Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 26. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 26.

 Kwa Sabrina & Jack!

Wakati wanaingia na Jacinta pamoja na Pendo na mumewe nao wakawa wanaaga. “Ngoja nikapike cha mchana na usiku. Mama ubakiwe na kazi ya kumlisha tu.” Pendo akaaga wakati anakusanya vitu. “Nashukuru sana mwanangu. Mungu akubariki kwa moyo wako wakujitoa kwa Sabrina.” “Amina mama.” Pendo akaitika kwa suati yake ya upendo kama jina lake. “Lakini unipigie kwanza Pendo. Unaweza kukuta mpaka umalize kupika, na sisi tumeruhusiwa.” “Sawa Jack.” “Nakushukuru sana Pendo. Asante sana. SANA.” Pendo akacheka. “Karibu Jack. Na mimi mnanihusu sana. Sasa hivi nyinyi ni jukumu langu.” Sabrina akajisikia vizuri, akafurahia hilo. “Asante da Pendo.” “Basi nitawaona baadaye. Popote mtakapokuwa, nitawaona.” Wakaaga na kuondoka Jack, akatoka kuwasindikiza.

Wakabakia wao tu watatu na watoto. Sabina akajua ndio wakati mzuri wakumuweka sawa Sabrina. Lakini Sabina akashindwa pakuanzia. Ni kama wote walishakuwa wakimuogopa sana Sabrina. Akatulia akifikiria pakumuanzia. Sabrina akamuona mama yake vile anavyohangaika na wajukuu. “Nakushukuru mama yangu. Umenifaa kweli! Maana nilikuwa hata sijui jinsi yakuvishika hivyo vitoto na hivyo vitomvi vinavyoning’inia! Natamani tukakae wote mpaka watoto wachangamke kidogo!” Sabrina mwenyewe akaanza. “Kwani mama wewe unashida? Tena ingekuwa vizuri ukae na wajukuu wako mpaka hamu iishe.” Sabina akadakia kwa haraka sana. “Hamu ya wajukuu haiishi, Sabina mwanangu.” Mama Sabina akajibu huku akimuweka sawa mjukuu wake na kumbusu. “Kweli mama? Unaweza kukubali tukakae wote kwa muda?” Sabrina akahamasika kweli.

“Bila shida Sabrina mwanangu. Nikishindwa na hapa tena, basi nitakuwa sifai tena kuwa mama.” “Nakushukuru mama yangu. Basi ngoja Jack akirudi nitazungumza naye.” Hilo likamfurahisha sana Sabrina. Jack akarudi. “Vipi?” Akamsogelea na kumbusu. “Nipo sawa tu. Vipi wewe?” “Mimi natamani kutoka hapa. Nishachoka. Tena hivyo nikiwaona wote mpo sawa, sioni sababu yakukaa hapa. Naona wanawabana wanangu tu.” Sabrina akacheka. “Tena nataka kumuomba mama twende naye.” “Singida!” Jack akashituka. “Akanisaidie kidogo mpaka watoto wakue.” Sabina mama yake wakabaki wakisikiliza. “Wewe unataka kuniponza ukweni Sabrina.” Wote wakacheka. “Kweli tena huyu anataka kuniponza mapema, nipokonywe mke! Tumchukue mama, baba abaki na nani? Labda wakubali tuongozane wote.” Mama Sabina akatamani kuruka kwa furaha. “Sasa ugeni wote huo si mtalemewa?” Akajibaraguza mama Sabina. “Hata kidogo mama. Sabrina huyu ametengeneza kinyumba cha nje, amekitolea muundo mzuri, wala hamtambana mtu. Mtaishi kwa utulivu kabisa, labda muwe mnahofia majukumu yenu, lakini kwetu sisi milango ipo wazi. Tena naona mtamchangamsha Sabrina, nitakapoanza kazi.”

“Hakuna majukumu baba. Kuku aliokuwa akitusaidia kufuga Sabrina, walikufa kufa pamoja na ng’ombe nao wakaugua. Lilibaki dume moja, ndio hilo tunafanyia biashara ya kupandisha majike ya watu. Wakileta jike likapandwa, wanatulipa.” Sabrina akashituka sana mpaka akakaa akiwa na maumivu. “Mama! Kweli?” “Acha tu. Tumeishiwa kweli.” “Ng’ombe walipatwa na nini?” Sabrina akauliza kwa kuumia. Ndiye aliyekuwa akiwatunza. “Magonjwa. Wakafa mmoja baada ya mwingine. Ndio hivyo. Na kuku nao walikufa, na kuuzika ikawa shida, tukaona tusiendelee kuagiza sababu ya hasara.” “Poleni mama.” Sabrina akaumia sana.

“Lakini mama, hawa wakiruhusiwa tu, tunaondoka jijini. Na kama alivyosema jana daktari, wakiendelea vizuri, leo wataruhusiwa. Mida hii ya saa 4 watapita. Ndipo tutajua.” “Kwa hiyo mkiruhusiwa leo, mnaondoka leoleo?” Sabina akauliza. “Inategemea. Kama ni leo asubuhi na nikapata nafasi ya ndege, tunaondoka leo. Kama tukichelewa, Mungu akipenda kesho asubuhi tunaondoka.” Sabrina akahisi kuna jambo linaloendelea ndio maana kuna uharaka wa kuondoka. Kwa kutomuona mama Msindai hapo mpaka muda huo na mumewe, akajua bado mambo si shwari. Lakini akamshukuru Mungu Jack yupo upande wake, akajiambia hilo linatosha. Moyoni akatulia. Wakatulia.

“Kama mama mmekaribishwa, labda upate muda wa kwenda kuzungumza na baba, mjiandae ndipo muwafuate Singida. Si ni sawa Sabrina? Au unasemaje Jack? Kwa hakika mtahitaji msaada.” Sabina akatoa wazo. “Kabisa. Muda na wakati wowote watakapokuwa tayari, wanakaribishwa.” Akajibu Jack kwa jumla tu, akamsogelea Sabrina. “Vipi, unajisikiaje?” “Vizuri, ila nina hamu ya kulala muda mrefu bila kuamka.” Jack akamcheka. “Nahisi hapa kazi ndio imeanza mama. Starehe zile zakulala mpaka asubuhi alam ituamshe, imeisha.” Wakacheka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Daktari akaingia na Mzee Msindai. Sabrina na Jack wakashituka. Wakamsalimia mzee Msindai kwanza. “Kwema?” “Kwema kabisa. Waliniambia wanataka kuwaruhusu leo, nikasema lazima niwepo kuangalia watoto ili mkiruhusiwa, tuwe na amani kuwa wapo sawa.” Akamsogelea Sabrina. “Ulilala vizuri?” “Hapakuwa na matatizo.” “Acha niangalie wajukuu wakati wewe ukimsubiria daktari wa wakina mama.” Mzee Msindai na daktari wa watoto wakahamia kwa wajukuu. Wakawatoa nguo zote kasoro diaper na kuanza vipimo upya. Wakaangalia kila kitu tena kwa upya. Wakapima kwa makini na mashine walizokuja nazo na nesi akaingiza nyingine, wakaona watoto wapo sawa.

“Hawa wajukuu wapo sawa kabisa. Hata wakirudi Singida wakapewa jembe kwenda kulima uwele, nitakuwa sina wasiwasi.” Wakacheka. Msindai akawatania hapo wale manesi na yule daktari aliyeingia naye, wakatoka. “Naomba tuzungumze nje kidogo baba.” Jack akamsogelea baba yake. “Sawa.” Wakatoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Sisi tukiruhusiwa leo, tunaondoka leo kurudi Singida.” “Ameniambia Junior na ndio maana nipo hapa kuhakikisha hamlali hotelini, mnaondoka leo kurudi nyumbani. Hawa watoto ni wadogo sana kulazwa mahotelini. Hivi tunavyozungumza hapa, Junior anashugulika na Jacinta pamoja na Willy, kuhakikisha mizigo yenu yote inapakiwa vizuri kwenye lori moja, iondoke leoleo kuwahi Singida. Ikichelewa sana, kesho asubuhi iwe imefika huko.” Jack hakuamini. Alijua kaka yake na familia wanakwenda kanisani, kumbe bado wanamuhangaikia! “Nashukuru sana baba.” “Nafikiri Pendo amepata tiketi zenu zakuondoka jioni. Itabidi muunganishe. Ila atawapigia simu kuwataarifu.” “Nashukuru sana baba. Asante.” “Karibu. Mungu akusaidie wewe na familia yako. Naamini mambo yatakuwa tu sawa.” “Naamini hivyo baba. Nampenda mke wangu, na kweli hajawahi kunirubuni. Sabrina amekuwa muwazi kwangu katika kila jambo. Ninayoyafanya ni katika kupenda kwangu.” Jack akajieleza kwa utulivu akitaka baba yake amuamini.

“Katika kila maamuzi, kuna faida zake na hasara zake Jackson. Ni wewe kupima. Kupi kunalemea? Na ukiridhia kwa moyo mmoja kabisa, ukamuomba Mungu na kuchukua hatua, utakuja kuona ule upande ambao hukuchagua unaanza kupewa nguvu na ule uliochagua. Hata kama ulichagua upande wenye hasara. Ukifanya kwa moyo bila kuchoka, utashangaa ule upande unaanza kuvuta mema taratibu na unakuwa salama tu. Kikubwa nia, na umuombe Mungu. Utafanikiwa.” “Nashukuru. Asante sana. Naamini tutakuwa salama.” Baba yake akacheka na kumpiga begani. “Umekuwa sana Jackson! Umekuwa na akili za kiutuuzima! Unawajibika kiume. Pongezi sana.” Jack akajisikia furaha kusikia hivyo kutoka kwa baba yake. Wakarudi ndani.

Sabrina aruhusiwa hospitalini akiwa mzima, waondoka jijini Dar bila kuagana na mama Msindai.

M

zee Msindai akaanza utani kwa mama yake Sabrina. Akamtania kwa hili na lile, wakawa wanacheka tu hapo ndani mpaka daktari wa wakina mama naye akapita. Akamsalimia Mzee Msindai, naye akamtania kwa hili na lile. “Sasa hawa wajukuu wawili, wanamtaka mama yao, wawahishwe shamba leo. Mapema kabla jua halijachwa. Uwele unaliwa na ndege huko Singida.” Wakacheka. Daktari akazungumza na Sabrina kidogo, na kwa kuwa hakuwa na tatizo, mkwewe ni dokta Msindai, akaruhusiwa. Msindai akazungumza nao kidogo, akawaaga na kubusu wajukuu, kwa ahadi ya kwenda kuwatembelea karibuni. “Nikija huko Singida mnipikie ugali na mlenda.” Akawatania wajukuu zake hapo, akawaweka chini na kuondoka.

“Kwa kuwa Pendo atakuja kunisaidia kujiandaa hapa na kutusindikiza uwanja wa ndege na Joy, mama wewe ungeenda kuzungumza na baba. Akiridhia, mpange safari. Nitakupigia nikifika nyumbani, na kuwatumia nauli.” Akafurahia sana mama Sabina. Wakachukua vyombo vyao, nakuondoka. Mchana wakarudi Pendo, Joy, Jacinta. Wakamsaidia Sabrina na kumsindikiza mpaka uwanja wa ndege. Walipofika uwanja wa ndege tu, na Junior pamoja na Awali nao wakaja. Mpaka hapo Sabrina akawa hajamuona mama mkwe wake na Jena. Lakini alishukuru Mungu. Hakutaka hiyo fujo na maneno maneno tena.

“Gari yenye mizigo yenu imeshaondoka. Mambo yakienda sawa, kesho watafika Singida. Nimewapa namba zenu wote wawili, na hii ni namba ya dereva na mwenzie anayemsaidia. Nimeshalipia kila kitu, na nimewaambia wasiondoke mpaka wahakikishe wanaingiza vitu vyote ndani. Wasiviache nje. Kwa hiyo mkifika, nyinyi muandae sehemu tu. Zaidi vitu vya watoto.” “Tunawashukuruni sana.  Asanteni.” Sabrina naye akashukuru. Pendo alileta viti vya watoto wachanga aina hiyo ya mapacha ambavyo Sabrina alipata zawadi kwenye baby shower. Jack na Sabrina wakaaga kwa kuwapa mikono na kukumbatiana, wakaingia ndani uwanja wa ndege.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Sabrina alikuwa akimuona vile Jack anavyohangaika naye na watoto utafikiri ni watoto wake wakuwazaa! Alimsaidia Sabrina kwa kila namna hapo uwanja wa ndege wakisubiri kuondoka na kwenye ndege hivyohivyo kuhakikisha watoto wapo sawa. Alikuwa akiangalia mpaka diaper kwa kila mtoto! Sabrina akabaki amkimfikiria Jack, nakumshangaa. Hakutaka Sabrina asumbuke. Alifanya kwa moyo kabisa akijituma bila kuchoka wala kutumwa. Sabrina akabaki akishangaa upendo mkubwa wa kiasi kile! Kuwepo hapo na Jack bila kumuona mama yake, inamaana mambo hayapo vizuri kati ya wapenzi hao wawili. “Inamaana Jack amenichagua mimi dhidi ya mama yake!” Sabrina akabaki akiwaza kwenye ndege. “Niliwezaje kuwa kipofu kwa muda wote huo nisione mapenzi makubwa hivi tokea mwanzoni!” Sabrina akajilaumu akiumia. Mawazo yakamrudisha chuoni.

Walipokuwa Chuoni.

I

likuwa mida ya jioni siku ya ijumaa hapo chuoni, Jack alishamsaidia kuweka mambo yake na uongozi wa chuo sawa, akiwa ameshakusanya ripoti aliyosaidiwa na mpenzi wa Jack na kurudi darasani rasmi. Ikawa imebaki kazi ya Sabrina kujisomea ili kuendelea kulingana na wenzake darasani. Alitoka usingizini mida hiyo baada ya kutoka darasani alipojisikia kichwa kumuuma sana, na baridi akaamua kulala, ndipo akaamka sasa akijisikia bado mgonjwa. Ilikuwa mwaka wa mwisho. Miezi miwili ilibaki kumaliza chuo. Ile hali aliyokuwa akijisikia, alihisi ni malaria tu, kwani bado alitetemeka baridi katika jiji hilo la Dodoma, msimu huo wa kiangazi. Joto. Na mwili mzima ulikuwa umepatwa moto. Hakuwa na pesa hata kidogo. Alitoka kuzungumza na wazazi asubuhi hiyo, wakamwambia hawana pesa. Sabina alikuwa amemtumia pesa mwezi uliopita, akaona aibu kuomba tena. Kaka yake ndio alikuwa ameanza kazi na hakuwa mtoaji. Mara zote alikuwa hana pesa. Hakuna aliyekuwa akipata pesa yake.

Sabrina akaona aende kwa Jack, hata kama atashindwa kuomba pesa, basi dawa ya maumivu. Akatembea mpaka kwenye jengo hilo lililojulikana ni la viongozi. Moja kwa moja kwenye chumba cha raisi ambaye alikuwa Jack. Akagonga kidogo tu kwa sauti ya chini. “Nani?” Akauliza Jack. “Sabrina.” Sabrina akakumbuka kusikia purukushani kidogo ndani ya hicho chumba. Sabrina akarudi nyuma kidogo akiwa amekunja uso nje ya mlango uliokuwa bado haujafunguliwa. Akaanza kujiuliza kama aondoke au asubiri kufunguliwa kwani bado purukushani ndani zilikuwa zikiendelea. “Naweza kurudi baadaye!” Sabrina akazungumza kwa sauti ya chini na wasiwasi kidogo. Hapo hapo mlango ukafunguliwa. Akachungulia Jack akiwa na wasiwasi kama aliyefumaniwa na mkewe, wakati ni Sabrina aliyemkataa hadharani, wapo kumsaidia tu. Sabrina akakumbuka kumuona akiwa amevaa suruali yake ya jinsi bila hata mkanda na nguo ndogo ya kiume ya ndani. Singilendi.

“Kwani anaingia ndani ili na mimi nivae?”  Akasikia sauti ya Phina akiuliza ndani kwa kulalamika. “Halafu angekuwa hata anapiga simu kukutaarifu kuwa anakuja jamani! Anawezaje kutokezea tu!” Phina akaendelea kulalamika. Sabrina akazidi kujisikia vibaya. “Samahanini sana jamani! Ni kweli nilitakiwa hata kupiga simu. Sikukusudia kuingilia.” Sabrina akaongea kwa hofu na sauti ya chini kama asiyetaka majirani wasikie. Jack akarudisha kichwa ndani kama kutaka kumjibu Phina, hapohapo Sabrina akaondoka kwa haraka bila hata kuaga. Jack kutoa tena kichwa nje, Sabrina hayupo, akawa alishaondoka.

Sabrina alirudi chumbani kwake akachukua madaftari na kurudi kusoma akiwa mgonjwa na njaa. Jack alimkimbiza akiwa vilevile bila viatu. Alishuka mpaka chini hakumuona Sabrina. Akarudi chumbani kuvaa shati na viatu kwa haraka, Phina akiwa amebaki kitandani, akishangaa. Anaacha mapenzi kumkimbilia Sabrina! Hicho kitu kikamuuma sana Phina, akashindwa kuelewa, akahisi amedhalilishwa vibaya sana. “Sikuelewi Jack! Unaniacha hapa, unamkimbilia Sabrina?” Akili ya Jack wala haikuwa pale tena. Hakumjibu kitu Phina. Akaendelea kuvaa viatu baada ya soksi kwa haraka. “Wewe Jack!?” “Naomba tuzungumze baadaye Phina.” Jack akavuta shati na kutoka kwa haraka, akamuacha Phina kitandani.

Phina akavaa nguo zake akaona machozi yanamtoka. Akajua ndio ameachika, akaanza kuona aibu jinsi atakavyodhalilika pale chuoni. Kujulikana ameachwa na Jackson Msindai! Raisi wa chuo! Phina akahisi kuishiwa nguvu kabisa. Akakaa pale akifikiria, akaamua kumpigia simu Jack. Akaona simu zake zinakatwa, asijue Jack kwa muda huo hakutaka muingiliano wowote kwenye hiyo simu. Alikuwa akimpigia simu Sabrina huku akimsaka kila mahali. Alianzia chumbani kwake, akamkuta msichana anayelala na Sabrina hapo chumbani yupo na wenzake wamekaa wanaangalia tv. “Sabrina amepita hapa sasa hivi?” Wote wakakaa sawa, ni Jackson Msindai, raisi wao, ndiye anayeuliza. “Alikuwa amelala hapa. Nafikiri anaumwa, maana alikuwa akitetemeka baridi. Akatoka mara moja, akarudi tena. Akachukua madaftari yake na vitabu, akatoka tena. Hakukaa.” Jack akatoka tena hapo kwa haraka. Akapita maktaba ya chuo. Akazunguka kila meza kila kona. Hakumkuta. Akaenda darasani kwake. Sabrina hakuwepo. Akaendelea kumtafuta huku akimpigia simu kama mwehu bila mafanikio.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Huku kwa Phina nako akatoka, akaona aende kwa Ibra, rafiki wakaribu sana Jack. Akamkuta Ibra chumbani kwake. “Mbona kilio tena ‘first Lady’ wetu!” Jina lililompa heshima kubwa sana Phina hapo chuoni, akijulikana kama first lady, kwa kuwa alikuwa mpenzi wa Raisi wa chuo. Kote walimuita first lady hata alipokuwa na Jack mwenyewe. Na Jack hakuona tatizo Phina kuitwa first lady. Ikabidi Phina amuelezee Ibra mkasa mzima.

Japokuwa Ibra alishachoshwa na Jack juu ya Sabrina, na hakuwa akimuelewa kabisa, lakini ilibidi kumchukulia hivyo hivyo na huo udhaifu wake. Ndipo ikabidi kumkalisha chini Phina na kumuweka sawa. “Kaa kwanza hapo kwenye kiti, uniangalie na kunisikiliza kwa makini.”  Phina akakaa mbele ya Ibra. “Haya, futa machozi kabisa, kwa kuwa haya mambo hayahitaji papara. Ukijichanganya tu, utaharibu na utanikumbuka. Ila ukinisikiliza vizuri, utafaidi kwa kuwa Jack sio mchoyo na ni Msindai. Sijui kama unanielewa?” Phina akatulia ili kuelewa.

“Sijui Jack alikwambia nini juu ya mahusinao yenu mwanzoni kabisa mnaanzana na sijui unamfahamu kwa asilimia ngapi! Lakini ana vitu vichache sana anavyopenda na kusifia. Hana madhaifu mengi kama mwanadamu. Mimi ni mtu wake wa karibu sana. Mpaka umuudhi Jack au akuhesabu ni adui, sijui utakuwa umefanya nini! Ndio maana unamuona anakubalika kila sehemu na kila mtu. Ana hekima yake ya kuishi kwenye jamii na ana uwezo mkubwa sana wa kuendesha mambo. Nadhani unaona kwenye uongozi wake.” Hapo hata Phina akakubali.

“Tokea namfahamu Jack. Tunapokuwa naye nje ya hapa, yaani huko mtaani, nyumbani na hapa pia chuoni ni mtu mwema sana. Ila anao udhaifu mmoja wa ajabu sana, unaitwa Sabrina.” Hapo Phina akakunja uso. “Linapokuja swala la Sabrina, hana mipaka wala undugu. Naweza nisikueleze kwa undani ukanielewa, lakini Ney, huyu unayetuona tunazunguka naye sana hapa chuoni tukiwa na Felix pamoja na Msindai mwenyewe, anaweza kukueleza.” Ibra akaendelea kumuweka sawa Phina.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakati huku kwa Jack akiendelea kumsaka Sabrina karibu kuchanganyikiwa. Kumbe Sabrina alipochukua madaftari yake ijumaa hiyo ambayo karibu wanachuo wengi wanakuwa wameshaanza weekend. Miziki mikubwa vyumbani, wanaokwenda baa wanakwenda kustarehe, wenye ndoa zao wanakimbilia majumbani mpaka jumapili, yeye Sabrina ambaye hakuwa hata na rafiki wa kusoma naye, akaona akajifiche kwenye darasa la certificate. Akaenda kukaa nyuma kabisa ya darasa, akiwa amevaa koti zito, akajifunika na kitenge chake, akajiinamia akisoma.

Baada ya muda waliingia wenzake wa darasa moja. Walijulikana kundi lao la kujisomea na wengi waliwajua kama ni wasongo. Kusoma kupita kiasi. Waliingia wakatengeneza duara lao mbele kabisa. Wakike na wakiume. Wakaanza kusoma na vicheko vikiendelea. Hawakumsalimia Sabrina kabisa japo walimuona. Sabrina akatulia tu akijisomea peke yake. Wakati mwingine mmoja wao alisimama mbele kabisa ubaoni akiwafundisha kama mwalimu wengine wakiuliza maswali, huku wakiendelea kusoma.

Baada ya muda tena Sabrina akaanza kuona watu wachache wakiingia na kukimbilia viti vya nyuma karibu na yeye ambako kuna utulivu. Sabrina akatulia kabisa, akaendelea kusoma. Mara akasikia wakimsalimia Jack. “Karibu mkuu uungane nasi.” Lile kundi kubwa la mbele likaanza. Akijua mkuu ni Jackson Msindai, Sabrina hakunyanyua hata uso kutizama. Akasikia sauti ya Jack akiwasalimia na kuuliza maswali machache, kisha akawasikia wakijichekesha. Sabrina akatulia kimya. Akasikia akiwaaga, pakazuka ukimya.

Kiti kikavutwa mbele yake. Jack akakaa. “Vipi?” Jack akaanza, Sabrina akaitika, “Safi tu.” Kwa sauti ya chini bila hata kumtizama. “Simu yako iko wapi?” Jack akauliza. Sabrina akakunja uso akiwa vilevile ameinamia madaftari yake bila hata kumwangalia, kisha akaanza kuitafuta mifukoni kwake. Akaikosa, akarudi kwenye begi lake alilokuwa amebebea vitabu. Akaikuta humo ndani. Akaitoa. Akakuta missed calls 27 kutoka kwa Jack. Akashangaa na kumwangalia Jack. “Samahani, sikuona. Simu ipo kwenye silence.” Akaongea kwa sauti ya chini huku akiitizama simu yake nakuendelea kuhakikisha missed  calls zote alizokuta. Akajiridhisha kuwa zote zimetoka kwa Jack. “Sikuwa nimeshika simu.” Sabrina akarudia kwa sauti ya chini. Kisha akakumbuka kumwandikia ujumbe kwenye kikaratasi, Jack akimtizama. ‘Samahani, sikukusudia kuingilia au kuwasumbua kule chumbani kwako. Sitarudia tena. Samahani.’ Akamgeuzia kile kikaratasi, lakini Jack alishakuwa amekisoma wakati akikiandika. Akakumbuka kumuona Jack kukivuta kile kikaratasi, akakikunja na kukiweka mfukoni bila yakujibu.

“Mbona umejifunika vitu vingi na kuvaa koti? Unaumwa?”  Akamuuliza. Walijua wazi watu wa pembeni wanawasikiliza, Jack hakujali. Kimya, Sabrina ameinama akichora alama ya mshale kwa kurudia rudia. “Brina?” “Hapana. Nipo tu sawa.” Sabrina akajibu bila yakumtizama. Akashitukia Jack ameweka mkono kwenye kipanda uso. “Mmmh!” Jack akahamaki. “Una homa kali! Umekunywa dawa?” Jack akauliza. Sabrina akatingisha kichwa kukataa. “Unafikiri inaweza kuwa malaria?” Jack akauliza tena. “Sijui!” Sabrina akajibu sauti ya chini. “Twende tukaangalie mjini mara moja.” Sabrina akakunja uso na kumtizama. Macho yakagongana. “Twende hospitali.” Jack akaongea akisika kujali. Kwa kuwa darasa zima lilikuwa kimya gafla, hata waliokuwa wakisoma kama kundi, nao wakawa kimya, Sabrina akajua kila mmoja anasikiliza. Akakusanya vitu vyake na kurudisha kwenye begi lake. “Nikusaidie?” Jack akauliza kwa kujali zaidi. “Hapana, asante.” Sabrina akasimama, wakatoka. Jack mbele, yeye nyuma.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Huyu Sabrina ndiye aliyekuwa amemkataa Jack kwa jeuri kubwa na ukali, akijua ni mke mtarajiwa wa Emma. Akaachika vibaya sana, tena kwa kudhalilishwa mbele za watu, chuo kizima kikajua. Jack amerudi kuwa mkombozi. Anamjali kama mpenzi wake! Akakumbuka kumtongoza tena kwa mara ya pili. Sabrina tena akamkataa akijua atakuwa mke mtarajiwa wa Tino. Tino akamuacha kikatili akitaka hata asibakie na watoto wake! Jackson huyo huyo akamfuata Moshi na kumchukua. Amefunga naye ndoa ya hali ya juu. Amezaa watoto wa kizungu, lakini bado Jack yupo naye hapo akihangaika naye. Kutokuagana na mama Msindai, na yale aliyoyasikia kutoka kwa huyo mama akimsengenya na kumsingizia uchawi, inamaana wamekosana na Jack kwa ajili yake. Sabrina akaumia sana moyoni. Akamtizama Jack ambaye macho yake yalikuwa kwa mtoto aliyekuwa amekaa naye yeye. Jeiline. Na Sabrina alikaa na Keiline. Sabrina akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu kama kusafisha kifua na mawazo. “Nilishindwaje kuona mapenzi mazito hivi kutoka kwa Jack!”  Akaendelea kujilaumu, jinsi alivyompuuza Jack na kuwapa wanaume wengine kipaumbele wakati hata hawakustahili. Mawazo yakamrudisha tena chuoni.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Ulikula?”  Akakumbuka Jack kumuuliza wakati wakitembea kufuata gari ya Jack. Jackson Msindai alikuwa na usafiri wake hapo chuoni. Kila mtu alijua kama Jack anayo gari. Alipokuja mwaka wa kwanza, muhula wa kwanza, hakuwa na gari. Lakini muhula wa pili, akarudi chuoni na gari yake. Japokuwa alikuwa akiishi hapohapo chuoni, lakini alikuwa na usafiri wa maana. Gari nzuri sana ya heshima aliyokuwa akiegesha kwenye sehemu maalumu wanapoegesha walimu wa hapo chuoni. Na kwa kuwa hakuwa akiitumia kila siku, na Dodoma kulikuwa na jua kali na vumbi, alikuwa akiivalisha plastiki yake maalumu ambayo ilikuwa kama nguo ya gari. Akitaka kutoka ndipo alipokuwa akiitoa kirahisi tu, na kuikunja. Akirudi anaivalisha tena. Hata walinzi hapo chuoni walijua ni gari yake.

“Brina, umekula?” Ikabidi Jack amgeukie na kumuuliza akimuonyesha anataka jibu la hakika. “Nilikunywa chai asubuhi.” Sabrina akajibu taratibu, Jack akataka kuuliza swali jingine, akaona anyamaze. Wakatembea mpaka kwenye gari yake. Akatoa plastiki ya juu, Sabrina akimshangaa tu jinsi anavyohangaika naye. Amejikunyata, akitetemeka baridi ya kutoka ndani ya mwili wake wala haikuwa baridi ya nje. Akamfungulia mlango. “Twende hospitalini.” Sabrina akapanda kwenye gari, Jack akaondoa gari. Akapita kwenye baa moja ambayo haikuwa mbali na hospitalini, akamnunulia chakula, akamletea na soda. “Kula kabla hatujafika, ili ikitokea unapewa dawa, isikusumbue tumboni.” “Asante.” Sabrina akashukuru na kupokea. Bila kuchelewa, Sabrina akaanza kula. “Wewe ulikula?” Jack akamgeukia akiwa anaendesha. “Nina vyakula chumbani. Nipo sawa. Wewe kula.” Sabrina akaendelea kula mpaka wanafika hospitalini akawa bado hajamaliza kula. Jack akaegesha gari nje, akamalizia kula ndipo wakaingia ndani.

Akapimwa na kukutwa na malaria. Jack akamwambia daktari waliyemkuta hapo zamu na kuwahudumia kuwa Sabrina ana kazi nyingi sana chuoni, kama angeweza kumuandikia dozi nzuri na zakutumia muda mfupi, ingekuwa jambo zuri. Mtoto huyo wa Msindai akasema pesa isiwe tatizo. Daktari akacheka na kumuandikia dawa Sabrina, za kushusha homa na hizo za malaria.

Wakati wanatoka hospitalini, Ibra akapiga. “Uko wapi wewe? Hata gari yako haipo!” “Nipo hospitalini, nimemleta Brina. Ana malaria kali na homa ipo juu.” “Daah! Mpe pole.” “Atasikia.” “Sasa?” Akauliza Ibra. “Ameandikiwa dawa, ndio tunakwenda kununua, kisha turudi chuo. Kwema?” Jack akauliza wakati wanapanda kwenye gari. “Kwema tu. Nilikuwa nakucheki. Siunakumbuka discussion ndio muda huu?” “Nyinyi endeleeni tu.” Jack akajitoa kabisa huku akijua wenzie wanamtegemea. “Labda tuahirishe Jack. Unajua hakuna kitakachoendelea bila wewe pale. Ile topic ni wewe mwenyewe ndiye uliyeelewa na ukaahidi washikaji utawasaidia leo.” “Basi waambie nimepatwa na dharula, iwe kesho.” Kirahisi tu Jack akaahirisha na kuaga. “Tutaongea baadaye basi.” Akakata kabisa simu na kurudisha mfukoni bila kusubiri majibu ya Ibra.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Unaweza kunipa hiyo karatasi ya dawa, nikanunue dawa, wewe uwahi chuoni ukasome na wenzako Jack. Mimi nitakuwa sawa tu.” Sabrina akaona asimuharibie ratiba zake. “Watakuwa sawa tu. Twende tukanunue dawa, ukapumzike.” Sabrina akajirudisha kitini, akatulia. Wakaendesha mpaka duka la madawa kubwa hapo Dodoma alipokuwa ameelekezwa na huyo daktari kuzipata aina hiyo ya dawa. “Naona hapo pembeni kuna duka. Mbali na maji ya kunywa, unataka nikununulie na nini kingine?” Jack akauliza walipofika. “Toilet paper na dawa ya mswaki tafadhali.” Sabrina hakutaka hata kujivunga. “Na nini kingine?” Sabrina akashangaa kuwa bado anaulizwa tena. “Niongeze tena!?” “Wanaonekana ni duka kubwa, lina vitu vingi. Sidhani kama utakosa mahitaji yako hapo. Au unataka twende wote?” Sabrina akababaika kidogo. Kisha akasita. “Brina! Mimi ndiye niliyekwambia. Hujaomba. Kama umeishiwa na unadhani utapata vitu vyako hapo, shuka umwambie muuzaji, mimi nitalipa.” “Nimeishiwa vitu vyote vya msingi Jack. Na hapo naona kama ni super markert. Bei zitakuwa juu sana. Kuna sehemu huwa nakwenda kununua vitu vyangu. Wanabei nzuri.” “Wewe mbona muoga wakati hata hatujajua bei? Naomba twende.” Wakashuka wote garini.

Jack akaenda upande wa dawa, akaagiza, na kulipia. Wakahamia upande wa pili. Sabrina akabeba kikapu kidogo, wakaingia ndani. Jack akampokea. “Mimi nitabeba. Wewe chagua.” “Asante Jack.” Sabrina hakujivunga. Hakuwa na vitu vingi tu vya muhimu, vya kike na vya kawaida. Akaweka vyote, Jack akiwa anamfuata kwa pembeni. Akawa akichukua kwenye shelfu na kuweka kwenye kapu, mpaka akamaliza. “Nashukuru Jack.” “Unauhakika umekumbuka kila kitu?” “Ndiyo, asante. Nilikuwa nimeishiwa mpaka sabuni ya kuogea!” Jack akatabasamu tu. Wakalipia na kurudi chuoni.

Waliegesha gari ya Jack palepale walipoitoa mwanzo, Jack akaifunika, wakaelekea chumbani kwa Sabrina. Walipoingia wakakuta wale wasichana wamejaa pale na wanapiga kelele. Walipomuona tu Jack, wakatulia. “Samahanini. Sabrina anaumwa. Tumetoka hospitalini, amepewa dawa anatakiwa kupumzika. Niombe radhi kwa usumbufu, kama mnaweza kuhamisha hii sherehe chumba kingine ili yeye apumzike, ingemsaidia sana. Samahanini sana.” Kwa heshima zote wakakubali na kumpa pole Sabrina wakati hilo kundi ndio waliokuwa miongoni wakumcheka Sabrina na kila wakiingia humo ndani walimfanya ajisikie kama hayupo. Wakatoka.

“Nakushukuru Jack. Maana nilikuwa nikiwaza nitalalaje hapa ndani na kelele za hawa watoto wanaonidharau hivi! Maana walikuwa wakianza kucheka hapa, mpaka inanibidi mimi ndio niondoke. Na leo kichwa kinaniuma sana, nahitaji kupumzika.” “Pole. Kunywa dawa zote, ndipo utaamka ukiwa na nafuu.” “Asante sana, na usiku mwema.” “Mbona kama unanifukuza!?” Sabrina akacheka kidogo kwa aibu. “Nataka nibadili nguo nilale.” “Oooh! Haya. Usiku mwema, nitakuona kesho.” Jack akatoka.

Sabrina akabadili nguo, na kumeza dawa. Akaanza kupanga vitu alivyonunuliwa na Jack kabatini. Baada ya dakika tano tu kumeza dawa, akasikia zinapanda. Akakimbilia bafuni, akazitapika zote. Aliona zile dawa zote alizomeza amezitapika kama zilivyo. Akatamani aziokote asiharibu dozi, lakini akashindwa, ilikuwa chooni. Akatoka hapo akiwa amesikitika sana. Dawa alinunuliwa aghali sana na Jack. Hana pesa. Anafanya nini tena na kwenda kwa Jack alisikia mpenzi wake akilalamika kufika kwake bila taarifa! Sabrina akajiambia amebakiwa na dawa za kupunguza tu maumivu na kushusha homa, dozi ya malaria ilikuwa kunywa tu mara moja. Akapoa akiwaza chakufanya. Akarudi kunywa maji. Akatapika tena. Kichwa kikaendelea kumuuma, akajaribu kumeza tena dawa, akatapika. Usiku huo ukawa wakutapika mpaka mwenzie aliporudi katikati ya usiku, akaondoka tena. Maana Sabrina aliamua kutapikia ndoo yake ya kuogea baada ya kuchoka kukimbilia chooni, ikamkera mwenzie akaona ampishe.

Jumamosi. 

K

wenye mida ya saa mbili na nusu Jack akarudi. “Atakuwa amepitiwa na usingizi muda huuhuu huyo. Mimi nilishindwa kulala usiku sababu alikuwa akitapika mfululizo nikashindwa kulala. Nikaenda kulala kwa rafiki yangu, nimerudi kwenye saa moja, pia nimemkuta akitapika.” Yule binti akamwambia Jack. Jack akashangaa. Sabrina alimuacha jana yake akiwa na homa tu, hata daktari alipomuuliza kama anatapika, akakataa na kumwambia vidonge vitamfaa! Akaenda kukaa kitandani kwake. Sabrina akiwa usingizini akahisi mikono ya kiume ikimpapasa kichwani. Akageuka. “Jack!” “Homa ipo juu sana. Vipi!?” “Natapika, Jack! Sijui nifanyeje? Kila ninachoweka mdomoni kikikaa sana dakika mbili, kinatoka.” “Dawa?” “Nilitapika usiku uleule.” “Pole, sasa kwa nini hukuja kule kwangu?” Sabrina akamtizama kidogo na kunyamaza. Jack akakumbuka fumanizi. “Au basi hata kunipigia simu?” Jack akabadili. Sabrina akanyamaza. “Itabidi turudi hospitalini.” “Tena Jack!?” “Sasa unafikiri utaponaje? Lazima kurudi. Umebakiza muda mfupi sana wakumaliza chuo, Brina. Huna muda wakuugua.” “Ni kweli.” Wakarudi tena hospitalini.

Daktari akamuwekea drip ya maji maana Sabrina alimwambia anasikia kizunguzungu na amechoka sana. Akamwambia Jack, anamuwekea dripu ambayo itamsaidia kumrudishia nguvu na pia itakuwa na dawa ya kuzuia kutapika. Ilipoanza kuingia mwilini, Sabrina akaanza kusinzia. “Nasinzia Jack. Sijalala usiku.” “Lala usiwe na wasiwasi. Ikiisha nitakwenda kumuita nesi.” “Asante.” Sabrina akashukuru.

Mara Phina akampigia. Jack akapokea. “Nilikwenda chumbani kwa Sabrina kumuomba msamaha, jana nahisi niliropoka. Nikaambiwa na yule msichana anayeishi naye, umemrudisha hospitalini. Mko wapi?” Jack akamuelekeza hospitali walipo. “Lakini hatutalala. Amewekewa dripu moja tu, kisha tutaruhusiwa.” Jack akaongea bila hata wazo la pili mpaka akamshangaza Sabrina mwenyewe. Phina akaumia lakini akajikaza. “Angalau nimletee hata uji tu! Asilale na njaa.” Hapo akawa amemgusa Jack. “Hilo wazo zuri. Nashukuru. Kina Ibra pia wanakuja, mpigie Ibra simu mje naye, wasikuache.” “Sawa.” Jack akakata. Sabrina akapotelea usingizini asimuelewe Jack.

Kufika majira ya saa tano asubuhi, uongozi wote wa chuo wakahamia hapo kwenye hicho chumba alichopumzishwa Sabrina. Kila mmoja akitaka aonekanike kwa Jack kuwa anajali. Jack alipoona kelele zinazidi, akawaambia wahamie nje. Stori zikaendelea. Wakahamisha makao hapo. Lakini Phina akajisikia vizuri na yeye kuwepo hapo na bado wanamtambua kama first lady na Jack hakatai wala hana wasiwasi juu ya hilo. Akaamini maneno ya Ibra. Kila wakati walimuona Jack akirudi ndani kumuangalia Sabrina aliyekuwa amelala hana habari. “Vipi lakini?” Ibra akamuuliza wakati anatoka. “Daktari ameniambia baada ya hiyo dripu, atakuwa sawa. Analala sana sababu ya dawa, na usiku pia hakulala. Alikesha akitapika.” Jack akaeleza bila hata wazo la pili mbele ya wenzake na Phina.

Dripu liliiisha Jack akiwepo chumbani, akaenda kumuita nesi, akarudi naye chumbani na daktari. “Brina!” Wakamsikia Jack akimuamsha kwa upole. Sabrina akaamka. “Nasikia usingizi!” “Pole. Lakini daktari anataka kuzungumza na wewe.” Sabrina akajigeuza taratibu. Unajisikiaje?” Daktari akamuuliza. “Nimelala muda wote, hata sijaamka kutapika.” “Sasa kwa kuwa umeacha kutapika, nakuandikia tena dawa ile ile. Utakunywa mara moja tu na kuendelea kunywa dawa za maumivu. Baada ya ya leo na kesho utaanza kujisikia vizuri.” “Nashukuru sana.” Sabrina akamshukuru. “Sasa kabla yakuondoka, utakunywa hapahapa hiyo dawa. Tukihakikisha imekaa humo ndani, ndio tutakuruhusu.” “Hilo litakuwa la msingi dokta. Ili tusirudi tena.” Akaongeza Jack.

Nesi akatoa ile dripu akaacha sindano. “Hii nitatoa mwishoni kabisa tukishahakikisha haitatumika tena.” “Inamaana kama sitatapika tena?” Sabrina akamuuliza yule nesi na sauti ya usingizi. “Sawa sawa.” Akamalizia alichokuwa akifanya, akaaga. “Nitarudi na dawa baada ya muda mfupi.” “Asante sana.” Jack akashukuru, yule nesi akatoka. Phina akarudi ndani. “Vipi Sabrina?” Phina akamsogelea pale kitandani. “Safi tu, na samahani Phina. Jana sikukusudia kuingilia. Nilikosea kuja bila taarifa.” Sabrina akaongea kwa sauti ya chini tu na ya taratibu. Jack alikuwepo hapohapo chumbani nyuma karibu na dirisha, akawa ameinamia simu yake. Ibra ndiye aliyemshitua Phina kuwa huo ndio wakati wakwenda kuzungumza na Sabrina, Jack akiwepo. “Wala usijali kabisa. Nahisi na mimi nilipaniki ndio maana niliongea hivyo.” Phina akajibu kwa upendo, Jack akiwasikiliza. “Naelewa, lakini naahidi sitafanya hivyo tena Phina. Ikiwa ni lazima sana, nitakuwa nikikupigia wewe simu. Kuliko kuwatokezea tu! Nakiri si sawa na sina sababu yakuwafanyia hivyo.” Moyo wa Jack ukapasuka, nusura aangushe simu. Wote wakamwangalia.

“Huhitaji kuwasiliana na mimi kupitia Phina!” Jack hakuweza hata kuvumilia wala kuliwekea kiporo. Hapo hapo akasawazisha. Sabrina na Phina wakabaki wakimwangalia, Phina akiumia sana moyoni. “Ni kitu kilichotokea mara moja, na tutarekebisha.” Akaongeza Jack akionekana amebadilika kabisa usoni. Akarudisha macho kwenye simu yake. Sabrina hakujua azungumze nini tena. Phina alibaki ameduaa akijua watu wa nje pia wamesikia. Akabaki kama aliyepigwa na bumbuwazi. Jack akawa muungwana, yeye mwenyewe akajirudi. Akajisogeza kwa Phina na kumshika kiunoni. “Phina amekuletea uji, ungependa kujaribu?” Akamuuliza Sabrina aliyekuwa ameshageukia ukutani. “Nashukuru kujali Phina. Lakini naogopa nisije nikaanza kutapika tena, Jack!” “Sasa tutajuaje kama dawa zimesaidia au la! Sitaki tena turudi chuo, uanze tena kutapika. Heri ule, ukitapika hapa daktari atajua chakufanya.” Sabrina akakaa.

“Ni kweli. Bora ujaribu hata kidogo.” Phina akamuwekea kwenye kikombe, akamkabidhi. “Nashukuru Phina. Asante sana.” Sabrina akashukuru tena akiwa amejawa wasiwasi asije kukosana na first lady bila kujua Phina mwenyewe analazimika kumkubali tu, akiangalia maisha yake ya badaye. Phina alifikishwa kwenye usemi wa ‘mtumikie kafiri...’ Japokuwa alikuwa akimpenda sana Jackson, lakini alishajua hapatakuja kuwa na ndoa kati yao. Halafu alishajijengea heshima hapo chuoni yakuitwa first Lady! Phina akaona kama Jackson hatamuacha, kumchukulia Sabrina aliyemuonyesha anamtambua yeye kama mpenzi wa Jack, haitakuwa ngumu. Na Ibra naye alishamwambia akae mkao wa kuajiriwa popote anapotaka baada ya kumaliza chuo, akaona kumchukulia Sabrina kwa kipindi hicho ni garama ndogo sana. Kwanza alijua Sabrina amebakisha muda mfupi sana amalize chuo, ataondoka na kumuachia Jackson. Akakaza moyo, akaendelea kujituma.

Sabrina akaendelea kukumbuka jinsi alivyokuwa akiunywa ule uji kwa makini akiomba Mungu asitapike ili aruhusiwe aondoke hapo hospitalini na kuondoa hiyo fujo ya Jack na viongozi wenzie. Akakumbuka wakati akimalizia, nesi naye akaingia. “Vipi?” Nesi aliuliza. “Nakunywa uji, naona unakwenda vizuri. Ila usingizi ndio umenijaa!” Sabrina akaongea kwa kulalamika. “Dawa zakuzuia kutapika ndio zinaleta usingizi. Kunywa hizi dawa za malaria. Zikitulia baada ya nusu saa, tunakuruhusu ukapumzike nyumbani.” “Nashukuru sana.” Sabrina akashukuru na kupokea dawa. Akazinywa. Akamalizia uji, akaenda chooni. Akajisaidia na kurudi kujilaza pale kitandani.

“Vipi?” Jack akamuuliza wakati amejilaza. “Nipo sawa. Ni usingizi tu. Asante Jack.” “Karibu. Ila kama una usingizi, wewe lala tu. Muda ukifika, nitakuamsha turudi chuo.” “Daah! Hapo sawa.” Akavuta shuka, akajifunika vizuri. “Nikuongezee shuka nyingine?” Jack akauliza kwa kujali. “Kama lipo karibu, lakini sio uende kutafuta mbali.” Phina akaangalia pale chumbani, akakuta mashuka yamepangwa pembeni. “Hili hapa. Tena yapo mawili! Nikufunike yote?” “Nitashukuru Phina. Asante.” Sabrina akapotelea tena usingizini.

Akalala mpaka alipoamshwa tena na Jack. Akakuta Jack alishalipia, wakaondoka na gari ya Jack. Ibra alikaa mbele na Jack ambaye ndiye alikuwa dereva. Phina na Sabrina walikaa nyuma. Alichofanya Sabrina nikujiegemeza  dirishani, akajifunika na kulala tena. Kukawa kimya. Alikuja kuamshwa tena na Phina. “Tumefika chuo.”  Sabrina akaangalia nje, akakuta wapo chuoni. “Jamani niwashukuruni wote. Asanteni sana. Acha mimi nikalale, nimalize huu usingizi.” “Basi nitakuletea chakula baadaye. Unahamu ya kula nini?” “Naomba nisikusumbue Phina. Huu uji uliobaki humu kwenye chupa, unatosha. Niruhusu tu niende na chupa, nikimaliza uji, nitakuletea chupa yako chumbani kwako.” “Lazima kula Brina. Hata kama husikii hamu ya kula, lazima ujilazimishe ili usichoke.” Jack akaingilia. “Basi nikiamka, nitatafuta chakula. Naomba niwaache. Jack, nashukuru sana.” “Karibu.” Sabrina akashuka, Ibra kimya. Akaondoka.

Sabrina akakumbuka kuoga na kurudi kitandani kama mlevi. Hakunywa hata huo uji. Alilala, asijue ni saa ngapi. Chumba kilikuwa kimya kabisa. Kila aliposhituka, na kupata ule utulivu, alirudi kulala. “Brina!” Baadaye akiwa usingizini, akakumbuka kusikia sauti ya Jack. Kugeuka, nje kulishakuwa giza. Akamkuta Jack na Phina. “Vipi?” “Nasikia baridi Jack! Nahisi homa inataka kupanda.” “Tokea mida ile tulipotoka hospitalini, ulimeza tena dawa za kushusha homa?” Sabrina akafikiria. “Sidhani!” “Unazo dawa zenyewe lakini?” Phina akauliza. “Ninazo. Naomba niangalizie kwenye kabati, tafadhali.” Phina akaenda kabatini kwa Sabrina. “Umepanga vizuri!” Phina akasifia. “Asante.” Sabrina akajibu na kurudi kulala. “Usilale tena sasa! Meza dawa ule ndipo urudi kulala.” Jack akamuwahi. “Sisikii njaa Jack! Acha nilale.” “Hapana Brina. Kula hata kidogo.” Sabrina akakumbuka Jack kumkatalia kwa kujali. Akakumbuka baridi aliyokuwa akiipata siku ile! Alikaa akitetemeka. Akajifunika vizuri. Phina akampa dawa na maji, akameza.

Kisha Phina huyohuyo akampa chakula. Walikuwa wamemletea ndizi za mchuzi. Sabrina akafurahia hicho chakula. Akala chote bila hata kubakisha. Jack na Phina walikuwa wamekaa wakiangalia simu ya Jack pamoja. Sabrina akataka maji ya kunywa. Akaona shida kuwasumbua. Akatoka pale kitandani alipokuwa akila. “Wapi tena?” Jack akauliza. “Naenda kusafisha kinywa bafuni ili nikirudi nilale moja kwa moja. Nawashukuru sana, kwa kila kitu.” “Sasa hivi hata ukirudi kulala mpaka asubuhi, hamna tatizo.” Jack akaongeza. “Kweli.” Sabrina akatoka na mswaki mkononi, akawaacha hapohapo. Alidhani wangeaga waondoke, lakini wakaonekana kama wamefika. Aliporudi na kupanda kitandani ndipo Jack akaaga.

Kwa Jack na Sabrina sasa.

Y

ote hayo Sabrina aliyakumbuka vile Jack alivyokuwa akimtanguliza yeye popote na kwa yeyote. Wala safari hii kwa mama yake haikuwa mara yake ya kwanza! Ikawa kama amefunguliwa macho na kuona kila kitu. Akamtizama tena Jack pale alipokuwa amekaa na Jeiline. Macho yakagongana. Akacheka. “Ninahamu na wewe!” Sabrina akanong’ona. “Nikuvulie shati unuse?” Sabrina alicheka mpaka machozi. Akamwangalia tena Jack, akazidi kucheka. “Au awamu ya kunuswa imeshaisha jana?” Jack akaendelea kuuliza. “Ujue Jack unahitaji kukua ili watoto wakikua wakute baba yao alishakuwa!” “Mimi nimeuliza kwa upendo tu mama. Kosa langu lipi? Maana enzi zetu wenyewe, sasa hivi ungekuwa hapa kifuani ukininusa mpaka unalala!” “Watu wanakusikia Jack, bwana!” “Gafla unaogopa watu wakati ulikuwa ukivaa mashati yangu mbele ya Pam tena bila hata wasiwasi!” Sabrina akakumbuka nakuzidi kucheka.

Kisha akatulia kama anayejaribu kuvuta kumbukumbu. “Jack wewe!” “Kumbe! Mwenzio alikaribia kuchanganyikiwa! Lakini wewe ukawa huna habari!” Sabrina akazidi kucheka. “Usiniambie nimekwisha thamani?” “Hata kidogo. Jana yenyewe nililala vizuri sababu ulikuwa umelala pale pembeni ya kitanda changu. Nikawa napata harufu yako sawia!” Jack akacheka sana. “Kwa hiyo bado soko lipo?” “Sana tu. Wewe wangu.” Wakavuta masikio ya watu. Wakawa wakiwasikiliza wao wakizungumza sauti ya chini huku wakicheka. Wamekaa viti mbalimbali na watoto wao.

Walifika nyumbani kwao wakiwa wamejawa cheko. Jack akapitiliza chumbani. Baada ya muda akatoka Sabrina akiwa anawaweka sawa watoto. “Sasa mzazi wangu? Nipike nini?” Sabrina akacheka sana. “Unataka kunipikia Jack?” “Nakupikia mzazi wangu. Nimechukua likizo maalumu kwa ajili yako tu Brina wangu. Wewe pumzika chumbani. Nishaandaa chumba kwa ajili yako na watoto. Leo itabidi tulale nao wote mpaka kesho tutakapoletewa vitanda vyao.” Sabrina akasimama na kwenda kumbusu Jack. Jack akamkumbatia vizuri. “Nakushukuru kwa upendo Jack. Unanipenda sanaaa. Leo nimekutafakari, mpaka nikaumia moyoni!” “Umeona ulivyojichelewesha kupendwa?” Sabrina akacheka sana. “Bwana mtoto umeniringia wewe!” “Najuta Jack wewe, acha tu. Nimerudi mpaka chuoni, nikaumia sana. Kweli nimejichelewesha.” “Tena sana.” Sabrina akazidi kucheka.

“Bwana Jack mwenzio nipo serious.” “Aliyekwambia mimi simaanishi ni nani? Nakuhurumia sana tu.” “Sasa safari hii nipo kupendwa. Ushindwe mwenyewe.” Jack akacheka sana. “Brina huyo!” “Kumbe!” “Basi wewe utapendwa mpaka ushangae.” “Nishaanza kushangaa.” Sabrina akajibu. “Unashangaa wakati mambo ndio yanaanza!” “Kwa hiyo hapa bado?” Sabrina akazidi kucheka. “Nakwambia tulia mtoto wa kike, upendwe.” Sabrina alicheka mpaka akarudi kukaa. “Sabrina napendwa mimi! Umesikia Keiline? Mama anapendwa.” “Na anaahadi yakupendwa mpaka ashangae.” Akaongeza Jack na kuelekea jikoni, akamuacha Sabrina akicheka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Jack ameondoka jijini bila kumuaga mama yake kitu ambacho hakijawahi kutokea kwa wapenzi hao. Amemuacha Mama Msindai akiumia, akiona Sabrina na wanae wakizungu, wamempora mapenzi ya kiziwanda wake. Na mama Msindai anasifa ya kutokukubali kushindwa.

Usikose Muendelezo kujua kitakachojiri.

 Katikati ya ugomvi wa mama mkwe, msomi, mwenye uelewa wa mambo, Je, Sabrina atafanikiwa kupendwa mpaka kushangaa?

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment