Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 40. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 40.


Siku hiyo Pendo alirudishwa nyumbani akiwa amejawa furaha haswa. Mzima kabisa. Willy alikuwepo hospitalini wakati wakiruhusiwa. Lakini alikwenda kazini. Kwa kuwa alishapata baraka za wazazi, ikabakia yeye tu. Akaanza kupanga mipango ya kumvalisha pete. Mtu sahihi aliyemfikiria kwa haraka ambaye angemsaidia kuweka sawa mipango ambaye alijua Pendo ana mkubali akawa amebakia Sabrina pekee. Akaamua kumpigia simu.

Kwanza Sabrina hakuamini kama ni Willy. “Kwema!?” “Kwema kabisa. Habari za familia?” Willy akauliza. “Tunamshukuru Mungu hatujambo.” Sabrina akawa amemaliza. “Nataka kumuona Pendo.” Sabrina akacheka sana. “Sasa nataka kumvalisha pete ya uchumba. Najua furaha yake itakamilika, wewe ukiwepo.” “Mbona Mungu akubariki! Maana nilikuwa natafuta sababu yakunitoa humu ndani, sikuwa nayo.” Willy akacheka.

“Sasa wewe mpigie simu Jack. Mwambie lazima mimi niwepo. Ukimuweka sawa huyo, nakuja na timu yangu yote. Nimechoka kukaa humu ndani, na kucheza na watoto tu.” Willy akazidi kucheka. “Kwani hauji tena Dar kufanya baby shower ya huyo mtoto mwingine?” “Ukitaka kumuudhi Jack, mwambie mambo ya kuja Dar kwa baby shower.” “Kwa nini?” “Sijui walimwambia nini mume wangu juu ya baby shower ya hawa wanae wawili, naona amechukia, hataki tena. Kwanza hataki nije huko nisije nikajifungulia huko Dar.” Ndipo Willy akakumbuka hekaheka ya alipojifungua hao mapacha wakizungu pamoja na fujo alizosikia mama Misindai alitaka kufanya siku ya baby shower yao hao watoto lakini Jacinta akamtuliza.

 “Wewe mpigie simu mpange. Na uweke msisitizo Willy, lasivyo Jack hawezi kukubali. Hataki nifanye chochote au kwenda kokote, nalea tu hii mimba! Nimenenepa kwa kula na kulala kama Pendo ambaye yupo bed rest wakati mimi sina tatizo jamani!” Willy akazidi kucheka. “Nitafanya hivyo.” Wakazungumza kidogo, wakaagana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Uzuri ikawa jumapili hiyo ndiyo birthday ya mapacha wa Jack na Sabrina. Sabrina ana mimba ya miezi nane tayari, watoto wake wakawa wanatimiza mwaka. Ikawa rahisi kuweka mipango ya huko kuchumbiwa kwa Pendo kwa siri bila Pendo mwenyewe kujua. Wakamwambia Pendo wanakwenda kuwafanyia birthday yao Dar ambako yeye yupo, kwa kuwa hawezi kusafiri. Pendo alifurahia sana. “Na nguo zao mimi ndio nitanunua na...” “Sasa usianze shuguli Pendo, mwishowe Willy atatufukuza kwenu.” Wakacheka. “Aunt yao, Jacinta na Joy wamesema wataandaa sehemu ya kufanyia pamoja na keki. Wewe naomba upumzike.” “Waambie nguo ni mimi.” Pendo akaweka msisitizo. “Nguo tu, basi.” Wakacheka na kuendelea kuzungumza wawili hao ambao walikuwa hawakosi chakuzungumza.

Birthday ya Mapacha,

Na Kuchumbiwa tena Kwa Pendo.

S

abrina na familia yake walishukia nyumbani kwa Pendo ambako walishakuwa na chumba chao hapo. Wote na watoto wao walikuwa wakilala chumba kimoja. Ukiwaweka chini, wanasambaa kila mahali. Pendo alijitahidi kuwaandalia vitu kutokana na umri wao. Bado hawakuwa wakiweza kutembea wenyewe, wanashika sehemu ndipo wanatembea. Jacinta aliwaambia ameweka reservation, Cliff Hotel meza karibu na mchangani baharini ili watoto wote wacheze, hilo likawa limekaa vizuri. Wakakubaliana familia zote wakutane hapo kuanzia saa 9 mchana. Uzuri wakati wanafika hapo siku ya ijumaa jioni, ndugu wa Pendo nao walikuwepo. Kwa kuwa wote Sabrina alijua wana watoto, akawaomba mbele ya Pendo kuwa wawalete watoto wao ili wawaimbie Jeiline na Keiline. Bila kujijua Pendo naye akaweka msisitizo kwa mama zao wasikote. Basi mpango ukakamilika vizuri tu. Pendo hajui kama mlengwa ni yeye.

Ilipofika mchana, Sabrina na familia yake wakaondoka na gari ya Pendo, Willy na Pendo pamoja na msichana wao wa kazi wakaondoka na gari ya Willy. Familia hizo hawakuchelewa. Wakajikuta wamekuwa wengi. Familia ya Msindai wote mpaka wazazi. Junior waziri naye akawepo na familia yake. Familia ya Pendo wote. Mpaka wazazi, familia ya Kenton, na Nancy pia. Wazazi wa Sabrina wote wawili na Sabina pamoja na rafiki yake nao wakawepo.

Usingeshindwa kuzungumza na mzee Msindai. Alikuwa mcheshi mno na mtu wa utani. Hata baba yake Sabrina ambaye hakuwa msomi, alijisikia vizuri kuwa naye. Mazungumzo yake yalikuwa yakawaida sana ambayo hayakuhitaji kufikiria ila kucheka tu. Akiwa katikati ya kundi na hivyo alikuwa daktari wa watoto, mngecheka tu. Sasa wakakutana na Jackson mwanae wote wanapenda watoto. Michezo ikaanza ni vicheko hapo, Pendo asijue wote wamekusanyika hapo kwa ajili yake yeye.

Jack alikuwa busy na watoto wake hao wakizungu, utafikiri amezaa na mzungu. Na hao watoto walimjua Jack. Akiwepo mahali, akili na mawazo yao yote yapo kwa baba yao tu. Na hawatakubali mtu awaguse ila baba yao tu. Jack aliwabebea michezo yao akaisahau kwenye gari. “Sasa hapa tutafukuzwa Jack. Watazagaa hapa na kuvuta wageni wa watu. Naomba ukawaletee michezo yao, akili iwe kwenye michezo yao tu, tutulie.” Walishafika meza za pembeni na kusimama kwenye viti wakichekea watu huku wakimwangalia baba yao. “Waoneni jamani! Acha kuwapungia mkono bwana Jack! Waite.” Watu wakazidi kucheka. Jack akanyanyuka ili akafuate michezo. Walikuwa wakifuatana kila mahali kama mchwa.

Walipomuona baba yao ananyanyuka tu, wote wakaanza kurudi kwa haraka. “Nakuja sasa hivi, nisubirini.” Jack akawaambia, wote wakaanza kulia. Pendo akawaita ili wamfuate yeye. “Hapo walipo hakuna anayekumbuka jina lake hata mmoja.” Sabrina akafanya wacheke. “Njoo Jeiline, mama.” Bibi yao akaita. “Mimi nakwambia hapo hajijui kama yeye ni Jeiline, mama. Acha tu.” Na kweli huyo mtoto hata hakumwangalia bibi yake, macho kwa baba yao wakilia. “Kwa nini unasema hivyo?” Akauliza Pendo. “Labda baba yao aondoke ndio akili zao zinawarudia. Hata uwaite mpaka sauti ikauke, hakuna atakayekugeukia, akili na macho yao ni kwa baba yao tu. Mimi ninachofanya wakiwa wanacheza na baba yao nakwenda kuwakwapua.” Wakazidi kucheka. “Na hawatanyamaza mpaka baba yao awachukue hapo. Ukiwagusa ndio watazidi kulia.” Jack akarudi kuwachukua walishakuwa wekundu.

“Sasa Jack akitaka kutoka?” Akauliza Junior. “Inabidi kuwakimbia. Anawaingiza chumbani, anacheza nao na mimi naingia hapo. Michezo ikikolea. Ndipo Jack anatoka taratibu.” “Hawalii sasa wakigundua ameondoka?” “Na wao wanatoka hapo chumbani, wanaanza kumtafuta. Watamtafuta mpaka wakutane na mchezo mwingine, ndio wanatulia. Wanaingia kwenye kila chombo, kila mahali.” Wakacheka. “Muulizeni Sifa. Leo kawakuta wapo kwenye madroo ya jikoni. Wakifika, kama umeweka vitu humo, wanasaidiana. Wanatoa kila kitu, halafu wanaingia ndani na kukaa. Kama kuna sufuria wanazoweza kutoa kabatini, wanatoa, halafu wanaingia wao humo ndani. Na wanasaidiana mpaka kila mmoja apate pakuingia, ndio wanatulia.” Watu wakazidi kucheka. Ungependa kuwaona hao watoto. Walishakuwa na nywele ndefu za kuanguka mabegani. Lakini kwa kuwa bado zilikuwa zakizungu, zinateleza kusukika, walikuwa wakiegeshwa riboni tu zenye ua. Ungependa kuwaangalia.

Willy na Jack wakaongozana kwenye gari huku Jack amewabeba juu akiwaendesha kama ndege, basi walikuwa wakicheka sana na machozi shavuni. “Ila wana michezo yao ya kujenga. Hiyo ukiwawekea sehemu wanayomuona baba yao, wanatulia na kujenga kwa muda mrefu tu, hutawaona wanazunguka.” Sabrina akaendelea kujibu kila wakiuliza juu ya hao watoto. Kwa kuwa wao ndio walikuwa watoto zaidi pale, walivuta macho ya wote na masikio.

“Jack anawapenda hao watoto! Kutwa anatuma video zao na story zao haziishi. Ukitaka Jack acheke, muulizie wanae.” Jacinta akaongeza. “Na ukita mzungumze jambo la maana, asiwe na hao watoto. Hana cha maana anachoongea. Akiwa nao hapo nyumbani, nakuwa na watoto watatu. Ukimwambia watoe watoto ndani ya masufuria, anakwambia na yeye mwenyewe anatamani kama angekuwa na uwezo wa kukaa humo ndani ya hayo masufuria ili apate ule ubaridi wake.” Mpaka mama yake Jack akacheka. “Hana analozungumza la maana mkaelewana akiwa na watoto. Wala hana analofikiria. Mkiwapeleka watoto kucheza ziwani, ujue unarudi na watoto watatu wote wamejaa mchanga ni wakusafisha usiku kucha!” “Na Jack?” Pendo akauliza huku akicheka. “Na Jack, ndiyo. Mnalala usiku mito inajaa michanga, basi hamuwezi tena kulala. Inabidi uamke uanze na yeye kumkwangua kichwa kumtoa michanga!” Wakazidi kucheka. Jack akarudi na wanae akiwa amewashika mkono wanatembea.

Joy akaona alete keki wakate, wamalize la watoto ili kumpa nafasi Willy. “Nilikuwa namuuliza mke mwenzangu juu ya baby shower ya dume.” Joy akamchokoza Jack wakati anasimama. Jack akamwangalia Sabrina. “Mbona unaniangalia mimi, wakati anazungumza na wewe?” “Sabrina akakujibuje?” Jack akauliza wote wakacheka. “Sijaelewa jibu lake.” Joy akatumia akili kwa haraka akajibu hivyo. Jack akamwangalia tena Sabrina. “Sasa mimi nimefanya nini Jack!?” “Wameshaanza kukushawishi na wakati tulikubaliana kabisa, Sabrina.” Wakaanza kucheka. “Hakika sijashawishika.” “Kwani hamtaki baby shower?” Sabina akauliza.

“Hatutaki baby shower. Au sitaki baby shower. Anayetaka kumpa mtoto zawadi, anakaribishwa. Lakini sitaki baby shower, na huyo mtoto anazaliwa Singida wala si hapa. Sitaki hekaheka nyingine.” Jack akaweka msisitizo. Kila mtu akakumbuka walipozaliwa hao wazungu. “Na masharti ya mimi kuwepo hapa leo ni nisije kushawishika hata mama Msindai aseme nini!” Sabrina akaongea kwa sauti ya chini lakini wote wakacheka. “Wewe msikilize tu Jack.” “Umeanza mama. Nilishakwambia hapana, na tunabakia na hapana. Si ndivyo Sabrina?” “Yeah! Kama alivyosema Jack.” Jibu ya Sabrina ikawafanya wote wacheke. “Mimi naona muda wakuondoka hapa unakaribia. Joy naomba keki, wanangu wakate, tuwahi ndege ya Singida, jioni hiihii.” “Acha hizo Jack!” “Sabrina anakosa msimamo kaka. Atashawishiwa na mama, utashangaa tunarudi hapa wakati hali yake sio yakusafiri safiri! Atazalia kwenye ndege bure!” Jack akakaa chini kabisa mchangani na watoto wake. Wakaangaliana hao watoto na kucheka kama kawaida yao wakipiga makofi.

“Sasa huko Singida mnadaktari mzuri wa kukusaidia siku ya kujifungua?” “Nakusikia mama. Naomba hayo maswali niulize mimi, wewe muache Sabrina.” Kila mtu akacheka. “Na huko Singida watoto wanazaliwa kila siku wala Sabrina hatakuwa wa kwanza. Na kujibu swali lako, anaye daktari mzuri sana. Hata baba anamfahamu na kumsifia.” “Na wewe Msindai mambo mengine usiwe na haraka kujibu, uwe unaniuliza mimi kwanza!” Wakazidi kucheka. “Ili anidanganye na kunitia hofu?” Jack akauliza huku akijenga mchangani na wanae. “Jiachie tu mama. Hiyo baby shower wala haitakuwepo.” “Wala siachi. Si kirahisi hivyo!” “Wala hadanganyi huyo Sabrina. Niulize mimi.” Wote wakacheka Jacinta alivyosema hivyo. Walimjua mama Msindai.

“Naomba muache Sabrina mama. Wewe zungumza na mimi.” “Ndio usikilize sasa. Kila mtoto anakuja na baraka zake na furaha yake. Kwa nini huyu asikaribishwe vizuri?” “Basi tutaandaa kule Singida, tutawakaribisha mje. Lakini sio hapa Dar. Hiyo pesa tunayotumia kwa tiketi za kwenda nakurudi si tungenunulia hizo diaper?” Jack akasimama. “Twendeni wanangu tukacheze mbali na mama Msindai.” Wakazidi kucheka. “Hutaki tena?” “Mimi namjua mama, hatakunywa maji leo mpaka nikubali.” “Joy ameenda kuleta keki.” “Mtatuita.” Jack akabeba wanae, akamuomba Claire ambebee michezo ya wanae wakaondoka watu wakicheka.

Keki ikaletwa, Joy akaandaa meza vizuri wakaitwa wote. Wakawaimbia Jeiline na Keiline wakiwa wamekaa juu ya meza wanapiga makofi huku wakimwangalia baba yao tu. Jack akawasaidia kuzima mishumaa. Wakaingiza mikono wala sio kisu. “Ustaarabu wa Singida huu!” Sabrina akaongea wakicheka. Wote wawili wakawa wanataka kumpa Jack. Wanashindana. Wakamshika shati na kusimama wakiwa na keki mkononi. Kila mtu anacheka. “Sasa mpeane zamu jamani. Dad atakulaje hivyo?” Jack akafungua mdomo, Keiline akawa wakwanza kumuwekea keki baba yake, Jack hakufunga mdomo, Jeiline naye akamlisha. Ndio Jack akafunga mdomo kila mtu akacheka. “Ndio kazi yao hata nyumbani. Sasa subirini muone, hawajamaliza.” Wakashangaa wote kwa pamoja wanambusu kila mmoja shavu lake, halafu wakajipigia makofi. Kila mtu akacheka na kupiga makofi.

Ungejua tu hao watoto wanampenda Jack. Akili na mawazo yao yote yako kwa Jack kila wakati. “Haya mlisheni na mama yenu nyinyi watoto!” Pendo akawageuzia kule kwenye keki tena. Wakachukua keki na kufanya kama walivyofanya mwanzoni. Wakampa Jack. Watu wakazidi kucheka. “Mbona hapo kazi washamaliza!a Mimi tena ndio basi. Waone wanavyocheka kama mazuri.” “Watakupa mama, njaa za nini? Acha mimi nilishwe.” “Basi utamaliza keki nzima wakati wenzio tunataka na sisi kula.” Jack alijazwa keki mdomoni. Akawalisha na wao kwa pamoja. Wakacheka na kupiga tena makofi. Akawashikisha keki na kuwasaidia kumlisha mama yao. “Umeridhika sasa?” Jack akamuuliza Sabrina. “Mbona mimi mara moja tu!” Watu wote wakacheka. “Basi hiyo keki mtamaliza wenyewe na watoto wenu.” Jacinta akafanya wacheke. Wakawa na wakati mzuri hapo wakicheka.

Penzi La Mpaka Kifo.

W

akati bado watu wamekusanyika hapo, wakila keki wakati wanasubiria chakula kiletwe, Jack akaomba watulie kidogo. Kwa kuwa walijua kinachoendelea wote wakawaambia watoto wao watulie. Pendo akashangaa Jack aliyesema watu watulie, anamwangalia Willy. Willy akamsogelea Pendo pale alipokuwa amekaa, akapiga goti. Pendo akashangaa sana, akamwangalia baba yake na kukunja uso. Baba yake akacheka na kurudisha macho kwa Willy aliyekuwa amepiga goti mbele yake. Akahema mara mbili na ya tatu. Watu wakcheka. “Daah!” Akasikika Willy na kufanya watu wacheke. Akamvuta mikono yote Pendo aliyekuwa amekaa na tumbo lake hapo kitini.

“Pendo, maisha yamenipa nafasi ya pili mbali na wewe. Nikazunguka na kuhangaika, lakini bado moyo wangu unajikuta nakuchagua wewe tu.” Watu wakapiga makofi kushangilia. “Na ninajua kabisa, hata nitoke tena, bado nitakuchagua tu wewe, tena na tena. Narudi kwako si kwa sababu ya watoto, lakini ni kwa ajili yako wewe Pendo.” Hapo watu wakatulia.

“Kuna siku nililala kwenye gari nikiwa peke yangu sijui pakwenda. Nimechanganyikiwa, lakini mtu pekee niliyekuwa nikimfikiria ni wewe. Nikatamani kukupigia kukwambia ninapopitia na nilipo, lakini nikajua nastahili kila pigo ninalopitia.” Willy akaendelea. “Nikapata kazi nzuri, nikatamani kumwambia mtu kuwa ndoto zangu zimetia, lakini nikajikuta ni mpweke zaidi kwa kuwa haukuwepo kwenye maisha yangu, Pendo. Ninachotaka kusema, nataka kurudi nyumbani, kwako. Sio kwenye kile chumba ninacholala sasa hivi.” Watu wakacheka. “Nataka kukuoa tena, uwe mke wangu. Ni sawa?” Chozi la Pendo lilishafika kifuani. Hakutegemea wala kutarajia. Akamwangalia Sabrina, Sabrina akacheka. “Nakupenda Willy.” Pendo akajibu wote wakashangilia. Willy akamvalisha pete nzuri sana ya uchumba na kuanza kumbusu.

“Kwani kila mtu anakuwa bibi harusi mara mbili, dad?” Claire akamuuliza baba yake wote wakacheka. “Na mimi nataka kuwa bibi harusi mara mbili.” Claire akaongeza nakufanya wazidi kucheka. “Mjibu sasa mtoto.” Mama Msindai akafanya wazidi kucheka. “Mwanao anataka harusi mbili kama auntie Pendo.” “Mimi naona kwa sasa tuombe uwe unasimamia tu. Utakuwa umesimamia mara mbili.” Baba yake akajibu nakufanya wote wazidi kucheka. “Kwa hiyo utaniombea?” “Nitawaomba baadaye.” Baba yake akamtuliza. “Kwani tunaoana tena kama zamani?!”  Pendo akauliza kwa mshangao, wote wakacheka. “Kabisa. Nimeuliza taratibu za mahari, naona nimesamehewa mahari.” Wakacheka. “Lakini nataka kuwapa mkono wa shukurani wazazi wangu kwa kuwa na wewe kipindi hicho cha miezi mitano nilipokuwa sipo.” Akamfanyia ishara Jack, Jack akaelewa. Akatoka hapo akiwa amebeba watoto wake.

“Naomba msubiri kidogo.” Willy akaongea akisugua mikono kama aliyepatwa wasiwasi tena na anachotaka kufanya. Watu wakacheka wakisubiria. Baada ya muda kidogo, Jack na wanae wakarudi na muhudumu akiwa amebeba mifuko, wazi ilionekana ni ya nguo. Wakasogea mpaka pale. Kenton naye alikuwepo. “Hii ni suti ya baba, akipenda anaweza kuvaa siku ya harusi yetu.” Willy akamkabidhi, watu wakapiga makofi. “Na hii ni nguo ya mama. Shemeji yangu Nancy amenisaidia kuchagua. Asante sana mama.” Wakapiga tena makofi yakushangilia. “Jamani mimi nilibarikiwa wakwe wazuri, najua wote ni mashahidi.” Willy akafanya watu wacheke na kushangilia. “Sijamaliza. Na hii ni bahasha yao. Najenga. Kwa hiyo hiki ni kidogo tu, kusema asante.” Akamkabidhi baba yake Pendo. Pendo akiwa haamini. Wakashangilia hapo na pongezi zikaendelea.

“Sasa mbona wasimamizi wenu hawapo?”  Akauliza Joy. “Ile ndoa ilikufa, tunaanza upya. Ndoa mpya, na watu wapya.” Akajibu Willy. “Nataka Sabrina na Jack watusimamie.” Pendo akafanya wacheke. “Sasa na tumbo hili wewe Pendo!” “Nataka huo upako wako Sabrina. Tumepita kwingi sana mimi na wewe, nataka uwepo kwenye maisha yangu daima.” Sabrina akasimama na kumkumbatia Pendo. “Wale wasimamizi wa kwanza waliniumiza sana. Walinikatisha tamaa na kumwambia Willy anajidhalilisha kuendelea kwenda kutoa mbegu hospitalini, mimi sina uwezo wa kuzaa.” “Jamani!” Wote wakashangaa. “Kweli tena. Muulizeni Willy. Lakini Sabrina amekuwa na mimi, akaamsha ari ya kuwa mjamzito. Akaniombea, tena ndani ya gari nikiwa na mimi naongea lugha yakushindwa kama wengine na akiwepo daktari pia aliyekuwa akisema sitaweza kuja kushika mimba.” Pendo akaongea kwa upole.

“Nikamkatisha tamaa Sabrina. Nikamwambia asijisumbue hata kuomba. Umri umepita na sina mayai. Sabrina akaniambia yeye ana mwita Mungu anayependa kutembea kwenye magumu na mtenda miujiza. Akaniambia nitembee kwenye imani yake yeye, atanibeba tu. Mimi nitulie nishuhudie kile Mungu atafanya. Nakumbuka akaanza kuniombea kwenye gari mpaka Jack akaja, akatukuta kwenye gari akaungana kuomba na sisi. Ilikuwa siku ya baby shower yake.” “Unakumbuka na maombi aliyoomba Sabrina siku ile ukumbini?” Akauliza Jacinta.

“Na kweli ulipokea kwa kiwango ulichokuwa umejitoa Pendo. Ulijitoa sana kwa Sabrina.” “Mpaka leo Pendo anajitoa kwangu mimi na Jack pamoja na watoto wetu. Mungu amekutendea dada yangu na amekurudishia ndoa yako.” Wakacheka, “Na unakumbuka usemi wako wa Mungu atanitendea jambo zito, mpaka watakaosikia masikio yatawasha?” Wote wakacheka. “Jamani Mungu ananitendea, acheni niwape ushuhuda juu ya yale Mungu amenitende.” Watu wakatulia.

“Huyu Mungu wa Sabrina, anashangaza watu na madaktari wanaotuhudumia mimi na wanangu. Vimbe nilizokuwa nazo, muulizeni mama. Zilikuwa Zimeota huko tumboni kama uyoga! Watoto wakikua, na zenyewe zinakuwa zinamaliza damu mwilini mwangu. Majuzi nilipandisha pressure, nikajua ndio shetani anataka kumaliza wanangu, kumbe ndio ilikuwa njia ya mimi kurudi hospitalini kupewa habari njema. Nikidhani watoto wangu watatoka kabla ya siku sababu ya pressure, waliponifanyia ultrasound ndio wakakuta zinanywea. Jana tumerudi tena na Willy hospitalini, wakatuthibitishia kabisa kuwa ni kama zimenywea kabisa, wanangu wananafasi yakukua. Na...” Wakati Pendo akishuhudia, Jack akashangaa mkewe amepotea pale kimawazo, anaangalia kwa wasiwasi kwenye kona ingine kabisa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Taratibu na yeye akageuka. Akashangaa hakuna kitu cha ajabu kinachomfanya mkewe ashangae huko alipokuwa amepotelea mawazoni ila wateja tu wakawaida. Akazunguka kule alipokuwa amekaa mkewe, akambusu kichwani na kumsugua na mguu wa Keiline aliokuwa amewabeba wanasinzia. Sabrina akanyanyua uso kumtizama. Akamuona amebadilika kabisa usoni. Akajua kuna jambo. “Twende ukanisaidie kuwabadilisha hawa, niwapakate walale.” Akamnong’oneza kwa sauti ya chini. Ilikuwa njia yakumtoa pale. Sabrina akamuaga Pendo wakatoka.

Wakaelekea ndani ili kutafuta sehemu ya kusafisha hao watoto na kuwabadilisha nguo hizo zilizokuwa zimejaa michanga na keki ili wapate usingizi wa mchana, Jack alikuwa amewabeba wote wawili. Wamejilaza kila mmoja pembeni ya shino ya baba yao. “Upo sawa?” “Naona nikuchoka tu.” Jack akasimama mbele yake na kumwangalia kama vile anayemwambia nipe ukweli. Sabrina akahema kwa nguvu na kugeuka nyuma kama kuangalia kama kuna mtu anawasikiliza.

“Ni nini hicho kilichokuogopesha gafla?” “Nina uhakika yule aliyekuwa amekaa pale akikuangalia sana jinsi unavyocheza na watoto ni Tino.” Kwa sekunde kadhaa Jack akabaki akimtizama. Sabrina naye akabaki kimya kama hajui aseme nini tena. “Kwa hiyo!?” Jack akauliza kwa mshangao kidogo. “Sijui Jack! Nahisi sikutegemea kumuona au sitaki kumuona tena. Na jinsi alivyokuwa akikuangalia ulivyokuwa na hao watoto, sijapenda.” “Niambie wasiwasi wako ulipo.” Jack akawa ametulia tu. “Itakuaje akianza kutusumbua? Tino ni mtu wa kesi kesi sana.” Jack akakunja uso. “Anatusumbuaje? Labda sielewi Brina. Kuwa muwazi zaidi.” Sabrina akavuta pumzi kwa nguvu na kutafuta jinsi yakueleza.

“Napenda familia yangu Jack. Napenda amani na utulivu tulionao mimi na wewe pamoja na watoto wetu. Sitaki ije itokee siku moja tunapoteza hiki tulichonacho sasa hivi.” “Labda kifo. Lakini hivi wanne tulivyo, tutabakia hivyo labda Mungu atuongezee mwingine au amchukue mmoja wetu.” Jack akaongea kwa uhakika lakini Sabrina akabaki na wasiwasi usoni.

“Niangalie mimi Brina.” Sabrina akamwangalia. “Tino hana chake hapa. Aliua watoto wake yeye mwenyewe kwa pesa yake. Hawa watoto ni wangu Mungu amenipa, hakuna atakayeninyang’anya. Asikutishe kwa kesi za kipuuzi alizokuwa akishinda. Hawa ni wanangu, hakuna mwanasheria wala pesa itakayoweza kutoa hawa watoto mikononi mwangu.” Ikamgusa sana Sabrina. “Kweli Jack?” “Hujanijua linapofika swala la familia yangu. Kwanza nashangaa hata kwa nini umuhofie! Huna anachokudai. Alikuacha akiwa ameridhika mmeua watoto wenu. Hawa ni wangu mimi na wewe. Usitishwe na uzungu wao, hawa.” Sabrina akacheka na kuwaangalia wanae.

“Kila siku natamani niamke niwakute wamebadilika angalau wafifie hiyo rangi, tufanane nao kidogo!” “Mimi nataka waendelee kuwa hivi hivi binti zangu. Wakati Mungu alipotupa hawa watoto, alitupa wakiwa wamekamilika. Hakufanya kazi nusu. Aliwaleta kwetu akijua sisi ni weusi, wao weupe. Watakuwa wakijipenda na kujithamini vile walivyo jaliwa na Mungu. Siwaonei aibu, na wala sina sababu yakujificha nao. Ni wanangu, na nitawalinda na kila mtu hata iweje.” “Akitaka kuwa anawaona?” “Huyo Tino!?” “Ndiyo Jack.” Jack akacheka kwa kujiamini. “Hivi wewe Sabrina nahisi hujanielewa vizuri. Awaone kina nani!? Yeye akiwa kama nani kwanza!?” Jack akauliza kwa mshangao sana.

“Eti Brina? Wewe ulishaona wapi mtu anakwenda kwenye familia za watu na kuanza kudai kuona watoto wao? Yeye si rafiki yangu, wala ndugu yangu mimi wala wewe. Anaona wanangu wa nini? Haitakaa ikatokea Brina. Kama vile nilivyomkatalia mwanasheria wake usoni ndivyo itakuwa kwake hivyo hivyo. Hakika mwache aje. Namsubiria kwa hamu sana.” Jack akaongeza kwa uhakika kabisa.

“Nitataka aje atuambie sisi kama wazazi wa hawa watoto na aelezee uma hicho kitakachokuwa kimebadilika ni kipi! Atake kuwaua tena kwa kukubembeleza, mpaka kukusindikiza hospitalini na kulipia garama zote za mauji yao. Akajiridhisha wamekufa ndipo akapata amani ya kukuacha kuwa huna mnachodaiana, halafu eti leo huyo muuaji atake kuwaona! Wewe unanitania Sabrina! Hakuna mahakama nitashindwa kuingia kulipigania hilo na kuhakikisha namuwekea restrain order, hata asiwasogelee wanangu. Akitimiza adhima yake  ya kuwaua pindi atakapofanikiwa kuwa nao karibu! Usinitanie kabisa. Hakika mwache aje, ndipo atanitambua.” Sabrina akajishika tumbo na kulipapasa kama aliyeridhika.

“Na wewe wala usimuogope. Hata ukikutana naye uso kwa uso, tembea kama jasiri. Hakudai na wala huna watoto wake. Alilipa pesa nyingi sana muue watoto wake. Na walishakufa, hawa watoto ni wetu mimi na wewe, na kaka yao anakuja. Na hatutaki baby shower.” Sabrina akacheka sana. “Naomba uwe na msimamo katika hilo Brina bwana! Acha kuwa njia panda.” “Mimi nataka.” Jack akatoa macho. “Huyu mtoto atazaliwa tu bwana, Jack! Acha kuwa na wasiwasi na wewe.” “Hapana Sabrina. Unakumbuka shida tuliyopata ulipojifungua hawa? Walikugeuka.” “Sasa huyu Msindai mwenyewe, watanigeuka nini na wewe?” Jack akashangaa sana.

“Wewe huoni kama wanafanya upendeleo!?” “Ndiyo, wanafanya upendeleo, lakini si wote ni wetu! Acha mama amfurahie mjukuu wake. Wewe unakumbuka alipopitia Willy na mama yake?” Jack akanyamaza. “Hawa wazee wanapenda wajukuu zao Jack. Maamuzi na maisha mabaya niliyoishi mimi zamani, yasimpunje na kumfanya huyu mwanangu akalipa garama yake.” Akajishika tena tumbo.

“Acha bibi yake amfanyie kile atakacho. Hayo mengine sisi tutajua jinsi ya kuyasawazisha tukiwa na watoto wetu nyumbani. Lakini usimzue kwa kuwa anachokifanya si kibaya. Ukubali ukatae, huyu ndiye mjukuu wake.” “Sasa hapo unataka kuharibu Brina.” “Ni ukweli ambao unataka kuupinga kwa nguvu nyingi bila sababu! Mwache dume langu likaribishwe kwa furaha zote. Kwanza wewe umeona wabibi wangapi wanahangaika na wajukuu zao kwa kiasi hiki? Hii ni baraka ya mwanangu, Mungu ameruhusu kwa makusudi kwa ajili yake yeye Briyan, mwache mwanangu apokee.” Sabrina akaongea bila wasiwasi.

“Hivi unajua ule mfuko aliokuja nao asubuhi pale nyumbani umejaa nguo zake huyu kaka yao?” “Haiwezekani Sabrina!” Sabrina akacheka. “Kabisa. Ila akaleta na vibanio vya nywele vya hawa wadada. Sasa kuna hasara gani, wakati na huyu ni wetu?” “Sikujua! Mimi nilijua ameleta zawadi za kina Jeiline!” Jack akashangaa sana. “Hata mimi. Lakini akanifuata chumbani na kuniambia kabisa, anataka nguo za kwanza atakazovaa Briyan ziwe zakutoka kwake.” “Haiwezekani Brina!” “Kabisa. Lakini wewe jiulize Jack, ubaya upo wapi!? Angekususia kabisa kwa kuwapokea hawa na kujitenga moja kwa moja! Ungefanya nini? Ungepoteza mahusiano mazuri sana uliyonayo na mama yako. Na ninakujua Jack, ingekutesa sana. Sasa Mungu amekurudishia mama, tena anataka na mjukuu niliyezaa mimi! Tatizo liko wapi?” Jack akanyamaza akimtafakari mama yake.

“Mwenzio nikacheka na kufurahia. Alete tu. Briyan ni mwanangu kama Jeiline na Keiline. Na yeye ni mama yako. Huwezi kumbadilisha atakachojisikia kwao, na maadamu sasa hivi anawaita wajukuu, unataka nini tena! Mambo mengine yaache tu kuwe na amani. Hautakaa ukapata mama mwingine. Naomba tumchukulie hivyo hivyo atakavyotujia.” “Ila sifurahii Brina. Sipendi.” “Mimi sijui ni kwa nini Jack! Hata hainikeri hata kidogo! Nina amani, sana tu. Sijui ni kwa kuwa naona wameshapata upendo mkubwa sana kutoka kwako!” Jack akamwangalia.

“Kweli Jack. Waangalie hapo walipo.” Jack akawachungulia akakuta wametulia kimya. “Wanasinzia.” “Sasa ndio nakuuliza Jack, unavyowaona hao watoto, wanahitaji upendo mwingine zaidi ya huo?” Jack akacheka. “Kwanza wenyewe hawataki!” Wote wakacheka. “Akili na mawazo yao yapo kwa mtu mmoja tu, wewe. Basi. Sasa leo unataka iweje? Mimi mwenyewe nadhani ningekuwa nao peke yangu nisingeweza kuwapenda hivyo.”  Jack akajisikia vizuri sana kuona Sabrina anaona na kuthamini mapenzi aliyonayo kwa hao watoto. “Kama wewe umeridhia sawa Brina. Mimi sikutaka upendeleo.” “Wewe mwache mwanangu apate upendeleo. Ndilo aliloandikiwa na Mungu.” Jack akacheka huku akifikiria. Wakaelekea sehemu ya kubadilishia nguo watu wanaenda kuogelea. Nje tu.

“Tukiwaogesha watachangamka, heri tuwafute tu.” Jack akacheka. “Si ndio vizuri wacheze! Leo siku yao bwana! Waache.” “Wanazagaa sana bwana, watu wanashindwa kufanya mambo yao inakuwa ni wao tu!” “Hata! Si kosa la wanangu. Kama wao wanavutiwa na uzuri wao ni tatizo lao, nitashindwa kuwasaidia.” “Basi na wewe uwafundishe kukubali watu Jack. Watoto gani hawataki kuguswa.” “Hawawajui je! Unataka wawakubali ili iweje? Wawasalimie hivyohivyo kwa mbali. Wawaache wanangu.” Wakasaidiana kuwasafisha na kuwabadili. Wakachangamka kweli na kuanza kupiga makofi. “Si nilikwambia wewe! Ona walivyotoa macho.” Jack akawa anacheka nao bila wasiwasi.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Umelichulia vipi swala la nyumba aliyokwambia shem? Hiyo bei ni rahisi sana Jack. Tunaweza tusipate dili nzuri kama hilo tena.” “Kwa hiyo upo tayari tukope kwa ajili hiyo?” “Sasa hivi hatuna hiyo pesa, ila huwezi kujua kesho yetu mpenzi wangu. Kwanza unaweza kujikuta hiyo nyumba ikaja kujilipa yenyewe. Tuichukue, kama kuna kukarabati, tukarabati na kuikodisha. Hata kama sasa hivi pesa inasumbua, lakini huwezi kujua kesho! Tukiwa na nyumba kule Singida na Dar, sio jambo baya. Na uzuri unamkopa kaka yako, hakuna riba, hatuna chakupoteza.” Jack akashawishika. “Basi kabla yakuondoka, nitamwambia atusindikize tukaone nyumba yenyewe tusije uziwa mbuzi kwenye gunia.” Hilo wakakubaliana bila shida.

“Lakini ujue mama atakuomba uje ujifungulie nyumbani.” Sabrina akatulia kidogo. “Ndivyo alivyokwambia?” Sabrina akauliza. “Aliniomba kama mwezi umepita, nikamkatalia. Akaja kukumbushia tena na akaniambia atazungumza na wewe.” Hapo Sabrina akapoa. “Huna sababu ya kukubali.” “Nafikiria tu.” “Unafikiria nini?” “Nilitaka mama awepo kunisaidia. Ukumbuke nitakuwa na watoto watatu Jack! Halafu ukweni! Naona kama sitakuwa na uhuru.” “Tunaweza tusikae sana. Hata juma moja tu.” Sabrina akajua na yeye anataka.

“Kwa hiyo na wewe ndivyo unavyotamani iwe?” “Sio lazima.” Akajitoa Jack kama kuepuka lawama. “Lakini unatamani iwe hivyo?” Sabrina akambana. “Sio mbaya. Lakini unajua mimi nitakuwa na wewe Brina. Usiogope.” Sabrina akacheka moyoni. Akambusu mdomoni. “Wakati wote upo na mimi Jack. Na ndio maana unaniona naishi bila hofu. Umekuwa kimbilio langu tokea chuo. Sasa kama hili ndilo unataka liwe kwa huyu au bibi yake anataka iwe hivyo, sawa. Mimi sina shida na wala sina kinyongo. Watoto wote ni wangu. Na hata hao uliowapakata hapo wakikuchekea na kukulamba kama pipi ni wangu tu!” Jack akacheka na kuwabusu kichwani. “Bwana mimi napendwa!” Jack akajisifia. Sabrina akacheka huku akiwatizama wanae. “Basi hata hao yupo atakayewapenda tofauti tofauti. Ujiandae na kwenda na upepo.” Wakasimama huku wakirukaruka hapo miguuni kwa baba yao.

“Sasa tusikae hapa wakati watu wapo kule Jack. Twende.” Wakaanza kukusanya vitu vya watoto pale. “Umesikia tunatakiwa kusimamia harusi?” “Hata sijui itakuaje na hili tumbo! Kwanza tujue ni lini ndipo tujipange.” “Willy anaonekana anataka iwe mapema kabla mkewe hajajifungua.” “Sio mkewe bwana!” “Aaah! Vinachanganya hata huelewi! Juzi alikuwa mkewe, jana wakaachana, leo anamchumbia, sielewi.” Sabrina akacheka huku akiendelea kukusanya vitu vya watoto, Jack amebeba hao watoto akimfuata kwa macho akimtizama anachokifanya.

Palipo na Amani, Na Uharibifu Kunyemelea!

Wanasimama baada ya kukusanya kila kitu, na Tino naye akawasimamia mbele yao. Sabrina akaduwaa, kwa muonekano ule na vile alivyo Tino, Jack akajua ni yeye tu. “Tukusaidie nini?” Jack akamuuliza akimtizama machoni akiwa amebeba watoto wake. “Naitwa Tino.” “Kwa hiyo!?”  Jack akamuuliza kama anayemshangaa. “Nilitaka kusalimia tu.” “Ukimwangalia Sabrina hivyo alivyo, anaonekana anataka salamu yako?” Tino akamtizama Sabrina. “Habari za siku Sabrina?” Jack akacheka. “Achana na mke wangu, wewe. Twende Sabrina.” Wakasogea mbele kidogo wakiwa wanaondoka, Tino akaanza tena.  

“Mbona hasira wakati ni salamu tu.” Jack akageuka na kucheka. “Hujaniona nikiwa na hasira, na ninauhakika hutataka kuniona. Narudia tena, achana na mke wangu. Na kama unalo jambo jingine lizingumze sasa hivi, au..” “Au nini? Au nini Jack? Utanifanya nini?” Tino akauliza kama anayemwambia sikuogopi. Jack akacheka na kurudi nyuma. Sabrina akamshika. “Utajua utakapofanya nilichokuonya. KAA MBALI NA MKE WANGU.” Jack akaweka msisitizo huku akimtizama machoni.

Tino akacheka. “Twende Jack. Twende. Hana hata hadhi ya kuzungumza naye huyo. Atakupotezea muda tu na kukuharibia siku.” “Mbona wewe sijawahi kukuharibia siku ila kukuachia faraja mpaka sasa mnafurahia matunda yangu!” Tino akaongea kwa kejeli akiwacheka wote wawili huku akiwatizama. “Si nilikwambia Jack? Twende. Hana jema litakalomtoka kinywani mwake isipokuwa maovu yaliyojaza moyo wake. Twende mpenzi wangu.” Sabrina akamshika Jack, Tino akacheka huku akiwatizama. “Twende Jack.” Jack akaona ni heri aondoke tu kama Sabrina alivyomshauri lakini alionekana ameshakasirika sana na kama anayezuia maneno.

Lakini wakati wanaondoka wakamsikia tena Tino akisema. “Mtasikia hivi karibuni kutoka kwa mwanasheria wangu.” Sabrina akashituka sana karibu adondokwe na vitu alivyoshika mkononi.  Akajua maji yameshamwagika.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Katikati Ya Ndoa Tulivu, Kwenye Amani, Tino Amerudi.

Nini Kitaendelea? Usikose Muendelezo.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment