Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 27. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 27.

 Kesho yake kwenye saa nne asubuhi mizigo kutoka Dar ikaingia. Ikaanza kazi ya kupangwa. Wakaweka vitanda vya watoto chumbani kwao wao wenyewe. Vikaenea hapo ndani japo chumba kilijaa sana. Lakini wakaona ni bora hivyo, hawakutaka usiku kuanza kukimbilia chumba cha jirani ambako ndiko chumba walichochagua kitakuwa cha hao mapacha, ambacho ndicho alichokuwa amepewa Sabrina mwanzoni anafika kwenye hiyo nyumba. Kwa hiyo huko ndipo wakapanga vitu vya watoto wao na vitanda vya kuwalazia mchana. Nguo zao zote na vitu vyao vingine. Nyumba ya Sabrina ikabadilika. Ikakaa sasa kama nyumba ya familia yenye watoto.
Sebuleni nako kukawekwa viti vyao vyenye sehemu ya kuwalaza vidogo tu. Kuna jinsi ukiwasha vinazunguka taratibu na nyimbo za taratibu za kitoto au milio yakuwabembeleza walale au wasilie. Kuna jinsi ukiwasha vitoi vilivyoning’inia juu vinazunguka na mziki na kuzubaisha watoto wasilie hata wakiachwa peke yao. Vyote hivyo alipewa Sabrina kwenye baby shower. Vikamfaa kweli. 

Mama Sabina.

S

iku inayofuata usiku mama yake Sabrina akapiga. Sabrina akaanza kucheka. “Vipi?” “Nakwambia leo tumecheza ngoma zote na hawa wajukuu zako. Mpaka ikabidi Jack akaite nesi atusaidie kuwaogesha lakini pia ikashindikana.” Wakacheka. “Nesi amekuja, ameanza kuwaogesha, nayo ikawa shida. Jack anasema wanaumizwa kwenye vitovu. Hilo zoezi limeendelea hapa, zaidi ya masaa! Mara Jack aseme wafunikwe kwanza, anahisi huyo nesi anakosea. Sasa yeye Jack mjuaji ndio akawa anamuelimisha huyo nesi jinsi anavyojua yeye juu ya watoto. Haya, nesi akifanya anavyotaka yeye, anakasirika anasema anahisi anavyowashika yeye vile wanaumia! Ikawa shida hapa, mwishoe akasema wafutwe, na kuvalishwa hivyohivyo. Inatosha.” Mama Sabina alikuwa anacheka mbavu hana.

“Kwa hiyo watoto wakike leo wamelala bila kuoga!?” “Na sidhani kama wataogeshwa hivi siku za karibuni.” “Basi vitomvu vitaoza!” “Mimi naona bora uje tu mama. Tumekutana wajuaji wawili tusiojua. Hakuna tulilofanya kwa watoto zaidi ya kubishana na kunyonyesha siku nzima.” Mama Sabina akazidi kucheka. “Baba yao ana elimu aliyopewa siku moja ile ya baby shower, na kuona kwa watoto wengine kupitia kwa baba yake, daktari bingwa wa watoto hapa nchini! Huna utakalomwambia akakubali. Mjuaji halafu muoga. Anasema watoto wake ni walaini sana, anaona sio sawa wakashikwa shikwa bila gloves. Gafla ameamua hakuna tena kutafuta msichana wa kazi, mpaka wakomae. Lasivyo anaweza kuja mtu akawaambukiza magonjwa.” Mama yake akazidi kucheka. “Nakwambia ni kazi wala si ndogo. Huyo nesi mwenyewe alimuomba awashike na gloves.” “Sabrina!” Mama Sabina akashangaa sana. “Kweli mama. Na amesema kuanzia sasa, hakuna mgeni kuwashika tena. Wawe wanawaangalia tu.” “Kama mbuga za wanyama?” Wakazidi kucheka.

“Naomba tu uje, utusaidie kwa muda mama. Lasivyo hakuna kitakachofanyika hapa, na naona kazini hatarudi. Tuna hekaheka hapa, haziishi. Kila kitu anafanya mwenyewe. Kupika na watoto pia ni yeye, mpaka namuonea huruma. Hataki nifanye chochote, anasema nipumzike. Mpaka nahisi atachanganyikiwa.” Wakacheka. “Mimi nipo tayari.” “Na baba? Nahisi mkija naye akili itatulia. Huku tuko wenyewe. Nyumba ni kubwa na kuna nafasi. Jack mtu mzuri, hana shida.” “Tumemuona. Sasa utatusaidia nauli? Maana hali sio nzuri. Ile mahari yako ilitusaidia kulipa ada za wadogo zako na kulipalipa madeni tuliokuwa tukidaiwa. Na ikatusaidia kwenye..” “Mama, ile pesa ilikuwa yenu. Matumizi ni juu yenu. Huhitaji kuniambia jinsi mlivyotumia. Nakurushia pesa sasa hivi, au unafikiri Jack awasaidie kukata tiketi? Wanaye mtu wao ni Agent wa ndege.” Mama Sabrina akashituka.

“Unataka tuje na ndege!?” “Ndio naona itakuwa rahisi, huku mbali! Au unafikirije?” Akasikia mama yake anashangilia. “Tutaondoka na ndege baba Sabina!” Akasikia akimwambia baba yake, wakacheka. Sabina akachukua simu. “Naona unataka kuwafanya kina mama washindwe kulala! Mama haamini!” Sabrina akacheka tu. “Jamani kuzaa kuzuri. Na mimi napanda ndege kwenda Singidaaa!” Sabrina akacheka wala asijue kama wangefurahia hivyo. Wakazungumza wakitaniana. Wakaagana. 

Wazazi wa Sabrina, Singida.

M

ida ya mchana Jack alikwenda kuwapokea wazazi wa Sabrina uwanja wa ndege. Ilipofika jioni wakaingia. Sabrina alikuwa ameshawaandalia sehemu ya kufikia kwenye chumba alichokuwa akiishi Emma. Nacho walikitengeneza vizuri tu. Wakaongeza choo humo ndani na kujengea sakafu ya marumaru mpaka bafuni. Kikawa chumba kizuri na hadhi. Sabrina alitandika mashuka masafi na kuwawekea mataulo safi bafuni. Kikawa kipo tayari kutumika. Jack akawaingizia mizigo yao hapo ndani kwenye hicho chumba. “Kweli mnanyumba nzuri sana! Kuanzia nje mpaka ndani pako vizuri sana.” Baba yake Sabrina akasifia, na mama yake akaongeza. “Asanteni.” “Ni kazi ya Sabrina hii. Palikuwa jangwa hapo nje. Tulikuwa na kazi ya kumwagia maji uwanja kila siku asubuhi kupunguza vumbi lisiingie ndani.” Wakacheka.

“Sasa wajukuu wameogeshwa leo?” Mama Sabina akauliza, Sabrina akaanza kucheka huku akimwangalia Jack. “Sasa unacheka nini? Si mseme mimi ndio nimewaogesha?” Jack akajibu. “Amewafuta. Kule sio kuogeshwa bwana.” Sabrina akajibu akicheka. “Vyovyote utakavyosema. Wanangu hawajaenda kucheza nje. Na mbona husemi jinsi nilivyowafuta vitomvu vizuri, mpaka nesi mwenyewe amenikubali.” Sabrina akazidi kucheka. “Na leo pia nesi alikuja!?” Mama Sabina akauliza akishangaa. “Leo alikuja kuangalia tu, wala hakuruhusiwa kushika mtoto hata mmoja. Baba yao ndio alikuwa akiwahudumia, sisi watizamaji.” Wakazidi kucheka. “Lakini dad amefanya kazi nzuri sana, mpaka nesi amemsifia.” “Asante sana Sabrina. Hilo ndilo ulitakiwa kulisema tokea mwanzo.” Jack akaondoka hapo akaelekea jikoni kuandaa chakula.

“Sasa hao watoto lazima waoge Sabrina na wanyooshwe.” Mama Sabina akanong’ona baada ya Jack kuondoka. Sabrina akaanza kucheka. “Mimi naona mazungumzo hayo uyafanye baba yao akiwepo hapa. Nahisi kwako atakuonea aibu.  Huyo nesi mwenyewe ni hivyo wanafahamiana, anamjua Jack na anaelewa ni watoto wa kwanza. Lakini ingekuwa mtu mwigine, asingerudi leo. Jana alimgombesha kabisa.” Mpaka baba yake akacheka. “Sasa hapo walipo kwenye hivyo vibembea, wanatolewa au ndio tunawaangalia tu?” Baba yake akauliza, huku amewasogelea wakizungushwa kwenye vibembea vyao, wamelala. “Wewe baba kaoshe mikono hapo sehemu ya kulia chakula kuna sinki linatoa maji. Kuna sabuni hapohapo na taulo la kukaushia mikono. Uje uwashike utakavyo. Nyinyi atawaonea aibu. Au unataka nikuletee hapohapo unawe kwenye beseni?” “Wala haina sababu. Acha nikaoshe kwenye maji mengi. Tumekuwa na safari ndefu, tumeshika kila mahali. Nahitaji maji mengi. Nitakwenda tu. Ila tu sitaki tumuudhi.” “Hawezi. Si anajua mpo hapa kutusaidia! Nyinyi atawasikiliza.”

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Bila ya kuchelewa wala kusita mama Sabina akashika kazi ya ulezi kwa hao watoto. Akaowaogesha hao wajukuu kwenye maji mengi tu na kuwasafisha vizuri. Akawafanyia mazoezi yakuwanyosha vizuri, akawavalisha nguo za kulalia, wakachanwa na nywele, Jack mwenyewe akakiri watoto wake wamependeza. Huyo mama alishika usukani wa maisha ya pale ndani akawa kama mwenyeji. Jack alipomuona anayoyafanya, akajua  ndiko Sabrina alikorithi. Akiwa ametulia bila paniki wala papara alifanya mengi kwa wakati mmoja. Alianza kwa watoto na mzazi. Inafika muda wa usiku, mzazi na watoto wote amewaogesha. Mzazi akamkanda tumbo la uzazi. Chakula kizuri kwake, na wanae wakanyonya vizuri akimsaidia kuwachezea vimiguu vyao, wakanyonyeshwa mpaka bibi yao mwenyewe akaridhika na kwenda kuwalaza. Usiku huo wa kwanza tu, mambo yakawa yameenda vizuri na kwa utulivu. Jack mwenyewe alipata muda wa kupumzika.

Siku zilivyozidi kusogea yule mama akapata uhuru mle ndani, akamsaidia Jack hata mambo ya mle ndani. Akawa akimuuliza tu Jack anataka kufanywe nini, basi huyo mama anamsaidia mpaka kupika vyakula vya nyumba nzima, Jack akabaki kushika tu watoto wasafi, hana kazi, akifurahia likizo yake ya uzazi na wanae. Baba Sabina yeye akawa amkisaidia kazi za nje. Wazazi hao watu wa shamba, wanajishugulisha. Kazi za mkono si tatizo. Basi baba Sabina yeye akawa akimka tu, anaanzia nje kwenye maua na usafi wa ua. Jack alikuwa akiona haya, wakwe kutumika nyumbani kwake! Lakini Sabrina akamwambia awaache wafanye, ndipo watajisikia kuishi pale kwa uhuru. Hata baba mkwe wake alimwambia yeye na mkewe ni watu wa shamba. Maisha yao ni kazi. “Tutakufa haraka sana kama tusipofanya kazi baba.” Jack akacheka. Walikuwa wazazi washupavu, miili mizuri kama hawana watoto wakubwa kama kina Sabina. Jack akabaki kushukuru tu.

Vitomvi vikakauka mpaka kuanguka na watoto wakaendelea kukua vizuri tu hata miili kuongezeka na kuanza kuonekana vizuri kwani walizaliwa wadogo sana. Huyo bibi yao akawa akiwapigania lishe, akiona tu muda wao wakula umefika, hata kama yupo jikoni, ataweka kila kitu pembeni, na kwenda kumuamsha Sabrina aanze kunyonyesha. Na kweli vitoto vikaonyesha kubadilika vizuri vikawa vikivutia sana. Swala la kunyolewa nywele zote hapo Jack alikataa kabisa. Akataka wakatwe tu ncha za juu wasibakishwe upara. Ikabidi mama Sabina akubaliane naye. Nywele zenyewe zilikuwa zikiota kama uyoga. Vichwa vilijaa nywele nyingi, nyeusi zilizojiviringa. Vimidomo vya pinki kama Tino. Wakaendelea kukua watoto wasio walizi kabisa. Ukiwasahau nao hutawasikia wakilia. Kimya hata wakitoka usingizini, utawakuta tu macho, wametulia. Hilo likampumzisha Sabrina.

Angalau kwa mara ya kwanza Sabrina naye akaanza kuongezeka mwili kwa kula vizuri na kupumzika. Mama yake alikuwa akimsisitiza awe anakula mara kwa mara sababu ya kunyonyesha. Mwili wa umama wa Sabrina ukaanza. Kwa mara ya kwanza maishani, Sabrina akawa mtu wa kula kulala na kunyonyesha tu. Akapendeza haswa. Akaanza kujazia sehemu za mwili wake. Uzazi ukawa mzuri. Akawa anamuona vile mama yake anavyojituma kwa moyo mmoja, baba yake akisaidia nje asiamini Mungu alivyomkumbuka na kumrejeshea hao watu wa muhimu kwake. Na yeye akabaki akimshukuru Mungu kwa hao watu alioruhusu wamzunguke kwa wakati huo.

Mwezi ukaisha likizo yake nayo ikaisha Jack akarudi kazini watoto wakiwa wameshachukua sura za tofauti. Wamekomaa japo walizidi kuonekana na asili ya kizungu kabisa. Lakini mapenzi ya Jack hayakuwahi kubadilika. Akitoka kazini, yeye na watoto tu. Imani naye akarudi kusaidia kazi wakati Jack akiwa kazini, basi anafika hapo kumsaidia mama Sabina kazi atakazompangia. Akawa anakuja asubuhi mpaka mchana. Mama Sabrina anampangia kazi, akimaliza zaidi usafi wa nyumba, anaondoka. Sabina naye alikwenda kuwatembelea. Alikaa siku mbili tu, akarudi kazini. Sabrina akakazana na kunyonyesha. 

Sabrina akakazana na kunyonyesha. “Hivyo unavyokazana, watakuwa haraka sana.” Mama yake akamsifia. Sabrina hakuwa mvivu wa kunyonyesha. Si mchana, si usiku wanae wakiamka tu, anawanyonyesha. Na alipenda wote wanyonye kifuani si kwa kutumia chupa akihisi anaweza asiwe msafi wa kusafisha chupa ipasavyo. Na akamwambia mama yake maadamu yupo tu nyumbani, ni bora wakiwa wadogo vile wanyonye tu. Basi wakiamka kwa pamoja atatumia mto aliopewa kwenye baby shower yake, atawapanga hapo, wanaanza kumnyonya mama yao wote kwa pamoja mpaka washibe.

Walipofikisha miezi mitatu hapo Jack ndio akawa kama amechanganyikiwa na hao watoto. Shingo zilishakomaa, wakilala na tumbo wanaweza kunyanyua shingo, basi kama hatalala nao chini kabisa sakafuni chumbani kwao ambako kulitandikwa kapeti, basi utamkuta Jack kitandani akicheza nao na kuzungumza nao kama mtu mzima. Na walishaanza kucheka kwa sauti, hapo usingemkuta Jack kwenye simu. “Mgeni akija hapa, hajui watoto ni wapi, na baba ni yupi!” Sabrina alikuwa akisema kila wakati. Jack hatajali ataendelea kucheza nao tu. Aliwaita kwa majina yao kila wakati akitaka wafanye hiki na kile. Na Mungu akawa upande wao, hawakuwa wakiugua. Ilimradi washibe tu, basi.

Mama yao alikuwa akiwavalisha vizuri sana. Kila wakati watoto hao ni wasafi na riboni yenye uwa kichwani. Jack alikuwa na kazi ya kupiga picha mchana na usiku. Akirudi Jack kutoka kazini, hao watoto wakisikia tu sauti yake, wote vichwa juu wakimtafuta. “Mtoto mwenzao karudi.” Sabrina alikuwa akimsengenya. Wakiwa na miezi mitatu tu, waliweza kumjua baba yao na sauti yake. Walipofikisha miezi minne, wazazi wakaondoka hapo, na kurudi nyumbani kwao. Wakawaacha watoto wamechangamka kabisa.

Mapenzi kati ya Jack na Sabrina yakazidi. Usiku nyumba wanaachiwa wao wawili tu na watoto tu. Hakuna Emma, wala wazazi. Imani anayekuja asubuhi kusaidia kazi akindoka mchana anabaki Sabrina akimsubiria Jack. Jack akitoka kazini, anarudi nyumbani kucheza na watoto, anakwenda kwenye mambo ya chama, akirudi watoto tena mpaka walale wanabaki na Sabrina, mapenzi ya haja yanaanza. Wataridhishana hapo, ndipo kulala. Mida ya asubuhi ambayo Imani anakua nyumbani, ndipo na yeye Sabrina alikuwa akitoka kwenda kwenye shuguli za chama. Mpaka muda huo watoto hao walikuwa hawajatolewa nje zaidi ya kliniki tu.

Sabrina alibadilika, akanona, umbile la kimama likawa zuri kwake. Mikono ya Jack ikawa haiishi mwilini kwake akimtaka mkewe. Walikuwa na utulivu wa namna yake hapo kwao. Hawakuwahi kumzungumzia mama Msindai, ila alikuwa akipata salamu kutoka kwa mzee Msindai. Wengine wote kasoro Jena, walikuwa wakimpigia simu Sabrina mwenyewe kumsalimia na kumjulia hali ya watoto.

Baada ya mwezi mmoja kuondoka wazazi, wanae wakiwa na miezi mitano na siku kadhaa, Sabrina akagundua hajapata siku zake week moja ilishapita ambayo alitakiwa kupata siku zake. Wasiwasi ukamwingia, lakini akaona atulie. Siku 15 zikapita, hamna kitu. Akaona ampigie simu mama yake. “Mwenzio sipati siku zangu.” Mama yake akaanza kucheka. “Usinicheke bwana mama!” “Wewe si nilikwambia utumie uzazi wa mpango, ukawa mbishi unasema ni mjuzi sana wa kuhesabu! Sasa umeruka kidole?” Ikabidi Sabrina acheke. “Kwa hiyo nimeruka namba?” “Ndio useme sasa.” Sabrina akazidi kucheka. “Ila wanangu bado wadogo mama! Kuja kuongeza mtoto wa tatu sasa hivi!” “Sasa hayo unayalalamikia sasa hivi, wakati mimi kila siku nilikuwa nikikwambia hapo Sabrina? Twende mwanangu ukawekwe kitanzi, ubishi. Basi jua watatu anakuja.” Sabrina akacheka na kukata simu. Akawaangalia wanae. “Sasa mnacheka nini na nyinyi? Hayawahusu. Waone.” Watoto wakazidi kucheka. “Mmetumwa na bibi yenu nyinyi, wala sio bure.” Sabrina akaendelea kuzungumza na wanae.

Pendo na Willy.

Wasimamizi wa harusi ya Jack & Sabrina.

P

endo akaamua kuamini pamoja na Sabrina. Maana Sabrina hakuacha kumwambia yeye bado anamuamini Mungu juu ya mtoto kwa niaba yake. Alipomuona Sabrina hakati tamaa ndipo na yeye akaamua kuchukua hatua ya kutafuta tena mtoto kwa upya kabisa. Kazi yake ilikuwa ikimchukulia muda mwingi sana na daktari alimshauri akiwa anatafuta mtoto, basi asiwe kwenye mazingira ya kum stress. Wawe kwenye mazingira matulivu. Waende hata sehemu kwa mapumziko kwa muda huo. Akamuomba Willy tena kwa upya. Lakini akamuona Willy anakuwa mzito sana. Swala lakuomba likizo pamoja nalo likawa lakumbembeleza mno. “Naomba usinikatie tamaa Willy! Naomba tujaribu mara ya mwisho. Ikishindikana safari hii basi.” Pendo akabembeleza sana na ikawa hiyo ndio ajenda pekee, mpaka Willy akakubali kuchukua likizo. Hakumwambia mambo mengi juu ya wanachoamini  na Sabrina ili asimchoshe, halafu akakataa, maana swala la kutafuta mtoto lilishakuwa la miaka mingi tena la shida.

Alipokubali tu, Pendo akaandika barua ya kuomba likizo kutokana na siku zake ambazo angeshika mimba. Akaanza kumeza dawa za kupevusha mayai tena kwa ajili ya watoto mapacha. Akafuata masharti tena bila kumwambia mtu yeyote. Hata marafiki walishachoka. Alizinunua hizo dawa kimya kimya na kuzinywa akitegeshea siku zake za kupevuka yai wawe mapumzikoni. Siku zilipokaribia akiwa anatumia hizo dawa yeye akaanza likizo, kwa makubaliano siku inayofuata ndipo Willy naye aanze.

Aliondoka kwenda kazini kama kawaida, akamuacha Pendo nyumbani akijiandaa na safari. Alikwenda kutengenezwa saluni karibu siku nzima. Pendo akafanyiwa waxing mwili mzima ili tu kumfurahisha mumewe huko mapumzikoni. Akatengeneza kucha, na kwa kuwa kwa asili Pendo alikuwa mzuri wa sura na umbile, akapendeza haswa. Akarudi nyumbani mida ya saa kumi na mbili jioni akitarajia kumkuta Willy, lakini hakuwepo. Akampigia simu mara kadhaa, hakupokea. Ila akamtumia ujumbe, ‘nitakupigia baadaye kidogo’. Pendo akakunja uso. Akaweka simu pembeni na kuendelea na shuguli zake.

Usiku wa saa nne ndipo Willy akarudi. Pendo yupo sebuleni akimsubiria. “Kwema? Umenitia wasiwasi.” “Nilikuwa nyumbani. Hali ya mama sio nzuri, tunafikiria kumpeleka India.” Pendo akajua tayari mipango imeshaharibika. “Vipi yule daktari wake aliyekuwa akimuona hapa?” “Hata yeye ameshauri kama uwezo upo, apelekwe India.” Pendo hakufurahia jinsi alivyojibu. Akaona atulie. “Chakula?” Akauliza tena Pendo. “Nilishakula. Nimechoka, nataka tu kulala.” Willy akapitiliza chumbani. Pendo akabaki akifikiria, kama aulizie swala la safari au anyamaze.

Akamfuata chumbani, akamkuta anaoga. Akasubiri kitandani. Akatoka. “Kwa hiyo mipango inakuaje sasa?” Pendo akauliza taratibu tu. “Unatania au unamaanisha Pendo? Au hujaelewa kuwa mama amezidiwa?” Pendo akatulia. “Unawezaje kufikiria safari ya kwenda kupumzika wakati mama ni mgonjwa? Najua hamkuwa kwenye maelewano, lakini ni mama yangu mimi. Onyesha hata utu kidogo basi!” Pendo akashangaa sana. “Naomba unisahihishe Willy. Lakini ninavyokuona, ni kama unatafuta sababu ya kugombana na mimi!” “Kwa hiyo..” “No, subiri Willy. Naona hiyo hali imekuanza hata kabla ya leo. Ni nini kinaendelea?” “Wewe uniambie.” Pendo akakunja uso.

“Mama amekuwa akiumwa muda mrefu tu. Swala la kumpeleka India sio la leo. Sisi ni wafanyakazi wa kuajiriwa. Kosa langu ni lipi leo kuuliza mipangilio wakati ukijua wazi nimechukua likizo twende mapumzikoni?” “Kwa hiyo sasa unataka kuniambia ugonjwa wa mama ndio umeingilia kushika mimba kwako?” Moyo wa Pendo ukapasuka, akafungua macho yote wazi. “Tumepoteza pesa kiasi gani na muda kwa ajili ya swala la mtoto? Ugumu wa wewe wakutoweza kusubiri ili mama apone ni upi? Kipi kipya tutafanya safari hii ambacho kinakuhakikishia tutapata mtoto?” Pendo akashindwa kujibu kabisa. Kwa mara ya kwanza Willy akaongea moyo wake bila kuficha wala huruma kwa mkewe. Pendo akabaki akimtizama jinsi Willy anavyoendelea kugomba. Aliongea maneno ya hasira mpaka akachoka.  Akalala.

Pendo alikuwa ameumia sana. Alijua watu wanamsema, lakini sio Willy wake ambaye alikuwa akimpa moyo wakati wote. “Mpaka Willy amechoka!” Akaanza kulia Pendo pale sebuleni alipokuwa amehamia. Akalia. Akajiambia kwa uchungu ule muda ule akimpigia simu mama yake, atamuumiza. Akikaa pale kesho yake bila kwenda kazini, akajiambia atachanganyikiwa, akamtumia ujumbe bosi wake kumuomba arudi kazini tu. ‘Sawa.’ Hapo hapo bosi wake akajibu.

Kesho yake akaenda kazini akiwa amepoteza pesa ya nauli ya tiketi za ndege alizokuwa amekata Pendo kwa pesa yake, kuelekea nje ya nchi kwa mapumziko. Alitaka waende mbali kabisa na Tanzania ili akatulie na Willy akijaribu kushika mimba. Asubuhi hiyo waliondoka bila hata kuongeleshana. Jioni alirudi nyumbani, akakuta msichana wa kazi alishapika hakuingia hata jikoni. Akaoga na kulala. Kwenye saa nne tena ndipo Willy akarudi. Pendo akanyamaza. Hata hakugeuka. Kesho yake ikawa hivyo hivyo.

Akiwa kazini Sabrina akamtumia picha za wanae na ujumbe. ‘Wanao wamekumiss.’ “Oooh noo!” Pendo akakumbuka amemeza dawa za ujauzito. Kadiri wanavyozidi kununiana na Willy, ndivyo siku za kushika mimba zinavyozidi kuisha na ni hasara kwake. Hapo hapo ikajiambia lazima ajirudi kwa Willy ili angalau usiku huo wafanye tu tendo la ndoa, lasivyo jitihada za mwezi huo nazo itakuwa bure. Akamtumia ujumbe, ‘Pole kuuguza mpenzi wangu. Najua upo kwenye kipindi kigumu. Namuombea mama na wewe pia. Mungu awafariji familia nzima. Na ninaamini Mungu atafanya njia. Na mimi nipo na wewe. Niambie tu chakufanya. Na kama kuna mchango, na mimi unihesabu mpenzi.’ Akautuma ule ujumbe akabaki akisubiria.

Kwa Sabrina.

Akashindwa kusubiri. Akampigia simu Sabrina hapohapo. “Ili hao watoto waendelee kuwa na antie, lazima uniombee sasa hivi. Nachanganyikiwa Sabrina.” “Ni nini tena da Pendo?” Sabrina akauliza kwa kujali. “Mimi sielewi vita vinaanzia wapi, lakini Willy amenibadilikia Sabrina, hutaamini. Mkali, na wazi ameniambia amechoka.” Pendo akamsimulia mkasa mzima. “Sasa na mimi nyumbani kwao hawanipendi kabisa. Hata kwenda huko imeshakuwa tatizo, mpaka mama akashauri nisiwe nakwenda. Maneno ya kunikashifu ya waziwazi hayajawahi kuisha.” “Kutoka kwa nani sasa?” “Zaidi mama Ngoi mwenyewe na dada zake wote. Baba yake yeye tatizo lake ni mtu wa wanawake mno. Huwa najitahidi kukaa naye mbali.” “Da Pendo!” Sabrina akashangaa.

“Sikutanii Sabrina. Nakwambia wewe tu kwa kuwa nimekuona unakifua chakubeba mambo, lakini huwezi amini yule mzee alishanitongoza.” “Haiwezekani dada!” Sabrina akazidi kushangaa. “Mungu wangu nishahidi. Kuna siku ndio alinichosha zaidi. Nilimkuta nyumbani peke yake, akaniambia kama Willy anashindwa kunizalisha, yeye anisaidie.” “Mungu wangu!” “Wewe acha tu. Sikuamini, na akafika umbali wa kuniambia kama naona shida kukutana naye hapa mjini, tusafiri naye. Si unajua mzee Ngoi anazo pesa?” “Nimesikia.”  “Basi pesa anazo kwa uhakika wala si ya kubabaisha. Akaniambia atanipa pesa yeyote ninayotaka, nitangulie, yeye atanifuata. Nikaondoka bila hata kumjibu, na wala sikumwambia mwanae, ndio ugumu wa kwenda kwao ukaongezeka mbali na maneno ya mama yake ambaye ndio mgonjwa. Willy anakaa huko mpaka usiku. Kesho ndio siku ya mwisho ya kushika mimba. Sitaki ahadi yakuniombea baadaye. Hapa nipo chooni. Wewe niombee sasahivi, angalau huyo mwanaume leo aniguse Sabrina.” Sabrina hakupoteza muda, akaanza maombi hapohapo kwenye simu, akimwita Mungu wa amani na aliyebariki ndoa yao amkumbuke Pendo. Akamaliza, Pendo akarudi kazini.

Ilipofika kwenye saa 9 jioni, Pendo akaona ujumbe kutoka kwa mumewe. ‘Nashukuru kujali. Nilikuwa busy kidogo nikishugulikia mambo ya mama tokea asubuhi. Nitakuona nyumbani.’ Pendo akajisikia kutokwa na machozi. ‘Umefikia pazuri?’ Pendo akatuma ujumbe mwingine. ‘Lipo tumaini. Nitakueleza vizuri ukija nyumbani. nimechoka, naona leo nitawahi kulala.’ ‘Sikujua kama umesharudi nyumbani!’ ‘Ndio nimeingia muda si mrefu.’ ‘Pole mpenzi wangu. Yatapita tu. Naamini na mama atapona.’ Pendo akatuma na huo ujumbe huku akikusanya vitu vyake arudi nyumbani haraka. ‘Amina. Na nashukuru.’ Ujumbe huo anasoma Pendo, yupo ndani ya gari yake tayari kurudi nyumbani. Njia nzima akirudia maombi ya Sabrina.

Alifika nyumbani, msichana wa kazi akamwambia mumewe alifika hapo, akala, na kuingia chumbani. Pendo aliingia chumbani, akamkuta mumewe amelala kama usiku wa saa saba. Simu ameweka pembeni, taulo kwenye kochi, wazi kuwa alishaoga ndio akalala, kuashiria amemaliza siku. Pendo aliumia sana. Kesho ndio ilikuwa mwisho. Hawezi kumuamsha. Atamwambia nini? Akakaa hapo chumbani kwenye kochi akimuomba Mungu mumewe aamke lakini wapi. Akaoga na kwenda kula. Mpaka saa tano usiku Willy alikuwa amelala kama mfu. Pendo akaamua kulala tu akiwa amekata tamaa kabisa.

Karibu kuna papambazuka, akasikia mumewe akimpapasa. Hakuamini. Akamgeuza bila hata romance, akamuinamisha nakuanza mapenzi. Akashangaa ile nguvu aliyokuwa nayo Willy, Pendo akatoa ushirikiano wote. Willy akafanya mapenzi na mkewe, akamaliza. “Daah! Samahani. Nahisi nilikuwa nikiota. Sikukusudia kuwa kama mnyama.” Pendo akacheka. “Hamna neno, japo nilishangaa kidogo.” “Sijakuumiza?” “Hapana. Nipo tu sawa.” Willy akamvuta vizuri, akamkumbatia na kurudi kulala. Pendo hakutaka hata kugeuka ili mbegu za mumewe zisije kutoka. Akajiegemeza vizuri hapo ubavuni, akamshukuru Mungu kwa machozi. “Asante kunikumbuka Mungu wangu.” Pendo akaendelea kutokwa na machozi ya furaha kana kwamba alichofanya safari hii ni cha tofauti. Alishakunywa aina hizo za dawa zaidi ya atakavyokumbuka. Alishategesha hizo mimba nje na ndani ya hicho kitanda chao zaidi ya atakavyosema. Wakichukua likizo na kwenda sehemu mbalimbali wakidhani watafanikiwa swala la mtoto bila mafanikio. Lakini alfajiri hiyo hakujali kama mimba itashika au la, lakini kile kitendo chakushikwa na Willy, akakifurahia kwa ajabu.

Alikuja kuamshwa na alarm ya saa 11:30 asubuhi. Akakimbie kwenye machine kidogo ndipo arudi kuoga awahi kazini. Akakumbuka ujauzito. Akajiambia asubuhi hiyo asikimbie asije kuharibu mambo. Akazima alarm na kuelekea bafuni kuoga. Wakati anaoga, Willy akaingia. Bila maneno mengi akamkumbatia na kuanza romance. Pendo alifurahia, asiamini. Willy hakuonyesha haraka, akamtoa mkewe hapo, wakahamia kitandani vilevile na maji. Pendo alifurahia hayo mapenzi. Willy alionekana kutulia na kumfurahia mkewe mwanzo mpaka mwisho, akimnung’unisha mkewe hapo kwa penzi la kituo, mwenyewe alifurahia kuwa alifanya kazi nzuri asubuhi hiyo. Pendo akaondoka kwenda kazini, akamuacha mumewe akizungumza na dada yake.

Safari ya mama Ngoi nchini India.

B

aada ya majuma mawili na siku tatu, maandalizi ya safari ya kwenda nchini India kwa matibabu ya mama Ngoi yakakamilika. Dada yake mkubwa Willy ndiye aliyekuwa akimsindikiza mama yao nchini India kwa matibabu. Siku moja kabla, Pendo alimuomba Willy amsubiri ili waongozane nyumbani kwao akamuage huyo mama. Alifika pale akakuta kuna chakula cha pamoja kwa ndugu na marafiki wa karibu, kama tafrija yakumuaga huyo mama kwa maombi. Pendo aliumia sana kuona wameshindwa hata kumkaribisha kiunafiki tu! Inamaana asingeamua yeye kwenda ndio asingejua yote hayo! Lakini akaona anyamazie tu. Watu walikuwa wengi tu hapo na hekaheka nyingi. Kila alipotaka kusaidia ni kama alikatazwa. Akaamua ajitulize tu. Hata siku alipokwenda kumuona huyo mama hospitalini alipokwenda kliniki yake ya kawaida tu, kwa kuwa ilikuwa mjini, Pendo akajua wapo hapo, akatoka kazini na kwenda kumuona. Alijuta. Walimpuuza kwa hali ya juu ni kama waliokuwa wakimuuliza amefuata nini hapo! Willy hakuwepo, aliwakuta dada zake Willy, na marafiki zao. Alipoona wanampuuza na yule mama hataki hata kumtizama, Pendo akaaga na kuondoka. Walikaa hapo mpaka mwisho, wakaaga na kuondoka na mumewe.

Willy alikuwa akiwasiliana na dada yake huko nchini India kujua maendeleo ya mama yao. Pendo naye akawa akiuliza kila alipoona Willy ametulia. “Operation ya kwanza imekwenda vizuri. Wameweza kutoa uvimbe wa kwanza, huo wa pili wameamua kumpa muda kidogo. Upo karibu sana na ubongo.” “Pole babe. Mungu atamponya tu.” Kwa sauti yake tulivu Pendo akamfariji wakati hakuwa hata akijua kama huyo mama alifanyiwa upasuaji. Akaona anyamaze tu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ilikuwa siku ya jumatano ya saa 9 usiku nchini Tanzania, siku ya 13 tokea kuondoka kwa mama yake Willy nchini, Willy na mkewe wakiwa wamelala, wakati simu kutoka nchini India kwa dada yake mkubwa Willy aliyekuwa na mgonjwa ilipoingia. Willy akakaa kwa haraka na kupokea. Alichoweza kusikia Pendo ni kilio cha uchungu sana. Akajua mambo si mazuri. Na yeye akakaa. “Haiwezekani jamani! Mbona nimezungumza na mama kabla sijalala na alisikika mzima kabisa!” Yule dada akazungumza akieleza hata madaktari wameshangaa. “Hakuzidiwa wala kuonyesha mabadiliko yeyote mabaya. Tena walikuwa wakisema wanashangaa jinsi anavyopona kwa haraka na hata wakafikiria kumfanyia upasuaji kwa mara ya pili jumatatu ijayo! Tumeshangaa muda mfupi uliopita mashine zinapiga kelele. Nesi kuingia, akaita madaktari kumsaidia. Wamehangaika hapo, lakini ikashindikana. Mama ametuacha Willy.” Willy akaanza kulia hapo, Pendo akimbembeleza.

“Itabidi kuwataarifu wengine mpenzi wangu. Pole.” Hapo Willy ndio akaanza kusambaza habari za msiba, na yeye Pendo akamtarifu bosi wake na wazazi wake. Kufika saa tatu asubuhi wakawa wameshaingia nyumbani kwa kina Willy, Masaki. Saa nne asubuhi ndugu wote wa pale mjini na marafiki wa karibu wakawa wamefika hapo msibani. Saa sita mchana kukawa kumeshawekwa turubai nje na viti, watu wa catering walishakuwa wamepigiwa simu na ndugu wa huyo mama, ikawa hekaheka tupu na vilio vya hapa na pale.

Kufika jioni marafiki wa karibu waliokuwa wapo kazini nao pia wakawa wamefika hapo. Mambo yakaendeshwa kitajiri, na fahari. Pesa ya huyo mzee ikafanya kazi kwenye msiba huo. Walikuwepo watu maalumu wa chakula na ndio waliogawa vyakula na vinywaji. Na ndio haohao waliokuwa wakikusanya sahani zao chafu. Kazi kubwa ya msibani ikawa imepunguzwa. Wafanyakazi wa watoto wake huyo mama wakisaidiana na wafanyakazi wa hapo ndani kwa mama Ngoi wao wakashika usafi wa nyumba. Kwa hiyo kazi iliyokuwa imebaki hapo kwa mtu kama Pendo ambaye hata mawifi zake hawakuwa wakimtaka aguse vitu vya mama yao ilikuwa kukaa kama wageni wengine. Kila alichoshika aliambiwa aache tu, na yeye akatafuta mahali akahema.

Akamtumia ujumbe Sabrina kumtaarifu  huo msiba. Sabrina ndiye mtu wake wa karibu aliyebakia sababu ya kuombeana.  Sabrina akampigia simu. “Tutakuja kwenye kuzika da Pendo. Pole sana. Nitamwambia na Jack.” Akamfariji hapo, akamshauri awapigie simu kina Jacinta, Joy na Jena waende wawe naye asikae hapo peke yake. Akaona jambo zuri. Akawatumia ujumbe wote. Ilipofika saa mbili na nusu, wote wakawa wamefika hapo mpaka mama Msindai na mama yake mzazi Pendo. Angalau akapata watu wakumpa pole na yeye na kuzungumza naye. Wakamzunguka hapo, wakatengeneza kundi lao.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Jumamapili ndio mwili ulikuwa ukiingia, mazishi ilikuwa siku ya jumatano. Sabrina, Jack na watoto wao wote wawili wakatua jijini Dar siku ya jumamosi. Pendo akaenda kuwapokea. Walikwenda nyumbani kwa Pendo, Jack akaja kuchukuliwa na kaka yake, wakaenda naye msibani. Pendo akabaki na Sabrina hapo nyumbani wakimsubiria mama yake Sabrina aje akae na wajukuu zake, wao waende msibani. Baada ya muda kidogo mama yake na Sabina wakaingia. “Wewe Sabrina! Hao wanao wanazidi kuwa warembo!” Sabina akashangaa sana. Ungetaka kuwashika watoto wa Sabrina. Walikuwa wazuri mno. “Wana kazi yakucheka tu kama baba yao.” “Mmemuacha baba yao?” “Subutu! Jack hajiwezi bila hao watoto. Hapa ilikuwa shida kuwaacha mpaka kaka yake alimwambia anamuacha ndio akaondoka. Ukimkuta amekaa nao hapo chini, utafikiri na yeye ni pacha mwenzao!” Wakaanza kucheka.

“Unafikiri natania? Yaani utafikiri nina watoto watatu humo ndani jamani! Anajifunza kutambaa nao! Hamna mnaloongea na Jack akiwa ameshika hawa watoto mkaelewana. Bora wawe wamelala, ukimwambia jambo ndio anaelewa.” “Sasa na wa nne ndio anakuja.” Mama yake akamfanya Sabrina azidi kucheka. “Wewe Sabrina ni mjamzito tena!” “Mwaya mama sijui yukoje! Nimemwambia asiseme.” “Wewe si ulisema hurudi tena leba mpaka miaka saba!?” Sabina akashangaa sana wote wakacheka.

“Wala mimi sikupanga kushika mimba.” “Ulitaka sana. Mtoto nilimbembeleza huyu! Namwambia Sabrina mwanangu twende ukawekwe kitanzi au tumia dawa. Akawa mbishi. Ooh, ‘mimi mzuri sana wakuhesabu. Wala sina sababu ya kutumia njia ya uzazi wa mpango’. Nashangaa ananipigia simu eti, ‘Mama, mbona sipati siku zangu?’ Nikamwambia...” “Eti akanijibu labda niliruka kidole kimoja wakati wakuhesabu.” Wote wakazidi kucheka.

“Ndio miezi mingapi sasa?” Sabina akauliza. “Naenda wa tatu. Hivi hata Jack hajui.” “Haiwezekani Sabrina!?” Wote wakashangaa. “Kweli tena. Kuna mambo yangu nafanya sasa hivi. Namjua Jack. Nikimwambia tu, tutaanza kufuatana nyuma, nitakosa uhuru. Nataka nimalize kila kitu, vikikaa sawa, ndipo nimwambie, tuanze tena kulea mimba kwa mara ya pili.” Wote wakashangaa. “Nashauri umwambie Sabrina.” Pendo akasisitiza. “Sina nitakalofanya da Pendo. Mimi namjua Jack. Au muulize mama hali aliyonikuta nayo kule Singida.” “Utafikiri mgonjwa mahututi.” Akamalizia mama yake Sabina wakacheka. “Sasa ndio hiyo hali itazidi mara mbili akijua ni mjamzito. Mimba ya hawa watoto, ilikuwa mpaka kero. Atataka kujua upo wapi na unafanya nini. Na kiwe kitu anachoona yeye si hatarishi. Mpaka nikamuomba daktari azungumze naye na kumwambia natakiwa kutembea. Maana nilifika hatua, akinisikia nimetoka hapo ndani, utamuonea huruma. Anasema mimba itatoka.” Wakacheka.

“Kweli. Acheni tu nimalize project yangu.” “Ni nini?” Akauliza Sabina. “Kuna project ya chama nafanya na wanawake huko na huku. Naona nimepata uungwaji mkono mzuri! Kaka yake Jack amenitafutia watu wakutufadhili. Ikikamilika hiyo, mume wangu akaikubali na kuifungua ramsi, hapo nakaa nyumbani bila shida. Lakini sio sasa hivi. Atanisumbua sana Jack. Mwache acheze tu na hawa hawa wawili.” Wakacheka. “Na ukimuachia watoto hapo nyumbani siku za jumamosi ambazo haendi kazini, ukirudi unaweza kutamani kulia. Unafungua mlango, unakaribishwa na toi mlangoni. Yeye amelala kwenye sehemu ya watoto na wanae, wanacheza hawana habari. Watoto wanatambaa, na yeye nahisi amesahau kutembea. Anatambaa kama watoto!” Wakazidi kucheka. “Nimebakisha kidogo tu nimalize mambo yangu, nitamwambia tu.” Wakazungumza kidogo, Sabina akawa akiwapiga picha hao watoto wa mdogo wake mpaka akaridhika. Wakamuacha mama yao na hao watoto, wao watatu wakaondoka kwenda msibani.

“Nimefurahi umekuja Sabrina! Nilishapatwa na hamu na wewe.” Sabrina akawa anacheka wakiwa njiani kuelekea msibani. “Nipo hapa mpaka mzike.” “Bora.” Wakaendelea kuzungumza mpaka sibani.

Msibani.

W

alipoingia ndani getini, Pendo akawaambia waende wakakae wanapokuwa wanakaa na ndugu zake, haswa wanawake. Wakaongozana. “Naona wewe na mumeo mmependeza!” Jacinta akamuwahi, Sabrina akacheka. “Shikamoo wifi.” “Marahaba Sabrina, watoto wako wapi?” “Nimewaacha na mama. Nisingeweza kuja nao hapa, wapo kwenye kutambaa, ningekuja nao hapa, pasingetosha.” Wakacheka. “Jack anakazi yakunitumia video zao naona kila week.” “Basi utakuwa umeona hiyo fujo. Hapo kwa da Pendo imebidi kuondoa meza zote ili wapate uwanja wa kutambaa.” “Hawajachoka na safari?” “Walilala njia nzima, wameamkia nyumbani kwa da Pendo.” Wakacheka, ndipo Sabrina akaendelea kusalimia wengine, asijue mama yake mkwe alikuwa ameinamia simu yake pembeni, akisikiliza tu.

Akawasalimia wote kwa kuwashika mkono, wakavuta kiti pembeni. “Naona Singida sio pabaya Sabrina.” Joy akamtania. “Nakwambia uje, uniletee Claire wangu aone watoto, unaniringia. Singida mlenda unang’arisha.” Joy akacheka sana. “Shauri yako.” “Si ungetubebea na sisi?” “Mlenda wa Singida, uulie Singida ndio unajibu.” Sabrina akaongea kwa sauti ya chini na kumfanya Joy azidi kucheka. “Sabrina wewe mtundu.” Stori zikaanza hapo. Wakajikuta wameungana, Joy, Jacinta, Jena, Sabrina, Sabina, Pendo, dada yake Pendo, Nancy, na marafiki zao. Mama Msindai na mama yake Pendo pamoja na wa mama wengine wakaendelea kivyao lakini kundi la pembeni yao tu. Jena akakaa kidogo, akaondoka bila kuongea chochote na Sabrina ila salamu tu.

Usiku wakaondoka kurudi nyumbani, kesho yake tena wakarudi msibani. Mama Sabina ndiye akawa anabaki na wajukuu zake muda wote. Huko msibani Sabrina akawa akiongozana na Pendo kila mahali mpaka chooni. Ilipofika siku ya jumapili mchana msafara ukaelekea uwanja wa ndege kupokea mwili wa marehemu ukaanza. Kukajaa vilio huko uwanja wa ndege, wakatoka tena huko kurudi nyumbani wakiwa na mwili wa mama Ngoi.

Msiba ukaanza rasmi. Jumatatu na jumanne ikawa maombolezo hapo. Jumatano wakaaga mwili wa marehemu nyumbani, ibada kanisani, mama Ngoi akapelekwa kwenye safari yake ya mwisho kwenye makaburi ya Kinodnoni. Willy na ndugu zake, kaka na dada zake walikuwa wakilia sana, hakika ungewahurumia. Maana huyo mama ndiye ni kama alikuwa ameshika familia yake wala si baba. Mzee Ngoi alikuwa mkorofi ambaye hafikiki hata na wanae. Kwa hiyo swala la kwenda nyumbani ilikuwa ni kwa sababu ya mama, na ndiye aliyekuwa akiendesha hata maisha yya wanae kwa ushauri na msaada kifedha. Kwahiyo hapo walilizwa na mengi. Ni kama nguzo yao ndio ilikuwa imeondoka. Wakazika, watu wakatawanyika palepale makaburini. Ndugu wa karibu wa familia tu ndio wakawa wanarudi nyumbani kwa Ngoi kama kumaliza msiba. Sabrina peke yake ndiye aliyerudi na Pendo nyumbani kwa wakwe zake. Hata wazazi wake Pendo waliagana makaburini.

Kikao Cha Familia kilichoibua mapya.

W

akaingia sebuleni, baba yao akapata nafasi yakushukuru wote kwa kushiriki. Dada mkubwa aliyekuwa na mama yao nchini India naye akapata nafasi ya kusimulia tena kwa kifupi yaliyotokea huko. “Lakini mama alisema kwa kauli yake mwenyewe, ikitokea chochote kinampata, wakati nagawa vitu vyake, lazima wifi Zelda apewe nafasi ya pekee achukue kile anachoona kitamfaa yeye na watoto wake ili ije kuwa kumbukumbu kwa wajukuu zake.” Pendo akashangaa huyo wifi anayezungumziwa hapo ni yupi! Wake za kaka yake Willy aliwafahamu vizuri tu. Willy ndio kijana wa mama Ngoi mdogo wa mwisho, yeye ndio mke, mtoto wa mwisho ni wa kike. Pendo akawa hajaelewa.

“Mama amekufa akiwa anatamani sana kumuona mjukuu wake huyu anayekuja. Lakini Mungu ame...” Wakaanza tena kulia na kumchanganya Pendo zaidi. Katika watoto wa kike wa huyo mama hapakuwa na mjamzito na wake za watoto wake wa kiume pia hapakuwa na mjamzito! Ila akamuona dada mmoja ambaye alishamuona hata na huyo mama hospitalini alipokwenda kumuona, na hapo yupo ndiye pekee mjamzito. Akamtizama vizuri, kweli tumbo lilikuwa kubwa ila hakuwa akimfahamu kwa undani zaidi ya kumuona tu na marehemu mama mkwe wake! Alikuwa akilia na dada zake Willy wakaonekana kumpa sana yeye pole. Hapo sasa ikabidi kumtizama kwa makini akajua sasa yeye ndiye huyo wifi wanayemzungumzia, swali mume ni nani!?

Baada ya vilio vya hapa na pale mwishowe wakatulia tena. Lakini alishangaa wake za kaka yao Willy hao wawili wao wamenyamaza kimya, hawalii wala hawazungumzi wapo kama wanahasira. “Kwa hiyo nafikiria, hiyo siku ya 40 ambapo tutatoka kusoma misa ya mama, wote turudi hapa, tuje tugawane vitu vya mama.” Akamalizia huyo dada mkubwa kabisa ambaye ndiye mtoto wa kwanza wa hiyo familia. “Labda mimi niulize. Katika hiyo siku, nani anaruhusiwa kurudi kuja kuchagua hivyo vitu? Maana wajukuu aliyetambuliwa hapa na bibi yao ni huyo wa Willy ambaye bado hajazaliwa. Sasa ndio nauliza hiyo siku ya 40 baada ya misa hawa wajukuu wengine tunarudi nao hapa, au tuwarudishe nyumbani wasije kuanza maswali yasiyo na majibu?” Mke wa kaka yao mkubwa, akauliza ki ukali kidogo. Sabrina akakunja uso, Pendo akaanza kutetemeka. “Sijaelewa?” Akaongea Pendo kwa sauti yake ya chini iliyojaa hofu.

“Sasa tunamjibu nani na kumuacha nani? Maana wote mnauliza maswali kwa pamoja!” “Hakuna swali gumu hapa, Stella. Wewe ndiye umeanza kutoa maelekezo. Una...” “Mbona jazba mama?” Mumewe akamuuliza kwa upole. “Lazima jazba shemeji. Mnachotaka kufanya hapa sio sawa. Pendo ni mke halali wa Willy. Halafu na sisi ni wake zenu na tumezaa na nyinyi. Iweje leo Zelda aliyekuja juzi tu hapa ndio apewe heshima zote, na kutangazwa hapa kwa kishindo kama sisi tunashida na mali bwana!” Akapokea mke wa kaka wa pili ambaye ni mtoto wa tatu wa hiyo familia. Ugomvi ukaanza, na kutukanana. Nusura Stella dada mkubwa na wifi yake washikane, kupigana. Wanaume wakaingilia. Mke mwenzie, yaani wa mtoto wa tatu akawa mkali akitaka kuchangia kwenye huo ugomvi.

“Msitufanye sisi watoto wadogo hapa. Zelda, Zelda! Kwani anazaa ulimwengu!” “Mnakuwa kama sio wakristo nyinyi! Leo gafla Zelda amekuwa wa maana kuliko Pendo mke halali wa Willy! Acheni kutudhalilisha kwa kiasi hicho jamani!” Pendo alikuwa akitetemeka hajui hata amwangalie nani amuache nani! Mambo yalikuwa yakiendelea humo ndani ya familia, yeye hana taarifa! Mumewe ana mwanamke mjamzito, mimba kubwa kabisa, anafahamika mpaka ukweni, yeye hajui! Pendo akabaki amekufa ganzi. Sabrina akamshika mkono, wakabaki wakiwaangalia wake wenzake Pendo jinsi wanavyompigania, Pendo akiwa hajui chakusema. Hata Willy mwenyewe akashindwa kumtizama mtu usoni, akabaki ameinama.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kikulacho Ki Nguoni Mwako. Yamemfika Pendo. Akidhani Ipo Amani, Kumbe Uharibifu Umeingia Mpaka Ndani Ya Ndoa Yake.

Nini Kitaendelea Kwa Wapenzi Hao Wa Tokea Wadogo, Wakiwa Chuoni, Kama Jack Na Sabrina?

 Usikose Muendelezo.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment