Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Nilipotea! - Sehemu ya 23. - Naomi Simulizi

Nilipotea! - Sehemu ya 23.

 

N

et akamjibu mama yake kwa utulivu tu, “Ndiye huyo huyo Tunda, mama.” Mama Cote  aliduwaa kwa muda kama haamini. “Umechanganyikiwa!?” “Hapana mama. Kwa nini?” “Umekosa nini hapa duniani mpaka ukajiingize kwa kahaba yule!? Unaficha wapi sura yako!?” “Tunda ametubu mama. Mungu amemsamehe, na wewe ulisema umemsamehe. Sasa nini tena?” “Una nini wewe Net!? Kwani kusamehewa kwa Tunda kunaondoa uchafu aliofanya!? Unaoa mwanamke ambaye kila mwanaume hapa mjini anamjua ndani na nje!? Una shida gani!? Unataka na wewe uonje wenzako walichopewa?” “Naona unaanza kunitukana mama. Tunda anakuwa mke wangu simchezei kama watu wengine. Nampenda Tunda.”

“Unampenda sasa hivi baada ya watu wote kumkinahi huyo msichana!?” “Nampenda Tunda. Hata babu anajua.” “Sasa babu yako hayupo hapa. Mimi ndiye nipo. Nimesema huyo kahaba hatakaa akakanyaga humu ndani, na wala hutamuoa. Amekosa soko kwa wanaume wote wa hapa Tanzania ndio anakufuata wewe! Haitakaa itokee Net. Labda kama mimi sio mama yako.” “Najua ni habari mpya kwako mama. Unahitaji muda wa kuzitafakari. Tunda ndiye mwanamke atakayekuwa mke wangu. Naomba upate muda wa kutafakari na kukubali. Kwa kuwa hilo linatokea. Tena ninataka kumuoa haraka sana.”

“Na kwambia Net, labda kama mimi siye niliyekubeba tumboni miezi tisa. Hutamuoa Tunda. Labda usubiri nife kwanza, ndipo umuoe huyo Malaya, lakini sio sasa.” “Naona unahitaji muda mama. Na mimi nipo tayari kukupisha. Nahamia nyumbani kwangu ili kukupa nafasi.” “Yaani unaniacha mimi hapa peke yangu sababu ya Tunda!?” “Umesema hutaki kumuona Tunda anakanyaga nyumbani kwako. Na mimi nimekuhakikishia nilazima nitamuoa Tunda. Sasa unafikiri itakuaje? Nakupa nafasi ya kutafakari, utakapokuwa tayari kumpokea Tunda, unajua pakunipata mama yangu.”

“Kweli Net!?” “Nimeamua mama. Lazima nitamuoa Tunda. Unajua ninavyokupenda na kukuheshimu. Lakini katika hili huna nafasi hata kidogo. Ni eitha ukubali uungane nami katika kukamilisha furaha yangu, au utajumuika nasi hiyo siku utakapo kuwa tayari. Haina haraka. Naelewa kuwa unahitaji muda, chukua muda wowote unaotaka hapa duniani. Lakini ujue jinsi unavyochelewa ndivyo utakavyopitwa na hatua muhimu sana kwenye maisha yangu, na ningetamani uwepo kushuhudia. Maana nitaoa mara moja tu maishani, na nitamuoa Tunda.” Net akaingia ndani na kuanza kufungasha vitu vyake huku akiviweka kwenye gari lake, usiku uleule.

          Alipomaliza, akamsogelea mama yake, akambusu. “Nampenda sana Tunda, mama yangu. Na nimaamuzi niliyoyofanya kwa muda mrefu sana, sijakurupuka. Nimempokea vile alivyo. Nakuombea Mungu na wewe uweze kumsamehe kabisa na umpokee. Maana ndiye atakayekuwa mke wangu.” Net akaondoka nakumuacha yule mama haamini kama Tunda amefanikiwa kumchukulia wanaume wawili, aliobakiwa nao hapa duniani, ambao aliwapenda na wenyewe walimuonyesha mapenzi na heshima zote.

Jumatatu!

Tunda aliamshwa na ujumbe mzuri kutoka kwa Net. ‘Naweza kukupigia?’ Tunda akamtumia huo ujumbe. Baada ya sekunde chache simu yake ikaanza kuita. “Uliamka salama?” “Ndiyo. Asante kwa ujumbe mzuri.” “Karibu. Mchana utakuwa na ratiba gani?” “Nitakuwepo tu ofisini.” “Naweza kuja kukuchukua tukale wote chakula cha mchana?” Tunda alifurahi sana. Akacheka.

“Unacheka nini sasa?” “Bado siamini! Nina furaha ya ajabu ambayo siwezi nikaeleza mtu akaelewa! Sikuwahi kufikiria kama naweza kuja kupendwa.” “Nakupenda mpaka nakuonea wivu.” Net akajibu na kumfanya Tunda azidi kucheka. “Nina mahali nakwenda asubuhi hii, sina uhakika nitamaliza saa ngapi, lakini nikitoka tu nitakuja kukuchukua tukale wote. Ila ukiona nachelewa, uende tu, nitakutoa jioni.” “As a date?” “Yes Ma’am!” Tunda akazidi kucheka.

“Kwani siwezi kupata vyote?” Tunda akauliza kwa deko. “Wewe tu na ratiba yako. Ukiwa tayari tutaenda kula wote chakula cha mchana na nitakutoa usiku.” “Basi nakusubiri mpaka utoke.” “Sawa.” “Usisahau kupata kifungua kinywa, Net.” “Nitachelewa. Sitaki kuwapa sababu ya kuninyima hiyo tenda.” “Pole. Nakuombea ufanikiwe.” “Asante.” Wakaagana, lakini Tunda akabaki kitandani akiendelea kurudia rudia ujumbe aliotumiwa na Net.

‘Hakuna usiku niliolala vizuri kama usiku wa siku ya kuamkia leo. Nikijua wewe ni wangu na utakuwa wangu daima. Asante kwa kunikubali Tunda. Nakupenda na ninaahidi kukupenda na kukulinda daima.

Net.’

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Tunda aliingia kuoga na kujitengeneza vizuri kama kawaida yake, akijiandaa kutoka na Net kwa chakula cha mchana. Alijizungusha kwenye kioo kwa muda mrefu sana. Alibadilisha muundo wa alivyoweka nywele, akabadilisha nguo zaidi ya mara tatu, rangi ya kucha. Kila kitu hakuridhika nacho.

Simu yake ikaanza kuita. “Huu sio wakati wakunipigia kabisa, mama Penny. Nimechanganyikiwa.” “Kinacho kuchanganya nini?” “Sina nguo kabisa.” “Umegawa zote!?” “Hapana bwana. Net anataka tutoke naye kwa chakula cha mchana na usiku atanitoa pia.” “Kumbe na wewe unachanganywa na vitu vya kijinga kama hivyo!? Hebu vaa utoke hapo kwenye kioo.” “Ulijuaje kama nipo kwenye kioo?” Tunda akaanza kucheka.

“Hapa jasho linanitoka!” “Acha ujinga Tunda. Wewe ni mzuri tu. Na chochote unachovaa kinakupendeza.” “Kweli dada?” “Sikudanganyi. Unavutia kwa kila nguo unayoweka mwilini mwako.        Sijawahi       kukuona     umechukiza. Si ningeshakwambia?” “Kweli wewe ungeshaniambia.” Wote wakacheka.

“Nagawa watoto mwenzio.” “Nipe Penny.” “Huyo ukimtaka hata sasa hivi nenda kamchukue hukohuko shuleni.” “Kafanyaje tena msimamizi wangu wa harusi?” “Si Julius kapita hapa nyumbani asubuhi hii, kuna mambo alikuwa anaongea na Mchungaji, kawakuta mezani wanakunywa chai ili waende shule. Acha aanze kumcheka Julius. Eti anamwambia, ‘Mwenzako auntie Tunda anaolewa na Mzungu!’ Nusu nikae chini.”

“Mungu wangu, Penny jamani!” “Ungemuonea huruma Julius jinsi alivyoshtuka na kumgeukia Mchungaji kumuuliza.” “Uwii! Nilitaka kuja kuzungumza naye mwenyewe.” Tunda alikaa chini. “Sikutaka aje asikie kutoka kwa mtu mwingine jamani! Julius ali..” Tunda akasita.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alikumbuka jinsi Julius alivyomweleza kuwa anampenda. Alitangaza kwa kila mtu pale kanisani kuwa Tunda ndiye atakuwa mkewe. Kanisa zima walijua mwisho wao itakuwa ndoa tu. Julius alikuwa kijana aliyetulia sana na mcha Mungu, kitu kilichokuwa kikimuogopesha sana Tunda. Ni kijana aliyekuwa na maadili mazuri, hakutofautiana sana na Net.

Wakati wote hakuwa akielewa hivi mtu unawezaje kumkosea Mungu kwa uzinzi! Mara kadhaa kwenye maongezi yake na Tunda, alimuonyesha kushangazwa na watu wanaokuwa na mahusiano ya kimapenzi kama si nje ya ndoa basi kabla ya ndoa. Tunda alimuona ni mwanaume mzuri, mwenye juhudi, lakini alijua hawezi kuja kumfaa hata kidogo. Alijua atashtuka sana akija kujua historia yake.

Hakumjibu moja kwa moja hapana, lakini alimwambia wapeane muda wakufahamiana zaidi. Kila Tunda alipokuwa akitaka kumweleza ukweli juu ya historia yake ya maisha, alishindwa kutokana na mwelekeo wa mazungumzo ya Julius. Familia yake, ndugu zake, jinsi walivyokuzwa na jinsi anavyoelewa misingi ya familia inavyotakiwa kuwa. Utaratibu wa wazazi wake kutaka kufahamiana vizuri na wazazi wa kila mkwe anayeletwa nyumbani kutambulishwa kwao kabla ya ndoa. Huo ulikuwa mtihani mkubwa sana kwa Tunda.

Ukizingatia baba yake yupo jela kwa kosa la wizi na mama yake ndiye hataki hata kumuona Tunda kwa kosa la kulala na mumewe. Mama yake alimchafua Tunda kupita kiasi. Alijua pindi ukweni watakapotaka kukutana na wazazi wake, haitawezekana kabisa kueleza ukweli juu ya wazazi wake. Kwa hiyo aliendelea kumzungusha Julius ili siku aje amwambie ukweli au yeye mwenyewe aje ajue historia yake na kuamua kuachana naye kabisa.

Uzuri wa Julius hakuwa na makuu. Kila kitu alimshirikisha Mchungaji wake, hata kukutana na Tunda walikutana nyumbani kwa Mchungaji, au ofisini au sehemu ya hadharani kwenye macho ya washirika wengine. Kwa hiyo hata hakuwa akimwambia Tunda maneno yeyote yale ya kimapenzi, kwa hiyo hata Tunda hakuwa na hisia zozote zile za kimapenzi juu yake kama Net aliyekuja kwa muda mfupi. Akaeleza nia yake yakutaka awe mkewe. Kama tu Julius. Lakini Net yeye akambusu, kamkumbatia na kumfariji katika hofu yake.

Kwa siku moja tu, Net akawa ameshampita mbali sana Julius aliyekuwa na Tunda hapo kanisani wakati wote na kutangaza kuwa Tunda ni mkewe. Japokuwa alikuwa amesoma na kazi nzuri, lakini bado alikuwa na misingi mikali ile ya zamani kabisa ya wokovu. Alifuata sheria zote za maadili ya kanisani. Hakuwahi kuwa na faragha na Tunda.

Jumbe alizokuwa akimtumia Tunda kila siku ni neno la Mungu, asubuhi na usiku muda wa kulala. Akijitahidi sana atamtumia nyimbo za dini. Lakini alimsifia kila alipomuona kuwa umependeza sana na kumkumbatia, tena wakiwepo watu. Basi. Alikuwa kaka mtaratibu sana. Tunda hakutaka kumuumiza hata kidogo alitaka kuja kujitoa taratibu akimtafutia sababu.

Sasa akaja Net. Anayemjua ndani na nje. Net anaonyesha uozo wa Tunda unathamani kwa kusaidia wengine. Kaka wakizungu. Mzuri. Akapata faragha. Kayasema yote. Kamuweka Tunda mikononi na busu! Ahadi ya kuwa naye daima, ipo. Net amekiri hajakurupuka. Alikuwa akimfuatilia na kumpenda tokea ni kahaba.

Net amemsindikiza Tunda mpaka kwa baba yake gerezani. Akaonyesha heshima yote kwa baba yake Tunda. Akamtamkia kuwa naye katika kila hatua yake hapo jela. Net anamfahamu Tunda na uozo wake wote. Huwezi kumlinganisha na Julius hata kidogo. Julius anamfahamu Tunda nadhifu ambaye anasubiri kwa wakati muafaka, atakuja kupelekwa kwa wazazi wa Tunda ambao anadhani nao wapo na hali kama wazazi wake. Kwa hakika Tunda alijua Julius hawezi kuja kuwa mumewe, lakini pia hakutaka kumuumiza.  Julius alikuwa mtaratibu na muungwana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“We Tunda?” “Nipo. Namuwaza mchumba Juli.” “Pole mwaya. Utafanyaje?” “Itabidi nimtafute na kwa mara ya kwanza nimwambie ukweli.” “Utakuwa umefanya vizuri. Nitakupitia ofisini kwako. Nina safari ya huko.” “Umempikia kitafunio gani mchungaji?” “Sitaki kuombwa.” “Mimi na wewe mama Penny!” “Nishakufungashia. Nitakupitishia. Usijali.” “Ndio maana nakupenda.” “Acha kuniibia. Na utoke hapo kwenye kioo, uende kazini.” Tunda akacheka na kukata simu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Tunda alifika ofisini, akakuta wafanyakazi wake walishafika. Alijawa furaha hata wao waligundua hilo. Walianza kutaniana, baada ya muda kidogo zikaanza simu za wateja na wengine wakaanza kuingia mle ofisini wakitaka kuonana na Tunda kwa ushauri na kuona picha za kazi alizokwisha fanya. Wengine walikuwa wakiangalia picha, wengine wakiongea nao huku wakiuliza maswali. Pakawa na shuguli nyingi tu asubuhi hiyo.

Mama Cote kwa Tunda.

Wakiwa kila mmoja akihudumia wateja wake, Mama Cote akaingia pale ofisini kwao. Tunda alipomuona aliwaomba wateja aliokuwa akizungumza nao, wamsubiri kidogo, akamsogelea Mama Cote. “Shikamoo Mama.” “Umenivunjia uchumba wangu. Sasa hivi ningekuwa nimeshaolewa na mimi. Isingekuwa mama yako kukutoa mimba, ungekuwa umezaa na baba yako. Ushajiuliza umevunja ndoa ngapi mpaka sasa hivi? Umeshajiuliza ni maafa kiasi gani umesababisha kwenye jamii?” Tunda alikuwa kwenye mshtuko, akabaki ameduaa.

“Au umeshajiuliza ni majeraha kiasi gani umesababisha kwenye maisha ya watu? Kana kwamba haitoshi umeingia kwenye maisha ya Net!  Kijana mdogo asiye na hatia. Na yeye unataka kumuongeza kwenye idadi ya wanaume utakao kuwa umewavulia nguo hapa duniani! Wameshafika wangapi? Eti Tunda?” Wateja wote walibaki wakimsikiliza yule mama huku wakimwangalia Tunda.

“Unataka kulala na baba na mtoto wake!? Yule mchumba wangu mimi ni kama baba yake Net. Umelala naye, halafu sasa hivi umemgeukia mwanae! Huna kinyaa!? Basi kama hilo hulijali, umelipuuza, basi kumbuka mahusiano uliyokuwa na kaka yake, Gabriel! Umemchanganya Gab karibia amuache mkewe kwa ajili yako, mpaka watu tukafunga na kuomba ndio Gab akashtuka na kukujua kama wewe ni shetani.” Tunda kimya.

“Jamani wewe binti! Wewe ni mchafu wa kiasi gani? Umenyimwa aibu  na huruma kabisa! Umeingia mpaka kwenye nyumba ya Mungu! Umeangusha wazee wakanisa. Gab alikuwa kijana ambaye ametulia kwenye ndoa yake, mcha Mungu, lakini umefanikiwa kumuangusha dhambini yule kijana!”

“Naomba umuhurumie Net, tafadhali. Amejitunza mwanangu maishani mwake kote. Leo unataka kumuharibia mwanangu maisha! Na ninajua wazi, umeokoka kwa ajili yake. Umeokoka ili umpate mwanangu. Tunda muogope Mungu wewe mtoto! Hata kama huna dhamira, lakini nataka kukwambia Mungu yupo na anakuona kwa unalotaka kumfanyia Net. Nakuapia kweli kabisa Tunda, Mungu atakuadhibu kwa ukatili na unyama unaotaka kumfanyia mtoto wangu. Hajafaidi maisha hata kidogo, leo unataka kuja kumuua na UKIMWI!”


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment