Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 30. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 30.

Willy alishampenda Pendo na akajiambia ni lazima awe naye. Japokuwa alishatishwa na aina ya mwanaume aliyekuwa naye, huyo Chris aliyekuwa akimsikia kutoka kwa Pendo mwenyewe, lakini akajiambia Chris ni tatizo atakalopambana nalo akishasawazisha upande wake. Akajua njia pekee yakumwaminisha Pendo ambaye alianza kumkwepa hata akimuona anakuja kwa mbele anageuza njia kabisa, akajua ni kutoonekana na Wema kabisa. Akajua kwa kuwa watu wanaongea pale chuoni, habari zitamfikia Pendo kwamba kwa wakati huo hawapo na Wema. Alichofanya Willy alihama kabisa kundi la kujisomea. Akawa anamkwepa na yeye Wema. Akawa mtu wakujitenga na kutoa sababu, mwishoe akaamua kutafuta chumba nje ya chuo. Mama yake akamsaidia kulipia kodi ya mwaka mzima. Willy akawa anaishi chuoni kipindi cha mitihani tu, kama sio hivyo  baada ya madarasa kuisha, alikuwa akiondoka kabisa hapo chuoni.

Hata wakaacha kuonana na Pendo isipokuwa darasani tu ambako wanakuwa na darasa moja. Na kwakuwa wao watu wanao somea masoko walikuwa wakienda kwenye darasa A ambalo wanakuwa wapo kina Willy, na wanafunzi wengine wa uhasibu kama kina Willy ambao ni darasa C&B hukutana na darasa A wanafanya kipindi chao cha uhasibu kimoja. Wakimaliza hicho darasa C&B wanatoka ndipo wanaingia sasa darasa la Masoko la kina Pendo wanakua pamoja na darasa A la uhasibu, ndio hilo la kina Willy. Pendo na Eva waliendeleza tabia yao ileile. Wakiingia hapo darasani basi hukaa viti vya mbele pamoja na kundi lao la masoko. Wakimaliza hicho kipindi bila kugeuka nyuma kwani kilikuwa chumba kikubwa tu. Basi wao huondoka, lakini Willy alikuwa akimuona Pendo kwani yeye alikuwa akikaa mwisho kabisa na macho yake yanakuwa kwake kuanzia anaingia mpaka anatoka.

Muhula huo ukaisha fununu zikienea kuwa Willy ameachana na Wema na amehama pale chuoni. Pendo akajua ndio sababu hamuoni mara kwa mara.

Muhula wa pili Willy alirudi chuoni. Lakini safari hii hakuchukua chumba kabisa pale chuoni. Kupishana kukaendelea. Kina Pendo, watu wa masoko wakapangiwa kipindi chao na watu wanaosomea uhasibu lakini safari hii na darasa C. Kwa hiyo hata Willy akawa hamuoni tena Pendo. Mwishoni mwa muhula huo ili wamalize mwaka wa kwanza, mambo yakazidi kuwa magumu kwa wote kwenye kundi lao la wanaosomea mambo ya Masoko. Mitihani nayo ikawa inakaribia, ikabidi watafute msaada. Wakakubaliana siku ya jumamosi, siku chache kabla ya mitihani wakutane kwenye moja ya madarasa, kila mmoja alete mtu yeyote ambaye anaweza kuwasaidia.

Weekend hiyo hakuna hata aliyekwenda nyumbani. Kila mmoja alihangaika kivyake kusoma, ndio mida ya mwisho ya lala salama ya kumaliza mwaka wa kwanza. Jumamosi wakakutana kwenye hilo darasa, hakuna aliyemleta mjuaji. Wakakutana walewale wote wanatatizo hilohilo. Wakabaki kucheka tu. Wakati wanakaribia kuondoka hapo ili kila mtu akaendelee kuhangaika kivyake, akaingia Willy na Kyande kujisomea hapo kwenye hilo darasa, ila wakakaa mbele kabisa. Mmoja wao akawanong’oneza. “Kile ndio kichwa cha watunza pesa, mwaka wa kwanza.” Wote wakawaangalia. Pendo akamuona Willy amewapa mgongo.

“Naenda kumuomba atuelekeze kidogo tu. Au mnasemaje?” Wote wakamwambia aende. Alikuwa mwenzao wanaesoma nae mambo ya masoko. Alikuwa kijana wa kiume. Wakamtia morari wakamwambia aende. Akasimama na kuwafuata pale walipokuwa wamekaa. “Tunaomba msaada kidogo.” Willy na Kyande wakamwangalia. “Kuna namba zinatuweka macho. Tunahisi kuna sehemu kidogo tu tunakosea. Tunaomba msaada wenu, tafadhali.” Willy na Kyande wakaangaliana. “Nenda kawapige tafu, Kyande.”  Kyande akageuka. Akakuta kundi zima linawaangalia. “Acha kutaka kunidhalilisha mbele ya warembo Willy!”  Wakacheka. 

“Kwani ni topic gani?” Willy akauliza. “Labda niwaletee kitabu kabisa.” Wakati mwenzao kina Pendo anafuata kitabu pale walipokuwa wamekaa kina Pendo, Willy naye akageuka. Macho yakagongana na Pendo. Pendo akakwepesha haraka, akainamia kitabu kilichokuwa mbele yake. Hata hakikuwa chake au upande wake. Mapigo ya moyo ya Willy yakaanza kwenda tena kasi baada ya kumuona Pendo. Akajiambia nilazima yeye ndio atakwenda pale. Akaletewa kitabu akaangalia. “Ona Kyande! Haya mambo yako kabisa haya!” “Nenda bwana Willy, nini?” Willy akacheka huku akiangalia. Akasimama. Pendo akamuona akija pale. Ukweli Willy alikuwa amependeza. Alivaa kiume, akajipangilia na mwili wake. Akaonekana msafi na amenyoa vizuri, Pendo mwenyewe akavutiwa.

“Habari zenu?” Akasalimia Willy. “Nzuri.” Wote wakaitika. Willy macho kwenye kitabu. “Naona hapa tutaelekezana, tusaidiane wote. Na mimi najifunza. Mnataka niandike wapi?”  Akauliza Willy akiongea kiungwana, akijua yeye ndio anatakiwa awasaidie. Wote wakatoa madaftari yao na kumuonyeshea Willy kwa kushindana kila mmoja akitaka aandike kwake. “Chukua hiki Willy.” “Hapa ndio kuna nafasi yakutosha Willy.” Wakabishana wakimtaja jina kabisa, Willy akatulia macho kwenye kitabu akipekua na kuwaacha waendelee kubishana. Akanyanyua macho akamtizama Pendo. Akachukua kijitabu kilichokuwa mbele ya Pendo ambaye alikuwa amenyamaza kimya, hagombanii kama wenzake. Akajua ni lake tu.

Akavuta kiti akakaa na kuanza kuwaelewesha taratibu huku akiuliza kama wameelewa. Mara nyingi alimtizama Pendo. “Tupo pamoja?” Akimuuliza Pendo. “Kama unaswali uliza kabla hatujafika mbali.” Wakashangaa ameweka msisitizo zaidi kwa Pendo. Pendo akaongeza ujasiri akaanza kuuliza ambapo hajaelewa. Willy akaendelea kuwaelekeza mpaka Kyande alipowasogelea na kumgonga mgongoni. “Ndio muda wenyewe?” Willy akauliza. “Washaanza kupiga simu.” Kyande akajibu, wakamuona Willy anatoa simu mfukoni akacheka. “Wanajua unawatosa.” Kyande akaongeza. “Naona na hapa nimemaliza, nishapata waalimu wengi. Si ndio Pendo?” “Nashukuru nimeelewa. Asante.” Pendo akashukuru. “Basi. Na kwa kuwa daftari ni lako, endelea kuwaelekeza wenzio huku mkikumbushana. Acha na mimi nikafundishwe huko.” Willy akaweka kalamu chini. “Asante.” Wote wakashukuru, Willy na Kyande wakaondoka kabisa hapo darasani. Pendo akabaki na furaha yakumuona Willy, akajishangaa mwenyewe.

Darasa la kina Pendo wakawa wakwanza kumaliza mitihani, wenzao bado. Kwahiyo wakawa na kazi yakuzurula tu mtaani kabla hawajarudi majumbani kwao. Pendo angeondoka kurudi nyumbani, lakini akaamua muda huo ndio atumie kuzurula mjini kabla hajarudi kufungiwa nyumbani. Kwa hiyo wakabaki wakisubiria mwaka wa kwanza wenzao wamalize wafanye Pikiniki yakuaga mwaka wa kwanza. Walio walevi wakaendelea kulewa wakifanya fujo hapo chuoni, wakati wenzao wakimalizia mitihani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Siku moja katika kufurahia kumaliza mitihani Pendo akamsindikiza Eva kwenye kampasi za chuo kikuu cha Mlimani, Mabibo ambako yuko mpenzi wake Eva. Wakakaa huko mpaka jioni ya saa 10. Eva alipoamua kulala hukohuko, Pendo akaamua yeye arudi chuoni. Kwanza alishazunguka sana na Eva siku hiyo. Alimwambia siku hiyo ndio huwa kuna mitumba mizuri Buguruni. Wakazunguka, wala Pendo hakupata vitu vya maana, ndipo akamwambia washukie hosteli ya Mabibo, akamsalimie mpenzi wake, ndipo akaishia hapohapo akitaka kulala. Ikabidi Pendo aondoke.

 Akatembea taratibu hutoka ndani mpaka nje kabisa akielekea kituo cha daladala akiwa amebeba mizigo yake. Akaona gari imempita na kusimama mbele yake. Kwa kuwa hakuwa anaijua, hakukimbilia. Akaendelea kutembea taratibu mpaka akaifikia. Akaona kioo cha dereva kinashushwa. Hakutaka hata kuangalia. “Ungependa nikusogeze?” Pendo akageuka, alikuwa Willy. Akacheka. “Sikujua kama ni wewe! Unaelekea wapi?” Pendo akauliza na tabasamu usoni. “Kijitonyama. Lakini naweza kukupeleka wewe kwanza. Mvua inataka kunyesha, utasumbuka na daladala.” “Haitakuwa usumbufu Willy?” Pendo akauliza kwa kujali. “Hata kidogo. Twende.” Pendo akazunguka upande wa abiria akiwa amebeba mizigo yake akapanda garini.

“Unatafuta nini huku Mabibo?” “Eva huyo! Amenidanganya leo Buguruni ndio wanafungua mitumba mipya. Tumezunguka karibu siku nzima!” Willy akacheka. “Nakuona na mifuko.” “Hamna kitu chochote cha maana hapa. Nimenunua tu ili nisirudi mikono mitupu.” “Sasa mbona sikuoni naye?” “Nimemuacha kwa mpenzi wake.” Willy akacheka kama haamini. “Eva ana mpenzi!?” Mpaka Pendo akacheka. “Utashangaa jinsi anavyokuwa mpole, kama sio yeye Eva!” Wakacheka.

“Sasa siku za mitumba mipya Buguruni si leo.” Akamtajia siku yenyewe. “Siku hiyo ndipo wanafungua marobota na ndipo unapata nguo nzuri kwa bei nzuri.” Pendo akashangaa mpaka akamgeukia Willy. Willy akacheka. “Wewe mwana masoko gani hujui habari za masokoni?” “Wewe umejuaje Willy!?” Willy akacheka sana. “Niambie bwana!” “Kwa kuwa ndio biashara yangu hiyo.” “Unauza mitumba!?” Willy akacheka kidogo. “Mimi naingiza yale marobota. Nayauza kwa mnada. Wakishanunua, ndio wanasambaza masokoni.” Pendo akashangaa sana. “Kweli Willy!?” Willy akacheka. “Huniamini?” “Samahani kama nimesikika kama sikuamini. Nahisi nimeshangaa tu. Hongera.” Willy akacheka.

“Kumbe ndio maana umekimbia kuishi na sisi chuoni!?” Pendo akamfanya Willy aendelee kucheka. “Umekimbia kukaa na vijana wenye akili za kitoto!” “Si umefurahi kwa kuwa hunioni tena? Hakuna mtu wa kukuomba umsikilize akanushe habari za uzushi za mtaani!” Pendo akamwangalia na kuinama. “Eti Pendo? Nilikuwa na kukera?” “Hapana Willy. Sikutaka matatizo.” “Kwa Wema au Chris?” Pendo akashangaa kidogo na kumwangalia Willy akaishiwa maneno. “Eti Pendo?” Willy akamwita tena taratibu. “Hukutaka matatizo kwa nani?” “Sikutaka matatizo tu kwa ujumla, Willy.” Akajibu kwa upole akiwa ameinama. Willy akamwangalia na kunyamaza.

Mvua ikaanza kunyesha kama iliyofunguliwa. “Kweli ningekwama njiani! Nashukuru kwa lifti.” “Subiri kwanza tufike ndipo ushukuru. Mvua za Dar huwa zina mtindo wakufunga barabara.” “Umemaliza mitihani?” Pendo akamuuliza taratibu. “Nimebakisha mmoja wa kesho mchana. Najua nyinyi mlimaliza tokea jumatatu asubuhi.” Pendo akacheka. “Ndio maana tunazurula tu.” “Umeonaje lakini?” “Nahisi hesabu nitakamatwa tu. Sikuwa nafanya vizuri sana, halafu mtihani wa mwisho ukawa mgumu kweli! Sidhani kama nitapona.” “Pole.” “Asante. Lakini nashukuru nimemaliza. Kesho mchana mwalimu amesema ataturudishia matokeo yetu. Ndio nitajua.” “Naamini utapita tu. Na hata kama utashikwa hiyo moja tu, hutashindwa kusawazisha.” “Naamini hivyo.” Wakafanikiwa kufika Ubungo. Wakakata kulia kama wanaelekea Posta, ili Willy amrudishe chuoni. Walipofika Shekilango karibu na mataa, wakakuta ajali. Basi kubwa likiwa tupu, limegonga gari ndogo.

Wakasimama hapo kama dakika kumi. Mvua inanyesha, magari ya kutoka posta yanapita kwa shida sana pembeni ya basi lililosababisha ajali. Na ya kwenda Posta ndio yakawa yamezuiwa kabisa. “Nikwambie Willy, hapa utakesha na wewe una mtihani kesho. Wewe katisha hapa Shekilango upite Sinza utafika Kijitonyama kwa haraka. Mimi nivuke hii ajali kwa miguu, nitatafuta hapo mbele ya ajali usafiri wa kunifikisha chuoni.” Willy akafikiria, giza lilishaanza kuingia. “Naona sio sawa kukuacha katikati ya mvua!” “Hamna shida Willy!” “Hapana. Tufuate ushauri wakuchukua wote njia hii ya Sinza, tukifika Kijitonyama, sio mbali na chuo.” “Nakuonea huruma wewe.” “Usijali. Mimi nipo sawa.” Willy akaanza kutafuta jinsi yakutoka hapo kuingia Sinza. Akafanikiwa.

Wakasogea taratibu wanavuka Sinza madukani, wakakutana na foleni nyingine. “Najisikia vibaya Willy! Pole.” “Kwa nini?” “Naona nimekuchelewesha. Isingekuwa kuja huku, ungekuwa umeshafika!” Pendo akalalamika. “Hapana. Mimi nimefurahi angalau tumepata huu muda Pendo. Ulikuwa ukinikwepa kabisa mpaka kubadili njia kama ukiona nakuja mbele yako!” Pendo akacheka kwa sauti ya chini na kuinama. “Kwa nini?” “Nilikuwa naogopa Willy! Ukumbuke wakati ule ulikuwa na Wema. Halafu nikasikia mliachana. Nikasikia tena Wema ana winda yeyote atakayeonekana na wewe.” “Haiwezekani!”  Willy akashangaa sana. “Kweli Willy. Mimi nikaingiwa na hofu.” Willy akashangaa sana.

“Hakika sijui ni kitu gani kilichomfanya Wema adhanie mimi ni mpenzi wake!” Pendo akamwangalia kwa mshangao. “Mpaka yeye mwenywe ilinibidi kumuomba msamaha.” “Nani?!” Pendo akauliza kama haelewi tena. “Wema! Nahisi kuna namna ambayo nilimuonyesha. Au mazingira fulani nilimuwekea, akajiaminisha mimi ni mpenzi wake wakati mimi sina habari!” Pendo akamwangalia kwa muda kama akimshangaa, Willy alipomtizama akainama. “Unakumbuka nilikuomba unisikilize upande wangu?” Pendo akamwangalia tena. “Ni kwa kuwa na mimi baada ya wewe kukataa kabisa nisije chumbani kwako siku ile na kuniambia mambo ambayo mimi mwenyewe sikuwa naelewi, ikabidi kumuuliza Kyande, kutaka kujua ni nini kinaendelea kwa Wema. Akaniambia mambo kama yale na wewe uliyosikia. Nikashituka sana nakujilaumu kuwa nimetengeneza mazingira mimi mwenyewe.” “Kwani yeye Kyande alikwambia nini?” Pendo akauliza taratibu.

“Haikutofautiana na wewe, sema sasa Kyande ndiye aliyenifafanulia zaidi kwa sababu yeye yupo karibu sana na sisi.  Na Kyande alikuwa akilala chumba kinachofuata kutoka kile nilichokuwa nikikitumia wakati ule naishi chuoni. Akanieleza vile Wema alivyokuwa akilala chumbani kwangu, na kuwepo pale kwa muda mrefu. Mambo aliyokuwa akinifanyia au kufanya mbele za watu bila mimi kupinga, kila mtu akaamini ni mpenzi wangu wakati mimi najua anahitaji msaada wangu wa shule na anarudisha shukurani kwa ninayomsaidia! Hakika sikutafasiri vinginevyo kwa kuwa wakati ninapokuwa naye, anaonyesha kuniheshimu sana tu. Hapakuwa hata na dalili za mapenzi!” “Labda kwako lakini kwake yeye alikupenda.” “Sikutaka iendelee, ikabidi kuzungumza naye kabisa.” “Willy! Ukamwambia nini sasa!?” Pendo akashangaa.

“Ilibidi kumuweka wazi kabisa juu ya mahusiano yaliyokuwepo, ninayoyajua yapo, na ninayotaka yaendelee kuwepo kati yetu kuanzia hapo. Na kumuomba kabisa radhi kama kuna mazingira mimi mwenyewe niliyasababisha na kumfanya afikiri vinginevyo.” Pendo akamwangalia na kunyamaza. “Ilinibidi Pendo. Sikuwa na jinsi. Niliona amepokonya uhuru wangu! Watu wananiogopa kwa maneno yasiyo kweli! Angekuwa ni mwanamke wangu, hakika nisingejali.” “Kwa hiyo hukuwahi kuwa na mahusiano naye hata siku moja!?” Pendo akauliza kiuungwana. “Unamaanisha kufanya naye mapenzi?” Willy akaweka sawa lile swali, Pendo akainama tena. “Hata midomo yake sijui ina ladha gani!” Pendo akaona aibu na kugeukia dirishani kabisa.

“Nasema kweli na Mungu wangu ni shahidi. Sijawahi hata kubusu midomo yake! Kama alisema vinginevyo, basi ameongopa.” “Hapana. Mimi sijasikia mambo mengine ya undani. Ila niliambiwa ni kama mlikuwa mkiishi naye pale hosteli.” “Na ndio maana nilihama pale hosteli. Sikutaka tena shutuma za kijinga ambazo si za kweli. Nijulikane nafaidi penzi wakati hamna kitu!” Pendo akacheka taratibu. “Sikutaka kabisa. Nikaona niondoke kabisa.” Pendo akanyamaza. Willy naye akanyamaza.

Foleni ikawa inasogea taratibu, Pendo akajiegemeza kitini. “Hii mvua mpaka inanifanya nitamani kurudi tu nyumbani! Nishuke hapo Sayansi, nichukue daladala au nimpigie simu baba anifuate.” “Sasa kwa nini bado upo hosteli mpaka sasa?” “Nipo na Eva. Eva ameniomba nibaki naye mpaka siku ya Pikiniki ya mwaka wa kwanza ikiisha ndio turudi nyumbani. Aliona tukirudi nyumbani, ndio tuombe ruhusa ya Pikiniki wazazi hawataturuhusu.” Wakacheka. “Eva mtoto wa mwanajeshi yule. Baba yake hamruhusu atoke hovyo.” “Na wewe?”  Pendo akacheka na kunyamaza.

“Kwa hiyo unakwenda Pikiniki?” “Nitakwenda Willy. Wewe je?” “Sijui! Mpaka sasa sijaamua. Naona kutakuwa na fujo nyingi zisizo na sababu! Wewe huogopi?” “Nikiwa na Eva, mwenzio huwa siogopi.” Wakacheka tena. “Halafu Eva amemchukulia tiketi mpenzi wake na marafiki zake. Tutakuwa wengi, siogopi.” “Na wewe umemchukulia Chris tiketi?” Willy akachomekea swali la kiuchokozi, Pendo akainama. “Eti Pendo?” “Hapana. Hata hivyo Chris asingeweza kukubali kwenda kwenye vitu kama hivyo.” “Kwa nini?” “Chris anaustaarabu fulani hivi! Anapenda vitu vyenye viwango vikubwa sana. Kama una moyo mdogo, inachosha. Ni mtu anayependa vitu sasahihi, na kwa wakati sahihi. Hapendi kelele. Zile shangwe za huko Pikiniki za vijana, tena usiku! Kwanza atashangaa sana hata nawezaje kufikiria kwenda.” Pendo akaongea kama anayemfikiria Chris.

“Kwa maana nyingine wewe una moyo mkubwa ndio maana unamvumilia, au mmekutana sifa zenu zinaendana?” “Hapana! Hatuendani na Chris hata kidogo. Naona ananivumilia tu. Mimi nahisi naendana na kila mazingira. Sina kinyaa cha watu.” Willy akashangaa kidogo. “Kinyaa cha watu!?” “Yaani ile kuona watu wa daraja fulani ndio wanafaa na wengine hawafai! Au watu wa namna fulani ndio sawa na wengine sio sawa! Mimi sichagui watu kwa aina ya rangi yao ya mwili, urefu au ufupi, unene au wembamba. Nakuwa nao sawa tu.” “Mfano wa mtu gani yeye hapendi?” Pendo akacheka na kunyamaza kama aliyesita.

“Niambie nisije nikatokezea, nikamuudhi shemeji.” “Chris hawezi kuwa shemeji yako. Wala usiwe na wasiwasi.” Pendo alimfanya Willy acheke sana. “Kweli Willy! Yaani unakuwa naye lakini unatamani muagane! Ukiwa kwake huna raha! Ukiwa naye hotelini pia huna raha! Ukimtambulisha kwa marafiki pia huna raha! Anawakosoa rafiki zako! Eti wewe umeona wapi hiyo jamani?” “Kwa hiyo alimkosoa Eva?” “Ulijuaje! Eti ananiuliza nawezaje kuwa karibu na mtu kama Eva! Kweli jamani!?” “Kwani anasema Eva yukoje?” “Eti vile alivyo na mwili mkubwa kama baunsa, halafu eti na rangi yake! Mimi nikamwambia akimpa nafasi atagundua muonekano sivyo jinsi ya mtu alivyo. Halafu ujue Eva ametokea kunipenda sana mimi! Eti Chris akaniambia kwa mimi kuwa karibu na mtu kama Eva tu, kunaanza kumfanya anitilie mashaka. Hampendi Eva kabisa. Kuna siku nilipita nyumbani kwake nikiwa na Eva, ungejisikia vibaya Willy!” “Alifanyaje?” “Mimi sijui labda kwa kuwa ninamjua Chris anapokuwa na watu wake, lakini sikupenda alivyomchukulia Eva. Ni kama alimuonyesha dharau za waziwazi! Hakika sikupenda. Tena hasa wakati nilishamwambia Eva ni rafiki yangu!” Pendo akajisahau na kuanza kulalamika kwa Willy juu ya mpenzi wake.

“Eva yeye alihisi kudharauliwa?” “Ni vile Eva huwa hajali watu. Lakini aliniambia mpenzi wangu anaonekana mtu wa viwango vya juu. Hawezi watu wa kawaida. Niliumia Willy! Mimi sikupenda.” “Pole. Labda atakuja kubadilika baadaye.” “Hawezi. Anaamini mafanikio aliyo nayo ni kutokana na hizo kanuni za maisha alizojiwekea. Tatizo kubwa hata linalonifanya hata kumkwepa ni kutaka mimi nibadilike niwe kama yeye.” “Unamkwepa?” “Kabisa Willy! Wewe sasa hivi Eva yupo kwa mpenzi wake, mimi narudi chuo! Unafikiri angekuwa mtu wa kawaida si ningekuwa kwake! Pale kabla hujanipa lifti nimetoka kumtumia ujumbe nikamwambia bado tupo kwenye mitihani siwezi kwenda kwake.” “Sasa kwa nini humwambii ukweli? Ni bora umwambie ukweli kuliko kumdanganya.” “Unaona simfanyii vizuri?” Pendo akauliza taratibu tu na sauti yake ya taratibu.

“Sio kwake tu, hata kwako wewe Pendo. Unastahili kuwa huru na kuwa na mtu anayekufurahisha. Au unataka pesa zake?” “Hapana Willy! Huwezi amini huwa hajui hata kuhonga! Chamaana atakachokufanyia ni kukutoa kwenye mahoteli mazuri, ukale vizuri, basi. Akiwa anashuguli ofisini kwao au kwa marafiki zake, akitaka uende naye, ndio anakupa pesa ukanunue nguo ya gharama na viatu ili upendeze. Mpaka wakati mwingine nakosa raha ya kwenda.” “Kwa nini?” “Labda ni mimi tu. Lakini inakuwa kama anakwenda kunifanyia maonyesho tu, sio mapenzi ya kweli. Kwa nini ni mpaka iwe kwenye shughuli zake tu na si zangu! Halafu ana wivu ambao hauna sababu mpaka nahisi wakati mwingine ananitafutia sababu tugombane.” “Kwa nini?” Willy akauliza taratibu tu, akitaka kumjua zaidi.

“Yaani si mnakuwa mnakwenda kwenye party. Hataki anione nazungumza na wenzake hata kuwasalimia na wakati wananifuata na yeye akiwepo! Namuuliza sasa wakinisalimia nifanyaje? Anasema eti ninyamaze, rafiki zake ni wahuni sana wanataka kulala tu na mimi!” Willy akakunja uso. “Sasa mnakuta mmetoka kwenye party nzuri, umependeza, umekula vizuri, mnarudi njiani anagomba na kulalamika. Mimi mpaka nikamwambia nahisi ananitumia tu. Kazi na mimi ikiisha, ndio ananitafutia sababu. Kama hivi anahangaika ananitafuta, ujue ipo tu sababu. Lakini nimechoka Willy. Unakuwa naye, unakuwa huna raha! Una winda maneno yakuongea kila wakati, na nimkosoaji haswa. Popote mbele ya yeyote yule anaweza kukukosoa. Naona sitamuweza.” “Basi mwambie.” “Naona kweli nitamwambia tu. Mwache aendelee kupiga piga kwanza. Nikirudi nyumbani nitamtafuta tuzungumze naye.” Willy akamwangalia.

“Yaani hamuwezi kuachana kwa simu ni mpaka muonane!? Au unataka mkaagane?” Pendo akashangaa kidogo na kuinama. “Eti Pendo?” “Hapana Willy! Nilidhani huo ndio utakuwa ustaarabu!” Willy akamwangalia na kurudisha macho barabarani. “Hata wewe uliniambia ulimuita Wema, mkawekana sawa.” “Wema hakuwa mpenzi wangu. Na nilitaka aelewe hilo. Ila kumtafuta mwanaume aliyekuwa mpenzi wako. Mnapata faragha ya mazungumzo ya kuachana, unafikiri ni nini kitatokea baada ya kutoa malalamiko yako au unapomuaga?” Pendo akanyamaza. Willy naye kimya. Mvua ikazidi kunyesha.

“Nina samaki kwenye cooler box hapo nyuma ya gari. Sikuwa na barafu ya kutosha huko. Nahisi kadiri muda unavyozidi kwenda na bado tupo barabarani, wanaweza kuharibika.” “Labda mimi unishushe hapa Willy, nitachukua daladala wewe uwahi nyumbani.” “Siwezi kukuacha barabarani Pendo. Naomba twende nikaache samaki nyumbani, halafu nitakupeleka chuo. Ni sawa?” “Kwangu ni sawa. Sina ninapowahi ila nakuhurumia wewe.” “Usijali.” “Sasa utasoma saa ngapi Willy?” “Huu ni mtihani wa mwisho na sikuwa na mtihani wowote tokea jumanne. Na kesho tunafanya mchana. Nitakuwa sawa.” “Hapo sawa. Tukifika kwako naweza kutumia choo?” Pendo akauliza. “Bila shaka, kama tutafanikiwa kufika mapema. Au unataka tuingie mahali tuombe ujisaidie?” “Nitajikaza.” “Unauhakika? Maana naweza kusimama popote tukaomba.” “Sitaki tena  kushuka, halafu nikaloa, nikarudi kwenye gari nachirizika maji! Acha nivumilie.” “Basi ukizidiwa uniambie.” “Sawa.” Wakaendelea na safari, Willy akiendesha kwa makini.

“Samaki umewapata wapi huko Mabibo?” Willy akacheka. “Pendo uko makini!?” “Kwa nini?” “Basi tu. Pale kwenye kafteria ya Mabibo, huwa nawapelekea samaki wa ziwani na wakati mwingine kuku wakienyeji. Huwa nawauzia pale na hoteli moja ipo Buguruni. Leo nilikuwa na mzigo uliofika, lakini anaye nisambazia amepatwa na dharula, ndio maana imenibidi niende mwenyewe.” Pendo akamgeukia vizuri Willy. Willy akaanza kucheka. “Kabla hujashangaa. Mama yangu ndiye anayefuga kuku wa kienyeji na wa kisasa. Ana maduka ya nyama. Kwa hiyo huwa nanunua kwake kwa jumla na kusambaza mahotelini, tena akiwa nao. Kwa hiyo kujibu swali ambalo ulikuwa unakaribia kuniuliza, nina biashara ya mitumba na hiyo.” Pendo akacheka. Na Willy akacheka.

“Nimezaliwa kwenye familia ya wafanya biashara. Mama anafanya bishara, na baba naye hivyo hivyo. Kwa hiyo unachukua kidogo huku na kule.” “Kumbe akili yako si ya darasani tu, mpaka nje!” Willy akacheka sana. Ndipo Pendo akahisi mpaka gari anayoendesha ni yake si ya baba yake. “Hongera Willy.” “Namshukuru Mungu si mbaya japo si kubwa sana. Ndio ninaanza. Ya mitumba nafikiri hata haijamaliza miezi sita. Ya nyama ya kuku na samaki nafikiri ni miezi kama miwili tu.” Akafikiria kidogo. “Yeah, ni mitatu. Kwa kuwa niliaza kipindi tulipotoka ile likizo fupi.” “Hongera.” “Lakini zina changamoto zake! Si umeona kama sasa hivi nipo kikazi na si shule?” “Ni kweli. Inabidi uwe una uwezo mzuri darasani, lasivyo shule itakushinda.” “Nafikiri kujipanga zaidi.” Willy akaongeza, Pendo akapotelea mawazoni.

Wakaendesha mpaka wakafanikiwa kufika nyumbani kwa Willy. Akaona geti linafunguliwa. Nyumba nzuri sana. “Usifikiri hapa ni kwangu. Jamaa amenipangisha nyuma huko, chumba kimoja tu.” Pendo akaanza kucheka. “Nilishaanza kujipanga kukupa pongezi.” Willy akacheka. “Ulikuwa unaepuka kuloa, lakini itabidi tu. Gari inaishia hapa. Huko kwangu inabidi kutembea na sina mwamvuli.” “Nimebanwa Willy, sina jinsi. Naomba twende tu.” “Sawa. Basi tushuke, halafu nitakuja kuchukua mizigo.” Willy akawa anakimbia, Pendo anamfuata nyuma. Alikanyaga maji yakutosha tu. Mpaka wanafika barazani Pendo ameloa kabisa.

“Hamna choo cha nje, Willy? Ona jinsi nilivyoloa na kuchafuka! Nitakuchafulia ndani kwako. Heri nisiingie ndani.” Willy akamgeukia. “Pole. Lakini hakuna choo cha nje. Ingia tu ndani.” “Ona matope Willy! Mwenzio nilikuwa nakanyaga majani sio vile vimawe kama wewe.” Willy akacheka. “Vua tu viatu. Utajisuuza ndani. Halafu nitakuoshea viatu.” Willy akafungua mlango, Pendo akavua viatu hapo nje. Wakaingia kwa haraka Willy akijua amebanwa, akamuonyesha choo kilipo.

Akakuta bafu safi na bado linaonekana jipya. “Pendo!” Baada ya muda akamsikia Willy akimuita nje ya mlango. “Tumia taulo hilo hilo unaloliona limening’inia hapo bafuni, chukua kubwa lake. Ni safi, hilo sijatumia.” “Asante. Lakini naona hata nikitumia nitaloa tena, haina maana. Bora nikirudi chuoni ndio nioge moja kwa moja.” “Nikupe nguo ubadili?” Pendo akanyamaza. “Pendo?” “Nitaloa tena Willy. Acha nikabadili moja kwa moja chuoni.” “Ni sawa tukisubiria mvua na foleni ipungue?” Pendo akafungua mlango, akachungulia akamkuta Willy amesimama nje ya huo mlango. “Unamaanisha tusubirie hapa!?” Pendo akauliza. “Ndiyo. Hapa kwangu, kama hutajali. Lakini ukitaka, nitakupeleka hivyo hivyo. Ila naona foleni haisogei sababu ya mvua. Barabara zimefunga sababu ya maji. Si umeona njia ya kuingilia hapa kwangu?” “Mwenzio nilikuwa naogopa usije ukaingia mtaroni, sema nilishindwa kukwambia.” Willy akacheka. “Nilikuona. Sasa sijui huko mbele itakuaje. Utajali kusubiria?” “Hapana. Nakushukuru.” “Karibu. Basi anza kuoga, nikutafutie nguo zitakazokufaa wakati unasubiria.” “Sawa.” Pendo akarudi bafuni kuoga.

Willy akamletea tisheti na pensi yake kama ya kuvaa tu ukiwa ndani. Pendo akajikausha, akavaa na kutoka. “Nimekuwekea chai kwa kuwa ulilowa na kuoga maji ya baridi.” “Hapa nilikuwa natamani nikuombe blangeti.” “Na hilo utapata.” “Nilikuwa nakutania bwana!” “Wala usijali. Ninalo blangeti dogo tu, naamini litakufaa.” Akakaa kwenye kochi, Willy akaenda chumbani. Jikoni, sebuleni pametenganishwa na makochi tu. Hapakuwa pakubwa, ila kwa mtu mmoja kulitoshea. Akatoka na blangeti akamfunika pale alipokuwa amekaa kwenye kochi. “Mbona na wewe hujabadilisha?” “Nilikuwa nakutengenezea wewe chai kwanza, na kukupashia moto chakula. Wakati unakula, mimi ndio nitakwenda kubadili.” “Nitakunywa tu chai, chakula nitakusubiri tule wote.” Willy akacheka. Akamuwekea chai kwenye kikombe, akaacha chakula kwenye microwave, akarudi chumbani kwake, akamuona anatoka na taulo tu. Pendo akakwepesha macho kwa haraka, Willy akamuona akacheka. “Bafu lipo moja tu mgeni wangu. Nivumilie.” Pendo akacheka bila yakujibu.

Akamsikia akioga, baada ya muda akatoka tena na taulo tu. Safari hii akapita mpaka jikoni kifua wazi. Alipogeuka, Pendo akajiiba kuangalia hicho kifua kilichokuwa kikisifiwa na watu wa chuoni kwao. Akageuka kwa haraka, akakuta Pendo akimwangalia. Macho yakagongana. “Unataka nikusaidie wakati unavaa?” “Mgeni sio siku ya kwanza?” Willy akamuuliza akiwa amemgeukia. Mpaka Pendo akahisi anajionyesha kifua chake mpaka tumbo lililojaa misuli. “Hamna shida ili usiingiwe baridi.” Pendo akajibu huku akijaribu kukwepesha macho hapo kifuani. “Usijali. Hata hivyo namalizia. Sina vyakula vingi. Ni wali tu na nyama.” Akageuka kupasha nyama. Akaacha tena kwenye microwave akapita hapo mbele ya Pendo kurudi chumbani kwake. Akatoka na pensi, na singlendi. Vilimkaa vizuri, Pendo akabakiwa kutokwa mate. Ni kweli Willy alivutia. Alipenda mazoezi na yeye ndiye aliyemfanya hata Pendo kuanza mazoezi na kudumu kwenye mazoezi wakati wote.

Akamsogezea chakula palepale, akamwambia ajiwekee kwenye sahani yake kile kitakachomtosha. Pendo akajiwekea. Na yeye akajiwekea akakaa pembeni yake. Akawasha tv, wakaanza kula taratibu. Hapakuwa na maongezi mengi sana wakati wanakula. Pendo akala na kunywa chai yake, huku wakiangalia taarifa ya habari wakiangalia mafuriko yaliyoanza hapo jijini yakitangazwa na vyombo vya habari. Wakazungumza hili na lile huku mvua ikiendelea kunyesha. Pendo akawa mstarabu akatoa vyombo hapo, Willy akamsaidia kusafisha meza wakati yeye akiosha vyombo vichache walivyotumia.

Akarudi kukaa kwenye kochi na kujifunika. Willy akarudi kukaa palepale.  Akamuona amejikunyata. Akacheka. “Sasa wewe muoga wa baridi hivyo, nakutoaje kwenye hiyo mvua hapo nje?” “Mvua na matope Willy!” Pendo akalalamika, Willy akacheka. “Tutajenga yetu yenye cement mpaka mlangoni! Hakuna kukanyaga tope tena. Sawa mama?” Pendo akacheka sana. “Lakini ukiwa tayari kunisindikiza, mimi sina neno. Twende tu. Nilikuwa nakutania.” “Mimi ukiniambia unalala hapa mpaka kesho, ndio itakuwa nafuu na furaha yangu.” Pendo akamwangalia na kucheka. “Eti Pendo? Si ulisema kama sio kero za Chris sasa hivi ungekuwa kwake? Kwa maana nyingine huna kinachokukalisha chuo. Kwanza Eva hayupo.” Pendo akacheka. “Kwa Chris nina kila kitu changu. Kule ni kama nyumbani. Hapa ugenini.” “Niandikie orodha ya vitu unavyotaka viwepo hapa, nitanunua ili na hapa pawe nyumbani.” Pendo akamwangalia na kuinama.

“Pendo?” Pendo akacheka akiwa ameinama. “Au hapa kwenye matope hapawezi kuwa nyumbani?” Pendo akashituka kidogo. “Hapana Willy! Nyumbani ni popote moyo wako ulipo. Sio eneo. Mbona kwa Chris ni pazuri sana. Nikikwambia ni pazuri, amini ni pazuri haswa. Kuna kila kitu cha kisasa. Lakini mbona kumenishinda, nimebakia pale hosteli nikioga bafu la watu wote? Sio kwa sababu hapa pana matope bwana! Naomba usichukulie vibaya. Nilikuwa nakutania tu.” “Najua ulikuwa ukitania. Lakini nikuombe kitu?” Pendo akacheka taratibu, akainama. “Mbona kama umeshajua ni nini nakuomba na umeshakataa?” “Hapana Willy. Niambie tu.” Pendo akaongea kwa kubembeleza.

“Naomba uweke na moyo wako hapa. Hata kwa leo tu. Tulale. Kesho wakati nikienda chuoni kufanya mtihani wangu wa mwisho, twende wote.” Pendo akababaika kidogo. “Usiogope, sitafanya wala kukuomba chochote. Najua upo bado kwenye mahusiano.” Pendo akainama na tabasamu. “Utalala kitandani. Mimi nitalala hapa kwenye kochi ili nisome baadaye. Ni sawa?” “Sawa. Na ninakushukuru.” “Karibu.” “Basi ukiwa tayari kulala, uniambie ili nikupeleke.” “Labda niende sasa hivi ili na wewe upate muda wa kujisomea.” “Hamna haraka. Tunaweza kukaa tu. Naweza hata kuamka asubuhi na kusoma.” Pendo akajirudisha nyuma vizuri akajiegemeza kichwa  kwenye kochi, akajifunika vizuri akatulia.

“Una mwamvuli?” “Unataka kwenda wapi tena?” Willy akauliza. “Nimeacha simu kwenye pochi, ndani ya gari yako.” “Okay. Ngoja mimi nikafuate.” Willy akatoka, baada ya muda akarudi na vitu vyote vya Pendo alivyoacha kwenye gari. “Nimekuta simu yako ikiita ndani ya pochi.” Akamkabidhi. “Asante.” Pendo akatoa simu. Akakuta ni Chris amempigia kama mara 4. Akamwandikia na ujumbe. ‘Tafadhali nipigie, ni muhimu.’ Pendo akafikiria, akamrudishia ujumbe. ‘Nitakupigia kesho.’ ‘Kwa nini kesho na si sasa hivi!? Tafadhali pokea simu yangu.’ Ujumbe huo ukaingia na simu ikaanza kuita tena.

Pendo akaitizama kwa muda, akapokea. “Nini kinaendelea Pendo?” “Nilikuwa busy Chris, na nimetoka kukuandikia ujumbe masaa machache yaliyopita. Kuna nini!?” “Wewe ndio nikuulize kuna nini! Hujibu jumbe zangu na hupokei simu zangu! Is everything okay?” Akauliza Chris kwa wasiwasi. “Nilikutumia ujumbe jumamosi kukwambia sitaweza kuja. Nilikuwa nasoma na wenzangu na jioni hii pia nimekutumia ujumbe kukwambia sitaweza kuja bado nina mitihani! Kwani hujapata jumbe zangu?” Pendo akadanganya tena. Alishamaliza mitihani na Willy alimwambia asimdanganye tena. “Unamaliza lini mitihani?” Akataka kuendelea kumdanganya lakini akakumbuka maneno ya Willy. “Kuna nini Chris!?” “Kwa nini unashindwa kujibu swali dogo tu hilo?”  Chris akauliza kwa ukali. “Usigombe Chris!” Pendo akasikika akilalamika. “Unanishangaza Pendo!” “Samahani, lakini nimekuwa na mambo mengi. Kesho naweza kukufuata ofisini kwa ajili ya chakula cha mchana, tukazungumza vizuri. Ni sawa?” “Nitashukuru. Maana kuna safari nilitaka twende wote. Kama kunisindikiza, lakini na wewe utapata mapumziko baada ya mitihani.” Willy akamuona Pendo anacheka taratibu akajua ameshalainika.

“Ni safari ya wapi, na siku ngapi?” “Tutapanga kesho vizuri. Nina hamu na wewe Pendo! Umekuwa hadimu kupatikana! Ni mitihani tu au kuna jingine linalo endelea? Sio kawaida yako!” Pendo akafikiria kidogo. “Pendo?” Akaita Chris kwa kubembeleza. Pendo alishamjua akiwa na shida huwa anajishusha. “Niambie mpenzi wangu.” “Unavyonibembeleza Chris! Mpaka napatwa wasiwasi! Sio kawaida yako mpaka uwe na shida. Unataka nikusindikize wapi huko kunakokufanya ujishushe kwa kiasi hicho!?” Akamsikia Chris akicheka sana. “Mimi nakupenda sana Pendo, sema mazingira ndio yanakuwa mabovu.” “Mapenzi yako ya muda Chris! Unakuwa unanihitaji kwa sababu fulani, ikiisha na wewe unakuwa, sijui nisemeje!” “Nakupenda Pendo.” “Usinidanganye, wewe niambie unataka nikusindikize wapi, basi.” Chris akasikika akicheka zaidi, Pendo asijue anavyomuumiza Willy.

 “Chris?” “Ni safari nzuri Pendo. Nakuhakikishia safari hii utafurahi.” “Mmmh! Huwa tunaishia kurudi kwenye ndege tukiwa hata hatuongeleshani Chris!” “Sio safari hii. Nakuhakikishia hii utafurahi.” “Acha tuzungumze kesho. Lakini nakuomba wakati unakwenda kazini, unijie na lile begi langu dogo lina baadhi ya vitu vyangu. Nimeweka stoo.” “Lakini si unajua utaondoka na vitu vya huku! Huna haja yakubeba vitu vingine. Utatumia vya huku.” Akapoa baada ya kumkumbusha unyanyasaji wake. “Pendo?” “Hilo begi nalitaka sababu ya vitu vyangu vilivyopo ndani. Nina shida nalo. Tafadhali nijie nalo kesho.” “Sawa. Nakupenda Pendo.” Pendo akanyamaza. “Pendo!” “Asante Chris, nitakuona kesho.” Akakata na kubaki akifikiria. Willy alishahamia mezani kujisomea, lakini akabaki akifungua vitabu vyake. Hata akili haikuwa kwenye kusoma ila kwenye mazungumzo ya Pendo na Chris.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Willy Alimkuta Chris Mwenye Mapungufu Ndiye Mwenye Kisu Kikali, Na Ndiye Aliyebakia Kula Nyama. Alifanikiwa Vipi Kumpindua Mpaka Yeye Ndiye Akabakia Na Pendo?

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment