![]() |
“Subiri
kwanza Ritha. Acha maneno mengi. Wewe si mama yake Net? Inamaana unazo haki
zote za kumkomboa mwanao kwa njia takatifu kama wewe ulivyo mtakatifu. Mbingu
inajua unayo haki, hata kuzimu kule unakosema mimi ninaenda, wanajua kuwa wewe
kama mama yake Net, unayo haki na Net. Sasa kwa nini unahangaika na mimi ambaye
hata sijaunganishwa na Net kwenye agano lolote!?” Tunda akamuuliza taratibu tu
bila jazba kama yeye alivyokuwa akiongea kwa jazba.
“Usifikiri
ndio umeshinda Tunda. Namuombea mwanangu. Ila ujue maombi ni kotekote. Ni mimi,
na Net mwenyewe aamini.” Tunda akamtizama kwa kumsuta. “Na usifikiri
nimeshindwa. Nipo kwenye maombi yakumfungua akili zake mpaka afunguke. Net ni
kama amechanganyikiwa kwa kuwa anataka kuwa mtumishi wa Mungu kama babu yake,
ila hajui ni jinsi gani atumike. Kwa kuwa wewe ulikuwa malaya, na bibi yake
anapambana na haki za wanawake na kutoa wanawake wenye hali kama yako na
kuwawezesha kimaisha ili waweze kujitegemea, ndio anaona wewe utafaa.” Akaanza
kuropoka, Tunda akimtizama kwa mshangao.
“Kwanza
atakutumia wewe kama kielelezo cha kufikia roho za watu waliopotea na pili
anaona anamfurahisha bibi yake kwa kumuunga mkono kwa kile anachokifanya kwako
wala si mapenzi. Ndio maana anadhani wewe utamfaa.” Hilo likamwingia Tunda na
kumuumiza sana. Ila akajikaza mbele ya Ritha.
“Upo
wewe kama daraja kutimiza ndoto zake, na ndio maana hata bibi yake pia yupo
hapa leo kuhakikisha Net anafikia ndoto zake na yule bibi anajipatia sifa
kimataifa. Kuwa ni mkweli kwa kile anachokipigania. Kwani ameweza kuruhusu hata
changudoa kama wewe kuolewa na mjukuu wake. Usifurahie jinsi unavyoitwa Mama
Cote leo, ukadhani kuna kitu cha maana walichokiona kwako au uchawi wako pekee
ndio umeshinda. Hamna kitu.” Tunda alibaki kimya ametoa macho. Habari zilikuwa
mpya, ngeni lakini kweli zilianza kumuumiza.
“Wewe
loga utakavyo. Lala makaburini utakavyo. Lakini jua mimi nipo. Na uelewe kabisa
nawajua wazungu kuliko wewe. Wanajua kutumia watu. Umeruhusiwa na yule bibi
kuwepo na Net kwa ajili ya kumnufaisha yeye mwenyewe yule bibi. Kimataifa na
kiuchumi. Na kwa upande wa Net, kama nilivyokwambia. Ila sasa, ujue wazi, MIMI
nipo. Sitakubali kwa nia yao yeyote ile, wewe unufaike kwa kile ninachostahili
mimi.”
“Nimehangaika
sana kufika hapa. Mchana na usiku kujenga hili jina huku Tanzania. Nani alijua
Cote huku Tanzania kama sio mimi? Hapa uliposimama, ni kwangu nimejenga kwa
jasho langu. Hata kama Net alikwambia babu yake ndiye alijenga hapa, lakini
ujue mimi ndiye niliyekuwepo hapa kuhakikisha jengo linasimama.” Na hapo napo
Ritha akajikuta anaropoka mengiii kwa hasira huku Tunda akimshangaa. Hakuwa
anaelewa chochote anachozungumza pale.
“Kwa
hiyo ujue sitakubali. Wakati wewe unahangaika na suruali za wanaume, mimi
nilijua kufunga miguu yangu, nikatumia akili, mpaka kumfikisha hapo alipo hata
huyu Net ambaye sasa hivi unafurahia mali zake hapa nchini Tanzania. Yupo hapa
nchini kwa sababu ya juhudi zangu wala sio pesa. Hawezi kuishi Tanzania bila
idhini yangu mimi ambaye ni raia wa Tanzania.” Hapo napo Tunda hakuwa hata akielewa.
“Sasa,
sitakubali hata iweje uvune usipopanda. Labda usubiri niwe nimekufa ndio
utakuja kuitwa mama Cote. Vinginevyo ujue utapambana na mimi na utajuta, malaya
mkubwa wewe.” Tunda akatabasamu. “Umemaliza?” Tunda akamuuliza mama Cote swali
lililomshangaza, tena akiwa ametulia tu. Kimya.
“Acha
kuniogopesha Ritha. Wala sitakuita Mama Cote maana umejishusha sana. Mimi huwa
sitishwi. Na wewe wala usifikiri ndio wa kwanza kunijia na vitisho. Tokea
napata akili zangu, nimeishi na watu wa aina yako. Vitisho imekuwa sehemu ya
maisha yangu. Yaani wewe hapo ulipo hivyo, hunitishi hata kidogo.” Tunda
akaendelea taratibu tu.
“Unanisikia
Ritha? Sikuogopi. Halafu na uache kujipa kazi zitakazo kuchosha bure! Ngoja
nikusaidie tu kwa kuwa umenizalia Net. Huko unakonitafuta mimi simo tena.
Nimetoka na nimeamua kupumzika. Mungu alishanitoa makaburi na kwa waganga wa
kienyeji, muda mrefu sana. Nimeacha kuvua suruali za wanaume muda mrefu sana na
wala sijivunii kwa hilo. Najua nimesamehewa, lakini bado nipo na majuto tu.
Nasikitika kuwa na wewe umekuwa muhanga na maisha niliyoishi zama...” “Acha
kunipa maneno unayomdanganya nayo Net. Mimi ni Ritha Cote. Najielewa. Na
nimekwambia hata Net anakutimia tu.” Ritha akamkata. Tunda akacheka kwa
kumuhurumia.
“Hata
kama Net ananitumia tu. Au bibi yake ananitumia. Sijali. Nataka ujue na mimi
msaada ndio nilio kuwa nikiutaka siku zote za maisha yangu. Net amepata
alichokuwa anakitaka maishani mwake, na mimi nimempata mwanaume ambaye hata
sikuwahi kumuota na heshima kubwa ambayo hata sikuwahi kufikiria nina stahili.
Wewe ni shahidi kwa kile tu kilichonitokea leo. Ulikuwepo tokea asubuhi
ukishuhudia kile kinachonitokea mpaka sasa hivi uliposhindwa kuvumilia. Umeona
heshima iliyowekwa kwa Tunda tu!” Tunda akacheka taratibu.
“Kwa
hiyo kwa upande wangu mimi, kwa ufupi, sina chakupoteza hata kidogo. Kama Net
na bibi yake wataendelea hivi, aisee ujue mimi ndio nilichokuwa nikikihangaikia
tokea zamani mpaka kulala makaburini nakushindwa kukipata kwa shetani ila kwa
huyu Mungu ninayemtumikia sasa hivi. Sasa kama na yeye unamwita shetani, hakuna
injili itakayowahi kuja kunitoa kwa huyu Mungu ninayemtumikia sasa hivi.
Nakushauri na wewe umfuate. Analipa. Na itakupunguzia kupambana na watu au
kuzunguka kwenye maofisi ya watu ukijidhalilisha bila wewe mwenyewe kujijua.”
Ritha alishtuka sana asiamini.
Tunda akataka
kufungua mlango ili aondoke lakini akageuka. “Na wala usipate shida na uwepo
wangu. Nitajitahidi tusionane kabisa mpaka utakapo kuwa tayari kuniona tena.
Naomba uniagie Net.” Tunda akaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Baada ya
muda kupita bila kumuona Tunda, Net akaanza kumtafuta. Aliingia ndani na kutoka
mara kadhaa, mwishowe akakumbuka kumuona mama yake akiingia ndani wakati Tunda
yupo ndani. Akamsogelea, “Umemuona wapi Tunda?” “Aaah! Nilisahau kukwambia.
Aliniambia nikuage yeye ameondoka.” Net akakunja uso na kujiweka sawa.
“Umemwambia nini tena, Tunda?” “Kwa nini unafikiria
maneno yangu ndio yamemuondoa hapa?” “Mama?” Net akaita kwa ukali kidogo.
“Umemwambia nini Tunda?” “Labda atakuwa hajanielewa.” “Juu ya nini?” Net
akauliza. “Acha kunihoji maswali mengi. Hapa ni nyumbani kwangu.” Ritha
akambadilikia mwanae.
“Ni nini kinaendelea mama!? Shida yako ni nini? Kwa nini
umeshindwa kumpokea Tunda kama mwanamke ninayempenda?” “Kwa kuwa umekataa kukaa
chini na kumfikiria vizuri.” “Unataka nifanye nini kukuthibitishia kuwa Tunda
amebadilika? Umempa mtego wa Gab, ameshinda. Nini unataka kutoka kwake!?
Ulitaka afanye nini!?” Net alikuwa anamshangaa mama yake nakushindwa hata
kuelewa.
“Nishakujibu kuhusu Gab. Ule sio mtihani wakumpima mtu kama
Tunda, nakusema ameshinda. Gab angekuwa mwanaume mwingine, hakika asingemkataa.
Mbali na sababu nyingine nyingi za mwanamke kama Tunda, kwanza lazima ujue bado
ana uchungu na Gabriel ndio maana alimkataa. Na yeye si binadamu bwana! Anaweza
kuumizwa. Huwezi kumpima mtu kama Tunda na Gab wakati amekukamata wewe. Nini
atanufaishwa na Gab ambacho hatapata kwako? Anajua hilo ndio maana anajifanya
mtakatifu kwako.” Yule mama akaendelea.
“Siwezi kuwa mjinga au kudanganywa na Tunda kama alivyofanya
kwa Gab na wewe sasa hivi. Eti nimekaa hapa, namwangalia tu anavyojidai kuwa
amebadilika, ameokoka, eti sasa hivi ni malaika na wewe unataka kumuoa! Hata
kidogo. Sikubali.”
“Wageni wote hapa wakiume, karibia asilimia 90, kasoro ya
aliokuja nao bibi yako tu, amelala nao. Kwa nini unataka kunidhalilisha hapa
mjini? Wasichana wote waliojaa humo makanisani, leo unakuja kumuoa yeye!? Kwa
nini Net? Naomba pata muda ufikirie. Tunda hawezi kuwa mke wako. Naomba
mwanangu punguza mwendo. Umefanya haraka sana juu ya huyu Tunda.” Net akazidi
kuumia.
“Nafikiri nimefanya sana haraka kwako mama. Hata hii shuguli
sikutakiwa kuifanyia hapa. Nana angeshukia nyumbani kwangu, na mambo mengine
yangeendelea kama kawaida, nyumbani kwangu. Lakini sikutaka haya mambo yaende
mbali. Sikutaka tumuingize Nana katika hili ndio maana nikamleta hapa na
kumrudisha Tunda kwako japo ulimuumiza sana.”
“Nakupa muda zaidi. Utakapokuwa tayari utanitafuta. Lakini
ukae ukijua nitamuoa Tunda, tena haraka iwezekanavyo. Unajua pakunipata pindi
utakapo kuwa tayari. Na kwa kuwa Tunda ni kero kwako, nitajitahidi kumuweka
mbali sana na wewe, ili asikukere na usimuumize.” Mama Cote alishtuka sana.
Akajua Net akihama pale ndani tena, akarudi nyumbani kwake, bibi Cote atafahamu
na kuibua maswali zaidi.
“Kwa hiyo na wewe unaondoka!?” “Humtaki Tunda, na Tunda
atakuwa mke wangu hivi karibuni, unafikiri nitafanya nini?” “Na kazi unaacha?”
“Kwa nini niache kazi!?” “Sijui. Labda unataka
kuniadhibu.” Mama Cote alitumia silaha yake kwa haraka, aliyojua kumvuta
nayo Net. Machozi. Net akamsogelea. “Nakupenda sana mama yangu. Na nilimuahidi
baba nitakuwa na wewe wakati wote. Hakuna mtu wala kitu kitaingilia katikati
yetu. Siwezi kuacha kazi. Nilikuahidi maisha yangu ya familia hayataingilia
kazi yangu, na bado itabaki hivyo.”
“Siwezi kukuadhibu kwa kutokumkubali mwanamke ninayempenda
mimi, lakini naona haitakuwa sawa kuendelea kukuletea Tunda, halafu unaiishia
kumuumiza. Sio sawa kwako wala kwake. Nilikubali kuja naye hapa leo, kwa kuwa
ulisema huna neno. Lakini sasa hivi nimejua kuwa ulikubali sababu ya Nana.
Ulijua Nana asingefurahia kuona Tunda hakaribishwi nyumbani. Lakini usiwe na
wasiwasi, Tunda hatakubugudhi tena na wala haya mambo hayatafika kwa Nana.
Usiwe na wasiwasi juu ya hilo. Usiku mwema mama.” Net akambusu mama yake, akaenda
kumsindikiza bibi yake kitandani huku wakitaniana. Waliomba naye, kisha
akondoka kwenda kumfuata Tunda.
Net kwa Tunda.
Net alimkuta Tunda, ameshaogo na kuvaa nguo zake za kulalia,
amejilaza kwenye kochi anaangalia tv. “Nilikuomba usiwe unanikimbia Tunda.”
“Nilimuomba mama yako aniagie.” “Tangia lini mimi na wewe tunawasiliana kwa
kupitia mama yangu? Ingechukua dakika ngapi kuniaga pale wakati unaondoka?”
“Sikutaka kukusumbua katikati ya wageni. Halafu nilikuwa nimekasirika Net,
sikutaka kuongea kabisa. Kuhofia kuongea neno ambalo lingekuudhi bure, wakati
nilikuona unafurahia na wenzako.” Net akakaa, Tunda akasogeza miguu vizuri kama
kumpisha apate nafasi vizuri.
“Net!” Tunda akaita na kukaa vizuri. Net akabaki
akimwangalia. “Naomba uniambie ukweli. Na kumbuka maisha ambayo nimeishi. Tokea
nazaliwa nimekuwa mtu wa kukataliwa na watu, nimeishi kwenye majumba ya watu
kwa kubembeleza. Nataka kujua ukweli ni kwa nini unataka kunioa wakati…” Tunda
akaanza kulia. “Mimi naona..” Tunda
akakwama.
“Unaona nini Tunda? Niambie unachotaka.” “Sijui Net. Naona kama najiingiza kwenye matatizo.
Nilitegemea kupata faraja kwenye ndoa, lakini inaanza na vipingamizi vikali!
Tena kutoka kwa mtu wa muhimu sana kwako, anayenitangazia vita mpaka kifo
chake. Niambie itakuaje? Tutakuwa na ndoa ya namna gani?” Net akavuta
pumzi kwa nguvu, akakaa vizuri na kujiegemeza kwenye kochi.
“Hata mimi sijui Tunda. Sikuwahi kupenda kabla, na wala
sijawahi kuoa. Sitakuwa na majibu yote ya maswali yako.” Net akanyamaza kwa
muda. Kisha akaendelea. “Unajua umenifanya nijiulize Tunda. Hivi kweli
unanipenda wewe au ni kwa kuwa nimetokea tu unanifahamu? Hivi mtu akikuuliza
kwa nini unakubali kuolewa na Net, utasemaje?” “Nakupenda Net.” Net akakaa
sawa.
“Kweli? Naomba usichanganye upendo, na wewe kujikuta
umeangukia mikononi mwangu. Mtu unayempenda huwezi ukawa ukimfanyia hivi. Hii
ni mara ya pili kunikimbia Tunda. Tena leo umeniacha katikati ya tafrija yetu,
mbele ya wageni niliowaalika kuja kuona nikimvisha pete ya uchumba mwanamke
niliyewatangazia nina mpenda. Mimi ndiye nimekuwa mtu wakukukimbilia kila
wakati na kukuomba urudi. Mimi ndiye nimekuwa mtu wakupigania haya mahusiano
yetu kila wakati!” Net alikuwa amekasirika na yeye.
“Unamuacha Nana, Maya na marafiki zangu waliosafiri safari
ndefu kuja maalumu kwa ajili ya hili tukio. Bila kuaga, tena katikati yao! Huonekani kama mwenzangu unahaja na haya
mahusiano hata kidogo. Unanifanya nitilie mashaka viwango vyangu vya uanaume.
Labda sijafikia viwango vya mwanaume unayemtaka maishani mwako.” “Hapana Net.”
Tunda alijua angebembelezwa, kumbe ameharibu uzunguni.
“Naomba nikuombe kitu kimoja Tunda, tena kabla hatujafika
mbali. Pata muda wakufikiria. Nataka ufikirie kama kweli mimi nafaa kuwa mume
wako au la. Usiogope kuniambia, nitakuelewa tu.” “Net na..” “Usiharakishe
Tunda.” Tunda alitaka kujibu, Net akamkatisha. “Naomba pata muda. Tutaongea
zaidi baada ya hapo.” Net akasimama.
“Ukiondoka humu ndani, ujue unaondoka na mimi Net. Hutaniacha
nikilia tena. Nimeamua kuwa mke wako, wala sihitaji kufikiria. Niliondoka
kuepusha vurugu pale mbele za wageni. Mama hataki kuniona na wewe. Naomba
usiondoke tafadhali. Nakupenda na nimeamua kuwa na wewe. Ila naomba nisiwe
naenda pale kwa mama yako kwa kipindi hiki. Naomba tumpe nafasi.” Tunda alikuwa
amesimama na yeye. Net akarudi kukaa.
“Kweli nakupenda Net,
wala sihitaji kufikiria juu ya hilo. Umekuja kwangu nikiwa sijajiandaa kama
naweza kuolewa na mtu kama wewe na mpaka sasa siamini kama utakuwa mume wangu.
Naona kama naota!” “Usicheke Tunda! Unanitia wasiwasi bwana! Kila wakati wewe
unanikimbia tu!” “Mimi mkeo, Net. Wala huna haja yakunikimbia.” “Wewe ndio
unakimbia.” “Napaniki vibaya sana, hasa nikivamiwa na watu kama mama Cote. Huo
ndio udhaifu wangu. Nitajirekebisha.”
“Kwani alikwambiaje?” “Haitasaidia hata nikikwambia. Ila
nimemuahidi sitamsumbua kwa kufika nyumbani kwake au sitafika mahali ninapojua
atakuwepo, mpaka atakapokuwa tayari kuniona.” Tunda akarudi kukaa pembeni ya
Net na kuanza kuangalia pete yake.
“Umeipenda?” Net akauliza. “Sanaaaaa! Imetoka kidoleni kwa
bibi Cote! Usinitanie kabisa. Nahisi nipo ndotoni. Sasa unajua kinachofuata
nini?” “Sijui.” Net akajibu huku akicheka. “Na wewe uende ukweni.” “Wapi tena?
Nishamuona baba na akanipa baraka zote.” “Ujue siamini! Baba atakuwa amefurahi
sana!” “Sana. Ila nimemuhurumia. Alitamani kuwepo. Na anaonekana mgonjwa.
Umefikia wapi maswala yake?”
“Naona nimepata wakili mzuri kweli. Anafanya mambo kwa
haraka! Ameshaanza kukusanya uthibitisho. Yaani hii ni siku kama ya 10 tokea
aanze, ameshakwenda kuzungumza na baba zaidi ya mara tatu, ashakata rufaa.
Ijumaa alinipigia simu kuwa anashugulikia jumanne apate ruhusa ya kwenda
hospitalini. Japokuwa kampuni yao inadai pesa nyingi, lakini naona wanafanya
kazi kwa ukweli.” Tunda akaendelea.
“Pesa ya kodi ya hapa nimemuomba mwenye nyumba anisubirie
kidogo. Ili kuwalipa wao wanasheria kwanza, ili wajue ninampa baba kipaumbele,
wafanye haraka. Na nimelipa kodi yote ya kule ofisini. Ili mwenye nyumba
asinitoe. Pale napapenda. Ni rahisi watu kufika, halafu pako wazi, barabarani.
Panajiuza penyewe. Sitaki kupapoteza kwa sasa. Kwa hiyo kuhusu baba, naona
jumanne, anaweza kupata ruhusa ya kwenda kutibiwa. ” Tunda akamalizia hivyo.
“Cha kwanza nakupongeza Tunda. Umekuwa na malengo
unayohakikisha unayafuatilia. Unanifanya nijisikie vizuri.” Tunda akacheka.
“Najitahidi hivyo hivyo.” “Unafanya vizuri sana. Halafu kuhusu hapa, kwani
unampango wa kupafanyia nini baada ya kufunga ndoa?” Tunda akacheka tena,
nakuzungusha pete yake ya uchumba.
“Bado siamini!” “Ndio tunatakiwa kufikiria hilo.” “Kwani
ulitaka tufunge ndoa lini?” “Haraka iwezekanavyo.” Tunda akatulia kidogo kama
anayemtaka afikirie zaidi. “Au wewe ulifikiriaje?” “Mimi tena! Sina kipingamizi
Net. Nasubiria kwa hamu kweli!” “Kwani kodi ya hapa inaisha lini?” “Mwisho wa
mwezi huu. Nilitakiwa kulipa kodi tokea tarehe moja.” “Basi mwambie mwenye
nyumba kuwa utahama. Unaomba umlipe ya mwezi mmoja mwingine, lakini unaweza
usikae mpaka huo muda ukaisha.” “Akipata
mmpangaji kabla hatujafunga ndoa?” Tunda akauliza.
“Cha kwanza nitajitahidi kuhakikisha tunafunga ndoa haraka.
Nitazungumza na mchungaji wako na wangu. Japo walishatangulia kuniambia, ni
lazima itangazwe mara tatu. Inamaana kama tukifanya kwa haraka, wataanza
jumapili ijayo. Zipite jumapili tatu, Mungu akisaidia pakawa hakuna
kipingamizi, basi, jumamosi ya nne yake, itakuwa harusi yetu.” Tunda akacheka
kama asiyeamini.
“Ikitokea kuna jambo hapo katikati, tukashindwa kuona kwa
muda huo, sitashindwa pakukuweka mpaka tufunge ndoa.” Tunda akajisikia vizuri
sana. “Asante Net. Ninafuraha yakupitiliza.” Net akacheka. “Karibu.” Akajibu
Net.
“Lakini Net, baba akitoka jela, nilitamani kuishi naye kwa
muda. Angalau arudie hali yake ndipo nimtafutie kitu chakufanya awe na maisha
yake.” “Na mkewe?” Net akauliza. “Kwa jinsi alivyonisimulia, ni kama yule
mwanamke alimwambia waachane siku tatu kabla ya hukumu. Akambembeleza
wasiachane, amsamehe kwa lolote linalomsababisha kumuomba talaka. Lakini
anasema siku moja kabla ya kwenda mahakamani, mama Chale, alimwambia
ameshafuatilia mipango ya talaka. Hamtaki tena. Hata kama atashinda kesi,
akitoka mahakamani asirudi tena nyumani. Aendelee na maisha yake. Na baba
anasema hajamona tena tokea afungwe.”
“Alishajaribu kumtafuta kwa simu?” “Hizi ni jela za Tanzania
Net. Anamtafutaje? Ila anasema alipokuwa mahakamani siku ile, alimwambia dada
yake, mama Sera, akamwambie Mama Chale kuwa amehukumiwa kifungo na atakuwa
Segerea. Hakumtafuta mpaka juzi ijumaa mimi nazungumza naye, baba hajamuona
wala kumsikia.” Net akanyamaza.
“Sitaki akitoka jela ajikute peke yake mtaani.” “Hata mimi
nisingetaka iwe hivyo. Tutajua chakufanya siku hiyo. Ila kwa sasa chamuhimu ni
kumkazania huyo wakili wake, ahakikishe anakwenda kutibiwa. Amedhoofu sana.
Halafu nilimshika ni kama anahoma.” Tunda aliinama na kunyamaza.
“Atakuwa sawa tu. Jumanne sio mbali. Nikuwatafuta tena kesho
na kuweka msisitizo.” “Nitampigia tena kesho kujua amefikia wapi. Na nitakwenda
kumuona baba kama nitaruhusiwa kumuona. Nijue anaendeleaje.” Net akamsogelea na
kumbusu kichwani pale alipokuwa amekaa na kuinama kama anayefikiria. “Asante.”
Tunda akamgeukia na kumshukuru. Akampa tabasamu.
“Unafikiria nini tena? Mbona hilo la baba ni kama limekaa
vizuri?” “Kuna sehemu mbili nataka kwenda.” “Wapi?” Net akauliza wakati
anamvuta mkono. Akaubusu. Tunda akacheka. “Kwa shangazi. Huko ni lazima twende
wote, kama kuwaringishia tu kina Sera, lakini nitajidai nimeenda kuwashukuru
kwa kunipa hifadhi wakati ule mpaka nikakutanishwa na wewe.” Net akacheka sana.
“Tunda!” “Oooh kabisa Net. Walijaribu kuzuia baraka zangu,
lakini ona Mungu alivyohakikisha mpaka nimepata, japo kwa kuchelewa!” Tunda
akamuonyeshea Net kidole chake chenye pete. Wakacheka.
“Usifanye mchezo na Mungu wangu! Hatatulia mpaka
aone napata aliyonikusudia.” “Sasa mbona unatingishwa na mama kama unalijua
hilo?” “Mama yako yule habari nyingine. Kwanza ujue ni kama kwake inabidi
kujirudi kidogo. Nimemuumiza yule mama. Anahaki. Tuendelee na sehemu nyingine
ninayotaka kwenda. Japo...” Akasita na kumwangalia Net, macho yakagongana,
ikawa kama ameamsha kitu kwa Net. Akashangaa Net anamvuta karibu nakuanza
kumbusu.
Tunda akaona alitendee haki lile busu. Akapandisha
miguu yote kwenye kochi, akamgeukia Net akawa kama amejilaza kwake. Walipeana
mabusu ya muda huku Net akimpapasa vizuri, mpaka akamuamsha Tunda, nakuanza
mihemo. Ile hali ikaendelea, Tunda akiendelea kupata busu huku akisikia mikono
ya Net mwilini mwake nakumfanya azidi kujisogeza. Kasi ikaongezeka, wakaanza
kung’ang’aniana kwa uchu na tamaa, kila mmoja anamtaka mwenzake zaidi. Net
alipoona na yeye anakaribia kupitiliza, akasimama kwa haraka, akaenda kwenye
friji ya Tunda.
“Kuna maji ya kunywa humu?” Tunda akaendelea kuvuta
pumzi taratibu huku ameinama kwa aibu akijaribu kutulia na Net mwenyewe
akijaribu kutulia huko alipokua. Tunda hakumjibu wala kumwangalia. Akamsikia
anafungua friji. Kimya kikazuka. Akamuona anaelekea chooni. Tunda kimya,
ameinama palepale sebuleni. Nyumba ikawa kimya kama hakuna mtu.
“Niambie
sehemu nyingine unayotaka kwenda.” Baada ya muda akamsikia akiongea akiwa
anatokea chooni. “Kwa mama.” Tunda akatulia kidogo. Net akarudi kukaa palepale
kwenye kochi. Akambusu tu kichwani. Tunda akacheka kwa aibu bila hata kumtizama
akaona aendelee. “Nataka nikamuombe msamaha, kwa chochote nilichokosea,
ilimradi tu yaishe. Nataka kuanza maisha mapya. Hata asiponisamehe, lakini
nataka niwe nimefanya upande wangu, hayo mengine namwachia Mungu kama
ulivyonishauri.” “Ni uamuzi mzuri.” Tunda akatulia kidogo.
“Nakuonea wivu Net! Unaye mama anayekupigania.
Hataki akuone unaingia matatizoni, kitu ambacho mimi sikuwahi kukipata
maishani. Hicho tu ndio kitu ninacho muheshimu mama yako. Anakupenda sana.”
“Ila natamani ajifunze kuheshimu maamuzi yangu. Naona anavuka mipaka.” “Hapana
Net. Yupo sahihi. Sio rahisi kwa mama mwenye upendo wa kiasi kile kwa wanae eti
kuruhusu tu, mwanae awe na mtu kama mimi! Haijalishi Net. Niwe nimebadilika au
la, bado ni ngumu. Ndio maana naona nimpishe kabisa. Anione pale itakapo lazimu
tu, sio vinginevyo. Lakini sijui nifanyaje upande wa mali.” Net akakunja uso.
“Mali tena?” Net akauliza akiwa hajaelewa. “Hata
sielewi Net. Ujue mama yako anapokuwa na mimi anapandwa sana na hasira sana.
Anazungumza mambo mengi, sijui lipi ni lipi.” “Niambie kuhusu mali. Alikwambia
nini?” “Naweza nisipatie sana, lakini ni kama alitamka kuwa sasa hivi
nakung’ang’ania wewe simtaki tena Gabriel kwa kuwa wewe una mali nyingi kuliko
Gabriel.” Moyo wa Net ulipasuka paa! Walimuonya mama Cote asije zungumza na
Tunda mambo ya utajiri unaozunguka hiyo familia ya Cote.
“Umesema nini juu ya mali!?” Net akataka kujua sasa
zaidi kile mama yake amesema. Kama ameharibu mpango mzima au bado. “Ni kama
alisema nimejua kuwa umeachiwa urithi mkubwa sana na babu yako, na ni kama bibi
yako pia akifa, wewe ndio mtawala wa mali zote huko nchini Canada. Kitu kama
hicho, sijui! Akasisitiza kuwa siwezi kuwa mtawala kwenye Cote. Yeye ndio
anastahili kwa kuwa amehangaika tokea mwanzo kujenga. Akasema hata kama babu
yako ndio amelipia kujenga ile nyumba pale anakoishi, au sijui alisema nini,
ila amesisitiza uwa yeye ndio amesimamia ujenzi wa ile nyumba kuanzia mwanzo
mpaka mwisho.”
“Amesisitiza hakuna Cote hapa nchini bila yeye.
Yaani hata wewe upo hapa nchini kwa sababu yake. Kitu kama hicho. Halafu
anasema nakudanganya wewe na bibi yako
kuwa nimebadilika. Lakini yeye sio mjinga na wala nisidhani kuwa nimeshinda.
Mnanitumia tu.” “Kivipi!?” Net akauliza akiwa hajaelewa.
“Ni mambo mengi magumu hayaelewiki Net.” “Lakini
yeye alisemaje? Niambie kile alichokwambia yeye.” “Amesema wewe na bibi yako
mnanitumia kila mmoja kwa sababu zenu tofauti tofauti. Vile bibi yako leo
alivyonitangaza mimi kama ndiye mama Cote au mrithi sijui wa kiti chake! Wale
rafiki zako na Maya wakachangamka sana pale?” Tunda akataka kumkumbusha Net,
asijue Net mwenyewe bado yupo kwenye mshtuko wa hilo tangazo.
“Nakumbuka. Ehe?” Net akataka aendelee. “Mimi
sikuelewa pale. Lakini yeye anasema ni kwa ajili ya mambo yake anayoyafanya. Ametangaza
vile kwa ajili sijui ya watu wa chama anachokiongoza na wakubwa sijui
wanaomfuatilia au watu wanaomfuatilia sijui sina uhakika! Lakini amesema
amenitangaza mimi malaya ili kuonyesha na kuaminisha ulimwengu kuwa anakubali malaya,
au machagudoa kwa kiasi cha kukubali malaya kama mimi kuolewa na mjukuu wake
ambaye alikuwa akisubiriwa na kila mtu kujua atamuoa nani!” Net akaumia sana.
“Haya.
Akasema na wewe umenichagua mimi sio sababu ya mapenzi, ila ni sababu kama za
bibi yako. Lakini zaidi kumfurahisha bibi yako kumuonyesha unamuunga mkono
kwenye hizo harakati za wanawake, sijui kitu kama hicho! Yaani kuoa kahaba, au
Changudoa kama mimi ni kumuunga mkono kwenye anachokifanya! Sijui bwana Net! Lakini
ni mambo yanayofanana na hayo lakini
sikuelewa vizuri kwa kuwa zilikuwa shutuma nzito, zinazoendana na kweli.” Tunda
akaendelea.
“Haya, ukimsikiliza tena zaidi ni kama hata mimi
mwenyewe haniamini! Anasema nimekuloga. Nimekuzika makaburini ili nirithi
mapesa yenu ambayo mnayo mengi, sijui! Kwa hiyo hatakubali huo utajiri au
urithi ukaja kwangu wakati yeye amehangaika sana na kina Cote. Hapo napo
aliongea sana Net. Mambo mengi. Sikuelewa na wala sijui katika hilo
namsaidiaje.” Tunda ndiye hakuwa ameelewa. Lakini Net akafunguka macho na akili
ikapata mwanga, juu ya chuki kubwa ya mama yake kwa Tunda.
Aliumia sana Net, akabaki akijiuliza hili na
kujumlisha lile. Akajua mengi yanatokana na mali tu! Yeye akidhani ni mapenzi
kutoka kwa mama yake, kumbe analinda mali! Ilimuumiza sana Net. Mama yake
alimwambia Tunda mambo mengi ambayo alishaomba familia nzima, wasimuhusishe
nayo Tunda, ili yeye Tunda aweze kumtenga Net na mali kama wasichana wengi
nchini Canada. Wanaompenda yeye Net kwa kuwa ni Cote.
Net alimtaka Tunda amtizame yeye kama Net kwanza.
Kabla ya Nathaniel Cote anayetangazwa na kuabudiwa huko alikozaliwa, aliko bibi
yake. Kitu kinachomkera na kuona ni bora kuwepo nchini Tanzania ambapo yupo
huru, hakuna anayemfahamu isipokuwa huyo mama yake na kina Gabriel. Alikotoka
Net, chochote watakachofanya familia hiyo, ni tukio la kuuza magazeti kitu
kinachowanyima uhuru wakuishi maisha yao.
Leo mama yake amemkosea sana, na kumuumiza sababu
ya pesa! Tena akiwa amejitoa akimtumikia kwa kiwango cha chini sana akizunguka
kumtafutia tenda zilizokuwa zikimuingizia yeye pesa wala si Net. Hakumdai zaidi
ya mshahara wake tu. Net aliumia sana.
“Lini sasa tunaenda ukweni?” Tunda akauliza na
kujisogeza kwa Net aliyekuwa amepotelea mawazoni akiwa amefunga macho. “Au
umebadili mawazo, ndoa hutaki tena?” “Kukuoa wewe, sijambo nililokurupuka
Tunda. Mungu alisha niandaa kwa muda mrefu sana. Nakupenda na lazima nitakuoa
tu. Lakini siku kama ya kesho, jumatatu nakuwa na kazi nyingi sana, labda
twende jioni.” “Sawa kwa kuwa itakuwa jioni, tuanze kwanza kwa mama. Kesho iwe
mama tu.”
“Nataka nimalize hili la mama kwanza. Ikiwezekana
tuwekane sawa ndipo niende kwa kina Sera. Lakini kwa kina Sera lazima.” “Sawa.”
Waliendelea kuongea wakiweka mipango, mwishowe Net akaaga na kuondoka akiwa
ameumia sana, Tunda sijue.
Jumatatu!
Siku hiyo ilianza na hekaheka kweli hasa kwa Tunda. Alianzia
ofisini kwa wakili wa baba yake. Wakazungumza na kumuhimiza ni lazima baba yake
kesho apelekwe hospitalini. Baada yakumsikia mikakati yake na pale alipofikia,
akaridhika na kuondoka kurudi ofisini kwake. Siku za jumatatu hawakuwa
wakiwasiliana sana na Net zaidi ya salamu ya asubuhi kabla hawajatoka
kitandani. Watapeana mipango ya siku nzima, siku inaanza.
Hakuwa amemsikia Net siku hiyo, na yeye akaendelea na kazi
zake akiwa na Betty tu, wakiongea hapa na pale. Betty alikuwepo kanisani siku
iliyopita. Akataka kuiona kwa karibu pete hiyo ya Tunda. Basi, akaitizama na
kuishika. “Umeuchinja dada Tunda!” Pesa huleta heshima. Japokuwa Betty alikuwa
mkubwa kwa Tunda bosi wake, aliweka heshima. Tunda alicheka tu.
Kazi ziliendelea, ilipofika mchana Jaz, msichana aliyemkimbia
Tunda pale kazini, akarudi kuomba kazi tena. Week ilishapita, hakuwepo kazini,
na siku ya jumatano alipokwenda kwenye bible study, hakumsalimia Tunda bosi
wake. “Kwa nini unataka kurudi na kwa nini uliondoka Jaz?” Kimya. “Umesambaza
maneno mengi machafu kanisani juu yangu.” “Nisamehe.” “Nimekusamehe lakini hapa
sitahitaji tena mtu wa pili. Tumeshauriana na mama Penny, tumeona Betty peke
yake atatosha. Kwanza ameweza kufanya kazi zote bila shida. Ni kweli hata
ukirudi humu, hutakuwa na kazi ya kufanya. Halafu sitaweza tena kukulipa na
wewe kwa kuwa nimeamua kumuongezea mshahara Betty, kwa kuwa nimemuona ameweza
kufanya kazi zako vizuri bila shida wala kulalamika kama wewe Jaz. Nashauri
urudi kwa mama Penny, anafahamiana na watu wengi. Atakusaidia kupata kazi
kwengine.” Tunda akamuaga, ikabidi Jaz aondoke. Hata Betty hakuamini kama Tunda
amefanya hivyo. Na yeye nidhamu ikaongezeka.
Baada ya miaka mingi, Net mrudisha Tunda kwa
mama yake mzazi, Akiwa mchumba.
Ilipofika
kwenye mida ya saa 10 jioni, Tunda alirudi nyumbani kwake kwenda kujitayarisha
kwa kwenda kumuona mama yake. Wasiwasi ulizidi kumsumbua. Hofu ya kuja kuiona
tena sura ya baba Tom, ikazidi kumkandamiza nakutamani kama asiende tena. Baba
Tom alikuwa msaliti mkubwa sana kwake. Alimtelekeza akiwa na mimba yake!
Net
alifika nyumbani kwa Tunda. Alimkuta ameshajiandaa lakini anawasiwasi sana.
“Umependeza sana. Lakini usoni unaonekana una hofu yakupitiliza!” “Nimeshindwa
kula siku nzima, namuwaza yule baba. Nafikiria kwenda kuomba msamaha ambao
nilikuwa nikisubiri miaka yote kuja kuombwa mimi!” Tunda akaanza kulia.
“Hujui jinsi alivyonitesa, tena bila msaada wa mama, Net.”
“Nisikilize Tunda. Unafanya kitu sahihi. Unasamehe kwa ajili ya nafsi yako si
kwa ajili yao. Utaona amani utakayopata baada ya hapo. Muachie Mungu atapambana
naye. Wewe twende ukafanye kwa nafasi yako.” “Mama
akinifukuza?” “Tutaondoka. Wala usiwaze upande wao, twende ukafanye
upande wako.” Tunda na Net wakaondoka mpaka nyumbani kwa mama yake Tunda huko
mitaa ya Kitunda alipowaacha wakiishi.
Kitunda kwa Mama Tunda!
Tunda
alishangaa kukuta familia ngeni kabisa kwake. Akamsalimia mama aliyemfungulia
mlango, kisha akaeleza shida yake. “Tunaweza kumuona Mama Tom?” Akaguna yule
mama akiwa amesimama palepale mlangoni. “Sipendi usumbufu wa usiku usiku!”
“Samahani. Tumechelewa kwenye foleni.” Tunda akajibu kiustarabu. “Sijui kama
huyo Mama Tom Yupo! Labda mpite huko nyuma.” Alijibu mwanamke aliyewafungulia
mlango, huku akionyesha kidole kuwaashiria wapite. “Asante sana.” Tunda akashukuru
na kumvuta Net mkono.
Nyumba
ilikuwa imejaa watu asiowafahamu kabisa. Ule usafi aliouacha kwenye ile nyumba
haukuwepo kabisa. Kwa kuwa alikuwa akiifahamu ile nyumba, Tunda hakupata shida
kutokea vyumba vya nyuma, ambavyo havikuwa vikitumiwa kipindi anaishi kwenye
nyumba hiyo isipokuwa chumba kimoja kilikuwa kama stoo na kingine alikuwa
akilala mfanyakazi wa kiume.
Na huko
uwani nako Tunda alikuta watu wengine.
Alisita kidogo. “Habari zenu?” Wote walibaki wakimtizama. Mara ukagongwa
mlango wa nyuma, mtoto akitaka auziwe icecream. Alisimama binti ambaye alikuwa
na umri unaokaribiana na Tunda, akaingia ndani na kutoka na icecream. Tunda
akabaki ameshangaa.
“Tunda!”
Net akamshtua kidogo. “Samahanini jamani. Tunataka kumuona Mama Tom.” Wakatizamana
na kucheka. “Na nyinyi pia mnamdai?” Walimuuliza Tunda na Net. “Kama mnamdai
muandike maumivu tu. Wenzenu wanapishana hapa! Hivi ni jana tu walikuja kumbeba
wanawake wenzake wakampeleka polisi. Kala pesa ya kikoba!” Wakacheka wote kwa
kupokezana. Tunda aliumia sana.
“Sisi
hatumdai. Mimi ni mwanae na huyu ni mchumba wangu.” Wote wakabaki wametoa
macho. “Wewe ndio Tunda!?” Mmoja wao akauliza. “Ndiyo.” Tunda akajibu. “Mama
Shangazi! Mama Shangazi!” Mmoja aliita. “Njoo umuone Tunda!” Tunda akabaki
ametulia. Alishangaa kuona watu wengine wanatoka nyumba kubwa na wengine
vyumbani kuja kumshangaa yeye kama mnyama wa mbuga za wanyama.
“Jamani,
kwani Mama Tom yuko wapi?” Ikabidi Tunda kuuliza tu. “Wanae wapo chumba hicho
hapo. Anawafungia kama kuku!” Tunda akasogea mpaka kwenye hicho chumba
alichoonyeshwa, huku Net akimfuata nyuma.
Akaanza
kugonga. “Nani?” Sauti kutoka ndani ikauliza. “We Tom! Ni mimi Tunda. Fungua
mlango.” Waliona taa ya ndani imewashwa kisha mtu akachungulia dirishani.
“Umesema Tunda, dada Tunda?” “Ndiyo. Ni mimi, fungua usiogope.” “Wewe Tom, mama
amesema tusimfungulie mtu yeyote. Shauri yako.” Walisikia sauti ya mtoto wa
kike ikimuonya Tom.
“Ni
Tunda. Tunda yule dada yetu. Wewe humjui ulikuwa mdogo sana. Tena alikulea.
Nimfungulie?” “Sijui.” Walikaa kimya kwa muda. “Kwani mama yuko wapi?” Tunda
akauliza. “Ametoka muda kweli! Amesema tusitoke wala kufungua mlango mpaka yeye
mwenyewe awepo.” Tom akajibu. “Basi sisi tunaenda kumsubiria nje kwenye gari.
Akirudi mama, mje kutuita.” Tunda akashangaa mlango unafunguliwa, kisha Tom
akatoka.
“Mbona
uliondoka bila kuniaga?” Ndio swali la kwanza Tom akamuuliza Tunda. “Sikujua
kama sitarudi tena. Mnaendeleaje?” “Njooni ndani.” Tom aliwataka waingie ndani.
Tunda na Net wakaingia kisha akafunga mlango tena. “Aneti amekuwa mkubwa! Njoo
unisalimie. Sijui unanikumbuka?” Tunda alimuongelesha yule mtoto wa kike kwa
upendo.
“Mimi
ndiye nilikuwa nikikulea.” Tunda aliongeza, lakini Aneti hakujibu. “Umekuwa
mkubwa Tom! Mnaendeleaje?” “Umependeza sana Tunda, dada yangu!” Tom akajibu.
“Asante.” “Huyo ni nani?” Tom akauliza. “Ni mchumba wangu, anaitwa Net.”
“Umepata mchumba wa kizungu!? Ndio maana umebadilika Tunda. Anaonekana ni
mzungu mwenye hela. Anasikia Kiswahili?” Tunda akacheka. Akakumbuka utundu wa
Tom.
“Anaelewa
kila kitu. Hapo alipo anakusikiliza na anaelewa kila kitu unachoongea.” “Acha
masihara bwana Tunda! Usiniogopeshe. Mbona haongei sasa?” Tunda akazidi kucheka.
“We Tom hujaacha utundu tu?” “Mambo yamebadilika dada! Mama amekuwa kama
kichaa.” “Baba yako yuko wapi?” “Amefungwa.” Tunda akashtuka sana. “Nini
tena!?” Tom akanyamaza, akaonekana kusita.
“Kuna
nini Tom?” “Alikuwa akimfanyia mambo mabaya Aneti, halafu alimbaka dada wa
kazi.” “Yule niliyemuacha?” “Yule alizaa naye, mama akamfukuza na kuletewa na
bibi mtoto mdogo kutoka kijijini. Ndiye aliyekuwa akitusaidia kazi.” Tunda
alimwangalia Aneti kwa kumuhurumia sana. “Pole Aneti.” “Hapo bado yupo kwenye matibabu.
Tulikuwa hatujui kitu anachomfanyia Aneti, mpaka akaanza kunuka sana.” Tom
akaendelea.
“Kumbe
alimuambukiza mtoto ugonjwa wa zinaa, mama kuja kumpeleka hospitalini akaambiwa
Aneti ameharibika sana na anaugonjwa wa gonorea. Ikabidi asafishwe sana. Alikuwa
ameoza. Wakati mama yupo hospitalini amelazwa na Aneti, baba akambaka yule
msichana wa kazi. Sasa mimi wakati najiandaa kwenda shule asubuhi, nikashangaa
yule mtoto haamki kunisaidia kuandaa chai. Kwenda kugonga, nikamkuta amepoteza
fahamu.”
“Ndio ikabidi
nimpigie simu mama, baba alikuwa ameshatoroka. Nahisi alimziba mdomo na pua ili
asipige kelele wakati anambaka, ndio akapoteza fahamu. Mama akatuma majirani
waje wamchukue na kumkimbiza hospitalini. Mambo yakafika polisi, baba
akatafutwa na kukamatwa.”
“Hivi
hao wote unaowaona hapo ni ndugu zake baba, wametuchukia sana. Wanatulaumu eti
kwa nini tulimshitaki baba ambaye anategemewa sana huko kwao. Wanatuambia ni
mambo ambayo tungepaswa kuyamaliza kindugu tu. Tangia waje baada ya baba
kukamatwa, hawajaondoka tena. Wametufukuza kwenye hiyo nyumba kubwa, lakini
mama amekataa kuondoka, ndio ameomba tupewe angalau hiki chumba kimoja wakati
anatafuta pakwenda kuishi. Mama amechanganyikiwa kabisa, Tunda. Kazi
imemshinda, anakazi ya kukopa mpaka aibu! Kila siku anakuja kudaiwa hapa, tena
anadhalilishwa kweli!” Tunda alizidi kuumia.
“Amekwenda
wapi sasa?” “Anasema kuna mahali anadai pesa zake. Ni mwezi sasa, anazifuatilia
hizo pesa. Nikimshauri aachane nazo tuanze kuhangaika kutafuta pesa kwa njia
nyingine, anakuwa mkali kweli. Anatufungia mchana na usiku. Hataki tutoke.
Akitukuta nje, utamuonea huruma. Anakuwa kama mwehu. Biashara zote zimemshinda.
Anazurula tu mtaani.”
“Sasa na
wewe shule?” “Na kwambia siruhusiwi kumuacha Aneti hata sekunde. Nampeleka
mpaka chooni. Hataki nisogee hata hatua moja mbali na Aneti. Nikimwambia
maswala ya shule, ni kama haelewi naongea nini. Nikikwambia hali ni mbaya, si
utani.” Tunda akabaki amepigwa na butwaa. Net alikuwa kimya akisikiliza tu.
Akavuta mkono wa Tunda na kuubusu. Tunda akavuta pumzi kwa nguvu nakubaki kimya
akiwatizama wale watoto.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Usikose
muendelezo kujua kitakachojiri mbeleni...
0 Comments:
Post a Comment