~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ikaita
mara mbili akapokea. “Nimeomba ufikirie unipe jibu
Brina. Naomba usiharakishe.” “Sihitaji kufikiria Jack. Kwa kuwa sina
chakufikiria. Nilipaniki mpenzi wangu. Nilipaniki kusikia ni watoto wawili.
Nikahisi kama giza na nikaona kama utalemewa na watu watakusema zaidi. Najua
umekasirika Jack, lakini nakuomba unifikirie na mimi ni binadamu. Kuna sehemu,
nawakati naingiwa hofu sana. Huwezi amini jinsi ninavyojilaumu nakutamani kurudisha
siku nyuma mpaka siku nilipoenda kumsaidia Tino, niwe nimekuja huku halafu
nikosee na wewe, sio yeye. Huyo mtu hayupo mawazoni kwangu kinamna hiyo,
nimpaka mtoto aanze kucheza. Unanielewa Jack?” Sabrina akauliza maana
Jack alikuwa kimya kabisa.
“Kwa hiyo unachotaka kuniambia kila hao watoto watakapokuwa wakicheza,
utakuwa unamkumbuka Tino?” Sabrina akafunga
macho, akajua siku hiyo ni yakuteleza maneno. “Sasa
hivi walikuwa wakicheza hapa, nikakukumbuka wewe mpenzi wangu. Nikasema Jack wangu
angekuwepo, angefurahia. Na ndio maana nikakupigia.” “Unanidanganya Brina.”
Akajilalamisha Jack. “Hakuna kiumbe anayenipenda hapa
duniani kama wewe Jack. Na mimi si mjinga. Nishafanya kosa, siwezi kurudia
kosa. Leo umenithibitishia kwa umbali mkubwa sana kuwa mimi na hawa watoto ni
wako. Sasa hivi wala siogopi tena.” Kimya.
“Jack?” Kimya. “Njoo
basi mpenzi wangu. Najua nikikushika utatulia. Najua nimekushitua, lakini
umepokea ujumbe tofauti, kipenzi changu. Sikuwa na maana uliyofikiria wewe au
anayotaka kuitumia shetani kutugombanisha mimi na wewe.” “Sasa nikirudi
utanishika tu au utanituliza kidogo? Maana mimi hali mbaya Brina.” “Kuanzia leo
tunaishi kama tulivyokabidhiwa siku ya mahari.” “Usinidanganye Brina!” “Kweli. Mimi si mkeo?” “Ndio mimi nikashangaa,
baada ya juhudi zote zile alizofanya baba yangu mpaka kukutoa pale hadharani,
na kukulipia tena zaidi, tunatoka pale, baba anajua ameniolea mke! Kila akipiga
anauliza mkeo hajambo, kumbe hajui huku nyuma umenigeuka.” Sabrina
akaanza kucheka moyoni. Jack alilalamika kama mtoto mdogo.
“Njoo mpenzi wangu. Kuanzia leo tunaishi kwa kuzungumza, hamna kubeba vitu moyoni.” “Kama ndio hivyo basi acha mimi nianze. Wewe ni mke wangu Brina, lakini hunitaki.” Sabrina akashindwa kujizuia akaanza kucheka. “Usicheke bwana.” “Njoo Jack wangu. Mimi mwenyewe nina hamu na wewe, nakaribia kuchanganyikiwa. Hapa nishaanza kutoa nguo.” “Utanifanya nipate ajali Brina. Natafuta sehemu nigeuze gari.” “Taratibu bwana. Sasa unataka unikute wapi? Hapa au chumbani kwako?” “Ukienda kule kwangu ndio nitajua umeamua kabisa.” “Sawa. Utanikuta nikikusubiri.” “Nakushukuru Mungu wangu. Acha nipige simu kazini niwaambia leo siendi, nalala na mke wangu.” Sabrina akacheka na kukata simu.
Aluta Kontinua.
S |
iku hiyo
akaamua amtulize Jack haswa. Akahamia chumbani kwa Jack na akaoga hukohuko bafuni
kwake. Wakati anamalizia, akamsikia Jack ameingia. Akacheka. “Na mimi nije?”
“Subiri kwanza nakuja kukupa sababu yakuoga.” Jack akashangilia sana. Sabrina
akatoka na tumbo lake akiwa amejikausha. Mchana huo jua kweupe nje, wawili hao
wakaanza mapenzi ya kiu. “Asante Brina.” Jack alishukuru huku akiendelea kufaidi
penzi. Akashangaa Sabrina ndio akaonyesha uchu kumzidi yeye. Jack hakumuelewa.
Aliendelea kumng’ang’ania hapo kitandani mpaka akaridhika yeye na kujitupa
pembeni. Jack akashangaa amepotelea usingizini. Akamfunika vizuri na kurudi
kumkumbatia.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Wawili
hao maisha yakaanza upya yakichukua picha ya mke na mume. Jack akasaidia
kuhamisha mizigo ya Sabrina chumbani kwake. Akampisha kwenye sehemu ya
makabati, angalau Sabrina naye akapata nafasi. Akapanga mizigo yake hapo.
Maisha yakaendelea kwa wawili hao. Jack akiwa ametulia, hamna tena hasira.
Anapata penzi muda na wakati wowote anaotaka, tena Sabrina mwenyewe ndio
akaonyesha uhitaji zaidi.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Sabrina akashangaa siku hiyo jioni akipika, Sabina anampigia. “Kwema!?” “Mbona unashituka? Nataka kukusalimia tu.” Sabrina akacheka. “Nashukuru dada yangu. Sijazoea kupata simu kutoka kwenu za salamu. Itabidi kuanza kujifunza.” “Sasa mbona na wewe mwenyewe hata huwa hupigi?” “Da Sabina! Napiga nakwambia nini? Naanzia wapi wakati hatukuwahi kuwa na huo utaratibu na wewe wakati wote ulikuwa ukilalamika upo busy!? Naogopa kukusumbua.” Sabina akatulia kidogo.
“Unaendeleaje lakini?” Sabrina
akauliza. “Vizuri tu. Mbali na salamu pia nilitaka
nikukaribishe kipindi cha harusi ushukie kwangu.” Sabrina akanyamaza. “Hata wakina mama watakuwa hapa kwangu. Ndio nikaona angalau
na wewe utokee hapa. Naona kama itakuwa heshima zaidi! Ndugu wa mke na bibi
harusi tunatokea sehemu moja.” “Wazo zuri, lakini nahisi kama tumechelewa.”
“Kwa nini?” Sabina akauliza akisikika kuishiwa nguvu kabisa. “Familia ya kina Jack waliweka mipango tayari. Nafikiri Jack
aliwaambia huwa nakuwa nashuguli nyingi sana nikiwa huku. Hivi hii jumamosi
nitakuwa huko, kushugulikia maswala ya gauni.” “Basi shukia kwangu.” “Nitakuwa
na Jack hotelini.” Sabina akanyamaza.
“Natamani kama ningejua mapema.” “Kwa hiyo nani atakusaidia kutafuta
hilo gauni?” Sabina akauliza. “Huyo dada anayenisimamia, mama yake Jack na dada yake mkubwa
atakuwepo. Nikikamilisha maswala ya gauni, mama yake Jack alitaka nitulie hapo
Dar mpaka siku ya harusi nyumbani kwa huyo dada na mume wake wanaotusimamia
harusi, lakini Jack amekataa. Anataka nirudi naye hiyo jumapili. Amelalamika
anasema week mbili ni nyingi sana. Labda siku tatu. Sasa nilimsikia hapa jana
akibishana na mama yake. Mama yake akimwambia nilazima niende Dar week mbili
kabla ya harusi ili nipate muda wa matayarisho na kupumzika. Akamwambia sehemu
ilishandaliwa. Napo Jack ni kama alikataa, mama yake akaishia kusema ni lazima
niende nikapumzike japo hata kwa siku 8 kabla ya harusi. Sasa sijui nitakuja
lini huko, ila najua sehemu ilishaandaliwa tayari na kuna mipango kabisa.”
“Mmmh! Basi mwaya.” Sabina akaongea kwa kusikitika.
“Lakini nashukuru sana kwa kujali dada yangu. Nashukuru.” “Basi
nikuombe kitu Sabrina.” “Karibu.” Sabrina
akajibu kwa unyenyekevu tu. “Mimi najua haukuwa na
mahusiano mazuri na watu wa humu ndani, yaani sisi kwa ujumla, lakini kumbuka
bado sisi ni ndugu zako.” “Sawa dada.” Sabrina hakutaka ubishi.
Akakubali. “Yapo makosa ulitendewa hapa nyumbani. Lakini
kama ulivyoona, wazazi walijirudi Sabrina. Umewaletea heshima. Wewe ndio
wakwanza pale ndani kuolewa. Hapajawahi kufanyika harusi, harusi yako ndio ya
kwanza. Usiwanyime hiyo furaha.” Sabrina akatafuta mahali akakaa.
“Labda sijaelewa! Nilitakiwa kufanya nini ambacho sijakifanya kwenye
hii familia jamani!?” Sabrina akaanza taratibu tu. “Sitaki tukosane Sabrina. Mimi nilikuwa natoa tu ushauri.”
“Sawa kabisa. Ndio nauliza safari hii nilitakiwa kufanya nini tena? Maana
niliacha shuguli nzima ya mahari yangu mikononi mwenu, tena nikiomba muiongoze
mtakavyo nyinyi mpaka tukafanikiwa. Mimi na Jack hatutaki kitu kingine zaidi ya
harusi ambayo inaandaliwa na kina Msindai. Sasa mimi nilitakiwa kufanya nini?
Tafadhali niambie tu pale nilipotakiwa kufanya, sikufanya nione kama nitaweza
kurekebisha.” Sabrina akaongea kwa kulalamika.
“Mimi sijui, ila nimeongea tu.” “Hapana. Lazima unalo wazo ndio
maana umeongea hivyo. Naomba uongee tu. Mimi nitasikiliza.”
Kimya. “Da Sabina?” Sabrina akaita. “Mimi naona si sawa wewe kutokea ukweni kuelekea harusini.
Mambo yako ya harusi, tulitakiwa sisi ndio tukuandalie.” “Unaposema sisi ndio
kina nani dada yangu? Nani ambaye ashawahi kuwa tayari hapo nyumbani
kushugulikia mambo yangu bila malalamiko, na kusema nimezidi matatizo? Ambaye
leo amenipa msaada nikasema hapana, sihitaji
msaada wako, ninaye mtu wakunisaidia? Naomba uwe mkweli dada. Niwakatalie kina Msindai
leo, halafu iweje?” Kimya.
“Hivi unajua nimekaa hapo Dar kwa muda gani nikihangaika bila mtu
hata mmoja wenu kunitafuta kujua nipo wapi na ninaendeleaje?”
Kimya. “Kaka yupo mzima na kazi yake. Wewe upo hapohapo
mjini. Mama na baba wapo Chalinze. Nimeondoka nyumbani zaidi ya miezi minne,
sijakuta ujumbe hata wa mmoja wenu kunitafuta kujua nipo wapi na ninafanya
nini! Leo naanzia wapi kukataa hifadhi ya kina Msindai hapo Dar? Ningejuaje
kama safari hii shuguli zimepungua, unaweza kuniweka nyumbani kwako? Hakika
ungeniambia mapema, ningeshukia nyumbani kwako! Sina kinyongo na yeyote yule.
Ila utaratibu wa nyumbani ndio upo hivyo dada, na wewe ni shahidi.”
Sabrina akaendelea taratibu tu.
“Halafu pia sitokei kwa kina Msindai. Natokea kwa dada mmoja anaitwa
Pendo, ambaye yeye na mume wake ndio watatusimamia harusi mimi na Jack. Ni msichana
ambaye amekuwa na kina Jena dada yake Jack. Anaonekana ni dada mzuri tu. Jack
anasema amesoma na ana kazi nzuri sana, pengine wewe wa huko jijini unaweza
kumfahamu. Mimi nimeanza kufahamiana naye zaidi kwa kuwa karibu kila siku
ananipigia simu kunijulia hali na kuweka mipango ya harusi. Sina chakuongeza
huko dada yangu. Wamejipanga haswa. Wanaratiba yangu ya kila kitu, ninachosikia
hapa ni wakigombana na Jack sababu ya muda. Sasa hebu niambie dada yangu,
nilitakiwa kufanya nini hapo?” Sabrina akauliza
taratibu tu.
“Basi Sabrina.” “Hapana. Sitaki lawama baadaye. Niambie tu kile
nilichotakiwa kufanya dada. Maana hata mimi mwenyewe kuna mambo Pendo ananipigia
na kuniambia hata sikujua kama natakiwa kufanya!” “Kama nini?” “Kuwekwa kwenye
sauna, sijui na waxing ya mwili mzima!” Ikabidi
hata Sabina acheke. “Kweli tena. Sasa hayo yote mimi Sabrina ningeyajua wapi
kiasi chakuomba msaada?” “Haya mwaya. Sisi tunakutakia kila la kheri. Kwa hiyo
na sisi tutakuona ukumbini kama wageni wengine?” “Hilo nalo pia sijui dada
yangu. Niamini nikikwambia sina nijualo zaidi ya nini na kipi kipo kwenye ratiba, basi. Ila lini vinafanyika, sijui.” “Basi
na mimi naomba uniombee niwe kwenye hizo ratiba zao. Angalau wakuone na wewe
una mtu wa kukuwakilisha.” “Sijaelewa dada. Unataka nikuombee ratiba ya nini?
Siku ya harusi au?” “Yaani hivyo wanavyotaka kukufanyia. Angalau na mimi na
mama tuwepo mdogo wangu. Mama na yeye azunguke
madukani au kwenye masaluni na wewe binti yake unayeolewa?” “Oooh! Kwa hiyo
mama ndiye amekutuma kwamba na yeye anataka kuwepo au unamuongelea tu?”
Sabrina akauliza.
“Nikitu tulichokifikiria kwa pamoja. Kwa ufupi na sisi tunataka
kushiriki Sabrina. Hata kama tulishindwa zamani. Tukakuacha peke yako. Basi jua
sasa hivi mimi nipo. Nipe tu nafasi ingine hata kwa jambo dogo tu.” “Na mimi
pia.” Sabrina akashituka kusikia sauti ya
mama yake. “Nimeshindwa kuvumilia. Naona mwenzangu
nimemtuma atuongelee wote, anaishia kujiuza peke yake.” Sabrina
akacheka. “Shikamoo mama.” “Marahaba Sabrina mwanangu.
Mnaendeleaje?” “Tunamshukuru Mungu sisi hatujambo. Nashukuru kwa kutaka kunisaidia.”
“Na mimi nijidai mwanangu! Sijawahi kuozesha.” Sabrina akacheka.
“Najua nilikuwa mkatili kwako Sabrina, mama. Nisamehe mwanangu.
Najua nimekosa, tumekuwa watu tusio kujali, lakini mimi naongea kwa niaba ya
baba pia, tusamehe mama. Tafuta jinsi utusamehe mama.”
Mpaka machozi yakamtoka Sabrina. “Mimi kama mama yako
nimekuwa nikikutamkia maneno ambayo yamekuumiza. Nimetubu mbele za Mungu.
Nimekuwa nikiyabatilisha na kukutamkia kuwa wewe ni mbarikiwa, sio mwenye
shida. Naamini Mungu amenisikia na kunisamehe. Nataka tuanze mahusinao mengine.
Inawezekana au unataka tukupe muda?” “Wala
hakuna sababu yakufanya hivyo mama yangu. Mimi nimesamehe. Na yameisha.”
Akasikia ukimya mkubwa.
“Nimesamehe kabisa jamani, na ninashukuru kwa kunikaribisha
kwenye umoja wenu. Hakika nilikua nikitamani. Lakini nafikiri wakati wa Mungu ni
sasa.” Wote wakajisikia vibaya sana. “Nisamehe mwaya Sabrina mdogo wangu. Nahisi nililemewa na
mambo, na mimi nikawa nakusahau ikawa ni mpaka unitafute. Sasa hivi ukitupa
uhuru, tutakuwa na sisi tukikupigia kukujulia hali.” Sabrina akacheka akijifuta
machozi.
“Sasa mama yangu? Nakaribishwa na mimi huko kwenye maandalizi?”
Mama yake akauliza kwa upendo. “Nitazungumza na Pendo. Nijue utaratibu wote. Nilimuachia
yeye kila kitu sikutaka hata kujishugulisha. Lakini sasa hivi nitafuatilia
kisha nitawajulisha ili kama mtaweza muwe mnajumuika na sisi.” “Basi labda
niseme hivi, nimeona au nimemuomba Sabina niwepo kwake kwa muda. Naweza na mimi
nikaenda hapo kwa Sabina week moja kabla ya harusi. Utakapokuwepo, uniambie na
mimi niwe nakuja tuongozane. Angalau na mimi nionekane ninashuguli.”
Sabrina akacheka tena.
“Au unaona tutakuingilia na wakwe zako?” “Hata kidogo mama. Mimi
siwaonei aibu hata kidogo. Ni vile sikuyajua haya yote mapema. Sikujua kama
mtataka kujihusisha kwa ukaribu huu. Imenitia moyo, na ninajisikia vizuri sana.
Nawashukuru kwa ukweli, wala sidanganyi. Nitazungumza na Jack juu ya kufikia
hapo kwa da Sabina. Ili...” Akamsikia Sabina na
mama yake wanapiga vigelegele, Sabrina akashangaa sana. “Yaani ndio mnanitaka kwa kiasi hicho!?” “Sanaaa! Mimi nishajidai kwa
rafiki zangu, sema tu nimechelewa. Nishatangaza kwa kila mtu kuwa kina Msindai
wanaoa kwetu. Wewe hukuona lile kundi la mashoga zangu walivyokuja nyumbani
kwenye mahari yako?” Sabina akamfanya Sabrina acheke sana. “Mimi nataka mahusiano Sabrina mama. Na mimi nifurahie uzazi
wangu. Mama yangu atanisema sana akiona unatokea ukweni, kwenda harusini.”
“Kama namuona bibi!” Sabrina wakafanya
wakacheke.
“Ashaanza kuulizia lini unawekwa ndani.” “Mmmh! Mwambie bibi
shachelewa! Alitakiwa kuniweka ndani mapema. Sasa hivi ni mama nakaribia kujifungua
mapacha.” Wakashtuka sana. “Nilikuhisi Sabrina, lakini nikaogopa kukuudhi. Nilijua umjamzito.
Hongera mama.” “Asante mama yangu.” “Basi mimi hata sikukujua! Niliona tu
umependeza.” Sabrina akacheka. “Hongera mdogo
wangu. Hongera sana. Unaingia kwenye ndoa na baraka.” Sabrina akavuta
pumzi kwa nguvu akijua pongezi hizo anayesababisha ni Jack. Wasingempongeza
hivyo kama angerudi nyumbani na tumbo hilo bila Jackson Msindai, akaeleweka. “Namshukuru Mungu.” Ndio kwa mara ya kwanza wanaweza
kumsikia Sabrina akiongea mambo yake ya ndani, na wao kumsikiliza.
“Kwa hiyo ndio miezi mingapi sasa?” Mama
yake akauliza. “Wa tano. Ila bado hatujajua jinsia.
Jack amesema mpaka tukitoka honeymoon ndio tutakwenda kuangalia jinsia. Ila
tulirudi jana kwa daktari. Amesema wote wapo salama, wanaendelea vizuri.”
Akamsikia mama yake akipiga vigelegele, Sabrina asiamini kama wamepokea vizuri
kwa kiasi hicho! Akawa anacheka tu. “Sasa nani
anakusaidia kazi?” Akauliza Sabina kwa kujali. “Hamna hata kazi hapa.
Kama kufua naona mama yake Jack amenirahisishia. Jumamosi hii alituma mashine ya
kufulia na kukaushia, na fundi kabisa. Wamehangaika hapa na Jack, naona
jumatatu wakafanikiwa. Usafi wa nje yupo kijana anakuja kusafisha. Na ndani
yupo dada mimi na Jack tulimuomba atusaidie kutafuta msichana wa kazi, lakini
Jack anahisi anafanya kusudi ili afanye yeye mwenyewe. Maana alisema wakati
anatutafutia, anaomba tumpe yeye hizo kazi. Anakuja asubuhi siku ya ijumaa,
anasafisha kila mahali, tunamlipa. Naona siku zinazidi kwenda, haleti msichana,
anakuja yeye tu.” Wakacheka. “Sasa chakula nani anapika?” Akauliza mama yake. “Chakula changu na Jack tu! Napika mwenyewe mama. Hapo sitaki
msaada wa mtu kunilishia Jack wangu. Hapana kwakweli.” Wakacheka. “Napika mwenyewe.” “Na wewe unapenda kupika! Najua hapo Jack
atafaidi.” Mama yake akaongeza kwa kumsifia. Sabrina akacheka. Emma
alishamaliza mitihani yake ya kidato cha sita na kuondoka hapo kurudi kwao.
Wakabaki Sabrina na Jack tu ndani ya hiyo nyumba.
“Sasa ukijifungua si utataka msaada?” Akaongeza
Sabina. “Jack kashamlalamikia mama yake juu ya huyo
dada kuwa anamuhisi hataki kutuletea msichana wa kazi ili afanye yeye mwenyewe.
Lakini akamwambia tutahitaji msaada zaidi nitakapojifungua na hadhani kama huyo
dada ataweza kwa kuwa anamajukumu yake. Ni mke wa mtu na watoto wadogo. Na tupo
kwenye mahusiano naye, hataki aone tumemkatili. Ndio mama yake ametuambia
atatuletea msichana. Tusiwe na wasiwasi. Kwa hiyo...” “Brina!” Akamsikia
Jack.
“Sasa Jack amerudi. Hakuna tena kitakachoendelea hapa. Huwa anataka
akiwepo hapa kila kitu kiwe kwake. Macho, masikio, mdomo mpaka mikono viwe
kwake tu. Hatutaongea tena...” “Mama Msindai upo?” Akaita
tena Jack, Sabrina akacheka. “Njoo jikoni, nazungumza na simu.” “Nani tena sasa
hivi wakati mimi ndio nimerudi?” “Nenda kamsikilize Sabrina.”
Mama yake akamsikia Jack akilalamika. “Ni mama na Sabina, we Jack. Acha
kulalamika.” Akafunga mdomo kwa mikono yote miwili. “Aibu zako.” Sabrina
akamcheka. “Shikamoo mama.” Jack akasalimia kwa
sauti. Mama yake Sabrina akacheka. “Marahaba Jack
mwanangu. Hujambo?” “Sijambo kabisa. Habari za nyumbani? Baba hajambo?”
Jack akauliza akiwa amesogea kwenye simu, Sabrina ameishika na kuweka kwenye
spika. “Hatujambo baba, nimepiga tu kuwajulia hali.”
“Tunashukuru.” Jack akamjibu mama yake Sabrina. “Na
mimi nipo shemeji.” Sabina akaingilia, Jack akacheka. “Habari shemeji?” “Salama tu. Haya, tuwaache ili upumzike.” “Tunashukuru
kwa simu.” Akamalizia Jack bila kuvunga, kuashiria ni sawa kabisa
wakifupisha mazungumzo. “Haya, muwe na jioni njema.” “Asante
mama.” Sabrina akashukuru na kukata.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Nilikuwa
na hamu na wewe!” Sabrina akacheka. “Mbona umekuja na furaha hivyo? Kuna habari
gani njema?” “Nimefurahi kukuona mpenzi wangu! Wewe vipi?” Sabrina akacheka na
kusimama. “Sasa unaenda wapi?” “Kumalizia kusafisha, nilikuwa napika kabla
hawajanipigia simu.” Akambusu mdomoni akasogea kwenye vyombo. “Kwema?” “Kama
hakuna lililojificha nyuma yake, naona wameamua kutafuta undugu na mimi kwa
hali na mali.” Sabrina akamsimulia Jack kila kitu, Jack akanyamaza. Hakuongeza.
“Sasa mbona kimya?” “Mimi sijui Brina. Mambo ya ndugu ni magumu! Magumu sana.
Ninachoogopa ni wasije kuharibu mwishoni. Mimi nataka kuoa Brina.” Sabrina
akamgeukia.
“Usifikiri
mipango yote inayowekwa ni bure! Ni kwa kuwa nimethibitishia watu na kuwahakikishia kuwa nimekusudia kuoa
kwa wakati tuliokubaliana, Brina. Sitaki kitu kiharibike. Ndio maana unaona ipo
mipango inayoeleweka. Haya mambo ya kujitokeza katikati, tena ya gafla, kukiwa
na mipango mikamilifu tayari! Inanitia wasiwasi mama. Kumebaki siku chache tu.
Watu wameshajipanga kwa kila kitu, kwa nini tena tuingize mambo mapya
katikati?” “Nafikiri nia ni nzuri Jack. Wanataka kurudisha mahusiano.” “Basi naomba
mama awe anafuatwa hapo kwa Sabina, na kukusindikiza popote atakapotaka, lakini
utulie kwa Pendo.” Sabrina akanyamaza.
“Nimekubali
Pendo na mume wake watusimamie katika kila jambo kwa sababu Pendo ametulia.
Nyumbani kwake pana utulivu wa hali ya juu. Pale hutapata mtu wa kukukera, wala
kukusumbua. Hivyo unavyomsikia Pendo kwenye simu, na kumuona siku ile kwa muda
mfupi tu, ndio yupo hivyohivyo. Mtulivu sana. Bado hajajaliwa watoto. Wanaishi
wawili tu na mumewe pamoja na msichana wao wa kazi, ndio maana hata mama ameona
kwake ni sehemu sahihi uende kwa muda upumzike kabla ya harusi. Pendo
amejiandaa kwa ajili yako Brina.” “Umejuaje?” Sabrina akauliza. “Ni rafiki wa
Jacinta na Jena. Wanafahamiana kwa karibu na anawashirikisha kila kitu
anachofanya. Ameshaanza hata kukununulia mahitaji yako a\nayoona utahitaji
pale. Namaanisha ameshaanza kukuandalia chumba chako. Sitaki tena michanganyo
Brina. Naomba turidhike na mipango iliyopo.” Sabrina akanyamaza
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Maandalizi
ya harusi yakaendelea vizuri, hapakuwa na tatizo. Watoto wa Msindai na marafiki
waligawana majukumu. Pendo msimamizi wa harusi yeye akawa akihangaika gauni la
harusi na vitu vyake. Kila alipoona magauni mazuri huko madukani, alipiga picha
na kumtumia Sabrina. Sabrina akapenda matatu, akawa anasubiriwa yeye tu kwenda
kujaribisha na kama kunamarekebisho kidogo yafanyike. Joy mke wa waziri Msindai
alikuwa akishugulikia wasimamizi wa mbele na nyuma. Akawa akimshirikisha
Sabrina juu ya sare na kutuma picha za hao watoto. “Au
sio sawa?” Joy akauliza. “Wewe fanya kile
unachoona kitafaa na kupendeza Joy. Wala katika hilo sina ushauri. Hao
wasimamizi ni juu yako. Ukiharibu ni wewe mwenyewe.” Joy akawa anacheka
kila akimtaka Sabrina mawazo na Sabrina kumuachia jukumu zima. Kuanzia nguo
zao, viatu mpaka jinsi ya kucheza ikawa juu yake Joy.
Sabrina
alitangulia siku 8 kabla ya harusi, tena kwa kulazimisha haswa. Ilibidi mpaka
mama Msindai awe mkali kwa Jack ambaye ilimbidi yeye abaki Singida bila Sabrina
sababu ya kuendelea na kazi ili kuweka siku za likizo kwenye harusi na
honeymoon. Alilalamika sana akitaka Sabrina amsubirie, waondoke naye Singida.
Hapo mama yake akawa mkali na kumwambia kama Sabrina hatakuja siku hiyo, basi kesho
yake angemuona yeye mwenyewe mama Msindai hapo Singida akimfuata Sabrina. “Usitake kutuharibia shuguli nzima, sisi wote tuje kuonekana
hovyo! Huyo bibi harusi mpaka sasa hana gauni la harusi wala viatu vya uhakika!
Unataka abaki huko muangaliane tu!” Hapo ndipo Jack akakubali, Sabrina
akaondoka.
Sabrina
Mjini Kabla Ya Harusi.
Kwa
mwezi mmoja tu tokea waachane kwenye mahari, Sabrina alibadilika haswa. Tumbo
likawa lipo dhahiri. Pendo na mume wake ndio walikwenda kumpokea uwanja wa
ndege, Pendo akabaki anamshangaa. “Usiwe na wasiwasi bwana!” Sabrina akawa
anacheka. “Nguo moja lazima nirudishe. Haitakukaa vizuri. Labda ile ambayo inaanza
kuchanua chini ya maziwa.” “Ile imejaa sana Pendo. Si itanichosha kutembea?”
“Ule mkia wa nyuma unatoka. Ukichoka tutakuwa tunatoa.” Wakaendelea kuzungumza
akielekea nyumbani kwa Pendo.
Ni
kweli Sabrina alikuta maandalizi mazuri. Kila kitu kipo kisafi na hali ya juu.
Vitu vipya na vizuri tupu. Kuanzia nguo za kulalia, mashuka, nguo zake yeye
mwenyewe za kuvaa, nje na ndani. Viatu vya kuvaa ndani ya hiyo nyumba na nje.
Nyumba ni tulivu kama alivyosema Jack. Safi kila mahali. Na mumewe akaonekana
hana tofauti na Pendo, watulivu halafu wote wakakutana wazuri. Akatamania ndoa
yao. Kasoro tu, hawakujaliwa watoto. Pendo na Willy walishahangaika kwa kila
mtaalamu waliyesikia anaweza kuwasaidia kupata mtoto, lakini ikashindikana.
Wamebaki wao tu wawili na msichana wa kazi.
Kulikuwa
na ratiba kuanzia siku hiyo anafika mpaka siku ya harusi. Alifika nyumbani na
fundi wa nguo akaja usiku. Akajaribisha magauni ya harusi, moja likamkaa vizuri
sana, wala usingemtambua kwa haraka kama ni mjamzito. Lilimkaa kama lake, wala
halikuhitaji marekebisho. Zuri haswa, Sabrina hakuamini kama ndio linamsubiria
yeye. Hilo likaisha na kupita vizuri.
Sabrina
akawa mwaminifu, kila anapotoka, lazima ampitie mama yake nyumbani kwa Sabina.
Wanaenda kuzunguka naye. Kama ni saluni, basi mama yake alikaa tu kwenye viti
akisubiria mpaka amalizwe. Wakati mwingine Sabina alikwenda na kuwa nao, wakati
mwingine alimpitia mama yao nyumbani kwa Pendo kama alirudi na Sabrina na
kurudi naye mama yao nyumbani kwake Sabina. Siku ambazo Sabrina hakuwa akitoka,
mama yake alikwenda kukaa naye hapo mpaka jioni Sabina akitoka kazini.
Anakwenda kumfuata na kumrudisha nyumbani mpaka maandalizi yakakamilika.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Jack alitua jijini tayari kwa kufunga ndoa. Yeye alifikia kwao. “Au na mimi nishukie kwa wasimamizi wetu?” “Acha ujanja Jack. Tulia nyumbani.” Kaka yake akamkatalia. “Unauhakika hakuna mawaidha kwa bwana harusi?” “Ndio maana leo usiku tuna bachelor party. Wanaume tunakwenda kukufunda.” Msimamizi wake, yaani mume wa Pendo, Willy akamuwahi. “Daah! Mafunzo hayo ningepewa na mwenzangu!” Wakazidi kucheka. “Wewe shida yako ni kumuona Sabrina. Pendo hawezi kukubali umuone hata iweje. Wewe twende tukafurahi leo, kesho unapewa mke, ukahangaike naye mwenyewe.” “Daah! Imekuwa ngumu zaidi nilivyofikiria!” Kaka yake akamwangalia na kucheka. “Dogo anaona kukaa mbali na mke siku 8 ni nyingi!” Rafiki wa Junior akachomekea. “Tutamtafuta tena baada ya miaka 5 halafu tumpe mapumziko haya haya tuone kama atayakataa.” Wakaanza kucheka. “Mitano Junior!? Mwaka tu.” Wakaendelea kucheka marafiki hao wa Junior wakitaniana hapoa nyumbani kwa mama Msindai.
Harusi ya Sabrina &
Jack.
I |
likuwa mida
ya saa kumi kamili jioni wakati kanisa zima limesimama, Sabrina akiingia
kanisani akiwa ameshikwa mkono na baba yake. Kweli uzazi mzuri! Mzee huyo
mfugaji tu, shule hamna wala salio halisomi vyakueleweka, lakini siku hiyo wakuu
wa nchi walisimama akiwa anaingia na binti yake hapo kanisani kulikokuwa
kumeimarishwa ulinzi haswa. Alifika mjini akasafishwa vizuri haswa. Kuanzia
kichwani mpaka mguuni, Sabina alihakikisha baba yake yupo vizuri. Alivaa suti
nyeusi nzuri ya hadhi, na shati jeupe. Akafungwa ua dogo lenye rangi ya njano, pembeni
ya mfuko wa suti. Kiatu cheusi, safi kinawaka. Alitembea kwa furaha na ujasiri,
akijua kina Msindai wanasubiria binti yake siku hiyo. Ile hali yakutizamwa na yeye,
na wakubwa wa nchi, akitembea katikati ya kanisa hilo kubwa, ikaweka furaha ya
ajabu sana ndani yake.
Ulinzi
nje na ndani ya hilo kanisa ulikuwa mkubwa haswa kwani ni kama bunge kuu
ilihamia hapo. Mawaziri wastaafu wa awamu ya tatu ambao walifanya kazi na mama
Msindai walikuwepo. Madaktari bingwa wenye majina makubwa nchini ambao walisoma
na kufanya kazi na Mzee Msindai, walikuwepo kumsindikiza kwenye kuozesha kijana
wao wa mwisho. Wabunge, manaibu waziri, mawaziri wa awamu hiyo ambao wanafanya
kazi na kutumika na Junior pamoja na marafiki zake ambao si wana siasa, pia
walikuwepo kushuhudia harusi ya mdogo wake, waziri Msindai. Bado marafiki wa Jacinta
Msindai ambaye ni kiongozi wa usalama wa taifa nchini. Jena naye alikuwa na
marafiki zake ambao nao ni madaktari kama yeye. Kwa hiyo kulikuwa na ulinzi
mkali sana.
Wasimamizi
wote walishajipanga mbele kabisa ya kanisa pamoja na bwana harusi, wakimsubiria
bibi harusi, Sabrina. Maandalizi ya tokea anafika jijini Dar kutokea Singida
mpaka anafikishwa hapo kanisani, Sabrina alikuwa akimshangaa sana Mungu. Kazi
na kujitoa kote alikokuwa akikufanya gizani, akifanikisha watu wanaosifika
hadharani, leo Mungu amemuinua na kumkalisha na wakuu! Yeye mwenyewe hakuwa
anaamini. Walishapita watoto wanne wakike kumwaga maua, kabla hajaingia. Kapeti
jekundu lililokuwa limetandikwa maalumu kwa ajili yake, lilijaa maua, kiasi ya
kwamba alikuwa akitembea, miguu unafunikwa na maua. Alivaa shela ndefu na nzuri
sana. Watu wote walikuwa wamesimama wakati Sabrina na baba yake wanatembea
taratibu, wakisindikizwa na mziki uliokuwa ukipigwa na vinanda hapo kanisani.
Kanisa lilipambwa vilivyo. Hata wadogo zake wakiume wawili, walienda kuombewa
ruhusa shuleni ili waweze kuhudhuria harusi hiyo. Hukuhitaji kuambiwa kuwa
Sabrina ameinuliwa.
Watu
wote pale kanisani walikuwa wakimsindikiza kwa macho binti huyo aliyefunga
kuoza kwenye familia ya Msindai. Hakuwa daktari, wala profesa au mwanasheria. Shule
yake ya mambo ya stoo ilibaki vilevile kichwani tena kwa ngazi ya diploma tu,
na hakuwahi kupata ajira na kuitumia shule yake. Akabaki Sabrina wa kutoka
Chalinze. Hakuwa mweupe akiwaka kama jua. Sijui miguu minene, au umbo namba 8
au 6. Alikuwa Sabrina mwenye mimba ya watoto mapacha. Anaolewa na Jackson
Msindai! Hata Jack mwenyewe hakuwa akijua ni kwa nini anachanganywa na Sabrina
kwa kiasi hicho.
Alisoma chuo kilichojaa warembo, lakini
akampenda Sabrina karibu kurukwa na akili. Alishatembea na warembo, lakini
nafsi yake ilimuhitaji Sabrina. Alimtizama akiwa anamsogelea, asiamini kama
siku hiyo anakabidhiwa watu watatu kwa mpigo. Wakati wengine waliojua Sabrina
kuwa anaujauzito usio wa Jack, wakimshangaa Jack na kumuhurumia, lakini kwa
Jack yeye aliona ni kama anakabidhiwa ulimwengu mzima na fahari yake. Tena kaka
yake alimtania na kumwambia ni ‘double blessings’.
“Nani
anamtoa binti huyo?” Akauliza mchungaji wa kanisa hilo, ambaye alipata bahati
yakufungisha ndoa hiyo ya kina Msindai watu wake wakaribu. “Ni mimi.” Baba yake
Sabrina akajibu, na kumkabidhisha kwa Jackson akimpa maneno machache kama
alivyofundishwa baba huyo. Isivyo kawaida, Jack alivyokabidhiwa tu, akatoa
shela na kumbusu kwa kina hapohapo. “JACKSON MSINDAI!” Mama yake akahamaki kwa
sauti ya juu, na wengine wote wakashangaa. Jackson akamuachia. “Sijamuona siku karibu
8 sasa! I missed her.” Jack akajibu kwa sauti na kumfunika. Watu
wakacheka kidogo wengine wakabaki wanashangaa. “Sorry ma!” Akamgeukia mama yake
ambaye alibaki ameduaa. Sabrina akacheka na kuinama. Vigelegele vikaendelea
hapo wakishangilia, ikabidi mchungaji aombe watulie. “Bado Jackson. Muda mfupi sana tutakukabidhi.” Mchungaji
akaongea akicheka. Jack akamshika Sabrina mkono, wakasogea mpaka mbele kabisa
alipokuwa amesimama mchungaji huyo, ibada ikaanza.
“Umependeza
sanaaaaa!” Jack akamnong’oneza Sabrina. Sabrina akacheka. “Na wewe Jack.
Nimefurahi umenibusu. Ninahamu na wewe Jack!” “Hata mimi. Mpaka nahisi
kuchanganyikiwa. Tukitoka...” Ikabidi msimamizi wa Jack, Willy, amguse. “Mnaongea
kwa sauti wakati wa mahubiri Jack! Tulia bwana.” “Okay. Samahani.” Jack na
Sabrina wakacheka na kunyamaza. Wakatulia mpaka mahubiri yalipoisha.
Ukafika
wakati wa kiapo. Yeye Sabrina akasoma kiapo cha kwenye kitabu tu, akamaliza.
Akashangaa mchungaji anatangaza kuwa Jackson ameandaa kiapo chake. Sabrina
akashangaa na kumtizama Jack. Jack akasogezewa kipaza sauti. “Mara ya kwanza kabisa kukuona Brina, moyoni nilijua kwa
hakika utakuwa mke wangu, wala si rafiki tu, japo ulinikataa.” “Jack!”
Sabrina akashangaa sana, tena kwa sauti. Watu wakacheka na vigelegele kidogo. “Muda wote nimekuwa nikikusubiri nikijua wewe ni wangu Brina.
Umekuwa ukipenda kusema neno au kutumia neno, ‘wakati
wa Bwana’. Kwangu naamini huu ndio wakati wa
Bwana kunibariki wewe kuwa mke wangu. Sichukulii hiki kiapo leo kama ahadi tu,
lakini nachukulia kama upendeleo mkubwa sana ambao Mungu amenipendelea hapa
duniani. Yaani mimi Jackson Msindai, kupata upendeleo wa kuishi na wewe! Kucheka
na wewe mchana na usiku! Kulia pamoja na wewe Brina! Mimi Jackson kupewa bahati
na Mungu ya kunitumia kuwa faraja yako unapopita katika kipindi kigumu kama magonjwa,
maradhi hata kutokuwa na furaha tu! Kwangu ni heshima ya pekee sana ambayo
hakuna kitu Mungu atanipa zaidi ya hii.” Watu walishangilia kana kwamba Jackson
amemaliza, lakini bado.
Kanisa
zima walisimama, Sabrina akifutwa machozi na Pendo kwa kuwa bado Jack alikuwa
amemshikilia mikono yote miwili, akitoa kiapo chake. Walipotulia akaendelea, “Nilishakwambia wewe Brina, hata mama nilimwambia hili. Siku
Mungu anakuumba wewe Sabrina, alikuwa akinifikiria mimi.” Watu
wakasikika
wakisema, “Waooo!” Jack
akaendelea huku yeye mwenyewe akifuta machozi. “Unanikamilisha
katika kila eneo la maisha yangu. Siku ya leo, nikisimama hapa mbele ya
mashahidi wengi, namwambia Mungu asante kwa upendeleo alionipa mimi kuniwezesha
kuwepo kwenye maisha yako Sabrina. Kwamba katika maisha yangu yote nitayokuwepo
hapa duniani, mimi Jackson Msindai, niyatumie kukupenda wewe, kukujali,
kukulinda, kuwa faraja yako mpaka kifo kitakapo tutengenisha.” Watu
wakazidi kushangilia sana. Ngoma zilipigwa, vinanda, vigelegele, waliokuwa na
hisia za karibu wakafuta machozi. “Naahidi kuwa
mwaminifu kwako Brina, naomba uendelee kuniombea, Mungu anisaidie.” Jack
akamaliza mpaka mchungaji akapiga makofi. “Waooo!” Akasikika mchungaji
huyo. Jack aliongea bila kusoma, akiwa amemshika Sabrina mikono yote miwili
mpaka mwisho.
Baada ya kutulia, wawili hao wakavalishana pete za ndoa, ndipo mchungaji akawabariki na kumruhusu sasa Jack ambusu mkewe. “Yes!” Akasikika Jackson akishangilia na kufanya kila mtu acheke. Akamgeuza Sabrina, akambumbatia vizuri bila haraka, watu wakicheka, akaanza kumbusu taratibu bila haraka. Akanyanyua mkono mmoja juu kama anayeshangilia huku akiendelea kumbusu mkewe. Mama yake akainama akitingisha kichwa. Watu walicheka sana na vigelegele. Askofu akamalizia ibada baada ya kuweka saini kwenye vyeti vyao vya ndoa. “Naomba niwatambulishe kwenu, bwana na bibi Msindai.” “Yesss!” Jackson akasikika kwa sauti na kumbusu tena Sabrina. “Kissing part is over Jack!” Willy msimamizi wake akamuwahi. Jack akacheka. “Kidogo tu!” Watu waliendelea na vigelegele wakati Jack na Sabrina wakitoka huku wakipunga mikono. Walipewa muda wakutosha kutoka wao wenyewe ili video na picha vichukuliwe vizuri ndipo wakafuata wazazi na wageni wale wa maana huku ulinzi ukizingatiwa.
Kutokana
na muda, lengo la Jack lakutaka wapelekwe kwanza hotelini kumpumzika baada ya
ibada, kabla ya ukumbini, halikutimia. Hapo kaka yake akawa mkali kabisa. Jack
akapoa. “Tunakwenda na Muda, Jack. Mapema sana tutamaliza.” Wakapelekwa kupiga
picha zao wao na familia za pande zote mbili. Bibi yake Sabrina alijawa furaha,
Sabrina alikuwa akicheka tu. Zilipigwa picha nyingi mpaka wapiga picha
wakaridhika, safari yakurudi ukumbini, ikaanza.
Ukumbini.
W |
aliingia
wageni wote, ndipo wakaanza kuingia wasimamizi wakicheza. Wote walisimama
wakati Jack na Sabrina wakiingia. Wao hawakuingia wakicheza kama wasimamizi wao,
ila kupunga tu mkono, Jack akiwa amekumbati mkono wa Sabrina mpaka katikati ya
ukumbi. Walipofika tu katikati wimbo ukabadilishwa, wa taratibu ukasikika,
wakajipanga wasimamizi vizuri, Jack akamkumbatia Sabrina, akavuta mkono wake wa
kushoto mpaka kifuani kwake akiwa ameushikilia vizuri, wakaanza kucheza mziki
wa taratibu wa, ‘Perfect’. Jack alikuwa akiimba huku akicheza vizuri
sana na mke wake. Ungependa kuwatizama. Walifanyia mazoezi huo wimbo wakiwa
Singida kwani Jack alimwambia lazima wataucheza huo wimbo. Na yeye Jack
alimuomba kaka yake uwe ndio wimbo wao wa kwanza kabisa kabla ratiba haijaanza.
Jack
alicheza na mkewe tu. Hakutaka mwanzoni mtu mwingine yeyote acheze. Mc
alishatangaza. Ni wimbo maalumu kwa Sabrina, kutoka kwa Jack. Walicheza vizuri
sana. Jack alimzungusha mara kadhaa na kurudi kumkumbatia na kuendelea kucheza.
Ukumbi ulipambwa vizuri ukatangaza umaarufu wa Msindai. Hata Jack wenyewe
alikiri hakuwahi kwenda kwenye harusi iliyo nadhifu kwa kiasi hicho. Hakika
kaka yake alimuandalia mdogo wake harusi nzuri sana. Familia ya Sabrina
walibaki wakishangaa wasiamini kama yule bibi harusi ni Sabrina. Kila wakati MC
alitangaza na kukumbushia kuwa ule usiku wakina Msindai waliutoa maalumu kwa
ajili ya Sabrina. Hakuna cha maana ambacho ungekitazama kwa Sabrina ukakiona
kwa nje haraka, ukavutiwa nacho. Msichana wa kawaida tu ila usiku huo ni kweli
Mungu alimthaminisha.
Ratiba
ilikwenda kwa haraka na ufanisi kama ilivyopangiliwa. Zawadi zilikuwa zikipokelewa
na watu maalumu mlangoni. Zilikuwa nyingi mno. Wakati watu wakila na kunywa
ndipo Jack na Sabrina walipokuwa wakipita kusalimia watu au wageni wa muhimu na
kupongezwa. Usiku huo kwa mara ya kwanza Sabrina akashika mikono watu wakubwa
wa nchi. Mawaziri wastaafu na wawakati huo waliokuwa meza za upande wa Msindai.
Sabrina mwenyewe hakuwa akiamini.
Akafika
kwenye meza ya Joy na mume wake wakiwa wamekaa na marafiki wengine. Junior
alikuwa amempakata mwanae Claire akiwa ananyonya kidole chake. Wote wakaanza
kucheka. “Lakini amejitahidi mwanangu. Si ndio mama?” Junior akambusu kichwani.
Alionekana amezidiwa haswa, anasinzia. Clai akawa anacheka huku akimnyoshea
kidole mdogo wake. “Si nilikwambia anti?” “Wewe unataka kulia Clai! Bora
unyamaze.” Joy akamuwahi mwanae wakiume huku kaka yao ametulia tu. Sabrina
akazidi kucheka. “Si nilikwambia umependeza eeh?” Sabrina akamuuliza kwa
upendo, akatingisha kichwa kukubali. “Basi mimi na anko tunakushukuru kwa kazi
nzuri uliyofanya.” “Mimi ndio nimemwaga maua mengi.” Akaongea na kidole chake mdomoni.
Wote wakacheka. “Niliona.” “Mwenzio aliishiwa maua palepale kanisani. Ikabidi
mama amtafutie mengine ya kumwaga hapa ukumbini.” Clai akamsemelea na kufanya
wazidi kucheka. Wakawashukuru wote. Junior na mkewe kwa kuwaandalia harusi
nzuri sana. Wakakumbatiana hapo. Wakiwa wanatoka hapo wakisogelea meza ya kina
Jacinta, wakapita kwenye meza ambayo alikuwa amekaa Max na mkewe.
Sabrina
akapigwa na butwaa. Jack akamuona na yeye akasimama. “Hujambo Sabrina?” Akamsalimia
mke wa Max. “Sijambo. Shikamoo.” “Marahaba. Hongera sana. Umependeza, na harusi
nzuri sana.” “Nashukuru Mungu. Na asanteni kwa kuja.” Sabrina akawapa mkono na
kumgeukia Jack. “Jack, huyu ni Max mwanasheria ambaye yupo karibu sana na Tino
na mkewe. Tino alinipeleka mpaka nyumbani kwao, ndipo nilipofahamiana na mke
wake pia.” “Nimefurahi kuwafahamu. Na asanteni kwa kuja kwenye siku muhimu
zaidi kwangu.” Sabrina akamsukuma kidogo na kucheka. Wakaondoka moyo wa Sabrina
ukiwa unadunda. Hata Jack alimuona amebadilika kama aliyeingiwa hofu.
Kabla
wajafika kwenye meza ya kina Jacinta, Jack akamgeuza. “Niangalie mimi.” Sabrina
akamwangalia. “Wewe ni mke wangu. Huna sababu ya kuingiwa hofu wala wasiwasi.
Umenisikia?” Sabrina akavuta pumzi kwa nguvu. Jack akamvuta karibu na kuanza
kumbusu akiwa amemkumbatia. “Kaka amefanya ratiba ndefu, mpaka maharusi
wameanza honeymoon hapahapa ukumbini!” Jena akafanya watu waanze kucheka mpaka
wengine wakawageukia. “Mbea wewe!” Jack akamwambia dada yake. “Mimi nimesema
tu.” Jena akajitetea huku akicheka. “Hayakuhusu.” Wakaendelea kusalimia.
Jack
hakutegemea kama mkuu wa chuo walichosoma hao wawili angekuwepo. Walifurahi
sana. “Sikuwa na uhakika kama ungekuja! Nilimuomba tu kaka akutumie mualiko
nikiwa sina uhakika kama ungeweza kuhudhuria sababu ya muda mfupi. Nimefurahi
sana na tumejisikia kutuheshimu. Karibu sana.” Jack akampa mkono na kumkumbatia
huyo mkuu wa chuo. “Ingekuwa ngumu kukosa tukio la kihistoria kwa nyinyi
wawili.” Sabrina na Jack walicheka sana. “Naona Msindai umepambana mpaka ukaoa
kabisa!” “Ilikuwa lazima nimiliki mkuu!” Wakaendelea kucheka. Jack akaomba mpiga
picha wao achukue kumbukumbu nzuri hapo wakiwa na mkuu wa chuo walichosoma.
Wakamshukuru tena kwa kufika, wakaendelea.
Walisalimia upande wa kina Sabrina, Jack akiwa na heshima zote akiwashika mkono kila mmoja mpaka wadogo zake. Wakashangaa akiwataja majina kabisa. “Nawafahamu muda mrefu tu, ni hivyo hatukupata nafasi ya kukutana. Baba!” Akamgeukia baba yake Sabrina. “Nashukuru kuwaombea ruhusa kina Sethi angalau kuhudhuria siku hii muhimu kwetu. Asante sana.” “Karibu baba. Tunashukuru kwa heshima uliyotupa.” Sabrina akamgusa bega. “Bibi anakuuliza lini utakwenda kumtembelea kwake Bagamoyo si Chalinze?” Jack akacheka na kumgeukia bibi yake na kumtizama Sabrina. “Wewe jibu Jack, acha kuniangalia mimi.” Jack akacheka tena kama aliyekosa jibu la haraka kisha akatumia akili ya haraka kujibu. “Naomba tusitoe ahadi ya siku. Lakini niseme nilazima tutakuja kukutembelea nyumbani. Pengine tukitoka mapumzikoni kabla yakurudi Singida, tunaweza kuja kukuona bibi. Tutampitia mama ili atulete.” Mama Sabrina akajisikia vizuri sana. Wakapiga hapo vigelegele. Watu wakawageukia, Jack na mkewe wakazidi kucheka. “Asanteni sana.” Jack akashukuru tena na kuondoka na mkewe. Akiwa amemuwekea heshima kubwa sana Sabrina.
0 Comments:
Post a Comment