Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 38. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 38.

Willy akajikaza kiume. “Najua wote mnajua kuwa nampenda Pendo. Si kwa kujitetea hapa, ila najua nyinyi mmekua mashahidi wa maisha yetu kabla. Tokea chuo nimekuwa na Pendo. Sikuwahi kumtenda vibaya. Nimekuwa naye katika shida na raha. Nilimlinda hata mbele ya familia yangu, tena wewe Nancy ni shahidi wa karibu sana wa haya ninayozungumza. Unatujua mimi na Pendo vizuri sana.” “Hata mimi nilidhani nawajua!” Nancy akajibu. “Nilikosa. Nimekosa. Sio kwa kujitetea, lakini nataka kuwa mkweli kwenu kwa sababu ya kumpenda Pendo. Nitaongea ukweli tu. Niliingiziwa hofu kwa muda mrefu mkapa ikafanikiwa kuniingia kuwa mama yetu atakufa bila kuona hata mjukuu mmoja kutoka kwangu. Mama alinisihi mpaka kwa machozi, mwishoe nilikubali kuzaa na yule msichana, ili tu kupata mtoto, bila kumuumiza Pendo.” “Ulimuumiza sana tu.” Akadakia Nancy.

“Nikisema kumuumiza ni ile heshima niliyoweka kwake hata nikiwa kwenye hiyo shuguli ya kutafuta mtoto. Nilikuwa makini kiafya nikijua yupo Pendo.” Willy akaendelea kwa tahadhari. “Mama aliponiwekea pressure na mimi nikamuona ni kweli ni mgonjwa na madaktari wote wanakiri kuwa hatapona, ndipo nilipokubali kuzaa na yule msichana kwa masharti. Kuhakikisha anapimwa magonjwa yote, na anakaa nyumbani, atunzwe pale na kuangaliwa asije kuwa ni malaya, akaishia kutuua mimi na Pendo. Na sio kwamba nilikuwa nikifanya naye mapenzi kwa starehe! Ilikuwa ni siku alizokuwa akiniambia ni za hatari ambazo ni za kushika mimba. Ambazo pia nilikuja kugundua au alikiri wazi kuwa alikuwa akinidanganya. Alilala na mimi akiwa tayari alishakuwa akilala na baba. Anakuja kuniambia ni siku za kushika mimba, kumbe zile zakushika mimba alikuwa akizitumia na baba.” Hapo wote kimya.

“Na katika yote hayo pia, nilitunza heshima ya Pendo, ndio maana hamkuwahi hata kumsikia Pendo akilalamika kuwa nimebadilika. Nilijitahidi kuwa na mke wangu, japo nakiri, mwishoni baada ya yule msichana kuniambia ni mjamzito, ni kama juhudi yakutafuta mtoto na Pendo, ikaisha wala sikupunguza. Niliacha kabisa. Na ninajua ndio kitu pekee ambacho Pendo atakuwa hata shahidi wangu atasema ndicho alichoona mabadiliko na uhuru wa mapenzi kwake uliisha kabisa. Ni kwa ile hali ya hukumu kuona nalala na mwanamke mwingine nje, halafu nakuja kumshika na yeye.” “Ikawaje?” Kenton akataka aendelee.

“Nilipotoka sasa hapa ramsi kwa talaka na kwenda kumfuata na kumwambia atoke pale nyumbani twende tukaanze maisha kama wazazi ndipo yote yalipofunguka. Kumbe walikuwa na mahusiano mazito yenye ahadi ya kuja kufunga ndoa baada ya kumzika mama ili sasa walee mtoto waliyejua ni wao wala si wangu. Kufupisha habari, walijaliwa kupata mtoto wa kike. Ana miezi miwili, na mwezi ujao wanaoana.” Kimya.

“Najua nimekosa wazazi wangu, lakini naomba mkumbuke mapenzi niliyokuwa nayo kwa Pendo na jinsi nilivyohangaika kutafuta watoto na Pendo. Tafadhali kumbuka mama yangu. Kumbuka jinsi nilivyomlinda Pendo na kumkinga na maneno ya watu. Wakati wote nimesimama na Pendo, Nancy najua unajua. Hata kama umenichukia, lakini unajua wazi nampenda mdogo wako na sijawahi kumsaliti kwa miaka yote tokea tupo chuo. Maisha yangu yote nimekuwa nikimtanguliza Pendo. Jamani nyinyi ni mashahidi, nampenda Pendo. Na nipo hapa si kwa ajili ya watoto tu, hata Pendo mwenyewe.” Kimya wote wakimtizama.

“Nimemuomba Pendo anipe muda. Hata kama si kama mume, basi angalau kama mzazi mwenzake. Niwepo kumsaidia yeye kwanza. Pendo amesimamisha maisha yake yote, kazi nzuri ambayo anaipenda na ameihangaikia, yupo hapa akipambana kutunza uhai wa watoto wetu. Na mimi naomba kusaidia. Kwa namna yeyote ile naomba kusaidia. Na mimi niwepo tu, sio nije nijitokeze wakati watoto wamezaliwa au wamekua! Sidhani kama ni sawa jamani, na hata nyinyi sidhani kama mnaona itakuwa sawa, eti nije nirudi hapa watoto ni wakubwa!” “Nafikiri vitanda vyote vipo chumbani kwao. Ni vyakufunga tu.” Baba yake Pendo akamwambia Willy. “Asante sana Mzee wangu. Nashukuru.” Pendo akavuta pumzi kwa nguvu maana ni kama baba yake alifunga huo mjadala, na ndugu zake wakaliheshimu hilo.

Willy akamgeukia tena Pendo. “Mnaendeleaje?” Akarudia kuuliza. Akaona wanatoka mmoja baada ya mwingine, wakabakia wao wawili. “Tumeamka vizuri kabisa. Vipi wewe? Utakuwa ulilala kweli! Uliondoka usiku sana.” “Nililala. Acha nikachangamkie kazi kabla sijaonekana hovyo zaidi.” Pendo akacheka. Akambusu shavuni na kutoka. Mara mama yake na Nancy wakarudi. “Kwa hiyo utamsamehe?” Kabla Pendo hajamjibu Nancy, Willy akarudi na maua. “Niliyaacha kwenye gari. Acha niyatoe haya yazamani, niweke mapya.” “Nipe niyashike kwanza kidogo, kabla hujayaweka kwenye maji. Nitayaweka hata jioni. Asante sana.” “Karibu.” Akamkabidhi na kumbusu shavuni.

Nancy akakohoa. “Nampenda Pendo, na wewe nishahidi Nancy.” “Upo hapa Willy kwa kuwa kule kulishindikana. Najiuliza, kama kule mambo yangeenda sawa, ungerudi hapa? Na kabla hujajibu hilo, je kama Pendo asingekuwa mjamzito leo, ungekuwa hapa?” Kabla hajajibu, akaongeza swali jingine. “Na kama huna taarifa, Pendo bado yupo kwenye kubembeleza mimba. Sisemi kama itatokea, ila ikitokea, kesho ukarudi hapa, ukakuta hakuna watoto, utafanyaje?” Nancy akaendelea kwa jazba. Kabla hajajibu akaongeza tena. “Kwa taarifa yako tu, ulimuacha akiwa mjamzito. Na aliteseka sana kubaki hapa bila wewe. Unachotaka sasa hivi hapa, nikumtonesha. Naku....” Akaingia mume wake Nancy na kumbemba mkewe juu juu. “Niache bwana Leon! Huyu Willy anamfanyiaga Pendo vitu anavyojua akiondoka, anamuacha mwenzie mnyonge. Kwa nini..” Akamtoa hapo chumbani kwa nguvu.

Wakabaki watatu hapo chumbani. “Nilikosea mama yangu. Lakini sasa hivi nimejifunza kutokana na makosa. Huko nje nimeona panavyotisha mama. Maisha yangu yapo kwa Pendo. Na nitatulia hapa mpaka Pendo atakaponikubali. Hata kama itachukua miaka, mimi nitatulia tu. Hutakaa ukasikia tena.” “Mungu akusaidie Willy. Nancy anaongea hivyo kwa wasiwasi wa sisi wote. Uliumiza kila mtu Willy! Uliondoka vibaya sana. Uliondoka wakati mwenzio akikuhitaji! Umemchafua sana hapa mjini, ukamuacha akichekwa.” “Mama, hata mimi nimechekwa mno. Wala si Pendo peke yake. Mungu amenichapa nje hadharani. Nilikuwa siwezi hata kutizama watu machoni. Siwezi hata kupokea simu za marafiki zetu. Nimejifunza mama yangu, na nipo hapa si kujaribu tena. Nimerudi na nimefunga milango yote ya nje, na nimetupa funguo zote, na Mungu atanisaidia tu. Naombeni mnisamehe kwa kuwafedhehesha. Nisamehe mama yangu. Nimekosa.” “Watamaliza kutengenezeza chumba cha watoto huko.” Mama Kenton akaongea taratibu kama Pendo mwenyewe. Willy akatoka kwa haraka.

 

Willy alimkuta mkwewe yaani baba K, na shemeji yake, huyo Kenton ndio wapo kwenye hicho chumba cha watoto. Nancy na mumewe walikuwa nje wakitengeneza nyama. Mke wa Kenton alikuwa jikoni akimsaidia Sifa kupika. Alipoingia tu hapo, pakazuka ukimya. Willy akajikaza akabaki tu humo ndani hata hajui ashike nini! Mwishowe baba Kenton akaanza. “Kwa hiyo sasa hivi unaishi wapi?” “Kwenye apartment zile.” Akaelekeza anakoishi, wote wakamgeukia. “Zile wanazolipa kwa dola!?” Shemeji yake akamuuliza kwa mshangao. “Ndiyo. Lakini natafuta sehemu ya bei ya chini kidogo.” “Kwani kazi bado upo palepale au uliuza kiwanja cha Kigamboni?” Willy akacheka kidogo kwa kusikitika. “Najua natumia pesa nyingi pale, lakini sikuwa na pakwenda, ndio nikalipia pale kwa miezi 6. Hivi hapa nakaribia kumaliza mkataba wangu. Na hapana. Sijauza kiwanja cha Kigamboni. Na kazi nilipata kwengine.” “Wapi?”  Shemeji yake akaendelea kumuhoji. Willy akamtajia. “Oooohooohh! Ndio maana. Pesa ipo.” Shemeji yake akaongea hivyo na kuendelea na kazi.

Wazi Kenton bado alionekana na hasira naye na hawezi kuwa naye karibu. Alimpuuza hapo ndani akamfanya ajisikie si kitu. Lakini Willy akajiambia atabaki tu mpaka mwisho wao ndio wamuache hapo. Alitoka mara kwa mara kwenda kumuangalia Pendo. Wakati mwingine alimkuta na Nancy au mama yake, na kumlazimu kutoka bila kukaa sana. “Nilikuja kukuangalia kama unahitaji kitu.” Aliishia kusema hivyo alipowakuta hao wawili na kutoka baada ya Pendo kujibu, “Nipo sawa Willy, asante kujali.” Aliweza kuona uangaliwaji mbaya kutoka kwa Nancy, lakini si mama yao. Kidogo yeye alikuwa muugwana. Kule kwenye chumba cha watoto nako, shemeji yake ni kama alimnyima kazi. Mara nyingi akaishia kuwa mtizamaji tu, lakini hakukata tamaa.

Chakula kilipokuwa tayari alikaribishwa kama kawaida. Ili asiwaudhi, alipoona Pendo anakula chakula chake chumbani, na yeye akaenda kwenye chakula cha watu wote, akachukua chakula chakumtosha na kwenda kukaa nje kabisa upande wa jikoni. Wakaendelea kuongea na kucheka bila ya kujali. Pendo akatoka na chakula chake ili ale pamoja nao. Wakamuandalia sehemu ya kukaa, akajipanga vizuri, na kukaa ili ale. Lakini akagundua Willy hayupo pale katikati yao. “Willy yuko wapi?” Akauliza Pendo akiangaza macho. “Nilimuona akipakua hapo, labda ameenda kula ndani.” Akajibu wifi yao. Pendo akatulia kidogo, wakamuona na yeye anasimama. “Wapi tena mama wawili?” “Naenda kumtizama Willy.” Pendo akajibu kwa upole, akijua wapo kinyume naye. Pendo mtoto wa mama na baba K, mziwanda wao, hawajui kumkatalia kitu, akabaki wakimwangalia.  Pendo akaona utizamwaji wake.

“Willy amekosa, na ametuumiza. Zaidi mimi. Lakini amerudi, halafu ni baba wa watoto wangu. Angeweza kutorudi na kujaribisha kwengine, lakini amerudi kwangu akiwa hana uhakika wa watoto, na nilimwambia mara ya kwanza tu tulipoonana juzi kuwa hawa watoto wanaweza wasizaliwe, lakini Willy alirudi. Na ninajua wote mnajua ananipenda Willy. Amekosa, naomba mumsamehe tumpe nafasi nyingine hata yakuwa baba.” Wote kimya. “Kaka K?” Pendo akamuita kaka yake ambaye ndio mkali kuliko wote. “Mimi nakufikiria wewe Pendo. Sitaki aje akuumize tena.” “Siwezi kujibu ya baadaye, lakini wewe mwenyewe ulishaniambia kuwa ni kweli Willy ananipenda. Ukawa ukimtizama kama mdogo wako. Mnazungumza na kuongea. Amekosa, naomba msamehe na mpe nafasi nyingine. Hivyo hivyo Nancy. Nyinyi ndio watu wangu wa muhimu na ndio mpo karibu na mimi na watoto wangu. Mkimchukia Willy mnaniweka kwenye wakati mgumu.” “Kwa maana nyingine wewe umeshamsamehe?” Akauliza Nancy. “Ndiyo.” Akajibu Pendo kwa haraka sana na kumshangaza dada yake.

“Huyu Willy si amerudi juzi tu? Unajuaje kama atakaa?” “Sijui dada yangu. Lakini unajua jinsi Willy anayonipenda Nancy, na jinsi alivyonibeba tokea chuoni, wewe ukiwa shahidi. Lakini amerudi, Nancy. Na sisemi ndio tunarudiana kimapenzi, lakini ameniomba angalau awepo kwenye maisha ya watoto wake. Na wote mnajua jinsi mimi na Willy tulivyokuwa tukihangaika makanisani na mahospitalini kutafuta mtoto. Naombeni kwa swala la ubaba, tumruhusu. Kama hamtafanya kwa ajili yake, basi naombeni mfanye kwa ajili ya mimi, mdogo wenu.” Hapo anaongea Pendo machozi yapo kifuani.

“Mimi naona Pendo yupo sahihi.” Baba yake akaingilia. Lakini wote walijua lazima Pendo atetewe na baba yao. Alimpenda huyo Pendo kama mtoto wa miaka 7. “Hata tufanye nini, bado ni mzazi mwenzake. Naona hilo tuliheshimu na tumpe nafasi ya ubaba. Wote hatujawahi kumuona akiwa baba. Labda katika hili atafanya vizuri.” “Hata la mume alijitahidi jamani! Tuweni waungwana.” “Asante mama na baba.” Pendo akashukuru kuona wazazi wanamuunga mkono. “Hapana. Penye ukweli tunasema, si ndio Nancy mama?” Mama yake akataka Nancy atulie. “Au nasema uongo Kenton mwanangu?” Kenton na yeye kwa mama yake, huwa wakati wote mama yake hakosei na baba yake alimjua. Hampi mashitaka ya mama yake, labda Nancy. Lakini wakati wote Kenton alimtetea mama yake na akiona kama kweli amekosa, basi atamtafutia sababu ya kumtetea. “Ni kweli mama. Nafikiri hatukutegemea kukutana naye hapa. Imekuwa gafla.” Wakatulia, Pendo akaingia ndani.

Akamtafuta kila mahali, mwishoe akaamua kumuuliza Sifa. “Kaka yupo nje.” Pendo akajivuta mpaka nje, akamkuta amekaa kwenye ngazi za nje ya jiko, akila. “Unatafuta nini huku Pendo!? Hizi ngazi ndefu sana!” “Mbona umekaa huku peke yako?” “Nimeona niwape nafasi. Lakini nipo sawa kabisa.” Willy akasimama. “Umemaliza kula?” “Bado, nilikuwa nakutafuta.” “Mimi nipo sawa, nimeona nikae huku. Twende ukamalize kula.” “Unataka tukae wote hapa?” “Nenda tu ukakae na wageni mpaka watakapoondoka. Mimi sitaondoka mapema. Nitakaa kama jana.” Pendo akabaki akimtizama. “Kweli mimi nipo sawa kabisa. Nenda ukale.” Mara wakamuona Kenton anakuja akiwa ameshika sahani yake. Alizunguka nyumba.

Wote wakamgeukia. “Naona huku nako umepatengeneza vizuri!” Pendo akacheka. “Kazi niliyokuwa nikifanya usiku nilipokuwa sina usingizi.” “Pamependeza.” Kaka yake aliongea huku akiangalia maua. Pendo na Willy wakabaki wamesimama kama waliofumaniwa. “Nashukuru kunijumuisha kwenye matayarisho ya chumba cha watoto.” Willy akaongea akibabaika. Pendo akamuhurumia Willy. Kama aliyekuwa akijikomba! Gafla nyumbani kwake mwenyewe. Nyumba aliyojenga kuanzia msingi, akageuka mgeni! Kenton ni mwanasheria mzuri sana hapo mjini. Alijijenga hapo jijini, na mkewe alikuwa mfanyabiashara mzuri tu tena wa muda mrefu. Kwahiyo uwezo wa kifedha ulikuwa upo. Kenton akamgeukia. “Wakati mwingine maji yanapozidi unga, simama kama mwanaume, uache kukimbia hovyo.” “Nimejifunza kutokana na makosa.” Kenton akaondoka, ni kama aliyekuja kutangaza msamaha, Pendo akavuta pumzi kwa nguvu kama aliyepata aughueni.

