Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 28. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 28.

Ukalipuka ugomvi mwingine, safari hii ilibidi waume zao wawatoe hapo ndani. Sabrina akamshika mkono Pendo, wakatoka hapo ndani kimyakimya. “Naomba nipeleke popote alipo mama yangu, Sabrina.” Pendo alikuwa akitetemeka kama aliyeingiwa baridi kali. Sabrina akaingiwa hofu, akachukua simu yake akampigia mama yake Pendo. “Pendo, mama?” “Hapana mama, mimi Sabrina.” Huyo mama akashangaa ni kwa nini Sabrina awe na simu ya kiziwanda wake. “Kwema? Mbona unanishitua?” “Naomba usishituke mama. Nataka kuja nyumbani, naomba unielekeze.” “Pendo yuko wapi!?” Akauliza kwa wasiwasi zaidi. “Nipo naye, lakini hana hali nzuri. Ameomba nimlete popote ulipo wewe.” “Unajua hatuishi mbali na kwake?” “Sikuwa najua!” “Yeye anakaa Salasala juu, mimi chini. Njooni, ukifika karibu na kwake nipigie tena nikuelekeze.” Sabrina akatoa gari hapo Masaki, safari ya Salasala ikaanza.

Alielekezwa mpaka akafika nyumbani kwa kina Pendo, akamkuta mama yake na baba yake pamoja na msichana wa kazi wakimsubiria. Wakatoka nje baada ya geti kufunguliwa. “Kuna nini mama?” Mama yake akafungua mlango alipokuwa amekaa Pendo. “Najisikia vibaya mama, sijui nieleze nini?” “Kwa nini!?” Pendo akalia kwa muda, baba yake akaja kumtoa garini wakaingia ndani. “Kuna nini Sabrina?” Sabrina mwenyewe alibaki kama amepigwa na butwaa. “Naomba mumpe nafasi Pendo aeleze mwenyewe.” Sabrina akaongea huku akifikiria.

“Willy ana mwanamke mwingine ambaye anafahamika kwao. Yaani yule mama amekufa akimtambua yeye kama mke wa Willy, na anaomba apewe urithi mkubwa kama kumbukumbu yake kwa wajukuu atakaozaa na kuendelea kuzaa na Willy.” “Subiri kwanza Pendo, huyo mwanamke ni mjamzito!?”  Mama yake akauliza. “Tumbo kubwa kabisa mama yangu! Naumia kuwa mjinga. Ni kama Willy alibadilika kidogo, si sana lakini kuna vimabadiliko niliviona kwake na si kawaida yake, nikawa nikimtetea nafsini mwangu kumbe mwenzangu ana mke huko!” Pendo akalia weee. Wazazi wake wakawa kama wamepigwa na butwaa hawaamini. Willy kwa Pendo! Bora ingekuwa wanandoa wengine si wao! Wote wakabaki wamepigwa na bumbuwazi.

“Naomba twende ukaoge ulale da Pendo. Kesho nitakuja kukuona kabla hatujaondoka.” “Sidhani kama nitaweza kulala Sabrina! Willy!” “Nitakuombea na kukupa dawa ya usingizi. Utalala tu.” Akili ya mama yake ikamjia. Akasimama na yeye. Wakampeleka chumbani, sababu ya vumbi la makaburini, Pendo akaoga vizuri, mama yake akamletea dawa za usingizi na nguo za kulalia, Sabrina akabaki naye hapo kitandani mpaka akalala.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Jack akapiga simu. “Uko wapi mama, nataka maziwa ya wanangu.” Sabrina ndio na yeye akakumbuka ana mapacha. “Kwani niliyoacha wamemaliza?” “Bibi yao anasema walimaliza mapema tu, na ameshawalisha viazi vyakupondwa, wanataka kulala. Ndio nikaona wapate maziwa kabla hawajalala.” “Nakuja sasa hivi, nipo karibu. Msiwape chochote wala kuwalaza mpaka nije, hapa maziwa yanamwagika. Wawekeni chini waendelea kuchangamka.” “Sawa.” Jack akakubali kwa haraka. “Hapana bwana Jack, umejibu bila kufikiria, usiwapakate, watalala.” Jack akacheka. “Ulijuaje?” “Nakujua wewe. Tena sasa hivi wanasinzia, najua utakuwa umewaweka kifuani hapo.” Akamsikia Jack anacheka. “Umejuaje? Hapa nasikia raha!” “Bwana Jack! Watalala wakati mimi maziwa yamejaa, yanauma! Waweke chini.” “Sawa mama.” Jack akakubali bila ubishi.

Baba yake Pendo ndiye aliyemshusha Sabrina nyumbani kwa Pendo na wala hakuingia. Jack akawa hajaelewa. “Pendo yuko wapi?” “Leo atalala nyumbani kwao. Waone hawa walivyofurahi! Washike bwana Jack nikaoge mara moja!” “Mpaka wanangu wakuzirie hilo ziwa!” Jack akalalamika mpaka mama yake Sabrina akacheka. “Naoga mara moja tu. Mama nenda kapumzike mwaya. Pole na ulezi.” “Kwani wanao wanashida! Ilimradi washibe na wawe wakavu. Watazunguka hapo na michezo yao, na wala hawaendi mbali. Hapohapo ulipowaacha. Baba yao alipokuja ndio nikaona wanamfuata kila anaposogea. Na kula nako wala si shida. Tena nimewakalisha hapo chini, ukiwasogezea kijiko, wanafungua mdomo.” “Nishamwambia baba yao, usichana utawashinda hao wanae. Watakuwa vibonge mpaka nguo zishindwe kuenea. Waone wanavyoniangalia!” “Naomba uende bwana Brina, kabla hawajalia! Umekuta wanangu wametulia, unataka walale na machozi?” Sabrina akakimbilia chumbani. Kweli wakaanza kulia. “Nilijua tu.” Jack akalalamika. Akawabeba wote. “Nenda kapumzike mama. Hawa wakishanyonya tu, watalala.” Jack akamuaga mama mkwe wake na kupotelea chumbani.

Sabrina akasikia watoto wake wakilia hapo chumbani. “Natoka sasa hivi.” “Wewe usiongee, toka.” “Sasa nitatoka na mapovu Jack?” “Sasa ukiongea hivyo ndio wanazidi kulia.” Jack akawasogeza mpaka mlangoni kwa mama yao. “Jeiline mama?” Sabrina akamuita, Jeiline akasikia na kunyamaza. Na mwenzie pia akanyamaza. “Mnalia nini?” “Bwana Sabrina!” Sabrina akaanza kucheka bafuni. Wanae wakaanza kulia tena. “Kwani mimi nimefanya nini?” Akaanza kuwaimbia, wote wakanyamaza. Alichofanya Sabrina ni kutoka bafuni, akajikausha akajifunga khanga na kukaa kitandani kifua wazi. Jack akawaweka wale watoto kitandani, kila mmoja akasogelea ziwa lake, wakaanza kuvuta wakiwa wamepiga magoti. Jack akaanza kucheka. “Kama watoto wa mbuzi!” Wakacheka.

Alipoona wanaanza kulemewa, akawapanga sasa pembeni ya makwapa na kuwaegemezea juu ya mito kila mmoja na ziwa lake. Wakanyonya mpaka wakalala. “Walikuwa wamechoka.” Akanong’ona wakati Jack akimchukua Keiline ili kumfanya ateuke, Sabrina akamuweka Jeiline begani. Akamsugua kidogo tu akateuka. Wakawalaza kwenye kitanda kimoja cha watoto. “Watakanyagana leo, mpaka wachoke.” Jack akawafunika vizuri na kurudi kukaa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Imekuaje Brina? Kwa nini hujarudi na Pendo? Wakati ndiye anayetupeleka uwanja wa ndege kesho?” “Makubwa na mazito yamejiri. Acha nikamwangalie mama yangu kwanza, nakuja.” Sabrina akavaa nakutoka. Akahakikisha mama yake amelala vizuri, akarudi kumsimulia Jack mwanzo mpaka mwisho. Jack akainama. “Jack?” Sabrina akamuita kama kutaka kumsikia maoni yake. “Ile siku ya baby shower nilimuhisi vibaya Willy, mpaka nikamuuliza kama ni kwema! Alikuwa akiingia na kutoka pale kwa kaka, hatulii. Na kuna muda akapotea kama lisaa hivi. Wakawa wakimtafuta ili anionyeshe kitu, hakuonekanika. Aliporudi nikamuuliza kama kila kitu kipo sawa, akakubali. Sasa si unajua Willy ni mweupe, kwa hiyo nikaona lipstick shingoni kwake. Nikamwambia kwa kifupi tu, ‘labda hiyo iwe lipstick ya Pendo, lakini kama siyo, bora ukaoshe shingo.’ Sasa kule kuondoka kwa haraka akielekea chooni kama aliyepaniki, kukanitia wasiwasi. Nikasema kama ingekuwa ni Pendo, asingepaniki hivyo. Na nikajiambia huyo msichana ni mkorofi. Anawezaje kumuacha mwenzie na lipstiki kama sio anataka kumfikishia Pendo ujumbe! Nikaumia sana, lakini nikanyamaza wala sikuzungumza naye tena.” “Ungemuonea Pendo huruma, Jack! Aliingiwa kama baridi kwa mshituko.”

“Hawakumfanyia vizuri hata kidogo.” “Lakini niliwapenda wale wake wenzake. Wake wa kaka zake Willy, walimtetea sana. Nusu zipigwe pale. Wote wawili wakataka kumchangia Stella yule dada yao mkubwa.” “Sasa yule ni kopi ya mama yake. Ukorofi na roho zao zinafanana kabisa. Na haogopi mtu yule dada.” “Nilimuona alivyo na jeuri. Halafu baba yao alikuwa kimya mpaka mimi nikashangaa kwa nini haingilii! Wanae wanagombana, yeye kimya.” “Nasikia hata yeye na mke wake hawakuwa wakipata hata kidogo.” Wakabaki kimya wakifikiria, wakaamua walale.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mpaka asubuhi wanaondoka hapo, wenye nyumba wao hawakuwa wamerudi. Jack akampigia simu Willy kumuaga, hakupokea, akamtumia ujumbe. Sabrina naye akampigia Pendo simu kumwambia wamechelewa kuamka, inabidi wawahi uwanja wa ndege. “Nani sasa anawapeleka?” “Da Sabina alishafika muda mrefu. Hapa tunavyozungumza mimi ndio wa mwisho kupanda kwenye gari tuondoke, Jack kashatangulia na wanae. Ukichoka na kelele za Dar, njoo Singida upumzike.” “Kweli Sabrina?” “Jamani da Pendo! Kila siku nakuimbia huu wimbo.” Akamsikia ameanza kulia. “Usilie bwana. Naomba utulie ili uweze kufikiria vizuri dada. Kulia haitasaidia tena.”

“Sikuchagua ugumba Sabrina mdogo wangu!” “Najua na ninaelewa. Ndipo tutamuita Mungu tuliyemuomba na kumwamini. Hata katika hili atoe suluhu. Nishakuwa kwenye hali ngumu kuliko hiyo dada, lakini Mungu alinitoa kwa heshima.” “Hakuna mwanadamu amepita hapa nilipo Sabrina!” Pendo akapinga akilia kwa kusononeka. “Dada! Unaweza usiamini, lakini nakwambia hapo ulipo, wala si pa aibu! Kama binadamu kwa sasa utajisikia vibaya sana nakuona ulimwengu wote unakukodolea wewe macho, unakuzomea na hujui chakufanya.”

“Lakini dada, kama usipo kata tamaa, upo mlango wako wakutokea. Mungu wako anakujali. Wala hajasinzia kuwa asikuone muda huu unapolia. Dada, Mungu wa haki yupo, na anajibu. Sema yeye huwa hana kelele nyingi kama shetani na kazi zake. Ila hiyo siku akinguruma yeye, kila kitu kinawekwa chini yako na watakaosikia kile atatenda, masikio yatawasha. Naomba tulia dada, muonyeshe shetani kuwa mtetezi wako yu hai, na atapambana naye tu. Hata kama hujisikii, piga magoti, lia mbele za Mungu wala si mwanadamu ukazidi kuwapa sababu ya kukufedhehesha. Futa machozi mbele za watu, mlilie Mungu sirini. Sijui kama unanielewa?” “Nashukuru Sabrina mdogo wangu.” Kidogo Pendo akasikika kutulia. “Tutazungumza nikifika. Acha nisichelewe.” Wakaagana, Sabrina akapanda garini na kuondoka.

Hasidi na Asili Yake.

J

ack akasukuma watoto kwenye kigari chao, Sabrina anafuata nyuma na begi la watoto ambalo wataingia nalo ndani kwenye ndege. Wakakaguliwa kila kitu, wakaenda kukaa sehemu ya kusubiri juu kabisa. Kama asiyeweza kutulia akaanza kucheza na watoto. “Jack! Waache bwana ili hapa pawe na utulivu! Unataka wakulilie ili upate sababu ya kuwatoa hapo wakati wametulia.” “Ulijuaje!?” Jack akawa anacheka huku akiendelea kuwachokoza makusudi ili watake kutoka pale walipofungwa. “Kuna unachotafuta Jack wewe! Utafukuzwa hapa na hao wanao!” Jack akaendelea kucheka. Mara awabusu, mara awapungie mkono. Wote wakaanza kumlilia. “Umefurahi sasa?” Sabrina akamuuliza. “Sanaa! Njooni wanangu.” Akaanza kuwafugua, mmoja baada ya mwingine. “Hakika mimi siwajui nyinyi.” Sabrina akageuka upande mwingine kabisa. Jack akazidi kucheka. “Eti mami hatujui sisi watatu? Ametugawa bureeee!” Jack akatoa watoto wote kwenye kigari chao, akaanza kucheza nao.

Sabrina akasikia wakicheka na kelele zao, yeye mwenyewe akaanza kucheka. Akasikia baadhi ya watu wakimsifia Jack kuwa ana watoto wazuri sana, na wenyewe wanacheka. Sabrina akavutiwa akawageukia. Wala hawakuwa na habari naye, wapo busy wakicheza na baba yao. Akagundua kuna mtu ameshika gazeti anawatizama sana. Hakuwa mbali na walipokuwa wamekaa wao ni kama na yeye alikuwa upande huohuo wanao subiria hiyo ndege. Alipomuangalia vizuri akagundua ni Max. Sabrina alishituka akatamani akusanye familia yake akimbie hapo huyo mwanaume asione wanae, akatibua mambo.

Alimjua Max mpenda kesi. Ataunganisha habari, atagundua ni watoto wa Tino na kuanzisha kesi tena. Akabaki ameduaa macho yakashindwa kutoka kwa Max. Wakajikuta wanaangaliana. Max akasimama na kumsogelea Sabrina pale alipokuwa amekaa. Ili kujituliza, Sabrina akaona asalimie. “Shikamoo!” “Marahaba. Niliwaona wakati mnaingia, nikasema labda nimewafananisha!” Sabrina akaingiwa na wasiwasi zaidi akajua ameshawaona tokea wanangia, hawezi kujificha tena. Jack mwenyewe alikuwa amejaa pale na watoto wake, huwezi kuwakana. “Hapana. Ni mimi na timu yangu yote. Kelele hizo za watoto hao watatu zinanihusu.” Max akacheka, kwamba na Jack ni mtoto.

“Umebadilika na kupendeza sana Sabrina! Nilisikia mnaishi Singida.”  Sabrina akashangaa na kuzidi kuingiwa hofu, kwamba mpaka anajua anapoishi! “Tulikuja kwenye msiba.” Hakutaka kumuhakikishia wanapoishi. “Poleni sana. Nani amefariki?” Max akaendelea kudadisi, Sabrina asimuelewe nia yake. Lakini akajibu tu. “Kama utamkumbuka yule msimamizi wa kiume wa kwenye harusi yetu, aliyesimama na Jack, mama yake alifariki jumatano iliyopita, nchini India.” “Poleni sana. Kumbe alikuwa mgonjwa?” “Kwa muda mrefu tu. Watoto na mama hawajambo?” Sabrina akaona abadili mazungumzo kumtoa kwake.

“Tunamshukuru Mungu, hatujambo. Ukaribie tena nyumbani.” Jack akasogea na watoto. “Nimehesabu dakika za hii salamu, nimeona zinazidi kwenda, nikajua naibiwa mke hapa Dar. Mimi ni mume wa Sabrina. Huyu dada mkubwa anaitwa Jeiline, na huyu dada mdogo anaitwa Keiline. Watoto wetu.” Sabrina akajisikia vizuri mbele ya Max aliyekuwa akijua hila yake dhidi yake hata asiogope tena kukutwa na hao watoto wa kizungu. “Huyu ni Max. Unakumbuka nilikutambulisha ukumbini na mkewe siku ya harusi yetu?” Sabrina akataka amkumbuke Max vizuri. “Akili siku ile, tena mida ile, haikuwa pale kabisaa. Mawazo yalishahamia honeymoon.” Sabrina akampiga ngumi Jack akiwa ameshangaa asiamini ameongea hivyo. Jack akacheka na kukimbilia pembeni kidogo. “Watu tunaadhibiwa kwa kuwa wakweli!” Jack akalalamika. Akamgeukia Max. “Ningekupa mkono lakini kama unavyoona, binti zangu wamejaa kila mkono wa dad yao!” Jack akabusu mikono yao kwa pamoja. Max akacheka akiwatizama.

“Mnafamilia nzuri sana. Hongereni.” “Asante.” Wakaitika kwa pamoja wazazi hao kama walioiba watoto wakizungu. “Basi mkiwa hapa mjini msiache kuja kututembelea. Mke wangu alikupenda sana Sabrina.” Sabrina akacheka kinafiki akishangaa kipi kilichobadilika! Ni kweli walimkaribisha nyumbani kwao na kuwaaga vizuri sana. Lakini Max akaja kubadilika sana baadaye na kuchangia kumbadilisha Tino kwa hali ya juu. Sabrina akawa anamshangaa moyoni asimuelewe sasa hivi anachokitaka ni kipi baada yakufanikiwa kumtoa kwa Tino! Au kwa kuwa amemuona kwa kina Msindai ndio anajikomba!

Jack kimya akiendelea kucheza na watoto kama hawasikii, ila amesimama pale pale. “Hivi unajua mke wangu anafanya kazi chini ya kaka yako?” Jack kimya, akaendelea kupeana mabusu na wanae palepale mbele yao. Sabrina na Max. Walikuwa wakipeana zamu, Jack anambusu mmoja baada ya mwingine, wanachekaa kisha na wao wanarudisha mabusu kwa baba yao kwa pamoja, kisha wanacheka tena kwa sauti na kujipigia makofi kama kujipongeza.

“We Jack?” Sabrina akamshitua kwani walibaki wakiwatizama wao. “Kumbe unamzungumzia kaka yangu mimi!?”  Kumbe Jack alisikia! “Yeah! Tena wanafahamiana vizuri tu na mke wangu. Wapo ofisi moja kabisa.” “Safi sana.” Jack akajibu tu hivyo akarudisha akili kwa watoto wake. Max akamgeukia Sabrina. “Kama hutajali, naomba namba yako ya simu ili tuwasiliane.” Jack akashituka mpaka akatoa macho. Akamtizama Max akiwa amebadilika kama sio yeye aliyekuwa akicheka muda mfupi na wanae. Max akababaika kidogo maana Jack aliwasogelea tena kidogo. “Heki No! Tena ya msisitizo mkubwa kabisa. HAPANA.” Bila aibu Jack akakataa. “Kwa nini!?” Max akauliza akibabaika, Sabrina akajua mumewe amemkumbuka Max vizuri tu na ndio maana alisogea pale. Sabrina akabaki kimya akifurahia moyoni amepata mtetezi dhidi ya Max aliyemtenda kupitia Tino walipokuwa Moshi, Max asijue Sabrina anajua.

Jack akawaweka sawa  wanae ili kujibu swali la Max kwa msisitizo. “Nimekataa kwa sababu mimi ni mumewe, sitaki uwe na namba ya simu ya mke wangu. Nafikiri hiyo ndio sababu kubwa na itoshe!” Akajibu hivyo Jack akimtizama Max machoni. “Samahani sana, nia ilikuwa njema tu. Kwa salamu. Zaidi kwa mke wangu. Alimpenda sana Sabrina.” “HAPANA. Leo ndio mnatafuta kuwa na mawasiliano na mke wangu mimi!? Mlikuwa wapi muda wote huo!? Mlisahau kama mnampenda!?” Max kimya, Sabrina akainama.  “Naomba tuheshimiane na kuwe na mipaka jamani! Twende Brina. Naona salamu inatosha.” Watu wa karibu walikuwa wakiwatizama, Sabrina alijua wazi wanafuatilia kila kitu  kinachoendelea pale, kwani tayari walishavutiwa na watoto wao, wakawa wakiwafuatilia tokea zamani.

Sabrina akakusanya vitu vyake pale mezani, akaondoka pale kuelekea alipokuwa amekaa Jack na wanae kabla hajawasogelea pale, tena bila kuaga wala kumtizama tena Max, Jack akafuata nyuma na kuendelea kucheza na wanae bila kuonyesha kama kuna alilofanya la ajabu. Watoto wake walipoona baba yao amerudisha akili kwao, wakaanza kucheka tena upya kama mwanzoni. Safari hii Sabrina alikaa nao karibu kabisa. Walimuacha Max amesimama palepale na hawakuonyesha kumjali tena.

Kwa bahati mbaya wote wakapanda ndege moja kuelekea KIA, na wote wakakaa viti vya karibu kabisa huko mbele ila Max alikaa nyuma yao. Huko kwenye ndege ungemsikia tu Jack na wanae wanavyocheka na kucheza kwa sauti. Ndege ilipotulia tu angani, akamtoa Jeiline kwenye kiti chake alipokuwa amekaa na mama yake, akahamia naye alipokuwa amekaa na pacha mwingine. Michezo ikaendelea. “Mnapiga kelele Jack na wanao jamani! Abiria wengine wamechoka wanataka kupumzika. Mrudishe Jeiline hapa mtulie.” “Keiline ndio anacheka kwa sauti ya juu.” Akamtekenya na Jeiline. Akacheka sana na yeye. “Kumbe na Jeiline pia! Mami anasema muache kelele binti wa Msindai. Mmesikia?” Jack akaendelea kucheza na wanae bila kujali.

“Hakika mtashushwa njiani.” Jack akacheka sana. “Watatupa na parachuti mimi na wanangu?” “Hakika watawashusheni bila parachuti!” Jack akazidi kucheka na abiria wa mbele yao nao wakacheka na kugeuka. Ndio wakajua watu wanawasikiliza. “Mna watoto wazuri sana. Mke wangu alikuwa akiwaangalieni tokea hatujaondoka!” Jack na Sabrina wakacheka. “Asanteni, lakini nakaribia kuwafunga mdomo wote watatu. Ili hapa patulie. Samahanini kwa kelele jamani.” “Hawakeri hata kidogo.” Mkewe huyo abiria mwenzao akaongeza. “Umesikia Sabrina?” “Wewe acha kelele Jack bwana!” Wakazidi kucheka. “Tena hivyo wanavyocheka ukiwasikiliza, unapata burudani!” “Asante mama yangu. Sasa nashangaa Mami anaita kelele na si burudani!” Jack akarudi kucheza na wanae, Sabrina akaguna. “Safari nyingine mnakwenda kukaa nyuma kabisa ya ndege. Viti vya mwisho kabisa huko.” Watu wakacheka tena. “Kwani sisi tunashida! Eti wanangu? Mnajali mlipo nyinyi au ilimradi dad awepo?” Watoto wakaendelea kucheka huku wakiongea kitoto Jack anafurahi! Max kimya viti vya nyuma lakini Sabrina alijua anawatizama tu na kusikia ile fujo.

Walimuacha Max KIA, wao wakasubiri ndege nyingine ya kuunganisha kwenda Singida. Abiria waliokuwa nao mbele wakawa wanapita wakiwapungia mkono wale watoto, na Jack naye anajibu kitoto akiwa amewabeba wote wawili, “Bye Byee!”  Ilibidi Sabrina ndio asukume tu kigari cha watoto kwani Jack aliwabeba. Akamuona Max anawapita bila kuaga wala kuwasemesha chochote, Sabrina akaanza kucheka taratibu, Jack akamuona mkewe akicheka, wala asimuulize akaendelea na watoto wake.

Max kwa mkewe na Tino.

M

ax alikuwa amejawa na hasira kupindukia. Alidhalilishwa mbele ya watu vibaya sana. Alipotoka tu hapo uwanja wa ndege akampigia simu mkewe. “Umefika salama?” Mama Kundi, akamuuliza mumewe. “Nimefika salama, lakini niliyokutana nayo huku, yamenichanganya haswa!” “Nini na wapi tena!?” Mama Kundi akaendelea kuhoji. “Sijawahi kudhalilika duniani kama leo.” Max akalalamika kwa mkewe. “Pole. Ni nini tena!?” Mkewe akamuhurumia na kutaka kujua kulikoni. “Nimekutana na Sabrina pamoja na familia yake. Yaani mumewe, yule kijana wa Msindai na watoto wao.” “Ehe!” “Bwana ulikuwa sahihi. Ni mapacha, halafu nisikilize sasa, wakizungu kabisaaaaaa!” “Haiwezekani Max!” Mkewe hakusadiki.

“Kabisa. Jack na mkewe si wote maji ya kunde tu, sasa wale watoto wawili ni wakike. Ni kama Sabrina amejizaa mwenyewe. Lakini mama, wale watoto ni wazungu.” Max akamuelezea yale aliyoyaona kati yao hao wanandoa. Vile Jack alivyomdhalilisha mbele ya watu. Max akamlalamikia mkewe. Akaeleza vile Jack anavyojifanya ni baba kwa wale watoto ambao Max aliendelea kusisitiza kuwa sio wake hata kidogo. “Bwana watoto ni wazuri hao, huwezi kuwalinganisha na huyo mtoto wa Msindai hata kidogo! Mpaka nimewapiga picha.” “Haiwezekani Max!” “Nilishindwa kujizuia, nikasema nipate ushahidi, na hivi huyo Jack alikuwa mkorofi kwangu, nikahangaika mpaka nikawapata wote wanne, kisha ingine akiwa amebeba hao watoto.” “Nirushie na mimi.” “Lakini chonde mama, usije sambaza tukaingia matatizoni.” Max akamtahadharisha mkewe. “Mimi sio mjinga bwana. Nataka kupata fahari ya macho tu.” Mama Kundi akaweka msisitizo. Mumewe akamtumia.

“Umewaona?” Max akamuuliza mkewe. “Max! Hawa watoto huyu Sabrina kazaa na mzungu gani!? Inamaana alipoondoka hapa na Tino, huko Moshi akapata mwanaume wa kizungu! Maana kabla hajazaa alikuwa na kaumbo kama Miss Tanzania!” “Hata sasa ameongezeka, lakini si sana. Ni kunawili tu. Si umemuona?” “Hapa huwezi kumtambua vizuri, na hivi hujapata uso wake yeye! Bwana mtoto amebadilika huyu!” “Sana! Hakika amebadilika Sabrina. Hata ukimtizama sasa hivi, utajua mambo yake yapo tofauti. Nadhifu mno. Lakini mimi nimefikiria.” “Nini tena?” Mkewe akamuuliza, akisikika wazi bado akili zipo kwenye picha.

          “Tunaweza tukawa tunafikiria mbaliii, ukute hawa watoto ni wa Tino!” Mkewe kimya. “Upo?” “Haiwezekani Max, bwana! Hawa watoto ni wazungu kabisa!” “Mama yake Tino alikuwa muitaliano kabisa. Uliona picha za watoto wa mama zake wakubwa Tino?” Mkewe akatulia kama anayevuta kumbukumbu. “Basi kumbuka ile picha aliyotutumia Tino wakati ule ameondoka tu hapa nchini, akasema ni mmoja wa mtoto wa mama yake mdogo anayeishi nao huko. Walipiga wawili tu.” “Sasa nakumbuka.”  Mke wa Max akakumbuka. “Sasa uzungu ule na huo unatofauti gani? Ni hivyo hawa watoto wamefungwa hizo riboni kubwa zenye maua kichwani. Lakini ukiwaona hivi kwa karibu, nywele sio za mchanganyiko mama, ni za kizungu kabisa kama yule ndugu yake Tino.” Kimya mama Kundi akiendelea kuangalia picha.

“Hao watoto ni wa Tino kwa hakika. Sabrina haonyeshi kama ni malaya wa kiasi hicho. Piga mahesabu ya tokea waage hapo nyumbani na mpaka alipojifungua. Utagundua mimba ni ya kipindi Sabrina yupo na Tino. Hao watoto ni wa Tino bila ubishi. Tino hakubeba damu kali ya kizungu, wanae ndio wamechukua damu ya upande wa mama yake Tino.” “Mungu wangu Max! Ujue wewe ndio umesema kweli!”  Baada ya kuhesabu mama Kundi ndio akapata jibu. “Umeamini sasa?” “Kabisa. Siku zinagongana!” Mkewe akawa amekubali kabisa.

“Sasa jamaa yeye si anajidai mbabe, ananidhalilisha mimi mbele ya watu, nampigia Tino mwenyewe kumwambia watoto wake wapo, jamaa anamiliki. Asijidai mjanja. Namshawishi Tino mpaka akubali aje tudai watoto wake.” “Max!” Mkewe akaingiwa na wasiwasi kidogo. “Ulaji mwingine huo mama.” Max akaanza ushawishi. “Kesi dhidi ya Msindai! Itanguruma mno, kila mtu atajua mimi ndio naisimamia. Mama, nitakuwa gumzo hapa nchini. Na hivi ushahidi dhidi yake nitakuwa nao! Yaani mpaka sasa hivi, nishajua jinsi yakumshinda. Nitaua ndege wawili kwa jiwe moja. Nitamfanyia kazi Tino. Na unamjua Tino huwa analipa bila shida. Na nitazidi kuwa mashuhuri. Nitajulikana haswa.” Max akaongea kwa kujiamini akiwa amehamasika haswa.

“Naomba kuwa mwangalifu Max, usije niharibia ajira.” “Nikuharibie ajira kwani serikali ya Msindai hii!?” Max akashangaa sana tena kwa hasira. “Lakini anao uwezo wa kunifanya chochote, usije sahau hilo mume wangu.” “Akufanye chochote yeye kama nani!? Na yeye ameajiriwa kama wewe tu! Akileta na yeye ujuaji tunamtengenezea zengwe lake. Tena nitahakikisha tunakwenda kisheria kabisa. Tunamwanzishia kesi nzito tu. Hata kashfa dhidi yako. Tena tunaweza kumuwahi mapema kwa haraka kabla hajakugusa  wewe. Na yeye atatumbuliwa vilevile. Kwani uwaziri si cheo tu alichopewa? Sasa tutamuonyesha kwamba mjini wapo watu wanaakili na uwezo kuliko yeye aliyekutana na huo uwaziri wakupewa. Wasilete ujuaji! Nina uzoefu mama. Nitamuweka sawa na watatupisha tu mjini.” Mkewe akawa ameingiwa na hofu lakini Max akaendelea kumshawishi mkewe zaidi akimweleza atafanya nini na nini kwenye hiyo familia ya Msindai mpaka wao watabaki salama.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ø     Max amerudi kazini. Tena safari hii yupo tayari kupambana na kina Msindai wote mpaka bosi wa mkewe, waziri Msindai. Na sifa ya Max ni kutoshindwa kesi, na ameshamuweka mkewe upande wake, wapo tayari kumtengenezea zengwe Waziri Msindai, awapishe mjini. Kipi kitajiri?

Ø  Usikose kufuatilia na kisa cha mapenzi ya dhati ya Pendo na Willy na wao tokea chuoni, lakini kuja kuingiliwa kikatili kwa kiasi hicho! Kisa ni nini? Nani amefanikiwa kupenyeza mkono wake kwenye penzi zito na la muda mrefu? Ilikuaje? Historia ya Pendo na Willy?

 Usikose muendelezo. Mambo ndio yanapamba moto.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment