Asubuhi
akashituka kutoka usingizini wakati nesi akimpima tena pressure. Akakuta ujumbe
kutoka kwa Willy akiuliza kama waliamka salama. ‘Tupo
salama. Asante.’ Akajibu. ‘Basi nitawaona
baadaye. Nitawahi kutoka kazini ili kuhamisha mizigo.’ ‘Sawa.’ Pendo
akajibu na kurudi kulala.
Jioni.
W |
illy
anafika nyumbani Salasala jioni hiyo, akaanza kuingiza vitu vyake kwenye chumba
alichokuwa akikitumia zamani kama ofisi yake. Sifa alijua anajua alipo Pendo akamuacha
akiendelea na shuguli zake kuingiza vitu. Alishamwambia amefurahi amerudi nyumbani.
“Tulikuwa wapweke kweli!” Willy akacheka. Akaingiza kila kitu ndipo akaenda
chumbani kwa Pendo. Akashangaa Pendo hayupo chumbani. Akatoka kumfuata Sifa
jikoni. “Dada yako yuko wapi?” “Tokea walivyompeleka hospitalini, hawajarudi
mpaka sasa hivi.” Willy akashituka sana.
“Pendo
ni mgonjwa!?” “Mimi najua unajua kaka! Usiku bibi na babu walikuja kugonga,
nikawafungulia. Wakaniambia wamekuja kwa sababu dada aliwapigia kuwa ni
mgonjwa. Hata mimi nilikuwa nimelala, sikuwa najua kama ameanza kuumwa huko chumbani.
Nikaongozana nao chumbani kwa dada, babu akampima presha, wakakuta ipo juu.
Tukasaidiana na bibi kumvalisha, wakampeleka hospitalini. Ndio hawajarudi mpaka
sasa hivi.” Willy akashangaa sana. Aliwasiliana na Pendo!
Willy kwa
mama yake Mkwe.
Hapo
hapo Willy akampigia simu Pendo aliyekuwa akichat naye asubuhi asimwambie kama
yupo hopitalini. Ikaita bila kupokelewa. Ndipo akajikaza kumpigia mama yake.
Uzuri bado alikuwa na namba zao. Ikaita mara mbili tu akapokea. “Shikamoo mama.” “Marahaba baba, pole na kazi.” “Asante,
lakini niliwasiliana na Pendo,hakuniambia kama yupo hospitalini!” Akasikika
akilalamika. “Wamempumzisha. Presha ilikuwa juu. Lakini
naona jioni hii yupo sawa. Tulimuhamisha kule tulipokuwa tumempeleka hospitali
ya mwanzoni, tukamleta kwa daktari ambaye alikuwa akimuhudumia tokea mwanzo.
Naona amempumzisha.” Willy akashangaa sana ni kwa nini Pendo
hakumwambia.
“Sikujua mama! Mimi nilimuulizia hali yao, akaniambia wanaendelea
vizuri. Kwa hiyo nikawa...” “Subiri kidogo Willy.”
Kimya. Akasikia mlango unafunguliwa nakufungwa taratibu. “Willy?” Akamsikia akimuita, akaitika. “Nipo mama.” “Nilikuwa natoka nje, amelala. Daktari ameshauri
alale kabisa, kupumzika. Sikutaka tumuamshe.” “Samahani mama, sikukusudia
kusumbua.” “Hata kidogo, lakini Willy.” Willy alishapanda kwenye gari,
kuelekea hospitalini alipolazwa Pendo. “Nipo mama. Na
nipo njiani nakuja huko. Kuna kitu chochote labda kinahitajika?” “Hapana. Kama
ni chakula, daktari ameshauri ale cha hapahapa hospitalini kwanza ambacho wataangalia
chumvi, na maji tu. Asante.” Mama mkwe wake akashukuru.
“Nakusikiliza mama.” “Nilimuuliza Pendo kama amekwambia kama
amelazwa, alichonijibu ni kama maadamu watoto wapo salama, hutakuwa na
wasiwasi.” “Mama!” Willy akashangaa kwa kuumia sana. “Ndivyo alivyoniambia. Na kwa kuwa wamemfungia mashine
tumboni kuangalia mapigo ya watoto na wamemfanyia hata Ultrasound wameona
watoto wapo salama kabisa. Tena daktari wake ni kama amemwambia vile vimbe
zinanywea kitu ambacho si chakawaida, hajawahi ona! Kwetu ni muujiza.”
Kimya. Willy akifikiria. “Hizo ni habari njema Willy.
Inamaana hizo vimbe zikinywea, zinawapa watoto nafasi ya kukua.” “Naona kila
mtu anajua nimerudi kwa Pendo sababu ya watoto!” “Si ndicho kilichokuondoa?”
Huyo mama akauliza bila kuzunguka mpaka Willy akapoa.
“Wewe uliondoka sababu ya watoto. Mwenzio hakuwa akishika mimba. Leo
tunakuona umerudi kwenye maisha yake akiwa mjamzito, sasa hata kama ungekuwa
wewe, ungefikiri nini Willy mwanangu?” Kimya. “Nafikiri ndio maana hata yeye Pendo anaona akupe habari za
watoto tu ambao ndio anajua unajali zaidi, sio yeye.” “Sio sawa mama na si
kweli.” “Unakataa nini Willy mwanangu? Labda sijaelewa kwamba sasa hivi
tunazungumzia nini!” “Kweli mama umesahau mapenzi yangu kwa Pendo!?” “Siwezi kusahau
hata kidogo na ndio maana tulielewa ni kwa nini uliweza kumuacha mwanamke
unayempenda na kwenda kuzaa nje. Nafikiri hilo uliliweka wazi na lilieleweka.
Au kuna kitu kingine hapa kilijificha ambacho sisi tumeshindwa kuelewa?”
Mama yake Pendo akauliza taratibu tu.
“Hapana mama. Ila najua nimemuumiza sana Pendo, kwa kitendo cha kama
kumpa mwanamke mwingine mimba tukiwa kwenye ndoa.” “Kwani wewe ndio ungekuwa wa
kwanza, Willy? Watu wanakuwa na ndoa zao, wanakosea. Wanaomba msamaha kama
linakuwa ni kosa, uponyaji unachukua muda kwenye ndoa, lakini penye nia
ya ndoa pakiwepo, ndoa zinapona, na kuendelea. Lakini wewe
ulikusudia kutupilia mbali kila kitu na kwenda kuanzisha familia yako
Willy. Ulipima kwenye mizani ukaona mapenzi peke yake hayatakutosha
maishani, unahitaji familia na ndio maana ukaondoka kwa haraka sana. Hukutaka
hata kupoteza muda, ukasaini talaka na kwenda kuanza upya. Halafu hukusikika
hata kwa salamu, au kupotea njia kumwangalia mwanamke uliyekuwa naye kwa miaka
yote hiyo, kujua anaendeleaje! Unakuja kutokea akiwa mjamzito. Unafikiri habari
utakazokuwa ukipewa ni zipi kama si hizo?” Pendo
hakuwa na tofauti kuzungumza kama mama yake, ila Pendo aliongezeka na deko,
mtoto wa mwisho.
“Naomba nikwambie ukweli mama bila kukuficha na kwa heshima zote.”
“Nakusikiliza.” Akajibu kwa kutulia mama Kenton. “Narudi kwa Pendo si kwa kuwa ana watoto wangu. Ni wangu
aidha nipo na mama yao au la. Na wala wao hawatakuwa watoto wa kwanza kuwa na
wazazi waliotengana.” Huo ukawa ukweli. Mama Kenton kimya. “Kushindwa kwa Zelda kunibebea mimi mtoto, sio mwanamke wa
mwisho hapa duniani. Naamini mama yangu utakubaliana na mimi wapo wanawake
wengi tu wangekubali niwaoe na wanizalie watoto zaidi ya wawili ambao
nawatarajia kwa Pendo. Zelda aliangalia picha kubwa kwa haraka, akatumia akili.
Alijua mama angekufa, baba ana mali nyingi kunizidi mimi ambaye kila pesa
itakayoingia sasa hivi ipo kwenye kujijenga. Mzee ameshamaliza kujijenga, pesa
inayoingia sasa hivi ni matumizi tu. Zelda ameliona hilo na kwa kuwa wote
tumeshakuwa wakubwa, njia pekee yakuipata pesa yote ya baba na mali ni kumzalia
yeye mtoto ambaye hata baba akifa leo, anajua mali zote atamwachia yeye na huyo
mtoto.” Willy akaamua kuzungumza.
“Ninachotaka kusema, nipo kwenye maisha ya Pendo, au nimerudi kwenye
maisha ya Pendo kwa sababu ndiye mwanamke ninayempenda. Nampenda Pendo na ni my
SOULMATE. Hakuna idadi ya watoto itakayochukua nafasi ya Pendo maishani mwangu.
Hata azae hao halafu atake tena wengine, au asizae hata hao alionao sasahivi,
Pendo ni my Soulmate. Nampenda Pendo na ndio maana nimerudi na nitabaki
hata kama hakuna anayefurahia. Nitabaki na Pendo na nitafanya kila niwezalo aamini
nimerudi kwa ajili yake yeye sio hao watoto wanao muendesha kama gari bovu!”
Akaanza kukasirika.
“Nyinyi wote mnanifanya hata nichukie watoto niliowasubiri na
kuwahangaikia kwa muda wote huo!” “Wewe Willy!” “Kweli mama. Mnaniharibia
mahusiano yangu na Pendo. Kila kitu ninachofanya hamumuoni mke wangu mnamuo...”
“Aliyekuwa mke wako.” Mama K, akamkatisha kwa kumsahihisha. “Nitamuoa tena Pendo. Na nitamuoa hivi karibuni. Najua Pendo
bado ananipenda. Mnambana mpaka nakosa raha! Swala limekuwa watoto tu mchana na
usiku na si Pendo mwenyewe! Kila kitu ni watoto tu, mnajisahau. Mnafanya kila
kitu kunikomoa na kusahau mimi ndiye baba yao! Mnahangaika na vitu vya watoto wangu
na kunipuuza mimi mwenyewe!” “Si haukuwepo! Ulitaka maisha yasiendelee kwa kuwa
wewe umeondoka?” Akashangaa mama
K. “Basi nimerudi. Na nimerudi sababu ya Pendo. Na
Ninampenda.” Willy akaongea kwa ukali, akashangaa kimya. Akakumbuka
anaongea na mama mkwe, kipenzi cha Kenton, mtoto wake mkorofi haswa. Akapoa.
Alishafika
hospitalini. Mida hiyo ya jioni foleni ya kurudi mjini haikuwa kubwa. Akaegesha
gari. “Samahani mama yangu.” “Hapana. Umeongea moyo
wako. Ila sijui sasa unataka sisi
tufanyaje, Willy!? Uliondoka, ndio umerudi!” “Basi naomba mtambue kama nimerudi
mama yangu. Hilo tu.” “Hakuna anayejua haya
uliyoniambia sasa hivi. Na nina uhakika hata Pendo mwenyewe hajui hayo
unayosema, Willy.” “Kwa maneno naona itakuwa ngumu kuamini na kuelewa kwa
haraka. Naombeni nafasi kuyathibitisha hayo.” “Sawa Willy, mwanangu.”
Mama huyo hakuwa na mambo mengi. Akakubali na kuagana.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Willy
akaingia hapo chumbani alipokuwa amelazwa Pendo na mama mwingine kitanda cha
pembeni. Akamkuta mama K peke yake kwa upande wa Pendo. “Mbona mashine nyingi
wakati umeniambia anaendelea vizuri, mama!?” “Hizo mashine zisikuogopeshe.
Wanafuatilia mapigo ya moyo ya watoto na pressure yake huyo wanataka irudi
kawaida kabisa ndipo wamruhusu, ndio maana unaona yupo usingizini saa hizi na
wamemuwekea catheter ili asiamkeamke kwenda chooni. Tena hiyo ilikuwa kabla ya
Ultrasound na daktari wake kuona hizo vimbe zinanywea. Hamna aliye hatarini
hapo.” Mama K akamtuliza. Willy akabaki amesimama pale akimtizama Pendo.
“Utakuwa
hapa kwa muda gani?” Willy akamgeukia mama K aliyekuwa akinong’ona. “Nataka
nirudi nyumbani angalau nikaoge na kubadili, ndipo nirudi. Tulikuwa hapa na
kina Nancy muda wote nikapitiwa na wazo lakurudi nyumbani wakati wao wapo hapa.”
Ndipo Willy akajua kila mtu kwenye familia alikuwepo hapo kasoro yeye ndio
hakuambiwa, kwa kuwa kinachomuhusu ni watoto wake, na ameshaambiwa watoto wake
wapo salama, wakaona wamuache wasimtaarifu. Akaumia kuona hajataarifiwa habari
za kuugua kwa Pendo. “Sasa nataka kujua kama wewe utakuwepo. Na sitakawia.”
“Nitakuwepo mama. Nenda tu hata ukapumzike kidogo. Nitakuwepo.” Willy akajibu
akisikika kuumia. “Sawa. Asante na ikitokea unapatwa na dharula kabla sijarudi,
tafadhali usiondoke bila kunitaarifu ili nimtume hata Kenton ambaye yupo karibu
aje akae naye mpaka nirudi.” “Nitakuwepo mama. Hakuna dharula nyingine kwa sasa
isipokuwa hii ya Pendo kuwepo hapa hospitalini.” “Basi nitawaona baadaye.” Mama
K, akaondoka.
Willy na
Pendo Hospitalini.
W |
illy akasogeza
kiti mpaka karibu na kitanda alicholazwa Pendo, akakaa. Alikaa hapo akiwa
ameinama amepotelea mawazoni kama lisaa, aliponyanyua uso akamkuta Pendo ndio
anaamka. “Watoto wote wapo sawa Willy. Usiwe na wasiwasi. Hiyo unayoona na
kusikia hapo.” Akanyooshea kidole mashine nyingine iliyokuwa imesimama pembeni
na kufungwa kuzunguka tumbo lake. “Ni mapigo yao ya moyo. Huo mlio si
unausikia?” Willy kimya akimsikiliza. “Huo ni mlio mzuri, inamaana wapo sawa.” Pendo
akaendelea kwa sauti ya chini kama asiyetaka kumsumbua mgonjwa wa kitanda cha
pembeni. Willy akabaki kimya akimsikiliza wala asitazame hizo mashine. “Na Mungu
amenitendea muujiza mwingine, vimbe zimeanza kupungua, zinanywea, kwa hiyo
nafasi ya kukua kwao inaongezeka. Hawapo hatarini.” Pendo akaongeza taratibu
kama kutaka kumtoa yeye wasiwasi.
Willy
akasimama na kumsogelea. “Naomba nisaidie maji ya kunywa. Baba na wengine wako
wapi?” “Nilimkuta mama tu. Na amekwenda nyumbani kuoga, amesema atarudi kuja
kulala na wewe.” Willy akamsaidia kumpa maji. “Asante.” Akaona anavuta simu
pembeni ya kitanda, akapiga. “Baba!” Akamsikia
anasikiliza. “Najisikia vizuri, ndio nimeamka.”
Akamuona akisikiliza tena kwa muda kidogo kama akielezwa kitu, akamuona anajishika
tumbo na kujifuta machozi. “Asante baba. Usiku
mwema.” Akakata na kujifuta tena machozi.
Willy
akatulia kidogo kama kumpa nafasi atulie kisha akamuuliza. “Kwa nini
hukuniambia kama umelazwa?” Akauliza
taratibu tu. “Nilipoona hakuna hatari ya watoto, nikaona nisikusumbue. Nikuache
ufanye kazi tu.” Pendo akajibu taratibu tu. “Halafu baba ameniambia mama atakuwa
hapa kama kwenye saa nne, Willy. Ungeenda kupumzika. Naamini kila kitu
kitaendelea kuwa sawa. Nikisikia taarifa nyingine za watoto, nitakutaarifu.”
Kimya Willy akimtizama. “Kapumzike Willy, najua umechoka na kazi za siku nzima.
Kila kitu kitakuwa sawa.” Pendo akasisitiza.
“Sipo
hapa kwa ajili ya watoto tu Pendo!” Pendo akamwangalia kama asiyemsadiki. “Najua
unaweza usiniamini, lakini sipo hapa eti kwa kuwa nina wasiwasi sana kuwa kuna
kitu kibaya kitatokea kwa watoto! Na hata kama kikitokea, uwepo wangu hapa
hautasaidia chochote kile. Kwa sasa sina uwezo wa kufanya chochote kwa hao
watoto, isipokuwa wewe.” “Lakini sivyo ulivyosema jana wakati tunaagana, Willy!
Jana usiku ulisema unataka kurudi nyumbani si kwa ajili yangu ni kwa ajili ya
watoto.” Willy akashituka sana.
“Pendo!
Ni wakati gani niliongea hivyo!? Hata usingizini nikiwa nimelala, nina uhakika
nitakuwa sijaropoka kwa kuwa silo lililojaza moyo wangu! Sina sababu yakutokuwa
hapa isipokuwa niliona umeniongelesha vizuri na kunipokea siku ya kwanza kabisa
kuonana tokea tuachane. Kama ungenikatalia kuja nyumbani siku ile wala
nisingekusumbua! Kwanza swala la watoto kama ni wangu au sio wangu lilikuja
kujijibu baadaye kadiri nilipokuwa na wewe.” “Unawezaje
kufikiria hata kama watoto sio wako!?” “Subiri kwanza Pendo naomba
usilie unisikilize. Tafadhali. Nataka tuzungumze na si kukuudhi.” Akamfuta
machozi.
“Unakumbuka
ni mara ngapi wamechukua mbegu zangu na kukupandikizia kwa bomba?” Willy
akauliza taratibu tu. Pendo kimya. “Unakumbuka mazungumzo yetu siku moja na
daktari ya kuwa wapo kina mama ambao hawajaolewa wananunua hiyo huduma na
wanapandikiziwa watoto, wanazaa?” Kimya Pendo akimsikiliza. “Sasa nikwambie
ukweli tu, na Mungu wangu nishahidi. Nilipokuona mara ya kwanza kabisa. Nikajua
baada ya kuachana na mimi ulirudi kwa yule daktari, akupandikiziwa watoto kwa
kutumia mbegu nyingine walizo na uhakika nazo kuwa zina nguvu. Nikajisikia
vibaya baada ya kuona na kwako nilishindwa. Lakini nikaona upo sawa, na
unazungumza tu na mimi. Hukuweka dharau yeyote ile kwangu, ndio maana nikapata
ujasiri wakurudi nyumbani, wala nisijue kama watoto ni wangu, ila tu sikutaka
kukupoteza na wewe, kwa kuwa nimepoteza ndugu wote na marafiki pia.” Willy
akaendelea taratibu tu.
Akamshika
mkono kwa upendo. “Nimerudi kwako si sababu ya watoto, ni kwa ajili yako Pendo.
Nahesabu watoto ni kama nyongeza Mungu anataka kunipa. Sisemi wewe ni muongo,
lakini kwa hakika sikumbuki kukwambia narudi nyumbani sababu ya watoto, Pendo!”
“Basi labda nilielewa vibaya pale uliposema unataka tu kurudi nyumbani, na
si kuwa unataka kunioa.” “Na pia sikusema hivyo Pendo. Nilisema hivi,
naomba tu kurudi nyumbani, sio kwamba nakuomba kukuoa. Tena nilisema hivyo
baada yakuona unasita kuniruhusu kurudi nyumbani na ndio maana nilikwambia
naweza hata kutumia ile iliyokuwa ofisi yangu ili niwepo tu pale karibu na wewe
niweze kukusaidia. Na hayo yote ni kwa sababu kama hii. Yakuona watu wote
wanaweza kuacha shuguli zao na kuja hapa, mimi nakuwa sina taarifa!” Pendo
akanyamaza.
“Watu
wote wakaribu yako, ambao hawaishi pale nyumbani kama mimi, walipata taarifa
kama wewe ni mgonjwa, isipokuwa mimi, Pendo. Mimi sikuambiwa, nakuja kuambiwa
na Sifa ambaye na yeye alidhani najua! Ndio maana nikaomba kuwepo pale karibu
ili mengine ambayo unashindwa kuniambia sababu ya kutokuniamini, niyaone
mwenyewe kwa macho.” “Si kwamba sikuamini Willy.” “Ni hivyo tu Pendo.
Nimepoteza uaminifu kwako, nimepoteza sifa nyingi sana. Hilo najua, na ninajua
itachukua muda kuja kuniamini tena. Lakini nakwambia na kukuhakikishia nipo
hapa kukusubiri wewe wala si watoto. Nitasubiri mpaka uamini nimerudi kwenye
maisha yako, tuishi kama zamani ambapo tulikuwa tukiambiana mambo yetu wenyewe
na kuyatatua. Mpaka yakiwa mazito, ndipo ulipokuwa ukiwaambia wazazi. Lakini
mara zote mimi ndio nilikuwa kimbilio lako kwanza ndipo wazazi. Najua itachukua
muda kujengeka kama ilivyokuwa zamani tokea chuoni. Naamini kuna hatua nilifika,
ukajenga uaminifu kwangu, simu za nyumbani zikapungua, zikawa zinaishia kwangu.
Na nafikiri imekuwa hivyo kwa muda mrefu sana isipokuwa hii miezi mitano
nilipokugeuka.” Pendo kimya.
“Lakini
nimerudi Pendo. Na sina ninapokwenda. Watoto wawepo au wasiwepo. Nimerudi
nyumbani ambako kuna utulivu. Sijashindwa kabisa nje. Najua na wewe unajua.
Nimeshindwa kwa Zelda, lakini sio kwamba nitakosa mwanamke kabisa! Hapana.
Kurudi kwangu nyumbani ni kwa ajili yako ili angalau uone nimetulia na
ninamaanisha. Ukinifukuza leo, ukaniambia hutaki kuniona tena, nitaondoka na
kukuacha kwa amani kabisa nikijua niliharibu mimi mwenyewe, nitawajibika na
matokeo. Akaunti ya watoto ninayo, nilipiga picha kile kikaratazi cha benki
ulichonipa siku ile nikusaidie kuweka pesa. Nitaendelea kuwatunza wanangu na
sitawasumbua mpaka wewe uone upo tayari kuwakutanisha na mimi. Lakini
sitawatelekeza mpaka wafike umri wakujitegemea, kama Mungu atanipa uhai. Na
sitawasumbua hata kidogo. Nitaondoka Pendo, na kukuacha uwe na amani.” Pendo
akapoa kabisa.
Willy
hakuwa akidanganya. Aliongea ukweli. Willy kwa muonekano analipa vizuri tu. Ana
kazi nzuri na pesa ipo. Zelda alikimbia kwa kuwa alidhani amefilisiwa na mkewe
wakati wakiachana, akadhania Willy ni mlala hoi, hana hata pakuweka kichwa
chake kumbe Willy anajenga mjengo wa maana. Pendo akakumbuka picha alizokuwa
akionyeshwa na Willy usiku uliopita. Kwa hiyo akimuachia tu hapo, atakachokuja
kusikia ni kuoa kwa Willy. Akawa mpole. Na kwa kuwa Willy naye alimjua vizuri
sana Pendo, akajua kwa hakika mazungumzo ya usiku uliopita ndiyo yamempandisha
presha mpaka kulazwa hapo.
“Sijui
umenielewa Pendo? Tafadhali uliza popote na zungumza kile kilichopo moyoni ili
tuwe ukurasa mmoja. Nilishakuumiza kwa kukusaliti mwanzo, sitaki kuona
nikiendelea kukumiza. Hustahili. Wewe ni mtu mzuri, umejawa upendo na mema.
Sitaki mimi ndio niwe chanzo cha matatizo kwako. Kama ukiona nakuwa tatizo na
si msaada, nipo tayari kukupa nafasi mpaka utakapokuwa tayari.” “Natamani ubaki
Willy. Usiondoke.” Pendo akaongea kwa upendo bila hata kujivunga. Willy
akainama na kuanza kumbusu midomoni. Akambusu tena na tena. Akambusu tena.
Kisha akaendelea kumbusu akiwa amelala hapohapo. “Nakupenda Willy. Nakupenda
sana mpenzi wangu.” Willy akamuhurumia na kuzidi kuhukumiwa.
“Najua
unajua kama nakupenda Pendo. Nilikosa na mama aliniwekea pressure, nilikuwa
siwezi hata kuhema. Simu na jumbe za kifo chake akiniambia anakufa bila kuona
watoto kutoka kwangu tu, katika watoto wake wote watano zilikuwa haziishi,
mpaka nikasalimu amri. Nikajiambia kama nikuzaa tu, nizae huyo mtoto
aonekanike, sisi tuendelee na maisha yangu. Nilisogwa Pendo! Sina jinsi
nikakwambia ukaelewa. Ilibaki ikawa hiyo ndio habari inazungumziwa tu pale
nyumbani wala si ugonjwa wa mama tena. Walipojua tu kuwa mama hatapona, agenda
ikageuka kwangu. Nilikuwa sina raha!” “Pole Willy, ndio maana ukageuka ukawa
mtu wa hasira kwa vitu vidogo ambavyo havikuwahi hata kukusumbua!” “Hata sikuwa
najua Pendo. Samahani sana. Ila amini nilikuwa nimevurugukiwa haswa. Gafla
maisha yangu yakakosa maana kabisa sababu ya mtoto! Nikakubali ili kutulie,
kumbe ndio najiingiza kwenye matatizo zaidi!” Pendo akatulia. Yakaendelea
mabusu.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Mama
K alirudi akakuta bado wanapeana mabusu. Akajua habari ya Pendo na Willy ndio
imerudi upya. Akaona ajisogeza karibu ili wajue ni yeye ameingia, Willy
aondoke, amuache Pendo apumzike. Akaona hawamwangalii, Willy amemuinamia Pendo
pale kitandani akiendeleza mabusu. “Pengine ataruhusiwa kesho.” Pendo na Willy
wakacheka na kuachiana. “Naona ukapumzike baba, ili na huyu naye alale, kesho
kila mtu arudi kwake.” Wakazidi kucheka. “Basi naomba nimuage mama yangu.
Nitaondoka.” “Dakika tano tu Willy mwanangu, ili alale huyo.” Mama K, akatoka
kama kuwapa nafasi. Naye Willy akawa muungwana hata hakuchukua muda mrefu,
akatoka kumfuata mama K nje.
Willy anataka kurudisha Majeshi kwa Upya.
“Usiku
mwema Willy mwanangu.” “Nina shida kidogo mama. Naomba unisaidie.” Willy
akamsogelea. “Kwa sasa sina rafiki wakaribu wala ndugu. Tumesambaratika sina
wakumtuma kwenu. Nataka kumuoa Pendo.” Mama K akaanza kucheka. “Nataka taratibu
za mahari.” “Unataka kuanza uppya?” Willy akacheka. “Vyovyote mtakavyoniambia
mimi nitafanya wazazi wangu. Nisaidie tu kuzungumza na Mzee, nijue taratibu.”
“Kwa nini usimtumie yule msimamizi wenu wa harusi?” Mama K akauliza. “Kwanza
ile harusi waliyotusimamia, niliivunja. Pili wale walimuumiza sana Pendo.
Japokuwa mimi nilikuwa nikizungumza na mwanaume, lakini ilikuwa ni kama
tunalazimishia tu. Mahusiano yalibadilika. Naanza upya mama yangu.” Mama K akacheka akifikiria. “Nitazungumza na baba
K na Kenton, kisha tutakujibu.” “Nitashukuru ikiwa mapema.” “Sawa Willy.”
Wakaagana safari hii wakicheka sio kama mwanzo alipokuwa njiani.
Asubuhi
ya siku inayofuata, Willy alianzia hospitalini na maua mazuri, safari hii na
kadi kubwa sana ya ‘I Love You’. Mama K akacheka
Willy alipokuwa akiipanga mezani upande alipolazwa Pendo. “Bado amelala.” “Vipi
lakini, wamelalaje?” Akauliza Willy wakati akiweka na maua hapohapo mezani.
“Wamelala vizuri tu. Daktari wa zamu alipita usiku, akawaangalia wote, akasema
wapo sawa na Pendo naye pressure ipo sawa sasa. Amesema kila kitu kikienda
sawa, daktari atakayepita zamu asubuhi hii atamruhusu.” “Afadhali. Wametoa
masharti yeyote?” “Na mimi niliuliza, hakuna jambo kubwa zaidi ya kuwa
waangalifu tu na vitu vya msingi. Kama chumvi na kupumzika. Swala la kunywea
kwa vimbe ndio linashangaza karibia wote. Naona swala la hatari ya hao watoto
linaanza kupungua.” “Afadhali hata swala la honeymoon nalo litawezekana.” Mama
K akacheka. “Kweli umekusudia!” “Kabisa mama. Naamini hapatakuwa na ugumu kwenye
kuoa.” “Sio kwa baba yake.” Willy akasogea vizuri, akajua wamezungumza.
Wakatoka
hapo ndani. “Kwa hiyo hakuna masharti?” “Yeye amesema hatapokea tena mahari ya
pili. Heshima unayotaka kumpa Pendo, kumuoa tena kihalali, inatosha.” “Kweli
mama!?” “Kabisa Willy mwanangu. Si mngerudi tu kuishi kwani nani angezuia?
Lakini kurudi tena kuomba baraka za Mungu ni jambo zuri sana. Baba K amefurahi
sana.” “Nashukuru sana mama yangu. Basi nitataka hata kutoa zawadi ya shukurani
kwenu nyinyi wazazi, kwa kuwa naye kipindi mimi nilipomuacha. Angalau niwashike
tu mkono.” “Hilo hatuwezi kukuzuia Willy mwanangu.” “Sawa. Lakini naomba swala
la kumvalisha pete Pendo liwe la siri kidogo. Angalau apate kitu kipya na
kizuri. Na yeye apate suprise ya kuchumbiwa.” Mama K, akacheka
akionekana kuridhika. Wakazungumza kidogo, wakarudi ndani.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Akiwa amevunja ndoa ya kanisani, Willy anamtaka tena Pendo. Atafanikiwa? usikose kufuatilia kuon Ilivyo rahisi kuvunja/kubomoa kuliko Kujenga.
Jack & Sabrina nao?
Inaendelea…
0 Comments:
Post a Comment