Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 23. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 23.

 Fungate ya Jack&Sabrina.

Mwanzo mpya na ahadi zakudumu.

Harusi iliisha, Jack na Sabrina walichukuliwa chumba Hyatt hotel kwa siku mbili, ambapo siku ya tatu walikuwa wakisafiri kuelekea Afrika ya kusini kwenye mji wa Cape town, mwisho kabisa kwenye kona ya nchi iliyoingia baharini, eneo linaloitwa Cape point ambako ndiko Willy na Pendo walikokwenda na wao kwenye fungate yao na ndio walio watambulisha huko. Wakapasifia sana mpaka Jack na yeye akaona si mbayana wao waende huko. Sabrina na mumewe walifika huko wakiwa na siku 5 zaidi za mapumziko. Walikutana na hoteli nzuri sana na mazingira mazuri kama walivyosifia Willy na Pendo.

Mchana walikuwa wakitoka kutembea kidogo, na kurudi hotelini. Wakapata wakati mzuri sana wawili hao wa mapumziko. “Nikuombe kitu na kukuapisha Jack?” Sabrina akamuuliza Jack walipokuwa ufukweni wakitembea. Jack akasimama. “Nini?” Sabrina akavuta pumzi kwa nguvu na kujiweka sawa. “Usiwahi hata kwa kuropoka, kumtaja jina la aliyenipa hii mimba.” Jack akanyamaza. “Hata kwa mama yako mzazi. Acha ibaki hivyohivyo jinsi ilivyo. Ujulikane wewe kuwa baba wa hawa watoto, lakini siye aliyenipa mimba.” Jack akamtizama na kunyamaza.

“Au ulishasema?” “Hapana Brina. Ila nyumbani wanafahamu kuwa ulikuwa mjamzito kabla yangu.” Sabrina akafikiria. “Kwa hiyo unafikiri nilazima uwaambie mimba ni ya nani?” “Hapana. Nitaheshimu matakwa yako. Kwa wengine wote watabaki kuwa ni watoto wangu kabisa. Hata nyumbani nimewaambia watakuwa kina Msindai. Hakuna aliyepinga. Nakupenda Brina, na hata kuwa na hao watoto nahesabu ni upendeleo. Lakini najua ipo siku ukweli utatakikana kujulikana.” “Nakuhakikishia Jack, labda kutoka kwako. Kumtaja aliyenipa mimba mimi, litakuwa jambo la mwisho, na ninaomba Mungu anisaidie.” “Na watoto wakitaka kujua ukweli?” Jack akauliza. “Mimi si ni mama yao? Nakuhakikishia Jack, baba watakayemsikia kutoka kwangu ni wewe.” Sabrina akafikiria kidogo.

“Hawa watoto kama wanahisi na kuelewa, sauti ya mapenzi ya kweli waliyopata na kuifahamu mpaka sasa ni wewe tu. Mimi mwenyewe sifahamu jinsi unavyofanya wewe. Hata sijui jinsi ya kuzungumza nao zaidi ya kuwaombea tu.” Jack akajisikia vizuri sana. “Unajua ni nini ninachowafanyia hawa watoto?” “Nini?” Jack akataka kujua. “Kuwaombea kwa Mungu, kufuta mkosi waliowekewa na Tino kutaka kuwauwa wakiwa hawana hatia. Nikiwa peke yangu huwa natamka kama mwenda wazimu, kuwa wao kuletwa hapa duniani sio tatizo, Mungu hakukosea, analo kusudi nao. Nawaambia wanae baba wa mbinguni anayewapenda sana, na ndio maana ameamua kuwaonyesha mapenzi ya kweli kupitia wewe.” Jack akamfuta machozi.

“Ni kwenye maombi tu ndio naweza kuzungumza na hawa watoto, Jack. Ili kama nafsi zao zilisikia tokea mimba yao ikitungwa, au kama shetani alisikia na kutaka kuwapatiliza kwenye maisha yao hapa duniani, akome kabisa, na wao waelewe. Wanaupendo mkubwa sana unaowasubiri huku nje, sio wangu, wako. Nikikuangalia wewe hivyo, napata moyo wakuendelea Jack, na naamini Mungu anawajali. Sitathubutu kuja kuwaanzishia kitu kingine au mahusiano mengine ya mtu mwingine kama baba isipokuwa wewe. Hata wao waje waniulize wakiwa wakubwa Jack, nitawaambia wewe ndiye baba yao. Hilo halitakaa likabadilika. Ndio maana nakuomba Jack, usiwaambie vinginevyo. Sio wao wala mtu mwingine. Naomba iwe siri ambayo mimi na wewe tutazikwa nayo na ninaomba Mungu atusaidie. Kabla yakukubebesha mzigo mzito hivyo, unafikiri utaweza?” “Nitaweza Brina. Nitatumia hekima hata kwa mama, ili ibakie kama hivyo ulivyotaka.” “Asante Jack. Ni hilo tu.” Jack alijua amepewa jukumu zito, hakuna siri duniani, lakini akafurahia hiyo heshima.

Wakaanza kutafuta majina huku wakibishana kama watoto wadogo. Mwishoe wakaamua kuyaandika majina yote yanayowajia mawazoni. Yakiume na ya kike, wakiambiana kadiri siku zinavyozidi kwenda, watakuwa wakiyapunguza na wakijua jinsia ndio watakamilisha kabisa. Ushindani na kubashiri watakuwa watoto wa jinsia gani ukawashinda. Wakaamua wakifika tu Dar, kitu cha kwanza ni kwenda kuangalia jinsia. Wakakubaliana hilo. Kwa hakika walipata wakati mzuri. Walipomaliza muda wao, wakarudi Dar.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Walikuta wasimamizi wao wa harusi wakiwasubiri uwanja wa ndege. Wakapongezana na wao wakapata nafasi ya kuwashukuru kwa jukumu zima la kuwasimamia harusi, lakini kwa umbali mkubwa sana Pendo aliokwenda kwa Sabrina hata kabla ya harusi yenyewe. Kwa hakika Sabrina akawa amepata dada ambaye hakutegemea. Alimsimamia katika kila jambo na kumshauri kwenye mazuri tu ili kufanania na kina Msindai na aina ya wageni ambao waliwatarajia. Na kweli Sabrina alitokea katikati yao, akafanana na hadhi yao. Hiyo yote ni Pendo kumchukulia taratibu Sabrina na kumuelimisha kwenye mengi. Hakumdharau hata kidogo ila kumbeba kwa unyenyekevu kama alivyo Pendo mwenyewe.

Walifika jijini mapema tu. Wakawapeleka mpaka nyumbani kwao. Wakaambiwa mama yake Jack ameandaa chakula cha usiku, kuwakaribisha nyumbani wao kama familia sasa, na kufahamiana kwa karibu na ndugu wa Sabrina. Sabrina na Jack walipumzika mpaka jioni, ndipo wakaongozana mpaka nyumbani kwa Msindai.

Walikuta ndugu wa karibu wa pande zote wakiwasubiri. Familia ya Sabrina wote walikuwepo kasoro wadogo zake. Jack na Sabrina wakawashukuru wote kwa harusi nzuri sana waliyowaandalia, zaidi zawadi kubwa walizopata. Pesa yote iliyobaki baada ya maandalizi yote, usiku huo Juinor akawakabidhi. Hawakuamini. “Ni pesa yenu. Watu wasingechanga kama sio nyinyi. Kwa hiyo ni yenu.” “Tunashukuru.” Wakaonyeshwa zawadi zilizokuwa zimejaa chumbani kwa Jack. “Sasa hizo itabidi kukodishiwa gari ziwafuate.” Akaongeza mama Msindai. “Kwa kweli.  Maana hivyo zilivyo sijui tutamaliza lini kufungua!” Jack akaongeza na kufunga mlango.

Walipata wakati mzuri sana jioni hiyo. Hawakujua mzee Msindai alipata wapi nyimbo za Kingoni, anakotokea baba yake Sabrina, lakini zikaanza kupigwa. Kila mtu alikuwa akicheka vile anavyocheza. “Unapatia kabisa!” “Nakwambia mimi nimekaa sana na wangoni! Mpaka kuzungumza kingoni nilikuwa nafahamu, sema nimepoteza baadhi ya maneno.” Wakazungumza mengi wakifurahia na kupongezana mpaka wakaagana. Sabina akawarudisha wazazi nyumbani kwake, kwa ahadi ya kuwa kesho kama watawahi kutoka hospitalini, basi wafanye safari ya Bagamoyo kumuona bibi. Hilo likakaa sawa. Pendo naye akaondoka na mumewe na maharusi wao. 

Jinsia ya watoto aliobeba Sabrina.

K

wa kuwa walikusudia kuondoka siku inayofuata kurudi kwao Singida, asubuhi na mapema, Jack na Sabrina wakaanza mipango. Jack akampigia simu dereva wa nyumbani kwao kumtaka akanunue vyakula vya kupeleka kama zawadi kwa bibi yake Sabrina. Akamwambia akishanunu orodha nzima, awatafute na kuwapelekea. Sabrina naye akapiga simu asubuhi hiyo kumtaarisha mama yake kuwa watawapitia mapema tu, awasindikize Bagamoyo. “Kama kuna nafasi kwenye gari baba yako naye anaomba aongozane na sisi.” Mama yake akaomba kinyenyekevu. “Nafasi itakuwepo mama. Hamna shida kabisa.” Sabrina akajibu. “Na mimi nataka kwenda Sabrina.” Akasikia sauti ya Sabina dada yake. “Basi nyinyi mjiandae, naona chakula cha mchana leo tutakula kwa bibi.” Wakalifurahia hilo na kuagana.

“Naona safari imepata waumgwaji mkono wengi!” Sabrina akamwambia mumewe. “Na nani tena yupo safarini?” “Sabina, mama na baba. Nimewaambia ni sawa tu. Au kuna shida?” “Hata kidogo. Tena tukiwa wengi ndio vizuri. Wakaendelea kuzungumza mpaka walipofika sehemu ya ultrasound. Walikuwa na appointment ya saa tatu kamili. Mzee Msindai alifahamika vizuri sana hapo na ndiye aliyeomba wawaone asubuhi hiyo.

Waliingia chumbani, Sabrina akabadili nguo. Akaja mtu wakuangalia. Jack akasimama haraka kusogelea pale alipolala Sabrina. Akaanza kupitisha kifaa tumboni kwa Sabrina. Wakaanza kusikia mapigo yao ya moyo. Yalisikika vizuri sana. “Naona hawa watakuwa wakimbiaji!” Jack akaongea macho kwenye screen. Wakacheka, Sabrina ametulia tu. Wakawaonyesha wote wawili jinsi walivyolala. “Wanaonekana ni wazima kabisa. Mpo tayari kujua jinsia?” “Kabisa.” Akajibu Jack, Sabrina kimya akiangalia tu. “Haya, huyu wa kwanza niiii....” Akapitisha kile kitu tumboni kwa Sabrina taratibu. Kisha akajua. “Huyu wa upande huu huyu ni wa kike.” Jack akacheka. “Mwenzie?” Jack akauliza. “Na huyuuuu....” Akaendelea taratibu akitaka ageuke. Akamsumbua mtoto huko tumboni mpaka akageuka. “Na huyu ni wa kike. Mjiandae kupokea mahari hapa. Mnamapacha wa kike.” “Umesikia Brina? Mbona kimya mama? Tuna warembo wawili. Ulinzi lazima uwe mkali.” Jack akaonekana kuchangamka kuliko Sabrina.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Aliingia kwenye gari akatulia kitini. “Naona neema ya Mungu imenishukia. Anataka nife tajiri. Nikiozesha kila mmoja hapo kwa ng’ombe 30, 30! Mimi nitakuwa mtu mwingine kabisa.” Ikabidi Sabrina acheke tu. “Mama, sisi ni watu wengine kabisa!” “Nakuona ulivyofurahi.” “Hivi wewe umepaona pale nyumbani kwa kina Pendo kulivyopoa?” Sabrina akajaribu kufikiria. “Wanakila kitu wale, kasoro watoto. Wamehangaika, mpaka wanafikiria kwenda nje ya nchi kupandikiziwa. Sasa leo Mungu ametupa wawili kwa mpigo! Acha masihara mama. Kama wewe hujafurahi, acha mimi nifurahie.” Akaweka mziki, ukaanza kuimba na yeye akiimba. Sabrina anamsikiliza huku akicheka.

Wakaendesha mpaka nyumbani kwa Sabina. Kabla hawajashuka garini, akampigia simu dereva aliyemtuma vyakula vyakumpelekea bibi yake Sabrina. Akamwambia anamalizia. Ampe kama nusu saa. “Naomba usinicheleweshe Awali bwana! Nina mambo mengi.” “Nakuja bosi wangu. Mama alinituma pia.” “Sasa niambie ukweli. Umeshaanza kununua au bado?”  Awali dereva wa Misndai akaanza kubabaika. Jack akajua hajanunua. “Unajua nini? Acha tu, nitanunua mwenyewe. Endelea na shuguli zako kama umetumwa. Sihitaji tena ununue chochote. Sasa hivi naelekea sokoni mwenyewe.” “Acha kukasirika Jack. Nitajitahi..” Jack akakata simu.  Sabrina akabaki akimtizama. “Nini?” “Naomba usikasirike Jack. Tuwachukue kina mama hapa, tusimame pale sokoni. Tununue hivi vitu, twende.” “Amenichelewesha na kuniharibia utaratibu mzima!” Akalalamika Jack. “Haitachukua muda mrefu. Naomba utulie. Wewe sasa hivi ulikuwa ukiimba hapa, usiruhusu hasira bwana.” Jack akacheka. “Muone. Wewe unataka kufanya jambo zuri, liwe baya! Zawadi ni jambo zuri, ukianza kuonyesha ni kazi nzito kupata, inakosa maana. Tukiona tunachelewa, tutampa bibi pesa, tuachane na vyakula. Kwa hiyo tulia.” Jack akatulia.

“Sasa majina ya watoto?” Sabrina akacheka na kushuka garini. Jack akashuka kwa haraka na kumkimbilia. “Nipe basi hata busu lakunituliza. Si umeona pale kwenye gari nilishaanza kukasirika?” Sabrina akacheka sana. “Mimi nahisi naongezewa watoto niwe nao watatu. Haki kweli! Ni nini Jack?” “Nikukumbatie tu, nikubusu. Yule jamaa alivyokuwa anapitisha kile kitu tumboni kwako akiangalia watoto pale hospitalini nikawa nameza mate, nikasema ndio ingekuwa mimi pale!” Sabrina akashangaa sana. “Hivi ujue wewe Jack unahitaji msaada wewe!” Jack akaanza kucheka. “Ulikuwa uchi Brina!” “Ni tumbo tu ndio lilikuwa wazi Jack!” “Sasa mwenzio sikuishia tumboni.” Sabrina alicheka mpaka akainama.

“Mimi pale nikajua mwenzangu unaangalia watoto kumbe wala haupo pale!” “Kwa taarifa yako vyote viliendelea kwa wakati mmoja.” Sabrina alicheka na kubaki haamini. Mlango ukafunguliwa. “Karibu maharusi.” Alikuwa Sabina. “Kumbe bado sisi ni maharusi! Umesikia Sabrina?” “Naomba tuingie ndani Jack. Acha kabisa.” Akamvuta mkono, Sabina akawapisha mlangoni. Wakawakuta wazazi wapo tayari. Wakasalimia. “Mimi naona kama nyinyi mpo tayari, twendeni wala tusikae.” “Hamtakunywa hata chai!?” Akauliza Sabina kwa kulalamika. “Naomba iwe siku nyingine shemeji yangu. Muda umetubana haswa. Jumatatu natakiwa kazini. Lazima kesho tuondoke.” Sabina akabaki ameshangaa. Sabrina akacheka tu. “Tunashukuru sana shemeji. Ila naahidi tutakuja tena siku nyingine. Sasa hivi naomba twendeni tu. Sisi tulishapata kifungua kinywa. Na Pendo naye amemfungashia huyu vitu vya kula siku nzima. Hapo alikuwa anakula matunda kwenye gari, hata hajamaliza. Tutakuja siku nyingine, tukae kabisa.” Wakatoka. 

Safari ya Bagamoyo.

“Baba wewe kaa mbele na dereva wangu.” Sabrina akatoa wazo. Jack akamgeukia Sabrina akiwa amekunja uso. “Kaa na baba mbele Jack. Mimi nitakaa hapo nyuma yako.” “Au ukae tu na mwenzio mbele?” Baba yake akaongea kwa kujihami. “Atakuwa sawa tu. Wewe kaa mbele baba, usibanane nyuma na kina Sabina.” Sabrina akamshika mkono Jack aliyekuwa ameduaa, akamvuta mpaka upande wa dereva. “Sabrina!” Jack akanong’ona kama ambaye hajaridhika. “Bwana twende.” Sabrina akamfungulia mlango, yeye akapanda kiti cha nyuma. Jack akaingia na kucheka kidogo. “Unacheka nini sasa? Twende.” Sabrina akamuwekea msisitizo. “Naomba mfunge mikanda tafadhali, ndio tuondoke.” Jack akaomba kwa heshima huku anatuma ujumbe. “Nahisi utakuwa na ujumbe Sabrina.” Sabrina akacheka akijua Jack mwenyewe ndiye aliyemtumia.

     Akafungua pochi yake akatoa simu. “Pochi yako nzuri!” “Asante mama. Nimepewa zawadi na Jacinta. Dada yake Jack. Zipo set tatu zinafanana. Hii kubwa, ipo na wallet yake na kipochi kingine kidogo chakuwekea vitu vidogo vidogo.” “Umefunga mkanda mama Msindai!” Jack akauliza, Sabrina akajifunga. Akaona Sabina na mama yake wamekonyezana akacheka. “Sasa hivi nimefunga. Twende.” Wakamkonyeza Sabrina. “Mama Msindai!” Sabina akamfinya kidogo, Sabrina akacheka. “Huo ujumbe Sabrina!” Jack akamkumbusha Sabrina kusoma ujumbe. Akacheka na kuchukua simu. ‘Niongee nini?’ Jack akawa ametuma huo ujumbe. Sabrina akaanza kucheka. “Unanicheka Brina?” Jack akauliza nakumfanya Sabrina azidi kucheka. “Usisahau sokoni Jack. Na utulie.” “Sawa mama.” Akakubali kwa heshima, ukimya ukazuka.

Wakafika sokoni, hapakuwa mbali na anapoishi Sabina. “Tutashuka hapa sokoni kidogo. Hatutachelewa, ndipo tuendelee na safari.” Jack akawataarifu abiria zake wakati anaegesha gari. Wote wakaitika. “Twende Brina.” “Hamtahitaji msaada?” Akauliza baba yake Sabrina. “Hapana Mzee wangu. Nitaomba vijana hapo nje watabeba tu, usijichafue.” Sabrina akashuka. Wakaona wanacheka nje. “Huyu kijana anaonekana anampenda sana Sabrina.” “Baba anarudia hilo kila wakati!” Sabina akaingilia. “Ni kweli.” Wakatulia.

Baada ya muda wakaona Sabrina anarudi na vijana wakiwa wamebeba mizigo. Akawafungulia nyuma. Wakaanza kuingiza mizigo hapo, wote wakiwa wamegeuka. “Bibi yako atafurahi sana Sabrina. Asante kumkumbuka na yeye.” Sabrina akacheka tu. Jack naye akaja na mizigo mingine na vijana wawili. “Naona hapatakuwa na sehemu nyingine Jack. Inatosha. Tutamwachia pesa ajinunulie huko. Twende tuwahi kurudi.” “Naona wazo zuri.” Jack akawalipa wale vijana wakaondoka.

Wakati wanapanda kwenye gari, wakagundua baba yao amerudi kukaa nyuma. “Ungekaa tu mbele baba.” “Wewe kaa na mwenzio. Kwanza itakusaidia kujinyoosha.” “Nashukuru baba. Anahitaji kujinyoosha mgongo huyo.” Jack akaingilia haraka sana, Sabrina akabaki ameshangaa. “Njoo sasa.” Jack akamuita. Sabrina akacheka kidogo na kutingisha kichwa, Jack akacheka. “Njoo bwana!” Sabrina akaenda. Akamfungulia mlango, Sabrina akapanda akiwa amemsimamia palepale mlangoni. Akaanza kumtengenezea kiti. “Hapo vipi?” “Umelaza sana bwana Jack!” “Haya, Nishike mkono unyanyuke kidogo, nikinyanyue tena kidogo.” Akaendelea kumuwekea, abiria wao wakiwaangalia kwa kujiiba. Sabrina aliporidhika. Jack akambusu mdomoni, akafunga mlango. Na yeye akapanda.

          “Bibi yenu atafurahia sana hizo zawadi mnazompelekea.” Akavunja ukimya mama Sabina. Sabrina na Jack wakaangaliana. Jack hakujua aseme nini akabaki kimya, Sabrina akamuona anakunja uso. Akacheka. “Wewe ongea chochote bwana. Hakuna kitu sahihi. Ukoje Jack?” Akacheka na kunyamaza. Mara simu yake ikaita. Ikawa kama ameokolewa na hiyo simu. Alifurahi Jack mpaka Sabrina akaanza kucheka. Abiria wa nyuma wakiwatizama. “Ndio vizuri akapafahamu kwa bibi. Si ndio Jack?” “Kabisa.” Akaongeza Jack na kupokea simu kwa haraka kama ambaye hajui azungumze nini na hao ndugu zake Sabrina.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

     “Mbona Awali ameniambia umekasirika?” “Sipendi mtu anayesema ‘ndiyo’ halafu hafanyi. Kama angekuwa anamajukumu yake mengine, angeniambia mapema, mama. Mimi nakimbizana na muda.” Jack akamlalamikia mama yake. “Nilimtuma mara moja tu.” “Basi, nimefanya mwenyewe.” “Msamehe bwana. Mimi ndiye niliyemtuma. Nilitaka akanitafutie maboksi makubwa nianze kuweka zawadi zenu, ziondoke huku hata kesho.” “Sasa zawadi hizo za nini mama sasa hivi na wakati nilikwambia ni mpaka Sabrina afike kule aangalie na kuandaa sehemu? Hakuna sehemu yakuweka mavitu yote hayo. Uharaka ulikuwa ni wa manunuzi ya asubuhi hii, sio hizo zawadi.” “Jack!” Sabrina akamwita kama kumshitua aache kulalamika. Akatulia.

“Kwa hiyo mtakuja nyumbani usiku?” Jack akanyamaza. “Nitakupikia chakula chako unachokipenda.” Mama yake akaendelea kumbembeleza, Jack kimya kama ambaye bado amekasirika. Sabrina akampiga ngumi begani kumshitua. “Auuu! Sasa sijui tunarudi saa ngapi! Na kesho tunaondoka asubuhi sana, jumatatu nataka nirudi kazini ili nibakishe siku za likizo. Nizitumie Sabrina akijifungua.” Jack akajibu kisha akahamasika kama aliyekumbuka kitu. “Kwanza nimejua jinsia ya watoto wangu.” Hapo akaanza kucheka, mpaka Sabrina akacheka. “Ni jinsia gani?” “Labda nikwambie majina.” Sabrina akashangaa na kumgeukia.

“Mkubwa ataina Jeiline Msindai, mdogo wake ataitwa Keiline Msindai. Upo hapo mama Msindai.” Akamsikia mama yake akicheka. “Hongereni. Sabrina anasikia?” “Nasikia mama. Asante.” Sabrina akajibu akicheka. “Hongera sana mama. Sasa baby shower lini?” “Hapana mama. Naomba msianze jamani! Huyu Sabrina mlimchukua karibu siku kumi!” “Ni nane tu.” Mama yake akamrekebisha. “Ndio hizohizo tu hakuna tofauti yeyote ile. Ndio tumeoana tu mnataka tena habari nyingine! Hapana mama. Acha na mimi nikatulie na mke wangu. Heee! Shuguli haziishi!” Sabrina na mama Msindai wakaendelea kucheka.

“Wewe bado unalalamikia siku 8 zilizopita lini sijui! Hii shower itawasaidia kupata vitu vingi vya watoto.” “Hapana bwana mama. Nyinyi mnapenda shuguli bila kufikiria. Hapa tulipo kwenyewe hatujui tunaweka wapi hizo zawadi za harusi, leo mnataka kuongeza nyingine za watoto sijui! Nyumba yetu sio kubwa bwana. Acheni kuweka mipango yakujaza kupita kiasi.” Jack akaendelea kulalamika.

“Nisikilize Sabrina. Watoto wawili wanakuja na garama za diaper na baby wipes. Hela zitakuwa zinawaishia mchana na usiku.” “Hapana bwana mama, acha kumtisha Sabrina. Hatuwezi kushindwa kununua diaper.” “Wewe Sabrina usimsikilize Jack. Kubali wifi zako na Pendo wakuandalie baby shower nzuri upate zawadi nzuri. Watakaa chini, watakuandikia orodha nzuri ya vitu muhimu vitakavyohitajika vya watoto, kisha wagawane wao wenyewe na marafiki zetu. Halafu mimi mwenyewe nitakodi gari viletwe huko. Hutakuwa na haja yakununua vitu vya watoto au hata nguo za miezi ya mwanzoni. Sasa wewe umsikilize Jack, wakati huyo hajui hata vitu vya watoto! Utahangaika mwenyewe. Mimi nataka upumzike. Ufikirie kubeba tu. Mahitaji mengine acha watu wakusaidie.” Sabrina akaanza kushawishika.

“Basi ngoja nizungumze na Jack, halafu nitakwambia.” “Umemshawishi mke wangu mpaka amelainika! Sijui ukoje mama!” Sabrina na mama Msindai wakazidi kucheka. “Mwenzio ameona umuhimu wake tayari. Wewe kwa kuwa umekasirika tokea asubuhi ndio maana kila kitu unanikatalia wakati yote nayafanya kwa ajili yako! Zawadi ni zenu. Nia yangu ziwafikie zikiwa salama, na bado unakasirika!” “Nia nzuri lakini hapakuwa na kipaumbele mama. Mimi niliwapa maagizo vizuri tu. Nashangaa mpaka saa nne hamna vitu nilivyoagiza!” “Lakini si yameisha baba? Tupange mambo mengine?” “Mipango yako yakulazimisha bwana mama! Unachotaka nikumchukua mke wangu mje mumfanyie sherehe. Kwa nini msikusanye hivyo vitu bila yeye kuwepo?” “Sasa raha ya uzazi ataipata wapi mwenzio? Acha watu waje wampongeze, wamfurahie na yeye ajisikie vizuri.” Mama Msindai akaendelea.

“Mama Msindai siasa mpaka kwa mkwe!” Wote wakaanza kucheka mpaka ndugu wa Sabrina. “Umeuza agenda yako mpaka namuona Sabrina amekubali wala si kutaka tuzungumze tena!” “Sio sasa hivi. Wewe nenda kapumzike na mkeo mpaka karibu kabisa na kujifungua, akiwa anakuja kujifungua huku ndio...” “Hapana mama, naomba usianze tena.” “Sio mimi! Ni baba yako.” “Hapana. Nimemwambia baba nitafikiria. Na ninaomba usianze kulazimishia mama. Huko Singida kuna mapacha wengi tu wanazaliwa kila leo. Sabrina atakuwa sawa hata akijifungulia Singida.” “Jack...” “Kwa heri mama. Nakujua wewe. Hilo nalo ukilibebea bango, najua utamtia hofu Sabrina mpaka akimbilie Dar kujifungua, wakati mimi nipo Singida.” “Si umesema una siku za likizo wewe?” “Mama Msindai kwaheri. Mimi nakujua wewe ukitaka jambo lako. Mwishoe nitajikuta naishi Singida, nyinyi ndio mnakaa na mke wangu huku Dar. Hapana mama, kwaheri.” Sabrina na mama Msindai wakaendelea kucheka.

“Basi baba. Tutaongea vizuri mkija kwa chakula cha usiku.” “Ona mama jamani! Kwa nini wewe huwa hujui jibu la hapana? Nimekwambia sijui tunarudi saa ngapi kutoka Bagamoyo! Naomba usipange mipango yakutuhusisha na sisi.” “Ndizi za nazi nyingi na samaki!” Jack akaanza kucheka mwenyewe. “Tena sijui niongeze na lile pilau la Zanzibari? Niliweke minofu mingiii!” Mama Msindai alifanya gari zima wacheke.  Jack alishalainika na yeye. “Mimi naona niwapikie vyote. Au unasemaje Jack mwanangu?” “Lakini hatutakaa sana!” Mpaka mama yake akacheka kwa sauti. “Bwana ndizi zako tamu bwana na nimejua kwa nini hukuzipika jana, ilikuwa kusudi ili nirudi leo.” “Hapana. Ni ndugu zako wenyewe waliamua kuleta vyakula, na mimi ndio nikaona nipumzike. Wewe acha kufikiria mambo ya nyuma. Njooni jioni mle vizuri, tuagane kwa amani ndio muondoke.” “Utataka tena na kesho asubuhi tuje tule pamoja kabla ya kwenda uwanja wa ndege?” “Kwani itachukua muda gani!?” Mama Msindai akauliza kishawishi. “Si umemsikia mama? Basi ujue hatutakaa tukaondoka hapa Dar. Mama Msindai kwaheri.” Sabrina akazidi kucheka. Jack akakata mama yake akisikika akiendelea kucheka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Wewe muendekeze mama Msindai! Raha yake ni kutuona hapa kila wakati. Hata tukienda kwa chakula cha asubuhi, atataka tukae naye mpaka cha usiku ndio tuondoke.” Sabrina akacheka. “Anakupenda.” Akaongeza mama Sabina. “Sana. Unafikiri hilo lina ubishi mama yangu! Tatizo lake ni akitaka jambo lake, lazima liwe. Na akiona hajapanga hoja zake vizuri ukakubali, hana shida ya kukufuata ulipo akuweke sawa mpaka ukubali.” Wote wakacheka.

“Yaani hilo la baby shower kwa jinsi nilivyomsikia hapa, hiyo itafanyika tu. Unaweza kukuta anasafari ya Singida jumamosi ili kumuweka sawa Sabrina.” “Haiwezekani Jack!” “Sikutanii. Muulize Jacinta ambaye yeye ni mbishi kidogo. Huwa anamfuata mpaka ofisini kwenye vikao mpaka Jacinta aseme ‘ndiyo’. Akikataa, hana haraka wala jazba. Atatafuta tena muda ambao anajua upo na mambo mengi, anakufuata tena. Sasa na wewe si utachoka, lazima umkubalie tu.” Wakaendelea kucheka, angalau wakapata kitu chakuzungumza hapo.

“Kwa hiyo honeymoon mlikwenda wapi?” Akauliza Sabina na kufanya waangaliane na kucheka. “Sabrina alipapenda huko! Nilijua atakataa kuondoka.” “Jackson wewe! Sio wewe ndio ulikuwa hutaki kuondoka?” Wakacheka. “Ni Afrika ya kusini. Kwenye kona kabisa ya bara. Huo mji umeingia baharini. Unaitwa Cape point. Walikwenda huko Pendo na mumewe kwenye honeymoon yao. Wakapapenda, ndio wakaona na sisi twende. Nipazuri sana kwakweli. Kuna utulivu wa namna yake. Mipango inapangika, sema majina ya watoto ndio yaligoma.” Sabrina akacheka.

“Lakini nimesikia ukimwambia mama yako. Ni mazuri sana.” Sabina akasifia. “Sasa sijui kama bibi ataweza kuyatamka!” Sabrina akafanya wote wacheke. Walicheka sana huku wakimfikiria na kusema utundu wa bibi yao. “Umesema nani tena?” akauliza baba yao. “Jeiline na Keiline. Mabinti wa Msindai.” Jack akaongea kwa kujivuna. “Upo mama Msindai?” “Nakusikiza Jack. Naona majina yangu umeyakataa!” “Majina yako yale yakiutuuzima! Yaani unamuita mtoto utafikiri unamwita kibibi kizee!” Wote wakacheka. “Kwani alitaka kuwaitaje?” “Wala usitake kujua shemeji. Mtaishia kulala bure! Majina yenyewe mazito!” wakazidi kucheka. “Wewe bakiwa na Jeiline dada mkubwa, mdogo Keiline. Basi.” Wakaendelea kucheka njiani angalau pakatulia. Kila wakati walimuona Jack akimkumbusha Sabrina ale hiki na kile na kutaka kujua kama yupo sawa. Wakaendelea kukonyezana huko nyuma, mpaka wakafika kwa bibi yao.

Furaha aliyokuwa nayo huyo bibi, mpaka Jack akafurahia kufika huko. Aliita rafiki zake kuja kumuona mume wake ambaye ni Jack. Jack alikuwa akicheka kila wakati. Zawadi walizozileta, vyakula, bibi huyo aliimba kwa kutaja kwa jina akimshukuru kwa kimoja hadi kingine. Ilipofika saa kumi jioni Jack akaomba waondoke.

Palipo Na Amani, Uharibifu Nao Hunyemelea.

K

itendo chakumuona Sabrina kwenye harusi kubwa vile, iliyohudhuriwa na wakubwa wa nchi! Ukumbi wa thamani, kila kitu kilikuwa cha thamani na kutangazwa kuwa ule ni usiku wa Sabrina akiwa amepambwa kwa maneno mazito yaliyojaa sifa! Viapo vizito kanisani! Wakionekana ni kama waliojuana na Jack kwa muda mrefu! Ikazidi kumsumbua mkewe Max na kama wivu ukamuingia tena na Max mwenyewe. “Huyu Sabrina aliondoka hapa akisema anampenda sana Tino!”  Ikashindwa kuingia akili mwa mama Kundi. “Nakumbuka uliniambia ulimuuliza kabisa Sabrina kama kweli anampenda Tino kwa dhati!” Mama Kundi  akaongeza akisikika mawazoni akijaribu kuvuta kumbukumbu ya picha ya Sabrina na Tino aliowakarimu nyumbani kwake, na huyu Sabrina aliyekuwa bibi harusi wa Msindai! Max kimya.

“Eti Max?” “Alikiri kumpenda sana Tino.” Max akajibu. “Sasa haya mapenzi ya kwa mtoto wa Msindai mpaka kuolewa harusi kubwa hivyo, ni nini kinaendelea kwa huyu binti au ni tapeli huyu Sabrina?” Hapo Max akawa amepewa njia rahisi ya kutokea. “Ni tapeli tu. Alikuwa akitafuta pakuponea. Alipoona kwa Tino habari ndefu, kesi haziishi, mkewe kaja juu, akamtelekeza mwenzie.”  Akajibu Max kwa haraka na kuongeza. “Na ndio maana Tino aliporudi hakutaka tena mumzungumzie naye Sabrina, akakwambia uache tu. Si nakumbuka mwenyewe?” Max akamuuliza mkewe. “Na kumbuka. Maana mimi niliwaaga hapa vizuri kuwa wanakwenda anza upya. Tino akaonekana safari hii Mungu amemkumbuka, na yeye amepata mtu wake wakumfuta machozi! Kumbe ni yaleyale tu! Sijui Tino huwa anakosea wapi kwa hawa wanawake! Sabrina alionekana ni mtu anayemjali sana, si kama tapeli! Sijui ni nini kilitokea jamani!” Bado mama Kundi akashindwa kumuweka Sabrina kwenye kundi la Matapeli. Kwa jinsi alivyomuona na Tino, moyo wake ukakataa kabisa kumuweka kuwa tapeli. “Mimi nitazungumza tena na Tino kujua ni nini kilitokea.” “Acha bwana. Hayatuhusu.” Max akahamaki haswa. “Tino anatuhusu Max. Anatuheshimu sana yule kijana. Na sisi anatuhesabu kama ndugu zake tuliobaki hapa nchini. Kweli unataka aje asikie kutoka kwa mtu baki tu? Hapana kwakweli. Akipiga kusalimia, nitaanzisha hii topic.” “Basi acha mimi nizungumze naye.” Max akaona bora yeye azungumze na Tino, mkewe asije tibua mambo.

Kwa Tino.

Kipindi hicho yote hayo yanaendelea nchini Tanzania, Tino alikuwa nchini Italy kwa ndugu upande wa mama yake. Mengi yalimfanya akakimbilia huko. Lakini pia alikutana na matibabu mazuri yaliyochangia kuendelea kubaki kwake huko ili kuona kama watasaidia uponyaji wa huo mkono wake wa kulia. Na kweli, kwa muda mfupi aliokuwepo huko akifanyiwa matibabu, aliweza kurudisha asilimia 87 za uwezo wake wa zamani. Walianza kumfanyia mazoezi yaliyomfurahisha zaidi. Mazoezi ya kushika vifaa vyake vya uchoraji. Akaanza upya kama anayejifunza mwanzo kabisa wa uchoraji. Muda huo yuko huko, akaamua kuanza masomo ya muda mfupi mfupi kupatia kipaji chake leseni za kimataifa na akaamua kujifunza lugha ya kiitaliaono pia. Uzuri upande wa mama yake walikuwa na uwezo kiuchumi, na Tino hakukulia huko, kwa hiyo wakajisikia kuwajibika kumsaidia kwa mara ya kwanza akiwalilia shida.

Asidi na Asili Yake.

M

ax akampigia Tino. “Kwema huko kaka au kuna jingine tena?” “Jumamosi ile iliyopita tulihudhuria harusi ya kijana wa Msindai.” “Yule waziri?”  Akauliza Tino. “Hapana bwana. Yule waziri ni bosi wa shemeji yako, yeye waziri Msindai ana mke na watoto watatu. Yule mama Msindai mwenyewe aliyekuwa waziri awamu ya Mkapa, ana watoto wanne. Wakwanza na wa mwisho ni wakiume. Sasa huyo mdogo ndiye aliyekuwa akioa.” Tino akawa hajaelewa kwa nini yeye aambiwe yote hayo. Akaamua anyamaze asikilize. “Sasa bibi harusi ndiye ametuacha mdomo wazi na ndio kisa chakukupigia!” Tino akashangaa kidogo, ikabidi kuuliza. “Ni nani?” “Sabrina!” Pakazuka ukimya wa hali ya juu. Mpaka Max akaangalia simu. “Tino?” Akaamua kumuita ili kuhakikisha kama bado yupo naye. “Anaitwa Jack?” Tino akauliza. “Kumbe unamfahamu!?” Kidogo Max akashituka. “Nilimfahamu Jack kwa jina moja tu, tena kwa kupitia Sabrina mwenyewe tokea mwanzo kabisa naishi na Sabrina hapo Dar. Sikumjua kama ni Msindai!” Tino alisikika akiwa ameishiwa nguvu asiamini kama Sabrina alikuwa tayari kumuacha Jackson Msindai ili awe na yeye! Kidogo wasiwasi ukaanza kumuingia.

“Bwana yule mtoto sijui analoga vipi wanaume! Yaani kwa muda mfupi sana kumuingiza yule kijana kwenye mstari mpaka kapagawa! Kijana wa Msindai amechanganyikiwa kabisa! Amekusanya mawaziri wa awamu ya tatu ambao walikuwa wakifanya kazi na mama yake pamoja na viongozi sasa wa awamu hii wanaofanya kazi na Waziri Msindai huyu wa sasa. Kulikuwa na ulinzi, bila kadi huingii hata kanisani! Yaani kanisa lilifungwa kwa ajili hiyo tu. Sijaona watoto wa mtaani pale au kijiweni. Watu wazito watupu na wakatangaza eti ile ilikuwa ni siku ya Sabrina. Bwana Jack alimpamba Sabrina! Hicho kiapo alichomuapia Sabrina, mawaziri mwenyewe walisimama wakati Jack anatoa kiapo chake kanisani. Ikabidi na wengine pia tusimame tu, dogo! Kilikuwa kizito kisichopimika kikawaida. Nikajua wazi na yeye yule mtoto wa Msindai kashawekwa sawa. Amelogwa, hajitambui anachofanya. Sabrina amempika, mpaka akapikika.” Tino kimya.

“Si kawaida aisee! Yaani mpaka sasa shemeji yako haiingii akilini. Hata kama ni mapenzi, si kuchanganywa kwa aina ile! Maana si mlikuwa naye hata miezi sita haijaisha? Sasa iweje kijana akolezwe na mwanamke kama Sabrina!? Eti walipoingia tu ukumbini, eti wakatangaza watu wasikilize wimbo wa Jack kwa mkewe! Sasa wimbo wenyewe ndio utachoka. Ni ule wa Perfect! Mimi pale ndio nikachorea mstari na kusema huyu kijana wa Msindai kafunikwa kabisa, hajui nini anazungumza. Na mbaya zaidi mbele ya wasomi tunaojua maana ya maneno wa ule wimbo bwana!” Max akaendelea kama anayesoma ngonjera. Tino kimya akisikiliza.

 “Eti mapenzi yao yalianza zamani tokea watoto! Si ‘juju’ hiyo au nini?”  Max akauliza asijue Tino yupo mbali sana. Amerudi mbali mno. “Huku ishakuwa usiku sana kaka. Tutazungumza wakati mwingine. Lakini ni kweli, Jack hajakosea. Alikuwepo kwenye maisha ya Sabrina hata kabla yangu. Na Sabrina alikataa mwaliko wakumfuata Singida ili abaki na mimi kuniuguza. Kwa hiyo ni watu wa muda mrefu. Ni kijana aliyekuwa akimfuatilia sana Sabrina tokea wapo chuoni.” Pakazuka ukimya kwa Max. Tino akakata simu akiwa yupo kwenye hali mbaya asijue ni nini anachojisikia kwa wakati huo. Simu ya Max ilimvuruga vibaya sana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Tino alibakiwa na simu mkononi. Akakumbuka mwanzoni kabisa Sabrina kufika kwake na kumsaidia, alimwambia aina ya maombi yake kwa Mungu. Kilio chake na matamanio yake ambayo anamlilia Mungu ampe yeye. Akamwambia ni makubwa sana ambayo hayaendani na jinsi alivyo. Ni kama ya wale wasichana warembo kabisa, lakini Tino akakumbuka Sabrina kumwambia anayo imani kubwa sana kuwa Mungu atamfanyia na yeye. “Au ndio ushirikina huo anaousema Max, sio Mungu?!” Sauti nyingine ikamtahadharisha Tino, akatulia kidogo.

Lakini akakumbuka jinsi alivyokuwa akimtia moyo kwa upendo kuwa na yeye ajipe moyo na amwamini Mungu atamponya tu. “Angegusia hata swala la mganga kidogo!” Akajirudi Tino, maana neno alilokuwa akilisikia kutoka kinywani mwa Sabrina ni Mungu kila wakati, wala si kujaribu kumpeleka hata yeye kwa mganga ili apone! Akakumbuka jinsi Sabrina alivyokuwa akijituma kwake akimwambia anafanya kwa uaminifu kama akifanya kwa Mungu. Akijua Mungu anaangalia kila anachomfanyia yeye. Kwa mara ya kwanza Tino akapata muda wakufikiria, akaingiwa hofu ya ajabu na kuweka simu pembeni. “Iweje niwe nilijichanganya!?” Akajiuliza na kuogopa asije kuwa alidanganywa, akaamini bila kufikiria akaishia kumtenda Sabrina kinyume na alivyostahili. “Lakini Max hawezi kuwa alifika umbali wote huo kunidanganya! Ili iweje?” Akajaribu kumtetea Max huku moyo ukisita kwa hofu akitamani isiwe tofauti.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment