Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 33. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 33.

      Kwa Willy!

Baada ya talaka yake, Willy akaamua kuanza majukumu ya ubaba kwa roho moja. Alipomalizana na Pendo asubuhi hiyo ya talaka yeye alirudi kazini mpaka jioni alipoamua kumfuata Zelda nyumbani kwao. Bado alikuwa akiishi hotelini ambako alihamia hapo tokea aondoke na mizigo yake kulikokuwa nyumbani kwake na Pendo. Na Zelda naye bado alikuwa akiishi nyumbani kwao, yaani kwa mzee Ngoi, hakuwa ameondoka tokea alipohamia wakati wa uhai wa mama yao.  

Alifika jioni hiyo baada ya kutoka kazini, akaenda hotelini akabadili nguo za kazi ndipo akaenda huko kwao. Alimkuta Zelda na baba yake hapo sebuleni pamoja na dada yake mkubwa Stella. Akawaambia ndio ameondoka rasmi kwenye maisha ya Pendo. Dada yake akampongeza kwa kitendo cha kijasiri alichochelewa kukifanya kwa muda wote. Akamwambia hata mama yao huko alipo, atakuwa na furaha sana. Akawatakia mwanzo mwema yeye na Zelda, Stella akaondoka baada yakuzungumza na Zelda na kumpa maagizo ya hapo ndani.

Willy alipoaga kuwa anaondoka na Zelda, wataelekea hotelini kwa muda mpaka wapate nyumba ya kupanga, kwa kuwa amemuachia mkewe nyumba kwa makubaliano ya yeye kuchukua eneo la Kigamboni, ndipo baba yake akawaambia hakuna sababu ya kwenda kupanga wakati wanatarajia mtoto na Willy anataka kuendeleza ujenzi huko kwenye eneo alilochukua baada ya kuachana na Pendo, akawaambia waanzie maisha hapo kwake. Na kweli jumba la mzee Ngoi lilikuwa kubwa haswa halafu mama amefariki. Yupo Mzee Ngoi tu na msichana wa kazi. Willy akaona wazo si baya. Akamshukuru mzee, akaenda hotelini kuchukua mizigo yake.

Willy anahamia hapo nyumbani kwao kuishi kama mgeni lakini si Zelda. Hata kipindi cha uhai wa mama Ngoi, Zelda alikuwa akienda hapo na kulala mara nyingi tu akimuuguza. Kwa hiyo wote walijua Zelda yupo hapo kumsaidia kwa karibu mama yao aliyekuwa mgonjwa. Hata alipokuwa akilazwa, basi Zelda akawa kama mtoto wa hapo nyumbani. Mpeleka vyakula hospitalini, na kusaidia mambo ya hapo ndani. Kwa hiyo wakati huo Willy anahamia kuishi naye hapo kama mkewe, Zelda alishakuwa mwenyeji haswa. Hata Willy alifanya kuhamishia nguo zake kwenye chumba ambacho tayari alikuwa akiishi Zelda ndani ya hilo jumba.

Mama mwenye nyumba amefariki, mawifi wanampenda, basi Zelda akawa ndio mama mwenye nyumba hapo. Anajua kunapikwa nini na kunaliwa nini kwa muda mrefu sana. Alikuwa akimtunza Mzee Ngoi tokea mkewe yupo hai ni mgonjwa. Kilichoongezeka ni Willy tu. Hapakuwa na jipya. Akawa mwanamke wa wanaume wawili hapo ndani. Baba yake Willy yaani mzee Ngoi na mumewe sasa ambaye ndio Willy. Mimba hiyo ikalelewa kwa tahadhari yote, kila jicho likawa hapo.

Mzee Ngoi alikuwa mfanyabiashara na shuguli zake. Willy na Zelda wote waajiriwa. Zelda alikuwa mwalimu kwenye shule ya Internatiol school iliyopo Mbezi. Kabla hata ya mwezi wa pili kuhamia hapo kuisha Willy akamuona Zelda anatoka jumamosi hiyo kwenda saluni na gari ya mama yake. Ikamsumbua kidogo. Hiyo gari ilikuwa imefungiwa kwa muda mrefu tokea huyo mama ameanza kuugua. Na ilikuwa ni gari ya thamani sana na bado mpya kabisa. Aliiagiza mama Ngoi mwenyewe alipoanza tu kuugua na ilipofika nchini, aliiendesha muda mfupi sana, na kuifungia kwa baada ya kuzidiwa. Akabaki akiendeshwa na watu wengine na magari yao akipelekwa zaidi hospitalini maana alibaki mtu wa kitandani tu kwa muda mrefu kabla mauti kumfika.

 Zelda aliporudi akamuuliza. “Baba amenipa. Ameniambia naweza kulitumia tu. Au unaona shida?” Zelda akauliza. “Hapana, nilishangaa kuona unaondoka nalo bila taarifa!” “Wewe ulishangaa nini wakati limekaa tu hapo ndani!?” “Sina nia mbaya. Lakini kuna utaratibu wa kugawa vitu vya marehemu.” “Si ulisikia siku ile kutoka kwa kina wifi Stella wenyewe kuwa mama anataka kwa asilimia kubwa mimi ndio nichukue vitu vyake? Sasa kila mtu ana gari, ubaya uko wapi na mimi kuwa na gari kuliko haya maisha ya kupewa lift kila siku!?” Zelda akawa kama anamshangaa Willy, na Willy naye anashangaa baba yake anawezaje kufanya maamuzi makubwa vile bila kumshirikisha yeye au watoto wengine! Akanyamaza.

Baba yake aliaga anasafiri siku hiyo ya jumamosi asubuhi, kwenda Mwanza kikazi. Ilipofika jioni baada ya kula wakati wapo kitandani Zelda akaanza. “Kesho asubuhi nakwenda kwa mama. Kuna sehemu alitaka nimsindikize. Nahisi nikichelewa naweza kurudi jumatatu.” “Sehemu gani hiyo itakayokushinda kurudi kesho hiyo hiyo?” “Kuna shuguli ya mtoto wa rafiki yake Segera.” “Unamaanisha Tanga!?” “Ndiyo, kwani vipi?” Zelda akauliza kwa ukali kidogo. “Kwa nini unapanga safari za mbali na ujauzito huo?” “Kwani mimba ugonjwa! Hee! Acha woga bwana Willy. Tutakuwa hatuna maisha basi! Unataka ndugu wanione nimebadilika baada ya kuhamia hapa? Nitatengwa na ndugu bure sababu ya mimba. Najua hukuzoea haya maisha sababu ya mwanamke uliyekuwa naye mwanzo. Na ndio maana hata mama yako alikuwa hampendi. Hajui kujichanganya na watu. Anakuwa na kama mambo ya kizungu fulani hivi! Sisi ni watanzania Willy. Ndugu ndio utajiri wetu. Hatuwezi kutenga ndugu na kuwaonyesha sisi tupo bora zaidi yao.” Willy akanyamaza.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kwa hiyo hapo alipolala Willy, hakuwa mume wa mtu kihalali. Alitaka kumsoma Zelda tabia ili aone kama ni mwanamke wa kuoa au la. Lakini hata yeye akajua hatamtendea haki kama atamlinganisha na Pendo. Pendo alipitiliza kimaadili. Mtulivu haswa. Halafu walishaishi muda mrefu sana mpaka wakazoeana mapungufu yao, kiasi ya kwamba hata ukiwauliza kila mmoja mapungufu ya mwenzie, wanaweza wakashindwa kuyataja. Ni Willy na Pendo! Hata wao walijua wanapatana. Tatizo likawa mtoto tu.

 Willy akalala hapo pembeni ya Zelda ambaye alikuwa akiendelea kuperuzi simu yake, kitu ambacho kilikuwa kigeni kwa Willy. Alishazoea wakiwa kitandani, simu zinawekwa pembeni, inabakia wao tu hapo kitandani. Lakini kwa Zelda ikawa kama ndio kunapambazuka! Akajiambia na hilo nilakulichukulia.

Asubuhi na mapema alimuacha Willy kitandani, akahakikisha msichana ameandaa kifungua kinywa. Akala kwa haraka. Ilikuwa saa moja kamili, Willy akaangalia saa wakati Zelda anamuaga akiwa anapochi kubwa mkononi kuashiria wazi si wakurudi siku ile. Kwa hakika alikuwa amependeza. Willy akabaki akimtizama wakati anatoka. Akabaki akimtafakari.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ni kama amebadilika gafla na kuwa na pesa nyingi! Akamfikiria. Zelda alikuwa msichana wa kawaida tu. Mwalimu shuleni kwa mtoto wa mdogo wake Willy. Mziwanda wa hiyo familia. Prisca. Na Prisca kipenzi cha mama ndiye aliyemtambulisha Zelda hapo nyumbani kwao baada yakuona mapenzi ya Zelda kwa mtoto wake huko shuleni yamezidi, akajua atamfaa Willy, kaka yake. Akampanga mama yao mpaka mama Ngoi akaona wazo lake sio baya. Pendo anaweza kupinduliwa tu. Kwanza hawakuwa wakimpenda huyo Pendo, halafu hazai. Ndio mpango wa kumuunganisha Zelda kwa Willy ukaanza. Prisca akiwa ndiye ameshikia bango kuvunjika kwa ndoa ya kaka yake, ili Zelda aolewe yeye. Kwa asili Prisca na Stela walikuwa wakorofi haswa. Watoto wa kike kwenye hiyo familia walikuwa wakorofi kuliko hao kina kaka watatu.

Mbio za Sakafuni.…

Jumapili hiyo asubuhi Willy akaachwa hapo kitandani akifikiria mpaka akarudi tena kulala. Kwenye majira ya saa nne asubuhi akaamka, akawa tu yupo hapohapo nyumbani kwao. Ilipofika mida ya saa sita mchana, mdogo wake Zelda wa kiume akaja pale kumuulizia Zelda. Willy akamwambia msichana wa kazi amkaribishe ndani. Ilikuwa mara yao ya kwanza hao mashemeji kukutana. Wakasalimiana akamwambia anaitwa Paul, anasoma shule ya bweni. Alikuja kuomba ada kwa Zelda, na anatakiwa kurudi shule siku ileile akasema ndio maana yupo pale hakwenda nyumbani kwao.

“Mama ameniambia nije kwa dada Zelda.” Willy akashangaa kidogo. “Umezungumza na mama leo?” “Yeye ndiye aliyenielekeza hapa. Mimi nilikuwa nikipafahamu kule alikokuwa akiishi dada zamani, Keko. Akanielekeza hapa na kuniambia sitapotea, nije tu.” “Lini hiyo?” Willy akataka uhakika. “Unamaanisha nini!?” Akawa ameshamchanganya na Paul. Maana Paul alihisi amemueleza kila kitu kwa wazi tu. “Kuzungumza na mama.” “Ndiye amenielekeza kwa simu mpaka hapo getini! Mimi nilikuwa sipafahamu kabisa hapa.” Paul akaweka msisitizo akiwa kama hana uhakika tena na jinsi gani yakumuelewesha huyo shemeji mtu.

“Kwani anarudi saa ngapi?” “Sijui. Umejaribu kumpigia?” Willy akauliza. “Simu yake haipo hewani. Mama naye amejaribu, hajampata na anasema hata ujumbe haujaonyesha kufika.” Na Willy naye akajaribu kumpigia, hakumpata. Paul akasubiri hapo mpaka saa 10 jioni, ndipo akamuona dada yake yupo online Whatsapp. Akampigia kwa haraka. Alichosikia Willy ni matusi kutoka kwa Zelda akimgombesha sana mdogo wake. Akamuona Paul ananyanyuka, na kuondoka hapo bila yakuaga, simu masikioni. Willy akawa hajaelewa. Alimkarimu vizuri tu Paul, iweje leo aondoke bila yakumuaga! Willy akabaki akifikiria huku akijiuliza ni nini kinaendelea? Zelda aliaga anasafari na mama yake, mama yake naye anamtafuta! Akanyamaza.

Kufika saa tatu usiku Zelda akarudi akiwa amekasirika karibu kupasuka. Alikuwa amevuta mdomo kama aliyetayari kwa lolote. Akaelekea chumbani kwao moja kwa moja. Willy akamfuata. “Kwema?” Akauliza vizuri tu. “Kwema, kwani vipi?” “Nauliza tu Zelda. Mbona kama umekasirika wakati nafikiri mimi ndio nilitakiwa nikasirike kwa kilichotokea leo?” “Nisikilize Willy, sijui ulikuwa ukiishi maisha gani mwanzoni, lakini ninachojua ulikuwa na mimi wakati na wewe ulikuwa na  mtu wako.” “Mke wangu.” “Ewaa! Tulikuwa tukikutana, unakaa kidogo tu unamuwahi mkeo. Nilishawahi kukulalamikia?” Willy akashangaa sana.

“Jibu?” “Sasa huo mfano unaendana vipi na hili lililotokea leo? Umenidanganya Zelda!” “Sikukudanganya, ila nilibadili mawazo. Nikaamua kwenda kwenye shuguli zangu nyingine, nisiende na mama. Tatizo liko wapi? Siruhusiwi kubadili mipango?” Zelda akamjia juu. “Ulinikuta na mipango yangu, na wewe nilikukuta na mipango yako. Nikaheshimu mipango yako bila kukuweka chini kikao na kukuhoji kama hivi. Leo unapata wapi haki yakunihoji mimi kama mtoto mdogo au kulalamika?” Willy akakamatwa pabaya sana, akanywea kidogo.

“Naomba unisahihishe Zelda, nakuhisi kama umebadilika sana!” “Kivipi?” Zelda akauliza. “Sijui! Lakini japo sikuwa nikikufahamu sana zamani, lakini hivi ulivyo sasa, sivyo mwanzoni ulivyokuwa.” “Kama ulivyosema, hukuwa ukinifahamu na pengine ndio maana ulinichukulia poa.” “Unamaanisha nini Zelda!? Mbona kama nilikuheshimu sana tu!” Akaongea kwa mshangao mkubwa Willy. “Sijui nyinyi mama yenu aliwafundisha heshima ni nini, lakini wote nyinyi, mimi siwaelewi.” “Na nani tena!?” “Nimechoka Willy, nataka kulala. Sina muda wa kesi. Upo hapa kwa hiari yako. Sijawahi kukudanganya kwa lolote, sijawahi kukurubuni na wala mimi sina shida na pesa zako kama mwanamke wako aliyekupokonya nyumba.” Willy akazidi kuchanganywa.

“Wewe unazungumza nini Zelda?” “Usichoelewa nini? Mwanaume mzima unapokonywa nyumba, unahamia kuishi kwa baba yako! Yaani unaishi kwa mwanaume mwenzio! Unategemea tuishi hapa mpaka lini?” “Wewe ulidhania nikiachana na mke wangu nimpokonye nyumba, halafu sisi ndio tuhamie pale!? Ndivyo ulivyotegemea!?” “Yeye mgumba, ha…” “Usimuite hivyo. Tafadhali sana.” Willy akamuwahi. “Hata mama yako aliniambia unajaribu kukwepa ukweli. Mwanamke wako ni mgumba, mgumba tu. Ukubali ukatae. Ndio ukweli wenyewe huo. Inawezekana Mungu ameiona roho yake mbaya na mabaya aliyokuwa akimfanyia mama aliyemzalia mume, ndio maana Mungu akaona na yeye amnyime mtoto, kumkomoa.” “Unazungumza nini wewe Zelda!?” “Unafikiri dada zako walikuwa wakinificha? Mama yako anakufa huku na yeye akinionya niwe makini na huyo mwanamke wako. Wote wanajua amekushika masikio. Mwanaume mzima umerudi kuishi kwa baba!” Willy akakaa.

“Kwa hiyo haya yote unaongea kwa hasira ya mke wangu kuchukua nyumba?” “Utajijua mwenyewe. Mimi sijali, ila jua maisha yangu yanaendelea kama kawaida. Usifikiri utanirudisha nyuma kimaendeleo.” Zelda alionyesha wazi hababaishwi. Akavua nguo palepale na kuelekea bafuni. Willy akabaki akishangaa. Jeuri kubwa vile anaitoa wapi! Akamuhisi kama anatafuta sababu ya kuachana. Lakini Willy akajiuliza, na ile mimba na mshahara wa ualimu, anafikiria ataishije! Akahisi labda ni ujauzito tu. Amchukulie taratibu.

Akamsubiria atoke kuoga. Alipotoka akaanza tena taratibu tu. “Kama hapa unaona ni shida kuishi, tunaweza kwenda kupanga wakati naendelea kujenga.” Akamcheka kama mjinga wa mwisho. “Unataka kunirudisha kwenye nyumba za kupanga mimi! Huthubutu Willy. Kama wewe umeshindwa na hapa, ndio uondoke. Hapa mimi nimefika.” “Sasa mbona sikuelewi tena? Umetaka kuwa na kwetu, nakwambia tukaanze....” “Na nani!?” Zelda akamuuliza akimtolea macho. “Unataka ukaanze na nani na utuuzima huu?” Willy kimya.

“Asinishangae kwa kunitolea macho kama vile niliyekugeuka Willy! Mimi sikukugeuka. Au sema neno hata moja nililowahi kukwambia, leo limebadilika!” Kimya. “Nilitaka kukushangaa. Maana ulinikuta nimeshaanza maisha yangu. Hukunikuta barabarani.” “Nilikukuta hapa na mama, Zelda! Hapa nyumbani kwetu!” “Sawa sawa. Ulinikuta hapa, kwa wazazi wako. Sio kwenu. Wewe ulikuwa kwako,  na maisha yako. Mtumzima huwezi kulilia kwa wazazi unasema kwetu! Wewe vipi Willy!?” Willy kimya. “Sasa eti unikute hapa, aliponileta mama yako, halafu utake kunitoa hapa, unipeleke wapi tena!?” Willy akaondoka kabisa pale chumbani.

Usiku ule akalala kwenye chumba kingine. Ukweli Zelda hakumdanganya wala kuongeza neno, ila amebadilika sana tabia. Si mnyenyekevu kama alivyokuwa na mama yake akitoa tabasamu kila wakati kitu walichovutiwa nacho hapo nyumbani kwao na kuona atamfaa Willy! “Kweli hajadanganya. Lakini ni kama ametoa makucha yake kwa wazi kabisa!” Willy akawaza. Akaanza kufikiria maneno ya Zelda. “Ni kama haonyeshi kunitaka! Nilijichanganya vipi!?” Akajiuliza na kujishangaa sana. “Lakini sasa yeye anategemea tulee vipi mtoto!” Willy akashangaa na kuhisi aliharakisha mambo. Alifikiria Zelda atafurahia kitendo chakumuacha mke wake na kumfuata yeye, kama ishara ya kuwa amemchagua yeye na mtoto, lakini ikawa tofauti kabisa! Zelda anaonekana ana mipango yake asiyotaka kuingiliwa! Willy akashangaa msichana kama Zelda, anawezaje kumkataa mwanaume kama yeye! Akidhani anampa nafasi ya upendeleo kuwa naye, Zelda hana hata mpango. Mwenzie macho yanaangalia kwengine.

Singida.

S

iku moja kabla ya ufunguzi ya miradi aliyohangaika kubuni Sabrina na mumewe kumuunga mkono, zilianza kugawiwa tisheti za chama hapo mjini. Kukafungwa majukwaa na spika. Hekaheka ikawa kubwa. Pendo kipenzi cha Sabrina alishamtumia nguo za rangi ya chama. Sabrina mwenyewe alijua atapendeza. Kesho yake watu wakaanza kukusanyika uwanjani, mapema sana kwani hiyo shuguli ilikuwa inaanza saa sita mchana, mara baada ya wageni kuwasili. Sabrina na Jack walishatoka nyumbani tokea saa moja asubuhi kuhakikisha mambo hayaharibiki. Mji mzima ukasikika nyimbo za chama tawala zikiimbwa. Kuanzia siku iliyopita, mji ulishaanza kupokea viongozi wa ngazi ya juu wa chama, kutoka Dodoma na Dar. Ikawa hekaheka ya namna yake. Ilishajulikana nani atakuwepo siku hiyo ya ufunguzi. Mida hiyo ya asubuhi watu wakazidi kumiminika uwanjani, kwani nyimbo zilikuwa zikivutia na wasanii mbalimbali kutoka jijini Dar walishawasili hapo. Basi ikawa jambo ni moja tu siku hiyo, hiyo shuguli uwanjani. Kila mwenye uwezo wakutembea na akasikia, akataka kwenda. “MmmH!” Sabrina akaguna. “Nini?” Jack akauliza. “Kama uchaguzi mkuu, tuko kwenye kampeni!” Wakawa wanacheka tu.

Mida ya saa sita wakaona msafara unaingia uwanjani, ukipeperusha bendera za chama na ya taifa. Wakajua mgeni rasmi anaingia. Jack alijua mama yake yupo hapo kwenye msafara na Junior. Alijawa furaha na majivuno, Sabrina alikuwa kimwangalia na kumcheka. “Upo kama toto dogo Jack jamani!” Jack akawa anacheka na kufurahia mama yake kuwepo hapo akishuhudia. Sauti za waimbaji zikaongezeka wakisifu chama tawala. Ikawa shangwe kwelikweli. Na kweli, mgeni rasmi na wageni maalumu wakashuka hapo karibu na jukwaa, Junior na mama yake walikuwepo miongoni mwa wageni, wakapanda jukwaani, wakisifu chama.

Jackson Msindai mwenyekiti wa tawi hilo la vijana hapo Singida akafungua huo mkutano kwa hotuba fupi. Akataja majina ya watu walioshiriki kukamilisha hapo, kisha akamtaka mkewe asogee pale mbele. Vijana wa hapo walianza kupiga kelele na miluzi wakati Sabrina akisimama. Alikaa viti vya nyuma kabisa. Wakaanza kuimba wimbo wa, “Mama, mama!” Wote waliimba wakati Sabrina anasogea mbele. Ni vijana wake aliokuwa akifanya nao kazi bega kwa bega wakitaniana kila wakati wakazidi kumshangilia. Sabrina akawa anacheka huku akitetemeka kwa hofu. Alishamwambia mumewe asimtaje pale lakini Jack akamtaja.

“Karibu wageni wetu wote wamefika hapa, kwa kuwasiliana na mke wangu zaidi.” Wakampigia makofu, Sabrina akaondoka kwa haraka kama kumwambia asipoteze lengo, ajisifie yeye ndio mlengwa. Kijana huyo wa Msindai aliyekuwa akiongoza tokea shule ya msingi, akakaribisha wageni akisifia chama na kutoa hotuba nzuri sana akisema mazuri ya chama tawala. Yale Chama waliyoyafanya hapo tawini na mipango waliyonayo kwa kijana wa chama tawala. Jackson Msindai akaongea vizuri sana kuvutia watu na kweli watu walivutika hata yeye alijua amezungumza vizuri. Alipomaliza yeye ndipo akasimama sasa raisi na viongozi mbalimbali wa chama kupongeza na kusifia chama chao.  Likawa tukio lililovutia kila mmoja aliyehudhuria hapo uwanjani hata wasio wa chama tawala. Vijana wengi wakarudisha kadi za vyama vyao pinzani. Tena kwa kuchana palepale mbele ya jukwaa wakati wakipokea kadi mpya za chama tawala zilizokuwa zikigawiwa.

Kulikuwa na hekaheka, mpaka inafika saa kumi jioni, sherehe zikaisha, wageni wakawa wanaondoka bila mama Msindai kutajwa popote na mtoto wake ila kuzagaa sifa za Sabrina. Kikamuu huyo mama. “Huyu Sabrina amefika kwenye maisha ya Jack niliyemuwekea mimi msingi tokea anazaliwa, nikimtia moyo kwenye uongozi wote mpaka leo ameweza kusimama hapa, anasifiwa Sabrina!” Kikamsumbua yule mama lakini kwa kuwa alikusudia kurudi kwenye maisha ya Jackson, na alishajiambia Sabrina na wanae hawawezi kumtenganisha na mziwanda wake! “Hawa walinikuta, na wataniach…” Akasita baada ya kukumbuka Sabrina amebeba mtoto wa Jack, tena wa kiume. Hapo akashindwa kumalizia ni nini chakufanya na huyo Sabrina akishafanikiwa kuupata tena moyo wa mwanae. Akaona ajibaraguze tu hapo Singida, yaishe akajipange kwa upya.

 Sabrina akiwa anaagana na mama Mkapa ambaye walishakuwa karibu kwa mawasiliano ya hapa na pale, akashitukia mama Msindai na Jack wamemsimamia. Akamsalimia. “Hongera sana kwa kazi nzuri.” Sabrina akacheka. “Asante. Nimefurahi na wewe umekuja kuona maendeleo ya Jack.” “Nashukuru kunikaribisha. Naona wajukuu wamekua wakubwa!” Sabrina akacheka lakini hakutegemea, akamwangalia Jack. Wakacheka. “Wanashika sehemu wanatembea sasa hivi.” Sabrina akaongeza. “Kwa nilivyowaona, wamebakisha kidogo tu watachanganya.” Mama Msindai akahakikisha wanajua kama anawafuatilia. “Tunaamini hivyo.” “Niliwaletea zawadi zao.” Sabrina kwa hofu mbele ya huyo mama akawa ameshachanganywa. “Nani?” Akawa ameshapoteza mtiririko wa maongezi, akauliza wakati walikuwa wakizungumzia watoto. “Zawadi za kina Jeiline.” Akajibu Jack kumsaidia mama yake. “Aaah! Nashukuru sana. Asante.” Jack akawa anamkonyeza, Sabrina haelewi.

“Kungekuwa na uwezekano ningewakabidhi mwenyewe.” Hapo ndipo Sabrina akaelewa kuwa Jack alikuwa akimwambia amkaribishe nyumbani. “Watafurahi kukuona mama. Karibu nyumbani.” “Sitawabana?” Akauliza mama Msindai kiiungwana akicheka. Ndipo Sabrina akajua kumbe alikusudia kulala! Japokuwa bado hakuwa ameupata moyo wake. Akajisikia moyoni ni kama moyo wa huyo mama haujafunguka moja kwa moja kwake, lakini akaona furaha ya mumewe, akaona afunike kombe, mwanaharamu apite. Akamualika nyumbani akiwa na maswali mengi sana. Huyu mama alimsema vibaya sana yeye na wanae hao aliowaita wakizungu. Alishindwa hata kuwashika hao watoto baada ya kuwaona ni wa kizungu! Tokea aondoke siku ya kujifungua hao watoto, hajamuona tena ndio wanakutana hapo akionyesha upendo kwa watoto haohao ambao wanazidi kuonyesha uzungu! Leo anatoa taarifa kuwa anawafuatilia na kuonyesha ni kama anawajali sana na zawadi juu! Sabrina akahisi hila iliyofunikwa na kujirudi kwa maneno ya kimama kwa Jack. Akanyamazia tu. Baada ya wageni kuondoka, pamoja na Junior aliyekataa kulala Singida, aliwaambia yeye ni lazima arudi Dar siku hiyohiyo. Akaondoka na ndege ya hao viongozi wengine, mama Msindai yeye akabaki na kuongozana nao kurudi nyumbani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

 Ikawa ndio kwa mara ya kwanza kwa mama Msindai kufika nyumbani kwa Jack akiwa amemuoa Sabrina. “Hawa watoto ni wazuri kuwatizama hivi zaidi ya kwenye picha! Halafu wamekufanana sana Sabrina. Una damu kali!” Sabrina akacheka akiwaangalia hao wanae ambao hawakuwa hata na dalili ya kuja kuchukua rangi yake. Jack akawafanya mpaka wakakubali angalau kumsogelea huyo mama japokuwa walikataa kabisa asiwashike. “Wakiwa na Jack hao, huwa hawaoni kiumbe mwingine yeyote ila Jack tu. Mimi mwenyewe huwa inabidi kuwachukua kwa nguvu au mpaka Jack aondoke ndio angalau hata huwa wanakumbuka majina yao.” Ikabidi Sabrina kulainisha wakati hao watoto wakilia hawamtaki huyo mama. Kidogo wakacheka.

 Wakawa wanacheza wote watatu karibu na bibi yao, Jack akitaka angalau wamzoee mama yake wamkubali na yeye apate muda na mama yake. Sabrina akatoka jikoni na kuwakuta hapo. Akacheka. “Naona Jack ndio anacheza kuliko watoto wenyewe!” Sabrina akafanya wote wacheke. “Watu na wivu wenu!” Jack akaongea huku akicheza na wanae. Wakamkarimu huyo mama kwa upendo wote. Ila ni kweli alileta zawadi nyingi kwa hao watoto. Kama aliyekuwa anatangaza kurudi kwenye maisha yao moja kwa moja. Urembo wa kichwani ndio ulikuwa mwingi kwa hao watoto na nguo zao. Sabrina na Jack wakawa na kazi ya kushukuru tu hapo. Kesho yake asubuhi, mama Msindai akaondoka kurudi kwake. Angalau hilo likawa limesawazika.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Itakuaje Kwa Willy Na Zelda?

Mahusiano Ya Jack Na Mama Yake Ni Kama Yametengemaa. Sabrina Na Mama Msindai Katikati Ya Mafanikio Ya Jack! Nini Mikakati Ya Mama Msindai Katika Karakati Za Kurudi Kwenye Chati Na Kuchukua Sifa Zake Anazoona Sabrina Amezipora?

Inaendelea….

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment