“Mama
Msindai unataka kuanzisha jambo wewe!”
Kwa mara ya kwanza wakamsikia Jacinta, dada mkubwa akizungumza. “Jambo
gani? Si nasema ukweli?” “Jamani acheni mimi niondoke. Sitaki matatizo na Jack.
Nilichukua majukumu kumsaidia Pendo kuandaa shuguli ya leo. Nimefanya kwa
uaminifu kabisa. Nimekamilisha. Sitaki mniingize kwenye matatizo.” “Kama unajua
haya ni matatizo wewe Jacinta, kwa nini umkimbie mtoto wakati huu anapohitaji
tumsaidie?” “Naomba nikusaidie mama, pengine utasaidika. Kwanza kabisa, Jack si
mtoto. Ni mtumzima sana, mwenye akili na utashi wake. Kingine, Jack alizungumza
na sisi wote kabla ya kumuoa huyu binti. Aliongea kwa hekima na ukali kuwa huyu
binti ndiye chaguo lake. Anamtaka Sabrina vile alivyo na hao watoto wake.
Alilisema hilo wazi. Kama mkiwa wakweli, mtakiri Jack si mkurupukaji wala
mjinga. Lasivyo angeshaoa zamani sana, nyinyi ni mashahidi. Sally anamtaka huyo
Jack hata leo. Kumuoa huyu binti ni chaguo lake Jack.” “Sio chaguo, wamemchezea
mwanangu.” Akabisha mama Msindai.
“Kama
ingekuwa kuchezewa, hizi sifa zote Jack anazoimba juu ya mkewe zisingekuwepo
jamani! Acheni kuanzisha mambo mnayojua yatavunja amani. Jack amekiri kwetu
sisi wote juu ya huyu binti. Ameapa hakuna anayemjulia yeye kama huyu binti.
Leo Jack yupo kwenye vyombo vya habari anakiri wazi ni sababu ya mkewe. Jack
ameitwa bungeni, kuzungumza na wabunge, mwenyewe amekiri kwetu ni kwa sababu ya
kile anachokifanya Sabrina huko Singida. Jack anamwambia Junior, yeye ndiye
anayepata sifa lakini anayewajibika ni mkewe. Amekiri Jack zaidi ya mara moja
na nyinyi ni mashahidi. Sasa najiuliza, kama huyu Jack amelogwa huku
akitumikiwa na mke wake, na kuhakikisha Jack anafikia ndoto zake, tatizo ni
nini jamani!?” Jacinta akaongea kwa kuumia na sauti ya chini asisikike.
“Kama
wewe mama umeshindwa kuwapokea hawa watoto, ondoka kimya kimya, mwache Jack mwenyewe
na mke wake.” “Hawa watoto wakizungu hawawezi kunitenganisha na mwanangu.”
Sabrina akaumia sana. “Sasa nakuambia ukweli kabisa mama Msindai. Wewe ni mama yangu,
kwa hali niliyomuona nayo Jack leo akitoka na hao watoto huko leba. Jinsi
alivyowashika na kuwatambulisha hapa kwetu kuwa ni binti zake kwa furaha na
sifa zote, ni lazima ufanye uchaguzi tena nasikitika huna muda. Lazima uchague
kwa haraka. Ni ukubali kuwa ni watoto wa kizungu na ni wa Jack, ili uwepo
kwenye maisha ya Jack au uwakatae hao watoto, Jack akuone au hata akuhisi tu,”
“Atafanyaje?” Akauliza kibabe mama Msindai.
“Unakumbuka
alichotuambia siku alipokwambia au alipokuja rasmi Dar kutuambia kuwa Sabrina
ni mjamzito, lakini anataka kumuoa hivyohivyo. Unakumbuka hii hali hapa
ilikupata siku ile, ukawa mkali sana kwake na kwa Junior? Unakumbuka maneno ya
Jack?” Kimya. “Sasa wakati wewe na Jena mnazungumza mnachozungumza hapa, naomba
msaidiane kukumbushana. Na kama mmesahau, mkumbuke sasa hivi tupo hapa kwa
kutaka kwetu. Jack alikusudia kuachana na Msindai kabisa, awe na Sabrina. Kwa
amani kabisa akisema asiwatie aibu kama wewe mama ulivyokuwa ukigomba. Akataka
kuondoka arudi Singida kwa Sabrina, baba akamrudisha, wote tukasema tutakuwa
naye.” Sabrina akashangaa. Hakujua kama Jack alipambana na upinzani mzito hivyo!
Jack hakuwahi hata kuzungumzia hilo. Sabrina akaumia sana.
“Mimi
nashauri tu jamani, muwe makini. Ngoja mimi niangalie watoto, nitoke hapa
nikahangaike na ya kwangu. Sitaki kujihangaisha na ya Jack. Maana kwa muonekano
tu, Jack anaonekana mwenye furaha sana kuliko nyinyi. Ingekuwa mimi ni mwanangu
yupo na furaha hivi, kama ni kulogwa, ningefurahia.” “Si kwa kuwa huna mtoto
ndio maana!” Akaongeza mama Msindai kwa jazba akimkashifu mwanae. Wakamsikia
Jacinta amecheka tu. Akasimama.
Baada
ya muda kidogo Pendo na Sabrina wakasikia hatua za miguu zikisogea hapo. Wakajua ni
Jacinta. Pendo mwenyewe alikuwa akitetemeka kwa kuingiwa na hofu kwa kile
alichosikia. Sabrina akabaki kimya amefunga macho kitandani. Kisha wakasikia na
wa nje wanaondoka. Mama Msindai na Jena hata hawakuingia ndani. Kimya. Ndipo akaingia
dada mkubwa, kiongozi wa usalama wa Taifa. Ukimuona na harufu yake tu, akiwepo
sehemu utajua ipo neema.
“Kina
shangazi wamelala?” Akanong’ona Jacinta akisogelea upande wa vitanda vidogo vya
watoto vilivyokuwa vimewekwa pembeni ya kitanda cha mama yao. “Naona hawa hawatamsumbua
mama yao. Walalaji.” “Sasa kabla hawajaanza kiswahili kirefu, nipige nao picha
ili wakianza tu, niwakumbushe walipotoka.” Pendo akacheka na kumshikisha wote
wawili. “Sasa kwa pozi hili, nipige na nichukue video kidogo.” Pendo akacheka
na kuchukua simu ya Jacinta mwenyewe. Akampiga picha kadhaa. Mara ambusu huyu,
picha. Akambusu na mwingine, picha. Akachukuliwa sasa video. “Haya, nyinyi
warembo wa Jack na Sabrina, mimi anti yenu Jacinta. Mnapokuja kuwa mawaziri,
msinisahau mkajidai hamnijui. Nitawajia na fimbo huko bungeni.” Mpaka Sabrina
akacheka. Wakamgeukia, Pendo na Jacinta na wao wakacheka. “Kwani wanakawia
hawa! Utashangaa wanakwambia, ‘kama tulikuona sehemu vile! Au tumekufananisha?’
Hapo ndipo fimbo zitakapoanza.” Kidogo Sabrina na Pendo wakacheka.
“Asante
mwaya Pendo. Acha niwaache walale, wasije wakaamka sasa hivi, mama yao akaanza
ulezi wa shida leoleo.” Pendo akampokea mmoja. Wakawaweka kitandani. Jacinta
akamsogelea pale kitandani. “Hongera na pole Sabrina.” “Asante, nashukuru kwa
kila kitu wifi yangu.” “Wewe lala, asubuhi tunakujia na uji, mtori na kila
chakula ili maziwa yatoke.” “Nashukuru sana.” Jacinta akatoka.
Mama ni
Mama.
K |
ama waliopishana
na Jacinta, Sabina na mama yake nao wakaingia. Sabrina akaanza kulia. “Pole
mama. Pole sana. Hata hatukuwa tunajua. Jack ametupigia simu muda si mrefu.
Lakini nikamwambia Sabina, tusije mikono mitupu. Angalau tukoroge uji angalau
unywe. Kazi ya kusukuma watoto wawili si mchezo!” Ndio na Pendo akili zikamjia
kuwa huyo mzazi anahitajika kula. Mama ni mama. Hakuna hata mmoja wao aliyekuwa
akifikiria kula ya mzazi usiku huo, lakini mama yake kafika hapo na chupa ya
uji na chai ya rangi alimfikiria binti yake. Sabrina akaendelea kulia. “Inauma mama! Inauma si kidogo. Mpaka kamasi zilikuwa zikinitoka
bila kujijua, Jack ndio akawa anafuta!” Wote wakacheka. Mama yake akaenda
kumshika kwa upendo. “Pole sana mama, pole na hongera. Ndio umekua mama sasa. Furaha
ya watoto utakuja sahau uchungu wote! Utashangaa mwakani unarudia tena.” “Weee mama! Si mwakani. Labda baada ya miaka mitano au
sita.” Sabrina akapinga. “Sawa.” Mama yake akafanya wakacheke tena vile
alivyokubali kwa haraka.
“Nimefurahi
mmekuja mama.” “Niambie, ulipata sana shida?” Akauliza mama yake akimshika
tumbo. “Pale mwanzoni kabla sijaingia leba na nilipoanza na wa kwanza ndio maumivu
yalikuwa makali sana. Lakini Keiline, kama niliyepewa! Daktari anaongea,
akashangaa ametoka, wala sikusukuma sana.” “Huyu wa pili anakuwa anapita
alikokwisha fungua njia mwenzie. Yaani nyonga zote zilishafunguka. Halafu
unakuwa ushapata maumivu yote, kwa hiyo pale anapokuja mwenzie, hakuna jipya.”
Mama Sabrina akamfafanulia mwanae. “Pole na hongera Sabrina. Umekuwa mama sasa.”
“Asante dada.” Sabrina akaitika.
Mara
William akaingia. “Tumefika kwenye gari zikaanza stori za mzee Msindai wakati
tunamsubiri mama. Tukaanza kazi yakucheka tu mpaka mama akaja. Ndio wameondoka
muda si mrefu.” “Oooh! Naona tumepishana.” Akaongea kwa kulalamika mama yake
Sabrina, asijue yaliyosemwa hapo. Wakasalimiana na William. “Mimi niwapokeee
ulezi jamani. Mkapumzike. Hapa mimi ndio nimefika.” “Kweli mama!?” Akashangaa
Sabrina. “Kabisa. Ndio wajukuu zangu wa kwanza hao! Acha nishike.” Akawasogelea
pale kitandani, wakawa wamefunikwa vizuri na kufunikwa mpaka vichwa.
Wakabakizwa uso tu. Mama Sabina akawaangalia kwa furaha asiamini kama na yeye
ni bibi. “Naona umenizalia wajukuu wa nguvu! Weupee!” Akaongea kwa kufurahia
mama Sabrina huku akiwatizama kwa upendo asijue watoto wamebeba damu ya kiitaliano.
Wakacheka tu kwa furaha.
“Natamani
niwashike, lakini hivyo walivyolala, sitaki kuwasumbua.” “Naona si waamkaji hawa
mama. Tumebeba na kubeba, lakini wapi! Sabrina naona amependelewa na Mungu
huyu, amepata watoto watulivu!” Pendo akaongea. “Lakini wakati wakuzaliwa
walilia kama kengele mpaka mimi na Jack tukawa tunasema hakuna kulala.”
Sabrina akaongeza taratibu. Wakacheka
kidogo. “Lakini hata wewe Sabrina ulikuwa mtoto mkimya sana. Hukusumbua wakati
mchanga.” “Sasa nani aliyesumbua mama na wewe?” “Mmmmh!” Wote wakacheka baada
ya mama yao kuguna tu bila kujibu. “Kwa maana nyingine yupo aliyekuwa mlizi?”
Sabina akaendelea kuuliza. “Mimi sijamtaja mtu.” Wakaendelea kucheka.
“Sasa
mwali wangu! Nikuletee nini kesho?” Pendo akamsogelea Sabrina, Sabina na mama
yake wakasogelea watoto. Sabrina akaanza kufikiria nini chakuletewa. Akakumbuka
nguo za watoto wake. “Kesho tuwatoe kwenye hizo za hospitali.” Wakacheka. “Basi
nitawaletea vitu vyao.” Pendo na William wakaaga, wakatoka.
Hapo
hapo mama Sabrina akamuwekea uji. “Kunywa ndio ulale. Usilale na tumbo tupu.
Kazi ya kusukuma sio mchezo! Na wakiamka hao watataka kunyonya. Kula ushibe.”
“Afadhali mama yangu, hapa nilikuwa nasikia njaa!” “Umeona Sabina? Ulikuwa
ukinikatisha tamaa bure. Ona uji umemfaa mzazi.” Wakaendelea kuzungumza wakiwa
wamemzunguka mzazi. “Sasa mama kama wewe unalala, bora mimi nirudi nyumbani
mapema, kesho niwahi kurudi nije na vitu vyako wewe na chakula cha mzazi.” Hilo
likawa jambo jema. Kwa asili Sabina alijua kumjali mama yake. Hakuwa akitaka
mama yake aonekane vibaya. Hata kwenye hiyo baby shower alimpendezesha
mama yake. Alimnunulia nguo nzuri na akampeleka saluni. Ukweli alipendeza na
yeye akafanana na wamjini. Sabina akaondoka, akawaacha hapo.
Kwa Junior.
P |
endo na
mume wake walipotoka tu, Pendo akaanza kumsimulia Willy kila kitu. Yote
aliyoyasikia mama Msindai akizungumza juu ya Sabrina na watoto wake. William
akashangaa na kuumia sana. Hapo hapo akampigia simu Junior. “Samahani kaka!” “Hamna shida. Kwema?” Junior akapokea
akisikika akiwa kitandani tayari. “Nina ombi ambalo
naona lisisubiri.” William akaendelea. “Karibu.”
Akaitika Junior, mtoto mkubwa wa Msindai. William akamueleza yote aliyosimuliwa
na mkewe. Usingizi ukampaa Junior kwa mshituko. “Unauhakika
Sabrina mwenyewe amesikia?” Akauliza Junior akisikika akitamani jibu la
‘hapana’. “Labda nikupe Pendo mwenyewe.” William
akamkabidhi simu Pendo.
“Haikuwa nzuri kaka. Mwenyewe niliishiwa nguvu.” “Subiri kwanza
Pendo. Unauhakika Sabrina alisikia kila kitu?” “Kabisa. Kwa kuwa tulikuwa naye.
Binafsi nashauri uzungumze na mama, pengine kwa sasa awe makini na kila
anachozungumza. Swala la ujauzito wa Sabrina kabla ya ndoa, halikuwa kificho
kaka. Aina ya watoto aliozaa, nina uhakika na yeye amejua leo. Hili jambo la
baraka tusiliharibu. Mimi nalilia watoto, hata nikipewa wekundu nitapokea tu.”
Pendo akaanza kulia na yeye. “Ni hilo tu kaka. Mama
asilazimishwe kufanya jambo jingine la Sabrina. Hata leo ukumbini haikuwa
vizuri sana, alitaka kuharibu haswa, nafikiri Joy atakusimulia. Ilibidi Jacinta
awe mkali sana kwake, ndipo akatulia. Nafikiri apewe muda mpaka awe tayari na
Sabrina. Ni hilo tu.” Akarudisha simu kwa William. “Ni hayo tu kaka.” “Nashukuru kunitaarifu, ninakwenda
kuzungumza naye sasa hivi.” Junior akakata simu.
Kwa Sabrina.
H |
uku kwa
Sabrina akajua alishaachwa. Muda ulizidi kwenda bila yakumuona Jack kurudi
wakati alimwambia atarudi baada ya muda mfupi. Yale aliyoyasikia kutoka kwa
mama yake, akajua wamekutana huko nyumbani, amemuingizia kichwani, mpaka Jack akajiona
hastahili kuwa pale. Sabrina alikula vizuri, akashiba, lakini usingizi ukagoma
kuja. Akajifikiria ndio anarudi kwao na watoto wasio na baba! “Mungu wangu
nirehemu!” Akajikuta akiongea nafsini kwake baada ya kufikiria kurudi tena
kwao, tena safari hii na watoto wawili! Akabaki amefunga macho ili kumuaminisha
mama yake kama amelala ili na yeye alale, lakini alishakosa amani. Manesi
walikuwa wakipita kumwangalia yeye na watoto, kila aliyeingia Sabrina alidhani
ni Jack, lakini ikawa sivyo. Masaa yakazidi kuyoyoma bila Jack.
Akakumbuka
historia yake na wanaume. Hakuna mwanaume aliyekwisha kuwa naye, aliyewahi
kumfanikisha kwenye yake, akarudi kwake. Kumbukumbu zikamrudisha mpaka kwa
Emma, akaja Tino aliyemuacha kikatili zaidi kuliko hata Emma! “Heri Emma
aliondoka na mali zake kuliko Tino aliondoka na roho za wanangu!”
Akaendelea kuwaza Sabrina. Ndio Jack sasa. “Jack ameshakuwa mashuhuri. Mambo
yake yanamuendea vizuri sasa hivi. Na yeye hanihitaji tena. Hana sababu ya
kurudi tena kwangu.” Sabrina akawaza akilia moyoni kwa hofu. “Naomba usiniache Mungu wangu. Nitakwenda wapi na hawa
watoto wawili?” Sabrina akaanza kumkumbusha Mungu kuwa alishamkabidhi
hao watoto tokea ameachwa Moshi peke yake. “Naomba
usiwaache wanangu, Mungu wangu. Kumbuka maombi niliyokuomba.”
Sabrina akaendelea kumkumbusha Mungu moyoni mwake kana kwamba Mungu analo
tatizo la kukumbuka, mwishoe uchovu wa shuguli nzima ya baby shawer ya siku hiyo kuanzia maandalizi aliyoanza na
Pendo alfajiri siku hiyo mpaka usiku huo amezaa hao mapacha vikamfanya asinzie
katikati ya maombi.
Kwa wazazi.
J |
unior
anafika mlangoni kwa wazazi, akasikia Jack akigomba sana huko ndani. Baba yake
akamfungulia mlango. “Huna haja kuwa karibu na mimi na mke wangu, mama!
Sijalazimisha hata mmoja wenu hapa, na ninaomba msiniharibie amani ya nyumbani
kwangu. Kama nyinyi mnashindwa kuungana na mimi katika hili, kaeni pembeni
sitalazimisha mtu.” Junior aliingia na kumsikia Jack akifoka, baba yake, Jena na
Jacinta nao walikuwepo. Akashangaa wote wapo yeye hajui kama kuna kikao. “Ni
nini kinaendelea ambacho mimi sijahusishwa?” “Mimi simo Junior. Nimefika
nyumbani kwangu nikagundua nina zawadi nyingi na zamuhimu alizopewa Sabrina
kwenye baby shower yake. Nikaoana nisilale nazo, pengine atahitaji akiwa
hospitalini au niseme wakati huu. Maana vingi ni vya watoto wa umri wa 0 mpaka
miezi mitatu. Ndio nakuja hapa, nakutana na yaleyale niliyomkataza mama na Jena
kule hospitalini.” “Tafadhalini msiniingize.” Jena akaruka.
“Unafanya
nini hapa nyumbani muda huu na wewe huishi hapa, kama si upo hapa na mama ili
kuzungumza na Jack?” Jacinta akamuuliza
huku amemtolea macho. “Na mimi nimekuja kushusha mzigo.” “Sawa dokta Msindai!
Lakini mimi niliwaonya, na nipo hapa kuwashuhudia mkivuna nilichowatahadharisha
pale hospitalini.” Akaongeza Jacinta. “Na kwa taarifa yenu tu, Sabrina
amewasikia mambo yenu yote mliyokuwa mkizungumza pale nje hospitalini.” Junior
akaongeza na kumshitua sana Jack. “Juu ya nini!?” Jack akauliza kwa kuhamaki.
“Ndio
maana nipo hapa usiku huu. Naomba ukae Jack.” “Nataka kuondoka kaka. Nimemuacha
mke wangu na watoto kwa muda mrefu. Nilikuwa naoga na kumbembea yeye vitu,
wakati natoka ndio mama akanipigia kuniomba nimsubiri hapa. Akitaka kunifungua
macho.” Junior akatingisha kichwa kwa kusikitika sana. “Najua sasa hivi
hamuwezi kunielewa kwa kuwa fahamu zenu na nyinyi zimefungwa.” Akaongea mama
Msindai.
“Mimi
nikuombe kwa heshima kubwa sana mama.” “Najua unachotaka kusema.” Akajibu mama
yake kwa jeuri. “Basi naomba niongee na wengine wanisikie. Hata Jacinta naomba
nivumilie sitachukua muda mrefu.” Jacinta aliyekuwa amesimama atoke, akakaa. Jack
akakaa. “Samahani baba, naongoza kikao nyumbani kwako.” “Wewe endelea tu.” Baba
yake akamruhusu, Junior akashukuru.
“Naelewa
kwa sehemu sitofahamu ya mama na wengineo. Inamuhitaji Jack mwenyewe kupita
anakopita na kuwa na amani na uwezo huo wa utulivu na kuchukuliana. Hatuwezi
kuepuka huo mshituko wa kuzaliwa watoto wakizungu katikati yetu.” “Asante
mwanangu Junior.” Akashangilia mama Msindai. Jack akawa ametulia tu. “Maana...” “Lakini! Lakini! Tafadhali mama,
naomba nimalize.” “Hiyo ‘lakini’ itaanza kutukorofisha.” Mama Misindai akamtisha
Junior.
“Mwache
amalize. Mpe nafasi tumsikilize kama wewe tulivyokusikiliza wasiwasi wako wote.”
Akaingilia mzee msindai. “Asante baba.” Junior akashukuru na kuendelea.
“Mwanzoni kabisa, Jack alikuja hapa nyumbani kwa heshima ya hii familia.
Akatutaarifu juu yakumuoa Sabrina ambaye tayari alikuwa mjamzito. Nafikiri wote
mnakumbuka nini kilitokea.” “Asante Junior. Na hilo niliwakumbusha mama na Jena,
muda mfupi sana kule hospitalini. Nikawakumbusha vile Jack alivyokuwa akitaka
kuondoka hapa akaendelee na taratibu zake na mpenzi wake, kuepusha hii aibu
mnayolalamikia leo.” “Sawa sawa Jacinta.” Junior akakubali.
“Sijui
siku ile mama ulikubali kwa umbali gani na...” “Sio kwa watoto wa kizungu jamani!”
Akaingilia mama Msindai. “Sawa sawa mama, hilo limesikika na kueleweka
waziwazi. Ugumu uliokuwa nao umeongezeka zaidi kwa aina ya watoto waliozaliwa
leo. Lakini naomba kuweka angalizo na msisitizo hapo. Msiumize hisia za watu.
Hawa watoto waliozaliwa leo, ni kazi ngumu aliyofanya Sabrina. Kuanzia siku ya
kwanza anabeba mpaka hivi leo.” Mpaka Jack akalia. “Asante
kaka.” Akashukuru Jack kwa uchungu sana. “Tafadhali tusilisahau hilo.
Huyu mama ametoka kuzaa watoto wawili ndani ya nusu saa kama nilivyosikia
ripoti aliyokuwa akipewa baba.” “Ndani ya dakika 18.” Akarekebisha mzee
Msindai.
“Ewaa!
Tafadhali ndugu zangu, nawasihi na Mungu atusaidie, msisahau hilo. Huyu Sabrina
ana vidonda vibishi kabisa. Hata watoto wake hawajanyonya, kweli mnamfuata
sehemu kama ile, hajawaita wala hajalazimisha mtu kwenda pale, mnakwenda
kumwita mshirikina!” “Huwezi kuwa umekwenda kuzungumza hayo maneno kwa mke
wangu mama!” Jack akashituka sana. “Kwani mimi nilijua kama anasikiliza? Na
mimi ni mama, nina haki ya kuzungumza juu ya mwanangu.” Akajibu kibabe mama
Msindai.
“Mimi
hilo sipingi mama. Lakini si pale. Usimfuate, mwache.” “Nakwenda alipo mtoto
wangu.” “Mbona ulikuwa pale wakati Jack hakuwepo, mama? Hujampokea Sabrina
moyoni, si kwa hawa watoto aliozaa leo. Hata kabla hukuwa umempokea. Mwache.
Mtoto ambaye unamtaka uwe naye karibu, si mtoto huyu mama. Tafadhali fungua macho
na uelewe Jack si mtoto.” “Na hilo nilimwambia mama.” Akaongeza Jacinta.
“Jamani Jack si mtoto. Baba na mama, Jack ni mtu mzima sana na anamaamuzi yake.
Yanaweza yasilete maana kwetu, lakini haina maana amelogwa jamani!” “Unajuaje?”
Akauliza mama Msindai.
“Kama
hivyo alivyo amelogwa, basi inabidi wanaume wote walogwe na wake zao, mama!
Jack anafuraha. Wote tumemuona jinsi anavyokuwa na mkewe. Jack anampenda mke
wake. Mke wake anahangaika mchana na usiku akimuhangaikia Jack mpaka Jack anashangaa!
Sabrina na tumbo la mapacha, anahangaika kumsaidia mumewe kwenye mambo ya chama
ili Jack atulie kazini.” Jack akainama na kulia kwa uchungu sana. “Leo Jack
anavuma kwenye siasa, kwa muda mfupi sana Sabrina alipoingia kwenye maisha
yake. Sasa kama anamloga na kumuhangaikia hivyo, ubaya upo wapi jamani?” Junior
akauliza kwa kuumia sana.
“Eti
jamani? Bora lipi? Kulogwa na kutumikiwa au kutologwa na mwanamke anakupinga
katika kila kitu? Wapo wanawake wanaojiita wacha Mungu, nyumba zao hazina amani.
Jack amejawa furaha, ametulia kwake. Kazini amefanikiwa, kwenye mambo ya chama
pia anashamiri. Leo Jack anakuwa gumzo kwenye vyombo vya habari sababu ya kazi
kubwa wanayofanya na Sabrina. Nyinyi kama wazazi mnataka nini kitokee kwa huyu
kijana wenu?” Junior akawauliza akiwatizama wazazi wao kwa zamu.
“Jamani,
mnakumbuka sura aliyotoka nayo Jack kule leba akiwa ameshika watoto wake?”
“Asante Junior.” Akaongeza Jacinta. “Mnataka kuona nini kwa Jack jamani!
Mnawezaje kumpokonya furaha ya ajabu kiasi kile na kumfanya mnyonge, aliye, huyu
baba, mume ambaye anategemewa sana sasa hivi na Sabrina ambaye amekuwa
akisimama naye!? Msijisahau jamani, Jackson Msindai anasifika zaidi sasahivi
sababu ya mkewe. Jack mwenyewe amekiri mpaka bungeni akimshukuru mkewe!” Junior
anakumbusha, asijue hicho ndicho kilimuuma mama Msindai na kumchukia Sabrina
zaidi. Kiziwanda wake anamshukuru Sabrina hadharani na si yeye! Hapo ikajengeka
chuki wala si upendo kwa Sabrina.
“Sasa
hivi ambapo alitakiwa awe pale na watoto wake na mkewe, yupo hapa akijibu
shutuma kama hajalogwa! Kweli?” Junior akauliza akitizama kila mmoja wao. “Mimi
binafsi sidhani kama ni sawa ndugu zangu. Jack anapo kwake na ana maisha yake.
Mwacheni aishi maisha aliyojaliwa na Mungu. Sisi ni wakristo. Mama wewe unaomba
sana, muombee kama kuna linaloendelea, Mungu amponye. Lakini kama sio hivyo,
waacheni. Msifike alipo yeye na familia yake. Waacheni kabisa. Kwa kusema
hivyo, naomba niwaombe Jack aondoke sasa hivi arudi hospitalini kwa familia
yake. Yule binti atakuwa na wasiwasi sasa hivi. Naomba Jack aende.” Junior
akahitimisha.
“Naona
kaka amezungumza mengi na yanatosha. Sina nyongeza. Watoto wale wakizungu ni
wangu na watafanyika sehemu ya maisha yangu. Ili msimuumize mke wangu, naomba
mimi niwaage rasmi. Kama mtaweza kunitumia mizigo yangu na zawadi zetu Singida,
nitashukuru. Nikiona kimya baada ya siku 10 kurudi Singida, nitaanza kununua
mimi mwenyewe vile ninavyohitaji, zaidi vya watoto wangu. Naomba niwahi kama
kaka alivyoshauri.” Akasimama akarudi chumbani kwake.
Baada
ya muda wakamuona anatoka na mizigo yake na mkewe. “Naona vitu nilivyonavyo na
mimi kwenye gari ni muhimu Jack. Vichukue usiache. Ni vya watoto wa umri huu.”
“Nashukuru.” Jacinta naye akasimama. “Usiku mwema jamani. Natoka kumkabidhi
Jack vitu vyake, ndio na mimi nitakuwa nakwenda kupumzika moja kwa moja. Usiku
mwema.” Bila kusubiri Jacinta akatoka. Junior naye akasimama na kuondoka bila
kuaga.
“Nikusaidie
nini?” Wakamsikia Junior akiuliza nje. “Kwa sasa nahisi sijui nimechanganyikiwa
tayari! Sikumbuki tena.” Wakamsikia Jack akiongea kwa kulalamika. “Nashauri
uende ukatulie, ukikumbuka andika, kesho ukirudi hapa utajua nini chakubeba na
kuacha.” “Naona nifanye hivyo.” Jack akaafiki. Jacinta na Junior wakasaidia
kumuhamishia vitu kwenye gari, Jack akaondoka.
Hospitalini.
A |
kiwa
usingizini Sabrina akahisi mtu amembusu mdomo. Akashituka sana na kufungua
macho. “Jack!” Akaongea kwa kunong’ona akiwa haamini kama kweli ni Jack au yupo
usingizini. “Pole, nimechelewa kurudi.” Jack akambusu tena.“Nilidhani hutarudi tena!” Machozi yakaanza kumtoka
Sabrina. “Niende wapi bila wewe Brina? Na wanangu nao?” Sabrina akajifunika
nakuzidi kulia taratibu. “Utakapokwenda na mimi ndio hapo nitakuwepo mama. Wala
hutanikwepa kirahisi hivyo.” Jack akaendelea kuzungumza naye taratibu
akimfariji. Mama yake Sabrina alikuwa amelala kwenye kiti cha pembeni karibu na
wajukuu, akawa anasikiliza, kidogo maswali yakaibuka ndani. “Kwa nini awe na
wasiwasi mumewe asirudi tena?” Akajiuliza mama Sabina, lakini akaona
anyamaze.
Akambembeleza
mkewe kwa mabusu ya hapa na pale mpaka Sabrina akatulia. “Warembo wa dady
hawajaanza kulia?” Jack akawasogelea. “Naona walalaji hao! Mama amenipa
nijaribu kunyonyesha kabla njaa hazijawaanza wakalia kwa pamoja nikiwa sina
maziwa, na pia alitaka waanze kuvuta ili maziwa yaanze kutoka, lakini wapi.
Tumebembeleza wee, naona kila mmoja ameridhika hapo.” Jack akamnyanyua Jeiline.
Sabrina akamuona anambusu. Akamuweka vizuri. “Dad amerudi, ameleta zawadi
nyingiii, kwa ajili yako na mdogo wako.” Akaongea Jack kwa sauti ya chini. Akambusu
tena na tena na kusogea naye pale kwa Sabrina. “Hapa mama ulinzi lazima uwe
mkali!” Sabrina akacheka. “Na ukali utaanza kuongezeka. Ukaribu na vijana
wasiooa mwisho. Eti Jeiline? Dady atafuga mbwa wengiii ili alinde warembo wake?”
Akaendelea kuzungumza naye taratibu, akakaa pembeni ya kitanda.
“Vipi
lakini wewe? Maumivu yameisha kabisa?” “Wamenipa dawa ya maumivu, sasa hivi
nipo sawa labda nikikaa ndio naumia sababu ya mshono. Lakini nipo sawa. Na kwa
kuwa upo hapa, nahisi nitalala.” “Pole. Nilikuwa nakusanya vitu vyetu na vya
watoto. Jacinta naye kanijazia gari kwa ajili ya vitu vyao hawa, vya umri huu. Nikazidi
kuchelewa. Nataka ukiruhusiwa tu, turudi nyumbani kwetu.” “Nilifikiri nitarudi
naye huyo nyumbani na wajukuu angalau hata wakomae kidogo.” Jack akasimama.
“Pole
nimekuamsha mama.” “Hapana. Kulala ngumu sababu ya furaha ya wajukuu baba.
Kuona kizazi cha pili ni baraka mwanangu. Hapa nipo kama siamini! Natamani
kukaa nao angalau mwezi.” Jack akacheka. “Nitachanganyikiwa mama yangu. Mwezi! Utanifanya
na mimi nihamie hukohuko Chalinze, mwishoe nitafukuzwa na kazi.” Sabrina
akajisikia vizuri. “Hawa watatu sitawaacha popote mama yangu. Nilipo ndipo na wao
watakapokuwepo. Lakini tutakuja kukutembelea wakikua kidogo.” “Sasa huko mnaye
msichana wa kazi?” Akauliza mama Sabina. Akaona wanaangaliana. Wakacheka.
“Tunae
dada mtumzima kidogo. Huwa anakuja kumsaidia huyu kazi na alituahidi kutuletea
msichana kabla Brina hajajifungua. Sasa tunahisi ni kama haweki juhudi katika
hilo ili awepo yeye mwenyewe kazini.” “Lakini sio mbaya Jack.” Sabrina
akaongeza. “Kweli sio mbaya, lakini kwa hivi umeshajifungua, tutahitaji
msichana hata wa usiku.” “Sawa sawa baba. Maana unahitaji kupumzika Sabrina.
Kujifungua sio kitu kidogo. Unaweza usione madhara kwa nje, lakini unahitaji
kupona ndani. Lazima upumzike kwa muda.” Wakanyamaza.
“Kwa
sasa lazima huyo apate msaada.” Mama Sabina akaweka msisitizo. “Nina siku za
uzazi na mimi, napata kutoka kazini. Kwa hiyo nitakuwa naye nyumbani. Hatakuwa
peke yake. Na zikiisha kama sijapata msaada mwingine wakumsaidia watoto, naweza
nikachukua likizo ya hata mwezi. Sitamuacha peke yake na watoto. Usiwe na
wasiwasi mama. Tutakuwa sawa tu.” Jack akajaribu kumtuliza, asijue nia na maombi
ya huyo mama ni kukaribishwa huko Singida akalee wajukuu. Wakatulia, Jack
akamrudisha Jeiline na kumchukua Keiline. “Hey little girl!” Wakamsikia
Jack akizungumza na huyo mtoto, akambusu na kurudi kukaa naye hapo kwa Sabrina.
“Nijaribu
kumnyonyesha tena? Angalau avute kidogo maziwa yaanze kutoka jamani!” “Basi
usikae, lala hivyo hivyo nikuwekee pembeni.” “We Jack! Mwanzio bado mwanafunzi,
sijawa mzoefu wa kunyonyesha.” Jack na mama yake wakacheka. “Kweli. Watoto
wenyewe ndio nafundishwa kushika vizuri na mama, leo ninyonyeshe nimelala! Si watapaliwa?”
“Si umesema maumivu makali ukikaa?” “Acha nijitahidi bwana. Ila asante
kunifikiria.” “Basi nyanyuka nikupangie mito huko mgongoni.” Jack akawa ameshika
mtoto mkono upande wa kushoto, huku anamsaidia mkewe upande wa kulia. Mpaka
Sabrina akakaa vizuri. Akampa mtoto.
“Mkune
miguu labda ataamka.” Mama Sabina akatoa wazo. Wakacheka. “Sasa wewe Jack kuna
miguu, mimi nimshikilie.” Mama Sabina akaanza kucheka na kusimama. “Mtoto huyo
mmoja utafikiri unanyonyesha jeshi bwana! Nilikwambia unapomnyonyesha
umkumbatie kwa mkono mmoja. Tumbo lake ligeuke kwenye lako kabisa mpaka apate
joto lako, ndipo anyonye.” “Sasa hapo ndio wanapolala sababu ya joto.”
Wakacheka. Wawili hao wakaanza kazi ya kunyonyesha. Akavuta titi la mama yake
kidogo, akalala. Kila Jack alivyokuwa akimkuna mguu, anavuta. Akiacha na yeye
anaacha. “Mimi naona tuwaache. Wakisikia njaa wataamka wenyewe.” “Naona hilo
wazo zuri. Sasa na wewe ulale. Ili wakiamka uwe umepunguza uchovu.” Jack
akashauri. Wazo likawa jema.
Jack
akamrudisha mtoto kwenye kitanda, akarudi kumfunika Sabrina vizuri. Akambusu
wee, kisha akamwacha alale. Na yeye akavuta kiti pembeni, akalala. Wazazi hao
walilala kama hawana watoto! Mama Sabina aliyekuwa karibu na watoto ndiye
akabaki akiangalia wajukuu. Jeiline akaamka karibu panapambazuka. Akambadilisha
diaper ndipo akampeleka kwa mama yake. Sabrina akashituka. “Amelia?” “Kidogo
tu.” “Nilikuwa nimechoka mama! Nimelala sina habari.” Sabrina akawa anakaa
taratibu asimuamshe Jack ambaye amelala kama yupo kitandani. “Ndio mlezi huyo!”
Sabrina akamsengenya kwa sauti ya chini, yeye na mama yake wakacheka. “Atakuwa
amechoka.” “Sana. Jana alikuwa na siku ndefu sana. Mwache alale, akiamka hapo
yeye ndio analea ili na wewe ukapumzike kidogo.”
Sabrina
akamuweka kwenye ziwa. Wakashangaa anaanza kunyonya kwa juhudi. Wakaangaliana.
“Amejisaidia huyo ndio maana naona tumbo limefunguka, amepatwa na njaa. Ngoja
nimwangalie mwenzie.” “Hata sikuwa na habari kama mnabadilishana. Asante mama.”
Sabrina akashukuru. Yule mama akapatwa maswali zaidi. Maana wakati
wakumbadilisha Keiline akamtoa soksi na kofia ikavuka pia. Akaweza kumuona huyo
mtoto kwa wazi kabisa, ana damu ya watu weupe. Tena kali haswa. Sura ilikuwa ya
Sabrina. Hilo akaliona, lakini walikuwa kama watoto waliozaliwa na baba na mama
wakizungu kabisa. Yule mama akawa hajaelewa. “Naona hivi anavyovuta anafanya
maziwa kusisimkwa. Na hili jingine linakuwa kama linataka kutoa!” “Safi sana.
Naona na wewe utakuwa na maziwa mengi kama mimi. Mimi yalikuwa yakimwagika
haswa kipindi nikinyonyesha. Basi madume yangu yalikuwa hayalii njaa.” Sabrina
akacheka. “Nasikia raha hivi anavyonyonya! Siamini kama ni wangu.” “Watoto
watamu!” Wakacheka taratibu wakati mama yake akimwangalia Jeiline. “Na yeye
amejisaidia?” Akauliza Sabrina. “Naona wamefanana nje na ndani. Wanafanya kila
kitu pamoja.” Wakacheka taratibu, wakati akiendelea kumbadilisha na Sabrina
akinyonyesha.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Ndio
mlezi unalala hivi!” Jack akaamshwa na Willy asubuhi hiyo ya saa moja. Wote
wakacheka. Jack ndio akasimama. “Haiwezekani kama pamepambazuka!” Sabrina
akabaki akimcheka. “Lakini watoto hawajalia bwana! Eti Brina?” “Nimenyonyesha
mwenzio mara mbili! Hapa maziwa yameanza kutoka kidogo.” “Acha utani! Mbona
hukuniamsha?” “Najua ulichoka, nikamwambia mama tukuache upumzike.” “Daaah!
Nilikuwa nimechoka haswa. Lakini mngeniamsha tu.” Wakaendelea kucheka, Jack
akaelekea bafuni na kimkoba chake kidogo.
“Vipi?”
Pendo akauliza. “Nimeanza ulezi mwenzio.” Wakacheka. “Lakini mama ndio ananiamsha
ninyonyeshe. Naona wazazi sisi tunahitaji kuzoea. Tukilala hapa, hata watoto
waamke hakuna anayeamka kati yetu. Nipo kama Jack tu.” Wakacheka tena. “Lakini
walikuja mkiwa mmechoka. Jana ilikuwa siku busy sana kwenu nyinyi wote. Na
hekaheka za leba, mlichoka.” Pendo akamfariji.
“Acha
nikapige mswaki ndio nije kula. Mdomo mchungu, mama alikuwa akinipa vyakula
usiku.” “Uzazi, lazima ule.” “Ni kweli mama. Anahitajika kula sana.” Akakubali
Pendo. “Au usubiri mwenzio atoke, nije kukusaidia kukusafisha kabisa kabla
wageni hawajaanza kuwa wengi?” “Naona hilo wazo zuri mama. Aoge kabisa,
wataanza kuingia wageni sasa hivi.” Pendo akakubaliana na wazo la mama Sabrina.
Sabrina hakuwahi kumuona mama yake akimjali kwa namna ile. Kwa mara ya kwanza
akapata mapenzi ya mama haswa. Alijituma huyo mama, Sabrina akabaki akishukuru
tu.
Wakati
Sabrina yupo bafuni na mama yake, Pendo naye akawa na kazi yakuvalisha watoto.
Walikuwa wadogo, lakini wakapendeza. Aliwavalisha nguo za rangi nyeupe tupu. Akawavalisha
na kofia zenye uwa la rozi la pinki kubwa juu. Sabrina alitoka bafuni na kuanza
kucheka. “Naona warembo wameshaanza kupendeza.” “Wakichangamka tu, tunawatoboa
masikio.” Pendo akaongeza. “Hapana. Sio sasa hivi.” Jack akajibu kwa haraka
sana, wote wakamgeukia. “Mnajua yale madude yanaota kwenye masikio sababu
yakutoboa?” Willy akaanza kucheka. “Mzee unayaogopa?” “Kabisa. Mnataka
kuwaharibu wanangu sura? Hamna haraka. Kwanza wenyewe wanapendeza bila hereni.
Hilo zoezi la masikio ni la baadaye sana.” “Basi kazi hawa watoto watakuwa nayo
kama ndio hivyo. Dad ndio ana mashariti hivyo!” Pendo akafanya wacheke, Sabrina
akacheka tu nakurudi kukaa bila ya kuongeza hapo.
“Mimi naomba nile kwanza ndio ninyonyeshe.”
Mama yake akamuwekea mtori. “Pendo, mama umepika vizuri, na unanukia vizuri!”
“Asante mama. Nataka atunyonyeshee watoto wakue haraka.” Wakacheka, stori
zikaendelea. Akaingia Junior na familia yake wote wamevaa vizuri. “Mnakwenda
kanisani nini?” Jack akauliza. “Yeap! Mzazi unaendeleaje?” “Nina kazi ya kula
tu shemeji yangu.” “Unanyonyesha lakini?” Joy akauliza. “Wanaringa hao! Lakini
nanyonyesha. Naona bibi yao anawapigania kweli. Hata nikiwa usingizini,
ananiamsha wajukuu zake wapate lishe.” Wakacheka. “Kwa ulalaji tuliomkuta nao baba
yao, sasa kama na mama mtu naye analala hivyo hivyo! Watoto watashinda njaa.”
Wakacheka. “Tulikuwa tumechoka bwana. Siku ya kwanza, leo tutakuwa makini.”
Jack akaongeza.
“Claire umependeza msimamizi wangu!” Sabrina akamuongelesha. “Huyo kwa watoto! Hapo haoni mtu humu ndani ni hao watoto tu.” Mama yake akaongeza. Claire akacheka. “Asante.” “Salimia bwana, vipi wewe?” Baba yake akamwambia. Akasalimia kila mmoja. “Ulisema nitapakata watoto dad.” Claire akamgeukia baba yake. “Sasa usinyonye vidole wakati umepakata watoto, utawaangusha bure.” Wote wakacheka. “Dad unamsikia Clei anaanza uchokozi wake?” “Wewe kaa hapo kwenye kiti, nikuombee kupakata watoto. Na uwe makini ili Clei aone wewe ni dada mzuri.” Akafurahi Claire, mama yake akamuweka sawa kwenye kiti. “Nataka kuwabeba wote.” Watu wote wakacheka. “Sasa hapo ndipo utawaangusha bwana! Anza kwanza mmoja, Jeiline. Mami wake akiona umemshika vizuri, atakuruhusu umshike mdogo wake Keiline.” “Dad, mwambie na asinyonye kidole akasahau mtoto.” “Utalia Clei wewe! Unataka kumliza mwenzio ashindwe kubeba watoto!” Mama yake akamtisha, Clei akacheka na kumsogelea Jack taratibu akijihami. Wote wakacheka.
“Anapenda kunichokoza kila saa!”
“Sasa na wewe ukianza kulia tu, anko anakunyima watoto.” Baba yake akamuwahi.
Akajifuta machozi. “Clei mchokozi dad!”
“Wewe usimsikilize. Nilikwambia ukiwa unalia tu ndio atazidi kukuchokoza. Wewe
usimsikilize. Haya futa machozi mama yangu, nikupe mtoto.” Wakazidi kucheka.
“Mlezi huyu atakuwa analia na watoto wanalia!” Pendo akanong’ona. Wakacheka.
Akapewa mtoto. Baba yake akachuchumaa mbele yake. “Ona ulivyoshika mtoto
vizuri!” Baba yake akamsifia. Claire akacheka. “Mimi ni dada zuri dad!” Clei
akacheka kama kumchokoza. “Sasa unanicheka nini?” “Nimekwambia usimsikilize.
Kweli wewe dada mzuri.” Wakampiga picha hapo, akafurahi.
Jacinta
akaingia. “Naona warembo wamepata mlezi.” “Dad amesema mimi dada mzuri, anti.”
“Hata mimi nimekukubali. Acha nikupige picha anti wangu!” Akafurahi Claire.
“Halafu umependeza Anti! Si sisi tunafanana?” “Sana. Tumefanana sana mpaka
nywele! Halafu na wewe umependeza sana Claire.” Akafurahia. Zikazidi stori humo
ndani. Sabina naye akaongezeka. Kila aliyeingia hapo aliingia na maua, na baloons.
Kasoro Sabina aliingia na chupa za uji. Chumba kikapendeza.
“Mimi
sijaja na chakula, maana Pendo aliniambia anakupikia vitu vingi, nikajua na
mimi nikileta asubuhi vitaharibika.” “Nashukuru kwa kujali. Nimekula mtori
mzuri sana. Si umependa Jack?” “Makubwa! Na wewe Jack umekula cha mzazi!?”
Jacinta akashangaa. “Sasa nile wapi wakati nalea hapa?” Wakacheka. “Tutoke
kidogo Jack.” Jack akakubali kwa haraka, akijua kaka yake anataka akazungumze
naye. “Sasa Jack?” Pendo akamwita wakati wanataka kutoka. “Vipi?” “Si
utaniachia bibi harusi wangu nimsaidie kulea watoto hata mwezi tu?
Wakichangamka tu hawa warembo, nakutumia.” Jack akacheka. “Siachi mrembo wangu
hata mmoja, Pendo. Nikiondoka hapa jijini, naondoa majeshi yangu yote. Mke na
wanangu wote. Tutarudi kusalimia, lakini hao, siachii mtu. Nilipo ndipo
watakapokuwepo.” Wakamtania kidogo, Jack
akatoka, Willy na yeye akafuata nyuma. Sabrina akajisikia vizuri, roho ikatulia
kabisa.
“Mama
na wewe kula. Halafu da Sabina naona umrudishe mama nyumbani akapumzike kidogo,
arudi baadaye. Hajalala usiku kucha!” “Hawezi kukubali kuondoka huyu. Muulize
mwenyewe.” Wakacheka. “Nakuhurumia!” “Jamani mama yangu. Sasa si utakuwa
umechoka sana? Kalale kidogo.” “Wala usijali. Nioge tu, nibadili nguo na kula
wakati hawa wamelala, nitakuwa sawa tu. Mkitoka hapa, ndio tutoke wote.”
“Nashukuru mama yangu. Asante.” Sabina akaingia na mama yake bafuni. Wakamuacha
Sabrina na Jacinta, Joy na Pendo wakizungumza.
Junior kwa
mdogo wake.
“Mpango
ukoje?” Kaka yake akamuuliza baadaya ya
kutoka hapo ndani na kuhakikisha wapo mbali kidogo. “Wakiruhusiwa tu hawa,
tunaondoka kabisa hapa jijini angalau tukapumzike sasa. Shuguli zote zimeisha, sasa
nikulea.” “Ukiruhusiwa leo na mkatoka jioni, ndio nauliza mtakwenda wapi?”
“Oooh! Nilifikiria hotelini, ili kumfanya apumzike kabisa, halafu kesho yake
ndio turudi Singida.” “Kwa nini hotelini!?” Akauliza Willy na Junior kwa
pamoja. “Nyinyi mlifikiria niende wapi? Maana nyumbani mama amekuwa muwazi
kabisa, hawezi kumpokea Sabrina na wanangu!” “Hata nyumbani kwangu!” Willy
akaongeza kwa mshangao. “Au kwangu!” Junior naye akaongeza.
Jack
akakaa sawa. “Fikirieni vizuri tu. Wala msifanye haraka. Mnafikiri mtakuwa
salama kwa mama Msindai? Yaani yeye amfukuze Sabrina na wanangu, leo aje ajue
nyinyi ndio mnawahifadhi?” Wakatulia. “Watu wake wote wa karibu wanajua mimi na
mke wangu tuko nyumbani kwake. Leo ijulikane hatuko kwake, tena nimeondoka bila
maelewano naye, halafu nihamie kwa mwingine! Mnamjua mama Msindai au mmemsahau?
Mtanunua ugomvi wote na hatakaa akawasamehe. Huu ni ugomvi wangu na mama, na
ndio maana mmemuona baba amenyamaza kabisa na kutotaka kuingilia. Mnafikiri ni
kwa nini?” Kimya. “Baba anamjua mama. Sisi tunaweza kuondoka kwenda Singida
maisha yakaendelea, huku nyuma vita ikahamia kwake au kwa mwingine.” “Bado
sidhani kama ni sawa kupeleka watoto wadogo hivyo hotelini Jack.” Junior
akaongea kama anayefikiria.
“Bora
ingekuwa ni kwa kina Sabrina, lakini si hotelini!” “Kule ni mbali kaka. Siwezi
kusafiri mpaka Chalinze na watoto, kwa safari ya usiku mmoja tu! Halafu kesho
yake tena turudi huku kwa safari ya kurudi Singida! Hapana, nitamtesa mke wangu.
Na nyumbani kwa Sabina ni padogo sana. Sioni sababu yakujibana. Nitakuwa sawa
jamani. Naomba muwe na amani.” “Daah!” Junior akasikitika.
“Hata
hivyo sitaki tena maneno maneno kwa Sabrina. Nahisi anasimangwa bila kosa!
Brina hanakosa kaka. Hajawahi kunilaghai, na wala si eti yupo na mimi kwa sababu
amekwama maisha. Mimi ndiye namuhitaji Brina kuliko hata anavyonihitaji mimi!
Alipogundua ni mjamzito, alikataa kuja Singida kabisa kaka. Nafikiri
nilikwambia. Akijua nipo kwenye mahusiano yangu na maisha yangu. Hakutaka hata
kuja ili asinichanganye. Sijamtoa Brina barabarani jamani. Nimemkuta na mipango
yake na watoto wake, ametulia vizuri tu kwenye Vila. Mimi ndiye niliyemfuata
Brina. Mimi ndiye niliyemuomba tuishi wote Singida. Na tulipofika Singida pia
aliponikuta na Pam, akaona haitakuwa vizuri aishi pale nyumbani kwangu, na Pam
akiwa yupo kwenye maisha yangu. Brina akaondoka. Sikuweza kulala kaka. Nilihisi
kuchanganyikiwa, na nilikuwa na Pam. Ile hali yakujua Brina yupo, na hayupo
kwenye maisha yangu, haijawahi kunifanya nikawa na amani. Tokea siku ya kwanza
namuona Brina.”
“Watoto
aliozaa Brina, nahesabu ni wangu kaka. Wawe wakijani, wawe bluu, ni wangu.” “Naomba
nikuulize Jack. Samahani lakini.” Willy akaomba kwa tahadhari. “Baba yao yuko
wapi?” “Nimemwapia Sabrina, kwa kuwa ameniomba ramsi, nisiwahi kumzungumzia
huyo mtu. Ameniambia mpaka kifo chake, hata hao watoto waje waulize yeye akiwa
hayupo, wakiwa wameambiwa na watu vinginevyo, lakini kutoka kwa mdomo wangu
ameniomba nisiwahi kumzungumzia huyo mtu kwao, japo mimi ndio mtu pekee
ameniambia ukweli wote. Kwa hiyo Brina mwenyewe ameniomba kwa kuniapisha kuwa tusiwahi
kumzungumzia huyo mtu kwa mtu na wala hawa watoto, hawatamjua baba mwingine ila
mimi.” Wote wakashangaa.
“Wao!”
“Hakika kaka. Amesema atakufa akiwatambulisha watoto wake kama ni wangu. Sasa
kwa bahati hiyo kaka, kwa mwanamke kama Sabrina, nawezaje kukataa au kubadilika?
Nitapata wapi mwanamke kama Brina? Binafsi napenda watoto sana, kaka ananijua.
Leo niambiwe nimepewa watoto wawili!
Tena wakike! Jamani msinitanie! Mwenzenu nahesabu nimeokota zaidi ya lulu.”
Wakacheka. “Kweli tena. Mungu anipe nini? Nishakuwa na wanawake jamani. Lakini
sijawahi kulala usingizi wa amani, kama nilivyokuwa na uhakika kuwa Brina ni
wangu. Ananijali haswa. Tunalala tukicheka. Nawezaje kupoteza hiyo furaha?”
Kimya.
“Sasa
ndio maana, mimi mwenyewe, nitamlinda Brina. Nitatunza amani ya nyumbani kwangu
kwa njia yeyote ile. Maneno ya kumuudhi, hayo sitaruhusu, hapo mtanisamehe.
Nitamchukua mke wangu na watoto, nitawapeleka sehemu nitakayojua watakuwa
salama na amani, kisha tunarudi Singida. Najua watu watasema sana tu, lakini
sitajali. Hata wangekuwa weusi, bado wangesema tu. Niliwapokea hawa watoto hata
nikiwa sijui kama wapo wawili. Nikaja kujua ni wawili, nikapata amani japo
Brina alikaribia kuchanganyikiwa.” “Kweli?” “Kweli kaka. Nimetembea na Brina
katika huu ujauzito nikimtia moyo mpaka sasa, sijisikii kubadilika, kwa kuwa
mwenyewe pia nawataka hao watoto.” Kila mmoja akavuta pumzi.
“Basi
wakati mnaelekea uwanja wa ndege, unitaarifu ili nimwambie Awali aje achukue
gari huko uwanjani.” “Hapo utakuwa umenisaidia kaka. Ila naomba muamini
nawashukuru sana. Nilihitaji watu kama nyinyi kusimama na mimi katika kipindi
hiki. Ibra ambaye ni rafiki yangu wa karibu, na yeye pia ameshindwa kabisa
kunielewa. Amekataa hata kuja kwenye harusi yetu. Lakini nimeamua kumuacha kama
mama, tutaungana baadaye. Mimi ndiye najua nahitaji nini.” Wakaendelea
kuzungumza.
Mama
Sabrina kwa Sabina.
M |
ama yake
akaoga hapohapo ndani kwenye chumba alicholazwa Sabrina na kubadili nguo.
Akataka kuteta na Sabina hapo chooni, lakini akajua watasikiwa. Akamnong’oneza
kuwa watoke, waage wanakwenda kwenye gari ili wakaweze kuzungumza kwa uhuru. Na
kweli wakafanya hivyo. Wakaenda mpaka kwenye gari, wakaangaliana na kuanza
kucheka. “Haya mama!” “Kwanza watoto ni wakizungu. Si weupe, hata. Wazungu
kabisa.” “Mimi nilihisi jana. Lakini nikasema nisiende mbali.” “Sasa sikiliza.
Wewe si uliondoka mumewe akiwa hajarudi?” “Ndiyo.” Sabina akaitika akitaka
kujua yaliyojiri usiku.
“Sasa
alikuja kurudi usiku sana kama kwenye saa 7 hivi, nikamsikia Sabrina akimwambia
alifikiri hatarudi tena.” “Mama! Kwa hiyo alimdanganya mwenzie mimba ni yake?”
“Mimi nikahisi hivyo. Lakini mumewe akamuomba msamaha wa kuchelewa, halafu
akamuuliza, ‘nisirudi niende wapi bila wewe na wanangu?’.” “Mama!” Sabina akashangaa
sana kama ambaye hasadiki. “Kweli tena. Sasa hapo ndipo nilipopatwa na utata.”
“Kwa hiyo inamaana mumewe anajua watoto si wake tokea mwanzo basi!” “Ewaa!” Mama
yake akaafiki na kuongeza. “Inamaana alimuoa akiwa anajua anayo mimba si yake.”
“Mmmh!” Sabina akaguna.
“Kwa
hiyo kwa ndugu wa mume kuwepo hapa mpaka leo, wakiona watoto wa kizungu, pia
walijua Jack anamuoa mwanamke mjamzito!” “Ndio maana yake mama. Sabrina
amebahatika!” Wakaendelea kuteta wasijue moto unao waka ndani ya familia hiyo. “Lakini
Sabina, inamaana huyu Sabrina alikuwa na mahusiano na mzungu gani!? Maana hawa
watoto sio mchanganyiko. Nakwambia utafikiri wamezaliwa na baba na mama wakizungu
kabisa!” Hapo ndipo mama yake akamfunga kumbukumbu kabisa huyo Sabina hata
asimuhisi Tino. “Itakuwa ni baada ya kuondoka huko kwa rafiki yangu,
alikokwenda kuanza maisha huko ndipo akapata mzungu. Na kwa kamwili kake hako
kembamba, rangi ile, lazima alivutia mzungu mmoja huko alikokwenda labda
wakalala mara moja, mzungu akaondoka, akamuacha na mimba.” “Au alifanya
mahusiano kabisa. Bwana Sabrina amebadilika! Sie Sabrina tunayemfahamu sisi! Atakua
aliishi na huyo mzungu kabisa akachukua vijitabia vya kizungu.” “Ulimuona hata
alipokuja kwenye mahari kabla hajaolewa?” Wakaendelea kuteta mpaka wakaona
Junior na familia yake wanapita kwa mbali kidogo, wakajua wageni wanaanza kuondoka.
“Nataka kwenda nao, nikalee vijukuu Sabina, mwanangu. Niombee kisomi. Mimi nimeshindwa.” Sabina akacheka sana. “Mama! Unataka kwenda mpaka Singida!?” “Sasa nisipokwenda kwa hili, nitakwenda kwa lipi mwanangu? Sina ninalolifanya huko Chalinze. Sasa hebu niambie, watu wajue nimekwenda mpaka Singida kulea!” Sabina akacheka huku akifikiria. “Na baba?” “Ataelewa kabisa. Namwambia nakwenda kumsaidia Sabrina watoto. Lazima atakubali. Na hivi anataka tujirudi kwa Sabrina, na naona amependa sana huyo Jack. Anasema anamthamini sana Sabrina. Kwa hiyo lazima atakubali tu.” “Sawa. Ngoja waondoke wageni wao na mimi nijaribu.” Wakacheka nakuanza kurudi ndani.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ø Kwa wa Nyumbani Sabrina Bado thamani yake iko juu sana, ikaongezwa
na msimamo wa Jack. Japo watoto ni wakizungu, lakini bado amesimama na Sabrina. Anamtaka mkewe na watoto wake. Mama yake Sabrina anaonyesha kuhitaji mahusiano naye.
Itakuaje kwao?
Ø Huku kwa Msindai Vita ya mama Msindai na Sabrina ndio imeanza rasmi. Sabrina amemchukua kiziwanda chake! Na sifa ya huyu mama hakubali kushindwa japo safari hii Jack ameonekana kumshinda. Hawezi kuishi bila Jack, na chuki inaongezwa zaidi na watoto wa kizungu wa Sabrina. Amekiri hao watoto hawatamtenga na mwanae. Umbali gani atakwenda kumrudisha mwanae upande wake? Usikose kufuatilia.
0 Comments:
Post a Comment