Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 24. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 24.

 Singida Tena, kama Mke na Mume.

Jack na Sabrina walirudi mjini Singida wakiwa wamejawa furaha. Kama mume na mke haswa. Wakipanga mipango inayoeleweka kama wanandoa. Wakiweka juhudi kwa kile anachokiamini Jack. Sabrina ndiye akawa kama mwenyekiti wa vijana akiongoza mambo, wakati Jack akichukua sifa zote. Alifanya bila kuchoka, wakati huo pia akisimamia ujenzi wa nyumba wanayoishi pia, Jack kazini bila kukosa wala kuchelewa. Kwenye hiyo nyumba waliamua kujenga vyumba vya nje na kurekebisha ndani kuifanya nyumba ya kisasa haswa kama alivyoona Sabrina kwenye majumba ya watu alimopita kutumika na kuishi. Akaiga muundo wa ndani ya nyumba ya Tino kwa asilimia 85, na kwa Pendo alikoishi siku 8 kabla ya harusi yake. Akataka kufanane ndani na hayo majumba mazuri yaliyomvutia. Pesa walizopowe baada ya harusi yao ikawa msaada mkubwa sana kwa Sabrina, Jack mwenyewe alikuwa akishangaa hayo mabadiliko.

 Ndani ya miezi miwili, Sabrina akiwa na ujauzito wa miezi saba, nyumba ya Jack aliyoikuta ya kawaida kabisa, ikabadilika, ungesahau hiyo nyumba. Alibadilisha hatua kwa hatua. Kuanzia sakafu, Jack aliagiza vigae vizuri sana vya sakafu ya nyumba nzima. Walifanya kazi chumba hadi chumba, hatua kwa hatua mpaka wakamaliza sakafu nzima. Rangi ya kuta, safi na tulivu iliyobadilisha kabisa muonekano. Akabadili thamani za ndani na kuweka za kisasa kutoka Dar ambako Pendo ndiye aliyekuwa akimsaidia kutafuta na Mama Msindai kumtumia huko Singida. Jikoni nalo akalitendea haki, ungeona shida kuacha pachafu. Vyumbani akabadili kabisa na kutoa uhitaji wa makabati kwa kujengewa makabati ya ukutani kwa kila chumba.

Wakabadili madirisha na ndipo hiyo nyumba ikafungwa AC. Ungependa kuingia hapo ndani. Sabrina akapafanya kukawa nadhifu mno, Jack akabaki akijisifia nyumbani kwake. Nyumba hiyohiyo yakawaida, Sabrina akaipa uhai, pakavutia utafikiri mjengo wa thamani ulipo sehemu ya tofauti kabisa na ilipo! Nyumba ya nje ilipokamilika, pakatandazwa vitofali vizuri kwenye ua mzima ila kukaachwa sehemu chache sana za maua ambayo Sabrina mwenyewe alikuwa akimwagilia. Wakati mama Msindai anamsafirishia makochi, meza ya chakula, vitanda na thamani nyingine, aliweka na vyungu vya maua vizuri sana. Sabrina ana mimba ya miezi nane na nusu, nyumba yake ikawa imekamilika kuanzia ndani mpaka nje. Huku mambo ya chama yakizidi kupamba moto.

Jackson Msindai akawa akionekana magazetini na kwenye vyombo vya kijamii amefanya hiki, amefufua kile. Ilimradi kuleta maendeleo kwenye jamii. Na kwa kuwa familia hiyo alijulikana na wengi, haikumsumbua Jack kufikia watu wakubwa na kumsaidia kutekeleza kwa haraka mipango yake na Sabrina. “Wanasema katika kila mafanikio, yupo mwanamke nyuma yake. Kwa upande wangu, mke wangu ndiye anayesimama na mimi, mchana na usiku ambao hakuna anayetuona. Kuhakikisha ananijenga, ananitia moyo pale ninapotaka kukata tamaa na kuniombea.” Usemi wa Jack kila asimamapo au ahojiwapo. Na kwa kuwa alimuamini sana Sabrina, alikuwa akimsikiliza kwenye kila mtu. Na kweli, Sabrina alipewa uwezo wa ajabu. Nguvu ya kufufua kila kilichokufa, mpaka Jack alikuwa akimshangaa. Hakuwa na muonekano wa ajabu sana, lakini alikiri mkewe kichwa chake kipo vizuri na Mungu huwa na yeye kwenye kila jambo analoweka mkono wake. Heshima Mungu aliyompa Sabrina huko Singida, na vile Jack alivyokuwa akimbemba mkewe, kila mtu alimuheshimu pale mjini. Usingemkuta bar, wala kwenye umbea akisutana. Nyumbani na kama asipokuwa nyumbani, basi kwenye mambo ya muhimu.

Alipokaribia miezi 9, Sabrina alishalemewa. Tumbo lilikuwa kubwa kuliko mwili wake. Miguu ilikuwa mizito kunyanyua, akawa anajicheka. Akapunguza safari na shuguli. Uzuri bado Imani alikuwa naye karibu na wakielewana vizuri. Kwa hiyo ikawa rahisi kwa Sabrina kumtuma. Na yeye Imani alipenda vile anavyojulikana kuwa yeye ndiye mtu wa karibu wa Sabrina. Akabaki yeye kuwa miguu ya Sabrina. Akimtuma huku na kule akamilishe na kufuatilia hili na lile. Na alichopenda zaidi Imani ni vile ambavyo kila mradi ulipokuwa ukifunguliwa, yeye na Jack ndio walionekana pichani kwenye magazeti wala si Sabrina ambaye ndiye mtoa mawazo na mipango. Hakujali kutoonekana popote pale ilimradi afanikishe. Tena siku za uzinduzi ndio alitaka Imani apendeze zaidi akimwambia lazima kupania magazetini. Basi Imani alikuwa akilifurahia sana. Sabrina akawa kioo chake kwenye kila shuguli akijua anamtakia mema, wala hamuonei wivu.

Baby Shower Ya Sabrina.

A

lipobakisha majuma mawili kufika tarahe yakujifungua, Pendo na kina Msindai wakawa wamemwandalia Sabrina baby shower. Ilibidi amsubirie Jack atoke kazini ndipo wasafiri kwenda Dar kwa ajili ya sherehe hiyo. Safari hii walifikia nyumbani kwa Msindai. Sabrina alikuwa akimtizama huyo mama anavyomshika Jack kila wakati kama mtoto mdogo. Mara ampanguse mdomo. Akumbuke hajanywa maji ya kunywa ya kutosha. Mara amtengeneze kola. Ilimradi tu mikono yake iwe kwa huyo mtoto. Na Jack naye ni kama aliyezoea, kama hakuona kitu cha ajabu kinachoendelea. Na wengine hivyo hivyo waliona ni kitu cha kawaida kabisa, ila si kwa Sabrina! Ilikuwa mara yake ya kwanza Sabrina kuona wawili hao wakiishi nyumba moja. Yaani kulala na kuamka nyumba moja. Alijua wanazungumza sana tu. Ni kama kabla hajalala na kila anapotoka nyumbani kwenda kazini, lazima azungumze na mama yake, lakini hakujua ukaribu ule wa mama Msindai kwa Jack ni kama kwa mtoto wa miaka mitatu!

Kwa Sabina.

Ilikuwa ijumaa. Sabina aliwaalika nyumbani kwake kwa chakula cha usiku. Haikuwa nyumba kubwa lakini Sabina aliwaalika hivyohivyo. Wazazi wao kina Sabina, Pendo na mume wake walikuwepo na mzee Msindai pamoja na mkewe pia. Sabina na mama yake walijitahidi kuandaa chakula kizuri na mazingira yanayoendana na kina Msindai. Wakapata wakati mzuri wa pamoja, Pendo akaeleza mipango ya kesho yake. Mama Msindai akamsifia Pendo kwa maandalizi mazuri. “Nilijua tu utamfaa Sabrina. Nakushukuru sana Pendo mwanangu. Mungu akubariki.” “Karibu na amina mama.” Pendo akaitika kwa unyenyekevu kama mwenyewe alivyo mtulivu. “Na ni kweli ananifaa Pendo jamani! Haachi kunipigia simu kunijualia hali yangu na watoto! Akikutana na magauni mazuri anayojua yatanifaa, lazima aninunulie na kunitumia! Asante mama Matron wangu. Mungu akupe haja ya moyo wako.” Pendo akacheka. “Amina. Na wewe sio mgumu Sabrina. Unaridhishwa na vitu vidogo na nirahisi sana kukufanyia jambo. Huna mambo mengi.” Wakacheka na kuendelea kuzungumza.

“Na mimi naweza kusaidia kama kunahitajika msaada popote kwenye hiyo shuguli ya kesho.” Sabina akaingiza hoja yake katikati ya mipango. Pendo akafikiria kidogo. “Itakuwa jambo zuri. Acha nizungumze na dada Jacinta tuone. Maana yeye ndio mama mipango. Ndiye aliyenisaidia kuweka mipango. Nani awe wapi na yupi afanye nini. Ameweka marafiki zake kwenye kila idara. Mipango mingi tunafanya kwa simu, ila tunakutana mara moja kwa week angalau kujua kila mmoja alipofikia na kuwekana sawa. Mpaka jana tunazungumza, sijasikia aliyelemewa. Ila kesho asubuhi tutakutana ukumbini tena. Nitauliza nani atahitaji msaada, kisha nitakujulisha kama kuna uhitaji.” “Basi naomba na mimi niwepo hiyo asubuhi.” Sabina akaonekana kukusudia kuwepo.

Alikuwa na agenda mbili. Moja kama ndugu, lakini alitaka pia kujichanganya na hao wanawake. Pendo mwenyewe alionekana ni msomi na kazi ya maana. Nyumbani kwake mwenyewe Sabina alipokwenda alibabaika. Jacinta Msindai na marafiki zake ndio wapo kwenye kamati! Sabina akajua atapata bahati ya kukutana na wanawake wanguvu. Akakusudia awepo. Pendo akaona ni jambo zuri, akampa muda na eneo watakalokutania hapo ukumbini. Wakaondoka.

Mama Kundi.

H

uku kwa mke wa Max, mama Kundi, zikawa kama habari za Sabrina zinamtafuta yeye tu. Akiwa ofisini akasikia fununu za hiyo baby shower ya mke wa kijana wa Misndai. Akatamani sana na yeye kupata mualiko ili akashuhudie. Lakini tatizo ni baby shower. Akajua wazi waandaaji ni wanawake. Hakuwa karibu na mke wa bosi wake. Waziri Msindai, yaani Joy, ili kumuomba mualiko. Alishakutana na Joy mara kadhaa kwenye party au shuguli za kiofisi, lakini hawakuwahi kuwa karibu. Dada za Msindai mwenyewe, yaani huyo bosi wake, Junior Msindai, nao ni watu wazito kwenye jamii. Yeye kama mfanyakazi wa kawaida tu wa wizarani asingeweza kuwa nao karibu. Lakini akamwambia mumewe lazima aende akaoshe macho kwenye baby shower ya kina dada wasomi na mashuhuri hapo mjini.

Mama Kundi akafikiria jinsi ya kupata mualiko akaona hana jinsi, akamvizia siku hiyo waziri Msindai yupo ofisini kwake na hapakuwa na hekaheka nyingi. Maana yeye alifanya kazi kwenye wizara hiyohiyo, lakini kwenye ofisi ya waziri mwenyewe. Wakati anatoka akajidai na yeye anapita. “Hongereni sana muheshimiwa. Nimesikia bibi harusi wetu anafanyiwa baby shower!” “Yeah!” Junior akajibu. “Hivi leo ndio wanaingia hapa Dar, tayari kwa shuguli nzima kesho.” “Safi sana. Unajua kwa namna fulani nafahamiana na Sabrina?” “Oooh yeah!? Sikujua.” Ikabidi Junior asimame kidogo zaidi kumuonyesha kumsikiliza. “Sema tulipotezana. Alishafika mpaka nyumbani kwangu. Tukapata chakula cha pamoja. Ile siku ya harusi tulihudhuria nikiwa sijui kama yeye ndio bibi harusi!” “Acha kunishitua bwana! Tumeoa mke wa mtu nini?” “No no noooo.” Akajichekesha kidogo mama Makundi. “Hapana kabisa. Hakuwa ameolewa na wala sikusikia kama aliolewa.” Wakacheka kidogo. “Ningetamani na mimi kuhudhuria na hiyo baby shower, ili nilete hata zawadi ya diaper. Nilimpenda sana Sabrina.” “Ingekuwa vizuri. Ila sihusiki na baby shower.” Wakacheka tena.

“Nafahamu hayo ni mambo ya wakina mama.” “Namsikia tu Joy akiwa kwenye mipango. Ni kama msimamizi wake ndio ana shugulika zaidi, wakisaidiana na kina Jacinta. Subiri kwanza.” Mama Makundi akamuona ametoa simu akapiga. Akamsikia anasikiliza sauti ya kike upande wa pili. “Na mimi nipo katikati ya kitu Jacinta. Sikiliza.” Junior akamjibu hivyo Jacinta. “Unanafasi ya mtu mmoja au wawili kwenye baby shower, kesho?” Akamsikiliza kidogo, akacheka. “Sio mtu wa mtaani bwana! Ni mtu na heshima zake. Tunafanya naye kazi hapa.” Akamuona anasikiliza kwa muda. Kisha akajibu. “Naelewa. Upo sahihi kabisa. Ila huyu niliyekuwa nikimuombea mwaliko ni mfanyakazi wa hapa, na anafahamiana na Sabrina. Ningejua mapema, ningekuomba mapema. Lakini naamini ataelewa kabisa.” Akamuona anasikiliza. It’s okay. Usilazimishie. Ibaki kama mlivyopanga. Hamna shida kabisa. Ataelewa tu.” Akasikiliza kidogo. “Sawa sawa. Kazi njema.” Mama Makundi akawasikia wakiagana lakini akapoa kabisa akajua ndio amekosa.

“Samahani sana. Nafikiri tumechelewa. Wameandaa kutokana na idadi ya watu waliowaalika na waliokubali kuhudhuria. Hata ulinzi wa hapo umewekwa kutokana na wageni. Na chakula pamoja na vinywaji ni hivyohivyo. Vinaandaliwa kutokana na walichochagua watakao hudhuria. Anasema mialiko ilikwenda na Menu. Hapatakuwa na ziada ya chochote hata kiti cha ziada hakitakuwepo. Wanakwenda kwa idadi au majina. Na kingine jana usiku wameshafikisha kwenye vyombo vya usalama idadi kamili na majina yamehifandiwa ya watakao hudhuria hapo kwa sababu za kiusalama. Kuongeza watu leo wakati kesho ndio siku yenyewe...” “Naelewa kabisa mheshimiwa. Inamaana itabidi zoezi zima lianze upya.” Mama Makundi akaona amrahisishie tu. Junior alikuwa mstaarabu sana. “Ewaa!” Junior akaafiki. Wakacheka tena kidogo, Junior akaondoka, mama Makundi akabaki akifikiria hiyo aina ya baby shower. “Mmmmh!” Akaguna kila akimfikiria Sabrina aliyekutanishwa naye na huyu! Bado ilikuwa haiingii akilini. Alikwenda nyumbani kwake akiwa binti wa kawaida sana. Akawa bado yupo kwenye mshangao.

 ~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Lakini Max, nahisi kuna kitu hakijakaa sawa. Na Tino hataki kukizungumza.” Max alitoka kazini na kumkuta mkewe bado kwenye kumfikiria Tino na Sabrina. “Unazungumzia habari za Sabrina?” “Ndiyo!” “Umepata mwaliko?” Ikabidi mama Kundi acheke. “Hiyo baby shower sio ya kila mwenye zawadi, baba!” Akaanza mama Makundi. “Ni kwa mwaliko kamili. Nilimsikia mhehimiwa akizungumza na dada yake, naona huko sie wa kina sisi hapatufai.” “Eeh!” Max akataka kusikia zaidi. “Eti wageni walitumiwa mwaliko na menu. Ukisema unakwenda, unachagua aina ya chakula unachotaka kula siku hiyo na kinywaji chako. Kwa hiyo mpaka leo, wanajua nani anakwenda, atakula nini na kinywaji gani na washaandaliwa kiti kwa majina.” “Eee bwana weee!” “Subiri Max. Majina na idadi kamili ya watakao kuwepo kwenye hiyo shuguli, vipo kwenye vyombo vya usalama kwaajili ya ulinzi wa siku hiyo!” Max akabaki ametoa macho.

“Ndio ujue aina ya wageni hapo!” “Hiyo shuguli itakuwa sio mchezo! Wakina mama wazito watupu watakuwepo huko.” Max akaongeza akifikiria. “Lakini nilimsikia akimwambia kaka yake, angewahi hata siku tano zilizopita, pengine na mimi wangenichukua!” Wakabaki kimya kwa muda. “Mimi nahisi kuna jambo limejificha Max. Jaribu kumdodosa Tino.” “Si nilikwambia anakwepa hilo! Kila nikitaka tumzungumzie Sabrina, hataki kabisa na anabadili mazungumzo. Mara ya mwisho nilipompigia simu kuhusu Sabrina, si unakumbuka nilikwambia aliniaga kwa haraka akasema kule ni usiku anakwenda kulala?” “Nakumbuka. Sasa sijui kulikuwa na nini kinachoendelea walipotoka hapa kwetu! Maana waliondoka wakionekana wanamipango mizito! Leo Sabrina anaolewa na ujauzito ambao lazima utakuwa mkubwa tu!” Mama Kundi akamshitua sana mumewe ambaye bado alikuwa akimficha ukweli.

“Unataka kuniambia nini!?” Max akauliza na wasiwasi akitamani isiwe vinginevyo. “Sijui Max! Lakini mimi nilimuhisi ni kama siku ile ya harusi aliolewa akiwa na ujauzito mkubwa tu. Ile haikuwa mimba changa. Ila ile nguo ya harusi jinsi ilivyotengenezwa na kwa kuwa mwenyewe ni mwembamba, ndio maana hakuonyesha sana. Na ujue wazi baby shower nyingi wanafanya wakiwa wanakaribia kujifungua. Ndio ujue anao ujauzito mkubwa tu, na wa muda mrefu. Sasa wewe piga mahesabu. Waliondoka hapa lini, harusi ilikuwa lini, na leo Sabrina anajifungua! Wewe unaona inaleta maana?” Mama Kundi akamuuliza mumewe asijue anaibua jingine zito. Max akabaki kama amepigwa ganzi akifikiria, nani amemchezea visivyo? Tino alimuhakikishia Sabrina aliingia chumba chakutolewa mimba, na amemuacha Moshi hospitalini akiwa amepoteza damu nyingi baada ya kutoa mimba. Na daktari naye alilipwa pesa ya kutosha tu baada ya kuhakikishia wote kuwa alifanya kazi yake kikamilifu. Akahisi mkewe anachanganywa na kukosa mualiko tu. Akapoa na kushindwa kuendeleza hayo mazungumzo asije jikuta anaropoka ya sirini. Akabadili kabisa hayo mazungumzo.

Baby shower.

W

akati wanawake wanakutana kwa baby shower, wanaume ndugu na rafiki wa karibu wa Msindai walifanya nyama choma nyumbani kwa Junior wakimtania Jack na kumuandaa kuwa baba. Vilijaa vicheko na vitisho kwa Jack kuwa ajiandae kutolala usiku wala mchana kwa vilio vya watoto. Wakamfundisha kufunga diaper huku wao wenyewe wakikosoana kwa hili na lile, kwamba hata wao wenyewe hawajaweza au wameshasahau kufunga diaper. Walikuwa na mdoli mkubwa tu wakifundishana. Walichekana na kukosoana sana. Mpaka Mzee Msindai mwenyewe aliambiwa akumbushie enzi. Aingie kwenye hilo zoezi. Wakaamua waanze kutafuta mshindi kati yao hao wanaume ambaye ataweza kumuogesha huyo mdoli ndani ya beseni, bila kuingia baridi wala kumdondosha ndani ya beseni. Kuanzia mwanzo mpaka mwisho kwenye kumkausha, kumpaka mafuta, ndio diaper na nguo. Vilijaa vicheko na vya kilevi hapo, wababa hao wakawa kwenye ushindani wa hali ya juu akitafutwa mshindi ili wote wamchangie pesa aondoke nayo siku hiyohiyo.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Huko ukumbini nako upande wa wanawake, mambo yalikuwa ya namna yake. Kwanza kulipambwa vizuri sana. Mbali ya sehemu yenyewe hiyo shuguli ilipofanyika, na ndani pia kulipangiliwa kwa ustadi, pakawa nadhifu haswa. Sabrina alitengenezwa vizuri akapendeza na mimba yake. Akamshukuru Pendo kwa kumpeleka saluni akatengenezwa vizuri, na nguo ya thamani aliyomtafutia. Akawa ameendana na wale kina mama pale. Ilionekana ni shuguli iliyoandaliwa na watu wanao jielewa. Maana aliletewa hapo ukumbini mpaka daktari wa mambo ya watoto ili kutoa mafunzo. Akafundisha vitu gani vya kuzingatia kwa mtoto, kuanzia mtoto mchanga kabisa anayetoka kuzaliwa. Akaja mtu wa mambo ya lishe kwa watoto. Ikawa nzuri na muhimu kwa wote. Hapo napo Sabrina akajifunza mengi na wengine kuuliza maswali. Ikaongezeka michezo ya baby shower iliyowafanya wote washiriki. Kukajaa vicheko na hali ya ushindani pia ikaanzishwa ili wote kushiriki. Ukumbi huo uliojaa wasomi, wanawake wanaoshika nyadhifa tofautitofauti ndani na nje ya nchi, wakapata burudani ya namna yake.

Kukaendelea michezo, vichekesho, wakaja sasa wa mama waliogusa kila mtu hapo ukumbini. Kwani wao walitakiwa kumfundisha Sabrina jinsi ya kuweka balance kati ya watoto na mume. Nini chakufanya kama mama na mke. Akasimama mama mwingine msomi lakini mcha Mungu. Huyo naye akafundisha mama wa kwenye bibilia na mke wa kibibilia. Naye akaongea mengi na wapi watu wanakokosea. Akawa mcheshi haswa, akatoa mifano mingi yakukosoa, watu wakacheka mno lakini hapohapo wakajifunza.

          Zikaja zawadi zilizo zidi kugusa moyo wa Sabrina. Zilichaguliwa baadhi tu zakuonyeshwa pale kama kumfundisha Sabrina, nyingine zikaachwa zimefungwa na kuwekwa upande wa wageni walipoweka zawadi zao. Wakina mama hao wakawa wanamkabidhi na jinsi ya kutumia. Mama yake Sabrina mwenyewe hakuwa akiamini kama yote hayo anafanyiwa Sabrina mtoto wake aliyekuwa akimuhesabu na kumuona si kitu kabisa. Kitendo cha kuthaminiwa na mwanaume aliyeishi naye na kumuoa kwa kiapo kizito vile! Ni kigugumizi kilichopata familia nzima.

Mama Sabina alikuwa amekaa hapo haamini kama kweli yupo hapo kweli au ni ndoto tu, atakuja kuamka. Maana aina ya wanawake waliokuwa wamemzunguka hapo! Ilikuwa ngumu kuamini kama na yeye yupo miongoni mwao. Hakuwahi hata kudhania anaweza kuja kuwa nao chumba kimoja maishani. Wengi aliweza kuwatambua kwa kuwaona kwenye luninga, wengine walijitambulisha wenyewe wakati wakutoa zawadi au mada na wengine alikuwa akinong’onezwa na Sabina. Kila mmoja hapo alikuwa mtu mzito. Aina ya huduma zilizokuwa zikitolewa hapo, hata Sabina mtoto wa jiji alikiri kwa mama yake kuwa hajawahi kuhudhuria aina hiyo ya baby shower. Kila kitu kilikwenda kwa wakati na muda sawa sawa na kwenye ratiba.

Mwishoe Pendo alitoa shukurani kwa waalikwa wote, na akaomba wamuombee bibi harusi wake. Sabrina akataka kabisa kupiga magoti kabisa. Pendo na yeye akapiga naye magoti, wakawazunguka nakuanza kuomba nao. Wakamuombea kujifungua salama, kuwa mama mzuri na mke mwema. Maombezi yalipoisha, akapata muda wa yeye mwenyewe wa kushukuru. Sabrina alizungumza maneno mazito ya kinyenyekevu, mbele ya hao kina mama bila woga. Kikubwa aliweka msisitizo akisema, anamshukuru Mungu, amemjibu maombi yake kabla hajafa. Aliwashukuru kwa kusimama na yeye katika kipindi hicho. Aliongea Sabrina, mpaka wasomi hao wakapoa. Hakuongea kama msomi, lakini kama aliyemuona Mungu kwa namna ya kipekee sana.

“Kila mmoja wenu hapa, kwa nyadhifa zenu, sifa zenu zote, niliwaomba kwa Mungu. Tena kwa kufunga na kuomba zaidi ya siku tatu, au 7, au 14 au 21. Nilishafunga nakuomba sana nikabaki kushukuru kwa ajili yenu. Mimi ni mtu wa kawaida sana. Mama yangu ni yule pale kama mlivyotambulishwa, na dada yangu. Tumetokea kwenye familia ya kawaida sana, lakini namuabudu Mungu aliye mkuu mno, zaidi tumjuavyo na tumfikiriavyo. Pale ufahamu wetu unapoishia kumjua yeye, ndipo uwezo wake unapoanzia.” Watu wote wakapiga makofi wakiwa wameanza kuhamasika.

“Kuna mtu nilikuwa nikimtia moyo sehemu, akiwa kwenye hali mbaya sana yakufa. Nikamwambia amini tu. Amini kama utatoka hapo ulipo kwenye hiyo hali. Nikamwambia inaweza isilete maana sasa hivi kwa kuwa ninayekwambia ni mimi. Nikamwambia lakini yupo Mkuu aliyezidi vipimo vyote. Nikamwambia mimi nilikutana naye miaka michache iliyopita. Nikamsoma uweza wake. Nikamwambia huyo mtu aliyekuwa kwenye hali ya kufa aina ya maombi ninayoomba, nikamwambia nikimwambia yeye, angeweza kusema nimechanganyikiwa.” Watu wakacheka kidogo. “Nikamwambia lakini imani yangu haipo kwa kile ninachoomba, ila kwa yule ninayemuomba.” Watu wakapiga makofi.

“Kwa ufupi sana, kwa kuwa nilimjua ni nani nimuombaye, sikuomba vitu vidogo. Sikuomba maombi ya kitoto ambayo mtu yeyote anaweza kufanya. Kwangu kuolewa na Jackson Msindai, ni muujiza ambao unahitajika siku nzima kusimulia na kuuona ukuu wa Mungu kupitia kile alichonibariki ili Jack, mwanaume ambaye nimekuwa naye kwa miaka mingi sana, lakini nikajichelewesha kupokea baraka kubwa sana kuolewa naye.” Watu wakapiga makofi huku wakicheka.

“Mungu ni mwenye rehema. Ukimuita, huitika kwa wakati wake yeye Mungu wala si kwa wakati wetu. Japokuwa maisha yalinifinyilia, na kunikatisha sana tamaa, lakini Mungu alinitunzia Jack wangu mpaka akahakikisha ananikutanisha naye tena na kunikabidhi. Amekuwa rafiki wa karibu mno kuanzia tupo chuoni. Amekuwa faraja ambayo hakika, sistahili ila ni Mungu tu ndiye anayenistahilisha kuwa na mume kama Jack.” Sabrina akafuta machozi wakati wakampigia makofi. “Na leo kuzungukwa na watu wa muhimu kama nyinyi, mlioacha shuguli zenu za msingi, kuwepo hapa na mimi sasa hivi, hakika huyo ni Mungu wala si mimi. Wifi zangu, mama Msindai mwenyewe, mke mwenzangu Joy, wamekuwa wakinihangaikia mno pamoja na mama matron wangu ambaye kila siku lazima ajue ninaendeleaje mimi na watoto! Kila nikitafakari aina ya upendo na heshima ninayopata mimi, na kule ninakotoka, najua ni Mungu tu.” Watu wakapiga makofi.

“Jamani, yule Mungu aliyenitoa mimi mavumbini kabisa, nikiwa mnyonge na mpweke, akakutane na haja za mioyo yenu.” “AMEN!” Wote wakaitika. “Akawatendeeni mema mpaka mjue kama yeye ndio ametenda kwenu, kwa ule moyo tu wakutenda kazi pamoja naye kujidhihirisha kwangu kwa namna kuu mno. Kwa kule kukubali bila kunifahamu, na kutenda mnayonitendea, mlipotoa, pakaongezwe kwa namna ya ajabu.” “AMEN!” Wakaitika. “Kwa hili mlilonitendea mimi, mume wangu na watoto wetu, basi huyu Mungu mwenye ENZI yooote, akutane na kazi zenu, biashara zenu, familia zenu, aguse watoto wenu, asije potea hata mmoja. Na waliopotea Mungu akawarejeshe salama, kisha siku ya uhitaji wao, awakutanishe na watu sahihi wa kusimama nao.” “Waooo! AMEEN!” “Mungu akumbuke waume zenu. Aweke ulinzi kwenye majumba yenu, kilicho kibaya kisipite mchana wala usiku. Akawajaze kwa namna ya pekee mpaka na nyinyi mjue huyu Mungu amewabariki TENA kwa hili mlilonitendea mimi na watu wa nyumbani kwangu.” Vigelelegele na “Ameeen!” Wakaitika wakishangilia na kusimama. Wakafunga na watu wakatoka kwa wakati.

Wakati wakiagana na wageni wao, Sabrina akasikia kichomi kwa nguvu. Akashituka kidogo, akatulia. Akaanza kusikia mvurugano tumboni kama wanae wanageuka na kucheza. Akatafuta sehemu, akakaa wakati wenyeji wake wakimalizia kuagana na waalikwa. Kiuno kikaanza kuuma. Akawa ametulia kabisa kitini. Mama yake na Sabina nao wakapata nafasi yakushukuru. Wakawashukuru kina Msindai na Pendo kwa baby shower nzuri na ya heshima. Na wao wakaondoka. Mwishoe Pendo akaomba awaache ili amrudishe bibi harusi wake nyumbani. Wakaondoka. 

Atafafutaye Hachoki.

P

endo akaondoa gari. “Upo sawa mwali wangu?” “Naona sababu ya kucheza sana, kiuno kinauma kidogo.” Wakacheka story za ukumbini zikaanza. Wakazungumzia juu ya zawadi. Sabrina akamsisitizia lazima na wao wapange kwenda kuwatembelea Singida. “Nina chumba kizuri kwa ajili yako matron wangu. Ukichoka tu kelele za jiji, njoo Singida.” “Lazima. Hivi nilikuwa nikimwambia Willy tutunze siku za likizo ili ukijifungua tuje.” “Hayo ndio maneno. Nimebakisha majuma mawili tu, kwa hiyo anza kuandaa begi la safari.” Wakacheka na kuzungumza kidogo.

“Lakini da Pendo, mimi nataka kusimama na wewe, na tuamini pamoja juu ya wewe kupata mtoto.” “Wala usijishumbue Sabrina.” “Kwa nini!?” Akauliza Sabrina kwa mshangao. “Nilipimwa mwaka jana, mayai yalikuwa yamebaki machache mno! Umri umekwenda, halafu pia nina vimbe zimeota huko kwenye kizazi kama uyoga. Hivi hapa daktari alikuwa ananiambia nifikirie kutoa tu kizazi kwa kuwa hawawezi kuingia huko kutoa hizo vimbe bila kuharibu kizazi. Zimeota sehemu mbaya sana. Kwa hiyo hilo mbona tushafunga mimi na Willy! Naona tushakubali kuishia tu sisi wenyewe.” Sabrina akatulia kwa muda akimfikiria Pendo. Pendo akashangaa hajibu, ametulia.

“Maumivu yamezidi?” “Hapana. Ila nikuulize da Pendo, unakumbuka nyumbani kwetu? Si ulikuja wakati nalipiwa mahari?” Pendo akacheka. “Na wewe, pale kwenu ni pazuri bwana. Hujaona kwenye majumba ya watu wengine?” “Hapana da Pendo. Linganisha maisha yangu na ya kina Msindai au yenu. Kuwa tu muwazi. Mtu kama Jack, angeniona wapi mtu kama mimi?” Pendo akanyamaza. “Nikikwambia kuwa Jack alikuwa akipiganiwa chuoni na wadada warembo utaamini?” “Wala usiende mbali. Yule msichana aliyeleta boksi la baby wipes. Akasema ameleta nyingi kwa ajili ni watoto mapacha, akawa anakufundisha jinsi ya kufuta mtoto.” “Nimemkumbuka. Anakaumba kama namba sita hivi.” “Ewaaa! Anaitwa Salome, au Sally kama wengi tulivyozoea kumuita.” “Sasa amefanyaje?” Sabrina akauliza. “Anampenda Jackson yule, kufa. Tena wala hafanyi siri, ila tu ni mstaarabu. Hana mambo ya ajabu. Rafiki yake kipenzi Jena. Na wengine wengi tu. Tena ndio ilikuwa zaidi wakati Jack anaishi hapa Dar, tukawa tukimtania bora aoe, ili tupumzike” Sabrina akacheka.

“Sasa hali hiyohiyo ndio ilikuwa chuoni, wasichana kumgombania Jackson Msindai. Lakini da Pendo, jua tu Mungu yupo na hutoa kwa amtakaye yeye Mungu na hakuna wa kumuuliza. Mimi sijui amekusudia nini kwako, lakini dada, kama alifanya kwa Sabrina, hatashindwa kwako. Na usifikiri niliomba mara moja nikaacha! Nikikwambia siku 21, niamini ni 21 zile ngumu mno. Hivi unavyoniona sikuwa na marafiki ila Jack tu ndiye alikuwa rafiki kwa simu kipindi nimefungiwa nyumbani wala sijui nitatoka vipi. Kazi mchana na usiku na mengine mengi ambayo nilikumbana nayo, ila sitaki kuongea kwa kuwa nimesamehe. Dada Mungu yupo. Hafanyi mambo ya kijinga au yakawaida. Anataka kufanya jambo kwa watu kama wewe, ili kufedhehesha wenye hekima. Yaani wakisikia Pendo amepakata mtoto, masikio yawashe na wamtukuze Mungu. Nina uhakika wanao nifahamu mimi, wakasikia nimeolewa na Jackson Msindai, hawataamini. Lakini dada, ni Mungu. Mungu yupo. Kama umekata tamaa, tafadhali acha mimi nikubebe. Acha imani yangu ikubebe tu.” Akamuona Pendo anafuta machozi yaliyokuwa yamefichwa ndani kwa tabasamu la nje tu.

Sabrina akaanza maombi hapo kwenye gari. Aliomba Sabrina akimkumbusha Mungu yale magumu aliyomtendea yeye. Jinsi alivyomuona hata Singida. Yale amefanya huko kwa muda mfupi sana. Akamwambia Mungu, anamwamini kwa ajili ya Pendo. Akamkumbusha mengi Mungu aliyojidhihirisha kwake kwa kupitia Pendo, akamwambia amkumbuke Pendo. Sabrina aliomba sana. Mpaka Pendo akafika nyumbani kwa mama Msindai, akaegesha gari nje, akamshika Sabrina mikono. Sabrina akamshikisha ile mikono tumboni kwake. Akamwambia uwezo uleule na baraka zile zile za mapacha, zimshukie Pendo. Kisha wakashikana tena kuendelea kuomba.

Jack aliona gari likiwa linaingia hapo kwao, ila akashangaa Sabrina haingii ndani. Yeye akatoka akasogea mpaka garini, akakuta wakiomba, akafungua mlango, akamshika mkewe, na yeye akaungana kwenye maombi. Alipogundua wanamuombea Pendo, na yeye akaongeza nguvu. Wakaomba pamoja mpaka wakamaliza. “Ameen!” Wakasema wote kwa pamoja. Jack akamshukuru Pendo kwa kila kitu, akamsaidia mkewe kushuka garini, Pendo akaondoka.

Sabrina ajifungua na kuzua Mtafaruku!

Y

akaanza mabusu hapo hapo nje. Jack akamkumbatia mkewe na kumbusu tena na tena. “Tunaondoka kesho.” “Basi tuwahi kulala. Kiuno kimeanza kuuma ukumbini. Sijui nimecheza sana!” Sabrina akamsimulia waakaanza kucheka. “Mimi nimepata shule ya nguvu. Hapa najua kuogesha vichanga na kufunga diaper.” Jack akaanza kujisifia, Sabrina akamwangalia na kuanza kucheka. Akaendelea kumsimulia aliyojifunza wakiwa wamesimama palepale nje, mara kichomi kingine kikapita kwa nguvu sana mpaka Sabrina akakaa kwenye ngazi. “Vipi tena!?” Jack akauliza akionyesha wasiwasi. “Nasiki.... Aaaah!” Kalalamika Sabrina.

“Basi twende ukapumzike. Maana kumekuwa na shuguli nyingi kweli! Utakuwa umechoka na watoto hao washakuwa wakubwa.” Akamsaidia kusimama. Ile anamalizia ngazi ya mwisho, chupa ikavunjika wote wakabaki wametoa macho. “Si tumeambiwa bado majuma mawili!” “Naomba tukashangae hukohuko hospitalini. Nasikia maumivu Jack, naona hawa watoto wamechoka kusubiri.” “Kweli. Sasa nakubeba au naku...” Tayari Jack akawa kama ameshapaniki. “Acha kupaniki bwana! Wewe si umeniambia umefundishwa ku...., aaah!” Sabrina akashindwa kuendelea kwa maumivu mengine yaliyopita gafla.

“Kufundishwa na uhalisia nitofauti bwana! Niambie nifanye nini?” Sabrina akaanza kushuka tena ngazi. “Acha nikubebe.” “Naweza kutembea Jack, tulia, acha kupaniki.” “Unamaumivu makali sana?” Sabrina akanyamaza. “Sasa ukijifungulia njiani, itakuaje?” “Ndio nitakuwa nimejifungua Jack jamani! Acha kuwa na wasiwasi. Kwanza hebu niangalie.” Jack akasimama. “Tulia kabisa. Naomba tulia na niambie nitakuwa sawa. Nitajifungua salama na kila kitu kitakwenda sawa.” Sabrina akataka mumewe atulize akili. Jack akatulia akakumbuka alitakiwa awe faraja. “Nakuaminia Sabrina wangu. Hata hili utaweza tu mke wangu. Twende tukawapokee kina Jeiline na Keiline.” Sabrina akacheka moyoni, wakaondoka pale.

Wakiwa njiani kila maumivu yalipoongezeka aliamua kuvumilia ili asimtie hofu Jack ambaye alikuwa akipiga simu kwa kila aliyemjia. “Tupo njiani tunaelekea hospitalini. Naona wanangu wamechoka kusubiri. Wanataka kuja kukutana na baba yao.” Sabrina akabaki akimsikiliza akizungumza na simu yeye akigugumia taratibu. Maumivu yakaongezeka yakawa karibu karibu. Mzee Msinda akamwambia anampigia simu rafiki yake, ambaye ni daktari wa wakina mama, ili akutane nao hospitalini. Hilo likamfariji Sabrina kugundua kama yupo mtu wa kuaminika atakuwa akiwasubiri huko hospitalini.

Sabrina anafika hospitalini, akawa na maumivu asiyoweza kuvumilia wala kutembea. Jack akakimbia mapokezi akaomba msaada wa haraka. Wakati yupo mapokezi wanasubiria wheelchair kuletwa ili akamchukue Sabrina, akashitukia Sabrina anakuja. “Hawa watoto wanatoka Jack. Hakika nitazaa hapahapa.” Jasho lilikuwa likimtoka Sabrina, macho mekundu kwa maumivu. “Nasikia kabisa kitu kintoka huku chini. Nitaua wanangu Jack!” Hapo Sabrina akazidi kulia kwa sauti ya wasiwasi maana walikuwa wanachelewa. Mama mmoja naye alikuwa hapo mapokezi na mgonjwa wake akamkimbilia na kumshika, “Kaa chini kabisa.” Sabrina akakaa akisaidiwa na yule mama. Jack alishaanza kupiga kelele kuomba msaada akisema wanachelewa. “Wote uliowakuta hapa ni wagonjwa kaka yangu.” Akaongea muuguzi mwingine akiendelea kuandika hapo ndani mapokezi.

Mara aliyekwenda kuleta kitanda akaja. Wakasaidiana kumpandisha Sabrina na kumkimbiza labour. Wanaingia tu, muuguzi anamwangalia, kweli kichwa cha mtoto kilikuwa kinatoka. “Mungu wangu mtoto wa kwanza anatoka!” Jack naye alikuwepo hapo. Hapakuwa hata na muda wakuchomwa sindano yakumfanya asisikie maumivu, epidural, Sabrina akasukuma, mtoto wa kwanza akatoka. Akahema kwa nguvu kama aliyepata aghueni wakati mtoto wake akisikika akilia hapohapo hata kitovu hakijakatwa. “Haaa!” Wakashangaa wauguzi wote wanashangaa. Jack na Sabrina wakashituka. “Huyo ni Jeiline. Yupo salama?” Jack akauliza akaona wanaangaliana. Jack akasimama na kusogea. Akakutana na mtoto wa kizungu. Akatulia kidogo kama na yeye amekutana na kitu ambacho hajatarajia.

“Kuna nini Jack!?” Sabrina akauliza kwa wasiwasi. “Mtoto yupo mzima?” Jack akarudia kuuliza tena kama aliyerudiwa na akili. “Mzima kabisa, ila..” Aliyekuwa akimalizia kumtenganisha na mama yake akawa kama amepatwa kigugumizi. “Naomba kumbeba kama ni mzima.” Jack akampokea baada tu ya kufutwa kidogo. “Hey Jeiline! Njoo umuone mama.” Akamsogeza kwa Sabrina. Sabrina mwenyewe akashituka kukutanishwa na mtoto wa kizungu. Hakutegemea kabisa. Jack akamuwekea kifuani kama mkunga alivyomuelekeza ili apate harufu na joto la mama yake.

Wapo watoto wanazaliwa weupe, na nywele, lakini Jeiline alizaliwa mweupe wa kizungu kabisa, na nywele nyingi haswa kama mtoto wa kiarabu wala si wakizungu maana watoto wa kizungu asilimia 99 huzaliwa bila nywele. Uso mwembamba uliochongoka kama mama yao na midomo ya pinki kabisa.  Ndipo akili ikamrudia Sabrina, akakumbuka Tino alimwambia  mama yake alikuwa mwitaliano. Sabrina akamnyanyua vizuri akiwa kwenye kitanda cha kujifungulia, wakisubiri mtoto wa pili. Wakamuona anambusu mtoto wake. “Nimefurahi kukuona Jeiline. Umekuja kwa wakati wa Bwana. Namshukuru Mungu umezaliwa mzima.” Sabrina akaongea kwa sauti ya taratibu na machozi. “Wewe ni mtoto mzuri sana na Mungu ana mpango na wewe. Hujaja hapa duniani kwa bahati mbaya. Umebarikiwa kwa baraka zooote za rohoni na za mwilini. Kila ulimi uliotamka na utakaotamka kinyume na baraka za Mungu juu yako, na uhukumu mkosa. Katika jina la Yesu.” Akaongeza Sabrina kama anayemuombea mwanae na kumbusu tena. Wale wakunga wote pale ndani wakapoa. Jack naye akaitika “Amen.” Na kusogea karibu kabisa akajilaza pembeni ya bega la Sabrina wakawa wanamwangalia mtoto kwa juu. “Kweli wewe ni mzuri Jeiline! Na tunakupenda sana mwanangu.” Sabrina aliposikia hivyo, ikamfariji sana. Jack akajinyanyua na yeye akambusu tena na tena.

“Naruhusiwa kupiga picha ya sisi watatu kabla mdogo wake hajaja?” Jack akauliza. Wakamkubalia. Wakawasaidia kupiga picha yule mtoto akiwa vilevile alivyotoka kuzaliwa. Wakapata picha nyingi tu mpaka Jack akatosheka na picha ndipo wakamchukua sasa mtoto kumsafisha vizuri na kumvalisha. Wakati wanamsafisha, Jack akarudi kwa Sabrina. “Pole na hongera Brina. Naona umeniletea mzungu!” Jack akaongea na kumbusu. Sabrina hakujua kilio kilitokea wapi, akaanza kulia kwa kwikwi. “No no nooo! Which is good Brina. Usifikirie ni jambo baya. Ni zuri mnoo. Nimefurahi.” Jack akajua amemuudhi, asijue Sabrina amefurahia, hakutegemea kama Jack angewakubali watoto wa aina ile. Alimuona jinsi Jack alivyoshituka mwanzoni mara tu alipomuona mtoto. Lakini ni kama akajirudi kwa haraka. Wauguzi pale wakawa wanasikiliza, hawaelewi.

“Wazungu ni wazuri tu. Hata ungenizalia wajaluo, wakijani au wahindi, mimi sawa tu.” Mpaka Sabrina akacheka. “Kweli?” “Sasa wewe unafikiri nitaozesha hawa kwa pesa ndogo?” Kila mtu pale akaanza kucheka. Angalau ule mshangao pale ukapungua. Na Sabrina akasahau kama ana mtoto mwingine tumboni. Jack akaanza mabusu kwa mkewe wakati wauguzi wakimtayarisha mtoto na yeye mwenyewe kwa kujifungua tena. Jeiline akarudishwa. Picha zikaendelea. Jack akaanza kuchukua video ya selfie. Akawa anamuelezea Keiline kuwa wapo hapo wao watatu, mama yake, yeye na dada yake Jeiline wanamsubiria yeye. Wanahamu yakumuona na yeye. Sabrina akawa anacheka taratibu huku amemlaza Jeiline kifuani, yeye bado amejilaza huku amemkumbatia mwanae, Jack akitoa mabusu ya hapa na pale kwa Sabrina na Jeiline. Mara simu zikaanza kuingia.

“Sijui nianze kupokea ya nani, niache ya nani!” Wakati Jack akijishauri, daktari akaingia. “Sabrina Msindai?” Akauliza. “Ndio mimi.” Akamsogelea akionekana alikuwa akiharakisha kufika hapo. “Naona ushakumbatia mtoto wa kwanza.” Daktari akaongeza. Jack akamchukua mtoto kutoka kwa mama yake na kumbeba yeye vizuri kwa upendo na cheko usoni. Yule daktari yeye hakuonekana kumshangaa yule mtoto wa kizungu. “Hongereni sana bwana. Naona mama na Mzee wana wasiwasi sana na wewe Jack. Wangeona hiyo furaha! Wasingekuwa na wasiwasi.” Jack akacheka. “Ndio wajue nimekuwa baba, waache kunifanya mimi kama mtoto mdogo.” Jack akaongea macho kwa mtoto. Daktari akacheka na kuomba kuona vipimo vya mtoto huyo wa kwanza. Wakamuona anatingisha kichwa kama anayekubali. Wakamuona anacheka. “Naona na jina tayari!” “Nimempa huyo nesi ili asinichanganyie watoto.” Jack akajibu wote wakacheka pale.

Heshima ikaongezeka mara baada yakugundua ni kina Msindai. Mama Msindai alishakuwa Waziri wa afya. Mtoto mtu yupo madarakani na yule daktari alishasema wote wapo njiani na wengine wapo nje wanasubiria. Hata ule uwepo wa yule daktari tu pale kwa mama ambaye hana tatizo kama Sabrina, inamaana yupo pale kuhakikisha hakuna linalokwenda vibaya. “Anaonekana mzima kabisa. Huu mwili utaongezeka ukikazana kunyonyesha.” “Mmmh! Maana nimekaona kadogo! Nikajua amechukua mwili wangu.” Sabrina akalalamika. “Ni mara chache sana kupata mapacha wanaozaliwa wakubwa. Hata kwa hizi kilo na siku walizozaliwa, wamejitahidi sana.” Yule daktari akaongea huku akiendelea kusoma. Akarudisha lile jalada na kumsogelea tena Sabrina.

Akafanya baadhi ya vipimo. “Unaonekana upo tayari kuleta wapili.” “Itachukua muda gani, maana hapa nimepoa kabisa.” Yule daktari akacheka kidogo. “Wengine wanachukua mpaka masaa. Lakini wewe una dalili za...” “Auuuuh!” Sabrina akalalamika kama aliyesikia kichomi kwa nguvu. Hawajakaa sawa, Sabrina akasukuma mtoto wa pili kama mchezo. Wakabaki wametoa macho. “Naona hawa wamekuja na upako wao.” Akaongea yule daktari wakati akimpokea mtoto. Hapo hapo akalia. “Na watoto wenu wanaonekana wapo sharp! Wanatoka na kulia!” “Hicho ni kitu kizuri?” Akauliza Jack. “Sana. Inamaana hata akili yao ipo sharp.” “Yess!” Jack akashangilia huku amembeba Jeiline. “Unasikia Jeiline? Mmezaliwa kuwa vichwa nyinyi, sio mkia.” Akaongeza Jack na kumsogelea Sabrina akijua Keiline atawekwa hapo kifuani. Jack alishatoa simu yake na kuchukua video. Akavuta kiti akakaa upande wa juu alipolala Sabrina. Kuanzia kiunoni kwenda chini alikuwa amefunikwa.  Baada tu yakukatwa kitovu, akawekewa Keiline kifuani.

“Sasa hapa utakuwa mtihani. Mbona hawana tofauti!” Sabrina akashangaa machozi yakimtoka, wakacheka. Akambusu. “Kweli bwana! Hebu mgeuze huku kwangu.” Sabrina akamgeuza. “Oooh my! Jeiline, unamuona baby Keiline?” Jack akaongea kwa hisia zote. Na yeye akambusu. “Nimefurahi kukuona Jeiline. Umekuja kwa wakati wa Bwana. Namshukuru Mungu umezaliwa mzima.” Sabrina akarudia maneno yale yale aliyomwambia Jeiline na kumuombea pia. Wakapata picha moja, wakaomba wamchukue na yeye asafishwe. Wakati huo tayari Sabrina alikuwa akishonwa na kusafishwa. “Umechanika, lakini sio sana. Nitakushona vizuri sana.” “Asante.” Sabrina akashukuru, akamuona Jack anambusu kila mara Jeiline. Moyoni akaendelea kumshukuru Mungu.

Alipomaliza kusafishwa na Keiline, Jack akaomba wapigwe picha ya pamoja, akachukuliwa video akimkaribisha Keiline. Kisha akawaweka wote kwa mama yao. Vikajaa vicheko hapo, Jack asiwe na wazo la pili. Akaomba atoke na watoto wake wote. Akaruhusiwa. “Akampigia simu Willy na kumwambia akae tayari na kamera, achukue video wakati anatoka na watoto. Sabrina akatingisha kichwa. “Unashuguli Jack jamani!” Sabrina akamshangaa. Akacheka tu na kutoka akiwa amewabeba binti zake wote wawili.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alipotoka tu wakaanza kupiga makofi. “Asante, asanteni sana.” Jack akaongea kwa cheko kubwa. “Sasa, naomba niwatambulishe kwenu mabinti zangu wawili. Jeiline Msindai na Keiline Msindai.” Wakapiga makofi na kusogea. Wote wakapoa gafla baada ya kukutana na watoto wa kizungu, Jack akawaona. “Msishituke jamani. Binti zangu ni wakizungu.” Pakazuka ukimya wa gafla. Jack akawaangalia kwa zamu usoni. Akaanza kwa mama yake, baba, dada zake, Willy, Pendo, Joy na kaka yake. Angalau kaka yake na Pendo wakaonekana kufurahia. “Naruhusiwa kumbemba? Nimenawa mpaka mikono.” Kaka mtu akamsogelea. “Na mimi naomba mmoja, nipate upako.” Pendo naye akaongeza. Wengine kimya.

     “Naomba msiwachanganye, wanafanana sana. Wakulia ni Jeiline.” Akamkabidhi Pendo. “Usichanganye hata kubadili hivyo vitambaa, Pendo. Vimewekwa alama maalumu. Bodo hatujaweza kuwatofautisha. Macho yako yaende naye. Na huyu, ni baby Keiline. Ndiye mdogo.” Jack akaongea na cheko akamkabidhi kaka yake bila hata wazo la pili. “Come on baby, Keiline!” Junior akambusu. “Karibuni sana kwenye familia.” Junior akaongeza macho kwa mtoto. Jack akacheka. “Nashukuru kaka.” “Vipi lakini? Daktari anasemaje juu yao?” Mzee Msindai akauliza baada ya kumuona vile Junior alivyosimama imara si kama yeye baba mtu kufa ganzi. “Wamezaliwa salama kabisa baba. Sabrina hakupata shida, amezaa kama mchezo. Na daktari amewaangalia, anasema wapo salama kabisa. Amempigia simu daktari wa watoto aje kuwatizama, lakini anasema hawana tatizo, na mama yao mzima kabisa.” Jack akamjibu baba yake na kurudisha macho kwa wanae.

“Labda sasa hivi atakuwa ananitaka mimi.” Jack akamsogelea kaka yake na kumchukua Keiline. “Naona hamu haijakuisha!” “Bado nahisi nipo usingizini kaka. Siamini kama waha ni wangu kabisa. Yaani nikirudi nyumbani, narudi nao!” Jack akaongea kwa kuhamasika wala asimfikirie mama yake na dada zake waliokuwa kimya muda wote.

Daktari mwingine akafika pale walipokuwa wamesimama kina Msindai. “Hongereni sana. Naona vijana wenyewe wameshatoka nje kabisa, na mganga mkuu upo hapa, sina wasiwasi.” Mzee Msindai akacheka. “Mganga hajigangi bwana! Bado wanakuhitaji hawa wawili.” Akajibu Mzee Msindai mwenyewe na kumpa mkono kama kusalimiana. Wakazungumza kidogo, akaomba akawatizame ndani. Jack akachukua watoto wake, akarudi nao ndani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya muda Sabrina na watoto wake wakatolewa kupelekwa wodini. Fist class kama jina alilopewa na Mungu ukumbwani linavyofanana na hapo. Misindai. Halafu mzee Msindai mwenyewe daktari mkongwe, bingwa wa watoto hapo nchini alikuwepo hapo. Waziri yupo hapo na aliyekuwa waziri wa afya naye alikuwepo! Sabrina akapendelewa chumba kizuri tu. Akaingizwa humo na watoto wake wawili, Jack akaingia akiwa amechangamka na Pendo yeye akaelekea kwa watoto moja kwa moja. “Sasa naenda kuchukua baadhi ya vitu nyumbani, nitarudi baada ya muda mfupi.” Akambusu mkewe na kutoka kwa ahadi ya kurudi bila ya kuchelewa.

Akaingia Junior, mkewe, Willy na Mzee Msindai. Wakampongeza Sabrina. Joy akamsogelea Pendo aliyekuwa na watoto, akamchukua mmoja. “Sisi tunaondoka shem ili upumzike. Najua utakuwa umechoka na hekaheka ya siku nzima ya leo, na hii kazi ya kuleta hawa watoto wawili hapa duniani! Unahitaji kupumzika. Tutakuona kesho.” Junior akaaga. Mzee Msindai naye akaongeza pongezi na pole. “Asanteni sana kwa kuja.” Sabrina akawapa mkono. “Sasa Joy?” Junior akamsogelea mkewe pale kwa watoto. “Naona twende. Tutakuona kesho Sabrina. Pumzika mama. Naona kazi haikuwa ndogo. Tumecheza ukumbini, naona kina dada nao wakasikia.” Joy akamfanya Sabrina acheke kidogo. “Hongera sana. Unahitaji kupumzika.” “Asanteni kwa kila kitu.” Sabrina akashukuru. “Acha mimi niwasindikize. Nitarudi Pendo.” Akaaga Willy, Pendo akaitika macho kwa mtoto, Joy akataka kumrudisha mmoja kitandani, Pendo akataka ampe ili awapakate wote wawili. Joy akampakatisha vizuri. Wakatoka. Pakawa kimya.

“Hongera Sabrina na pole.” “Namshukuru Mungu wala sikupata shida dada yangu. Naona Mungu amenihurumia.” Wakacheka kidogo. “Kwa kuwa watoto wamelala, na wewe pumzika kidogo, ili wakiamka uwe hata na nguvu. Sitaondoka mpaka Jack arudi, kwa hiyo usiwe na wasiwasi.” “Asante. Japo nahisi nipo kwenye mshituko. Siamini kama na mimi nina watoto!” Wakacheka kidogo. “Nimechoka, lakini usingizi naona haupo!” “Wewe funga macho tu. Ni wako hawa. Utahangaika nao mpaka uchoke. Lala.” Sabrina akafunga macho. Pakawa kimya. Wakasikia watu nje ya chumba wakizungumza kwa sauti ya chini kidogo. Ikawavuta masikio kusikiliza.

Kumekucha…

W

akamsikia mama Msindai akiongea kwa kulalamika. “Hakika ipo namna! Hii sio akili ya Jack mwanangu. Hata kama kupenda, kupenda gani kwa fedheha hivi! Anafurahia watoto wakizungu! Yeye mweusi, na mama yao maji ya kunde tu! Haya wakitokezea na hawa watoto hadharani si ndio yatakuwa maajabu!” “Mmmh! Heri wangekuwa weusi mama, angalau unafunika. Wazungu!” Akasikika Jena akiongeza kwa mama yake. Pendo akaanza kuhisi miguu inamwishia nguvu. Akatamani atoke awaombe wakazungumze nyumbani, lakini alikuwa amebeba watoto wote wawili na akajua wazi na Sabrina anawasikia.

“Aibu gani hii!? Niambie unawaambiaje walimwengu jamani! Watoto wanaitwa Msindai! Wakina Msindai weusi! Hilo hata Jack angelifikiria kama anaakili yake ya kawaida!” “Sasa wewe mama unahisi nini?” Wakamsikia Jena anamuuliza mama yake. “Hawa watu wanatoka Bagamoyo jamani! Tusilisahau hilo.” Moyo wa Sabrina akashituka kama kumeanguka chuma sakafuni. “Na mnakumbuka mara ya mwisho walimpeleka Jack hukohuko kwao Bagamoyo?” “Jack alisema wanakwenda kumtembelea bibi yao, aliwakaribisha.” “Sasa huko nahisi ndiko walikomlisha vitu vyakumwaribu akili mwanangu.”

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mungu Ametenda, Mpaka Masikio Yanawasha.

Majibu Yake Sabrina Kutoka Kwa Mungu Ndiyo Hayooooooo! Yameanza Kuwasha Masikioni Kwa Mama Msindai Aliyeshindwa Hata Kuiona Sura Ya Sabrina Na Kumpa Japo Pole Na Hongera Ya Kinafiki!

Je, Nani Atahimili Hizo Baraka Za Mungu Za Kushangaza?

Usikose Muendelezo…..

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment