Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 37. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 37.

 “Njoo sasa hivi wakati wanacheza.” Mama yake akampisha pale akijua moyo wa Pendo. “Hapo atakuwa kashasahau kama alichwa! Pendo jamani!” Mama yake akawaza. Willy akaenda kukaa pembeni ya kitanda. “Huyu mmoja ametuna hapa.” Pendo akamshikisha mkono. “Halafu mwenzake huyu hapa.” Willy akawashika. Akashituka walivyoanza kuzunguka, Pendo na mama yake wakacheka. “Ndio wanazunguka hivi! Huumii?” Willy akauliza, wakashangaa kuona anatokwa machozi. Mama yake Pendo akashangaa. Willy akaendelea kuwashika huku akilia, mama yake Pendo akaona aondoke tu, kuwapa nafasi.

Pendo akamuhurumia Willy. Akajua kinachoendelea moyoni mwake, lakini akaona amuache tu. Amepitwa kila mahali. “Nakumbuka Jack alikuwa akisema huwa wakiwa tumboni ukiwaongelesha wana uwezo wa kutambua sauti.” Pendo akacheka na kufuta machozi na yeye. “Wanasema hivyo Willy. Sijui! Kila kitu nikufanya kwa imani tu.” “Nasikitika kupitwa! Najuta sana Pendo. Nilikula ng’ombe mzima, nikakimbia nikiwa nimebakisha mkia tu! Nimeacha watoto wangu, nikakimbilia nilipofedheheka vibaya sana!” Pendo na yeye akazidi kulia hapo nakushindwa kujibu. Willy aliwashika hao watoto taratibu huku akiwabusu na machozi yaliyokuwa yakimlowesha Pendo kwa muda mrefu mpaka Sifa alipoingia na sinia ya chakula. Ikabidi Willy asimame aelekee chooni. Pendo akajifuta machozi. “Chakula dada.” “Asante Sifa. Ninakushukuru.” Pendo akakaa. Sifa akampangia mito. “Bibi alipita.” “Nilimuona wakati anatoka. Nilikuwa uwani wakati anaingia.” “Sawa. Kuna chakula umpe Willy?” “Mimi nimekula nilichojipikia mchana. Kama hatawahi kuondoka, naweza kumpikia haraka.” “Hapana. Msihangaike kwa ajili yangu. Mimi nipo tu sawa. Asanteni.” “Unauhakika Willy? Usije lala na njaa.” “Nitakuwa sawa. Usijali.” Akakaa.

“Ndio unakula nini hapo?” Pendo akacheka akikoroga. “Mchemcho wenye samaki, na mboga mboga. Mama huwa ananiletea matembele. Natakiwa damu nyingi. Kwa hiyo nakula kila kijani unachojua kinaongeza damu. Nimepunguza wanga sana ili nipate nafasi ya aina hii ya chakula. Nahangaika kwa kila namna, ilimradi wakue tu.” “Pole Pendo. Naona kama unajinyima sana!” “Nipe hongera Willy. Unakumbuka tulivyokuwa tukihangaika? Hii ni garama ndogo sana ya kulipa.” Willy akanyamaza kwa muda.

“Hivyo virutubisho ambavyo mama anakununulia, ananunua wapi na ni lini vinahitajika tena?” “Kuna dada anatuuzia. Ni vya GNLD mahususi kwa mama wajawazito.” “Niandikie na unitumie na namba yake huyo dada ili nikanunue vingine ili usiishiwe.” “Nashukuru Willy. Asante.” Willy akamtizama na kuinama. “Sasa movie zenyewe ziko wapi?” “Nimeacha kwenye gari. Acha nikalete.” Willy akatoka, Pendo akaendelea kula. Akarudi na hizo dvd na maua mazuri. Pendo akacheka. “Nashukuru Willy.” “Karibu.” Akamkabidhi hayo maua, akayanusa. “Yananukia vizuri sana. Asante.” “Karibu.” Kisha akayaweka pembeni. Akamaliza kula. Akanywa dawa za virutubisho, Willy akimtizama tu. Akaenda kusafisha meno.

Aliporudi kutoka bafuni akaangalia saa. “Mmmmh! Usiku umeendelea Willy, nenda kapumzike, kesho kazini. Tutaangalia movie kesho.” “Wewe unalala sasa hivi?” “Maisha yangu ni hapo kitandani. Sijui nalalaga saa ngapi na kuamka saa ngapi! Ndio maana nakuwa na nguo ya kulalia wakati wote.” “Ni sawa nikikaa tena kidogo ndio niondoke?” “Hamna shida kabisa.” Pendo akarudi pale kitandani, akapanga mito vizuri ndipo akapanda hapo kitandani na kujilaza.

“Naomba kushika tena watoto, labda watanifahamu na mimi.” Pendo akacheka. “Ukitaka waamke, leta glasi ya maji ya baridi, tuwashikishe halafu wataamka.” “Kweli?!” “Nenda tujaribu.” Willy akatoka kwa haraka. Akarudi na maji baridi haswa. Wakaanza kumshikisha tumboni, Pendo anacheka na kuruka kwa baridi. Wakawasumbua huku wakiwaongelesha, kweli wakaanza. “Hao, wameanza. Ona!” Willy alikuwa akishangaa, anacheka na kufuta machozi. “Nimefurahi sana kuwaona, sijui niseme kuwashika!” Willy akaongea taratibu huku akipapasa tumbo la Pendo. “Nimefurahi sana. Nawapenda kuliko kitu chochote hapa duniani, nawaahidi nitakuwa baba mzuri sana kwenu.” Machozi yakaanza kumtoka na Pendo. “Kuanzia leo, na mimi nitakuwepo.” Willy akaendelea kuwapapasa. Pendo alisikia faraja ya namna yake. “Mnahitaji kukaa huko kwa mama yenu mpaka muwe wakubwa kabisa. Tutawaombea, na mtakuwa salama.” Akabusu tumbo la Pendo na kujifuta machozi.

“Umeridhika sasa?” “Hapana Pendo! Sidhani kama nitakuja kuridhika. Nikitu nilikuwa natamani mno! Nilipojua Zelda hana mtoto wangu, nikajiambia  basi tena. Nilijua wazi siwezi kupata mtu kama wewe. Zelda nilikaa naye kidogo tu, lakini alikuwa akinivunjia heshima mno. Kwangu ilikuwa mshituko. Sikuzoea matusi makubwa. Yaani kutukanana waziwazi! Kuitana mjinga, sijui fala!” “Willy! Alikuwa anakutukana hivyo!?” “Mbona hayo ni madogo Pendo! Acha tu. Basi ile hai ikaniogopesha sana. Nikajiambia maadamu Mungu amenitoa pale salama, nikajiambia sitahangaika tena. Nimejifunza, nikajiambia inatosha. Sikutegemea kama kuna muujiza wangu huku.” Pendo akacheka taratibu, mikono ya Willy bado ilikuwa ikizunguka, taratibu tumboni kwake, watoto wakatulia.

“Naona wamerudi kulala.” “Wameridhika.” Wakacheka kidogo wote wakiangalia tumbo. “Nikuache na wewe upumzike Pendo. Nitakuona kesho. Si umeniambia milango ipo wazi, naruhusiwa kuja muda na wakati wowote?” “Karibu.” “Asante. Usisahau kunitumia namba ya huyo dada anayewauzia shake na dawa.” “Nilishasahau. Nitafanya hivyo. Kwani ulibadili namba?” “Hapana. Ni ileile.” Akambusu shavuni, akasimama. “Nikusaidie nini kabla yakuondoka?” Willy akauliza huku akiangaza. “Nisogezee rimoti zote na nisaidie kupanga tena mito. Zaidi huku chini miguuni. Nilale kiuno kikiwa kimenyanyuka kidogo.” “Ndio mpaka asubuhi!?” “Nimeshazoea. Nalala hivyohivyo.” “Pole Pendo, najua sio ulalaji mzuri, lakini utakuja kupumzika.” “Pendo akacheka.” Akamuwekea mito vizuri. Akamfunika, akambusu tumboni na shavuni tena. “Nimeshakusogezea kila kitu. Acha mimi niondoke. Mlale salama.” “Asante, na wewe.” Willy akaondoka. Pendo alijawa na furaha, akatamani amwambie Sabrina, lakini ilishakuwa usiku sana. Akaamua amuache, akalala hapohapo kwa furaha ya kushikwa na Willy.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

S

iku inayofuata ya ijumaa mchana siku ya kazi, wakati akizungumza na Sabrina, akashangaa Sifa anamgongea kuwa Willy yupo sebuleni anataka kumuona. Akamuaga Sabrina, na kumwambia amkaribishe chumbani. Akajiweka sawa. “Vipi Willy!?” “Simu yako haipo hewani Pendo. Ulini block?” Willy akauliza kwa kulalamika. “Hapana. Nilibadilisha namba zote na kubakiwa na moja tu, tena mpya. Nilikusudia kupunguza stress kutoka kwa watu wa karibu. Pole za kuachika zilikuwa nyingi, sihemi. Halafu wengine walikuwa wakinipigia eti kujua ninaendeleaje baada ya wewe kuondoka hapa! Nilichoka. Na nilijua wazi wengine hawamaanishi Willy. Nikabadili kabisa namba, na kupunguza watu wakuwasiliana nao.” Willy akapoa kidogo, Pendo alimuona vile alivyoingia na uso wa kulalamika.

“Kwani ulinipigia sana?” “Uliniahidi kunitumia namba ya yule dada na vitu vya kununua. Na mimi nataka kusaidia pale nitakapoweza, Pendo. Nahitaji kushiriki! Najua unaweza ukaniona ni mbambaishaji, sio mtu wa kuaminika, mkimbiaji na...” Akasita, Pendo akimshangaa yote hayo yanatokea wapi! “Lakini nataka kusaidia. Hata kama unaniona ni mshindwaji, nipe nafasi hata ndogo ndogo tu ili kurudisha uaminifu. Na kama hutaki niwe na namba yako, basi naomba uniandikie hata kwenye karatasi tu.” “Willy! Naomba utulie. Nilisahau mpenzi wangu. Hakika nilisahau. Sina sababu nyingine yeyote ila ni kusahau.” “Nilifikiri ni vitu vya muhimu!” “Ni muhimu sana tu. Ila nafikiri sijui ni kwa kuwa mama ametoka kununua jana, na nishamlipa, nafikiri akili ikatulia, nikaona si muhimu tena. Nilisahau tu. Kaa kidogo.” Willy akajishauri kidogo akaenda kukaa pembeni yake hapo kitandani, akajiinamia. Kimya.

 “Pole.” Willy akamwangalia, akajisuta na kunyamaza. “Vipi kazini lakini?” “Safi tu. Bado sijatoka. Nimekuja mara moja tu, natakiwa nirudi. Nilitaka kukujulia hali yako na watoto. Tokea asubuhi naangalia simu labda utanikumbuka, naona kumbukumbu zako kwangu na zenyewe zimekuwa si za muhimu tena, Pendo! Nimekuwa nikisubiria simu yako tokea asubuhi, naangalia simu yangu kama mwehu nikidhani utanikumbuka lakini hamna kitu!” “Pole na samahani Willy. Tuliamka salama na watoto hawajambo kabisa. Walicheza asubuhi. Unataka kuwasalimia?” Willy akamwangalia na kujisogeza.

Pendo akamvuta mkono wake taratibu na kuuweka juu ya tumbo lake. “Nafikiri sasahivi watakuwa wamelala! Sijui hata nani ni nani na nini ni nini. Ni mchanganyiko tu.” Willy akacheka. “Sasa wewe waongeleshe hapo, waambie umeacha kazi, umekuja kuwaona, waamke wakusalimie, waache uvivu.” Willy akacheka kidogo. Akawashika, kisha kama aliyekumbuka kitu. Akaacha.

 “Unanipuuza Pendo!” “Hapana Willy. Kwenye mawazo yangu halikuwepo wazo la nini unifanyie, ila kukusubiri kukuona tu. Nilijua lazima utakuja ukitoka kazini. Naomba usikasirike tafadhali.” Kimya. “Niangalie Willy, sikupuuzi.” “Nahisi nilikuwa nikisubiria sana ujumbe wako ili nipate namba yako niwapigie simu kuwajulia hali.” “Naomba nipe simu yako.” Willy akatoa mfukoni akamkabidhi. Akaandika namba na kumwangalia. “Niweke jina gani?” “Naiomba, nitamalizia mwenyewe.” Pendo akampa huku akicheka. “Umeridhika sasa?” “Ndiyo. Sasa unataka watoto waje halafu wakute hata hatuzungumzi!” Pendo akacheka huku akimwangalia akiandika jina, akamaliza na kurudisha simu mfukoni. Akazungumza hapo na watoto, akambusu Pendo tumboni mara kadhaa, akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Jioni akarudi tena. Safari hii akaja na chakula chake na Sifa. Alimwambia Pendo amwambie ampikie yeye tu, atakuja na chakula chao. Walikaa na Pendo hapo chumbani, usiku huo wakizungumza na kuangalia movie. Watoto wakicheza, anamuita Willy. Anawashika. “Naomba na mimi nije kesho kwenye kufunga vitanda vya watoto chumbani kwao na kuweka michezo yao.” Pendo akatulia, hakujibu. Willy akakunja uso. “Pendo!?” “Sidhani kama ni wazo zuri Willy. Ni kitu baba alikuwa akikisubiria kwa hamu sana akawa anahimiza mafundi wamalize haraka ili yeye aje aanze. Na kaka naye amemwambia atakuja kumsaidia. Shem naye aliposikia, akasema na yeye atakuja. Mwishoe wakakubaliana familia ya kaka, familia ya Nancy, baba na mama waje hapa kesho, wafanye nyama choma, wakati wanatayarisha chumba cha watoto.” Willy akanyamaza kwa muda.

“Kwa hiyo unafikiri kesho sio siku nzuri ya mimi kuja?” Akauliza tena Willy. “Jumapili nitakuwa hapahapa. Sitakwenda kanisani.” “Kwa maana nyingine unaniambia nisije kesho?” “Walikubaliana kuanzia saa 4 asubuhi watakuwa hapa! Unajua mume wa Nacy akikutana na baba pamoja na kaka. Watakunywa hapa mpaka usiku. Hawakusema wataondoka saa ngapi. Ndio maana nafikiri labda uje tu jumapili ukitoka kanisani.” Willy akafikiria tena kidogo na kuona aulize tena. “Kwa maana nyingine hutaki nikutane na familia yako tena?” Lile swali likawa gumu kwa Pendo, akafikiria jinsi yakumjibu, akashindwa. Willy akabaki akimtizama.

“Pendo?” “Hata sijui tena Willy. Sielewi!” “Wewe ndio unayo majibu Pendo. Labda niseme hivi.” Akamuona anazima tv, akaenda kupiga magoti pembeni ya kitanda, Pendo akashangaa ni nini anataka kufanya. “Naomba unisamehe Pendo. Kwanza nilikusaliti, na nikakukimbia.” Pendo akabaki amepigwa na butwaa. “Nimeomba msamaha Pendo. Naomba unisamehe.” Pendo akabaki kimya. “Najua nimekuumiza, pengine huniamini tena. Pengine unahitaji muda, lakini naomba unifikirie Pendo. Nimekosa katika hili, lakini unajua nikiasi gani napenda watoto na jinsi nilivyokuwa nikiwahangaikia hawa watoto. Kumbuka nilivyosimama na wewe, Pendo. Njia zote ulizotaka na kushauriwa na daktari nilikubali bila shida. Hata zile njia ambazo wanaume wenzangu walikuwa wakisema nakwenda kujidhalilisha hospitalini, akiwepo msimamizi wetu wa harusi, nilifanya Pendo, na wewe ni shahidi. Au umesahau?” Pendo akajifuta machozi, akakumbuka shida aliyoipata na Willy wakati wakutafuta watoto.

“Au maovu yangu yamefuta kila kitu?” “Siwezi kusahau Willy.” Pendo akajibu. “Basi naomba nafasi ya kuwa baba. Sitakubugudhi ila kukusaidia. Ilimradi na mimi niwepo tu. Niwepo sasa hivi, hata kukusogezea mito na maji ya kunywa, na wakizaliwa. Najisikia vibaya wanangu waje kupata kumbukumbu za picha, waje kuona kila mtu yupo kwenye matayarisho ya chumba chao, halafu baba hakuwepo! Itawasumbua wanangu Pendo. Watafikiri niliwakimbia, wakati niliondoka nikiwa hata sijui kama wapo. Kwanza uliwezaje kunificha?” “Tafadhali usiende huko Willy. Huko ni papana mno, utapachukia.” Pendo akajiweka sawa.

“Hapana Pendo. Nimepiga mahesabu, inamaana hata siku tunaandikishana talaka, ulijua ni mjamzito! Tulikaa meza moja, kiti chapembeni yako. Uliwezaje kuficha kitu kikubwa kama hicho ulichojua nilikuwa nakisubiria kwa hamu?!” Pendo akashangaa sana. “Willy! Ulitaka nikwambie nini au ili iweje? Wewe ulikuwa na furaha ya kwenda kuanza maisha mapya ya mke na mtoto. Kweli nikwambie habari ya ujauzito ambao hata sikujua kama utafika hapa! Kumbuka mimi nakupenda Willy na ninakutakia mema. Mwenzangu niliona ulifanikiwa, ulitaka nikushike tena miguu ubaki njia panda!” Kimya wakati Pendo akigomba.

“Hata nyumbani kwenyewe niliwaambia baadaye sana, nilikwambia na wewe! Nafikiri mpaka nilipofika miezi minne! Ndugu mbali na Nancy, kaka na wazazi, hakuna anayejua wengine. Wale wasimamizi wa harusi ndio sikuwatafuta tena tokea wakati ule wanakushauri uachane na njia tulizokuwa tukishauriwa kwa kuwa nikujidhalilisha, mimi sina uwezo wa kuzaa.” Pendo akaendelea.

“Nilikwambia naogopa na kukwepa fedheha Willy. Hata hiki wanachokifanya kesho ni kwa kuwa ni baba yangu mzazi ndiye ametaka kufanya, sioni shida wala aibu nikipoteza. Najua wakati wote atabaki kuwa bega langu la kulilia. Sina hofu. Lakini nikwambie ukweli kabisa Willy, hata wewe naogopa usije anza kuwekeza kwa hawa watoto sasa hivi. Sitaki uingie garama wakiwa bado hawajazaliwa. Natembea kwa imani Willy! Tena wakati mwingine naona kama imani yangu ipo inayumba mno. Niseme natembea kwa imani ya Sabrina. Ndiye anayenibeba. Kila nikiamka najishika huku chini kuona kama sio mbichi! Nashinda na kulala na pedi kama nipo kwenye hedhi sababu ya hofu. Kila wakati nachungulia pedi kama ipo na damu au la!” Pendo akaendelea.

“Unafikiri mimi ndio nilifurahia kuachika na kubaki peke yangu?” Pendo akaanza kulia. “Unafikiri nilikuwa nafurahia kujua ni mjamzito na nitalea watoto peke yangu?” Kimya. “Nilikuwa naogopa Willy! Mpaka sasa sijui itakuaje. Sijui naleaje hawa watoto nikiwa peke yangu!” “Mimi nimerudi. Na nipo Pendo. Naongea na Mungu ananisikia. Hata kama Mungu atawachukua hao watoto, mimi bado utaniona tu. Na mimi nipo mpweke. Kama nilivyokupoteza wewe, ndivyo nilivyopoteza marafiki, na ndugu ni kama nilivyokwambia. Hatutafutani tena.  Nipo kama hivi unavyoniona, nimebakiwa na ile ahadi ya mwisho tu uliyonipa. Kwamba sisi tutabaki marafiki, ndio angalau nimebakiwa nikijifariji kwa hilo.” Willy akakaa.

“Namimi natembea na fedheha Pendo! Wako wanawake wengi tu wanavimbe lakini wanazaa. Japo wanaweza kuzaa kabla ya muda, lakini wanazaa. Lakini mimi sijawahi kumpa mwanamke yeyote yule mimba! Jamaa walikuwa wakinicheka, wakidhani ni utani lakini uliniumiza sana, walikuwa wanasema mpaka mzee Ngoi amenishinda kupiga bao!” “Willy!” “Mungu nishahidi Pendo. Kitendo cha kulala na mwanamke mmoja, kisha baba yeye ndio ampe mimba mimi nishindwe, unafikiri nilijisikiaje? Hata hofu yakuja kuoa tena iliniingia kuepuka fedheha. Nilijiapia sitaoa wala sitajaribu tena kwa aibu. Na ndio maana na mimi nilijitenga na marafiki. Na utani huo walinitania tukiwa wengi tu, wala hatukuwa wachache. Uliendelea huo utani kwa muda wakicheka kila mmoja akiongeza lake kwa utani, mpaka mimi nikaondoka. Nimekuwa na miezi mitano sasa, lakini migumu mno Pendo. Mno. Kutoka kuwa juu, nakurudishwa chini mavumbini nikichekwa mpaka na vijana! Sio kitu najivunia.” Pendo akanyamaza.

“Nihurumie Pendo, naomba nirudishe japo kwenye maisha ya watoto wangu. Nipe masharti yeyote yale, angalau na mimi nijisikie kuwa hapa duniani nimefanikiwa kumpa mtu mimba.” Pendo akamcheka. “Basi mimi mwenzio nilikuwa najua unatembea huko nje kama mshindi! Kidume cha Ngoi.” “Hata kidogo, unafikiri kwanini nimeisha hivi! Wala sipo kwenye diet. Ni mawazo.” Pendo akacheka na kubaki akifikiria. “Niambie nifanye chochote kile, nitafanya Pendo. Nipe masharti, chochote na mimi niwepo kwenye maisha ya wanangu.” “Mbona mimi sijakataa!” “Mbona sasa hutaki nije kesho?” “Wewe upo tayari kujibu maswali ya kesho?” “Ndiyo.” “Naomba ufikirie Willy kabla hujajibu, tafadhali. Jana mama alikuhoji maswali hapa, ujue ndio yatakayokuwepo kesho. Sasa utakuwa tayari kuyajibu?” “Kabisa. Acha nionekane mpumbavu, mjinga..” Pendo akaanza kucheka.

     Willy akasimama. “Najua niliuziwa mbuzi kwenye gunia na mama yangu mzazi. Najua na ninaelewa. Najua dada zangu wamehusika kwa asilimia kubwa tu, lakini Pendo, mimi mwenyewe ndio wakulaumiwa. Mimi kwa akili zangu timamu nilikubali na kukimbilia mtegoni. Yote niliyafanya. Siwezi kukimbia wanangu, nakile tulichonacho mimi na wewe kwa hofu yakuwajibika. Nitawajibika tu. Kwanza nahisi ni ndugu zako tu ndio ambao hawajui, lakini kila anayenifahamu mimi na familia yangu wanajua hiyo skendo. Sio siri.” “Sawa Willy. Wewe njoo. Lakini ujue wewe ndio utashinda nao huko nje na chumbani kwa watoto. Mimi nitakuwa hapa! Sitaki hekaheka za huko nje. Nitajituliza hapa kimya.” “Sawa Pendo. Mimi nitakuja, na nitabeba msalaba wangu mwenyewe.” “Wale watu wamekuchukia Willy wewe! Acha kuja.” “Siwezi kujificha Pendo. Mpaka lini?” Pendo akabaki akimtizama. 

Willy Mbele ya Wakwe Zake Tena.

N

ancy, mtoto wa pili au wakatikati kuzaliwa kwenye familia ya kina Pendo, na mumewe pamoja na watoto wake wakawa wa kwanza hapo. Nancy ndiye alikuwa na nyama. Alizilaza kwenye viungo. Mumewe alikuwa mchomaji mzuri sana wa nyama. Walipenda yeye akisimama kuchoma. Alitoa nyama nzuri kila mtu alipenda. Kaka yao ambaye ndiye wa kwanza na wakiume pekee kwenye familia, alikuwa akileta vinywaji, mkewe kachumbari na mama yao matunda. Msichana wa Pendo aliambiwa atengeneze viazi vya kukaanga, ugali na mchuzi kidogo. Saa nne na nusu, wote wakawa wameshafika, wapo chumbani kwa Pendo wakizungumza na kucheka wakati Willy anagonga.

Pakazuka ukimya wa gafla Willy alipoingia. Akasalimia. Wakaitika, kimya wakimwangalia. Willy akaona amsogelee Pendo. “Mmeamkaje?” Willy akauliza taratibu, lakini Nancy akamuwahi. “Ndio baba nani tena?” Akaanza Nancy dada yake Pendo. “Naam!” Akaitika Willy. “Nimeuliza ndio wanakuita baba nani?” “Bado ni Willy tu. Sikufanikiwa kubadili.” “Mambo ya kizungu! Hamwitani tena baba fulani?” Nancy akaongeza. Ikabidi Willy amgeukie vizuri. “Hapana Nancy. Sikufanikiwa kubadili jina kwa kuwa mtoto hakuwa wangu.” Pakazuka ukimya wote wamekodoa macho. “Haya, naomba mkacheze sebuleni au muwashe tv muangalie chochote mnachotaka mpaka mama zenu waje wawakataze. Haya, ongoza njia.” Pendo akafukuza watoto hapo chumbani kwake.

“Kwa hiyo inamaana uliparamia mimba isiyo yako?” Akauliza Nancy nakuanza kumcheka kwa waziwazi baada ya watoto kutoka. “Wifi!” Mke wa kaka yao akashangaa sana na kumfinya. “Bwana Willy uliondoka mbio!” Nancy akaongeza na kuzidi kucheka huku akimkimbia mke wa Kenton. “Wenzio wanasubiria kidogo angalau hata mpaka mtoto azaliwe lakini wewe ukakimbilia mtoto wa mwanaume mwenzio!” “Sio mwanaume mwenzangu, ni wa baba yangu.” Willy akaongeza. Hapo tena pakazuka ukimya mzito hata Nancy aliyekuwa akimkejeli akatoa macho, kimya. Pendo akabaki akiwatizama.

“Subiri kwanza Willy, inamaana ulikuwa ukitembea na mwanamke wa baba yako!?”  Baada ya kufikiria kidogo, Kenton akauliza hilo swali kwa mshangao mkubwa sana. “Hapana! Haikuwa hivyo. Mama alinitafutia yule binti, akisema atakuwa tayari kunizalia mtoto. Mwanzoni  huo ndio ulikuwa mpango waliokuwa wamenipa mimi. Mama na kina Prisca.” “Sema na Stella. Maana namjua Stella sana.” Akaongeza Nancy. “Na naomba niweke msisitizo katika hili, makosa yote ni yangu mimi. Nilifanya kwa akili zangu timamu.” “Lakini kwa ushawishi wa mama yako na dada zako.” Nancy akaongeza kwa jazba. “Kwani walianza kunishawishi jana au juzi! Ni miaka mingi tu, sema mimi mwenyewe ndiye niliyedhoofika na kuwa mpumbavu.” “Wala si kidogo!” Nancy akaongeza. Willy akamtizama na kunyamaza.

“Mimi bado nataka kukusikia Willy. Ikawaje ukaendelea kulala na mwanamke wa baba yako?” Kenton akazidi kumbana kwa swali la kumkera kama hakuwa amemsikia Willy utetezi wake tokea mwanzo kuwa, mwanamke alitafutiwa yeye na mama yake. “Niliambiwa nimetafutiwa mimi.” Hapo Willy akaweka msisitizo na kuendelea. “Ndio nikawaambia japokuwa mimi nataka mtoto, lakini siko tayari kumuacha mke wangu.” “Kwa hiyo ulidanganya ndugu zako au unatudanganya sisi sasa hivi, hapa?” “Ungemuacha amalizie kwanza!” Mme wa Nancy akamtuliza mkewe. Wazazi na Pendo kimya. “Sitaki atudanganye! Maana mtu ambaye hataki kumuacha mkewe, angekimbilia talaka kwa haraka kiasi hicho!” “Mimi sikukimbilia talaka.” Willy akajaribu kujitetea na kumuudhi Kenton zaidi.

“Sio wewe uliyerudi hapa nyumbani ukamwambia Pendo unaondoka na kwenda kwa mwanamke wako, aliyekubebea mtoto wako?” Kenton akauliza kwa ukali. “Nilisema hivyo ila..” “Ulitaka kuendelea kujulikana ni mume wa Pendo huku ukilala hovyo huko nje tena na mwanamke ambaye kumbe hata hukuwa ukijua tabia zake? Maana kwa kukusikiliza tu hapa kwa harakaharaka ni kama unaonekana ulikuwa ukilala huko nje na mwanamke ambaye na yeye alikuwa akilala na baba yako halafu unarudi hapa kwa Pendo!” Kenton akawaka. Na walimjua alivyo mkali. Baba yake kimya na mama yao, wakisikiliza.

“Ulitaka kuendelea kumuumiza Pendo mpaka lini!? Au wewe ulitegemea wote tukuache tu ucheze na kumuumiza Pendo vile utakavyo kwa kuwa mlijua hataweza kuzaa?! Uingie na kutoka vile utakavyo!?” “Hapana. Sikutaka kumuumiza Pendo na sikutaka niendelee kuonekana na mwanamke na mtoto nje, ndio maana nikamwambia ukweli Pendo kuwa inabidi nihitimishe kwake.” “Sasa hiyo ilikuwa ina maana gani kama si kuachana? Na kama uliamua kumuacha si ndio kukimbilia talaka huko anakokuzungumzia Nancy!?” Hapo Willy akaamini maneno ya Pendo. Kaka huyo alionyesha hasira kali sana. Alimuhoji hapo kwa ukali mbele ya wote.

“Ndio maana nilihitimisha kwa Pendo kwa haraka kwa sababu nilihisi ni kama nitakuwa namdhalilisha mpenzi wangu.” “Mpenzi wako yupi? Unaanza kutuchanganya. Huyo mpenzi wa baba yako?” Nancy akaendelea kumbana kwa maswali ya kumkejeli.  “Halafu acha kusema uliamua kuhitimisha kwa Pendo kwa haraka. Ulihitimisha baada ya Pendo kujua kama unaye mwanamke mwingine nje, tena mjamzito wa mimba kubwa tu! Ulikuwa ukimchafua dada yangu hapa, huku ukienda kuchangia mwanamke na baba yako huko kwenu!” “Na mwanamke wa namna hiyo hata hamjui mbali ya nyinyi wawili alikuwa na nani mwingine!? Ungemuua Pendo wewe!” Nancy akaongezea kwa kaka yake kwa hasira. “Na uache kutufanya sisi ni watoto wadogo Willy. Kama alivyosema Nancy, wewe ulitaka kuondoka hapa kwa haraka sana ila hukuwa ukijua ni jinsi gani utamkimbia Pendo, ukijua Pendo ana ndugu wanao mwangalia na kumjali si kama  huko kwenu mlikokuwa mkimuita majina mabaya! Nilichokusaidia nikuweka kwa maandishi tu. Tena nilifanya kwa haraka ili usilete mahawara zako hapa ndani.” Kenton akaongeza kwa jazba. “Au kuja kumuua Pendo kwa maradhi.” Nancy akakazania hilo kuonyesha uchafu wa Willy.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Willy Mbele Ya Ndugu Wa Pendo. Itakuaje?

Usikose muendelezo.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment