Kwa Mungu Yote Yanawezekana.
S |
iku hiyo Pendo
akaamua atoke, aende benki. Alikuwa na shuguli zake zakufanya kwenye benki
mbili tofauti. Alitoka kama mida ya saa nne asubuhi. Akaendesha taratibu mpaka Mlimali
City. Akawa anatembea taratibu humo ndani kuelekea tawi la CRDB palepale ndani Mlimani
City alikojua atapata huduma za benki zote mbili bila kuhangaika. Wakati yupo
karibu na benki hiyo macho yakagongana na Willy. Akacheka. “Umegoma kuzeeka Willy!
Umepunguza mwili wote!” Pendo akaongea huku akimsogelea taratibu, Willy akabaki
ameduaa. “Lakini umependeza.” Pendo akaongeza, akijua wazi anamshangaa. “Ni
wewe Pendo!?” Pendo akacheka. “Ni mimi Willy. Unanishangaa nilivyogeuka kuwa
kama nyumba?” “Hapana. Umependeza.” “Acha kunidaganya Willy! Si unajua na mimi
ninavyo vioo nyumbani kwangu? Najua usichana umeisha. Nakula siku hizi kama mchwa!”
“Hongera sana.” Akacheka. “Asante. Acha
niwahi hapo benki kabla muda wa chakula cha mchana kwa wafanyakazi haujafika,
wakajaa benki. Sina nguvu ya kusimama muda mrefu.” Willy akawa kama bado
anamshangaa.
Pendo
akacheka na kuanza kutembea tena. “Nimefurahi kukuona Willy, uwe na siku
njema.” Akampita huku akiongea taratibu na kujivuta taratibu kama anayeumwa
miguu. Willy akamkimbilia tena akawahi mlango wa benki, akamfungulia.
“Nashukuru. Maana nilikuwa nafikiria, nimwite yule askari anifungulie.”
“Nakuona unavyotembea! Unamaumivu?” Pendo akacheka. “Hata kidogo. Ila nabembeleza
huu mwili unitunzie wanangu. Nimetoka tu kitandani, lakini siruhusiwi kuzurula
hivi, ni basi tu.” “Ungejitahidi kufuata masharti Pendo!” “Najitahidi sana. Mbali
ya kutoka kwenda kujisaidia na kuoga, sitoki kitandani. Leo imenilazimu, na
sina wakumtuma. Dereva wangu amekuwa mama, na yeye leo anashuguli zake” Pendo
akapitiliza mpaka ndani, benki.
Kidogo
Willy akawa ameshapata habari kuu mbili. Watoto ni wawili, na
hakuna mwanaume mwingine kwenye picha. Ni mama yake tu. Akaingia na yeye ndani
akiwa Pendo amemtangulia. Akamtafutia sehemu ya kukaa. “Nitume mimi.” Pendo
akacheka. “Wewe wahi kazini. Mwenzio hii ndio kazi yangu kwa leo. Nikitoka
hapa, narudi nyumbani kulala.” “Kazini?” Willy akauliza. “Nilipewa mapumziko.
Kwa hiyo nipo tu nyumbani. Wala usijali Willy. Mimi nipo sawa. Kwanza nafurahia
kupata wakati kama huu. Nachoka kukaa tu nyumbani peke yangu.” Akamwangalia,
Pendo akacheka. “Unavyonishangaa! Kwani nimebadilika sana?” “Sana! Sijawahi
kukuona ukiwa umenenepa hivyo! Lakini umependeza, ukarudi kuwa mtoto!” Pendo akacheka
sana. “Sababu ya mashavu kuongezeka, yameleta baby face.” Akaongeza Pendo, wakacheka.
“Sasa
unataka kuweka pesa au kutoa?” “Nataka kutoa. Nina mambo mengi yakufanya hapo
nyumbani. Yote yanahitaji pesa. Na nilifungua akaunti ya watoto. Kama hivi
mshahara ulitoka, lakini sikuwahamishia pesa. Nilishindwa kuja. Kwa hiyo nataka
kutoa pesa hapa, nyingine niwapelekee kwenye akaunti yao. Sio hapa. Nilifungua
kwengine, lakini humu humu ndani Mlimani City. Pesa nyingine niondoke nayo.”
Akamuona Willy amebaki akimshangaa. Akacheka. “Nilikwambia nina mambo mengi
humu ndani. Wala sitoki leo.” “Subiri
tuanze kwa kutoa kwanza pesa.” Akaenda kumchukulia karatasi yakutoa pesa, akamletea.
Pendo akajaza kila kitu, Willy akisubiria huku akimshangaa bado. Pendo
akamaliza. “Sasa unataka nikupe wewe?” Pendo akamuuliza. “Naenda nayo pale mapokezi,
wala si kwa teller. Nisubiri tu.” Akachukua ile karatasi na kadi ya benki, akaenda
nayo mpaka hapo mapokezi. Pendo akamuona akizungumza nao, na kumnyooshea yeye
kidole.
Wakampokea,
mfanyakazi mmoja wa benki aliyemkuta pale akaenda kuchukua pesa kwa teller.
Baada ya muda akaona wote wawili wanakuja pale alipokaa. Akamkabidhi baada ya kuhakikisha
ni yeye, akaondoka. “Nashukuru Willy. Acha mimi nisogee benki nyingine.”
“Twende nikusindikize.” Akamshika mkono, akamsaidia kusimama. “Natembea
taratibu sana!” Pendo akaongea kwa deko akijilalamisha kama kawaida yake, mtoto
wa mama. “Nimekuona. Sawa tu, twende.” Wakatoka hapo.
“Vipi
familia yako lakini?” Pendo akauliza wakati wakitembea taratibu. Kimya. “Si
mtoto atakuwa ameshakuwa mkubwa sasa?” Pendo akaendelea kuongea huku akijivuta.
“Ndio miezi miwili sasa.” “Hongera Willy. Mungu amekujibu.” Akamuona
amenyamaza. “Hivi alikuwa wakike au wakiume?” “Wakike.” “Safi sana. Hongera.
Hatimaye na wewe umeitwa baba Willy! Mungu amekufuta machozi.” Akaendelea
kuzungumza taratibu huku wakitembea. “Na wewe una miezi mingapi sasa?”
“Nakwenda wa saba. Tunabembelezana na wanangu taratibu hivyo hivyo.” “Kwani una
matatizo yeyote? Au niulize ni kwa nini umepewa mapumziko?” Willy akauliza.
“Acha nikwambie tukitoka hapa.” Walikuwa
wameshafika benki. Akamfungulia tena mlango, akaingia. Akafanya kama
alivyofanya mwanzo. Akajaza karatasi za benki, akahesabu kiasi cha pesa alichotaka
kiwekwe kwenye akaunti ya watoto wake, nyingine akarudisha kwenye pochi. Willy
akamsaidia kwenda kuziweka. Wakatoka.
“Una
muda tukae tule?” Willy akauliza. “Hapana Willy. Nimeacha kula barabarani.
Najitahidi kula vitu muhimu kwa watoto ili wakomae. Tukae hapa nikwambie.”
Wakakaa nje ya hiyo benki ila ndani ya jengo. “Unakumbuka zile vimbe nilizokuwa
nazo kwenye kizazi?” Willy akaitikia. “Sasa kadiri watoto wanavyokuwa, na
zenyewe zinakuwa.” “Pole Pendo.” Pendo akacheka. “Lakini hazinisumbui, ila
hatari yake inaweza kusababisha nikajifungua mapema kabla ya muda. Na ndio
maana unaona tumbo kubwa hivi. Zinashindana na watoto. Sasa najitahidi kula na
kunywa kila kirutubisho kitakachofaa wanangu, Willy. Sijazi tumbo na vitu vidogo
vidogo ambavyo najua havitasaidia watoto. Nimezidisha umakini, ili wakizaliwa
wakati wowote ule, angalau wawe wamekomaa. Na ndio maana daktari alishauri
nipumzike kabisa ili watunzwe humo ndani.” Willy akainama kama anayefikiria.
“Vipi
lakini wewe? Tumepotezana kabisa! Umerudi kuwa kijana Willy! Au ndio maandalizi
ya harusi, suti ikae vizuri?” Pendo akampiga begani kidogo. Willy akamwangalia.
“Nimekuwa tu na mambo mengi. Mungu alinisaidia nikapata ile kazi. Unakumbuka
nilipokwenda kufanya usahili wakati ule?” “Willy! Kumbe walikuita?” “Walikuja
kuniita Pendo. Wanamshahara mzuri sana, marupurupu mengi. Na jumamosi na
jumapili hakuna kazi. Ni kampuni nzuri sana. Hakuna uswahili kama kule mwanzoni.
Kwa kweli namshukuru Mungu.” “Hongera Willy. Ila na wewe unajituma sana na
unanidhamu ya kazi tokea zamani. Lazima Mungu akuheshimu kwa hilo, akupe
makubwa. Nimefurahi kusikia hivyo.” Wakanyamaza kidogo.
Willy
akamwangalia. “Acha niende Willy. Nina mafundi hapo nyumbani, nataka
nikawalipe.” “Unajenga nini?” Pendo akacheka taratibu. “Sio kujenga haswa,
lakini natengeneza chumba cha watoto. Nimeshamaliza makabati yao. Kuna jinsi
nilitaka yakae kwenye kile chumba karibu na chumba kile tulichokuwa tunakitumia
mimi na wewe. Naona nilipata fundi mjuzi kweli! Amepatengeneza vizuri! Nikatafuta
fundi wa kupaka rangi niliyoona itaendana na wanangu, sasa hivi yupo mchoraji.
Nimetaka achore picha za kitoto huko ukutani, ndipo nianze manunuzi ya vitu
vyao. Vitanda, nguo na diaper. Nataka niwe na kila kitu kabla hawajaja.”
“Hutafanya baby shower!?” Pendo akajicheka na kuinama.
Akamuona
amebadilika sura. “Kwenye baby shower utapata vitu vingi Pendo. Umekuwa
ukiwafanyia watu baby shower na kushiriki pia kwenye za wengine. Huu ni
wakati wa wewe kufanyiwa Pendo! Unastahili.” “Hapana Willy.” “Kwa nini?” Pendo
akajicheka tena kidogo. “Kwanza sio watu wengi nimewaambia juu ya huu ujauzito,
Willy.” “Kwa nini!? Wakati ni kitu ambacho tumehangaika sana!” Willy akashangaa
sana. “Watu wanachoka Willy! Habari zangu na swala la watoto umekuwa wimbo
kwenye kila familia inayonifahamu, na marafiki. Tumbo langu bado lina matatizo
si kama kina mama wengine. Kwa hawa watoto kuwepo hapa mpaka sasa hivi ni Mungu
tu. Kila siku lazima mimi na Sabrina tupigiane simu, tuombe. Kila saa
ninayowaona wapo humo tumboni, kwangu ni muujiza ninao ushikilia kama
mboni ya jicho! Likitokea lakutokea watoto wasiwepo na nishatangaza kwa watu
watoto wanakuja, nahisi sina nafasi ya fedheha nyingine Willy! Swala la kuachika
kwangu sababu ya kutokuzaa limevuma na kusemwa kila mahali! Sitaki
kuwapa watu sababu nyingine yakunikejeli.” Pendo akaongea taratibu kama kawaida
yake, Willy akajisikia vibaya sana.
“Sasa
hebu fikiria watu ndio wanakupa vitu vya watoto. Unagarimu watu pesa na muda,
halafu inakuja tena kusikika, eti yule mgumba alishika mimba, lakini tumbo
lake limeshindwa kutunza watoto!” “Naomba usiseme
hivyo Pendo.” Willy akaongea kwa uchungu sana na kujifuta machozi. “Ni kipi si cha kweli hapa, Willy!?” Pendo
akauliza taratibu. Willy akainama macho mekundu. Wote wakaanza kutokwa na
machozi hapo Mlimani City, mchana huo taa zikimulika pia, na watu wakipita na
kuwaona. Mwishoe Pendo akasimama, akaanza kuondoka huku akifuta machozi. Willy
akamfuata.
Akajifuta
na yeye machozi akaongeza mwendo kumfikia. “Umeegesha wapi gari?” “Upande huu.
Karibu na mlangoni tu.” Wakaendelea kutembea. “Kuna kitu chochote unataka hapa?”
Willy akamuuliza walipokaribia gari ya Pendo. Ni gari aliyomuacha nayo,
anaifahamu gari yake. “Hapana. Mama ndio dereva wangu mwenzio. Wanapokezana na
baba. Kila nikiishiwa naandika na kuwatumia orodha nzima. Wananifanyia manunuzi
na kuniletea nyumbani. Kwa hiyo nipo tu sawa.” Akabonyeza rimoti za gari yake,
gari ikafunguka. Willy akaenda kumfungulia mlango. “Asante.” Pendo akaingia
taratibu na kujipanga kitini tena taratibu na kwa tahadhari, Willy amesimama
mlangoni akimtizama.
“Wewe
Willy ni malaika uliyetumwa leo kwangu na Mungu. Asante sana na Mungu akubariki
kwa msaada wote.” Willy akatoa tu tabasamu akimtizama wakati anavuta mkanda.
Akamsaidia kuuvuta na kumfunga. “Na asante kwa hili pia.” Pendo akashukuru
tena. “Karibu. Naomba kuja kukutembelea nyumbani.” Pendo akamwangalia kama anayemshangaa
kidogo.
“Unataka
kuja kuniona mimi!?” Pendo akauliza kama ambaye haamini. “Ulisema mbali ya ndoa
niliyovunja mimi, sisi ni marafiki tokea zamani, Pendo!” Pendo akacheka. “Kwa
hiyo unanifunga kwa maneno yangu mwenyewe?” “Mimi nakukumbusha tu.” “Sasa kama
ulilikumbuka hilo mbona hukuja siku zote hizo hata kuniona kujua ninaendeleaje,
ndio leo unataka kuja? Au majukumu ya familia yalikuzidia?” Pendo akamuuliza
akicheka taratibu kama alivyo hapendi kumuudhi mtu.
“Nilijua
utakuwa umenichukia Pendo.” “Kukuchukia hapana Willy. Ila niliumia, au tuseme
nina maumivu ya kukupoteza Willy! Unajua sisi tulikuwa marafiki wa muda mrefu
sana? Siwezi kukuchukia kwa kutafuta kwengine kile nilichoshindwa kukupa mimi Willy!
Nilielewa sana tu. Ila niliumia na kujichukia sana. Na wala sitakudanganyi,
bado huwa na kumiss pale ndani.” Willy akainama. Akakumbuka aina ya ndoa
aliyokuwa nayo na Pendo. Tulivu mno. Kila mtu aliwasifia. Wakatulia kwa muda,
Willy amesimama mlangoni, Pendo amekaa.
“Nakukaribisha
muda na wakati wowote Willy. Karibu. Milango ipo wazi.” Willy akanyanyua macho
akamtizama. Pendo akamuona vile macho yalivyo mekundu kama anayetaka kulia.
Akambusu shavuni. “Asante.” Willy akashukuru
na kujifuta machozi mbele ya Pendo. “Nitakuja basi
leo na movie tuangalie.” Pendo akacheka akamtizama na kuamua kumuuliza.
“Utakuja leo!?” “Ndiyo. Si umesema muda na wakati wowote?” “Acha bwana
kunifunga kwa maneno yangu mwenyewe, Willy!” Wakacheka. “Nikitoka kazini,
nitakuja. Huna kitu chochote unapenda kula?” “Nakwambia yale mambo sijui
yakujisikia hamu zile za mimba kula chochote imebidi kuonya akili. Nina ratiba
ya kula vitu maalumu kila wakati. Kabla sijaondoka nyumbani imebidi kunywa
juisi ya tembele. Na kwenye hii chupa unaona hapa kama thermosi, nimeweka
milkshake ya baridi. Ni ya virutubisho vya protein tupu. Nikirudi nina mlo
maalumu. Sasa nikijichanganya tu, nikaweka kitu kingine tumboni, inamaana nilichohitajika
kula cha wanangu sitakila.” “Naona mama umejikana haswa!” Pendo akacheka.
“Si
kidogo. Sitaki kuja kujilaumu Willy. Acha nifanye kwa sehemu yangu, mengine nimwachie
Mungu.” “Na mimi nakuombea Pendo. Mungu atakusaidia.” “Amina na asante sana
Willy. Uwe na kazi njema. Ukija utanionyesha picha za mwanao.” “Kwanza
hujaniambia Pendo.” “Nini tena?” “Ni watoto gani?” Pendo akacheka. “Mungu
amenipa wakiume na wakike Willy. Wakiume nitamuita Samuel. Kama vile Mungu
alivyomkumbuka Hana, akamfungua tumbo na kumpa Samweli. Namshukuru na mimi
kunikumbuka, nakunipa Samuel. Halafu wa kike ataitwa Sabrina. Amenibeba yule
mtoto jamani! Najua Mungu alimleta kwangu kwa sababu Willy. Ni kama ulipoondoka
wewe, Mungu akampa nafasi yako. Amekuwa faraja ya ajabu.” Machozi yalikuwa yakimtoka Willy kama mtoto
mdogo, tena wa kike mbele ya mwalimu mkali mwenye kiboko.
“Amenibebea
aibu yangu magotini bila kunichoka. Ile hali ya upweke pale kitandani usiku,
ilikuwa ikiisha kwa Sabrina. Hata katikati ya usiku nikimpigia, haachi kupokea
na kutoka kitandani. Anamuacha mumewe, azungumze na mimi. Basi tutazungumza
wee, mpaka akisikia nimetulia ndio anaacha nilale. Nilikuwa nikipatwa na hofu,
uchungu, yeye ndiye nilikuwa nikimpigia kama nilivyokuwa nikifanya kwako. Basi
nitalia mpaka nijisikie vizuri. Ndipo ananiaga. Hajawahi kunichoka. Na yeye
ndiye aliyeniombea nikiwa nimekata tamaa kabisa. Akaniambia marufuku kukata
tamaa, hili tumbo lazima libebe mtoto na mimi ninyonyeshe. Aliniombea kwenye
hili gari. Na ni yeye pekee alijua ni mjamzito, mpaka nilipofikisha miezi
mitatu ndipo nikamwambia mama. Mungu alinipa Sabrina wakati ule si kwa kumsimamia
harusi tu, alimleta kwangu kwa sababu, Willy. Ningechanganyikiwa bila yule
mtoto. Kwa hiyo huyu mtoto wangu wa kike, ni Sabrina wangu mimi. Mungu
amenikumbuka, na Mungu ni faraja yangu.” Willy akaondoka machozi yakimtoka,
akashindwa kuongea.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Akaondoa
hapo gari na kumpigia simu Sabrina. “Nimekutana na
Willy wangu, Sabrina.” Sabrina akaanza kucheka. “Da
Pendo na Willy! Anaendeleaje?” “Amerudi kuwa kijana mdogo! Mungu amemkumbuka na
yeye. Ana mtoto wa kike na alipata kazi nzuri. Yupo vizuri kwakweli,
nimemshukuru Mungu kwa anayozidi kumtendea. Amenisaidia sana hapa Mlimani city.”
“Hakika nampigia mama simu kumwambia umetoka kitandani!” Pendo akaanza
kucheka. “Mwache bwana. Ataanza kuongea hatutamaliza.
Lakini huoni hii safari imelipa?” “Kwa kuwa umemuona Willy?” Sabrina
akamuuliza kwa kejeli. “Kumbe! Wewe si nilikwambia
ninahamu yakumuona hata akipita kwa mbali?” Sabrina akacheka sana. “Hata unicheke, baba watoto wangu yule. Siachi kumuombea afya
njema, wanae waje kumuona siku moja.” Sabrina akaendelea kumsikiliza
vile alivyohamasika.
“Da Pendo!” “Kumbe? Na kwa taarifa yako tu, jioni akitoka kazini anakuja
na movie tungalie. Lakini Sabrina, sijui nimemsoma vibaya?” “Kwa nini?” “Kama
anajutia vile! Sijui mdogo wangu.” “Lazima. Na hata Jack alisema. Hakuna sehemu
Willy atakwenda asikukumbuke wewe da Pendo. Umetulia bwana.”
Pendo akaanza kucheka. “Kweli tena. Mimi nimekwenda
kwenye majumba ya watu dada yangu, kwako kumepoa haswa. Kuna ile hali ya
utulivu, lazima akumbuke. Halafu dada yangu wewe mzuri! Mungu alikujalia vitu
vyako vizuri vitupu mwilini mwako, hakuna sehemu Willy atakwenda akapata
mwanamke kama wewe.” “Bwana amelia!” “Da Pendo!” Sabrina akashangaa. “Sana. Amelia kama mtoto mdogo! Amelia ile yakuumia! Sijawahi
kumuona akilia hivyo, wala havifanani na vile vya kwenye msiba wa mama yake.
Amelia na kushindwa kujizuia mpaka akaondoka bila kuaga.” “Maskini Willy!
Atakuwa anakumiss.” “Sijui Sabrina. Lakini namuombea faraja Willy wangu.
Alipokosa, Mungu amsamehe, na amfariji.” Ikamgusa sana Sabrina.
“Una upendo da Pendo wewe!” “Nampenda Willy, Sabrina! Wala
sijisingizii. Ni mtu wangu wa miaka mingi. Hata hivyo alivumilia Willy jamani!
Alivumilia kupita kiasi. Aliniuguza yule mtu, acha Sabrina. Alikuwa akiniuguza
bila kuchoka, maana nilikuwa nikianza kutokwa damu, silali. Kama bomba.
Kuishiwa damu lilikuwa jambo la kawaida sana. Alinibeba mno. Tena alinibeba
akisimangwa na ndugu zake, lakini hakunichoka Willy. Naumia kuona alichoka mwishoni
kabisa.” “Lakini Mungu anamrudisha.” “Haitakuwa kama zamani Sabrina. Willy si
mume wangu tena. Anamajukumu ya familia yake sasa hivi. Na sitaki kumbembesha
mzigo nikamchosha.” Akaongea kiiungwana Pendo, taratibu
tu.
“Lakini unakumbuka nilikwambia mwache Mungu akufute machozi na
akupiganie?” Wakacheka sana. “Kwa hiyo sasa hivi nafutwa machozi kiuutuuzima?” “Achana na
Mungu aliye hai wewe. Ana mtindo wakunyamaza. Akija kutokezea, mbona masikio yatawasha.
Utaitwa heri! Walio kinyume na wewe wanakutafuta.” Pendo akazidi
kucheka. “Usifanye mchezo na wakati wa Bwana.” “Kweli
Sabrina.” “Sasa wewe kaa mkao wa kupokea na kusamehe. Maana maji
yameshatibuliwa, baraka zinamiminika. Watarudi mmoja baada ya mwingine. Kazi
yako ni kupokea na kusamehe tu. Wala usifanye moyo wako kuwa mgumu. Wakirudi
wengi na ukawapokea wengi, ujue ndio wanavyozidi
kukuinua. Maana Mungu anakurudishia waliokuwa kinyume na wewe, kusudi
wakuinue.” Pendo akazidi kufurahia.
“Sema tena kidogo.” Sabrina akacheka
sana. “Niambie Sabrina. Maana sasa hivi ndio naona
unayoongea yanatimia. Zamani nilikuwa nikikuamini kwa imani tu. Hakika sasa
hivi ndio naona.” “Sasa ili inoge, ufurahi, fungua mikono, lakini kwa
tahadhari. Kila anayerudishwa kwako sasahivi, ujue amebeba kusudi la kukusogeza
mbele. Wapokee tu, halafu uone jinsi Mungu atakavyowatumia kukupa mema.” “Yaani
mimi nasamehe kwa ajili yangu?” “Kumbe! Yaani wao wanakuona wewe kama mjinga,
vile unavyowatangazia msamaha na kuwamwagia upendo, kumbe unajua ni vyombo
vilivyosogezwa kwako ili Mungu awatumie, kwa ajili yako wewe mwenyewe.”
Wakashangilia wawili hao kwa furaha zote wakipeana maneno ya kishabiki.
Wakaongea mengi wakitiana moyo, mpaka Pendo akafika kwake. Wakaagana.
Mtakuja.
A |
lichofanya
Pendo baada ya kufika kwake, ni kuchukua chakula na kwenda nacho chumbani kwake.
Akala akiwa kitandani na kulala hapohapo. Msichana wake wa kazi akaja kutoa
vyombo na kumfunika vizuri, akamuacha alale. Ilipofika saa 12 na nusu jioni, Willy
akaingia hapo. Msichana wao wa kazi aliyekuwa akiwafahamu wanandoa hao
akafurahi sana kumuona aliyekuwa baba mwenye nyumba wake. “Karibu kaka. Ulitususa!” Willy akacheka. “Mahangaiko ya dunia. Hujambo
lakini?” “Sisi wazima. Tunaendelea vizuri. Nipo tu na dada hapa.” “Nashukuru
kwa kumsaidia dada yako, Sifa. Umekuwa msaada wakati wote!” Sifa akacheka.
“Lakini uliondoka ukatuacha wapekwe! Unaendelea vizuri huko?” “Namshukuru
Mungu. Yuko wapi dada yako?” “Yupo tu chumbani. Bibi ameniambia nihakikishe hatoki
kitandani, akitoka tu niwapigie.” Willy akacheka. “Karibu ukae nikamwambie kama
upo.” Willy akaenda kukaa sebuleni.
Alikuta
pako vile vile kama alivyopaacha. Akapotelea mawazoni. Ilikuwa ni ndani ya
mwaka tu. Lakini mengi makubwa na mazito yalimpata Willy. Akabaki ameinama.
“Dada anaomba uingie ndani.” Sifa akamtoa mawazoni. Willy akasimama. Akaanzia
kwenye hicho chumba cha watoto. Kweli kilibadilishwa, kikawa kizuri kweli.
Akasimama hapo kwa muda. Akasikia Pendo akimuita. “Willy!” “Nilikuwa naangalia chumba
cha watoto. Kimependeza sana. Umefanya kazi nzuri.” “Nashukuru nimepata pia
watu wazuri.” Willy akaingia chumbani. Na kwenyewe kulikuwa vilevile kama
alivyopaacha. Pasafi, kila kitu kipo vilevile.
Pendo
akamuona vile alivyopotelea mawazoni akiangaza macho pale chumbani. “Ona
ninavyolala sasa hivi!” Akamtoa huko mawazoni kulikoonyesha kumdhoofisha. Willy
akageuka na kucheka. “Kwa nini sasa?” “Mahangaiko tu! Ilimradi kujiridhisha tu
nafsi yangu. Hata sijui kama vina saidia au la! Nimebuni mwenyewe sijui hata
nafikiriaga nini! Naona sababu yakutokuwa na kitu chakufanya.” “Sasa huumii
mgongo?” “Naona maumivu nitakuja kusikia nikijifungua. Lakini kwa sasahivi
nafanya chochote kitakachonitunzia wanangu humo ndani. Pole na kazi.” Willy
akakaa hapo hapo kitandani. “Asante.” Wakabaki wakiangaliana. Pendo akacheka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
- Willy Amerudi Na Habari Za Mtoto Wa Kike Aliyezaa Zelda.
- Ilikuwaje Baada Ya Kuondoka Nyumbani Kwa Wazazi Siku walipoitishwa kikao na baba yao na Zelda kushindwa kutoa jibu la moja kwa moja juu ya ujauzito aliobeba?
- Marehemu mama Ngoi aliondoka akiwa ameacha makubaliano gani juu ya Zelda?
- Akiwa hana kazi, Zelda alimkataa Willy kwa jeuri sana. Jeuri yake anatoa wapi?
- Yote Na
Mengine Mengi Yaliyojiri siku ile Baada Ya Mzee Ngoi Kuitisha Kikao Wanae,
Yatajibiwa na siri zilizokuwa zimefichwa juu ya mahusiano hayo ya usaliti
pia zitafichuliwa,
Sehemu Itakayofuata….
0 Comments:
Post a Comment