“Yatapita Willy.” “Naamini hivyo Pendo. Nimeharibu sana, mpaka najisikia vibaya!” “Lakini uzuri umerudi Willy. Umerudi na unajua nini unataka. Hilo ni jambo jema.” Pendo akamfariji. Willy akabaki akifikiria, mwishoe akaona heri atoke kule nje, ili kumrudisha Pendo ndani. “Acha nikamalizie kusafisha pale chumbani kwa watoto. Wewe rudi kula.” Akamsaidia kupanda ngazi moja aliyoshuka, wakaingia ndani.

Ilipofika kwenye mida ya saa 10 jioni wakaanza kuaga, mpaka inafika saa 12 jioni Pendo akajikuta amebakiwa na Willy. “Unataka kwenda kupumzika?” “Kama ni sawa, naomba nibaki kidogo. Tukae wote.” Pendo akacheka akimuhurumia. “Njoo basi angalau ujilaze hapo kwenye kochi.” Willy akaingia na kukaa pembeni yake. “Unakionaje chumba?” “Naona kipo kwenye hali nzuri. Kuna vitu gani vingine unatamani viwepo humo?” “Niliandika, nikampa kaka. Naona wamegawana. Hivyo vitanda vya watoto na makabati yao ni baba na mama ndio wamegaramia. Na vingine waligawana familia ya Nancy, kaka K na kina Sabrina wamechukua vitu baadhi vya kununua. Kwa hiyo vitu nilivyokuwa navyo kichwani vimeisha.” Willy akanyamaza akiumia. Alisubiria hao watoto, kuyumba kwa miezi 6 tu, kumempokonya haki zote. Amekuwa mgeni kwenye nyumba yake mwenyewe! Amepoteza mamlaka hata kwa watoto wake mwenyewe!

Akabaki ameinama akisugua mikono. “Nisikilize Willy.” Willy akamwangalia. “Uliondoka, hakuna aliyejua kama utarudi, na watoto wanaendelea kukua. Kila nilipokuwa nikiwaambia wasubiri pengine wanaweza hata wasifike miezi mitano, bado wakawa wanaendelea kukua na kubaki huko tumboni. Sasa kila tulipokuwa tukienda kliniki na baba na mama, tukawa tunaambiwa wanakua vizuri tu niongeze kula hiki na kile, ndio maana baba akapata amani, akaniambia niandike kila kitu ninachotaka kukiona kwa hawa watoto. Ndipo nikatengeneza hiyo orodha yote. Wakaisoma na kuniachia mimi jukumu la kujilisha tu. Lakini mimi mwenyewe nikataka chumba kiwe na hiyo rangi uliyoona na kuchorwe kama hivyo, ndio nikajiongezea garama nyingine. Ila mambo mengine yote ya watoto wakagawana.” Pendo akaendelea.

“Ndio umerudi. Hakuna anayejua utakaa kwa muda gani, au hakuna anayejua dhamira yako ya kweli ya kurudi. Kwa sababu uliondoka kwa sababu ambayo bado hakuna mwenye uhakika kuwa hilo tatizo limetibika. Kwako nilikosa kigezo cha kuwa mke kwa sababu yakutozaa, ndio maana uliondoka kwangu, ukaniacha.” “Naomba usiseme hivyo.” “Ni hivyo tu Willy, na hata wewe umekiri hivyo. Najua usingeniacha kama ningekuwa nimekuzalia watoto. Lakini kwao nilibaki na nitabaki kuwa jukumu lao. Aidha nitazaa hawa watoto au la. Lakini hakuna mwenye uhakika na wewe. Kila mtu anawasiwasi wakutobaki kwako endapo hawa watoto hawatazaliwa. Kwa hiyo hakuna ambaye atakuwa tayari kukuachia chochote sasa hivi. Naomba uelewe Willy.” Willy akarudisha kichwa chini.

“Pole.” “Najisikia sina maana Pendo. Pesa yangu yote inakosa maana kama itashindwa kutumika kwa wanangu.” “Ni kwa sasa tu. Ni kwa muda Willy. Tutakuwa na hawa watoto kwa muda mrefu sana. Watunzie hiyo pesa, tutahitaji sana tu. Wakizaliwa tutakuwa na uhitaji mkubwa. Sabrina alikuwa ananiambia vile mapacha walivyo garama. Vile wanavyotumia pesa nyingi kwa ajili ya wale watoto. Inamaana ndio kitakachotupata na utashuhudia kama utakuwepo.” “Nitakuwepo Pendo.” “Basi tulia. Fanya kile utakachoweza, na kama hakuna, basi. Acha watusaidie.” Kimya. “Kwanza uwepo wako tu hapa unamaana sana. Si kwangu tu, na watoto pia. Ipo faraja ya namna yake na utulivu. Nakushukuru.” Willy akamfunua miguu na kuanza kuiminya minya. Pendo akacheka. “Sijafanyiwa masaji muda mrefu! Nahisi nitalala.” “Wewe lala tu, nitakuwepo hapa mpaka baadaye sana.” Pendo akaanza kusinzia.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mpaka Pendo alikuwa akimuonea huruma Willy. Akitoka tu kazini, anakwenda kukaa naye mpaka usiku kabisa. Akilala yeye ndio na yeye anaondoka. Akajitahidi hivyo hivyo. Na jumamosi tena akarudi asubuhi. Akakaa naye mpaka usiku wa saa sita. Jumapili tena akarudi asubuhi hata Pendo hajaamka. Pendo anaamka, baada ya kuoga wakati Sifa anampa kifungua kinywa, ndipo akamwambia Willy yupo sebuleni. Pendo akashangaa. “Naomba mwambie aje huku. Umempa kifungua kinywa?” “Aliniambia nisisumbuke, yupo sawa.” “Wewe unamjua Willy. Atakuwa na njaa. Naomba mtayarishie kifungua kinywa. Lakini mwambie aingie huku.” Sifa akatoka, Willy akaingia.

“Mmeamka salama?” “Wote naona tupo salama. Walikuwa wakinisalimia huko bafuni wakati naoga. Njoo ukae hapa.” Willy akakaa. “Mzima?” “Mzima. Nimekuja tukae wote.” Pendo akamuhurumia maana aitoka hapo usiku wa karibia saa 8. Na mapema hiyo ameshafika hapo! “Asante Willy. Nashukuru.” Pendo akaendelea kunywa uji, Willy ametulia tu pembeni. Sifa akamletea na yeye kifungua kinywa. Akashukuru na kula. Wakamaliza kula, Pendo akamkaribisha ajiegemeze kwenye mto, wakawa wamejilaza huku wakiangalia mahubiri mpaka wakapitiwa na usingizi.

Baba na mama yake Pendo wanapita kwenda kumsalimia Pendo wakati wanakwenda kanisani, wakawakuta wamelala usingizi mzito, hakuna mwenye habari hata kama kuna mtu ameingia hapo ndani. Willy alikuwa amemshikilia Pendo mkono kwa kupishanisha vidole, akavuta karibu na uso wake, wakawa wamelala. Wazazi hao wakawaangalia, nakuona waondoke bila kuwaamsha.

Walikuja kuamshwa na Sifa akimtaka Pendo anywe supu. “Bibi ameipitisha, alisema saa nne na nusu kama hujaamka nikuamshe unywe pamoja na dawa na juisi yakuongeza damu. Ameweka kwenye friji. Amesema ukimaliza ndipo urudi kulala.” “Mama alikuja!?” “Na babu.” Sifa akaongeza wakati anamuwekea supu.” “Asante. Hata sikuwasikia!” Willy akakaa na kumsaidia kuweka mito vizuri. “Eti mama na baba walikuwa hapa!” “Na mimi sikuwasikia.” Willy akajibu na kutulia. Pendo akamuona kama anawasiwasi wakuuliza kitu. Akamuacha kabisa. Hakutaka yeye ndio awe mstari wa mbele kuongea chochote juu yao.

Mchana wazazi wake wakapita tena kutokea kanisani. Willy akawa muungwana, akaona awapishe. “Nitawaona tena baadaye.” Akaaga mara wazazi walipoingia. “Mbona unaondoka bila kula? Nina uhakika Sifa anapika au ameshaivisha. Ungekula kabla hujaondoka.” “Sitakuwa mbali. Nitarudi.” Pendo akaelewa. Akamuacha vile anavyojisikia. Atoka hapo chumbani. Akamsikia akiwasalimia wazazi sebuleni. Wazazi wakaingia hapo kukaa naye kwa muda wakimpa habari za kanisani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Jioni, akarudi tena na mfuko wa matunda, samaki, nyama ya ngombe na kuku watatu wakiwa wamesha safishwa wamehifadhiwa kwa usafi, mafuta, nyanya, sukari, vitunguu, karoti, hoho, ndizi, viazi, mchele kwenye gunia, na vingine vingi vyakula mle ndani na alivyoona akitayarishiwa Pendo. Akashusha kila kitu jikoni, kwa kuwa hakukuta gari ya baba yake Pendo, akapitiliza chumbani moja kwa moja. Pendo alijua amefika, na wakati akiingiza vitu ndani Sifa alishamwambia. “Asante kwa vyakula.” “Karibu, lakini usijali. Huu mfuko ni wako.” Pendo akacheka na kupokea. Alimnunulia nguo nzuri sana za wajawazito, zakulalia. “Asante kujali Willy.” “Karibu. Nimeona unatumia muda mwingi kitandani, angalau uvae vitu vizuri na wewe ujifariji.” Pendo akacheka. “Nashukuru.” Bado akamuona ana kitu anataka kuzungumza lakini anasita. Alianza, nakubadilisha mbele ya safari. Pendo akamuacha kabisa.

Ilikuwa jumapili, lakini Pendo akashangaa anakaa mpaka saa sita usiku wakati kesho yake ilikuwa siku ya kazi. Akazunguka hapo ndani, kisha akaaga. “Njoo Willy. Kaa hapa.” Willy akarudi kukaa. “Wakati wote tumekuwa tukizungumza, na hatujawahi kushindwana. Hata kipindi tunaachana, unakumbuka tulizungumza hapahapa chumbani tukaweza kuelewana?” Willy akanyamaza. “Hiki chumba hakijawahi kushindwa kutupa nafasi na utulivu wa kuzungumza mazito na magumu na kupata majibu. Niambie tu.” Akaona wasiwasi unaongezeka anasugua mikono.

“Willy?” Pendo akamuita taratibu. “Naomba kurudi nyumbani.” Willy akaenda moja kwa moja kwenye pointi. Pendo hakutegemea, kidogo akapatwa kigugumizi. “Sio lazima ukanipa jibu leo. Lakini nilikuwa nikifikiria kutoka kwenye ile apartment ninayolipa pesa nyingi, halafu hiyo hela nikawawekea watoto, wakati naendelea na ujenzi kule kigamboni. Naweza kutumia hata kile chumba nilichokuwa nikihifadhia vitu vyangu, nimekiona bado nikitupu.” “Kumbe ulishaanza kujenga?!” “Pale ofisini wanatoa mikopo ya nyumba. Uzuri wanakata pesa ndogo sana huwezi hata kuisikia kwenye mshahara. Baada tu ya miezi mitatu, wakanipa. Nimetafuta contractor, ndio anapamalizia kuanzia pale tulipoishia mimi na wewe. Kwa mwezi mmoja nimeona amefanya kazi kubwa! Unataka nikuonyeshe picha?” Pendo akacheka na mshangao usoni.

“Ningependa kuona.” Akatoa simu mfukoni. Akaanza kufungua. Kilikuwa kiwanja kikubwa. Walianza kujenga na walikuwa wakijenga taratibu wakiambiana ndio nyumba ya ndoto yao. Walianza kuijenga ikiwa na ramani nzuri sana, na kubwa mpaka marafiki walikuwa wakiwacheka kwamba watakufa kabla hawajamaliza. Na walichimba mpaka sehemu ya bwawa la kuogelea. Walichofanya wakati wapo na Pendo, ni kuzungushia ukuta kwanza katika eneo la nyumba, kisha uzio wa kawaida tu wa fensi na michongoma kuzunguka eneo jingine linalopakana na hapo. Walinunua viwanja viwili, na ndio maana Willy hakuamini wakati Pendo anakubali kumpa eneo lile lote na yeye kubakiwa na hiyo nyumba tu!

Pendo alishangaa sana alipoona hiyo nyumba. “Willy!” “Ndio tofauti ya kuweka contractor na mjenzi wa kawaida.” “Na kuwa na pesa! Kwani wewe Willy wanakulipa kiasi gani huko kazini kwako!?” Willy akacheka sana vile Pendo alivyoshangaa. “Kumbe ulikuwa unamaanisha uliposema kuna marupurupu! Sasa hii nyumba si imeisha!” “Bado bwana! Yupo kwenye vigae, madirisha na milango. Week ijayo nampelekea madirisha. Nilisubiri kwanza mtu wa geti amalizie geti zuri kwa usalama ili wasije ng’oa vitu. Nikimaliza tu geti, amesema atapachika madirisha. Sasa hivi ndio wanajengea hizo nondo. Na anaonekana ukimpa pesa, analeta vijana wake, kazi inafanyika kwa haraka sana ndio maana unaona kwa mwezi tu na siku chache, amesimamisha hilo jengo, na pia ukumbuke tulikuwa tumefika nusu. Kwa hiyo yeye ameanzia hapo nusu nakupandisha juu.” “Hongera sana Willy. Umejitahidi mno.” Willy akacheka.

“Matusi mengine Mungu anayaruhusu kwenye maisha ili kukuchangamsha.” Pendo akacheka sana. “Zelda huyo?” “Na mumewe mzee Ngoi.” Pendo akazidi kucheka. “Wamekuweka sawa.” “Si kidogo. Usingizi ulipotea kabisa kama siku tatu mfululizo, silali mchana wala usiku. Kutoka kwenye kusifiwa na jamii, mpaka kuitishwa kikao cha kutukanwa! Acha Pendo.” Pendo akazidi kucheka.

“Nimeomba kurudi nyumbani.” “Sawa sawa, lakini mimi ninawazo la tofauti Willy, naomba subiri kwanza watoto wazaliwe.” “Pendo!” “Subiri kwanza Willy. Nina maana yangu. Angalau safari hii iongezeke sababu zaidi ya sisi kuwa pamoja.” “Sijaomba kukuoa, ila kurudi nyumbani, Pendo!” Hapo Pendo akapoa kabisa. Willy akamuona akaona aendelee kujieleza ili kumuweka sawa, asiharibu. “Sidhani kama ni sawa majukumu mengine niendelee kufanyiwa kama zamani nilipoondoka! Sasa hivi nipo, naweza kufanya mambo mengi kuliko kusumbua wazazi.” “Sidhani kama ni usumbufu kwao.” Pendo akajibu na kushindwa kabisa kumtizama tena usoni. Ujasiri ukamuisha, akabaki macho kwenye simu. “Sawa, basi niombe na mimi kushiriki.” “Sawa.” Pendo akakubali kinyonge. Willy akamtizama kidogo.

“Kwa hiyo hata kesho naruhusiwa kurudi?” “Muda na wakati wowote ule.” Pendo akajibu bila kumtizama. “Nashukuru. Asante sana. Acha niwahi nikapate muda wa kukusanya vitu vyangu.” “Sawa. Naomba wakati unatoka, nipelekee na hiyo trei jikoni. Asante.” Akaingia chooni na kufunga mlango. Willy akakaa hapo akisubiri akaona hatoki. Akaenda kumgongea. “Pendo?” “Nipo tu sawa.” “Oooh! Sawa. Basi natoka.” “Sawa. Usiku mwema.” “Na wewe.” Willy akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Usiku huwa ukawa mbaya sana kwa Pendo. Akajaribu kulala, lakini akashindwa. Kumbukumbu ya maneno ya Willy akimwambia sio kwamba anaomba kumuoa, akili yake ikayakuza na kuipa maana iliyomfanya akeshe. Akazidi kuumia kama ndio anachika upya. Yale maneno yakazidi kumwingia vibaya na kusikika kwa uchungu kuliko hata alivyomaanisha Willy mwenyewe. Pendo akaanza kulia. Alilia mno usiku huo. Moyoni bado anampenda Willy. Ni zaidi ya miaka 10 wawili hawa wamekuwa pamoja, Pendo hakuwahi hata kushawishika na mwanaume mwingine. Ni Willy tu. Kurudi kwa Willy na juhudi zote kuliibua tumaini jingine, lakini Willy anamtamkia sio kwamba anaomba ndoa! Pendo akazidi kulia. “Inamaana anarudi kwa sababu ya watoto sio mimi!” Pendo mpendwa kupendwa akazidi kulia kila akimfikiria Willy aiyerudi na mafanikio makubwa kuliko hata alivyoondoka! Mwili umerudi kama kijana mdogo. Pendo akajitazama jinsi alivyonenepa na hilo tumbo, akajua ndio maana hata Willy amekuwa muwazi kwake.

Pendo akalia mpaka saa 9 usiku bila kupatwa na usingizi. Akaanza kujisikia vibaya. Mapigo ya moyo yanakwenda mbio. Akajua pressure aliyoambiwa na daktari apumzike na kuhakikisha haipandi, imepanda, kwa hiyo atadhuru watoto wake. Akanyamaza kwa haraka. Akasafisha uso na kitambaa kilichokuwa pembeni ya kitanda baada ya kukimwagia maji ya baridi. Akajaribu kufunga macho kabisa, lakini akazidi kujisikia vibaya.  

Akampigia simu mama yake akilia. “Nitapoteza wanangu mama. Sijisikii vizuri.” Baada ya dakika 10 wazazi wake wakawa wameshafika. Baba yake akampima pressure, akakuta ipo juu. “Naomba usilie Pendo, mama yangu. Tulia kabisa ili na pressure itulie.” “Dokta aliniambia lazima hii pressure ikae chini, baba. Lasivyo ikipanda nitapoteza watoto wangu. Nimeingiwa hofu siwezi kunyamaza tena. Naogopa baba.” Wakamkimbiza hospitalini.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment