Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 36. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 36.

Mchuma Janga,...

“Nionyeshe picha za mwanao, Willy.  Amefanana na wewe au mama yake?” Kimya. Pendo akashangaa ametulia kidogo. “Willy! Nataka tu kumuona mwanao, au ni vibaya?” Willy akajicheka. “Ni nini?” “Hakuwa mtoto wangu, Pendo.” “WHAT!?” Pendo akashituka sana. “Mpaka aibu kusema, lakini ni mdogo wangu si mtoto.” Pendo akatoa macho. “Willy!” Willy akajicheka tena na kuinama kwa kuegemeza viwiko kwenye magoti, akabaki akijisugua mikono yake. “Usiniambie Zelda aliangukia kwenye mtege wa mzee Ngoi!” Willy akashituka na kumgeukia. “Unamaanisha nini?” “Kabla sijaongea mengi, wewe niambie kwanza, si ni mtoto wa mzee Ngoi?” “Ndiyo. Zelda sasa hivi anaishi na baba kama mke wake kabisa. Hivi wanapanga kufunga ndoa.” “Mungu wangu!” “Kweli kabisa. Na hawataki hata mmoja wetu. Baba ni kama alitufukuza.”“Haiwezekani Willy!” Bado Pendo alikuwa kama haamini!

“Ilikuwa kesi kubwa sana mpaka tukaomba wajomba na kaka zake baba watusaidie, lakini wale watu wameshikana Pendo! Wanaongea lugha moja. Mimi nikifikiria Zelda alitafutwa au anatunzwa pale nyumbani na mama kwa ajili yangu, kumbe walishakuwa kwenye mahusiano na baba ya muda mrefu tu, mama akiwa mgonjwa. Baba amesema anazo baraka zote za mama, kwani mama alimuachia ile nyumba Zelda. Wawili wale walikuwa wakilala chumba kimoja kama mke na mume, mama alipokuwa akilazwa hospitalini. Na alipokuwa nyumbani, baba anasema alikuwa akihamia chumbani kwa Zelda, na haikuwa siri. Mama aliridhia hilo ili ajipatie mtoto kutoka kwa Zelda.” “Subiri kwanza Willy. Hapo sijaelewa.” Willy akacheka.

“Ni mazito na ya aaibu, wewe acha tu!” “Yaani ilikuwaje?” “Nia ya kwanza kabisa ya mama, ni mimi nimuoe Zelda.” “Najua. Na wala Zelda si wakwanza.” Pendo akaongeza. “Sasa Zelda alikuwa mwalimu wa mtoto yule mkubwa wa Prisca. Alikuwa akienda nyumbani kwao kufanya naye homework, na kumsaidia yule mdogo pia wakati wazazi wanachelewa kurudi nyumbani. Siku na hiyo mama akiwa anaendelea kuugua, Prisca akamwambia dereva wao akamchukue Zelda na mtoto, akawashushe kwa bibi yao, ilikuwa ijumaa, yeye atachelewa kutoka kazini, atampitia mtoto hapo kwa mama. Ndipo mama alipokutana na Zelda, akampenda vile anavyopenda mjukuu wake, yaani mtoto wa Prisca. Akanifikiria mimi. Wakapanga mipango yao wao watatu, ndipo wakaniunganisha na mimi.” Willy akaendelea.

“Wapi pakukutania Zelda na Willy ambaye anajulikana ni mume wa Pendo, ikawa nyumbani sasa. Mwanzoni nikamkatalia mama kama kawaida. Safari hii mama akaweka presure, akisema atakufa bila kuona watoto wangu, akanisihi japo afe akiwa amepata mjukuu mmoja tu. Tukazungushana naye, tukipelekana kwenye maombi nikimwambia hatakufa, Mungu atampa umri mrefu tu, mpaka aje aone watoto wetu. Ndio wewe ukawa hupati mimba. Mama akaniita siku moja pale nyumbani, Akaniambia kama ugumu ni kukuacha wewe, basi nizae tu na Zelda. Zelda amekubali kunibebea mtoto wangu. Nisiwe na wasiwasi, wamezungumza hata na baba, wao watamtunza pale nyumbani, wala hataingilia ndoa yangu. Ikawa sasa, iwe siri, mtoto akizaliwa ndio tukwambie. Nikawaambia isije ikatokea hata kuropokwa, wewe ukajua.” Willy akaendelea.

“Basi, tukakubaliana. Wakati huo Zelda alishahamia pale nyumbani, kumbe kabla na baada wao wawili walishaanza mahusiano. Baba anaaga yupo kwenye safari za kibiashara, kumbe yupo Keko kwa Zelda.” “Haiwezekani Willy! Nyinyi nani aliwaambia?” “Baada ya kutufukuza nyumbani baba na Zelda, maana ni kama Zelda alibadilika sana. Akawa mbabe hata kwa wapambe zake. Stell na Prisca. Si ndio Prisca sasa ikabidi aanze kumchunguza kumjua ni mtu wa namna gani. Maana aliacha kazi akawa anaishi kwa pesa ya mzee Ngoi. Mwalimu mmoja ambaye alikuwa karibu na Zelda pale shuleni kwa mtoto wa Prisca ndio akamwambia Prisca kuwa mbona Zelda na baba wanayo mahusiano mazito mno. Yaani Zelda alikuwa akiwasimulia vile baba anavyochanganywa na mapenzi ya Zelda mpaka yupo tayari kuacha jumba Masaki, nakwenda kulala kwenye chumba kimoja huko kwa Zelda, Keko.” Pendo akabaki ametoa macho.

“Mama anamuombea Zelda aishi pale nyumbani, kumbe anamkabidhi fisi bucha. Mapenzi yakaendelea kama kawaida. Mama hana habari akilala sababu ya madawa yale, wenzie wanaendelea. Akamkabidhi mpaka chumba chake. Msichana wa kazi akasema kipindi mama amelazwa hospitalini, Zelda alikuwa akilala na baba chumbani kwao.” “Willy!” “Kweli. Sasa sisi wote tunajua Zelda yupo pale kwa ajili yangu, kumbe ni mama mdogo, mke wa baba. Si ndio kwa papara na ushauri wa familia, mbele ya baba na Zelda nikashauriwa sasa kuishi na mke wangu kama mama alivyotaka! Kumbe wao wanatusikiliza na kuumia kuona tunawaharibia. Ilikuwa mipango yao mama akifariki, mimi niendelee na wewe, wao wawili waendelee kuishi pale. Hata mtoto akizaliwa nikaambiwa ni wangu, wao wanaendelea na maisha yao, kuna shida gani! It’s a win win situation.”

“Sasa si ndio nikakuachia hapa nyumba nikaenda kulala hotelini mpaka siku ile ya talaka. Usiku ule mimi nikarudi sasa kumchukua mke huyo mwenye mtoto wangu, twende tukaanze maisha. Nafika pale nikawakuta na dada Stella pale. Akanipongeza mno kukuacha na kuniambia kwa hakika mama atafurahia nilichofanya.” “Yaani kuniacha mimi?” “Ndiyo.” Willy akajibu, Pendo akapoa kabisa na kujiinamia, Willy akamuona. “Naomba nimalizie. Najua ni mbaya, lakini wewe sitakuficha Pendo. Acha nikwambie aibu yangu tu, kama utazidi kunichukia sawa, najua nastahili, na kama utanicheka pia sawa, bora tubaki kuwa marafiki.” Pendo akamwangalia.

“Sasa namuaga baba kuwa ndio tunaondoka na Zelda, tukakae hotelini wakati natafuta pakuishi, Zelda akauliza haraka sana. Kwa nini iwe hotelini na sio nyumbani kwangu. Nikamwambia hii nyumba nilijenga na wewe tokea tupo chuo, tulinunu hiki kiwanja kwa pamoja. Tukajenga taratibu mpaka tulipomaliza. Nikamwambia sikutaka kung’ang’ania nyumba, kwanza mimi ndiye niliyeamua kuondoka, sio wewe. Sasa ukumbuke hapo Zelda anamaslahi mawili ambayo nilikuja kumsikia akitamka yeye mwenyewe wakati akinitukana.” “Kukutukana tena!?” “Acha Pendo. Mungu alinichapa hadharani, mbele ya watu bila kunibakiza. Wewe si unasema ulidhalilika kuachwa sababu ya ugumba? Basi mwenzio ilikuwa mbaya zaidi yako. Bora wewe ni kwa matatizo yakutojitakia.” Pendo akabaki haelewi.

“Mimi nilikuwa natukanwa na Zelda kama mtoto mdogo.” “Kwa nini tena!?” “Sikiliza sasa. Wakati nataka kumtoa Zelda pale, baba akaniambia hakuna sababu yakwenda kuishi hotelini, wakati pale ni pakubwa na yeye yupo peke yake. Nikafikiria kwa haraka, nikaona ni kweli. Kwa nini nipoteze pesa hotelini na kupanga wakati pale pako! Kumbe baba hataki nimtoe mwanamke wake pale. Mimi nikahamishia vitu vyangu kwenye chumba cha Zelda nikijua ni mwanamke wangu, kumbe kinawauma haswa. Baba wivu, hataki na mwanamke wake, Zelda ashanichukia haswa. Hanitaki mimi ambaye sina nyumba, anamtaka baba ambaye anajumba Masaki. Mimi kulala pale, kwa Zelda sio jambo zuri, nani analala na mzee wake! Si inamaana baba atachukua dogodogo mwingine. Unaambiwa wakabadilisha utaratibu. Mapenzi mchana ninapokuwa kazini. Nikirudi nyumbani Zelda amenuna anakaribia kupasuka. Mkali haswa.”

“Hakuna ninalomuuliza ananijibu vizuri. Hatukukaa sana sijui week mbili tu nikamuuliza mbona kama ananitafutia sababu ya kugombana!” Willy akamsimulia Pendo kisa kizima mpaka kutupiwa nguo nje, na kutukanwa mbele ya familia. “Mungu wangu Willy, pole!” “Wala usinihurumie Pendo. Nilistahili. Nakwambia siku mbili, nilikuwa nalala kwenye gari, sina pakwenda.” “Ungerudi nyumbani Willy.” Pendo akaongea kwa huruma. “Nilijiambia hata iweje, nisingethubutu kurudi. Nikajiambia itakuwa sio sawa kwako. Ni kama narudi kwa kuwa kule nimekwama! Nikasema nishakutenda ubaya, acha nitumikie adhabu yangu. Likabaki swala la mtoto. Sasa mtoto ni wangu au sio wangu!”

“Sasa kwenye kikao wakati mzee anatufukuza, mimi nikamuuliza Zelda, kwa hiyo mtoto ni wangu au sio wangu! Akanijibu jibu ambalo sio la moja kwa moja. Nikaondoka pale sijaridhika.” “Kwani alikujibu nini?” Willy akasita. “Willy?” “Aliniambia kwani kipindi yeye yupo pale, na mimi niko na wewe, na tunakwenda pale tunamkuta pale na ninampita nikijifanya simjui yeye sababu nipo na wewe, yeye alishaniuliza kama nalala na wewe au la! Yeye aliheshimu kuwa nina mahusiano yangu, hakuniuliza. Sasa iweje mimi nimuulize yeye swali la kijinga kama hilo?” “Willy!?” “Kama nimeongeza, ni kidogo sana. Alinijibu hivyo mbele ya watu wote, na baba akiwepo.” Pendo akashangaa sana.

“Sasa mimi nikawa sijaridhika, ndipo nikawaomba ndugu zangu tutafute msaada wa watu wazima. Ndipo sasa wakakusanyika wazee, tukiwa tumeshazungumza nao, wakamuomba baba kikao. Baba hakukataa. Akawakaribisha nyumbani kwake. Tulipokusanyika wote, akawawahi hao wazee kabla hawajazungumza kilichotupeleka pale yeye akawaambia amefurahi wamefika pale, alitaka kuwaita kuwaambia amepokea wito wa mama, ameamua kuhalalisha ndoa. Ndio watu sasa wakashangaa. Kwamba mama alikuwa anajua! Baba na Zelda wakakiri wazi kuwa mama alijua na alimruhusu Zelda alale na baba, ili kuona wapi mimba itashika kwa haraka...” “Acha Willy!” “Subiri kwanza Pendo. Ni mazito mno. Nililia na kuondoka pale kama mtoto aliyechapwa mstarini mbele ya shule nzima.” “Ehe!” Pendo akataka aendelee.

“Ndio Zelda akasema mama alimruhusu kulala na baba kwa haraka na mimi kama nitakubali ili ashike mimba. Akishashika mimba ijulikane kama ni yangu, ili sasa mimi nikishakuacha wewe sasa, na kukubali kuwa na Zelda na mtoto wangu, hapo ndipo atulie, anizalie mimi watoto. Lakini huyo wa kwanza asiwe na wasiwasi naye. Hata hivyo nisingejua, kwa kuwa mtoto atatoka anafanana na sisi tu.” “Mungu wangu Willy!” “Lakini wazee wakamuuliza, sasa mtoto ni wa nani! Ndio akasema kwa hakika ni wababa. Maana siku mama alizomruhusu kulala na baba zilikuwa za hatari. Mimi nilipokuja kukubali, alishakuwa amekosa siku zake zaidi ya siku kumi. Na bado walikuwa wakiendelea na baba. Zelda alikiri wazi, yeye anampenda sana baba. Ameishi naye kipindi mama yupo, ameona ndiye mwanaume anayemuhitaji maishani. Wakatumbia mtoto akizaliwa na akifikisha miezi mitatu tu, wanafunga ndoa. Hivi tunavyozungumza, mwezi ujao harusi. Baba amesema, tukijisikia kwenda sawa. Itakuwa njia yakumuenzi mama yetu. Tusipotaka pia ni sawa.” Pendo akabaki ameduaa.

Ukapita ukimya wa muda, Pendo akawa kama amefikiria kitu. Akamuuliza. “Sasa unaishi wapi muda wote huo?” Akamuona anacheka. “Wapi?” “Dada Stella nafikiri alianza kuhukumiwa moyoni kuona waliniingiza matatizoni, akanikaribisha nikaishi kwake, lakini Pendo, nilikataa.” “Ulikumbuka matusu ya Zelda na mzee Ngoi?” Pendo akamuuliza huku akicheka. “Kabisa. Wale watu waliniita mpumbavu, nilishindwa ndoa yangu! Nikajiambia hapa historia itajirudia na nitazidi kupoteza heshima kwenye jamii. Nakajitafutia apartment, naishi huko. Nigarama, mpaka moyo unauma.” Pendo akacheka kidogo na kunyamaza.

Kisa cha Mzee Ngoi na Pendo.

          “Mwanzoni ni kama ulimtaja mzee Ngoi moja kwa moja. Ulijuaje?” “Sikutaka kukwambia Willy, lakini sababu kubwa iliyonishinda kufika pale kwenu ni baba yako.” Willy akakunja uso. “Sikuelewi!” “Baba yako alikuwa akinitongoza na kunitaka kwa nguvu mpaka nikadhani mama amenihisi. Na ninahisi ndio sababu ya mama yko kunichukia, lakini nikaona ninyamaze tu. Na sikuwahi kumwambia mtu yeyote.” Willy akakaa vizuri. “Ilikuaje au hukumuelewa?” “Wewe si unamjua baba yako alivyomuwazi? Hakuuma maneno. Alinitongoza waziwazi Willy. Nilishituka, nikaondoka kabisa pale nyumbani.”

“Akaja siku moja pale ofisini, akaomba tukazungumze kwenye gari. Mzee Ngoi akaniambia yeye ananipenda kiukweli. Amevutiwa na mimi, anataka tuwe na mahusiano. Tena akasema itatusaidia hata kwenye ndoa yetu, kwa kuwa wewe huna uwezo wa kumpa mwanamke mimba, yeye atatusaidia. Mtoto atatoka anayefanana na wewe, na DNA hazitakuwa mbali.” “Haiwezekani Pendo!” Willy hakuamini.

“Mungu wangu ni shahidi. Siwezi kuongopa sasa hivi wakati namtegemea Mungu sana. Sitaki hata kumuudhi Mungu wangu. Basi, ndio ilikuwa mwanzoni kabisa tumeoana tu, tunatafuta mtoto lakini hatujui tatizo ni la nani. Mimi nikamwambia nampenda mume wangu. Awe hana uwezo wakunizalisha au la, sitamsaliti Willy, yeye ndio atabaki kuwa mtoto wangu.” Willy akajisikia vibaya sana, akapoa nakushindwa hata kumtizama tena .

“Hiyo ikapita, akaondoka. Siku moja mama yako akanipigia simu na kuniambia nikitoka kazini nipitie kwake, ana mashuka mazuri sana anataka kutupa. Nafikiri niliwahi kutoka kazini au nilichelewa, lakini tukapishana na mama Ngoi. Mimi naingia ndani, nikamkuta baba yako tena ni kama alikuwa anataka kutoka. Akanisalimia, nikamwambia mama aliniita nikafuate mashuka. Akaniambia mama ametoka na msichana wa kazi, ila anafikiri mashuka yapo chumba kile cha pale karibu na stoo. Mwisho kabisa. Akaniambia ndiko anakomuona mama yako anaweka vitu vyake kama mashuka na mapazia.” Pendo akacheka.

“Nini?” “Bwana mimi nikawa sina wazo wala wasiwasi. Si nikaacha pochi pale nikaenda kule. Ile nimeingia kwenye kile chumba baba yako naye akaingia.” “Pendo!” “Nilikaribia kuchanganyikiwa Willy. Akaniambia yeye anavutiwa na rangi yangu, nina weupe mzuri, na umbile langu linamchanganya kila akiniona. Ananitaka kwa hali na mali. Tukaanza kurupushani mle ndani, ananiambia nimtolee hata ziwa anyonye tu.” Willy akafunga macho.

“Nilihangaika tunazungushana pale chumbani akitaka kunikamata mpaka tukamsikia mama yako anaita. Ndio akafungua mlango. Mama yako akajua tupo kule. Sasa yeye anatoka, na mama naye anakuja. Yeye amesimamisha mpaka unamuona kabisa. Mimi nahema ndani, nimepaniki. Nikasikia kimya cha muda nje ya mlango. Sasa sijui mama alimkamata na kumuangalia ile hali aliyokuwa nayo, lakini mama akaingia ndani. Akiwa amebadilika Willy, mimi nikamuwahi nikamwambia nipo pale kwa kuwa baba alinielekeza mashuka yapo kule. Mama yako akajibu hana tena hayo mashuka, alishampa Prisca. Nikashangaa maana ndio alikuwa ameniita siku ileile, lakini nikaondoka tu.” “Ndio maana mama alikuchukia!” “Mbona bado.” Willy akatoa macho.

“Kuna siku, sijui kama utakumbuka Willy. Tulikwenda kwenu, mimi na wewe. Tulikuwa sebuleni wote wanne. Mama alikuwa ametupa chai, ilikuwa jioni. Kabla yakuondoka, nikasema nisaidie kutoa vyombo. Hiyo ilikuwa kama mwezi baada ya lile tukio. Maana niliacha kabisa kwenda pale nyumbani mpaka siku hiyo uliniomba nikusindikize, ukasema hatutakaa sana. Basi nimetoa vyombo pale. Nilibeba kwenye trei hivi. Na chupa ya chai. Nimefika jikoni nikaamua kusuuza vikombe ili nisiviche pale juu vichafu. Ile nimesimama kwenye sinki, nikashangaa nimeshikwa ziwa. Nilishituka mpaka nikavunja ile chupa ya chai ya mama Ngoi. Ilikuwa kubwa hivi ya rangi ya dhahamu. Unakumbuka wote mkakimbilia jikoni?” “Sasa nakumbuka.” “Basi mzee Ngoi alinishika ziwa, Willy. Nafikiri mama alijua kuna jambo lilitokea pale kati yangu na mumewe. Ndio kuanzia hapo, mama akanibadilikia kabisa. Akawa kama hanitaki pale kwake.” “Kwa nini hukuniambia, Pendo?” “Ningeanzia wapi!?” Pendo akamuuliza. Willy kimya amebaki na mshangao.

“Mbona bado!” “Acha masihara Pendo! Aliendelea?” “Kabisa. Siku nyingine akanishika kwenye matako palepale kwenu ila nje wakati nataka kuondoka. Nikisema kwenye matako sio juu ya nguo. Yule mzee alinivizia Willy, akanyanyua gauni nililokuwa nimevaa akanishika kwa nguvu.” Willy akahisia dunia inazunguka. “Sasa si unajua madirisha ya chumbani kwa wazazi wako yanaangalia upande ule wakuegeshea magari. Huwezi jua pengine mama aliniona. Lakini niliumia sana. Nililia Willy! Nililia sana. Kitu kilinishika kooni, nikajikuta nalia njia nzima. Nikaona ni ujinga. Nikaegesha gari pembeni, nikampigia mzee Ngoi. Nikamwambia siku akija kunigusa tena, naenda kumwambia baba yangu, wala sio wewe. Nikamwambia ile iwe mwisho asije kurudia tena. Akaomba msamaha, akaniambia alikuwa anajaribu kunionyesha yupo serious na mimi, kwa hiyo kama ni hofu, niondoe. Lakini kama simtaki, basi. Ila akaniambia natupa bahati, yeye angenitunza vizuri sana bila yakuniharibia ndoa. Nikamkatia simu. Hakurudia tena, ila hatukuwahi kuwa marafiki tena na mama. Sasa lililokuwa likimtoka mama yako mdomoni kwake akionyesha ni kwa nini namuumiza, ni kwa sababu sijampatia wajukuu, ila mimi nilihisi ni mengi Willy.” Willy akainama akiwa na macho mekundi sana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mama yake Pendo akaingia. “Willy Ngoi!” Akashituka karibu aangushe mizigo. Willy akasimama kwa haraka. “Shikamoo mama.” Akabaki kimya akimtizama, kisha akahamisha macho kwa Pendo. “Ni nini kinaendelea!?” “Willy amekuja kusalimia mama. Alikuwa amekaa tu hapa. Mbona hujapokelewa mizigo?” “Sijamuona Sifa hapo, nikapitiliza tu. Hata hivyo hivi ni vitu vyako vya humu ndani. Milkshake niliona imekuishia na dawa za watoto. Umeshindaje?” Willy akampokea. “Nimeshinda vizuri.” “Wajukuu?”  Akauliza mama yake. “Naona hawajambo, namshukuru Mungu. Mbona hujaniomba nikurushie pesa? Hiyo Milkshake ni gali kweli!” “Na kweli ni garama. Tutakatana juu kwa juu. Nilitaka usiishiwe kabisa.” “Nashukuru mama yangu.” Akampangia vitu juu ya meza.

Akamgeukia Willy. “Mtoto anaendeleaje Willy? Na mwenzio na wewe mwenyewe?” “Tunaendelea vizuri mama. Asante.” “Umetukumbuka leo?” Akauliza tena mama yake Pendo na sauti yake kama Pendo. “Sijawahi kuwasahau mama yangu.” “Karibu. Mtoto si atakuwa ameshakuwa mkubwa sasa?” “Miezi miwili sasa.” “Hongera sana Willy. Hivi Mungu alikubariki wa wakike au wakiume?” “Alizaliwa wa kike.” Willy alijibu wazi akionyesha kukosa ujasiri. “Hongera sana baba. Mungu ambariki, akue vizuri.” Kimya.

“Wajukuu zako wamekusikia, wameanza kucheza.” Pendo akavunja ukimya, mama yake akacheka na kusogea. Akamshika tumbo. “Mmeamka na njaa? Nimewaletea virutubisho vizuri, mama yenu anawapa sasa hivi. Mtulie humo ndani mpaka mkomae kabisa, mkitoka hapa sio kulala hospitalini. Chumba chenu kipo tayari, babu yenu anakuja kuwatengenezea vitanda jumamosi. Mcheze taratibu msimuumize mama. Sawa?” Pendo akawa anacheka. Willy kimya amesimama. “Sijui wanacheza mchezo gani! Ona huyu alivyotuna mama! Sijui ni dada mtu au kaka yake!” Wakaendelea kucheka huku wakiwagusa. “Walikuwa kimyaa, naona wamekusikia, wakaona wakusalimie kabla hujaondoka.” Bibi yao akawabusu huku akiwashika.

“Naomba na mimi niwasalimie Pendo. Sijawahi kushika mtoto akiwa tumboni.” Willy aliongea kwa huzuni, Pendo na mama yake wakamgeukia. Willy alikuwa amesimama tu pembeni. “Kama ni sawa lakini. Nilitaka na mimi niwasalimie tu.” Akaongea kwa kurudia na wasiwasi usoni. Mama yake akamtizama Pendo kama kutaka kujua msimamo wake kwa Willy aliyemkimbia.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment