Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Nilipotea! - Sehemu ya 25. - Naomi Simulizi

Nilipotea! - Sehemu ya 25.

 

N

et akacheka kwa kumsikitikia mama yake. “Usidharau hoja zangu Net! Sio watu wote ni waadilifu kama wewe. Watu wanaishi kwa ujanja ujanja sana hapa mjini!” “Binafsi nakuelewa kabisa mama yangu. Nakuelewa. Hapo ulipo sasa hivi, nilishakuwepo. Nikaamua kumchukia kabisa Tunda. Nikaamua kurudi Canada, nikataka kumuoa Chloe, lakini nilishindwa. Sijui Mungu ameniunganishaje na Tunda, mama! Nampenda Tunda. Na ninaona yeye ndiye atakamilisha hata maisha yangu yakumtumikia Mungu.” “Unajuaje kama ni Mungu ndiye anayekuunganisha na Tunda?” Mama Cote akauliza na kumfanya Net akunje uso.

“Sasa wewe unafikiri nini!?” “Watu wanatumia nguvu za giza Net.” Net akasimama. “Unajua nini mama, sina jinsi ya kukubadilisha hapo ulipo na kile unachokiamini. Naamini Mungu kwa wakati wake, atakusaidia na wewe. Maana hata mimi haikuwa kazi ya siku moja.” “Nisikilize Net. Usifanye haraka kuondoka. Uchawi upo, na unafanya kazi.” “Kuliko nguvu za Mungu!?” Net akamuuliza mama yake kwa mshangao, nakubaki akimtizama.

“Uniambie leo, kama tulichokuwa tukikiamini hakina uwezo wa kutulinda na hila na mitego ya shetani! Kwamba shetani amefanikiwa sana, na ana nguvu zidi ya maombi, na uwepo wa Mungu!” “Bibilia imeruhusu kujaribu kila roho. Wewe endelea, na mimi sitatulia mpaka nijue ni roho gani inafanya kazi ndani ya yule binti.”

“Kuwa tu mwangalifu mama yangu. Mungu hajaribiwi. Usije ukafika umbali ambao ukashindwa kurudi kwa mapenzi yako ya umama kwangu. Yapo mambo mengine ya Mungu, huwa hayachunguziki kwa akili za kibinadamu. Huwa hayana majibu. Humpa amtakaye. Muone pale Mungu alipomuweka Tunda. Ulimfukuza kikatili sana. Lakini ona Mungu jinsi alivyomfanikisha hata kifedha.”

“Wapo wapambaji wangapi hapa mjini? Lakini ukiangalia kazi ya Tunda, jinsi alivyojipanga, anavyozungumza na wateja wake! Huwezi kujua ni Tunda ambaye hakusoma. Ana kazi nyingi mpaka nyingine anakataa. Ushajiuliza ni kwa nini yeye, na wapambaji ni wengi? Leo kila mtu analalamika maisha magumu. Kwa nini Tunda anastawi kwenye nchi ya watu wanaolia shida?” Net akauliza.

“Nilishakujibu Net. Shetani anao uwezo. Na yeye pia hufanikisha watu wake.” “Kwa maana nyingine unasema hata kazi anazozifanya, na kufanikiwa pia ni kwa ajili ya ushirikina?” “Huwezi kujua.” “Basi shetani ni mzuri mama. Kama wewe unayemuomba Mungu, umefika hapo ulipo. Ulimtoa Tunda kwenye ofisi yako Arusha, ukaibiwa mpaka kufilisiwa kabisa. Halafu Tunda anayemtumikia shetani amefanikiwa hivyo, kwa nini tunaenda kanisani na sio huko anakokwenda Tunda?”

“Maana yeye anaonekana ana amani kuliko watu wengi sana ninao waona. Au ana marafiki wa ukweli, kuliko watu wengi wanao kuzunguka wewe mama.” “Sio kweli.” Akabisha. “Ni wewe mwenyewe umekuwa ukiwalalamikia kwangu marafiki wanao kuzunguka. Huna rafiki wa kweli mama. Mwangalie Tunda na mama Penny aliyesimama kumlinda Tunda mbele yako! Wewe unaye huyo mtu ambaye anaweza kukukingia kifua pindi watu kama wewe wakisimama mbele yako?” Mama Cote akababaika sana.

“Nimehangaika sana kufika hapa nilipo Net. Siwezi kuruhusu Malaya yeyote yule aje kwenye maisha yetu na kurithi jasho langu. Tunda anajua kuwa wewe unapesa, ndio maana anakuwa kama malaika wa nuru. Atakwambia na kukujenga kwa maneno yanayoendana na vile ulivyo ili aweze kukuaminisha.” Bila kujijua, kwa jazba mama Cote akaanza kufungua alichoficha ndani. Net akabaki akimsikiliza.

“Aliweza kulala na kina Meto, Mati na Gabriel, watu wa maana wa kanisani kwa kutumia uongo unao endana na wao. Alipokuchunguza wewe na kukujua upo hivyo, ndipo akaamua kuja na gia ya kukuokokea. Anajiliza bila kuchoka kwa kuwa nia nikufikia mfuko wako. Na usifikiri wewe utakuwa wa mwisho. Utamuoa na bado atakuwa na wanaume wengine. Siwezi kukubali eti wote tutumbukie kwenye mtego wa kijinga hivyo! Nitakuwa mama wa ajabu sana, kuruhusu uangukie kwa mwanamke kama Tunda.” Mama Cote hasira zilishapanda.

“Mimi nakuonya tu mama. Usipambane na Mungu. Hautashinda. Na utaikumbuka siku ya leo.” “Wewe niache mwenyewe. Una wasiwasi gani? Kama kweli amesimama, tutajua tu. Na wala sitajuta kwa kuwa Mungu ameniruhusu kujaribu kila roho. Na yeye nitamjaribu mpaka niridhike. Kama wewe ulipata muda wa kumuelewa mpaka ukamsamehe  basi tupe na wengine nafasi.” “Sawa mama yangu.” Net akamuhurumia mama yake. Akatamani isingekuwa Tunda ndio anayesimama kati yao.

Hakuwahi kusumbua nyumbani, leo amependa ndio imekuwa tatizo! Alikuwa ni kijana wa ‘ndiyo’ kwa mama yake, kila wakati. Aliacha kazi na maisha mazuri nchini Canada, akaamua kuja kuishi na mama yake ili amsaidie kazi. Alimuhurumia, lakini hakujua kitu chakufanya. Ni Tunda, msichana anayempenda na amekusudia kuwa naye.

“Au hasira hii kali kwa Tunda ni kwa ajili ya Meto!?” Net aliwaza wakati akimtafakari mama yake asielewe ukweli mzima juu ya chuki ya mama yake. Akanyanyua uso akamtizama mama yake. Akamkuta bado akimwangalia. “Unaendeleaje na Meto?” Net akamuuliza mama yake taratibu tu. “Nimeamua kuachana naye kabisa. Japokuwa amekuwa akinitumia jumbe zakuomba msamaha lakini nimeamua kumuacha kabisa. Nimeumia mno. Sina jinsi yakueleza mtu akaelewa. Nimeumia sana. Nimeamua niache kabisa kufikiria swala la ndoa tena.”

          “Sitaweza kuja kumuamini tena maishani. Itanisumbua mno. Nimekuwa naye kanisani, akiniambia na kunionyesha jinsi alivyo muaminifu kumbe anaishi maisha machafu huko nje! Nitakuja kumuamini vipi tena? Naanzia wapi kumuamini tena? Mtu anayekwambia hiki na kuishi vile! Hapana. Nimeamua kuishi tu peke yangu. Naona nimeshapoteza kila mtu sababu ya Tunda. Mimi ndio nimebaki muathirika wa maovu ya huyo Tunda. Naamini Mungu atafanya kwa wakati wake.” Mama Cote akajilalamisha akimtuhumu Tunda.

“Naelewa, unasababu zote za kibibilia zinazokuruhusu kuachana na Meto. Zote kabisa, zinazokuruhusu kutokusamehe kutokana na kosa la uzinzi, lakini pia unasababu zote kabisa za kibibilia zinazokufanya usamehe, mama. Naomba upime kwa manufaa yako si yamwingine. Unataka nini? Kusamehe na kuwa mwenye furaha tena, au kutokumsamehe na kuendelea kuwa mpweke?”

“Nitarudi nyumbani, lakini hivi karibuni nitamuoa Tunda, huwezi jua Mungu atatupa watoto lini! Hutakuwa ukiniona kama hivi. Nitakuwa nikihudumia familia yangu. Nitaumia kukuona unaendelea kuishi mpweke mpaka kifo chako. Samehe kwa ajili yako. Naamini amejifunza na hatarudia. Ona jinsi alivyokubali kutengwa mbele ya kanisa, amevuliwa madaraka pale kanisani, amebaki kuwa mtu wa kawaida tu. Angeondoka kama mwenzake, lakini yeye amekubali kutumikia adhabu yake. Huhisi kuwa amejutia kitendo alichofanya?” Mama Cote akajifuta machozi.

“Ukute na mapenzi ya kweli ndiyo yanambakisha pale kanisani, mama. Anataka uone na uamini kuwa amejutia kitendo alichofanya. Amemwambia Mchungaji ni kitendo alichofanya mara moja, tena baada ya mwenzake kumuunganisha na Tunda na kumwambia amemtafutia binti atakayemsaidia kwa kuwa amekaa muda mrefu bila mke. Anasema hata hakumwingilia Tunda. Ilikuwa kwenye gari tu, tena mara moja. Anajuta sana.”

“Halafu ni mzee mwenye uwezo, huwezi sema anakupenda kwa kuwa unapesa, kama wanaume wengine wanavyokufanyia. Yule mzee haiitaji hata shilingi yako. Nakuomba mama yangu, pata muda ufikirie juu ya hilo.” Net akasimama na kwenda kumzungushia mama yake mikono. Akambusu kichwani. Mama Cote akajivuta chini kidogo na kujiegemeza kwa mwanae. “Is gonna be fine mama.” “Hope so Net. Hope so baby.” Walikaa pale kwa muda, Net akaanza kumchokoza mama yake, na kuanza kucheka. “Kuna mtu aliniambia nisichanganye mambo ya familia na kazi. Sasa hivi ni asubuhi mama, acha nirudi kazini.” Mama Cote akacheka. “Amebarikiwa mwanamke aliyekuzaa.” Net akacheka akambusu tena na kuondoka.

  Mama Cote aanza mikakati yake kwa Tunda. Aanza kumuhusisha na Bethy.

Ni kweli mama Cote alishindwa kuvumilia. Moyo wake ulimkataa kabisa Tunda. Kila alipojitahidi akashindwa. Chuki juu yake ikazidi. Akaona isiwe shida, asije akafa pale ofisini. Akakumbuka Net alimwambia angerudi nyumbani, lakini siku za karibuni atamuoa Tunda. Na wakipata watoto anaweza hata asiwe anamuona. “Siwezi nikamuachia huyu Malaya, atawale mtoto wangu. Ameshanichukulia ndoa, hawezi kunipokonya Net.” Mama Cote akawaza nakuzidi kujipandisha hasira. Akampigia simu Bethy, mke wa Gabriel. Akaomba wakutane kwa chakula cha mchana.

Bila kubisha, kwa kuwa mama Cote alikuwa kama mkwe wake, na wapo karibu, Bethy akakubali. Walipanga wakutane saa sita mchana. Wote walifika bila kuchelewa kwenye mgahawa huo. Wakaagiza vinywaji, wakaanza kuzungumza.

“Unamjua mwanamke aliyekuwa amemchanganya Gabriel wakati ule?” Mama Cote akauliza. “Mpaka akataka kuniacha?” Mke wa Gabriel, Bethy akauliza na kuguna. “Ulishamjua?” “Nilivyokuwa nimechanganyikiwa wakati ule, na Gab alikataa kabisa kumtaja. Aliniambia tatizo haliko kwa huyo mwanamke wa nje, tatizo liko kwangu. Nikaonekana mimi ndio mbaya! Akieleza mabaya yangu kwa kila mtu! Nilichofanya nikukubali kosa ili akose sababu.” “Basi mwanamke huyo huyo, sasa hivi ndiye amemwingia na Net. Net amechanganyikiwa anataka kumuoa.” Bethy alishtuka, mpaka akasimama.

“Ni jini nini huyo dada!?” Bethy akauliza na mshangao mkubwa usoni. “Afadhali wewe unanielewa Bethy. Maana ile hali iliyokuwa imempata Gabriel, ndiyo anayo Net sasa hivi. Kaa chini.” Bethy akarudi kukaa akiwa bado na mshangao mkubwa sana. “Haiwezekani mama! Ipo namna. Net na Gab ni kama ndugu wa damu! Kwa akili za Net, hawezi kumuoa mwanamke aliyelala na Gab. Hata iweje, hawezi. Mimi namjua Net. Ipo tu namna mama Cote.” Hapo akamfurahisha mama Cote.

“Afadhali kama sasa unanielewa wasiwasi wangu ulipo. Maana Net hasikii wala haoni! Yule binti anatafuta wanaume wenye pesa tu. Sasa anaona umeshindwa kwa Gabriel, amehamia kwa Net kwa kuwa sasa hivi anajua Net anapesa nyingi za urithi. Siwezi kukubali yule binti akaolewa na Net. Heri kufa kuliko kumuona anaolewa na Net. Yaani na yeye aje aitwe Cote! Nahisi nitakufa.” Mama Cote akaweka msisitizo akitoa ya moyoni kwa Bethy.

“Hata mimi sikubali! Kwanza alivyonitesa kwenye ndoa yangu! Gabriel alinianika na kunichafua bila aibu wala huruma, kama hanifahamu ili tu kupata sababu ya kuwa naye! Hakika lazima kumuwekea kikomo. Mchafu na mshenzi wa tabia. Amenyimwa aibu kwa kiasi gani!” Hapo wakawa wameshapatana.

“Sasa tutafanyaje?” Mama Cote akauliza. “Nikumfungua macho Net, kwa kuweka wazi mabaya yake yule msichana. Ni rahisi sana mama. Wewe wala usihangaike na Net tena. Mimi namjua Net jinsi alivyo na msimamo. Ukiendelea kumpinga, ndio utampoteza.” “Mara ya pili? Alishahama na nyumba sababu ya kumkatalia kuwa na huyo binti! Kwanza anaitwa Tunda. Wala si binti, Malaya yule.” Mama Cote akavyoza.

“Mama wewe! Net aliyekuwa anasema hana mpango wakuondoka nyumbani, anataka aishi na wewe, leo ameondoka kwa ajili ya huyo Tunda!” “Kwani hamjui kama amehama nyumbani?” “Siku hizi ukaribu na Gab ni kama umepungua. Siwasikii.” “Anaishi kwake, Salasala. Na utengano huo wa Net na Gab, sababu kubwa ni huyo Tunda. Atavuruga kila aina ya mahusiano na kila nyumba!” Mama Cote akazidi kumwaga sumu kupandisha hasira ya Bethy zaidi.

“Mama Cote huyo msichana ana kitu. Sio bure.” “Nimemwambia Net mimi. Hajaniamini. Alimsaidia mwenzie kuokoa ndoa yake. Akaweka sawa akili ya Gabriel, naona amenaswa yeye sasa hivi. Na amembana kweli Net! Anataka kufaidi kwa wote wawili!” “Itabidi kumuweka mwangani haraka.” Wakapandishana morali, wakapanga na mipango yao ya jinsi ya kumuangamiza Tunda na kumuweka mwangani. Zaidi kumtenga na Net. Wakakubaliana vizuri, ndipo wakaachana.

Vita ya Tunda yaanza bila kujijua.

          Akiwa anafurahia penzi jipya. Jumbe za hapa na pale, kutolewa kwa chakula kiwe cha mchana au usiku, Tunda hakuwa na taarifa juu ya mipango mikali dhidi yake. Siku hiyo akiwa ofisini kwake, alikuja kijana na maua mazuri sana ameyashika mkononi na kadi. Aliingia hapo ofisini na kwenda moja kwa moja kwenye meza ya Bety. Akamwambia ametumwa kwa Tunda. Tunda alikuwa akiwasikiliza. Bety akamuelekeza kwa ndani kidogo, ilipo ofisi ya Tunda.

Tunda alikuwa amekodi kama nyumba. Lakini mbele kulikuwa na ofisi, nyuma kulikuwa na vyumba ambavyo ndiko alikokuwa akihifadhia vitu vyake vyote vya kupambia.

Yule kijana akaingia alipokuwa amekaa Tunda. Akamsalimia na kumkabidhi yale maua na kadi. Tunda alimshukuru akiwa amejawa furaha, akijua vinatoka kwa Net. Akatoa ile kadi kutoka kwenye bahasha, juu iliandikwa ‘I am Sorry!’  Tunda akakunja uso. Akaamua afungue ili kujua inatoka kwa nani huyo anayemuomba msamaha!

Moja kwa moja Tunda akasoma chini kujua inatoka wapi. Akakuta imesainiwa na Gabriel. Ilionyeshwa imeandikwa na Gab mwenyewe, akiomba msamaha, na kumtaka waonane baadaye kwa mazungumzo. Tunda alicheka, akamuomba yule kijana aliyetumwa kuleta yale maua na kadi arudi navyo na kumuonya asiwahi kurudi tena pale. Yule kijana akatoka na kila kitu alichoingia nacho. Maua na ile kadi. Alitamani kumwambia Net, lakini akaona itakuwa uchonganishi. Akaamua kunyamaza.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Jioni Net alifika pale ofisini kwa Tunda ili wakapate chakula cha usiku pamoja. Wakiwa hotelini, Net alimuona vile Tunda alivyobadilika. Net akajaribu kuuliza lakini Tunda akamwambia nikuchoka tu. Baada ya chakula cha pamoja, waliagana kila mmoja akarudi kwake.

Akiwa anataka kulala, ujumbe ukaingia. ‘Naomba tuonane kesho saa nne. Nina kitu cha msingi sana nataka kuzungumza na wewe. Gab.’ Alimtajia na eneo la kukutana. Tunda akabaki akiitizama ile simu kwa muda akifikiria chakumjibu Gab, akaamua apuuze.

Kesho yake tena akiwa ofisini, ukaingia tena ujumbe mwingine. ‘Ulipata ujumbe wangu? Nitakuwepo pale nikikusubiri Tunda. Tafadhali usipuuze hata kidogo.’ Tunda alianza kufikiria ni kitu gani hicho cha muhimu Gabriel anataka kuzungumza naye! Swali jingine lililomsumbua ni wapi Gabriel amepata namba yake? Akajiuliza hili na kujishauri lile, bila jibu.

Alibaki akimfikiria Gabriel. Alikuwa muungwana sana kipindi yupo naye. Kwa kifupi ni kama walishakuwa kwenye mahusiano ya karibu tofauti na wateja zake wengine. Gab alitumia muda mwingi na Tunda akimueleza matatizo yake ya ndani sana na kumfariji. Ndiye mteja pekee aliyekuwa akimpigia simu hata usiku sana na Tunda alipokea hata awe amelala na mtu. Alitoka na kwenda kuzungumza naye.

Muda mwingi walipokuwa wakiwa pamoja walitumia ndani kitandani wakizungumza na mapenzi, tofauti na wateja zake wengine ambao ilikuwa ni kazi tu.  Tunda alimfahamu Bethy na watoto wao wawili. Mara nyingi Tunda alikuwa akituma salamu za hao watoto kupitia Gabriel. Bethy alimfahamu kwa mabaya yake aliyokuwa akimfanyia Gabriel. Mbali ya nia yake yakumchomoa pesa, Tunda na Gabriel wakajikuta wanakuwa kama marafiki. Wakiambiana ya ndani sana. Haswa Gabriel ndiye aliyejikuta akimwambia Tunda mambo yake, kwani alisema hana pakusemea.

Alisikia mama Cote akiropoka kwa hasira siku alipomfuata ofisini kwake na kwenda kumtukana, kuwa alitaka kumuacha Bethy kwa ajili yake. Vikafanyika vikao vya nguvu ili kubadili akili yake Gabriel na kumrudisha kwa mkewe. “Kama kweli alinipenda kwa kiasi hicho, ni kwa nini anifukuze vibaya vile?!” Tunda akajiuliza. Akakumbuka jinsi alivyomtishia kumpiga kama hataondoka kwa haraka. Tena akiwa ametoka kulimlilia shida usiku ule wa baridi na mvua, akamkatalia kumsaidia. Tunda akakumbuka hofu iliyokuwa imemkamata usiku ule akiwa hana tumaini jingine tena, hasira zikampanda zaidi. Akaamua kumpuuza. Akaendelea na kazi zake.

Ilipofika saa nne, ujumbe mwingine ukaingia. ‘Naona unasoma kila ujumbe ninao kutumia Tunda. Nimeshafika hapa, nakusubiri. Nitakuwa nje tu, wala hatutajificha.’ Alisoma ule ujumbe. Kule kujua watakuwa nje, hadharani kukamtia moyo Tunda. Akaamua kwenda kumsikiliza ili amalizane naye amuache kwa amani. Ila akakusudia hatampa sikio lake tena kwa matatizo yake. Akanyanyua pochi yake na kutoka akiwa ameshapanga hoja zake.

Gabriel kwa Tunda Tena.

Kweli alimkuta Gab akimsubiria nje ya huo mgahawa. Amekaa peke yake. Akamsalimia baada ya kumsogelea.  “Habari yako Gabriel!” Hakutaka hata kumpa mkono. Gabriel alinyosha mkono, lakini Tunda alivuta kiti na kukaa. “Sina muda mrefu sana. Naomba tuanze mazungumzo.” “Hutaagiza kitu chochote?” “Hapana.” Tunda alimkatalia huku akimtizama machoni ishara yakutaka aanze kuongea.

“Nakupenda Tunda. Nataka kukuoa.” Tunda akacheka kwa kejeli. “Asante na hapana.” Akajibu hivyo tu na kusimama. Akavuta pochi yake na kuanza kuondoka. “Sijamaliza Tunda. Naomba unisikilize.” Tunda akasimama. “Nilikosea sana kukuacha. Lakini Net ndiye aliyenishawishi. Baada ya siku ile nilijuta sana. Sikuwa na furaha tena baada ya kukupoteza wewe. Kila aliyeniona alijua lipo tatizo.” Gab aliongea kwa upendo akibembeleza.

“Maisha yanakosa ladha bila wewe Tunda. Nakupenda na ninakuhitaji. Nimekutafuta sana, mpaka siku ile nilipokuona kwenye kikao cha harusi, yule mwenyekiti ndiye aliyenipa namba yako. Nakupenda Tunda, sitafanya ujinga niliofanya zamani. Nitakutunza, utakuwa wangu tu. Hakuna mwanamke anayenijulia kama wewe.” Tunda alibaki amesimama akimkodolea macho.

“Nakupenda Tunda.” Tunda alikuwa amekunja uso wa mshangao. Gab akamsogelea na kumkumbatia. Tunda akamsukuma. Kilikuwa ni kitendo cha muda mfupi hata Tunda hakujua kama angemkumbatia.

“Kwanza naomba nikusahihishe Gab. Hujawahi kuwa na mahusiano na Tunda, ila Nancy. Pili, sikuwahi kukupenda kama ninavyompenda Net, wewe nilikuwa nikikutumia kama wewe ulivyokuwa ukitumia mwili wangu kama wanaume wengine tu.”

“Sasa hivi anayeishi hapa ni Tunda, aliyesamehewa dhambi na kuishi maisha ya nidhamu mbele za Mungu. Kina Nancy walishatolewa kwenye huu mwili muda mrefu sana. Hawapo na wala hawatakaa wakaishi tena kutumia huu mwili uliotakaswa na kuoshwa na damu ya Yesu. Narudia tena, anayeishi hapa ni Tunda ambaye hujawahi kumfahamu ila Net.” Tunda akaendelea taratibu.

          “Net anamfahamu Tunda wa zamani sana ambaye hata angejiita Nancy, ninauhakika wewe Gabriel usingethubutu hata kumsemesha. Net huyohuyo, anawafahamu na kina Nancy, Fina, Ani, Maria na wengineo wengi tu walioishi kutumia huu mwili wangu. Tena aliwafahamu kwa kuwafumania na huuhuu mwili wangu, kila mmoja kwa wakati wake.”

“Alishanifumania nikiwa Nancy. Nafikiri unakumbuka. Maana tulikuwa wote na wewe ukimtumia Nancy kupitia huuhuu mwili. Haya, alishanifumania nikiwa Maria, na wengine wengi tu Net aliokuwa akiwafumania kupitia huuhuu mwili. Wakiishi vile watakavyo na kujipa majina watakayo wao. Lakini akiwa ananijua mimi kama Tunda ambaye wewe ulimfahamu kwa upande mmoja tu, Nancy.”

“Ninachotaka kukwambia Gab, kwa mabaya yote niliyofanya zamani, na yeye Net kujua kwa kushuhudia na kuambiwa. Tena mengine mabaya, machafu, yasiyoweza kutamkika hata kwa watu na sijawahi kumwambia mtu yeyote hapa duniani, nilikiri mimi mwenyewe kwake Net. Nikiwa nimefika mwisho. Wewe na wenzako waliokuwa wakitumia huu mwili kwa majina tofauti tofauti, mliponitelekeza. Nafikiri unakumbuka jinsi ulivyonifukuza kinyama kana kwamba tulikuwa maadui wakati nilikupa sikio langu hata saa sita za usiku. Nilikusikiliza Gab na kukufariji bila kuchoka. Sasa siku ile uliponifukuza kikatili huku ukitishia kunipiga nikiwa nakulilia shida Gab. Mvua na baridi ya Arusha ikinipiga. Tena nikiwa nimekwambia wazi, sina pakwenda usiku ule. Net alinipokea vilevile.”

“Net alihakikisha ananitoa kwenye kila kifungo kilichokuwa kinanishikilia bila kuchoka kwani haikuwa rahisi wala kazi ya siku moja. Ndani ya muda huo, nimemdhalilisha Net, ninauhakika wewe usingeweza Gab. Ziko siku nilizotaka kubebwa juujuu, nikiwa na Net na wanaume waliokuwa wakiutumia huu mwili wangu. Net alinipigania na kunitoa mikononi mwa wale wanaume wawili waliokuwa wakining’ang’ania usiku ule. Ziko sehemu nilizopita naye Net, ambazo wahudumu walinitambua mimi kama mwanamke wako, wakikuulizia wewe. Lakini Net alibaki na mimi akinivumilia.”

“Haikuwa rahisi hata kidogo kwa Net. Mimi mwenyewe nilikuwa najiuliza anawezaje! Aibu na fedheha niliyokuwa nikimtia. Lakini Net alisimama na mimi. Akanisaidia kuanzia pale uliponiacha wewe, nikiwa na kina Nancy na wengine wengi ndani yangu, mpaka msalabani ambako niliwekwa huru. Amenifundisha kuomba na amenijenga kiakili. Naishi kama msomi sasa hivi, nakuingiza pesa kwa kazi ninayofanya, kwa shule fupi aliyonipa Net nikiwa naye Arusha.”

“Alianza na mimi chini sana kwa elimu yangu ndogo ambayo ninauhakika nisingeweza kuajiriwa popote kwani hata kazi aliyoniachia nayo nilifukuzwa kwa kuwa sikuwa na vyeti japo niliimudu kazi vizuri tu. Net akiwa amenifundisha. Alinielimisha na kunijenga mchana na usiku bila kuchoka ndio maana sasa hivi ninaketi na wakuu sababu ya Net.”

“Na huo ndio nahesabu kuwa ni upendo. Upendo na jinsi anavyonithamini Net, hata ungenipa miaka kumi nifikirie kama nastahili hivyo, nisingekuja na jibu ya jinsi alivyo Net kwangu. Hakuna mwanadamu amewahi kuwa karibu na mimi, isipokuwa ananufaika na mimi kwa namna moja au nyingine, wewe ni shahidi. Ulikuwa karibu na mimi ulipokuwa unamatatizo na Bethy. Ulikuwa kama umechanganyikiwa kwangu Gab. Sijui kama unakumbuka! Mlipopatana na Bethy, hukuniaga kwa heshima Gab. Ulinifukuza vibaya sana. Kwa kuwa ulikuwa umeshamaliza matumizi yako kwenye huu mwili kama wanaume wengine, lakini si Net.”

“Sihitaji kutuzwa na yeyote kama ulivyosema mwanzo kuwa unataka kunioa na kunitunza. Nancy aliyekulilia shida wakati ule ukamfukuza, aliondoka na shida zake zote. Huyu Tunda anaridhika na pesa anayoingiza kwa jasho lake na mapenzi ya Net, basi. Nakushauri na wewe uanze kuridhika na mkeo. Ulifanya kosa sana kukubali kuwa na mahusiano na Nancy.”

“Wakati ule ulitakiwa unisaidie, kwa kuwa kwanza wewe ulishapata neema ya kushinda dhambi. Ulikuwa na uwezo wa kuishi maisha matakatifu, lakini ukakubali kunitumia mimi niliyekuwa nimefungwa na nguvu za giza! Nilikuwa na majini yaliyokuwa yakinitesa, Gab. Sikuwa nalala vizuri kwa hofu nikitumikishwa kwa hili au lile, mchana na usiku. Ulitakiwa unisaidie kunitoa kwenye ile hali kama Net alivyofanya.” Tunda akaanza kutokwa na machozi.

          “Lakini ukiwa na uelewa kabisa wa baya na jema, ulitumia mwili wangu kama wanaume wengine wasiomjua Mungu! Nimepata msaada Gabriel. Nimesamehewa dhambi. Huko kwenye hayo maisha sitakaa nikarudi tena. Nilitumikishwa na ibilisi mchana na usiku. Mungu amenifungua, nipo huru. Nimeanza biashara yangu kwa jasho langu bila kuhongwa, na sasa hivi ninafurahia maisha.” Tunda akafuta machozi.

“Naelewa unamatatizo na mkeo, lakini Gabriel, hakuna kinachomshinda Mungu. Mgeukie Mungu. Kuhangaika na wanawake hakutakusaidia, wote tunamadhaifu yetu, yanatofautiana majina tu. Rudi kwa mkeo, anza upya. Naomba uniache na usirudie tena kunitafuta, lasivyo nitamwambia Net.” Gab alikuwa amesimama amepigwa na butwaa kama sanamu. Tunda akageuka nakuondoka bila hata kugeuka nyuma. Alimuacha Gab akiwa amesimama palepale, akaingia kwenye gari yake akiwa na hasira sana, akarudi kazini kwake.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Net alimpigia simu baada ya muda kumtaka watoke kwa chakula cha mchana, lakini kwa kuwa hakuwa sawa kutokana na yale mazungumzo, akaona wasikutane. “Net yupo makini sana. Akiniona tu, atajua kuna kinachoendelea. Tokea jana ameanza kunitilia mashaka.”  Tunda akawaza. Akaona ampe sababu ya kiuungwana. Akamwambia ana kazi nyingi zakufanya siku hiyo, labda wakutane kesho yake.

“Mbona kama haupo sawa? Kwema?” Alitamani kumwambia Net, lakini akasita. Hakutaka kugeuka kuwa mchonganishi. “Tunda! Vipi?” “Kwema kabisa, ninashuguli nyingi tu. Naomba tuongee baadaye.” Akaamua kumuaga kwa haraka. Dhamira ilimsuta, kila kitu kwenye mwili wake kilimshawishi kumshirikisha Net juu ya Gab, lakini akasita.

“Hata hivyo hatarudia tena. Gabriel ni mstaarabu sana.’ Tunda akajipa moyo lakini bado hakuwa kwenye hali nzuri kabisa. Akili ilikuwa imevurugika kabisa. Siku nzima alishindwa kula kwa hofu yakuonana na Gab bila kumwambia Net. Historia ya maisha aliyoishi nyuma ya kupanga wanaume wengi kwa wakati mmoja ilimsumbua sana Tunda, akijua wazi Net anamjua alivyo mtaalamu kwenye hilo. “Sasa akija kujua kuwa nilikutana na Gab bila kumtaarifu, tena tukiwa tumezungumza asubuhi hiyohiyo, atajua narudia yale maisha ya kina Nancy.” Wasiwasi ulizidi kumtesa Tunda. Akaona afunike dhambi ya kwanza, yakuonana na Gab bila kumtaaribu Net.

Hata jioni ile aliamua kumkwepa kabisa Net. “Naomba nikuone kesho Net.” “Kuna nini? Mbona kama nahisi unanikwepa!?” “Hapana.” “Naomba kama kuna kitu chochote kile uniambie Tunda.” “Hamna Net. Kesho tutaenda kumuona baba?” Akaamua kubadili kabisa mazungumzo. “Mmefikia wapi na yule wakili mpya?” “Anaonekana atatusaidia. Japo wanadai pesa nyingi kidogo.” “Unataka msaada?” Net akauliza wakiwa bado wanazungumza kwenye simu.

“Hapana Net. Asante sana. Nitaweza tu.” “Ukikwama, usiache kuniambia.” “Nitafanya hivyo, japo..” Tunda akasita. “Nini?” “Natakiwa kulipa kodi ya mwaka mzima pale ninapoishi, na hapa ofisini pia wamenipandishia kodi!” “Wanataka kiasi gani?” Net akauliza. “Kuna kazi mbili kubwa nimepata mwezi huu na nyingine ndogo ndogo, naamini mpaka mwishoni mwa mwezi nitakuwa nimekamilisha pesa yote. Nakwambia hivi kwa kuwa nitakuwa na shuguli nyingi sana huu mwezi, ili kujaribu kukusanya hiyo pesa. Kwa hiyo usipokuwa ukiniona mara kwa mara ujue ni kwa muda tu.”

“Naelewa. Ila siku za jumamosi nitakuwa nikija kukusaidia. Si unajua siendi kazini?” “Kweli Net?” “Kabisa. Hata kukusogezea maua, si itakuwa msaada pia?” “Uwepo wako tu ni msaada tosha. Nitafurahi sana, lakini nakuwa na kazi nyingi hata muda wa kula huwa nakosa.” “Usijali. Kwa hiyo umekataa kuniambia kinachokusumbua sasa hivi?” Tunda akasita japo alijua Net sio mtu wakumpotezea. Hasahau jambo. Lakini akajiambia ni heri nusu shari, kuliko shari kamili. Akakusudia asimwambie. “Hamna kitu cha kukwambia Net. Kesho tutaonana. Usiku mwema.” “Asante na wewe.” Tunda akakata simu lakini akiumia sana moyoni.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alirudi nyumbani kwake akiwa amechoka zaidi mawazo. “Huu ujinga sitakuja kufanya tena.” Akajiambia. “Siku nyingine ni heri tu nimwambie mapema. Nimejawa hofu sina amani!” Tunda akaendelea kuwaza. Akaingia kuoga na kupanda kitandani bila hata kula. Kwa kuwa alishaagana na Net, alimpigia simu Mama Penny akaongea na watoto kidogo, wakaagana.

Kosa La Siri Laleta Balaa & Aibu!

Akazima sauti kabisa kwenye simu zake zote mbili na kujiweka vizuri kitandani. Akatulia akijaribu kulala lakini dhamira ilikuwa ikimsuta haswa na kushindwa kulala. Ni Net aliyemlipia gharama yote hiyo! “Nani ameniloga Tunda mimi!? Hivi ni kwa nini hata nilikwenda kuonana na huyo Gab! Heri ningemshirikisha kwanza Net, akanishauri au nikamsikia anasemaje juu ya hili. Net ananithamini sana, nawezaje kumsaliti. Hii ni tabia ambayo lazima niiache.”  Wakati anaendelea kuwaza, akaona taa ya simu yake inawaka. Jumbe nyingi za picha zikiingia kwenye hiyo simu yake ambayo ni ya watu wa karibu tu ndio wana namba hiyo.

Akavuta ile simu yake ili afungue aone ni picha gani. Kwa kuwa ilikuwa ni simu ile isiyo ya biashara, akahisi labda mama Penny anamtumia picha fulani za mapambo ili aone. Maana ni tabia yao, kutafuta picha za kumbi mbali mbali zilizopambwa vizuri mtandaoni na kurushiana ili kuiga.

Alikaribia kufa kwa mshtuko. Zilikuwa ni picha zake na Gabriel, walipokuwa wamekaa pale mgahawani na nyingine Gab amemkumbatia. Halafu mbaya zaidi, mtumaji alikuwa Nathaniel Cote. Bila kufikiria au kujijua Tunda akaitupa ile simu mbali akaruka pale kitandani. Uchovu wote ulimwisha, akabaki amejishika moyo wake. ‘Mungu wangu nisaidie. Mungu niokoe. Uwii jamani!’ Tunda akaanza kulia. ‘Ni mkosi gani huu!?’ 

Baada ya kulia kwa muda, akaona kulia haitasaidia. Ni heri amtafute tu Net ajieleze. Kwani Net alituma picha tu bila ujumbe wowote.

Tunda akaokota simu yake kwa haraka nakuanza kumpigia Net. Lakini iliita bila kupokelewa. Alipiga zaidi ya mara kumi bila majibu. Akaamua kutuma ujumbe. ‘Net, haipo kama inavyoonekana kwenye hizo picha. Tafadhali pokea simu nikuelezee ilivyokuwa.’ ‘Nilifikiri hakuna cha kuniambia Tunda! Naomba nilale. Mimi nitakutafuta.’ ‘Lini?’ Tunda akauliza kwa ujumbe. Kimya.

Akasubiri jibu kwa muda, alipoona hajibiwi akaamua kutuma tena ujumbe mwingine. ‘Lini utanitafuta Net?’ ‘Nitakapokuwa tayari.’ ‘Sawa Net. Lakini sijafanya kitu kibaya. Mungu wangu nishahidi mpenzi.’ Hakupata jibu lolote. Hakuna usiku uliokuwa mrefu kama huo.

 ~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Tunda aliamka na kubaki akiangalia simu yake akisubiri labda Net atapiga. Lakini hakuona kitu. Hapakuwa na simu wala jumbe za mapenzi asubuhi hiyo. Akasubiri na kusubiri, kimya kwenye hiyo simu. Siku hiyo hata mama Penny hakumpigia. Ila simu ya kikazi ikaanza kuita mfululizo. Akakumbuka uhitaji wa pesa alio nao, akaamua kwenda kazini.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alikwenda kazini, siku nzima macho yalikuwa kwenye simu yake. Alibeba simu zake mpaka chooni, bafuni kila mahali, lakini hapakuwa na ujumbe wowote. Usiku alikaa kitandani bila kulala akisubiri simu kutoka kwa Net lakini Net hakukosea hata kupiga. Tunda akaamua kutuma ujumbe. ‘Pole na kazi Net.’ Kimya. Akatuma ujumbe mwingine. ‘Bado nasubiri simu yako Net.’ Kimya. Tunda akaamua kulala na simu zake zote sauti mpaka mwisho.

Ikawa asubuhi ikawa jioni, siku tatu mfululizo bila kusikia chochote kutoka kwa Net. Tunda alikuwa halali vizuri kwa mawazo. Alilia na kujibembeleza. Alijuta sana kutokumshirikisha Net juu ya Gabriel.  ‘Net hawezi kuniamini tena, atajua nimerudia tabia zile mbaya.’ Tunda alikuwa akiwaza huku akilia.

Akaamua kumtumia ujumbe mwingine tena. ‘Net mpenzi wangu naomba katika yote usifikirie kuniacha. Utaniua. Nina hali mbaya, nakaribia kuchanganyikiwa. Tafadhali nipigie.’  Kimya.

 Kanisani nako moto.

Kanisani nako habari zilishafikishwa na Jaz msichana aliyekuwa akifanya kazi ofisini kwa Tunda na kushuhudia mama Cote akiongea mazito ya Tunda kwa kuumia. Walio na uwezo waliendelea kupeleleza zaidi, kama vile ilivyo kawaida habari mbaya huenea kwa haraka sana. Walioweza kuongeza ubaya ili kunogesha ubaya wa Tunda waliongeza. Ilimradi tu.

Tunda alipoenda katikati ya juma kwenye vipindi vya kanisani kama kawaida yake, hakuihitaji kuuliza. Ule uangaliwaji wake, alijua tu walishafikishiwa habari. Kila aliposogelea kundi, walipomuona walinyamaza. Alipoamua kukaa, walinyanyuka mmoja baada ya mwingine. Akajikuta anabakia na wawili au watatu.

Kikafika kipindi cha maswali wakati wa bible study siku hiyo ya jumatano. Mmoja wa wanawake ambaye aliheshimiana sana na Tunda, akanyoosha mkono. Mchungaji akamchagua aulize swali. Swali lake ndilo lililomchosha Tunda, akaamua anyanyuke na kuondoka kabisa. “Nina swali Mchungaji. Lakini litakuwa nje kidogo na ulichofundisha leo.” Akasimama. “Karibu.” Mchungaji alijibu huku akimtizama.

“Naelewa kuwa watu wanapookoka wanasamehewa dhambi. Lakini kama ni mtu ameanzisha biashara kwa pesa za umalaya na yeye bado anajiita ameokoka, na yupo kanisani, anaabudu pamoja nasi, huku akijua kabisa anaishi kwa pesa za dhambi. Je ni sawa?” Alipoweka tu kituo, mwenzake akadakia. “Maana humu makanisani kumejaa kondoo na mbwa mwitu.” Mwengine akadakia. “Tujihadhari jamani, chachu ndongo huchachua donge zima! Tuna vijana wetu wadogo humu ndani.” Mwingine akaongeza kwa hekima tu. Ikaibuka minong’ono, ndipo Tunda akanyanyuka nakuondoka. Siku hiyo Mama Penny hakuwepo. Alirudi nyumbani kwake kama mgonjwa. Akapanda kitandani na kuanza kulia kwa uchungu wakupitiliza, kama aliyefiwa. 

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Tunda hakujua chakufanya tena. Alishindwa hata kumwambia mama Penny kwa hofu. “Mama Penny na yeye hawezi kunielewa! Atajiuliza niliwezaje kwenda kuonana na Gab bila hata kumwambia hata yeye, kama Net nilishindwa! Watajua bado naishi yale maisha kwa siri. Mungu nitetee!” Tunda akaendelea kulia na kujutia.

Alijimbia endapo wale watu wakijua tena hata Net alimuacha kwa ajili ya kwenda kuonana na mwanaume mwingine ambaye alikuwa na mahusiano naye zamani, tena alikwenda kwa siri, ingekuwa mbaya zaidi! Hofu ilizidi kumwingia Tunda.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Je, Lipi JEMA kwa Tunda? Yale maisha na ujanja ujanja aliyokuwa akiishi kama kina Nancy akililiwa na kina Gab mpaka sasa, hata Arusha aliacha wafanyabiashara wakubwa tu wakipishana ofisini kwa Cote, wakimtongoza AU hivi alivyookoka anashindwa kuaminika na kupokelewa kwenye jamii? Tena wakitumia vibaya siri zake alizokiri kanisani, ili kupata ukombozi!?

Kwenye penzi la Net ambalo hata hakuwahi kufikiria kama anaweza kuja kustahili kupendwa kwa kiasi hicho, AMELIKOROGA YEYE MWENYEWE. Na hata Net akimrudia, amekutana na kipingamizi kikubwa, mama Cote anayemfahamu ndani na nje kama tapeli la mapenzi, anamwita ‘Malaya’. Amesimama kama Mlima akiapa Tunda hatakaa kuwa mrithi pamoja naye, yeye aliyehangaika kuanzia chini. Na ameanza kukusanya majeshi yake. Ameshampata Bethy ambaye naye amempandisha hasira na amekusudia kumlipa Tunda kisasi kwa fedheha aliyomsababishia. Kwa ufupi vita ya Tunda ndio imeanza rasmi.

 Sasa bora lipi?

v Vile alivyoacha ukahaba akakimbilia kanisani na siri alizozitoa madhabahuni kwa Mungu akikiri makosa, ndizo zinazomwangamiza sasa au

v Vile alivyokuwa amepagawa na mapepo, akitumiwa mwili wake lakini heshima na pesa ilikuwepo? Alikosa soko kwa muda tu. Lakini Tunda huyu wa sasa hivi anatakiwa mpaka na Gabriel na ameacha wanaume wakimpigania jijini Arusha.

 

1.    Nani ametuma zile picha?

2.   Itakuaje kwa Net?

3.   Umbali gani mama Cote na Bethy watakwenda kumuangamiza kabisa Tunda.

4.   Bethy atafanyaje akijua nia ya mumewe ya kurudiana tena na Tunda?

5.   Gabriel atafanyaje baada ya kujua mwanamke aliyetaka kumuoa tena akiwa tayari kuacha kila kitu, Net kama ndugu wa karibu akamkataza, ndiye na yeye Net anaye?

6.   Tunda ataamua lipi juu ya maisha yake, Net akiwa ameota mbawa? KIMYA. Mama Penny hawezi kumshirikisha tena kwa chochote ili amshauri, kwa kosa la kwenda kukutana na Gab kwa siri?

7.   Nani atasimama na Tunda huyu tena? Aliyekiri kuokoka, lakini kashfa ya kukutana kwa siri na Gabriel, mwanaume aliyekuwa naye kwenye ukahaba zamani, inamkabili?

 

Kanisani moto, kazini moto, aliowaibia waume zao nao moto! Itakuaje?

 

Yooooooote, na ya kusisimua, yanapatikana mbeleni. Vita ya kiroho na ya kimwili kwa Tunda inaanza rasmi. Tena akiwa na adui wasomi, wanaakili ya kufikiria/kupanga na wanayo pesa. {Mama Cote & Bethy}.

 

Usikose Mazito ya nilipotea.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment