Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Nilipotea! – Sehemu ya 26. - Naomi Simulizi

Nilipotea! – Sehemu ya 26.

 

T

ayari juma zima na siku kadhaa ilishakatika tokea apatwe na huo mkasa. Kanisani hapaendeki, nyumbani hapakaliki. Kula yake ilishakuwa ya shida, hakuwa akilala vizuri. Ilipofika jumamosi alikuwa amedhoofu kwa njaa na hofu, alitamani asiende kazini, lakini ilimbidi. Alikuwa na kazi kubwa inayomsubiri siku hiyo. Kupamba ukumbi wa harusi ya mtoto wa balozi wa Tanzania nchini Uholanzi. Na alishalipwa nusu ya pesa. Hata hivyo alihitaji sana pesa, ilikuwa lazima akafanye kazi. Alikumbuka jinsi alivyohangaika kuianzisha ile biashara, hakutaka kurudi kwenye ule umasikini wa zamani.

Alishtuka saa kumi asubuhi akaamua kwenda tu ukumbini kuanza kupamba mara baada yakukosa ujumbe kutoka kwa Net. Alishinda akipamba siku nzima, akitoka ukumbi mmoja kwenda mwingine mpaka usiku sana ndipo aliporudi nyumbani.

Akaamua kutuma ujumbe mwingine kwa Net. ‘Nimekosa Net, nimekosa kukuficha kuwa niliwasiliana na Gabriel. Nisamehe. Lakini sikuwa na nia mbaya mpenzi wangu. Sikutaka kuwachonganisha na Gab. Lakini nilimwambia kabisa kuwa nimebadilika, nimemkataa, na nilimwambia kabisa nakupenda wewe. Nakupenda Net, na nimejifunza kutokana na makosa, sitarudia kukuficha kitu tena. Naomba nisamehe.’ Tunda alikaa pale akisubiri mwishowe akaona simu ya Mama Penny inaingia.

“Mbona unalia na kanisani huji tena?” “Nimechanganyikiwa dada yangu! Ghafla maisha yamenibadilikia. Net ameniacha na kanisani wananisema vibaya sana. Nashindwa kurudisha sura yangu pale.” Tunda alikuwa akilia sana. Tokea jumatano ya juma lililopita alipotoka katikati ya ‘bible study’ wale kina mama wakimsema kwa kujidai wanamuuliza maswali mchungaji, hakurudi tena. Jumapili yake alimtumia ujumbe mama Penny kumwambia kuna kitu muhimu kule gerezani kwa baba yake, lazima aende kumuona. Ni kweli alikwenda na mwanasheria ili kuangalia hiyo afya ya baba yake atengenezee kesi. Jumatano kwenye kipindi cha ‘bible study’ kanisani pia hakwenda. Akamtumia ujumbe kuwa ana kazi, hatamaliza kwa wakati.

Sasa jumamosi hiyo usiku ndipo mama Penny akampigia. “Wale kina mama wa kanisani, Mchungaji aliniambia nimeshazungumza nao wote, wala usiwe na wasiwasi. Umesikia?” Tunda aliendelea kulia tu. “Net amekuacha kivipi!?” “Nilikosea dada. Net akajua kitu nilichofanya bila kumshirikisha. Amenikasirikia kuanzia siku hiyo, hajanitafuta wala hajibu jumbe zangu. Na nilishamwambia sikuwa na nia mbaya.” “Labda amesafiri ndio maana anashindwa kupata na kujibu jumbe zako.” Mama Penny akajaribu kumtuliza.

“Simu ya Net inapokea ujumbe wa yeyote, kutoka popote hapa ulimwenguni na yeye akiwa popote hapa ulimwenguni. Muda na wakati wowote, dada. Ni ameamua kuniacha tu.” “Usilie bwana. Naamini anayo sababu tu. Unataka nije?” “Nimechoka sana dada yangu, siwezi hata kusogea.” “Lala basi, kesho nitakuja asubuhi kabla sijaenda kanisani.” “Sawa.” Tunda akajivuta na kujilaza hapohapo kitandani bila hata ya kuoga.

Jumapili.

Asubuhi na mapema, mama Penny alifika nyumbani kwa Tunda kumuona kabla ya kwenda kanisani. Ikabidi Tunda amuelezee kila kitu bila kumficha. “Nilikosea dada.” “Najua Tunda, lakini huwezi kufa hapa na ukashindwa kuendelea na maisha. Tulia kabisa, mpe muda kama alivyoomba. Kama ni wako, atarudi, kama sio wako basi. Naomba ujiandae twende kanisani.” Alihakikisha Tunda amevaa vizuri, akampa kifungua kinywa akamwambia aache  gari yake yeye atamuendesha. Kidogo Tunda akatulia.

Maneno mengi ya Mama Penny yalianza kumfanya Tunda aanze kucheka njiani. Alimpa vituko vya wanae na mikasa mbali mbali ya siku iliyopita wakati ameenda kupamba. Tunda alikuwa akicheka, japo kinyonge.

Walifika kanisani, kwa kuwa Tunda alikuwa amechoka sana aliingia moja kwa moja ndani kanisani akatafuta kona ambayo alijua watu hawatamsogelea akaenda kukaa na kuinama ili alale kidogo. Mama Penny kama kawaida yake ya kuwahi na kuhakikisha kanisa limekaa vizuri. Kuanzia usafi wa mazingira, chooni, ndani na nje ya kanisa, na kumalizia kupamba kabla mumewe hajaja na watoto, aliendelea na pilika pilika zake wakati Tunda amelala kanisani.

Ibada ilianza, watu waliingia na kwa kuwa Tunda alijua kila mtu anamkwepa, hata Julius mwenyewe hakuonyesha kutaka kuwa karibu naye tena, kwa hiyo hakutaka kusumbua nafsi yake, alibaki ameinama bila kusimama wala kumsalimia mtu. Ibada iliendelea, nyimbo mbalimbali ziliimbwa, lakini hakuinuka.

Alisikia watu wa viti vya mbele wakihamishiwa viti vya nyuma kabisa kule alipokuwa amekaa yeye, huku akisikia minong’ono kuwa kuna wageni ambao watakaa viti hivyo vya mbele. Tunda aliwaza kidogo. ‘Kina nani hao!? Mbona Mama Penny hajaniambia kitu chochote?’ Lakini kwa kuwa alikuwa amechoka sana, hakutaka kuendelea kufikiria juu ya mambo ya wageni wakanisani wakati ya kwake yanamshinda! Akabaki ameinama vilevile.

Watu waliendelea kuimba na kucheza wakati bado Tunda amekaa chini huku ameegemeza kichwa chake kwenye kiti cha mbele yake, anasinzia.

Mara akasikia Mchungaji akiongea na watu wote wakakaa, ndipo Mchungaji alipokaribisha watu watoe ushuhuda. Walisimama watu wachache wakashuhudia yale mambo Mungu ametenda, kisha akasikia Mchungaji akisema, naomba mtulie kimya, msikilize. Kwani waumini wengine walikuwa wakishangilia yale waliyokuwa wakishuhudia wengine.

“Naomba msikilize kwa makini sana yale Mungu amefanya kwenye maisha ya huyu binti.” Kanisa zima likatulia.

“Nimepata msaada Gabriel. Nimesamehewa dhambi. Huko kwenye hayo maisha sitakaa nikarudi tena. Nilitumikishwa na ibilisi mchana na usiku. Mungu amenifungua, nipo huru. Nimeanza biashara yangu kwa jasho langu bila kuhongwa, na sasa hivi ninafurahia maisha.”

Tunda alisikika akilia kisha akaendelea.

 

“Sasa hivi anayeishi hapa ni Tunda, aliyesamehewa dhambi na kuishi maisha ya nidhamu mbele za Mungu. Na mabaya yote niliyofanya zamani, Net amenipokea na ananipenda kwa dhati. Naridhika na pesa ninayoingiza kwa jasho langu na mapenzi ya Net, basi.”

 

Ile sauti ikapotea. Tunda akahisi yupo usingizini anaota. Alianza kutetemeka palepale alipokuwa amekaa, akashindwa hata kusogea. Alijiambia ni ndoto kwani alikumbuka ni maneno aliyokuwa amemwambia Gab. ‘Lazima hii ni ndoto! Hii ni ndoto tu.’ Tunda aliwaza huku akifuta machozi. Alihisi ni uchovu wakuto kulala vizuri kwa muda mrefu.

Akaona kabla hajaharibu zaidi pale kanisani anyanyuke, akatafute taksii, arudi nyumbani akalale. ‘Isije kuwa naanza kuchanganyikiwa!’ Akajisemea Tunda akilini.

Suprise!

Tunda akahisi ukimya mkubwa sana pale kanisani, akaamua kunyanyua kichwa. Hakuamini baada yakumuona Net amepiga goti pembeni yake. “Net!?” Tunda akashtuka sana kumuona Net pale. “Ni nini, kina...” Tunda akasita. Mambo mengi yakaanza kupita akilini. Akatulia kidogo. “Naomba nisamehe Net. Nia ilikuwa nzuri, sikutaka kuwachonganisha na Gab. Lakini nakuahidi siku nyingine sitakuficha kitu. Nisamehe.” “Kama utakubali nikuoe.” Net akazidi kumchanganya Tunda. Usingizi, kutokulala kwa muda mrefu kwa wasiwasi na uchovu kwa ujumla, vilimfanya ashindwe kuelewa kwa haraka.

 “Nini!?” Alijaribu kukausha machozi kwenye macho yake ili amtizame Net vizuri, lakini machozi yalikuwa yakichirizika kama maji. “Nataka uwe mke wangu Tunda.” Ilibidi tu ainame. Alishindwa kujibu, wala kuelewa kwa sekunde kadhaa. Net aliacha kupokea simu zake na kujibu jumbe zake, leo anatokea kanisani, anasema nini! Alishindwa kuinuka wala kuongea.

“Kiss her already!” Sauti ya kizungu ya kike, ilisikika ikipaza sauti ikimtaka Net ambusu Tunda. Baadhi ya watu wakaanza kucheka. “Nathaniel Cote!” Ilirudia tena kumwita kwa msisitizo. “We are at the Church, Nana!” Net akababaika akijua maadili ya kiafrica na hapo walipo, kanisani! Anaanzia wapi kumbusu Tunda! “So what?” Bibi yake akamshangaa kinachomshinda ni nini kutoa busu kwa mpenzi wake. “Nooo!”  Net akakataa kwa mshangao.

“I thought we raise you well!” Aliendelea kumchokoza Net. “Yes you did.” “Then man up and kiss her.” “No Nana! We are here.., you know?” Net akajaribu kumuonyesha mazingira na watu waliokuwepo pale, wanao wazunguka. Kama kumkumbusha ni Africa!

“See what you have done to him? He can not even kiss his own fiancé.” Yule bibi alimgeukia Mama yake Net nakumlaumu.  Lakini Ritha alibaki kimya, akacheka kidogo tu kwa kujibaragusa. Maya yeye alikuwa akicheka sana mpaka machozi pamoja na watu wengine waliokuwa wakiwaelewa.

“I told you Nana! Look at him. She can not even kiss Tunda!” Maya akaongeza. Net na Maya walikuwa wakimwita bibi yao Nana na babu yao papa. “I bet your papa is very embarrassed by you, right now! Can’t imagine your dady!” Yule bibi aliendelea kumchochea Net akimwambia anawaaibisha babu yake na baba yake huko walipo.

“What am I suppose to do? She can not even look at me.” Net akasikika akijitetea kwa bibi yake kuwa hajui chakufanya kwani hata Tunda mwenyewe hamwangalii. “Mam up! Lift her up, hold her in your arms and then kiss her. That’s all!” Bibi yake akajibu kwa msisitizo akimwelekeza kitu chakufanya mjukuu wake kama asiyejua.

“You mean now?”  Net akauliza akionyesha wasiwasi huku akimwangalia mama yake. “Right NOW Son. Do it.” Akajibu yule bibi kwa msisitizo kwamba huo ndio wakati wa kumnyanyua Tunda, kumuweka mikononi vizuri na kumbusu. Kisha yeye na Maya wakaanza kushabikia kwa kuimba, “Do it! Do it! Do it! Do it!” Waliendelea kuimba kama kumtia morali Net, Ritha kimya.

Net alibadilika rangi akawa mwekundu mpaka jasho, kwa hofu. Maya na bibi yake hawakunyamaza mpaka Net aliposimama na kumnyanyua Tunda. Akamkumbatia huku akimsugua mgongoni. “I said kiss her not petting her back! What’s wrong with you!?” Bibi yake alipaza tena sauti kwa mshangao kuwa alimwambia amnyanyue na kumbusu, sio kuishia kumbembeleza tu! Bado watu walikuwa wakiwatizama na walioelewa kucheka.

Net akajikaza. Akamvuta Tunda nyuma kidogo, akashika shingo yake kwa mikono yake yote miwili huku akimtizama, kisha akaanza kumbusu. Yule bibi na Maya wakaanza kushangilia kishabiki, ndipo watu wakaanza kupiga vigelegele. “You are a man now.” Bibi yake akamsifia kwa sauti ya juu kuwa ameshakuwa mwanaume.

Net alipiga tena magoti na kuuliza swali huku ameshikilia pete yake. “Will you mary me, Tunda!” Tunda aliendelea kufuta machozi huku akitingisha kichwa kukubali. Mambo aliyokuwa akiyaona kwenye luninga, aliona yanamtokea siku ile. Net alimvuta mkono na kumvalisha ile pete. Tunda hakunyamaza. Busu hilo alilokuwa amelitunza muda wote, ameishia kulipata Nathaniel Cote, kijana wakichotara, aliyebeba damu nyingi ya weupe.

Net akamshika mkono wakataka kutoka nje. “No no no nooo. Hold up son!” Net akasimamishwa na bibi yake. “What!?” Net akamuuliza huku akimtizama bibi yake kwa mshangao. “She is not your wife yet!” Akamuonya mjukuu wake asije nogewa, si mkewe. “I know Nana! I just want her to calm down and then we will be right back.” Net akajitetea kuwa anakwenda tu kumbembeleza ili atulie, kisha warudi. Maana ni kweli Tunda alishindwa kunyamaza. Kitu kilimkaba kooni, akawa haelewi tena. “You better!” Bibi yake akaweka msisitizo. Wote wakacheka, Net akatoka na Tunda nje.

“Nilijua umeniacha Net. Nilijua hunitaki tena. Kwa nini ulinifanyia hivyo?” “Samahani sana Tunda. Sikukusudia kukutesa kwa muda mrefu mpenzi wangu. Nilitaka kukufanyia surprise kwa jinsi ulivyonifurahisha.” “Nimekufurahisha na nini tena!?” “Nyamaza kwanza.” “Hapa nina usingizi na njaa, Net. Sijalala vizuri tangia siku ile ya mwisho tulipowasiliana. Nilichanganyikiwa, nilijua umeniacha!” “Naanzia wapi Tunda!? Siku ile mnawasiliana na Gab, ule ulikuwa mtego tu.” Tunda akashtuka sana.

“Sitaki kukutia hofu, lakini nakutahadharisha tu. Unafuatiliwa sana. Wapo watu hawaamini kama kweli unanipenda kwa dhati, wanafikiri upo na hila.” “Kina nani!?” “Hilo sio la msingi ila ujue wanakufuatilia. Kuanzia siku ya kwanza Gabriel anakutumia ujumbe, halafu ukashindwa kuniambia, walianza kunicheka sana. Siku ulipoenda kukutana naye alikuwa amevaa spika, unasikika live, na kuna mtu walimuweka  kuwapiga picha. Niliumia sana nilipopigiwa simu kuambiwa umeshafika eneo la kukutania na Gab. Mwili wote ulikuwa ukitetemeka, nikiwaza itakuwaje kama utamkubalia Gab. Nilikuwa nashindwa hata kupumua. Nilitamani kuja pale nishuhudie, lakini nikajikaza.”

“Ikabidi kuja kuwapigia tena simu kuuliza mambo yalikwendaje, ndipo nikaambiwa kwa sasa umemkataa. Ndipo ikabidi kufuatilia mazungumzo yote waliyokuwa wamekurikodi. Nilifurahi sana, na kumshukuru Mungu wangu.”  Hofu ilimwingia Tunda  mwili mzima ukaanza kutetemeka.

“Sasa baada ya hapo, nikawa kama nimewasuta, lakini bado hawaamini. Wanahisi kwa kuwa ni Gabriel. Umemkataa kwa kuwa alikuumiza na umejua kuwa tunafahamiana. Wakasema kama ingekuwa mwanaume mwingine mwenye pesa ungemkubali tu. Lakini kwangu nilikuwa nafuraha yakupitiliza. Nikawa nina kazi yakurudia rudia yale mazungumzo kati yako na Gab.” Tunda alibaki anashangaa nakushindwa hata kujisogeza akifikiria kwa upya ni nini alizungumza na Gab siku ile.

“Nilifurahi nakushindwa hata kusubiri tena. Nikampigia simu Nana kumwambia kuwa nataka kuoa. Ndipo aliposema nilazima awepo kwenye kila hatua mpaka ndoa. Ikabidi nikate tiketi ili nikamfuate, aje ashuhudie ninavyokuvalisha pete ya uchumba. Sikujua kama naweza kuchukua muda mrefu kiasi hiki Tunda. Nilijua naenda Canada mara moja kumfuata Maya na bibi, kisha nirudi nao baada ya siku mbili, kisha nikuvishe pete ya uchumba wao wakiwepo. Lakini kufika kule kuna mambo yakajitokeza, ikabidi nimsubirie Nana kidogo. Tumeingia jana. Nimepata ule ujumbe wako wa jana, nikajua hali yako ni mbaya, ikabidi kumuomba mama Penny akupigie ili akutulize.”  Tunda akashtuka kidogo.

          “Mama Penny!?” Tunda akauliza kwa mshangao. Net akacheka kidogo. “Ndiyo, mama Penny. Anafahamu kila kitu. Na hata nilipokuwa kule niliongea na Mama Penny nikamuomba aniandalie mazingira yote, ili nikija iwe ni kukuvalisha hii pete tu. Lakini aliniambia nifanye haraka una hali mbaya. Pole sana mpenzi wangu. Sikukusudia kukutesa.” Bado Tunda alikuwa kwenye mshtuko na hofu.

“Twende ukalale sasa hivi, ili baadaye uweze kuhudhuria tafrija. Mama Penny amenisaidia kukuandalia tafrija nyumbani kwa mama ambako bibi na Maya ndiko walikoshukia hapo. Wale wageni wote niliokuja nao hapa kanisani kwenu ni wakutoka kanisani kwetu, na wengine nimarafiki zangu wa hapa na wachache tumekuja nao kutoka Canada. Wapo na marafiki niliokua nao tokea watoto. Wapo wawili, sijui kama umewaona?” “Mimi nimekuona wewe tu pale ndani.” Net akacheka kidogo.

“Basi na wao wamechangia kuchelewa kwangu. Nilipowaambia naoa, wakataka tuongozane nao waje huku nchini. Wanaondoka kesho asubuhi kurudi kuwahi majukumu yao. Jana nilipofika tu, nilienda kuongea na baba yako. Ilibidi kuomba kuwa ni dharula ili waniruhusu kumuona maana ilikuwa sio siku ya kuwatembelea. Nikaruhusiwa. Amefurahi sana. Amesema kesho tumpelekee picha.” Tunda alihisi yupo usingizini.

“Ungeniua Net!” “Sitarudia tena kufanya hivyo. Kwanza nilitaka kukupa onyo. Usiwahi kunificha jambo, na pia nilitaka kukufurahisha.” “Samahani Net. Naahidi sitarudia tena. Umenipa somo ambalo nimejifunza kwa mateso sana. Nilijua umeniacha!” Machozi yakaanza kumtoka tena Tunda.

“Lakini pia imekusaidia kufikiria Tunda. Angalau umejua kama unataka kuwa mke wangu au la. Unajua nilikuja kujilaumu? Ni kama nilikuja kukuvamia tu! Tokea mwanzo kila kitu kikawa kinaenda kwa vile nilivyokuwa nikitaka mimi. Angalau umepata muda mtulivu wakuwaza.” “Sikuhitaji muda wa kujua kama nakupenda au la Net. Nakupenda.” “Sasa hivi nimehakikisha.” Net alimvuta tena na kuanza kumbusu midomoni. Hiyo furaha aliyojisikia Tunda, hakuna jinsi angeweza kueleza. Alikuwa akikwepesha hiyo midomo akitaka kuja kupata busu la uhakika. Na kweli Mungu akamsaidia na kupata busu la Net. Alikuwa akifurahia sana.

Japokuwa Tunda alishakuwa na wanaume wengi hakuwahi kupata busu kama lile. Net alimshika vizuri na kwa heshima wakati akimbusu kama anashika mwili wa thamani sana kumbe ni mwili wa Tunda uliopitiwa na wanaume kibao, na yeye akilijua hilo. Tunda alilihisi lile busu katika kila kiungo cha mwili wake. Machozi ya furaha yalikuwa yakimtoka si huzuni tena, asiamini.

“Asante sana Net. Asante.” “Umeipenda pete?” Tunda akanyoosha mkono wake na kuanza kuiangalia ile pete. “Nzuri sana. Nimeipenda. Asante.” “Hiyo ni pete ya bibi. Alivalishwa na babu, alinitunzia kwa muda mrefu akasema nikipata mwanamke ninayempenda, nimvalishe.” Tunda akacheka.

“Anaonekana mcheshi!” “Anavituko huyo! Akiamua kukufungulia moyo, wala huhitaji siku nyingi zakumzoea. Ila anatupenda sana mimi na Maya.” “Nikwambie kitu Net?” Net alikuwa bado amemkumbatia Tunda, hapohapo nje ya kanisa huku akimwangalia kwa upendo kama aliyeokota lulu kumbe ni Tunda kituko kwa wengine.

“Mmhh!” “Umenipa heshima ambayo sikuwahi kufikiria hata siku moja kama naweza kuja kupata. Sikujua hata kama nastahili! Hapa nahisi nipo ndotoni. Asante sana.” “Wewe ni wathamani sana Tunda. Sio kwangu tu, hata machoni pa Mungu, ndivyo anavyokuona. Sijafika hata nusu ya punje ya mchele, vile Mungu anavyokupenda na kukuheshimu.” Kabla hajambusu tena, “Mnaitwa na Mchungaji mkaombewe.” Mama Penny alitoka na kuwakuta bado wamekumbatiana wakitaka kupeana mabusu tena.

“Asante sana mama Penny, kwa kila kitu. Naamini mpaka sasa tupo sawa.” “Karibu Net. Kila kitu kipo sawa kabisa.” “Tunashukuru sana, lakini naomba baada ya maombi tu, nimrudishe Tunda nyumbani akapumzike kidogo, halafu tutakuja kwenye tafrija baadaye akishatulia.” “Mnaacha wageni wenu hapa!?” “Wewe si upo?” Net alimshangaza mama Penny.

“Leo ni siku yangu na Tunda. Nataka aifurahie. Kwa jinsi alivyochoka hivi, sidhani kama atafurahia chochote kwenye tafrija.” “Utamuaga mama yako?” Akauliza mama Penny. “Nitaongea naye. Kwa kuwa tafrija itakuwa saa moja usiku, nyinyi mkitoka hapa mnaweza kwenda nyumbani kwa mama moja kwa moja, au mkaja hiyo jioni. Sisi tutakuja huko jioni.” “Sawa.” Akakubali mama Penny.

Tunda akamsogelea Mama Penny. “Kumbe ulikuwa unajua kila kitu, halafu ukaniacha mwenzako nalia mchana na usiku!” Mama Penny akaanza kucheka. “Net aliniomba sana nisikwambie, nivumilie. Mimi mwenyewe nilikuwa nikiumia, lakini nilijua mwisho wa yote utacheka tu. Haya hebu jione jinsi ulivyopendeza na hiyo alumasi hapo kidoleni, mdogo wangu! Mvumilivu hula mbivu.” “Lakini mmenitesa sana!” Wakacheka huku wakimuomba msamaha, mwishowe wakaingia ndani.

Net na Tunda walipiga magoti mbele ya kanisa, wakaombewa. Net alitoa neno la shukurani, nakurudia historia yake fupi yeye na Tunda, kisha akaomba aondoke kabla ya ibada haijaisha. “She is not your wife.” Bibi yake akarudia kwa sauti. “I know Nana.” “Just saying!”  Kila mtu alicheka, Net akaenda kumbusu mama yake, na bibi yake akataka kutoka. “Heyyy! What about me!?” Maya alishangaa kuona kaka yake anampita. “Tunda amechoka.” “It doesn’t take even a minute to give sugar to your baby sister!” “Fine!” Net akarudi akabusu mdogo wake. “Happy?” Net akamuuliza mdogo wake. “Oooh yeah!” Net akacheka na kumrudia Tunda aliyekuwa amemuacha amesimama, akamshika mkono. “She is not your wife.” Alisikia bibi yake akirudia tena kumkumbusha kuwa bado si mkewe, wasije wakapitiliza huko waendako. “I said, I know.” Net akamjubu bibi yake kuwa analijua hilo, huku akiondoka na Tunda akiwa amemshika mkono.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Walifika nyumbani kwa Tunda, akiwa anasinzia. Aliingia bafuni, akaoga tena hasa kusafisha uso uliokuwa umechanganyikana machozi na vipodozi.  Akavaa nguo za kulalia kabisa, akatoka pale sebuleni alipokuwa amemuacha Net. “Mbona nguo za kulalia tena!? Tutawaweka sana watu kule kwenye tafrija Tunda! Nilitaka upumzike kidogo tu.” “Utaniamsha muda unaotaka tuondoke. Nimechoka sana Net, nataka nilale vizuri.” “Pole.” Net akamsogelea, akambusu tena bila kumkumbatia ila kumshika tu kichwani ili kuweza kumbusu. Akamuachia.

“Twende nikusindikize.” Akamshika mkono na kuingia naye chumbani kwake, Tunda akiwa na wasiwasi. Alimuogopa sana Net.  “Njoo hapa.” Net akajilaza kitandani, kisha akavuta mto  akaweka chini ya kichwa chake. “Njoo ulale hapa.” Tunda alibaki amesimama, akakunja uso akionyesha wasiwasi na hofu. “Njoo usiogope, Tunda.” “Kifuani kwako!?” Akauliza kwa hofu kidogo. “Hutaki?” “Sio..” Tunda akasita. “Usiogope, njoo. Nataka ulale vizuri. Ni leo tu, hutazoea.” Tunda akacheka. “Nitagoma kuamka mimi!” Tunda akamfanya Net acheke.

“Ndio nabembelezea msamaha, kwa kukutesa kwa siku zote hizo.” Tunda akatabasamu, akapanda kitandani na kujivuta mpaka kifuani kwa Net. “I miss you so much Net.” “Miss you too, babe. Nitaongea na Mchungaji wako, atusaidie tufunge harusi mapema. Nataka tuanze kuishi pamoja.” Tunda akapitisha mikono yake kifuani kwa Net, akamkumbatia kwa nguvu na kupitiwa na usingizi bila ya kujibu kitu. Net aliendelea kumpapasa taratibu maeneo ya mgongoni na begani, huku akimbusu kichwani mpaka na yeye akapotelea usingizini.

 

Tafrija ya kuvalishwa pete ya uchumba Tunda.

Ilikuwa ni kwa mara ya pili Tunda kufika nyumbani kwa mama Cote. Mara ya kwanza alipopelekwa kutubu akiwa mwenye dhambi haswa. Baada ya kukiri alishajihusisha kimapenzi na mchumba wa mama Cote, uadui ukaanza. Sasa anarudi kwenye jumba hilo kama mchumba wa Net. Ilikuwa nyumba yenye thamani za kisasa, tena za aina yake. Nyumba nzuri, iliyojengwa kwa namna yake. Magari yaliyokuwepo hapo nje sehemu yakuegeshea tu magari, Tunda akajua ni watu wenye uwezo watupu watakaokuwepo huko ndani.

“Umependeza sana Tunda.” Tunda akatulia kidogo. “Nini?” “Itakuaje nikifika huko ndani nikakutana na..” Tunda akanyamaza. Net akamuona akifuta machozi huku akiangalia nje ya dirisha. “Naomba uniangalie Tunda.” Tunda akamgeukia. “Naona kama nakuingiza aibu tu Net!” “Naomba usipeleke mawazo yako huko kabisa. Kila mmoja utakayemkuta humo ndani anahistoria yake. Sema ya kwako umeigeuza imekuwa yamsaada.” Net aliendelea kumtuliza akisikika ametulia kabisa, bila hata wazo la pili la wasiwasi.

“Nilifurahi sana jinsi ulivyoweza kuongea na Gab. Umethibitishia kila mtu umeshakomaa Kiroho. Tumia ujasiri huo huo kwa kila atakayekusogelea. Na hakikisha unajitambua acha hofu kabisa. Nipo na wewe nikikujua vizuri, na nimeridhika na wewe. Kwa hiyo tembea mbele ya watu ukiwa huna hofu. Umenisikia?” Tunda akatingisha kichwa kukubali.

“Haya naomba tabasamu. Maana hii yote nimeandaa kwa ajili yako. Nataka ufurahie. Sawa?” Tunda akacheka taratibu. Walikuwa wameegesha gari nje ya hiyo nyumba ya mama yake, sehemu ya kuegesha magari. Net akamvuta karibu na kumbusu tena na tena bila kumuachia kama mwenye kiu naye mpaka simu yake ilipoanza kuita. “Mama huyo!” Net akasema wakati anaiangalia simu yake akaamua kupokea. Alisikiliza kidogo mama Cote akiongea, kisha Net akajibu. “Tupo hapa nje, tunaingia ndani sasa hivi.” Akakata na kumbusu tena Tunda. “Twende, Nana ameanza kusinzia.” Wote wakacheka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Bibi yake Net alimuomba Net,  amvalishe tena ile pete Tunda huku akichukuliwa vizuri video kama kumbukumbu ya familia, akidai kuwa siku hiyo ndipo anapomkabidhi Tunda cheo cha Bi. Cote rasmi kama mrithi wake. Kwanza alivaa pete aliyochumbiwa nayo yeye na pili anaolewa na mjukuu wake mwenye jina kama la mume wake. Alisema anakikundi cha marafiki zake kanisani huko nchini Canada, anafanya nao bible study, walimuomba arikodi kila kitu ili akifika awaonyeshe. Zile zilikuwa habari zilizomtibua mama yake Net, na kumnyima raha kwenye ile shuguli nzima.

Mama Penny alikuwa ameandaa sehemu si ya nje, lakini si sebuleni. Kulikuwa na eneo la ndani lakini kama baraza kubwa tu lililokuwa limezungushiwa kuta nzuri mpaka juu ambako ndiko vyumbani. Chini kwenye hilo eneo la katikati kulikuwa kama na bustani tena ambayo ilishamtoa macho Tunda tangia mara ya kwanza anaingia kwenye hiyo nyumba.

Haikuwa bustani kubwa lakini duara kubwa iliyozungushiwa majani mazuri, yaliyokatwa chini yakawa kama mkeka. Vyungu vya thamani vyenye maua mazuri yaliyokuwa yamezunguka kwenye hayo maua na pembeni ya kona kwenye hilo baraza zima na nguzo, mama Penny alitendea haki. Kuzunguka hilo eneo zima kulikuwa na fremu za picha nzuri sana na aina mbali mbali ya maua. Ndipo mama Penny akapaandaa vizuri na kupendeza.

Yote hiyo alifanya Net kwa ajili ya Tunda. Sasa mpambaji akawa ni mama Penny, nyumbani kwa Ritha, mama yake Net, asiyempenda Tunda. Leo Tunda anavalishwa pete nyumbani kwake akiwa ameonya asikanyage pale tena. Mbaya zaidi, anavalishwa pete ya thamani sana, urithi ambao yule bibi aliuwekea maana kubwa mbele ya watu! Mambo hayo yote wanayafanya nyumbani kwake! Hakuna jinsi mtu angeangalia moyo wa huyo mama ulivyochafuka, akaweza kueleza wengine.

Alikuwepo kanisani na pale kwenye ile tafrija japo ni nyumbani kwake, lakini sababu ya uwepo wa huyo bibi milionea ambaye hata Tunda hakujua uzito wa huyo bibi kuwepo pale. Alisikia akipiga kelele kanisani, akitaniana na Maya na Net. Asijue uwepo wa huyo bibi hapo nchini hata usalama wa taifa nchini Tanzania na Canada, unajua kama yule bibi yupo nchini Tanzania.

Waalikwa ambao Net alimwambia wengine ni wakutoka kanisani kwao na marafiki, wengi pale ni askari kanzu na usalama wa taifa walikuwa wamejaa hapo, kuhakikisha huyo bibi, raia muhimu sana wa huko nchini Canada yupo salama, na hakuna linalotokea, mpaka anarudi nchini kwake salama.

Na hao wazungu wachache aliowaona Tunda pale, hawakuwa ni rafiki wa karibu tu wa Net , ni askari waliopitia mafunzo makubwa sana ya kiaskari ya kimataifa, walifika nchini na huyo bibi kwa ajili ya usalama wake tu. Kwanza alitua nchini na ndege yake ambayo ndio ilibidi kufanyiwa taratibu ya eneo la kutua hapo nchini Tanzania. Kimya kimya bila gazeti lolote kuripoti ujio wa bibi huyo nchini Tanzania.

Mama Cote, au Ritha, alijua ni mapesa ya kiasi gani yamemwaga kwa huyo bibi anayefanya mchezo na kuonekana wa kawaida sana kuwepo hapo. Ritha alipigia mahesabu ya huyo bibi kuwepo tu hapo! Tena kwa ajili ya Tunda, ambaye amempokonya ndoa na mapenzi ya mtoto wake! Anamwita Malaya. Anajua wazi, amemchagua Net badala ya Gab kwa kuwa anamfahamu Net, anataka kunufaika naye. Ritha akajiambia hiyo pesa angefanyia kitu kikubwa sana badala yakupoteza kwa malaya, Tunda.

Kila neno alilotamka bibi Cote, halikuwa bure. Hakuwa mropokoji. Ni mwanamke aliyekuwa akiongea na maraisi na watu wakubwa sana ulimwenguni. Pesa yake na kile anachokifanya nchini Canada, kama mwanaharakati wa mambo ya wanawake si nchini kwao tu, bali ulimwenguni, kilimketisha na wakuu wa ulimwengu huu na kumwingiza sehemu kubwa mbalimbali hapa ulimwenguni. Alishahutubia mara kadhaa kwenye vikao vikubwa vya UNO. Kila aliloongea, watu walilinukuu na kulisikiliza kwa makini sana hata kugeuza ni habari ya kuuza gazeti lolote lile haswa nchini kwao anakofahamika na familia hiyo kufuatiliwa kwa karibu sana.

Ritha alijua na kuzidi kuumia kwa kila neno analozungumza huyo bibi Cote usiku huo kwenye tafrija hiyo. Alijua si mropokaji. Kwa hiyo hata usiku huo hakuna aliloropoka hata moja juu ya Tunda na Net. Inamaana ni maneno au hotuba maalumu aliyokuwa ameiandaa kwa muda mrefu kuja kuzungumza kwenye tafrija ya Net akichumbia. Na lazima hiyo hotuba au hayo maneno anayoongea hapo yamesomwa na kurudiwa na msaidizi wake wakaafikiana na ndipo anatamka mbele ya huo umati kirafiki tu kama akizungumza na familia yake, lakini wazi anajua ni habari nzito nchini kwao siku inayofuata, japo amezungumzia nchini Tanzania. Na akitamka yeye, ndio mwisho.

Ni ukweli ambao hakuna ambaye angesema, Tunda angeamini. Kwa hakika Tunda hakuwa akijua lolote lile juu ya Net mwenyewe wala huyo bibi. Net alikuwa makini sana anapozungumza na Tunda. Na alifanya makusudi akijua umuhimu wa mwanamke atakayemuoa. Sio tu kuitwa mke wa Nathaniel Cote, alijua atabeba majukumu mazito sana. Tunda asijue.

Net hakuwahi kujifungua kwa Tunda zaidi ya idadi ya waliozaliwa nyumbani kwao. Kile anachofanya pale nchini. Kazi za mama yake. Hakuwahi hata kuropoka utajiri mkubwa unaomsubiri nchini Canada. Au anavyosubiriwa kwa hamu huyo mke wa Net, huko nchini Canada. Hata kujulikana jina tu, ingekuwa habari ya kuuza magazeti. Picha yake ndio kabisa. Tunda hana hili wala lile. Anajionea ni bibi amekuja kwenye shuguli ya mjukuu akichumbia. Basi. Kumbe ameingia kwenye historia kubwa sana.

Vyombo vya habari vya nchini kwao na watu wengi walio ijua hiyo familia, na kuifuatilia walitaka angalau kupata fununu kujua hata kwa fununu tu, atakayekuwa mke wa Net. Anaposema video nzuri ichukuliwe Net anapochumbia kwa ajili ya marafiki zake wa kanisani, sio kwa sura hiyo aliyoelewa Tunda hata kidogo. Ni kumbukumbu ya vizazi hadi vizazi na ni habari nzito sana ambayo mtu anaweza hata kuuza kwa pesa nzuri tu za kicanada. Nathaniele Cote amechumbia siku hiyo! Ilikuwa ni habari kubwa yakuuza magazeti nchini kwao.

Lakini Tunda yeye kila kitu aliona kawaida tu, na Net alikusudia iwe hivyo. Hakutaka askari yeyote avae sare na wala pale pasionekane risasi yeyote ile hata ya kiunoni mwao. Kwa hiyo kila mgeni akaonekana wa kawaida. Nadhifu na wengi wamevaa suti. Kumbe suti hizo zimeficha mengi. Tunda na kina mama Penny pamoja na wageni wengine wakawa hawaelewi kinachoendelea. Kumbe hiyo nyumba ilikuwa chini ya ulinzi mkubwa sana tokea huyo bibi anafika pale.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Yakawekwa mazingira mazuri pale. Katikati ya kula na kunywa, watu wakicheka, Net akapiga tena goti akimuuliza Tunda aliyekuwa amesimama, kama atamkubali amuoe, “Will you mary me?”. Tunda akakubali, kwa kusema, “Yes.” Net akamvalisha tena ile pete akiwa amepiga magoti vilevile. Kisha akasimama, akamkumbatia vizuri na kumbusu Tunda.

Haikuwa mara ya kwanza kwa Tunda kupata busu au kukumbatiwa na mwanaume. Baba Tom alishambusu akiwa bado mdogo na mwili huo ulishashikwa na wengi tu. Kimapenzi na kupigwa kama mwizi. Lakini busu la Net na jinsi alivyomgusa huo mwili! Ilikuwa tofauti kabisa. Hakuna aliyeona asitamani. Wenye wivu ndio walizidi kuumia.

Net alijua wapi amshike kabla ya kumbusu, na hata jinsi alivyomwangalia baada ya kumshika kabla ya kumbusu, akili na mawazo ya Tunda alijua wazi anapendwa na kuthaminiwa sana. Ile hofu na aibu mbele ya wateja wake ilimuisha kwani ni kweli walikuwepo wanaume wakutosha tu ambao walikuwa wateja wake, lakini kwa jinsi Net alivyo mtizama na kumshika, hakuna jinsi Tunda ungemkumbusha kuwa alishakuwa changu, ukamuumiza.

 

Mama Cote na Tunda tena.

Wakati watu wakiwa wanaongea na kucheka, huku wakila na kunywa, Mama Penny na mumewe wakaamua kuaga. Muda ulishakwenda. Watoto wanatakiwa shuleni kesho yake. Wakamuaga Net na Tunda. Wao wakaondoka. Kwa kuwa walikuwa wamekaa meza moja na Tunda, walipoondoka, Net naye akasimama, akamwambia Tunda atarudi baada ya muda mfupi. Tunda naye akaamua kuingia ndani kutafuta choo kilipo ili angalau ajitengeneze vizuri na kujirudishia vipodozi na nywele. Kujitengeneza.

Wakati anatoka chooni, mama Cote au Ritha alikuwa akimsubiria mlangoni akiwa amejawa wivu baada ya kuona jinsi mkwewe alivyomthamini Tunda. Na ni kama alitangaza kumpa Tunda cheo kikubwa sana ambacho hakuwahi kupata mtu sahihi wakumpa ila Tunda. Lakini alitangaza kwa kujihami huku akisema, atatangaza rasmi au atamkabidhi rasmi cheo hicho baada ya kupata muda wakutosha wamazungumzo na Tunda.

Tunda alicheka tu kwa kuwa yule bibi aliongea kama kitu cha utani, kumbe ni jambo zito lililokuwa likisubiriwa kwa muda mrefu sana. Wengi walitamani kujua cheo hicho angalau yule bibi anamfikiria kuja kumkabidhi nani! Nani angekuwa mrithi wake! Nani anakalia kiti hicho! Angalau kwa fununu tu. Leo kwa mara ya kwanza, anatangaza, tena nchini Tanzania! Hata Net na Maya walibaki mdomo wazi. Hawakuamini.

Lakini si Tunda ambaye hakujua chochote. Alimuona jinsi Maya na wale wageni wote kutoka Canada wakishtuka mpaka kusimama na kushangilia sana, na Net kubadilika mpaka rangi ya sura akiwa ametoa macho asiamini kile bibi yake anafanya kwa Tunda. Tunda mwenyewe hata asielewe ni nini bibi huyo anaongea. Akajiambia ni mambo tu ya kizungu.

Tunda akawa ndio ametamkwa kwa mara ya kwanza na bibi huyo kuwa ndiye atakalia kitu hicho baada yake. Ritha alijua ni habari itakayoenea sana nchini Canada na picha za Tunda kuanza kuonekana huko na habari zake kufika kwenye nchi mbali mbali za wawakilishi wa umoja wa bibi huyo. Tunda hana habari.

Picha nyingi zilipigwa asijue umuhimu wake. Aliona mpaka rafiki wa Net wakimuomba akae vizuri wampige picha akiwa peke yake tena kwa kupokezana. Akiwa anacheka tu, akakubali kufuata maelekezo. Marafiki hao wakampiga picha akiwa peke yake, kisha wakamuomba mmoja mmoja wapige naye picha. Kwa zamu. Nyingine wakapiga wakiwa na Net. Ikawa shamra shamra imeongezeka gafla baada ya tangazo la bibi huyo, Tunda hana habari.

‘Tunda!’ Ritha aliumia sana. Bibi Cote alitamka kumkabidhi Tunda kiti ambacho inamaana yeye hakustahili! Tena anatamka hayo mbele za watu bila hata kuzungumza na wao kwanza kama familia, wakajua kama amekusudia kuwa ni Tunda! Hata wao watu wa karibu ndio wanasikia pale kama watu tu wa nje! Yule bibi hakumshirikisha yeyote. Yaani pale ndio anatoa hiyo habari kwa mara ya kwanza.

Alihisi ni kama yule mama mkwe wake ametangaza kumtoa kwenye familia kwa wazi tena kwa kumdhalilisha vibaya sana. Ni kama anasema Tunda ni bora kuliko yeye! Alichukia sana kuona anadhalilishwa pale mbele za watu tena nyumbani kwake! Ni Tunda, binti anayejihesabu amempita kwa kila kitu! Leo anapewa heshima yote aliyokuwa amebeba yeye, na kudhani anastahili yeye Ritha! Hasira zilizidi kumpanda na kumchukia Tunda zaidi.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Naomba tusogee hapa pembeni tuzungumze.” Tunda akamfuata nyuma. Akashangaa anamtoa kabisa pale mpaka sehemu ya nje karibu na mlango wa kutokea. Akaangalia kulia na kushoto, wakajikuta wawili tu. Kulikuwa na askari kanzu wawili nje ya huo mlango walionekana kwa kupitia kioo cha mlango. Yule mama akaonekana kuridhika na hiyo faragha.

Akamgeukia Tunda. “Upo hapa leo sababu ya huyu bibi, tu.” Mama Cote akaanza huku amemkazia macho. “Umenielewa Tunda? Unaweza kumdanganya kila mtu hapa, lakini sio mimi. Mimi sio mtoto mdogo au mjinga kama hao wanaume zako uliokuwa ukiwavulia nguo na kuwaloga. Najua janja yako. Upo hapa na kumkataa Gabriel kwa kuwa umejua Net anapesa kuliko Gab. Anamapesa ya urithi wa babu yake na bibi yake akifa ndio kabisa. Yeye ndio anakuwa mrithi au mtawala wa mali zote za Cote.” Tunda akakunja uso. Hayo yote hakuwa hata akiyajua. Na wala hajui kama hiyo familia ya Cote ina mali za hivyo!

“Sijui unamlogea wapi mtoto wangu! Sijui kama na yeye unamfanyia sadaka za makaburini au la! Lakini mimi na wewe tunajua wazi, kwa akili za Net hawezi kukupenda mtu kama wewe hata kidogo. Nina uhakika kuna ulichofanya kwa Net. Wewe ni mzoefu wa ushirikina, hushindwi kuzika akili zake. Na ninajua wazi, yale majini yanayosadikika kukutoka, hayajatoka. Bado yanaharibu akili za wanaume, ndio maana na Net amechanganyikiwa.” Ritha akataka kuendelea.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment