Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 21. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 21.

Jack akamvuta mikono yote miwili akiwa amepiga magoti mbele yake, akaanza taratibu. Sabrina hakuwa hata anaona vizuri kwa kilio cha furaha, asiamini yanayomtokea. Sio kwamba anaolewa tu, amekuja kuposwa akiwa mjamzito, tena anaposwa na mtu wa maana! Amefanikiwa kuleta wakubwa wa nchi nyumbani kwao! Hata baba yake alimshukuru kwa hiyo heshima kubwa kabla hawajaona ugeni wenyewe.

“Sasa naelewa ni kwa nini moyo wangu ulikuwa tayari kukusubiri miaka yote hiyo Brina wangu.” Jack akaanza taratibu, mbele ya Sabrina aliyekuwa akitokwa na machozi na wageni wote. “Unanikamilisha katika kila eneo la maisha yangu. Unanipenda kwa dhati. Unanijali na kunitakia mema wakati wote. Unafanya mengiii kwa ajili yangu Brina. Furaha yako ni kuniona na mimi ninafuraha, nataka mimi ndio niwe mume wako mpaka kifo.” Watu wakashangilia sana. “Nataka mimi ndio nimiliki upendo huo, mwingine asije kukuwahi. Nataka uwe mke wangu Brina. Utakubali nikuoe?” Sabrina alilia mpaka akainama mbele ya Jack. Jack akacheka.

Brina, will you marry me?” Ikabidi kijana huyo wa Msindai, aweke msisitizo. Makubwa na mazito ambayo Sabrina alijua kwa hadhi yake yasingeweza kumtokea ila watu wengine, akiamini kwa imani tu kuwa siku moja yatakuja kuwa na kwake pia, kama wale warembo mashuhuri wa mjini. Akimuomba Mungu siku moja yatokee na yeye kama alivyomwambia Tino mwanzoni kabisa, kuwa yapo maombi anamuomba Mungu. Akamwambia Tino, hata yeye angemwambia, angeona amechanganyikiwa, yaani mtu kama yeye Sabrina hayawezi kumtokea. Lakini siku hiyo Mungu asiye na upendeleo amejibu. Sabrina anayashuhudia majibu ya maombi yake kwa macho yake mwenyewe! Kilikuwa kipindi kilichomuogopesha hata Sabrina mwenyewe mbele za Mungu.

“Sabrina?” Jack akamwita kwa upendo. Akasema, “Yes Jack.” Watu walishangilia sana. Jack akamvalisha pete, na kusimama kumkumbatia bila kumbusu. Walishangilia watu. Wakapiga vigelegele na kucheza. Jack alimkumbatia vizuri sana, kwa muda mfupi tu, akamwachia. “Baba aliniambia mpaka tulipe mahari ndio utakuwa wangu. Nitakuja kudai busu langu, Mzee Msindai akishanilipia mahari.” Jack akafanya waliokaribu wacheke na kushangilia. “She said ‘Yes’, mama!” Jackson mtoto wa mama akamwambia mama yake kwanza kwa sauti. “She said Yes.” Jack akaongeza sauti na kufanya watu wazidi kushangilia. Wakacheza kwa shangwe, hata mzee Msindai alicheza na wanae. Kisha akaomba kuzungumza.

“Sasa kwa kuwa tushamuona mke wetu. Sasa tunaomba tumalizane kabisa, tumiliki kihalali. Tumekuja tukiwa tumejiandaa. Si ndiyo Junior?” Baba yake akamuuliza kijana wake mkubwa, Junior akasimama. Waziri huyo, kijana mdogo kabisa. “Ndiyo baba. Sisi tupo tayari.” Akajibu nakufanya watu wazidi kushangilia. “Sijui utaratibu wenu ulivyo, lakini tunaomba faragha wakati wakulipana ili kama kunakushindwana, tumalizane kimya kimya kwa amani.” “Hatuwezi kushindwana!” Wakajibu wakishangilia upande wa kina Sabrina.

Sabrina akarudishwa ndani, ndipo sasa wahusika wa kulipa hiyo mahari na wazazi wa Sabrina na wazee waliowachagua wao, wakaingia ndani pamoja na Mzee Msindai mwenyewe, wazee wenzake waliomsindikiza, Junior na baadhi ya marafiki zake pamoja na Jack akiwa na kina Felix rafiki zake na yeye. Ibra rafiki kipenzi wa Jack hakuwepo. Mama msindai na mabinti zake pia wakafuata nyuma wakiwa wamebeba masanduku ya maana pamoja na wanawake waliokuja nao. Wakazi wa Chalinze wakiwashangaa jinsi walivyo wa mama wa maana. Ilijaa neema tupu kwenye hilo eneo. Wakakaribishwa sebuleni ili walipe mahari.

Mzee Msindai akamuachia Junior. “Kwanza tushukuru kwa kutukaribisha nyumbani kwenu tuje kuoa, tena kwa muda mfupi sana.” Sabrina akiwa chumbani akawa akisikiliza. Wamama wakapiga vigelegele. “Kama hakuna aliyetuhujumu kwa kufuta chochote kwenye orodha ya mahari mliyotupa, mama alihakikisha imekamilika.” Wamama wakapiga tena vigelegele. Junior akaanza kusoma kimoja baada ya kingine wakivitoa nakumkabidhi baba na mama yake Sabrina. Wakaja swala la ng’ombe. Mzee Msindai mwenyewe akatoa hundi. Akasema ni kwa sababu za kiusalama. Watu wakazidi kushangilia huku zikipigwa picha nakuchukuliwa video. Ukafanywa huo utaratibu mpaka wakamaliza. Wakwe wakaridhika. Ndipo wakasema sasa, wanaweza wakaletewa hata maji wafurahie pamoja, kuunganisha undugu. Wakalifanya hilo ndipo nyimbo zikaanza sasa wakitoka nje.

Walimuacha Jack ndani ili atoke na Sabrina sasa, wakae sehemu maalumu iliyoandaliwa kwa ajili yao. Walipotoka wote, ndipo MC akatangaza sasa, wote wasimame wakati Jackson anatoka na mkewe.  Akasema kimilia Sabrina alishakuwa mke wa Jackson rasmi, ila kwa kuwa ni wakristo, wanasubiri kuwekewa mkono kanisani, ramsi. Wakasimama, wimbo ukaanza kupigwa ndipo Jackson akatoka na Sabrina. Wao wawili tu. Walipendeza sana. Sabrina alitoka akiwa amevaa gauni lilelile zuri sana la rangi ya njano iliyotulia. Lilimkaa vizuri mno wala usingejua ni mjamzito. Na rangi yake ya mwili, akazidi kupendeza. Jackson  alivaa shati la njano ndani, nje suti iliyokuwa imemkaa vizuri sana ya rangi ya bluu kama kaka yake, na baba yake pia. Watu wakashangilia wakati wakitoka, wakacheza na kupiga vigelegele.

“Hapa sikuachi mama. Nikiondoka leo, tunaondoka wote. Sirudi Singida bila wewe. Usiniletee mchezo mimi!” Sabrina alicheka mpaka akainama mbele ya watu waliokuwa wakiwashangilia. “Mimi nilifikiri mpaka ndoa!” “Subutu! Unataka niahamie hapa nini? Tunaondoka Sabrina. Acha mambo ya kwenu yakusema watakutunza mpaka ndoa. Nani atanipikia mimi?” Sabrina akazidi kucheka watu wakiendelea kushangilia na kucheza. “Hivi unanielewa Brina?” “Bwana tutaondoka! Acha kulalamika.” “Wewe mtu gani umeondoka nyumbani tokea alhamisi!” Sabrina akazidi kucheka. “Emma amekula chakula chote! Inafika ijumaa nataka kula ndio niondoke, eti hamna chakula!” “Haiwezekani Jack! Chakula chote kile?” “Wewe unamchezea Emma? Mimi naomba turudi tu nyumbani haya mambo ya mila tutayafuata tukiwa kwetu.” “Naona maharusi wenyewe wamefurahi sana.” Wakashitushwa na MC alipoongea hivyo. Jack akapunga mkono na tabasamu lakuzuga.

Kukaliwa na kunywewa. Marafiki wa Jack wote waliofika hapo wakahamisha viti pale juu, wakaendeleza stori wakicheka kwa sauti tu. Kwa kuwa walimfahamu Sabrina tokea chuo, utani ukawa mwingi. Sabrina akapata nafasi ya kuwasalimia kwa karibu wazazi na ndugu wa Jack. Na yeye Sabrina akatambulisha wazazi wake na kaka yao na Sabina. Akawaambia wadogo zake wapo shuleni. Ndipo na wageni waliokuja wakajitambulisha sasa na kuacha wenyeji mdomo wazi. Watu wazito watupu ndio na nyadhifa mbalimbali ndio waliokuwepo hapo. Wake kwa waume. 

Shuguli iliisha. Mzee Msindai akatoa neno la shukurani. Kwa walio sindikiza pale na wenyeji. “Mmetulisha na kutunywesha, tunashukuru sana.” Watu wakashangilia. “Sasa huyu Jackson amesema hapa haondoki bila Sabrina.” Watu wakacheka na kushangilia. “Na huyu Jackson ni mziwanda wetu. Mama yake anampa kile anachokitaka.” Ndugu wakacheka sana na kushangilia, mama Msindai akacheka na kutingisha kichwa. “Sasa mkimnyima Sabrina leo, Jackson atabaki hapa mpaka mumpe mke wake. Na Jackson akibaki hapa, mama yake lazima atabaki hapa kuhakikisha mnamlisha huyo mtoto wake.” Watu wakazidi kucheka. “Na mke wangu akibaki hapa, inamaana kitanda changu kimehamia hapa, na mimi itabidi nibaki hapahapa.” Watu wakazidi kucheka. “Sasa sidhani kama mnataka ugeni mkubwa hivyo, tena wa muda mrefu.” Watu wakapiga makofi. “Kama kuna malipo mengine yakututoza, mtutoze, sisi tuondoke na Sabrina, usiku wa leo kila mtu akalale kwake.” Mzee Msindai alionekana mcheshi sana. Wakakabidhiwa Sabrina rasmi, wakaagana, wageni wakaanza kupanda kwenye magari.

 Sabrina akaomba kuzungumza na wazazi wake ndani, pamoja na Sabina na kaka yake. Akawashukuru sana sana. “Hakuna jinsi mnaweza kuelewa shukurani niliyonayo moyoni jamani. Asante kwa maandalizi mazuri sana. Nyumba ilikuwa safi, pakapambwa vizuri kwa hadhi ya juu. Vyakula vilikuwa vizuri. Jamani nashukuru sana. Na Mungu wangu awabariki. Jack ananisubiri nje, lakini nitakapopata tarehe ya harusi, nitawajulisha. Kama mlivyosikia, itafanyika Dar, ambako ndugu wengi na marafiki wa familia ya Msindai wapo.”

“Huna hata fununu ya tarehe?” Kaka yake akamuuliza. “Bado hawajapanga tarehe rasmi, kwa kuwa Jack ameniambia mpaka kesho wazazi wakazungumze na mchungaji wao ambaye kama ni rafiki wa familia, waombe atufungishe hiyo ndoa yeye, na pale kanisani kwao, kwa haraka. Ikipatikana nafasi na huyo mchungaji, ndio watatuambia. Kingine, ukumbi wanaotaka hao kina Msindai kwa tarehe hiyo ulishakodiwa, upo wazi kwa tarehe za mbeleni sana. Jack hataki kusogeza mbele kwa tarehe hizo, na ndugu wanataka huo ukumbi. Kwa hiyo kuna mambo wanamalizia kuweka sawa. Na mimi nitaenda kuzungumza na Jack vizuri, nitawajulisha. Lakini nawashukuru sana.” Sabrina mpaka akapiga magoti. Akawashika mkono wazazi wake akitambaa kuwafikia. “Nashukuru sana kwa kujitoa kwenu kwangu.” Hilo likawagusa wote. Ni kweli Sabrina alionyesha hakutegemea huo wema kutoka kwao. Wakumtakia kila la kheri, wakamsindikiza kwenye gari ambalo alikuwa Jack na kina Felix.

 Wakamuaga Sabrina kwa nyimbo zilizomfanya mpaka Sabrina alie humo ndani ya gari. Wakazunguka hilo gari wakiimba nyimbo za kumuaga Sabrina. Wakaimba kwa kucheza kwa muda, Jack akamvuta Sabrina kifuani, akawa amemkumbatia kwenye hicho kiti cha nyuma, wakisikiliza wanavyoimbiwa. Mwishoe ndugu zake Sabrina wakamaliza, wakaondoka wenyewe. Ndipo safari ya kurudi Dar ikaanza Jack akiwa amemkumbatia Sabrina, asiamini kama ameagwa nyumbani kwa heshima kiasi hicho. Kwa mara ya kwanza, Sabrina akajisikia kupendwa na kuthaminiwa kwa hali ya juu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Jack na Sabrina walishushwa hotelini. Jack akafurahi sana. “Lakini hakuna kuvuka mipaka Jack!” Jack akacheka sana. “Kwani mimi nimesemaje? Si nimesema mazingira leo yametubananisha! Kwani umesikia nini?” “Wewe endelea kushangilia kama sijakupandisha taksii na kukurudisha kwa mama yako.” “Utamnusa nani usiku kucha?” Sabrina alicheka sana. “Halafu nilisahau kubeba ile tisheti yako.” “Niliiona juu ya kitanda chako, nikajua haraka zimekuponza.” Wakazungumza usiku huo, Sabrina akimshukuru Jack kumletea heshima nyumbani kwao. Jack akawa anacheka tu.

Wakapanda kitandani, Sabrina akajivuta mpaka kifuani. “Asante sana Jack.” “Na mimi nakushukuru sana Brina. Hakika unanijali na kuniwazia yaliyo mema.” “Nakupenda Jack.” “Na mimi nakupenda Brina wangu. Nilikwambia wakati Mungu alipokuwa akikuumba alikuwa akinifikiria mimi?” Machozi yakamtoka Sabrina. “Ndio maana hukuwa ukifiti au kuenea huko ulikokuwa ukienda kwa wanaume wengine. Kwa kuwa hapa.” Jack akajionyeshea ubavu wake. “Hapa ndipo ulipotolewa na Mungu, ndipo akakuumba.” Sabrina akajisikia vizuri sana. Akamsogelea mdomoni kuanza kupata busu. Akaanza kusikia mikono ya Jack kwenye chupi. “Unakaribia kuhamia kwenye kochi Jack.” Jack akacheka sana. “Kidogo tu Brina!” “Hapana Jack. Kumbuka jinsi Mungu alivyosimama na sisi mpaka kufika hapa. Angalau na sisi tumuonyeshe tunamthamini.” “Duuh! Mimi naona tuoane hata kesho bwana!” Jack akatoka kitandani akilalamika. Akaenda chooni. Sabrina akaona amuache atulie.

Akatoka mnyonge. “Njoo nikubembeleze ulale Jack wangu.” “Wewe ukinigusa unanifanya nikutake zaidi. Halafu nikikutaka unamwita Mungu mpaka napata hukumu!” Sabrina alicheka mpaka akatokwa na machozi. “Jack!” “Mimi naona tuone tu haya mambo yaishe.” Akachukua shuka akahamia kwenye kochi. Sabrina afikiria, akamuhurumia. “Njoo ulale hapa, sitakupapasa. Usilale kwenye kochi.” Kama mtoto mdogo, akarudi akilalamika. Sabrina akampa mgongo akiwa ameshika shati alilokuwa amevaa Jack siku hiyo, akawa ananusa. Jack akamuwekea mkono juu yake. “Kesho baada ya kifungua kinywa kwa mama, tunarudi Singida.” “Uliniambia. Ila naogopa?” “Ndio utapata nafasi yakuwafahamu ndugu zangu kwa karibu.” Sabrina akanyamaza.  

“Acha woga wewe. Utakuwa na mimi. Kwanza mwanangu anaendeleaje?” Sabrina akageuka na kumuachia tumbo. “Vizuri. Nahisi nyumbani hawajagundua.” “Kwani hujawaambia!?” Jack akashangaa. “Namwambia nani Jack? Wale watu yaani jana na leo ndio nimeweza kuona ukaribu wao kwangu. Halafu sikutaka kumfanya da Sabina ajue, halafu apige mahesabu. Aanze maswali yake, halafu ugundue mimba ni ya nani. Sikutaka kufanya hilo kosa.” Jack kimya.

“Nataka Tino asiwahi kuja kujua kama ninaye mtoto wake. Kama vile alivyokusudia tumuue huyu mtoto, ndipo alipoua mahusiani na huyu mtoto. Najua kwake ndio itakuwa nafuu, lakini wakati anakuwa huyu mtoto, kabla hajajua kwa kuambiwa na watu, baba atakayekuwa akimfahamu ni wewe tu. Hata iweje, itabaki hivyo.” Jack akajisikia vizuri sana. Akaendelea kumpapasa tumboni. Akakumbuka alivyowaambia familia yake kuwa huyo mtoto atakuwa Msindai. “Akiwa wa kike tutamuita nani?” Jack akauliza. Sabrina akacheka taratibu. Jack akambusu tumboni. “Eti nilifikiria tumwite Brina.” Jack akashituka sana. “Acha masihana Brina! Brina ndio jina langu kwako! Mwenyewe nikikuita hivyo najisikia vizuri zaidi ya kukuita mpenzi, sijui honey au sweetie! Brina jina lako wewe. Acha kabisa.” Sabrina akacheka sana. “Basi mwenzio ndio nilifikiria kumwita hivyo.” “Hapana. Tufikirie jina jingine.” Wawili hao wakaanza kuzungumza kama wazazi kweli. Gafla hali ya kumilikiana kama wanandoa kweli na wazazi ikawaingia. Wakalala kwa furaha, wakimshukuru Mungu kuwavusha hatua ya kwanza.

Sabrina ukweni.

S

abrina na Jack walifika nyumbani kwa wazazi wao mida hiyo ya saa tatu na nusu asubuhi, wakakuta wote walishafika. Jena akaanza kwa vigelegele. “Acha bwana Jena! Sasa vigelegele vya nini?” Jack akakataa. “Huyu bwana harusi vipi?” Wakaanza kucheka. “Sasa hapa unaona kuna harusi kama sio kutaka kumtia wasiwasi Brina wangu?”  Jena akaendelea kupiga vigelegele. “Unakera wewe!” Jack akapitiliza chumbani. “Huyu mbona anazunguka na suruali na singlendi tu? We Jack?” Mama yake akamwita alikuwa jikoni alimuona akipita. “Navaa mama!” Jack akajibu akiwa chumbani. “Kwa nini unazunguka uchi bwana!?” “Sikubeba nguo jana, nilikwenda hotelini nikiwa na suti tu.” Wote wakacheka mama yake akaguna. “Sasa si ungevaa koti, kuliko kubeba tu koti mkononi!?” “Mama ameanza. Mwanao anaoa huyo. Sio mtoto.” “Sasa ndio aoe huku anakohoa! Anazunguka jiji zima kifua wazi bwana!” Akalalamika mama Msindai. Sabrina akajua kazi atakuwa nayo.

“Naomba mumleteeni chai ya moto. Ashaingiwa na baridi.” Wote wakashangaa. “Hivi ujue mama mpaka wajukuu pia hawajala, tulikuwa tukiwasubiria hawa maharusi!” Juniour akaongea nakufanya mpaka baba yake acheke. “Sasa nyinyi si mmevalisha watoto wenu nguo! Jack atakuwa ameingiwa baridi.” Kila mtu akaanza kucheka. Sabrina hakujua kama huyo mama yuko kwa undani hivyo kwa Jack. “Huko nje ni jato mama Msindai. Acha wasiwasi.” Jack akatoka akiwa amevaa suruli ya jinsi na tisheti.

“Sasa ngoja nikutambulishe rasmi, Sabrina.” Jack akaaanza. Akatambulisha mmoja baada ya mwingine mpaka mwisho. Wakaonekana kumchangamkia Sabrina vizuri tu. Jacinta, Joy na Jena wakamuuliza maswali machache juu ya nini anafikiria kwenye harusi yake. “Ile njano uliyovaa jana ilikupendeza sana. Unaweza kufanya rangi ya harusi ikawa hiyohiyo, au unasemaje?” Jena akamuuliza Sabrina. “Itapendeza kweli?” Sabrina akauliza akiwa ametulia tu. “Ipo njano fulani hivi. Ikiwekwa vizuri, itafanya ukumbi upendeze. Au Jack na wewe unasemaje?” “Mimi ninachotaka harusi iwe ya haraka, na Sabrina awepo. Rangi yeyote ile mimi kwangi sawa.” Wakacheka na kujaribu kuweka mambo sawa.

Wote walikuwa wamevaa nguo za kanisani tayari kwenda kanisani muda ukifika. Joy akapata nafasi ya kumuombea mtoto wake. “Naomba kiziwanda wa dady na yeye asimamie.” Sabrina akashangaa wote wanacheka mpaka Junior kaka mkubwa. “Mimi nitapendezesha harusi, Antie.” Wakazidi kucheka. “Ataharibu huyo. Kwanza bado analala mchana. Asipolala, anaanza kulia hovyo hata shule wanamjua, ikifika mchana anaanza kunyonya vidole.” Kaka yake akaingilia, wakaanza kubishana. “Sasa wewe utalia, Cleiton.” Joy akamtisha mtoto wake wa kiume. “Kwani uongo mami? Atasimamia harusi huku ananyonya vidole? Claire ataharibu harusi huyo.” Claire akaanza kulia.

“Bwana Cleiton utalia wewe mtoto wewe!” Mama yao akamtisha tena. “Sawa mami. Lakini mtakuja kunikumbuka mimi. Si  unamuona anavyolia hivyo, basi anti Sabrina, uliaji wake ni hivyohivyo. Kitu kidogo tu mwenzio analia. Sasa usishangae katikati ya harusi anaanza kukulilia.”  Watu wakazidi kucheka, Joy akaanza kumkimbiza mwanae wa pili huyo Cleiton. “Nikikukamata wewe!” Joy akatisha, Cleiton akakimbilia chumbani. “Mwanangu halii hovyo, si eti mama yangu mzazi?” “Mimi silii hovyo, dady. Clei ndio mchokozi.” “Basi nyamaza ili anti akuone hulii hovyo. Njoo mama.” Baba yake akamuita. Akaenda na kuanza kunyonya kidole chake gumba. Kila mtu akaanza kucheka. “Sasa haya si ndio aliyokuwa akiyasema mwanangu Clei, mkaishia kutaka kumpiga?” Jacinta akaongea kwa sauti ya chini wote wakamwangalia Claire nakuzidi kucheka. Kidole mdomoni, analia huku baba yake amempakata akimbembeleza. “Hapo ndio katikati ya harusi, hali imemjia hivyo.” Jena akaongeza nakufanya wazidi kucheka. “Mnamuharibia mwanangu soko jamani! Hatalia. Si ndio mama?” “Mimi silii mami!” Akajibu Claire huku akilia, wakazidi kucheka.

“Hata hivyo bado hatuna wasimamizi, kwa hiyo naona tutamuhitaji tu Claire.” Sabrina akaongea huku akicheka. “Kwanza njoo nikuone msimamizi wangu.” Jack akamuita. Claire akatoka kwa baba akahamia kwa anko wake na kidole mdomoni. “Una nywele nzuri Claire!” Jack akamsifia. “Asante.” “Toa sasa kidole mdomoni ili Clei asizidi kukucheka.” “Clei mchokozi anko!” Akamsemelea kwa Jack. “Sasa mama atamchapa. Ushajua utavaa gauni gani siku ya harusi?” Wakamuona anacheka. “Kwanza nywele zangu nzuri, nitazibana.” Wote wakazidi kucheka. Huyo mtoto ni mrembo na alijipenda sana. Alifanana na mama yake wala si baba. Akajielezea atakavyopendeza wote wakimsikiliza na kucheka.

Wakapata wakati mzuri. Wakala pamoja. Sabrina aliona ni familia ya kawaida tu sio kama ukubwa wa jina lao. Walikuwa waungwana. Ila macho ya mama yao ukweli yalikuwa kwa Jack muda wote. Mara amshike. Mara ampanguse hapa na pale, ilimradi tu. Wengine hawakuonekana kushangaa, hata Jack mwenyewe alitulia tu akiendelea na mambo mengine huku mama yake akimfanyia hili na lile, ila yeye Sabrina ndio akawa anashangaa sana vile Jack anavyofanywa kama mtoto mdogo! Muda wa kwenda ibadani ulipofika, wao walipelekwa uwanja wa ndege na dereva, wengine wakaelekea kanisani.

Sabrina& Jack.

J

ack na Sabrina walirudi Singida, kila mtu akajua wamechumbiana. Walionyesha picha nyingi na kuwaambia watu karibuni sana watafunga ndoa. Ni kweli heshima iliongezeka hata wao waliona. Vile walivyoanza kumchukulia Sabrina, kila mtu kwa heshima kama mke wa Msindai kweli. Hata vijana walimsikiliza kama mke wa Msindai. Ikamuongezea heshima na nguvu ya amri kuongoza. Na kwa Jack vile vile ofisini. Bado pongezi ziliendelea kila leo wakimtania kwa hili na lile. Mambo ya maandalizi yote yakaendelea. Simu za hapa na pale wakiulizwa hili na lile juu ya harusi yao navyo vikaendelea.

Kanisani walishaanza kutangaza ndoa yao. Na wao wawili wakaanza kwenda kanisani pamoja. Siku moja walipotoka kanisani Sabrina akiwa amekaa tu kwenye kochi, akaanza kusikia mtoto anacheka. Alishituka mpaka akasimama. “Nini!?” Jack akamuuliza. “Nimesikia mtoto akicheka.” Akaingiwa hofu. “Njoo bwana! Ndio kitu kizuri.” Jack akasimama na kumvuta arudi kukaa. Akaweka mkono hapo kusubiria kucheza. Akacheza tena. Yeye Jack akaanza kupiga kelele. “Acha bwana Jack!” Emma akatoka kwa haraka. “Mtoto ameanza kucheza na mimi nikiwepo.” Jack akafurahia kuliko Sabrina mwenyewe. Sabrina akashangaa anapiga simu. “Ni nani unampigia?” “Mama! Mama!” Sabrina hakuamini alipokuwa akimwita mama yake. “Mwanangu amecheza, nimemsikia.” Mpaka Sabrina hakuamini. Akamsikia mama yake akicheka. “Hongera. Ameshaanza kliniki?”  Mama yake akauliza. “Bado. Lakini nimepatwa hamu yakumuona. Anacheza bwana!” Akacheza tena, Jack akaona. Akaweka simu pembeni akarudi tumboni.

“Naona leo mwanangu ameamua.” Jack akarudi tumboni akicheka kwa furaha mpaka Emma alikuwa akimshangaa. Wakati anakua Jack, alikuwa akimuomba sana mama yake atafutiwe mdogo wake. Kwa hiyo akakua akipenda sana watoto tangia mdogo. Ilikuwa akipelekwa nyumba zenye watoto, kuaga ilikuwa shida. Akammliki huyo mtoto, akajawa furaha kama wake. Kila alipokuwa akicheza, Jack alitaka amshike. Naye Sabrina anaegesha tumbo, Jack anashangilia hapo.

Wakati familia ya Msindai wakihangaika na maandalizi ya harusi ya baada ya mwezi na siku, Sabrina na Jack wakaendelea kuimarisha kambi ya chama. Kwa muda mfupi tu, wawili hao wakaweza kuwa na kitu kinachoeleweka. Miradi miwili wakaifufua na timu ikawa ikifanyiwa mazoezi ya uhakika maana walikuwa na kocha wakueleweka. Minong’ona ikaanza. Vijana wa chama wakaanza kujisifia mtaani. Jina la Jack na Sabrina kuwa wanafanya mambo makubwa likaanza. Sabrina alifanya bila kuchoka, huku akimtia moyo Jack.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ujauzito ulipofika mwezi wa tano na siku chache, na Jack kuona vurugu huko tumboni zinazidi, akamlazimisha Sabrina waanze kliniki. Sabrina ndiye aliyekuwa akiona uzito wa kuanza. Kwa kuwa hakuwa na mabadiliko makubwa sana zaidi ya kuanza kuchoka, kulala sana, hakuona mabadiliko makubwa zaidi, kwa hiyo akawa anamwambia Jack nitaanza kesho, au jumatatu. Jumatatu ikifika jumatano. Jumatano ikifika basi atamwambia asubiri tena jumatatu. Akaendelea kusogeza mpaka Jack akachoka akaona aingilie kati, kwani mama Msindai naye akaanza kuweka pressure akitaka Sabrina aanze kliniki. “Tumechelewa sana. Hakuna mama anaanza kliniki akiwa na mimba kubwa hivyo Brina. Si sawa kwako wala mtoto.” Hapo Sabrina akaamua kwenda. Siku hiyo Jack akaongozana naye. Hakutaka kuja kuambiwa hakwenda. Alikwenda kazini kuripoti, ndipo akarudi kumchukua.

 Tumbo lilishaanza kuonyesha kabisa mpaka Sabrina akawa analalamika lipo kubwa zaidi ya wakati wake. Alishabadilisha mavazi, akawa akivaa nguo za ujauzito. Na kwa kuwa alikuwa mwembamba, huulizi. Unaona tu. Kama kawaida ya utaratibu wa wakinamama wengine. Kupimwa mkojo, pressure na uzito. Akatakiwa kwenda kupimwa na damu kabla hajaingia kwa daktari. Sabrina akafanya yote hayo wakiongozana na Jack. “Nachoka haraka siku hizi! Kama ambaye nimelemewa wakati bado kabisa!” “Mimba ya miezi mitano Brina. Usiseme bado.” Alipimwa kila kitu akabaki akisubiria kwenda kwa daktari.

Zamu yao ilipofika, kwa kuwa ilikuwa mara ya kwanza huyo daktari akasalimiana nao na kuuliza maswali machache. Akawapa majibu. Damu tu ndiyo aliambiwa nilazima aanze kutumia vidonge vyakuongeza damu na vya virutubisho kwao wote wawili. Mama na mtoto. Ndipo akaambiwa apande kitandani asikilize mapigo ya mtoto. Wakamuona daktari anarudia tena na tena kumpima na kusikiliza mapigo ya mtoto mpaka akawatia wasiwasi Jack na Sabrina. “Kwema?” Ikabidi Jack aulize. “Nyinyi mnajua kama wapo wawili hawa?” Sabrina alishituka mpaka akakaa, Jack akasimama. “Mapacha!?” Akauliza Sabrina kwa mshituko kama anayetaka kuanza kulia. “Ndiyo. Kwani hamkuwa mkijua? Rudi kulala nikuonyeshe.” Sabrina akabaki amekaa akiwa ameduaa. Jack akamsogelea. “Naomba niangalie mimi Brina.” Sabrina akaanza kutokwa na machozi. “Niangalie mimi.” Sabrina akainama akitetemeka. “Maadamu kila kitu kipo sawa, acha sisi tuondoke, tutarudi wakati mwingine. Nashukuru sana.” Jack akaaga huku akimsaidia kumvalisha Sabrina, daktari akishangaa.

Akamsaidia kushuka pale kwenye kitanda, Jack akaaga baada yakukusanya kila kitu, akamshika mkono na kutoka naye akiwa yeye ndio amebeba kila kitu. Akamsaidia kupanda kwenye gari, wakaondoka. Alikwenda kununua dawa alizoandikiwa Sabrina. Akapitia sokoni kununua matunda. Akaongeza juisi kwa ajili ya Sabrina kumsaidia kuongeza damu. Wakarudi nyumbani. Sabrina akaongoza njia moja kwa moja chumbani kwake. Jack akamfuata.

“Naomba niambie hofu yako ilipo Brina. Bila kunificha.” Jack akakaa pembeni yake pale alipoinama akilia kitandani. “Naona mimi sitaweza Jack?” “Kuwa muwazi zaidi. Kwamba hutaweza kuwabeba sasa hivi, au kujifungua, au unamaanisha kunyonyesha?” Sabrina akazidi kulia. “Naomba tuzungumze bila kupaniki mama. Maana mimi nauona uwezo mkubwa sana ndani yako. Umekuja kufufua ari mpya ndani yangu. Umefufua miradi iliyokuwa imekufa ya chama. Umemudu kuwa katikati ya wale wanawake wenye midomo michungu kama shubiri!” Sabrina akaanza kucheka huku akilia.

“Kweli. Imani mwenyewe alishawashindwa, ndio maana umeona chama kilikufa sababu ya maneno yao. Wewe ukaweza. Sasa nataka kujua kwa ukweli kabisa, ugumu huu uliokushitua ni upi? Na kama nikuzaa, nilisikia siku hizi wanachoma sindano za kukata maumivu. Dar lakini. Sijui hapa. Unajifungua vizuri bila shida wala maumivu. Sasa naomba nipe hofu yako nyingine.” “Sikutaka kuwa na watoto wa Tino wawili?” Sabrina akaongea akilia sana.

“Watoto wa Tino wapi tena mbona unanichanganya!?” Jack akamfanya Sabrina ashituke. “Tino aliua watoto wake. Alikuacha akiwa ameridhia ameua watoto wake. Mimi nipo hapa na wewe, nikijua tumekubaliana kuwa watoto hao ni kina Msindai. Kila mtu namwambia nasubiria mwanangu, kumbe mwenzangu moyoni umenikataa!” “Sijakukataa Jack.” Ikabidi Sabrina akae kwa haraka. “Kumbe ni nini? Si umetoka kusema ulitaka kuwa na mtoto mmoja tu na Tino!? Au mimi sikuwa nimesikia vizuri!?” Jack aliongea kwa mshangao na kuumia sana. Ikabidi machozi ya Sabrina yakauke.

 “Naomba usiumie Jack. Mimi nilikuwa nakuhurumia wewe. Niliona ni kama nakupa mzigo mzito sana. Utalemewa kwa watoto wawili!” “Ambao ni wa Tino au wangu sasa!? Maana naona gafla nipo njia panda, sijui nafasi yangu tena! Nilijua huko tulishapita muda mrefu sana. Nasubiria watoto kumbe mwenzangu moyoni unajua si wangu!” Jack akasimama. “Ulinidanganya Brina.” Jack akalalamika. “Sijakudanganya Jack, naomba utulie.” “Hapana. Leo umezungumza moyo wako.” Jack akaonekana ameumia kupita kiasi, Sabrina hakuelewa kama neno dogo vile linaweza kuchukua maana ya tofauti.

“Unakumbuka usiku ule baada ya kukulipia mahari tukiwa mimi na wewe hotelini ulisema nini?” “Naomba Jack utulie mpenzi.” “Hapana Brina. Naomba zungumza ukweli wako. Usije kuniumiza baadaye. Ulisema nini juu ya huyo mtoto au hao watoto?” Sabrina akajua ameshaharibu. “Niambie ukweli Brina.” “Nilisema baba watakayemfahamu ni wewe, mengine watasikia kwa wengine lakini si kwangu.” Jack akapandisha nyusi zote juu kama anayemsuta. “Sasa, sasahivi Tino anaingiaje hapa?” Jack akauliza. Sabrina kimya. “Brina? Tino anaingiaje hapa?” Sabrina akabaki akifikiria.

“Sikujua kama ndivyo unavyofikiria moyoni mwako! Na ndio maana japokuwa tumelipa mahari na kila kitu kilichohitajika kwa wazazi wako na baba yangu alitangaza pale hadharani mpaka Mungu akasikia kuwa Jack haondoki hapa bila mke wake! Lakini upo radhi mimi nikalale kule peke yangu, wewe ulale hapa, ukimtumia Mungu kama sababu kumbe ni kwa sababu umenikataa moyoni! Ndio maana hutaki hata nikuguse!” Jack akaendelea kulalamika. Sabrina akabaki amekufa ganzi hajui aseme nini.

“Unajua nini Sabrina, mimi nimefanya kwa sehemu yangu bila unafiki wala kificho moyoni. Nakuachia wewe uamue. Na naomba jibu la haraka tafadhali, ili nisikupotezee muda wako na muda wa wazazi wangu wanao hangaika sasa hivi kuandaa harusi yetu. Pata muda wa kujifikiria, kisha jioni nikitoka kazini, utanijibu. Sitakulaumu. Maana najua, unaweza kumpeleka punda kisimani, lakini huwezi kumlazimisha kunywa maji. Sina uwezo wa kukufanya unipende na kunihitaji kwenye maisha yako. Nashukuru Mungu nimefanya kwa nafasi yangu. Na Mungu anajua jinsi ninavyokupenda Brina. Sijawahi kumpeleka msichana nyumbani kumtambulisha rasmi ila wewe. Nimefuata hatua zote mpaka nikakabidhiwa wewe rasmi kama mke, lakini bado tu!” Jack akatoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakati kina Msindai wakiandaa harusi ya kijana wao, huku nako kwa bibi harusi na bwana harusi maisha ya ndoa yanaendelea kama kawaida. Ugomvi wao wa kwanza huo. Maneno yakitamkwa huwa hayarudi. Kipi kitaendelea kwao kwenye vita ya ndani baada ya Jack kushinda ya nje, ambayo ilikuwa ya nyumbani kwao  mpaka kufanikisha kulipa mahari? Harusi ipo? Usikose muendelezo…

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment