi la watu, akamuacha Jack akimwangalia. Sabrina akaendelea kucheka.

Jumapili.

Kesho yake kabla yakuondoka jijini, Joy ambaye alikuwa akifanya biashara ya Real estate. Ananunua nyumba, anakarabati na kuuza au kupangisha, yeye ndiye aliyeona hiyo nyumba, akata wainunue wao sababu kwanza ilikuwa  sehemu nzuri sana, ilishakuwa na kisima kilichochimbwa na kujengewa vizuri, akapenda uzio wake, na bado ilikuwa mpya, haikuhitaji marekebisho yeyote, ni usafi tu na kuhamia hapo. Bei ndio iliyomchanganya zaidi. Alipomwambia mumewe, akamwambia hiyo itawafaa Jack na Sabrina.

Sabrina alipoiona, tamaa yakurudi kuishi Dar ikamwingia. “Hapa tunapata chumba cha kaka Briyan na dada zake wanapata chumba chao, na bado tunabakiwa na vyumba viwili mbali na chetu! Mungu atupe nini?” Joy akawa anacheka tu huku akiwaonyesha uzuri zaidi wa ile nyumba. Wakakubaliana wataichukua, waandikishane kila kitu, wao watatuma pesa kiasi, nyingine wawakopeshe. Joy akawahakikishia mpaka ifikapo jumatano nyumba itakuwa yao. Joy alikuwa na kampuni yake na wafanyakazi kabisa kwenye hiyo kampuni yake wanaomfanyia kazi. Kwa hayo alikuwa na uhakika wakuwakamilishia hiyo nyumba bila shida tena kwa haraka.

 Wakakutana kwa mama Msindai kwa chakula cha mchana. “Umefurahi sasa?” Jack akamuuliza mama yake. “Uwe unakumbuka kwenu, uache kujisahau.” Mama Msindai akamjibu hivyo. Lakini wote walishamjua huyo mama, akitaka kitu chake, atakaba mpaka kiwe. Jack na familia yake wakaondoka jijini kurudi nyumbani kwao.

Willy&Pendo.

Jumapili hiyo hiyo Willy na Pendo nao baada ya ibada wakaomba kuzungumza na mchungaji juu ya ndoa yao. Hawakuwa washirika wanaojihusisha sana na mambo ya hapo kanisani lakini walijulikana na watu baadhi. Na mchungaji alifahamiana na familia ya kina Ngoi zaidi. Aliwafahamu. Na ndipo kwenye kanisa hilo hilo walifanya ibada ya mazishi ya mama Ngoi. Kwa hiyo aliwajua Mzee Ngoi na mkewe zaidi. Alijua mengi yanayoendelea kwenye familia hiyo na alishafika mara kadhaa nyumbani kwa Ngoi enzi za uhai wa mama Ngoi akiwa mgonjwa kwa maombi hata hospitalini alipokuwa akilazwa, alikuwa akienda kuomba pamoja naye kwani mama Ngoi alikuwa mmoja wa viongozi walio mstari wa mbele hapo kanisani. Hata ndugu zake wengine walikuwa wakishiriki hapo japo sio washirika wa kila jumapili.

“Ni kama mmesambaratika sana Willium!” Mchungaji akaanza na Willy baada ya kutoa pongezi kwa Pendo. “Tupo.” Willy akajibu kwa ujumla. “Unawasiliana na ndugu zako? Sijawaona kanisani.” “Nafikiri majukumu yamekuwa mengi tu, lakini wapo.” Mchungaji akatulia kama kumpa nafasi kumsikia, maana majibu yake yalikuwa ya jumla kama anayeficha ukweli. Wakatulia tena kidogo Willy akitafuta pakuanzia. Akajiweka sawa, Pendo kimya na mchungaji kimya.

“Nataka kumuoa tena Pendo.” Akaanza Willy. Mchungaji akatulia. “Nataka utusaidie tufunge ndoa hapa kanisani. Nilitaka kujua utaratibu unakuaje.” “Ndoa ya kwanza nilifungisha mimi hapahapa kanisani. Labda niulize sababu ya kuvunjika.” Hapo likawa swali gumu sana. Willy akafikiria akatulia kidogo. “Kulitokea matatizo kidogo.” Akajibu Willy. “Udogo gani uliosababisha kuvunjika kwa ndoa, Willy?” Mchungaji akambana. “Kwa kurudi kanisani inamaana unakusudia kuanza upya. Sasa nilazima nijue kilichosababisha kuharibika kwa mwanzoni, ili turekebishe kabisa, pasitokee tena hilo tatizo unapoanza upya.” “Nilitoka nje ya ndoa, nikajua nimempa msichana mwingine mimba. Lakini mpango haikuwa kuachana na Pendo. Ilikuwa mtoto azaliwe, nizungumze na Pendo, akinisamehe, tuendelee huku nikilea mtoto wangu. Lakini mambo hayakwenda vizuri tukaishia kuachana, lakini nikarudi kwa Pendo, nimemuomba msamaha, amekubali turudiane, ndio nataka tufunge tena ndoa.” Willy akajieleza.

“Na unayemzungumzia hapa ni Zelda?” Wote wakashangaa kidogo mchungaji alipouliza hivyo. “Nataka uhakika.” “Ndiyo.” Willy akajibu. “Ni kitu gani kilikuthibitishia kuwa mtoto si wako?” Kidogo hilo swali likamfanya Willy kuingiwa na wasiwasi, akanyamaza. “Namfahamu Zelda na baba yako. Ukumbuke wazazi wako walikuwa washirika wazuri sana hapa. Hata ndoa ya baba yenu ya pili, alitaka ifungwe hapa.” “Walitaka!?” Willy akawa hajaelewa. “Nashauri kabla ya kuendelea na mpango huu wa Pendo. Kwa kuwa nimezungumza sana na Zelda. Kwa muda mrefu sana. Najua kilichokuwa kikiendelea. Na hayupo kwenye wakati mzuri na mtoto. Unahitaji...” “Sielewi mchungaji. Nini kinaendelea!?” Willy akawa haelewi, Pendo kimya.

“Ndio maana nakushauri kabla hujaendelea na hili lililowaleta hapa na Pendo, ili kusitokee kosa kama kosa la kwanza, mtafute Zelda mzungumze kwanza.” Wote wakabaki wakimtizama. “Siwezi kuzungumza mambo ya watu wanayoniamini nayo. Wewe nenda kazungumze naye yeye mwenyewe Zelda.” “Si bado anaishi pale kwa mzee?” Willy akauliza. “Sidhani. Nashauri umpigie.” Wasiwasi ukazidi kumwingia Willy, Pendo ndio zaidi. “Sina namba yake ya simu na wala sijawasiliana nao wote wawili tokea watufukuze nyumbani.” “Basi anzia kwa mzee wako.” “Siwezi.” Mchungaji akabaki kimya.

“Hao watu nilishachana nao muda mrefu sana na sitaki kurudi kwenye maisha yao.” “Nafikiri hilo huwezi kukwepa tena Willy. Na sitaweza kuendelea na hili mpaka nijue umefikia mwafaka na ulilolianzisha wewe mwenyewe kwa msaada wa mama yako, ndipo nitaweza kuwaunganisha nyinyi wawili tena. Lasivyo tutarudia mchezo uleule.” Wakatoka hapo kwa mchungaji wakiwa wamepoa, hawajui kwa uhakika ni nini kinaendelea. Pendo akajihisi anamkosi wakupitiliza.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Nini Kinaendelea kati ya Mzee Ngoi na Mpenzi Zelda?

Kilichobadilika kwa Tino na kurudi kudai watoto tena ni nini?

 Mazito na ya kusisimua yapo mbele.

Usipitwe.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment