S |
iku inayofuata, Tunda akiwa
ukumbini anapamba, mida ya saa mbili asubuhi, mmoja wa wafanyakazi wake, Jazi,
alimpigia simu kumwambia ametoka kuzungumza na simu ya wateja wake wa siku
iliyopita, wakina Mgeekwa, wanamuomba wakutane tena jioni yake, walishafikia
uamuzi. Jazi alikuwa ameandika kila kitu chini, muda na mahali. Tunda akamtaka
huyo huyo Jazi ndio aende kumuwakilisha muda huo utakapofika. Siku za jumamosi
usingeweza kumuweka Tunda kwenye kikao chochote. Anakuwa busy kupita kiasi.
Ilipofika
jioni Jazi alitoka kwenda kumuwakilisha Tunda kule kwa wale wanakamati
alipokuwepo Net na Gabriel. Jazi alitoka pale akiwa amejiandaa kwenda
kukamilisha oda, lakini alipofika pale walimkataa kabisa. “Tunda yupo na
majukumu mengine. Chochote mtakachoniambia mimi, kitamfikia na yeye.” “Hapana.
Kamwambie Tunda aje yeye mwenyewe. Na sisi pia ni wateja. Tunataka huduma yake.
Kwani ni bure? Na sisi tutamlipa.” “Siku za jumamosi inakuwa ngumu sana kumpata
Tunda jamani! Naomba mniamini kuwa, mkiniona mimi, ndio mmemuona Tunda.” “Bwana
wee! Sisi tunamtaka Tunda. Wewe nenda zako.” Wote wakamshambulia Jazi kwa
maneno wakimtaka Tunda, mwishowe Jazi akaondoka.
Alimpigia
simu Tunda akiwa analia kuwa amedhalilika sana. “Usichukie Jazi, ndio
changamoto za kazi hizo.” “Wamenifukuza, kama..” “Kwanza
ujue wengi wao pale ni walevi. Wala usiumie. Umenielewa Jazi? Nitawapigia simu
baadaye kuzungumza nao. Wewe rudi nyumbani ukapumzike. Pole sana.” Siku ya
jumamosi ilikuwa siku ambayo Tunda anakuwa na kazi mbili au tatu. Sasa jumamosi
hiyo alikuwa akipamba kumbi tatu, tena zote kubwa. Tangia saa 9 usiku au
alfajiri, Tunda alishafika kazini kwenye ukumbi wa kwanza.
Alichokuwa
akifanya ili kumaliza kwa wakati, kila ukumbi alitanguliza vijana wake waanze
kupamba kisha yeye alipita kumalizia. Hakuwa akipokea simu ya mtu yeyote
isipokuwa wafanyakazi wake na mama Penny, basi. Ile simu ambayo namba alikuwa
akiwapa wateja, alikuwa hata hagusi siku hizo za jumamosi. Kwanza hakuwa akitoa
kwenye pochi mpaka akimaliza kazi, ndipo ataitoa tena kwa ajili ya kumpigia
simu muhusika, afike hapo, amkabidhi huo ukumbi, basi.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Siku
hiyo alishinda kwenye kazi mpaka ilipofika usiku ndipo aliporudi nyumbani
kwake. Siku hiyo hakuwa hata na hamu ya chakula. Aliingia kuoga akatoka na
kujitupia kitandani kwake. Ni kweli alikuwa akitengeneza pesa, lakini
alihitajika nidhamu ya hali ya juu kwenye kazi hiyo. Kwa kuwa alikuwa akichukua
kazi nyingi, ilibidi kufanya kazi kwa bidii ili kuhakikisha hakuna anapokosea,
na hakuna anayemuudhi. Iwe wanaolipia pesa nyingi au wale wenye kutaka
kupambiwa kwa kawaida tu, kote alihakikisha anaridhisha wateja wake. Na mara
nyingi siku za jumamosi ndio alikuwa na kazi nyingi sana kuliko siku nyingine
zote.
Akiwa
anakaribia kupitiwa na usingizi, akasikia mlio wa sauti wa simu yake kuashiria
ujumbe umeingia. Alijichukia kwa kutokuzima ile simu kabisa. Bila kutaka
kuwasha taa, alinyoosha mkono kwenye meza ndogo pembeni ya kitanda chake, ili
kuivuta simu yake na kuizima kabisa, ili apumzike.
Wakati
anataka kuizima kabisa ile simu, akaonelea aone ule ujumbe ambao kwanza umeingia
muda ule, ukawa umemtoa kwenye usingizi. Alitaka kusoma kesho yake lakini
akaona amjue huyo msumbufu wake. “Anataka nini usiku huu jamani!” Tunda
akajiuliza kwa hasira. Akasoma. ‘Najua una mambo mengi
Tunda, lakini naomba utafute muda tuzungumze. Net.’ Tunda aliruka pale
kitandani, akakaa. Akaamua kujibu. ‘Tunaweza kuongea
wakati wowote.’ ‘Lakini leo hukupokea simu zangu kabisa, Tunda!’ ‘Samahani Net,
sikujua kama ni wewe. Siku za jumamosi nakuwa na kazi nyingi sana. Kama simu
siifahamu huwa sipokei. Sasa hivi ndio narudi nyumbani. Nimechoka kweli, hapa
nipo kitandani.’ ‘Pole.’ ‘Asante.’ Tunda akajibu, kisha akatulia.
‘Lini sasa unaweza kuwa na nafasi?’ Net akatuma ujumbe
mwingine. ‘Naweza kukupigia sasa hivi?’ Tunda
akauliza. Mara akaona simu yake ikiita. “Net!” “Vipi?”
“Safi tu. Nimeona ni heri tuongee tu kwa simu.” “Hutaki kuniona tena!?”
“Hapana. Sio hivyo Net.” “Hivi unakumbuka uliniacha sehemu ya kuegesha magari?”
Tunda akafunga macho na kuvuta kumbukumbu.
“Lakini nilikuaga Net.” “Unakumbuka mimi kukuaga?” “Hapana. Naomba
unisamehe. Nimekuwa na mambo mengi kweli! Yananivuruga akili.” “Nini tena?”
“Nahangaika kumtoa baba jela, anaumwa. Natamani atoke mapema ili akatibiwe.”
“Umepata wakili mzuri?” Net akauliza kuonyesha kujali.
“Nafikiri hivyo. Sijui. Ndiyo yupo anahangaikia kufufa hiyo kesi.
Ila baba amedhoofu sana, Net. Anatakiwa kutoka jela mapema ili awahi matibabu.
Kesho nataka niende nikamuone tena.” “Pole sana. Tunaweza kwenda wote
kumtizama?” “Twende wote jela!?” Tunda akauliza kwa mshangao.
“Si ndipo alipo?” Net akauliza kiustarabu tu. “Ndiyo. Bado yupo jela.” Akajibu kwa upole. “Basi tutaenda wote.” “Asante Net.” “Unaabudu kanisa gani?”
Tunda akamuelekeza na kumwambia ni muda gani wanaanza ibada. “Basi nitakuja kanisani kwenu kukutembelea.” “Nitafurahi
kukuona Net. Karibu.” “Asante. Basi ngoja nikuache upumzike, nitakuona kesho.”
“Asante, usiku mwema.” “Na wewe pia.” Waliagana, Tunda akabaki akijiuliza maswali
mawili matatu, mwishowe akaonelea alale tu.
Jumapili.
Net Kanisani kwa Kina Tunda.
Siku
hiyo ya jumapili, alimkuta Net ameshafika kanisani akimsubiri nje ya gari yake.
Tunda akaegesha gari yake pembeni ya alipokuwa amegesha Net gari yake. Kama
kawaida yake hakujikosea. Alikuwa amependeza haswa. Alishuka akiwa ameshikilia
pochi yake na bibilia yake mkononi. Akamsalimia Net huku akijaribu kuweka vitu
vingine kama simu yake ya mkononi na funguo za gari ndani ya pochi yake.
“Karibu sana, hapa ndipo Mungu alinipa familia
nyingine. Ni watu wazuri sana. Utamfurahia Mchungaji wetu na mkewe. Wamefanya
hapa kanisani kukawa kimbilio la wengi. Wanahimiza sana vijana kufanya kazi kwa
bidii. Mkewe ndiye mwenye kipaji cha kugundua vipaji vya watu na kuviendeleza.
Yeye ndiye amenisukuma kwenye hii kazi ninayofanya, tena nikiwa na hofu nyingi
kweli.” “Auntie Tunda!” Watoto wa Mchungaji walimkimbilia Tunda. Penny na mdogo
wake Pendo.
“Dady ametufukuza ofisini kwake.” Tunda akacheka.
“Huu ni muda wenu wa Sunday School. Muwahi msichelewe.” “Huyo ni mzungu?” Mmoja
wao ambaye Tunda alimlaumu sana mama yake kuwa alimuharibu mwanae kwa vituko,
Penny alimnong’oneza hilo swali Tunda lakini aliweza kusikika. “Na anasikia
Kiswahili.” Tunda akamjibu, wote wakacheka.
“Umekamatwa leo na maswali yako yasiyoisha we
Penny!” Mdogo wake alimwambia ndugu yake huku akimcheka. “Shikamoo. Naitwa
Penny, kipenzi cha dady.” Penny akamwambia Net. Net alikuwa akicheka tu.
“Muongo, mimi ndiye kipenzi cha dad and by the way, dady yetu ndiye bosi hapa.”
Net akazidi kucheka.
“Nilikwambia hili kanisa lina vituko! Sasa bado
hujakutana na wazazi wao. Ndio utachoka zaidi. Haya naomba muende Sunday
school.” Tunda aliwashika vichwa na kuwageuza, kama kuwaelekezea upande
lilipokuwepo darasa lao kwa kuwasukuma kidogo.
“Hata hatujamjua mgeni wakizungu sababu yako!”
Walimsikia mdogo wake Penny akimlaumu Penny. “Ni mchumba wa auntie Tunda?”
Pendo akamuuliza Penny, “Wewe! Akikusikia anko Juli, atakupiga makwenzi. Anko
Juli ndio mchumba wa auntie Tunda.” “Muongo.” “Kweli.” “Muongo.” “Kweli tena. Nilimsikia
mama akimwambia dady.” Waliwasikia wale watoto wakibishana huku wakielekea
darasani kwao. Walijawa fujo na kelele kupita kiasi. Tunda alibaki akitingisha
kichwa huku akicheka.
“Shalom!” Tunda na Net walishtuliwa na sauti
iliyokuwa ikiwasalimia, maana akili zao zilikuwa zimezama kwenye mazungumzo ya
wale watoto. Wote wakageuka. “Amina Juli. Shalom!” Tunda akajibu. Juli
akamsogelea na kumkumbatia Tunda huku akimtizama kwa tabasamu. “Umependeza sana
Tunda.” Tunda akacheka kidogo. “Usingenisifia ningeshangaa!” Wote wawili
wakacheka.
“Ni kweli bwana. Au hutaki nikupe sifa zako?”
“Hapana, nashukuru. Juli! Huyu anaitwa Net, Net huyu anaitwa Julius au Juli
kama wengi tulivyozoea kumwita.” Walipeana mikono. “Net ndiye mtu aliyenitoa
duniani nakunileta kanisani.” Tunda akaongeza huo utambulisho mfupi tu. “Tunashukuru
bwana kwa kutuletea kondoo. Maana kuna vifaa vingine muhimu sana kanisani, ndio
kina Tunda.” Juli aliongeza huku akicheka. Juli na Tunda walitaniana kidogo
mbele ya Net, waliposikia nyimbo zimeanza kusikika kanisani, Tunda akamwambia
Net waingie kanisani, ibada imeanza.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Tunda
alikaa na Net mpaka mwisho wa ibada, ndipo walipotoka na kwenda kusalimiana na
Mchungaji na mkewe ofisini. “Wote nilisha waambia juu ya Net. Nafikiri
mnakumbuka.” Tunda akaongea kwa hakika akijua lazima Mchungaji na mkewe
watakuwa wakimkumbuka tu Net. Wakabaki wametoa macho. “Jamani nyinyi! Net!?
Pale kanisani alijitambulisha kama Nathaniel Cote, lakini kwa kifupi ni Net.
Net yule niliyewaambia habari zake!” Tunda akashangaa wanawezaje kumsahau Net!
“Tunakumbuka
sana. Lakini sikumbuki kama ulituambia kama ni mzungu!” Mama Penny akajibu na
kumgeukia mumewe. “Au wewe baba Paroko unataarifa hizo?” “Hata kidogo.” Tunda
na Net wakaanza kucheka.
“Unaposimulia
jambo, usiwe unaondoa mambo ya muhimu.” “Sasa swala la uzungu wa Net ungeongeza
nini kwenye ushuhuda wangu?” “Usitutanie kabisa wewe Tunda! Kuna uzito wake
mkubwa sana. Wewe kutolewa jalalani na Mzungu na kuketishwa na wakubwa kama
sisi, sio kitu kidogo!” “Mama Penny wewe! ” Tunda alibaki akimshangaa.
“Kabisa!”
Kama kawaida ya mumewe kuunga mkono kila kitu anachoongea mkewe. Net alikuwa
akicheka tu. “Kwanza ujue Net anasikia na kuongea Kiswahili fasaha kama mtu
aliyezaliwa Tanzania. Yaani hata hapa anawasikia kila kitu.” Wakatulia kidogo.
“Eti ni kweli?” Mama Penny akauliza huku akimwangalia Net ambaye yeye alikuwa
akicheka muda wote. “Sasa unafikiri ile salamu ya pale kanisani alikariri?”
Mama Penny akamtizama Net na mumewe. “Tunajua sana kama anajua kiswahili.”
Mumewe akasaidia, wote wakacheka.
“Jamani
nimefurahi kuona Tunda yupo na watu wanao mjali.” Ikabidi Net azungumze tu.
“Sisi tumefurahi kukufahamu na kuja kututembelea Net. Hatujawahi kupata rafiki
wa kizungu tangia tuanze hii huduma.” “Jamani Mama Penny wewe!” Tunda akazidi
kushangaa. “Naongea moyo wangu. Kwa nini nisiseme ukweli?” “Mimi ndio kabisaaa,
sijawahi kuwa na rafiki mzungu tokea nizaliwe.” Mchungaji akaongeza. Wote
wakacheka.
“Net,
tuondoke zetu.” Tunda akasimama. “Lazima twende naye nyumbani akale.” “Nina
haraka mama Penny!” Tunda alitaka kukataa. “Haituhusu sisi. Ulimleta mwenyewe.
Kama unaharaka ndio mtangulie nyumbani, sisi tutawakuta huko huko. Huwezi
kumleta mgeni halafu ukaishia naye ofisini.” Mama Mchungaji akajibu.
“Atakuja nyumbani siku nyingine.” “Mbona hilo tunalifahamu? Na tutahakikisha lazima aje nyumbani siku nyingine. Leo haiwezi ikawa mwisho wake wakufika nyumbani kwetu” Tunda akatingisha kichwa, huku akiguna. Alijua jinsi mama Penny alivyo king’ang’anizi. “Twende Net mwaya.” “Ukajisikie nyumbani Net. Sisi tuko nyuma yenu tunakuja. Ngoja nikusanye vifaranga vyangu vyote. Tunakuja sasa hivi.” “Asante sana.” Net akashukuru wakatoka.
Tunda
na Net kwenye gari.
Wote wakajikuta
wakianza kucheka tena mara ya kutoka hapo ofisini. “Huwa wanakuwa serious
hawa?” Net akauliza. “Heri Mchungaji kidogo huwa anajitahidi, lakini huyo
mkewe! Sijawahi kumuona. Lakini
anaupendo sana. Hana roho ya wivu hata kidogo, anapenda kila mtu afanikiwe.”
Waliongozana mpaka kwenye magari yao.
“Unataka
tuendeshe magari mawili kama tupo kwenye msafara bwana! Njoo upande kwenye gari
yangu, tutakuja kuchukua gari yako baadaye.” Tunda akacheka, akaona ni wazo
zuri. Akaingia kwenye gari ya Net. Alipokaa tu, Net akamvuta mkono wake
wakushoto akaangalia vidole vyake. “Mbona Juli hajaweka pete bado!?” Tunda akatulia
kidogo kama anayefikiria.
“Hatujafika
huko.” Tunda akajibu baada yakumuona Net akimtizama. “Mmefikia wapi? Maana
naona mpaka mnakumbatiana.” “Nisalamu tu, Net jamani!” “Salamu yenu nyinyi
wawili tu!? Mnasalimiana kwa kukumbatiana?” Tunda akatulia tena kama
anayefikiria kwa kuvuta kumbukumbu. “Eti Tunda?” Net akauliza tena na kuwasha
gari kisha akaondoa gari pale kanisani.
“Watu
wengi huwa wanasalimiana pale kanisani kwa kukumbatiana.” “Oooh! Basi inabidi
nirudi tena. Maana leo sikubahatika kukumbatiwa kabisa, na wala sikubahatika
kuona watu wengine walio kumbatiana. Hata Juli mwenyewe hakunikumbatia na mimi
ila wewe tu wakati tulikuwa tumesimama wote.” Tunda akanyamaza.
“Kwa
hiyo sasa hivi mpo kwenye hatua gani ya mahusiano?” “Hatujafika popote.”
“Anatambulika mpaka kwa viongozi wako kama ni mchumba wako, bado hamjafika
popote!?” “Alinigusia tu nia yake yakutaka kunioa.” Tunda akaongea tu hivyo na kunyamaza,
Net akamgeukia kama kumwambia aendelee, anamsikiliza.
“Ndio na
mimi nikamwambia mama Mchungaji, au tuseme mama Penny. Yeye ndio kama rafiki
yangu au mshauri wangu, nafikiri watoto walimsikia wakati akimwambia mumewe.
Lakini hamna mwendelezo wowote.” “Unamaanisha nini?” “Tuliishia hapo hapo tu,
Net!” “Mbona sikuelewi Tunda? Mtu alikufuata kukueleza nia ya kutaka kukuoa.
Halafu unaniambia mliishia hapo hapo! Inamaana mmeishia hapo hapo kama
wachumba, au kama mke na mume au?” “Net
jamani! Nilishindwa kitu chakumjibu.” Net akamgeukia huku amekunja uso.
“Huyu
kaka anamtaka Tunda asiyemfahamu hata kidogo. Nilijua anataka kujiingiza kwa
mtu asiyemfahamu kabisa. Anamuona Tunda aliyesimama pale, lakini hamjui Tunda
wa kweli na maisha niliyoishi nyuma. Najua wazi Mungu amenisamehe, lakini hapa
duniani mambo yote niliyofanya bado yapo kwenye akili na miayo ya watu, Net.”
“Mama
yangu mpaka leo sina mahusiano naye kwa kosa la kutembea na mumewe na wanawake
wengine wengi ambao nimevunja ndoa zao au nimeathiri ndoa zao kwa namna moja au
nyingine. Ndugu zangu wenyewe hawaniamini hata na marafiki zao wakiume! Hebu
niambie Net, huyu Julius siku moja akitaka kuja kukutana na familia yangu
nampeleka wapi?” Tunda akauliza kwa upole.
“Wewe
ulikaa na ndugu zangu kwa muda mfupi sana, lakini waliweza kukwambia mabaya
yangu yote. Japo mengine ni ya uongo, lakini yanasababishwa na chuki waliyonayo
juu yangu kwa yale niliyo watendea. Naogopa hata kufikiria swala la mahusiano
na mtu yeyote yule, kuhofia kuja kunilazimu kueleza historia yangu ya aibu au
chafu kama vile! Sitaki nije nianze kupenda, halafu nikaumizwa kwa maisha
niliyoishi zamani.”
“Ni
ngumu kuja kuishi na mwanaume halafu akaja kukuamini kwa asilimia zote kama
ambavyo angemuheshimu mwanamke aliyeanza naye mahusiano ya kimapenzi. Namaanisha
labda msichana aliyemkuta bikra. Kwangu itakuwa ngumu Net. Nilishaharibu sana
maisha yangu.”
“Nikichelewa
kurudi nyumbani, atahisi nimetoka kwa mwanaume mwingine. Nikichelewa kupokea
simu yake, au niongea na simu na mwanaume yeyote asiye mfahamu yeye, au hata
nikiwa na mahusiano ya kawaida tu na mwanaume mwingine, huyo mume au mchumba wangu
atahisi vinginevyo. Kuja kuwa na mahusiano kwa upande wangu ni kukubali kuingia
kwenye maisha yatakayoninyima uhuru, furaha, na naona nitakuwa najiingiza
kwenye matatizo tu.”
“Nimeamua
niishi hivihivi, hata hivyo nimeshakinahiwa, halafu ninahofu yakuja kuingia
kwenye ndoa nikashindwa kuzaa. Nitateseka sana.” “Kwa nini?” Net akauliza.
“Mama
aliponitoa ile mimba, sijui walinitoaje! Sijui kama haikuathiri kizazi changu
au la. Sitaki kuingia kwenye ndoa, nikiwa na wasiwasi huu.” “Kwani hukuwahi
kushika mimba tena?” Net akauliza huku akimtizama Tunda. Tunda akainama.
“Ni Baba
Tom tu, ndiye mwanaume pekee niliye lala naye bila kondom. Alikuwa hataki hata
kusikia neno kondom. Ila baada yakutoka pale, au baada ya pale kila mwanaume niliyewahi kulala naye, hata Sadiki
nilihakikisha natumia kondom kila wakati. Sikuwahi au sikurudi tena kutotumia
kondom. Hata hivyo wengi nilihakikisha nawamaliza nguvu zakutoweza kuniingilia.
Niliishia kuwa..” Tunda akanyamaza. Akageukia dirishani, nakuanza kufuta
machozi.
“Nisikilize
Tunda. Hayo nimaisha uliyoishi zamani. Ulishakiri, Mungu amekusamehe. Hutakiwi
kuendelea kuumia kwa ajili ya hayo. Huko umeshatoka, na umeamua kutokurudi
tena. Naomba utafute jinsi yakutumia hayo maisha kuwa msaada kwa wengine.
Nilazima ubadilishe kutoka kuwa aibu na kuwa msaada kwa mtu mwingine. Ukikubali
kuwa ni kwa ajili yako tu, na ukakubali ikutese, kweli itakuwa shida ulizopitia
ni bure kabisa. Umenisikia?” Tunda
alikuwa akiendelea kulia.
Net akamvuta
mkono wake aliokuwa akijifuta machozi akaubusu kiganjani. Ilikuwa ni mara ya
kwanza Net kumbusu Tunda. Mwili mzima wa Tunda ulisisimka. Hakuwahi kujisikia
vile tokea anazaliwa. Eti mtu kumbembeleza akiwa mkosaji! Kwanza huo mwili
wengi waliugusa ili kujinufaisha nao. Wakike kwa wakiume. Sasa leo anapokea
busu la faraja! Ilikuwa faraja ya pekee kwake. Tunda hakuamini kupata busu
kutoka kwa Net anayemfahamu akiwa mchafu vile! Hata hivyo ni Net jamani!
“Huna
haja yakulia kabisa Tunda. Lazima tugeuze yale maisha yako kuwa msaada kwa
wengine.” “Nitafanyaje?” Tunda akauliza huku
akifuta machozi, hata yeye hakuwa anaelewa alipitaje kule kote. Aliwezaje!?
Hapo alipotulia ndipo picha ya kila kitu alichofanya nyuma ikaanza kumjia.
Wakati mwingine aliweza kuhudumia wanaume hata watatu kwa siku moja!
Kinyaa,
shida na mateso yote aliweza kuyapuuza akawa akifanya kama mchezo mwepesi sana.
‘Niliwezaje!?’ Ni swali alilokuwa akijiuliza kila wakati Tunda bila
kupata jibu. Achilia mbali kujidhalilisha alikopitia bila kufanikiwa. Ilikuwa
ni kama chombo cha thamani sana, kinachostahili kutumiwa kuwekea chakula hata
cha wafalme, halafu chombo hicho hicho umpe mtoto mdogo, asiyejua thamani yake,
achee nje kwenye matope.
“Kwa kuwa habari mbaya zinazagaa kwa haraka,” Net
akaendelea. “lazima wewe mwenyewe uwe msemaji wa habari zako. Geuza kuwa msaada
kwa mabinti na vijana. Huwezi kujua hata wazazi wengine wanaweza kupona.” “Kweli Net!?” “Kabisa. Acha watu wakufahamu kwa
yale maisha ya zamani, na waone kazi kubwa Mungu aliyofanya ndani yako. Hakuna
mwanadamu ambaye angeweza kukutoa ulipokuwa Tunda, isipokuwa Yesu mwenyewe.
Ulikuwa umefungwa na nguvu za giza tokea mtoto unaishi na baba Tom. Ufahamu
wako ulitekwa, ulikuwa ukitumikia falme nyingine kabisa. Kwa nini usitumie kile
ulichofanyiwa na Mungu kufungua wengine?” Net akaendelea taratibu.
“Wapo wengi wanapitia ulipopita wewe, lakini
wanakosa msaada. Ona jinsi ulivyofanikiwa kwenye maisha kwa kukubali kutumia
kipaji Mungu alichokupa tena bila shule ya maana. Lazima kutumia maisha yako
yaliyopita kwa ushindi. Yale shetani aliyokuwa amekusudia kuwa mabaya kwako,
Mungu amekugeuzia kuwa mema. Sasa kwa nini unalia tena? Lazima ufurahie kama
mshindi na si uliyeshindwa. Eti Tunda?” Machozi ya Tunda yalikauka gafla, akajawa
tabasamu kubwa usoni mwake.
“Nilimiss hayo macho na hilo tabasamu!” Tunda akajifunika
uso wake na kucheka kwa sauti. Net akaendelea kumfariji, huku akiendesha mpaka
Tunda akafunguka kabisa. “Unajua Net, Mungu anakutumia sana katika maisha
yangu? Kila wakati huwa unanitoa sehemu moja na kunipeleka sehemu ya juu!
Isingekuwa wewe unajua sasa hivi nisingekuwa hapa?” “Ndio nakushangaa sasa
unavyokuwa unanikimbia kila wakati!” Tunda akacheka.
“Sijakukimbia bwana!” “Unanipuuza sana Tunda!
Hunichukulii maanani hata kidogo.” “Jamani Net!” “Kweli Tunda. Hebu niambie ni
juhudi gani umefanya kunitafuta tokea ulipoondoka Arusha?” Tunda akabaki kimya.
“Inawezekana Arusha ni mbali sana. Lakini
tulikutana majuzi pale hotelini, ukaniacha sehemu yakuegesha magari! Niambie
ukweli Tunda, hivi ulikuwa hata na mpango wakuja kunitafuta tena?” Tunda
alijisikia vibaya sana. “Nilijua tungeonana tu.” “Kwa njia gani, Tunda? Maana
hata simu yangu hukuomba na kikao kilichofuata ulimtuma mfanyakazi wako aje
kwenye kikao sio wewe mwenyewe. Mimi ndio nahangaika kulazimisha mahusiano
ambayo hata sijui niite mahusiano au sijui niitaje.” “Ni mahusiano Net.” “Ni
mahusiano gani haya Tunda!? Mimi ndiye wakukutafuta kila wakati, lakini
mwenzangu ni kama nakusumbua tu.”
“Hunisumbui hata kidogo Net.” “Unauhakika Tunda?”
Tunda akatulia kidogo. “Nikwambie ukweli Net?” “Niambie tu.” “Naomba nielewe
kabisa. Nakosa ujasiri kwako.” “Kwangu tena!?” “Kabisa Net. Sijui nikujishtukia
au vipi? Najiona nakuchosha na kukugharimu sana. Kwa hiyo wakati mwingine
najiambia kukaa mbali na mimi ni kama unapumzika. Naona kama kazi yako
uliyoifanya kwenye maisha yangu ni kama imetosha, sasa hivi nalazimika mimi
mwenyewe kusimama, sio kukuchosha zaidi. Sijui umenielewa?” Walifika nyumbani
kwa Mchungaji.
“Tutazungumza vizuri baadaye.” Net aliongea hivyo wakati anaegesha gari.
“Lakini naomba uniamini kuwa hunichoshi Net. Nisamehe pale unapoona ni kama
nakupuuza. Sasa hivi nipo kwenye wakati wa hekaheka. Siwezi kusema mgumu, ila
ni kama mtoto ambaye yupo kwenye kutambaa, lakini mazingira yanamtaka akimbie.
Nina majukumu ambayo yote yananiangalia mimi na lazima niyatimize.”
“Siku kama ya leo ndio huwa napumzika. Ila siku
nyingine, akili inabidi kufanya kazi kwa haraka ili kuweza kuchukua hatua na
nisiharibu.” “Am so proud of you Tunda. Najivunia sana. Nilifurahi sana kukuona
juzi ukiongea kwa kujiamini. Tena ukijinadi kipaji chako!” “Yote hiyo ni wewe
Net.” Net akacheka.
“Na wewe Tunda. Ulikubali na kuchukua hatua.
Nilijua jinsi wanaume walivyokuwa wakikusumbua tulivyokuwa pamoja kule Arusha.
Wenye pesa na wafanyabiashara wakubwa. Lakini ulitulia. Umenifurahisha.”
“Asante.” Tunda akacheka taratibu na kumwangalia Net. “Umenisamehe sasa?” Tunda
akauliza kwa kujali akibembeleza. “Tutaongea zaidi baadaye. Twende ili
tusichelewe kila mahali. Si uliniambia kule jela wana muda maalum?” “Ndiyo.” “Basi
tusalimie hapa, halafu tuwahi.” Wakachuka garini.
Kwa Mara ya Kwanza Net Nyumbani, kwa Mchungaji.
Wakamkuta
Mama Penny alishafika. “Mlipitia wapi!?” “Net alitaka tupitie dukani angalau
tusije mikono mitupu.” “Ndio faida
yakuwa na mahusiano na wazungu! Maana wageni wengine wakija humu ndani,
utasikia naomba nikanunuliwe Fanta, mimi sipendi Coca, au sijui Sprite! Lakini
watu walio staarabika wanakuja na zawadi mkononi.” Mama Penny aliongea akimsuta
Tunda. Net akacheka tu.
“Yaani
mama Penny! Mwenzio nakuwa nimechoka, na Fanta pekee ndiyo inaniburudisha.”
Tunda akajibu. “Sasa uwe unanunua kreti nzima unaliacha hapa ndani, sio
kusumbua watu.” “Huwa naacha, ila wanao wanamaliza.” “Ni Penny huyo, anti.”
Pendo akadakia. “Hata dady anapenda Fanta.” Penny naye akaongeza na kufanya
watu wote wacheke.
“Watoto
hawana siri hawa! Kwanza mpenzi wangu huwa hanywi soda nyingi kwa siku, tatu
mwisho.” “Sasa kama anakunywa tatu, na wanao mbilimbili, hiyo kreti inakaa siku
ngapi?” “Na dada naye anapenda Fanta.” Penny akaongeza tena. “Haya umesikia
wanao?” Tunda akadakia. “Naombeni
muondoke nyinyi watoto!” Mama yao akawafukuza. Wote walikuwa wakicheka.
“Karibu
Net. Hapa ndipo nyumbani kwetu wote. Tukupokee mzigo, ila huna haja ya kuja
hapa na vitu bwana. Uwepo wako ni zawadi tosha.” “Asante Mama Penny.” Ulikuwa
ni wakati Net alioufurahia sana. Alikula na kucheka tokea anaingia mpaka
wanatoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Sijawahi
kuona Mchungaji na Mama Mchungaji wa namna hiyo!” “Nilikwambia mimi. Yaani mimi
nilikuja na uchungu moyoni, hata sijui viliishia wapi, na lini! Wana jinsi ya
kukuonyesha maisha sio magumu ki vileee!!” “Si umemsikia hata huyo mama
mwenyewe anavyosema?” “Basi ndio usemi wake kila wakati. Eti, ‘acha kuwa serious wewe, maisha sio magumu
hivyo!’ au utamsikia, ‘Usituharibie
hali ya hewa hapa kwa kuwaza kama unataka kuumba dunia wakati Mungu mwenyewe
alishasema imekwisha, kazi yetu sisi tutawale.’ Wakati wote husema watu
tunashindwa hutawala sababu ya ujinga tu.”
“Usimuone
maneno mengi vile, anapesa sana yule mama. Karibu kila siku anayo kazi
inayomuingizia sio chini ya milioni. Kama sio kupamba, basi anabiashara zake
nyingine. Jina lake linafahamika sana hapa mjini, ndiye aliyenisaidia kuniuza
kwa watu mpaka sasa na mimi nafahamika au napata kazi kwa jina langu. Mkarimu
na hana tamaa. Ukifanikiwa ndiyo furaha yake.” Tunda na Net waliendelea kuongea
wakiwa wanaelekea kumuona baba yake Tunda jela.
“Nimefurahi
Tunda. Nimepata wakati mzuri sana. Nilihitaji mapumziko ya akili baada ya
mawazo mengi.” “Unawaza nini tena Net!?” “Nitakwambia tukitoka kumuona baba,
kama bado utakuwa na muda wakunisikiliza.” “Hata kama ni saa sita usiku,
nitakusikiliza Net. Unajua ni wewe pekee ambaye sina haja yakujificha kwako?
Sina sababu ya kujifanya Tunda huyu wasasa tu. Nakuwa huru, najua nipo na mtu
anayenifahamu vizuri, na bado amenikubali.” Net akamtizama Tunda na kutabasamu.
“Nini
sasa? Si kweli?” “Ni kweli Tunda. Na sio kukukubali tu, najipendekeza pia.”
“Jamani Net! Hujipendekezi bwana.” “Unauhakika Tunda?” “Kweli Net. Nakuwa nakosa
tu ujasiri. Nilikwambia. Lakini nafurahia tukiwa wote. Unaniheshimu japo
unanijua kuliko yeyote yule hapa duniani.” Walifika gerezani, hapakuwa mbali na
nyumbani kwa mchungaji. Ni eneo hilohilo la Tabata. “Twende kwanza tukamuone
baba, kisha tutaongea.” Wakashuka.
Net
akiwa na Tunda gerezani.
Waliingia
ndani japo muda ulikuwa unakaribia kuisha wa kuwaona wafungwa, lakini baba yake
Tunda alifurahi sana kumuona Tunda. Waliongea kidogo, Tunda akamuahidi, kufanya
kila awezalo kumtoa humo. “Tunda aliniambia jinsi ulivyomsaidia kumtoa kwenye
matatizo. Nakushukuru sana. Nilimuacha mwanangu hospitalini bila msaada, tena
nikijua kila mtu hamtaki!” Baba yake akaendelea.
“Nilipo
hukumiwa pale mahakamani nililia kama mtoto wa kike nikimfikiria mwanangu pale
kitandani hospitalini. Nilimlaani Mungu kwa kukubali mimba ya huyu mtoto
itungwe siku nilipolala na mama yake. Na pesa yenyewe niliyompa ilikuwa ndogo
kweli, sikujua kama nitakuja kumuona tena Tunda!” Tunda alikuwa ameinama tu
kama anayefikiria wakati baba yake akisimulia. Akili zilimrudisha mbali,
akabaki akimsikiliza Net na baba yake huku akifikiria hili na kukumbuka lile.
“Nakushukuru
sana.” “Hata mimi namshukuru Mungu kunikutanisha na Tunda. Nampenda sana
Tunda.” Tunda akashtuka sana. Hakutegemea kusikia Net anasema vile, tena akiwa
na baba yake! ‘Upendo huu ni wa namna
gani!?’ Tunda akajiuliza kwa mshangao akanyanyua kichwa na kumgeukia Net
palepale walipokuwa wamekaa upande mmoja wakimwangalia baba yake. “Nisije kujichanganya. Nisifurahie mengine.
Net ni mzungu. Neno upendo ni kitu cha kawaida kutamka kwa wenzetu.”
Akajirudi Tunda, akiogopa kufurahia zaidi.
“Ni
kweli ni upendo pekee, ndio uliokuwa ukihitajika kumpokea Tunda. Nakushukuru
sana.” “Asante baba. Tunaweza kuomba pamoja?” Net akauliza kiuungwana. “Mimi
sijui kuomba Net, wewe omba tu kama utataka.” Baba yake Tunda akajibu. Na hapo
ndipo Net alipomfundisha yule mzee kuomba, na kumuhubiria. “Hata Tunda amekuwa
akinihubiria, lakini…” Yule Mzee akasita.
“Haina
haraka baba. Pata muda wakufikiria, kisha utaamua.” “Nina dini yangu nzuri tu.
Sitaki kubadili dini.” “Kuokoka si kubadili dini baba. Nikupatanishwa na Mungu.
Bibilia inasema watu wote tumekosa na kupungukiwa na utukufu wa Mungu. Kwa
kutubu na kumkaribisha Yesu maishani mwako, nikukubali yale Mungu aliyokusudia
kwa maisha yako. Kama ukiokoka, na ukaona dini uliyonayo inakusaidia kukusogeza
karibu na Mungu, ujue upo katika njia sahihi.”
“Lengo
la dini nikukupatanisha na Mungu, au iwe msaada kwa roho yako, basi. Lakini kama itakuzuia kuwa na mahusiano na
Mungu, basi itabidi ufikirie mara mbili, juu ya hiyo dini. Maana itakufaa nini
kuwa na dini halafu ikakukosesha mbingu? Au itakusaidia nini kuiacha dini yako
ukahamia kwenye kanisa, na pia ukakosa mbingu?” Net akaendelea.
“Lengo
si kuhama kanisa moja kwenda jingine, lengo ni kuhama kutoka falme ya giza na
kuhamia kwenye ufalme wa Mungu, na kukaa huko. Sio unahamia kwenye kanisa
jingine, wenye jina fulani, ukajulikana na wewe upo kwenye kanisa hilo kumbe
maisha yako ni chukizo mbele za Mungu. Ukibaki wewe peke yako na Mungu, hamna
mahusiano yeyote, huo sio mpango wa Mungu.”
“Mungu
anataka mahusiano na mtu mmoja mmoja si kanisa, wala dini. Ukifa leo mzee,
hutaulizwa dini yako. Mungu atataka mahesabu ya jinsi ulivyotumia maisha yako
hapa duniani.” “Maisha yenyewe yameisha haya kijana wangu. Nishatupwa huku.”
“Nilikwambia usikate tamaa baba. Nahangaika kukutoa.” Tunda akaingilia.
“Hata
hivyo, hata hapa ulipo pia utakuja kuulizwa na Mungu ulifanya nini?”
“Ananiuliza nini huyo Mungu wakati yeye ndiye amenileta hapa, tena bila kosa!?”
“Ewaa! Umezungumza sahihi kabisa. Kuwa Mungu alikuleta hapa kwa kusudi. Basi
ujue lipo kusudi. Kwa nini iwe wewe na sio mwingine? Inawezekana kuna kazi
anakupa humu gerezani uifanye au umeletwa humu kwa ajili yako mwenyewe. Unasema
unayo dini. Huwa unasoma bibilia?” “Hapana, lakini nafahamu vihabari vyake.”
Akajibu baba yake Tunda akiwa kama anavuta kumbukumbu.
“Unakumbuka
historia ya Yusuph?” Yule mzee akatulia. “Kwa utizamaji huo, naamini unaijua
habari nzima. Unakumbuka mwisho wake? Unakumbuka jinsi alivyotoka gerezani kitu
Mungu alimfanyia?” “Si ndiye alikuja kusaidia ndugu zake?” Net akatabasamu kwa
kuridhika.
“Si
ndugu zake tu, watu wengi walipata msaada kupitia kukaa kwa Yusuph gerezani.
Kama angelia na kubaki kulalamika, inamaana kuonewa kwake kule gerezani
ingekuwa bure kabisa. Tunda amekupa ushuhuda wake?” “Upi tena?” Net akamtizama
Tunda kama anayemuomba ruhusa, yakusema. Kwa vile Tunda anavyomfahamu Net,
akajua hawezi kumdhalilisha kwa baba yake. Akamruhusu asimulie chochote na yeye
akiwa na hamu yakusikia jinsi Net anavyoanza kutumia maisha yake kuwa msaada
kwa wengine.
“Nilimwajiri Tunda kwenye kampuni ya mama yangu. Nikasafiri nikamwacha Tunda pale ofisini. Huku nyuma mama yangu alimfukuza Tunda vibaya sana. Aliondoka Arusha akiwa hajui chakufanya, akilia njiani akimlaumu Mungu. Lakini Mungu alimfundisha kwa mfano wa kupitia watoto, huku akimuonya kulia hakutamsaidia, mpaka atakapoangalia mazingira yanayomzunguka, akasimama na kuchukua hatua.”
“Tunda
alitii, ndio maana yupo leo kama alivyo. Kama Tunda angeendelea kulalamika
mpaka leo asingekuwa hapo. Na yale ambayo shetani ameyakusudia kuwa mabaya
kwake, yangeendelea kumkandamiza na kumwangamiza kabisa.”
“Usikubali
maisha yako yakawa hayana maana. Kila kinachotokea katika maisha yako baba
yangu, kitumie kutengeneza hesabu ya kumpa Mungu siku ukisimama mbele zake.
Maana ni kweli wote atatudai tu siku moja. Lakini uzuri, kila utakapochukua
hatua, yeye anakuwa na wewe, anakuinua, atakutia nguvu na kukubariki.” Tunda
alikuwa akimwangalia Net bila kummaliza. Kijana mzuri wakuvutia kwenye kila
jicho la mtu anayemtizama, mpaka watoto! Aliyesoma vizuri, anayejua maisha
vizuri, na pesa nzuri yakueleweka na bado anasimama na Mungu wake!
“Kwa
mfano mwingine tu. Najua unajua maisha ya Tunda kwa sehemu. Tena ni maisha
yasiyofaa kutamkika mbele za watu. Lakini tutahakikisha, maisha hayo hayo
aliyoishi Tunda, yanasikika, tena vizuri, mpaka watu wakombolewe. Tutafundisha
vijana kwa wazee, wakina baba na mama, tutamfikia kila mtu kwa maisha aliyoishi
Tunda mpaka watu wapate msaada. Nje na ndani ya nchi. Wazi wazi bila kificho
mpaka shetani ataogopa kushika ndoa za watu, maisha ya vijana, watoto wa watu,
kila baya lililotendeka kwa Tunda, tena sirini, tutatumia mwangani kufikia
jamii nzima, mwenye sikio atasikia na kubadilika.” Tunda hakuwa akiamini. “Inamaana na yeye anajiweka!” Bado
Tunda hakuwa ameelewa.
Ilimgusa
sana baba yake Tunda. Hata yeye hakuwahi kuona mtu aliyempokea Tunda kwa kiasi
hicho. “Asante sana kijana wangu. Asante baba. Na mimi Mungu akinipa uzima, na
akanitoa humu ndani, nitaungana na nyinyi.” Net akacheka. “Si umeona Tunda?
Tunazidi kuwa wengi? Sasa wewe Mzee tunaomba uanzie humo ndani. Kwa kuwa mimi
na Tunda hatuwezi kufikia wafungwa wenzako, wewe ndio uwe nao.”
“Naanzaje wakati hata kuomba siwezi!?” “Tutakuwa na wewe kwa maombi. Na wewe kazana kusoma bibilia ili uwe unaongea habari unazozifahamu. Tutakuombea ili ujazwe na nguvu za Mungu, halafu mruhusu Mungu akutumie kwa jinsi apendavyo na alivyokusudia. Kama alikuleta huku, lazima ujue lipo kusudi, na yeye atakusaidia kufikia lengo.” Yule mzee alifurahi sana. Net alimuongoza sala ya toba, akamuombea na kumuachia bibilia yake.
Baada yakutoka gerezani kumuona baba yake Tunda, Tunda & Net.
Tunda hakuwa akiamini. Alishindwa
hata kuongea kwa muda. Net aliongea mambo kadhaa, yaliyomgusa na kumuogopesha
Tunda. Hakuwa akiamini na aliogopa asije akafurahia kama alivyofurahia kwa
Waziri Mbawala, ikawa tofauti. Ikaja kuwa ni Net aliongea yale yote sababu
yakufikia roho ya baba yake. “Net anapenda watu watubu na wamrudie Mungu.
Ingekuwa kunipenda mimi, angeniambia mwenyewe.” Tunda akaona
ajitulize.
Net akaendelea
kuendesha na yeye kimya, wakirudi kanisani kufuata gari ya Tunda. Alikaa kimya,
baadaye ndipo akaweza kushukuru. “Nashukuru sana kwa kumsadia baba yangu.
Umemuona jinsi alivyobadilika? Hata uso wake umechangamka. Asante sana. Mimi
nimekuwa nikimuhubiria kwa muda mrefu sana bila Mafanikio.” “Ndio maana bibilia
inasema katika kitabu cha {muhubiri 4:9 Two people are better off than one, for they can help
each other succeed.} Au kwa Tafsiri ya Kiswahili ni {Afadhali kuwa wawili kuliko mmoja, maana wapata ijara njema
katika kazi au unaweza sema wanasaidiana kufanikiwa katika kazi}. Si umeona jinsi mimi na wewe
tunavyoweza kufanya jambo likafanikiwa?”
“Mbona
mimi pale sikusema kitu?” “Si kweli. Ulishapanda mbegu kwenye moyo wake, ukawa
ukimwagilizia mimi nilienda kumalizia tu kuvuna.” Tunda akatabasamu kama
anayefikiria. Wakawa wameshafika kanisani.
“Karibu
nyumbani kwangu.” “Nilivyokuwa nasubiri kwa hamu huo ukaribisho!” “Bwana Net!
Kwangu usisubiri kukaribishwa.” “Lazima nisubiri, na hivi kuna kina Julius tena!”
Tunda akacheka na kushuka kwenye gari. “Unifuate nyuma, ndio itakuwa rahisi
kufika nyumbani.” Tunda akafunga mlango na kuingia kwenye gari yake, kisha
akaondoa gari yake, Net akawa akimfuata nyuma.
Net apasua jipu kwa Tunda.
Bado
Tunda alikuwa akiishi pale pale maeneo ya Kimara, karibu sana na Ubungo. Alimkaribisha
Net ndani, wakakaa kwenye makochi. “Hapa kwangu hakuna soda, nina maji tu. Ila
naweza kwenda kukununulia kama utapenda. Mimi sio mpenzi sana wa Soda. Labda
niwe nimechoka sana na kazi, ndio nitakunywa soda. Lakini sio hapa kwangu.
Najitahidi zisiwepo.” “Hapana. Mimi nipo sawa tu. Bado nimeshiba.” Tunda akaweka
vitu vyake ndani, akarudi kukaa hapo hapo kwenye kochi kubwa alilokuwa amekaa
Net.
“Hongera.
Naona nyumba imekamilika.” “Asante Net. Ndio moja ya vitu vilivyokuwa
vikiniliza mwenzio! Sina ndugu wala ukoo wakusema nakwenda kutembea. Sasa hata
nishindwe kuwa na kwangu! Ilikuwa ikiniuma sana. Nilianza kutafuta pakuishi
hata kabla ya gari. Nilijiambia lazima nipate kwanza kwangu. Angalau nipate
kimbilio.” “Hongera sana Tunda. Hakika umenifurahisha.” “Asante Net. Napambana
kweli!” “Na juhudi zako zinakulipa. Nimepitia kwenye website yako, upo vizuri
sana.” Hilo lilimfurahisha sana Tunda, kujua Net alimfuatilia zaidi.
“Nikuulize
kitu Net? Nahofia nisiwe nimekuelewa vibaya.” “Karibu.” Net akajiweka sawa na
kumgeukia. “Ulisema ‘utakuwa’ na
mimi kunisaidia kutumia maisha yangu kufikia jamii?” Net akacheka pale Tunda
alipoweka msisitizo kwenye ‘utakuwa’.
“Unajua
umenipa hamasa sana? Ni kama umenitoa kwenye kona na kunivuta mwangani! Sasa
hivi sioni haya tena. Lakini sijui ndio ninafanyaje! Umesema utanisaidia?” “Sio
kukusaidia Tunda. Tutakuwa wote.” Tunda akawa bado kama hajampata vizuri. Net
akaendelea.
“Nahisi
ndio kazi Mungu anataka niifanye, labda mpaka kufa kwangu. Nimejaribu kukwepa,
nikimpa Mungu sababu za msingi ili niweze kukwepa, lakini Mungu ananirudisha tu.
Hata nifanye nini, bado najikuta nimerudi hapa hapa.” Hapo ndio akawa
amempoteza kabisa Tunda. Akapandisha miguu yake kwenye kochi akaikunja vizuri
nakumgeukia Net.
“Sikuelewi
Net.” “Wewe kwa nini hushangai kila unavyozidi kunikwepa, ndivyo tunavyozidi
kukutana?” “Net Jamani! Mimi mbona sikukwepi?” Net akacheka.
“Siku ya
kwanza nafika nyumbani kwa shangazi yako, unakumbuka ulinifungulia mlango?”
Tunda akatingisha kichwa kukubali. “Huwezi amini, naweza kukwambia mpaka aina
ya gauni ulilokuwa umevaa siku ile, jinsi ile picha ilivyo niganda mawazoni.
Hayo macho yako ya kusinzia, siku ile ndio yalikuwa yamezubaa yakinitizama.”
Tunda alicheka na kufunika uso wake.
“Nikaanza
kujifariji ili niepukane na mawazo yako. Nikasema kule kupigwa na butwaa na
kunishangaa ni kitu ambacho nishazoea kwa watu wengi hasa wadada. Huwa
wananiangalia kwa namna yao, ambayo huwa hainisumbui hata kidogo, lakini wewe
ikawa tofauti.” “Mimi nilikuwa nakushangaa ulivyo mzuri zaidi ya nilivyosikia
sifa zako! Mzungu unayeongea kiswahili chenye heshima.” Net akacheka.
“Sasa
nikaanza kupuuza. Lakini bado nikawa nasumbuka. Ndio maana nikawa nahangaika
kuja pale nikuone ili nijue ulichonacho wewe cha tofauti na kinadada wengine ni
kipi! Nikawa nakuja mchana na usiku, ili nikuone, lakini sikufanikiwa. Nikawa
namuomba Mungu angalau uje basi hata kufungua mlango tena, lakini wapi.”
“Baadaye
nikajiambia niachane na wewe, usinisumbue. Tena hapo ndipo nilipokuwa nikipata
na habari zako mbaya kabisa. Nikawa nikijiambia nina sababu zote za kuwa mbali
na wewe. Lakini nikawa najikuta nataka kukuona tu. Mwishowe nikajiambia siwezi
kujitesa kwa namna hii ni afadhali nitafute hata sababu nikae na wewe, ili hata
nitafute sababu moja utakayonikera, nikuchukie, niondoke zangu nirudi shuleni
kwa amani niwe nimekutoa mawazoni.” Tunda alikuwa haamini.
“Unakumbuka
niliwakaribisha kwenye maombi nyumbani? Hukufanikiwa kuja, na nia ya
kuwakaribisha nyinyi wote mpaka Nyangeta ilikuwa nikupata muda na wewe,
nyumbani kwetu. Maana pale kwa shangazi yako ilishindikana kabisa kwa kuwa kila
nilipokuwa nikijaribu kukusogelea ndivyo Sera na mdogo wake walivyozidi
kunifuata, na kuishia kukutukana mbele yangu kitu kilichokuwa kikiniumiza
sana.”
“Uliposhindwa
kuja nyumbani siku ile, na mimi nikaona muda wangu wakurudi chuoni umefika,
lazima niondoke, na mimi ni mtu ambaye nikianza jambo lazima nimalize, ndipo
nikajitosa kumuomba shangazi yako nirudi kesho yake nije kuongea na wewe kabla
sijaondoka. Kumbe ndio naharibu zaidi.”
“Nilirudi
Canada chuoni, lakini sikuwa na furaha, nikafikiria kitu chakufanya, nikaamua
kutafuta msichana wa kanisani ili tuwe na mahusiano kuepuka msongamano wa
mawazo. Nilipata binti mzuri tu wa kanisa ambalo nilikuwa nikiabudu na bibi na
babu. Wazazi wake walikuwa wakifahamiana na kina babu. Kwa kipindi hicho wakati
mimi nipo chuoni na yeye pia alikuwepo chuoni, lakini ndio alikuwa akianza,
mambo yalienda vizuri sana.”
“Hapakuwa
na shaka kuwa siye mwanamke Mungu aliyenipa. Tulielewana kwa mambo mengi tu,
mengine yalikuwa madogo madogo yakurekebishana kama wanadamu au tuseme
yakuchukuliana.”
“Siku
moja nikiwa na yule dada nikajikuta nikijiambia afadhali nimeweza kuachana na
mawazo ya Tunda. Hapo ndipo ikawa ni kama nimerudisha kumbukumbu zote. Na ndio
ilikuwa nakaribia kumaliza chuo, na kwa muda wote huo hata sikuwa
nimekufikiria, tulikuwa na amani na furaha na Chloe. Nilijuta sana kuleta zile
kumbukumbu zilizokuwa zikinitesa bila sababu. Sikuwa nakufahamu, halafu
nilikuwa na sifa mbaya tu za kwako. Nikawa nikimwambia Mungu na kumkumbusha
mabaya yako niliyokuwa nimesikia.” Tunda akainama nakujifuta machozi.
“Shule
yangu ilipoisha, mama akaniomba nirudi nimsaidie kazi zake kwa muda. Kama
nitavutiwa kuishi naye sawa, nikitaka kurudi kuishi Canada pia ni sawa.
Nikakumbuka wosia aliokuwa ameniachia baba, juu ya mkewe. Baba alimpenda sana
mama. Wakati wote alikuwa akiniambia hata kama akiondoka kesho, I should watch
over Maya na mama, yaani nimtunze mkewe na Maya. Ukumbuke aliniacha bado
nikiwa mdogo tu, lakini sikuwahi kusahau hilo. Alinilea kuwa mwanaume wa familia
tokea mtoto na babu hivyo hivyo. Japokuwa mambo yangu yalikuwa yakienda vizuri
kule, ilinibidi nirudi Tanzania kumsaidia kazi mama.”
“Nilimuomba
Chloe aihirishe angalau mwaka mmoja ili tuje naye huku, nikishaweka sawa mambo
ya mama, tungerudi. Lakini Chloe alikataa. Nikamwambia hata kama itatulazimu
kufunga ndoa kwanza, naweza kumuoa kisha tukaja naye Tanzania, na babu
alimwambia endapo ataacha chuo kwa ajili yangu, akapoteza udhamini, babu
alimuahidi angemsomesha kwa gharama zozote zile mpaka amalize. Lakini alisema,
anaweza kunisubiri kwa huo muda wa mwaka mmoja, lakini hakuwahi kufikiria
kuishi maisha mengine nje ya nchini kwao na amejiwekea malengo ya kumaliza
shule ndani ya huo muda, hawezi kusogeza. Nikamkubalia, nikaja huku.”
“Baada
ya mwaka, nikarudi na kumwambia inabidi niongeze muda, maana mama alianza
kupata tenda za ujenzi wa barabara zilizokuwa zikimuingiza pesa nyingi sana
lakini zilihitaji mtu kama mimi kuwepo na kusimamia. Nikamuomba tuondoke naye,
bado akakataa. Akasema atanisubiri tu. Nikaamua kumvalisha kabisa pete ya
uchumba ili asije kubadili mawazo. Nikarudi huku nikawa nikifanya kazi kwa
bidii sana ili nimwache mama kwenye mazingira mazuri, na wafanyakazi wazuri ili
nirudi kwenye maisha yangu. Safari za Canada zikawa nyingi kumfuata Chloe kwa
kuwa alianza kulalamika anachoshwa na mahusiano ya mbali.” Net akatabasamu.
“Mambo
yalianza kunichanganya pale nilipokuona tena. Katikati ya kazi nyingi, na
mahusiano ya lawama, kati yangu na Chloe, kwa nini sipigi simu, kwa nini siendi
kumuona, na mambo kama hayo. Unakumbuka mazingira tuliyokutana tena? Ulikuwa na
mwanaume na wazi alionekana ni mume wa mtu. Niliumia mpaka nilijichukia.
Nilijaribu kujiliwaza kwa kukuunganishia na maneno ya kina Sera, na kusema sina
haja yakuumiza akili zangu, kwa msichana ambaye hukuwa na maadili, mimi ni
mchumba wa mtu. Unajua tena, ili kujipa aghueni moyoni. Lakini nilishindwa
Tunda. Nilikuwa nikiumia sana. Na Mungu naye alikuwa akinikutanisha na wewe
kwenye mazingira yaliyokuwa yakizidi kunitesa sana.”
“Nilikuwa
nikiumia nakujiuliza chakufanya, sikuwa najua pakukupata wala sikujua
chakufanya. Ukweli niliteseka Tunda. Kila nilipokuwa najaribu kukupuuza, ndivyo
nilivyozidi kukufumania. Hasira juu ya kila mwanaume niliyekukuta naye
ilinifanyanya nichukie hata kazi ya mama. Kwa kuwa wanaume wote niliokuwa
nikikukuta nao, ni watu muhimu sana kwenye biashara za mama.”
“Nilishindwa
kabisa kuendelea na ile kazi, nilijawa hasira, nikashindwa kuwa mvumilivu
kwenye kila kitu. Mama alidhani nimechoka kuwepo hapa Tanzania, akanishauri
nirudi tu kwa bibi na babu, lakini nikajikuta siwezi tena kuondoka kukuacha
kwenye mikono ya wanaume wanaotaka kukuchezea.” Net alicheka kidogo kama
anayefikiria.
“Huwezi
kuamini kutoka kwenye kukuchukia sana kwa kunisababishia maumivu ya uchafu unaofanya,
nikageuza hisia nikaanza kuona uthamani ulio nao. Na kuzidi kuchukia kila
mwanaume anayekuchezea. Nilikuwa nikijiambia wanakuchezea kwa kuwa hawajui
thamani yako. Unakumbuka yule Mzee tulikutana wote Mwanza pale baa akiwa
amelewa, akikuelezea jinsi ulivyo mzuri, na kueleza mambo kwa undani kabisa?”
Tunda alishinda hata kumtizama Net, akabaki ameinama.
Net
akaendelea. “Ukweli nilikuwa nikiteseka sana. Mwishowe nikaamua kujisalimisha
kwa Mungu. Nilikuwa sijui chakufanya Tunda. Kila ninapoenda nakutana na wewe
ukiwa na wanaume tofauti tofauti, huku Chloe naye ananitaka nirudi tufunge
ndoa, huku najiambia siwezi kukuacha. Nikamwambia Mungu akinisaidia nikakupata,
ukakubali kubadilika, nitaondoka haraka sana kurudi kwa mchumba wangu.”
“Siku
iliyoniuma zaidi ni pale nilipokukuta na Gabriel. Niliumia sana. Gabriel
alikuwa rafiki yangu tokea Canada. Baba yake alikuja kusoma kule, akawa chuo
kimoja na mama, kwa hiyo Gab alikuja Canada akiwa mtoto sana, nilizaliwa yeye
akiwa na miaka kama mitatu hivi. Tuliishi nao Canada, wao wakarudi huku nchini,
Gabriel akiwa na miaka 18. Na ndio watanzania pekee tuliokuwa nao karibu kule.
Hatukuacha kuwasiliana na Gab mpaka sasa. Na hata anapokuwa akija Canada, yeye
na mkewe au wazazi wake, wanafikia nyumbani kwetu. Kwa hiyo ni kama ndugu.”
“Kuja
kujua ulikuwa na mahusiano naye, nikaamua kuondoka kabisa nchini. Lakini Gab
aliniomba sana radhi, nikamwambia akuache kabisa na asirudie kukutafuta tena.
Maana alikuwa yupo tayari kumuacha mkewe kwa ajili yako. Nilimwambia endapo atamuacha
mkewe, kwa ajili yako ndio itakuwa hata mwisho wangu na yeye pamoja na familia
yake yote. Yaani mpaka wazazi. Ndio Gab akakubali kukuacha kabisa. Na kuniahidi
hatakutafuta tena.”
“Lakini
aliniudhi sana siku ile ulipomfuata hotelini unamlilia shida halafu anakwambia
atakupiga! Iliniuma toka moyoni. Unakumbuka nilikukuta umejificha kwenye kona ukilia?”
Tunda alitingisha kichwa kukubali akiwa anafuta machozi.
“Pale nilikuwa
nimeshazunguka sana. Na gari na kwa miguu huku nikikimbia kukutafuta. Nilijua ndio
wakati pekee Mungu alionipa kukupata. Kwa upande mwingine nilifurahi kuona
umefika mwisho, watu wote wamekukimbia. Nikajiambia nakaribia kumaliza kazi
yangu. Nikupatanishe na Mungu, kisha niondoke niende kwa mchumba wangu.”
“Kule kuishi na wewe Arusha ikawa msaada kwangu
mimi mwenyewe. Hukuwa umefikia hata maamuzi ya kubadili maisha, lakini nilikuwa
nikifurahia sana tukiwa pamoja. Nikaona jinsi ile ofisi inavyokuwa, nikajiambia
wewe ni mtu utakayenifaa kwenye mambo mengi. Kwamba ukikubali kumpa Yesu maisha,
nitakuwa nimeua ndege wawili kwa jiwe moja. Nitakuwa nimemalizana na wewe kwa
amani, na ofisi nitaiacha kwenye mikono salama. Sasa unakumbuka siku tumeenda
kwa mama akakwambia nitasafiri?” Tunda akatingisha kichwa kukubali.
“Alikuwa akijua muda wangu wakuondoka moja kwa moja
kwenda kwa mchumba wangu umeshakaribia. Maana nilishakuwa nimekupa muda,
nikasema ninakuachia muda fulani, uje ufikie maamuzi ya kubadilika bila mimi
kukulazimisha. Nikajiambia muda huo ukifika hujafikia maamuzi, nitaongea na wewe,
ukubali au ukatae, nikajiambia nitaondoka. Ndio nikawa nimemwambia mama kuwa
ikifika mwezi wa kumi na moja nitaondoka moja kwa moja. Kumbe ule muda
niliokuwa nimekupa wewe kukuangalia, ndio kipindi hicho na mimi nilianza
kukuzoea. Huwezi amini jinsi ilivyokuwa ngumu kukuacha usiku. Nilikuwa nikitamani
niwe na wewe wakati wote.” Tunda akamtizama huku amekunja uso, haamini.
“Siku zikazidi kwenda, wewe ukaokoka, lakini nikawa
nashindwa kabisa kuondoka. Chloe naye akawa amenipa muda, kuwa ikifika mwezi wa
kumi na moja sijarudi kule, hataweza kuendelea kunisubiri tena. Nilikuwa tayari
kwa hilo. Kila mama alipokuwa akiniuliza naondoka lini, sikuwa na jibu tena.”
“Ndipo babu akaugua sana, ikabidi niende tu lakini
hapo nilishakuwa nimeahirisha sana. Kila Nana alipokuwa akinipigia simu
akiniambia hali ya Papa, nilikuwa nikimwambia nitakwenda, lakini nashindwa
kukuacha. Huo mchezo ukaendelea, ndipo nikaambiwa majibu ya hospitalini
yameonyesha Papa hawezi kupona. Nana akaniambia Papa anataka kuzungumza na
mimi. Lazima niende haraka.”
“Ndio nikaondoka ule mwezi wa 11 mwanzoni. Kwa hiyo
ikawa nimefika kabla ya kipindi alichokuwa amenipa Chloe kuisha. Tukaanzisha
mahusiano kwa uhakika, huku nikimuahidi kutokuondoka tena Canada. Hapo
nikajihesabia nimemaliza kazi yangu. Umeokoka, na ofisi ipo kwenye mikono
salama.”
“Ila sasa mahusiano yakawa mazito sana kwangu,
kwani Chloe hakuwa Tunda. Sikuwa nikiona maisha yangu na yule binti hata kidogo.
Babu alinishauri labda nimchukue nimpeleke sehemu mbali mbali ili kupata naye
muda, labda zile hisia za mwanzoni zingerudi. Aliniambia ni kwa kuwa tuliishi
mbali mbali kwa muda mrefu sana. Nikamuacha babu akiwa bado anaumwa nikaanza
kuzunguka na Chloe.”
“Hata
Papa alijua angekufa, kwa hiyo alitaka kuniona nimeoa kabla hajafariki. Madaktari
walitupa muda uliobaki wa papa au babu uliobaki kuishi. Nikakusudia babu awepo
kwenye harusi yangu, angalau anione tu nikioa kwa kuwa ni kitu alichokuwa akikitamani
kuondoka akiwa ameniacha nimeanzisha familia yangu. Nilizunguka na yule dada,
lakini hakuwahi kuwa Tunda. Alikuwa na sifa zote za kuwa mke wa mtu, lakini sio
mke wa Net.”
“Nakumbuka tulitoka safari tulitua uwanja wa ndege
na Chloe nikaenda moja kwa moja hospitalini kwa babu. Nilimkuta na bibi yuko
pale, nikajikuta machozi yakinitoka, nikimuhurumia babu yangu, kuwa yale
aliyotamani nimeshindwa kumpa.”
“Nakumbuka babu alinitazama kwa huruma, nikajikuta
namwambia, ‘She is not Tunda.’
Alitabasamu na kuniambia kwa kifupi tu, ‘then
go and tell her, NOW’. Nikachukua ushauri wa babu pale pale, sikutaka hata
kusubiri. Nilitoka pale hospitalini nikamfuata Chloe nyumbani kwao. Nikamwambia
sitaweza kumuoa tena, nampenda mtu mwingine. Ilikuwa ngumu sana, lakini niliona
ni heri yale maumivu ya wakati ule kuliko aje aumie akiwa mke wangu.” Mwili
mzima wa Tunda ulikuwa ukitetemeka.
“Basi, nilirudi hospitalini nikamwambia babu, babu
alitabasamu na kuniambia hata baba yangu angekuwepo angenisifu kwa kufanya
maamuzi magumu na muhimu kama yale. Kwa hukumu yakuona nimemshindwa kumpa babu
yangu kile alichokitamani, kwa kutokuoa akiwepo, nilimuuguza bila kuondoka
pembeni yake mpaka alipofariki. Zilikuwa zimebaki siku chache afariki, kwa hiyo
mimi ndiye niliyekuwa naye pale hospitalini muda wote.” Tunda alikuwa ameinama
huku ameficha uso wake akilia. Net akacheka tena.
“Ungenihurumia pale mama alipokuja kwa mazishi,
halafu ananiambia uliondoka Arusha, hajui ulipo. Nilitamani wawe wamenizika
mimi sio babu yangu. Nilikasirika sana. Nikahisi Mungu anataka kunichanganya
akili tu. Nilikaa Canada sijui nirudi tena huku au niendelee na maisha yangu tu
moja kwa moja hukohuko. Mama alipopata matatizo kwenye ile ofisi ya Arusha
ilinibidi nirudi kuja kumsaidia.” Tunda akashtuka.
“Alipata matatizo gani tena!?” Tunda akajifuta machozi na kuuliza. “Safia
alimtapeli. Kwa kifupi aliiba wateja wote wa mama, kwa kuwaambia hatuna uwezo
wa kuwasafirishia tena mizigo yao. Kwa sababu tofauti tofauti. Mara awaambie
malori yameharibika, au yote yamesafirisha mzigo sehemu nyingine, kumbe akawa
ameingia ubia na mtu mwingine. Anamlipa kwa asilimia 40, kwa kila mteja
anayempelekea. Kwa hiyo tukawa tunatumia pesa nyingi kujitangaza, wakipiga
kuomba huduma, Safia anawapeleka kwenye kampuni ingine.”
“Safia alipoona amenogewa, akaja
kufungua kampuni kama ileile. Akawa anatumia magari yaleyale ya mama, lakini
aliajiri madereva wake. Wale niliokuwa nimeajiri mimi aliwatafutia sababu, mama
mwenyewe akawafukuza. Tena aliwafukuza vibaya tu. Basi, Safia akajinufaisha kwa
gharama ya mama. Mama kuja kushtuka, akakuta alishafilisiwa kabisa na anadaiwa
sana. Alimtia hasara kubwa tu.”
“Tuliuza ile nyumba ya Arusha na yale malori yakiwa
kwenye hali mbaya sana, tukalipa madeni yote tukabakia na biashara za huku Dar
tu.” “Pole Net.” “Mama amejifunza sana. Aliogopa kuniambia ukweli kama
alikufukuza, alijua ningemlaumu sana. Lakini juzi tulipokutana pale hotelini,
ulipokuja kwenye kikao, ukanisimulia
kila kitu, nikatamani kujua kwa nini alikubadilikia.” “Ulijua ni kwa nini?”
Tunda akauliza kwa upole, lakini Net alionekana kusita kidogo.
“Nimbie tu Net. Nataka kujua nini nilifanya kiasi
chakubadilisha moyo wa mama Cote. Alinipokea vizuri sana nilipofika Dar, na
alinipenda hata kabla hajaniona akawa haishi kunisifia na kunishukuru kwa kazi
nzuri niliyokuwa nikimfanyia. Lakini akaja kubadilika ghafla!” Net akavuta
pumzi kwa nguvu huku amefunga macho kama anayejishauri.
“Ukikubali kushindwa, ujue wapo wengine wanaotumiwa
na shetani kama vile ilivyokuwa kwako. Na ujue ndoa au mahusiano mengi yapo
hatarini. Wewe sio wa kwanza Tunda, na wala hutakuwa wa mwisho. Wapo
waliokubali na kutubu, na wapo wanaokataa na kuendeleza huo uchafu mpaka sasa.
Wewe umechagua jambo jema, lazima usaidie wengine. Hata hivyo binafsi
nakushukuru, maana bila wewe mama yangu angeolewa na mwanaume anayejua ni mcha
Mungu, kumbe ni tapeli tu.” Tunda aliendelea kulia.
“Nakupenda sana Tunda.” “Naomba
unisamehe Net. Nisamehe. Nimekuumiza sana. Naomba unisamehe.” Tunda
akapiga magoti. “Yamepita hayo Tunda. Nitafurahi kama utaishi na mimi bila hukumu.
Mungu amekusamehe, na ni kweli anakupenda. Aliniweka kwenye maisha yako
makusudi kunifundisha upendo wake kwa watu tunao wahukumu. Tokea unaishi
dhambini, wanadamu wakiwa wanakuchukia na kukuhukumu, Mungu alikuwa
akinionyesha mimi upendo wake kwako wewe Tunda.”
“Alinitoa kwenye nafasi ya kukuchukia na kukupenda
kupita ninavyoweza kukwambia. Aliuweka uthamani wako bayana kwangu. Na
amekuonyesha hata wewe kwa vile alivyo kufanikisha. Amekusamehe, amekupokea na
elimu uliyo nayo, na ameonyesha wasomi kuwa anaweza kubariki yeyote ampendaye.
Unamaisha mazuri kuliko wasomi wengi hapa nchini! Zaidi amekupa furaha na
amani.” “Amenipa na wewe.” Net akacheka.
“Ndiyo, na mimi ambaye nitakuwa na wewe kwenye maisha yangu yote.” Tunda hakuwa
akiamini.
Alifunga
macho yake tena na kuendelea kulia. Alianza kufikiria maisha yake kama mke wa
Net, aliyekuwa anamezewa mate na warembo wengi, wasomi wa kila namna.
Waliojitunza na kulelewa kwenye familia nzuri, lakini alishangaa vile Mungu
alivyomtunza Net, kwa ajili yake yeye aliyekuwa akihangaika na wanaume wa watu!
Tunda alishindwa kunyamaza. Net akamnyanyua pale chini, akakaa naye pale kwenye
kochi na kubaki amemkumbatia.
“Nakupenda sana Tunda. Sana.” “Asante Net. Nashindwa niseme nini!” Net akacheka.
“Kweli. Mpaka naogopa.” “Unaogopa nini
sasa?” Tunda akanyanyua uso wake, akamwangalia. “Nagopa
isije kuwa nipo usingizini halafu nikaamka nikakuta kila kitu ni ndoto tu.”
“Nini unachohofia zaidi?” “Kukupoteza tena.” “Hata
nikiamua kukutoroka, ujue Mungu wako atanirudisha tu.” Wote wakacheka.
Net akambusu Tunda kwenye kipanda uso. Hiyo ni mara
ya pili Tunda kupata busu la Net. Kwanza ilikuwa kwenye mkono na hapo ni mara
ya pili, na mara zote zilimsisimua. Hata kule kukumbatiwa ilikuwa ni mara yake
ya kwanza. Tunda alijivuta karibu sana na Net na kumkumbatia huku akilia tena.
Kwa mara ya kwanza alihisi ulinzi mkubwa sana. Alimkumbatia Net kwa kumng’ania
huku akilia na kushukuru Mungu kwa kumthamini.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Tunda aliyepitia kwa wanaume wengi, hakuwahi
kukumbatiwa maishani mwake kwa namna ile ya upendo. Hata tu mtu kutoa muda wake
na kumtaka atulie mikononi mwake. Si mama yake mzazi hata wanaume aliokuwa
akiwahudumia ilikuwa ni yeye kuwahudumia kwa juhudi zote waridhike, basi, labda
kidogo waziri Mbawala tena yeye mwenyewe Tunda alikuwa akiomba kukumbatiwa.
Hakuwahi kupendwa na kuthaminiwa vile.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Akiwa amejificha hapo kwa Net, wazo la kumtia hofu
likamji. “Lakini Net! Umeshafikiria tutakuwa na mahusiano ya namna gani? Kila
ninapopita yupo mtu anayenifahamu. Nimemuumiza mpaka mama yako mzazi, Gab naye
ndio hivyo, itakuaje? Si itakuwa kama nakudhalilisha tu kila wakati?” “Wao
walikuwa wezi tu, mimi ndio nimekabidhiwa na Mungu. Wanatakiwa waniogope mimi
sio mimi kuwaogopa. Halafu Tunda, kila mtu anamapito yake, tumetofautiana tu matukio.
Unakumbuka ule mfano wa Yesu walipomletea yule mwanamke kahaba?” Tunda
akatingisha kichwa kukubali.
“Walikuwa na sababu zote za kumpiga mawe yule
mwanamke. Lakini unakumbuka jibu la Yesu?” “Nakumbuka.” “Basi huna haja yakuwa
na wasiwasi, na kama nilivyokwambia, hatutasubiri watu watumie maisha uliyoishi
zamani kukunyanyasa. Sisi wenyewe tutayatumia kusaidia watu. Itasaidia kama
utakuwa jasiri, hata kama watakushtukiza kwa nia ya kukudhalilisha, unatakiwa
ujue jinsi ya kutulia wala usikubali hata mara moja mtu akakuumiza.”
“Itakuwaje kuhusu sisi wenyewe Net? Unaweza
ukaniamini kama ambavyo ungemuamini mwanamke ambaye hakupita mapito kama yangu?
Sitaki kuja kuumia tena. Sitaki uje unionyeshe upande wa
pili wa maisha ambao sijawahi ishi, halafu ukanikimbia.” Tunda alianza
kutokwa na machozi tena.
“Sijawahi kupendwa na kuthaminiwa
tokea mtoto. Wala sijawahi kuishi kwenye familia na mimi nikahusishwa na
kuthaminiwa mawazo yangu. Naogopa usije kunionjesha hayo maisha halafu baadaye
ukaja kuniacha, Net au tukashindwa kuishi kwa amani sababu yakutokuniamini kila
ninapokuwa na mtu mwingine au nimechelewa kurudi nyumbani.”
“Naomba Mungu anisaidie Tunda. Sitakuumiza hata
kidogo. Nimeamua kuwa na wewe nikiwa nakufahamu vizuri sana. Sijakurupuka. Ni
kitu ambacho nishajiuliza maswali yote ambayo wewe unaniuliza sasa hivi na
Mungu amenisaidia kupata majibu yake. Hakuna kipya kitakachobadilika.”
“Nakupenda, na nimekusudia uwe mke wangu. Nakuahidi
kukupenda Tunda. Nitakupenda kwa dhati na kukuheshimu, kama Tunda huyu
niliyenaye sasa hivi hapa mkononi. Tunda aliyeoshwa na kutakaswa na damu ya
Yesu. Sitaishi na Tunda yule wazamani.” “Asante
Net. Nakushukuru kunipokea.” Tunda alijirudisha kujiegemeza kwa Net na kukunja
miguu juu ya kochi. Wakatulia kila mtu akiwaza lake kama wasio amini.
Tunda
alijituliza pale akiogopa hata kusogea. Kichwa pembeni ya shingo ya Net
aliyekuwa amepitisha mikono yote miwili juu yake, akimpapasa taratibu kwa mkono
mmoja mgongoni. Wakatulia. Kama ambaye haamini, akanyanyua uso kumtizama Net
kuhakikisha kama ni yeye. Macho yakagongana. “Nimefurahi sana Net. Siamini!” “Hata mimi nimefurahi.” Tunda akajiweka
sawa.
“Sasa ndio tunafanyaje?” “Hatuna sababu yakusubiri
tena. Nataka kukuoa Tunda. Nataka uwe mke wangu. Nitaenda kuongea na mama, na
wewe kamwambie Mchungaji wako. Taratibu za harusi zianze.” Tunda akacheka. “Siamini kama na mimi
nimepata mtu wa kunioa! Nilijikatia tamaa.”
“Naomba salamu za kukumbatiana na Julius ziwe
mwisho.” Tunda alicheka kwa mshangao. “Husahau!?” “Nisahau wakati pale nilikuwa
nammezea mate jamaa? Yeye amekumbatiwa wakati mimi sijawahi kukumbatiwa hata
mara moja!” Tunda alizidi kucheka. “Eti na mimi nitaanza kuvaa pete za ndoa!”
Net akacheka lakini Tunda alipooza ghafla na kujitoa mikononi mwa Net.
“Nini tena?” “Nisipo zaa je? Kama waliharibu kizazi
changu wakati wananitoa ile mimba, nikapoteza uwezo wa kuzaa?” “Sijui Tunda.
Ila nakuomba usiniingizie hofu nyingii. Naomba unipe nafasi nifurahie hii hatua
niliyofikia leo. Hujui nilivyoteseka.” “Samahani Net. Nataka tusiharakishe,
tupate muda wakutafakari kwanza tusije tukakosa raha baadaye na kulaumiana.”
Hofu ilishamwingia Tunda, akamkumbuka Tunda halisia.
“Naomba unielewe Tunda. Haya mahusino yetu kwako
nimageni, lakini si mimi. Mwenzio nimekuwa nayo kwa muda mrefu sana. Nakwambia
hayo maswali yote nimeshajiuliza na Mungu amenipa jibu. Nikwambie swali jingine
ambalo nimeshajiuliza?” “Swali gani tena!?” Tunda akauliza, akisikika kuishiwa
nguvu.
“Itakuwaje kama tukienda kupima, nikakukuta
umeathirika? Umeshafikiria hivyo?” Tunda alibaki kama amemwagiwa maji yabaridi.
Akajivuta pembeni kabisa. “Sasa hata kabla hatujafika hospitalini mimi na wewe
tukapewa majibu yako, mimi nilishachanganyikiwa, nilishakuuguza, tena nilishajiona
jinsi nitakavyo kuuguza peke yangu kwa kuwa watu wamekususa, nimeshalia na
kuomboleza na Mungu wangu, mwishoni nikaamua kumuachia Mungu, nitembee kwa
hatua. Sitaki kuleta matatizo ya siku ya kesho, leo, Tunda. Ndio maana nakuomba
uache angalau nifurahie hii hatua ya leo. Naomba tutembee hatua kwa hatua, ili
tusije pitwa na chochote.” Tunda alijirudisha vizuri pembeni ya Net, akanyamaza
asiamini kama Net ni mtu wa kubaki naye maishani. Sio muondokaji! Amekusudia
kuwa naye.
“Sasa hivi kinachofuata nitaenda kumwambia mama.
Halafu nianze maisha ya kuwa mchumba wa Tunda. Niwe namtoa mchumba wangu sehemu
tofauti tofauti za starehe, nifanye yote ninayotakiwa kufanya kwa mchumba wangu,
kabla sijawa mume. Sitaki kupitwa na hatua hata moja kwenye maisha yako Tunda.
Hata kama tutaoana mwezi ujao, nataka hizo siku zilizobaki kabla sijakuoa,
nikutunze kama mchumba wangu.”
“Nataka nifurahie hatua yangu ya uchumba na wewe,
bila kuazima matatizo ya kesho. Leo nataka nikufurahie, msichana
niliyekusubiri, na kukutamani kwa muda mrefu sana.” Tunda alikuwa akilia
asiamini. Alijutia mapenzi aliyokuwa akiyagawa kwa kujidhalilisha. Hakujua kama
yupo mtu mahali fulani anampenda nakumsubiri kwa kiasi kile.
“Nilikuwa nikimuuliza Mungu kwa nini anachelewa
kukukabidhisha kwangu! Nilimuhakikishia kila kitu. Nilimwapia nitakupenda mpaka
kifo. Nikamwapia sitakusaliti wala kukunyanyasa. Yote hayo niliyafanya kama
mwehu ili tu anipunguzie siku za kunikutanisha na wewe.” Akajiegemeza kwenye
kichwa cha Tunda, aliyekuwa amemkumbatia, na Tunda alikuwa bado amekaa ubavuni
kwa Net, huku amekilaza kichwa chake hapo shingoni.
“Sina cha kusema Net. Sikuwahi hata kuwaza kama
unamawazo na mimi! Nilijua utakuwa ukinichukia kwa kunifumania zaidi ya mara
nne, tena na wanaume tofauti tofauti! Yaani hata sikuwahi kukuwazia hata
sekunde moja. Ila nilikuwa nikikuogopa sana. Kila ulipokuwa ukinifumania
nilikuwa nashindwa kulala kwa hofu.” Tunda akakaa vizuri.
“Nilijaribu kujipa moyo kuwa hunihusu, sikujui wala
hunijui kwa hiyo haijalishi lakini nilishindwa hujiliwaza. Nikaanza kupunguza
wanaume, nikabakia na wachache watakaonisaidia kuniweka mjini, lakini pia bado
niliteseka. Haya, mama Cote aliponifukuza Arusha, sikujua hata kama utajali.
Nikajua utashukuru Mungu kutuliwa mzigo. Sikuwahi hata kukuwazia kama unaweza
kuja kunitafuta tena, Net!”
“Nilipokuona pale juzi, nilifurahi
kukuona kama mtu muhimu ambaye umehusika kwenye maisha yangu. Lakini sikujua
hata kama nina maana yeyote kwako. Sikuwa hata nikijua kama uwepo wangu kama
una maana yeyote ile au unafanya kutimiza tu wajibu kama mkristo tu wakawaida.
Hakika wala sikudhani kama unaweza kuniwazia hivi. Nakushukuru kwa
kutokunikatia tamaa.” Net alikuwa akimsikiliza huku akitabasamu. Alimvuta mkono
mmoja, akambusu na kubaki wakiangaliana.
“Sasa inabidi nirudi nyumbani tu. Nikiendelea kukaa
hapa, naweza kushindwa kuondoka kabisa.” Tunda akatabasamu. “Nitakuona tena
lini?” Tunda akauliza, Net akacheka. “Kila siku nitajitahidi tuwe tunaonana.
Ila kesho itakuwa mchana, kuna tenda naifuatilia. Nikipata hiyo, najua
itamsaidia sana mama. Mambo yake yameenda pabaya sana. Biashara zake haziendi
vizuri.” “Mungu atakusaidia Net. Nitakuombea.” Net akatabasamu. “Afadhali
nimepata na mke muombaji.” “Umesahau wewe ndio ulikuwa ukinifundisha?” “Siwezi
kusahau. Lala. Kesho tutapata muda mzuri wakuongea zaidi.” Net akaaga na
kuondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Usingizi haukuja kwa Tunda. Alivaa haraka haraka
akapanda kwenye gari yake mpaka, Tabata, nyumbani kwa Mchungaji wake. Mlinzi
alipoona gari ya Tunda akafungua geti. Shida ikawa kufunguliwa mlango kuingia
ndani. “Bwana Mama Penny fungua!” “Hatukusikii, tumelala.” “Sasa mbona
unajibu?” “Unataka nini Tunda kwenye dirisha la chumbani kwangu?” “Kuna kitu
nataka kukwambia. Siwezi kulala mpaka tuongee.” “Kuna msiba?” “Hapana.” Tunda
akajibu.
“Umefukuzwa kwenye nyumba?” “Hapana.” “Basi naomba
utuache mimi na mume wangu, tumelala. Washirika wote tumewafundisha kuomba.
Hakuna haja yakutugongea milango usiku au simu za usiku usiku hatutaki. Kama
mtu anashida, unapiga magoti unaomba, halafu Mchungaji unaonana naye asubuhi.”
Tunda akaanza kucheka.
“Sasa muda wote huo unaongea hapo kitandani, mama
Penny, dada yangu, si ungeshakuwa umenifungulia mlango, tumeonge, na mimi
nimeondoka?” “Sitaki kutoka kitandani bwana! Wengine nyumba zetu zina AC. Usiku
tunawasha baridi. Nishajifunika, sitaki kutoka kitandani. Wewe niambie ukiwa
hapo hapo dirishani.” Tunda akatulia kwa muda.
“We Tunda?” Mama Penny akamwita. “Nimepata
mchumba.” Akaruka kitandani nakuanza kupiga vigelegele. Akawasha taa ya chumbani
kwake huku akipiga vigelegele. “Acha kelele mama Penny bwana! Watoto wamelala.”
Tunda aliongea kwa sauti ya chini kidogo, kama kumtuliza. “Siamini kama
nimepata harusi yakusimamia!” Tunda na Mchungaji wote walicheka kwa sauti.
“Hebu amka baba Penny, tukapange mipango ya
harusi.” “Hata mchumba mwenyewe hujaonyeshwa, unataka kuanza mipango!?” “Hebu
amka bwana na wewe! Yeyote tutakayeletewa huyohuyo tutampokea ilimradi na mimi
nisimamie harusi.” Alimsha watoto wote kwa vigelegele.
“Ingia ndani bibi harusi wangu.” Tunda alifunguliwa
mlango. “Kuna nini mama?” Penny akauliza akiwa na usingizi. “Anti Tunda
anaolewa?” Pendo naye akauliza baada yakusikia vigelegele vikiendelea bila jibu
kutoka kwa mama yao. “Na yule Mzungu?” Penny akauliza tena. Tunda akacheka
sana. “Penny wewe! Upo kama mama yako!”
“Hebu niambie Tunda. Mchumba ni nani?” Mchungaji
alitoka na yeye akakaa kwenye kochi, mkewe alikuwa akiendelea kushangilia hata
mchumba hajauliza. “Acha kelele bwana na wewe mama Penny. Mchumba mwenyewe hata
hujamjua!” “Atakuwa ni yule mzungu tu. Wewe hukuwaona hapa walivyokuwa
wakiangaliana? Yule mzungu alimpakulia chakula Tunda. Wewe hukuona? Atakuwa ni
yeye tu. Eti Tunda mdogo wangu?” “Ni yeye.” Yule mama akaendelea kushangilia.
“Afadhali tutapakata vitoto vya kizungu.” Tunda
akacheka sana. “Sasa wewe Penny mwanangu utakuwa msimamizi wa nyuma. Kazi yako
kuangalia shela ikae vizuri.” “Sasa nikikaa nyuma, kwenye picha si sitatokea!?”
“Utatokea kwenye harusi yako.” Mama yake akamjibu na kufanya wote wacheke.
“Mama Penny naomba ukae chini bwana tuongee.”
“Tunaongea nini? Hapa ni mipango ya harusi tu.” “Si ndio hivyo sasa! Mimi
nilijua wewe ndiye utakuwa mpambaji wa ukumbi na Mchungaji ndiye atatufungisha
harusi.” “Aka! He! Wewe Tunda ukoje? Mimi na mume wangu ndio wasimamizi.
Akitaka mwenyewe atafungisha hiyo ndoa, halafu atachukua nafasi yake ya kumsimamia
bwana harusi tukitoka kanisani. Lakini mimi nasimamia kila mahali.” Tunda
alitingisha kichwa huku akicheka.
“Sasa nani atapamba ukumbi!?” “Mimi na wewe haituhusu,
kwani sisi wanakamati bwana? Hebu tuongee mambo ya msingi.” “Haya Penny na
mdogo wako, mkalale.” Baba yao akaingilia. “Lakini mimi sitaki kusimamia nyuma,
dady!” Penny akalalamika. “Mama yako ameshakwambia, utulie mpaka utakapokuwa
mkubwa, ukileta mchumba wako, siku yako ya harusi utasimama mbele. Sasa hivi
unakwenda kulala, kesho shule. Haya simama haraka kabla sijakubadilikia.” Tunda
akabaki akicheka, Penny na mdogo wake wakasimama kuelekea chumbani kwao kulala
huku Penny akilalamika “Na mimi nataka kutokea kwenye picha! Sitaki kusimama
nyuma.” Akapotelea chumbani kwao huku akilalamika.
“Kweli hawa watoto wamepata wazazi!” Tunda
aliendelea kucheka. Waliongea kwa muda mrefu sana, Tunda akitoa historia yake
na Net, tena na tena huku machozi yakimtoka. “Ulikuwa unamzungusha Julius wa
watu, kumbe unaye mwanaume wako!” “Mungu wangu nishahidi mama Penny. Sikuwahi
kumfikiria Net kuja kuwa naye kwenye mahusiano hata kidogo! Hata dunia yote tungebaki mimi na yeye tu,
pia nisingefikiria kama yule kaka angekuja hata kutamani niwe mpenzi wake!
Sikuwahi hata kumuhisi. Net anamaadili na msimamo wakupita kiasi. Kwanza
nilikuwa nikimuogopa ile yakutetemeka.” Waliongea mpaka usiku sana, ndipo Tunda
aliporudi kwake.
Kwa
Net!
Huku kwa
Net nako, alirudi mpaka nyumbani kwao. Alimkuta mama yake sebuleni akisoma
kitabu. Alipomuona tu Net akaweka kitabu chini. “Sijawahi kukuona ukiwa na
furaha hivyo! Kuna nini?” “Tunda amenikubali mama.” “Hebu tulia kwanza. Tunda
amekukubali!?” “Yaani ni hivi, Tunda amekubali nije kuwa mume wake.” Yule mama
alishtuka sana, akavua miwani. Net alimuona jinsi mama yake alivyobadilika.
“Tunda,
Tunda!?” “Ndiyo mama. Tunda.” “Sijaelewa. Tunda huyu unayemzungumzia ndiye
Tunda huyu Malaya! Aliyekwisha shika mimba ya baba yake. Aliyevunja uchumba
wangu na kuvunja ndoa ya Mzee Mati baada ya mkewe kujua alikuwa akihudumiwa na
huyo Tunda na kumpeleka na mwenzie Meto! Aliyetembea mpaka na Gabriel, ambaye
ni kama kaka yako!? Achilia mbali msururu wa wanaume za watu ambao alishakuwa
na mahusiano nao kimapenzi!?”
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Itakuaje? Tunda akiwa na furaha yakupitiliza, maisha ya nyuma yanapambana
kumtoa Tonge mdomoni
0 Comments:
Post a Comment