Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Nilipotea! - Sehemu ya 21. - Naomi Simulizi

Nilipotea! - Sehemu ya 21.

 


T

unda alichoka kabisa. Akidhani ile bibilia ingemtia hofu yule mzee, lakini ndio ikawa

njia moja wapo ya kumtongozea. Akageukia dirishani. Moyoni akaanza kumwambia Mungu, ‘Nilikuomba unisaidie nisirudi huko tena, lakini mtu wa kwanza unanikutanisha naye baada ya maombi, ni huyu! Ni njia gani hii unatumia kunisaidia? Unanikutanisha na mtu kama huyu ambaye anauwezo wa kunipa msaada wa vitu unavyojua wazi ndio ninahitaji kwa sasa! Kwa nini hunihurumii? Nimeteseka miaka yote, ndio kwanza nafurahia utulivu nilio nao. Umenipa furaha na amani, kisha unachukua kila kitu kwa wakati mmoja! Umechukua kazi yangu, umenifukuza pale kwenye ofisi, halafu unaniletea mtu wakunisaidia kurudi kwenye yale yale maisha niliyokwambia siyataki!’ Tunda aliendelea kumlaumu Mungu kwa kunung’unika moyoni.

Akapitiwa na  usingizi, mpaka aliposhtuliwa na yule Mzee kumwambia ashuke wakale. Tunda akakataa. “Asante, lakini sitakula.” “Kwa nini?” “Nataka nipate muda wa kuongea na Mungu. Wewe nenda tu.” Yule Mzee alimtizama Tunda kwa muda mrefu kidogo, kisha yeye akashuka.

Alibaki peke yake kwenye basi, akafunga dirisha ili kupunguza fujo za watu wanaotaka kumuuzia vitu. Akainama nakuanza kuomba upya huku akijiuliza yeye mwenyewe maswali na huyo Mungu aliyetambulishwa na Net. Tunda aliomba huku akilia kwa hofu ya itakuaje. Akaendelea kumsihi Mungu asimjaribu zaidi. Alijua wazi mshahara aliolipwa na pesa nyingine alizonazo, haziwezi kudumu kwa muda mrefu.

Alifikiria wapi pakwenda mara baada ya kushuka kwenye hilo basi! Nini chakufanya mara baada ya kujua pakwenda! Yule mama alikuwa sahihi kabisa, hakuwa na cheti. Kama pale kwenye ile ofisi aliweza kufanya kazi vizuri, wakaona utendaji kazi wake na bado wakataka vyeti, nani atampa kazi bila vyeti wakati hawamfahamu? Maombi ya Tunda yalichanganyikana na maswali mengi sana. Alibaki ameinama ili aombe, akajikuta haombi tena anawaza tu.

 Tunda na fundisho la watoto njiani.

Aliamua kukaa vizuri na kugeukia dirishani aendelee tu kuwaza. Aliona watoto wadogo wawili wakicheza wakati mama zao wakiuza matunda. Mtoto mmoja alikuwa mkubwa kidogo kwa mwenzake. Yule mtoto mkubwa alikuwa na gari alilokuwa ametengeneza vizuri sana kwa vijiti, alivyovipangilia kwa ustadi, mpaka akatengeneza muundo wa gari. Akaweka matairi ya mifuniko ya soda{Visoda}. Tunda alimuona jinsi alivyokuwa akiendesha lile gari pembeni ya mama yake, akienda mbali kidogo na kurudi, lakini si mbali na macho ya mama yake.

Mtoto wa pili, yule mdogo, alikuwa akichezea vumbi tu, mwishowe yule mdogo akamuomba yule mtoto mwenye gari ampe achezee na yeye. Bila tatizo, akampa.

Yule mtoto mdogo, alionekana kufurahia zaidi lile gari kuliko mtoto mkubwa ambaye ni mmiliki. Alitoa milio mbalimbali kwenye mdomo wake kuonyesha akiigiza mlio wa magari ya kweli, kitu kilichomvutia Tunda na kuanza kucheka na kujikuta akifungua dirisha na kuendelea kumtizama yule mtoto aliyeazimwa gari. Alitoa mlio wa honi, kuweka breki kwa nguvu, huku akiendelea kucheza na gari ya mwenzake.

Mwenye lile gari alipoona yule mwenzake anafaidi na gari yake zaidi yake, akaamua ampokonye, tena kikatili, kwa jeuri kwa kuwa lilikuwa lake. Tunda akashtuka kwa kumuhurumia. Ulizuka ugomvi kati yao, lakini mwishowe mwenye nacho alishinda baada ya wazazi kuingilia kati.

Yule mdogo alianza kulia sana, akitaka lile gari ambalo halikuwa lake. Na yule mwenye nalo akaanza kuchezea kama yule mdogo alivyokuwa akifanya. Alitoa milio ileile, na alifanya zile zile mbwembwe kama mwenzake alivyofanya lakini haikupendeza hata kidogo. Mwishowe akaigiza kuweka breki kama yule mtoto, lile gari liligonga jiwe na kuharibika kabisa.

Lakini kabla ya lile gari kuharibika. Wakati yule mkubwa akiendelea kuchezea gari lake, yule mdogo aliacha kulia, akaokota boksi la biskuti, akatumia meno yake kutengeneza madirisha na mlango. Kisha akaokota pale pale vijiti vile vya kutolea uchafu kwenye meno ambavyo watu walisha tumia na kutupa tu. Akaunganisha kadhaa ili viwe virefu na vigumu. Akatoboa sehemu ya kuchomeka matairi, akaweka vile vijiti. Tunda bado akiwaangalia tu. Yeye ndani ya basi, wale watoto nje pembeni kwa mama zao, na wao wakiongea yao na kubembeleza wateja.

Kwa kuwa yule mtoto mdogo hakuwa na visoda, au mifuniko ya chupa za soda, yeye aliweka makaratasi magumu kidogo ndio yakawa matairi yake. Akaokota tena kijiti au mti mdogo, lakini mrefu na mwembamba akachomeka nyuma ya lile boksi, iwe kama usukani wake wakuongoza lile gari. Tayari akawa ametengeneza gari zuri tu, tena kwa muda mfupi, akaanza kuliendesha.

Wakati ndio analifurahia gari yake hiyo, ndio mwenzake akapata ajali na yakwake, ikaharibika. Kwa hiyo akabaki yule mdogo ambaye alinyang’anywa gari, akiwa na lake. Tunda alimuona yule mdogo akicheka sana. Akimcheka mwenzake, yule mkubwa aliyekuwa amekaa chini hana tena gari. Lilikuwa ni tukio la muda mfupi tu, lakini lilichukua akili za Tunda zote na kumfanya atulie na kutafakari.

            Basi lilianza kuondoka huku bado Tunda akiwawaza wale watoto. Alijiambia ni ujinga kuwaza jambo la kitoto kama lile, lakini bado akili ilimrudisha pale kwenye wale watoto. Akasikia swali mayoni mwake, Kama yule mtoto asingepokwanywa lile gari, je angepata wazo la kutengeneza gari lake?’ Tunda alifikiria kidogo akaamua kujijibu. ‘Lakini kweli! Afadhali alivyopokwanywa akapata akili ya kutengeneza gari lake.’ Tunda akajijibu. ‘Lakini alilia sana!’ Tunda akawaza kwa kumuhurumia yule mtoto.

             Likapita swali jingine. ‘Kama angeendelea kulia pale alipokuwa amekaa pembeni ya mama yake, bila kusimama na kuchukua hatua ya kutengeneza gari lake, angepata gari jingine?’ Tunda akafikiria na kukumbuka lile tukio tena. Alikumbuka jinsi mama yake alivyokuwa akimbembeleza kwa kumpa matunda ili atulie lakini yule mtoto alikataa kata kata, aliendelea kulia akitaka gari ya mwenzake mpaka alipoamua kunyanyuka na kutengeneza gari lake.

       ‘Afadhali alitumia akili. Angekubali tu kubembelezwa na mama yake akala yale matunda, angesahau kabisa kitu anachokita, gari. Akabaki hana gari mpaka sasa.’ Tunda akajijibu na swali jingine likamjia tena. ‘Kwani angekubali faraja ya mama yake, akaacha kutengeneza gari yake, ingeondoa ujuzi alionao wakutengeneza gari?’ ‘Hata kidogo. Si angekuwa ni mjinga tu, amekataa kutumia ujuzi wake na kubaki akililia gari la mwenzake!’ Tunda akajibu haraka haraka tena kwa hasira.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya hapo Tunda akapitiwa na usingizi, kisha akashtuka sana. Ikawa kama kitu kimemuamsha huko usingizini “Mimi ni mjinga sana, hata yule mtoto anaakili kunizidi mimi!” Tunda akamwambia yule Mzee na kumuacha akimshangaa. “Sipo hata nusu ya yule mtoto!” Tunda akarudia kumsisitizia yule Mzee, lakini yule mzee aliyekuwa amekaa pembeni yake akamtongoza, alijua Tunda anaota kwa kuwa alikuwa amelala. “Binti, punguza sauti. Ulikuwa umelala, na hapa tupo kwenye gari.” “Hapana sioti.” Watu wapembeni yao waliwageukia na wa mbele pia waligeuka kwani Tunda alikuwa akiongea kwa sauti iliyojaa kufunguka kimawazo.

“Ni kweli yule mtoto ana akili sana. Sikiliza nikwambie hiki kisa, kimetokea sasa hivi mliposhuka kwenda kula.” Tunda akasimulia kile kisa chote cha wale watoto na kuvuta masikio ya abiria wengi sana ndani ya lile basi. “Nisikilize vizuri. Mimi nimetoka Arusha sasa hivi sababu ya kufukuzwa kazi ambayo niliifanya vizuri sana. Sikuwahi kuiba, wala kukosea hata siku moja. Niliifanya kwa makini na juhudi zangu zote. Niliifanya ile kazi mpaka usiku bila kuomba malipo ya ziada.”

“Lakini leo asubuhi mwenye ofisi amemleta mtu mwingine, na kunifukuza mimi kazi kikatili, kwa kuwa tu sikuwa na vyeti.” “Kwa nini na wewe huna vyeti?” Yule Mzee aliuliza swali lililomfanya Tunda aliyekuwa akisimulia kwa kuchangamka apooze ghafla. Abiria wengine wakaongezeka kusikiliza. Maana wengi walikuwa wakisinzia mara baada ya kula chakula basi liliposimama. Ila kwa sauti ya kuchangamka ya Tunda, hata waliokuwa wamelala, wakaamka na kuendelea kumsikiliza Tunda aliyegutuka baada yakubaini ule mfano unamuhusu. Kwanza kwa sauti hiyo ya Tunda, lazima utataka kuisikiliza hata ukiwa mbali, utageuka tu ili kutaka kuiweka kwenye sura husika. Kuiona sura ya hiyo sauti.

“Sikusoma baba yangu. Nilipata hiyo bahati ya shule lakini ilichanganyikana na majanga mengi yaliyonifanya nishindwe kusoma kabisa. Sikubahatika kulelewa na wazazi wote wawili. Nimekuwa nikihama hama huku na kule.” Tunda akaelezea kisa chake kilichowavuta watu wote sasa kwenye lile basi huku wakimuomba aongeze sauti. Akapiga magoti kabisa kwenye kiti chake, nakusimulia. Wazazi wengine walianza kumtukana mama yake Tunda, wengine bibi, wengine mama wa kambo wengine shangazi ilimradi basi zima pakageuka kukawa gumzo juu ya Tunda.

 “Lakini baadaye niliishi maisha machafu sana, mpaka nikakutana na mtoto wa huyu mama aliyenifukuza kazi.” Napo hapo Tunda aliwaacha midomo wazi. “Mmmh! Pole sana mwanangu. Dunia mzunguko! Inaweza kukufanya ukafanya jambo ambalo hata hukutegemea.” Mama mmoja mtumzima pembeni yake aliongea.

“Ndio muache kuwasema machangudoa. Hamjui kwa nini wanafanya wanayofanya.” Dada mwingine kiti cha mbele alidakia. “Ndio maana yake. Maana kuna watu wanapenda kweli kuhukumu watu.” Mwingine akadakia. Abiria wengine wakawageuzia na wao macho kuwasikiliza na wao wakizungumza kwa jazba.

“Lakini mimi Mungu amenipa nafasi nyingine. Mtoto wa huyo mama alinirudisha kanisani, nikatubu, Mungu amenisamehe. Nilitolewa majini kwa mapepo kwenye huu huu mwili watu waliokuwa wakiutamani na kutumia. Wasijue walikuwa wakilala na majini pia. Anyways, baada ya yote, huyo kijana akanipa na hiyo kazi niliyopokonywa.” Tunda aliwakata maneno.

“Bahati yako wewe ulimpata huyo kijana. Sasa unakuta ndio kama hivyo mtu hana maisha, leo unamwambia aache uchangudoa, unataka aishije? Wewe umepata kazi, ndio maana umeacha.” Huyo dada aliongeza, kila mtu alihisi yule dada na yeye ni changu.

“Lakini nisikilize dada, nakwambia leo nimefukuzwa kazi. Hapa nilipo naelekea Dar, sina pakwenda, sijui chakufanya na wala simfahamu mtu yeyote huko Dar japo nimeishi kwa miaka mingi na nilikuwa na kwangu tena pazuri, kama nilivyowasimulia. Nipo kama hivi mnavyoniona.” Tunda akaendelea akiwa amejawa nguvu hata asijue amewezaje kuzungumza vile bila woga.

“Mlipokuwa mmeenda kula nilibaki humu ndani nikilia, ndipo nikaona kisa cha hawa watoto. Nikikwambia kulia, nilianzia kulia kule hotelini. Lakini huu mfano wa huyu mtoto mdogo, umenifundisha au unanihusu. Huku kulia kutanichelewesha na mimi kupata changu. Kurudi kuwa Changu ni kama nakubali faraja ya matunda ya muda mfupi, itakayonifariji kwa muda mfupi tu, nakusahau nini nataka katika maisha.” Tunda akaendelea.

“Lazima nisimame na mimi nitengeneze chakwangu. Hata kama sijasoma, na mimi nitaanza kwa kuokota maboksi, vijiti vyakutolea uchafu kwenye meno ambavyo watu wanatupa, nitatengeneza gari yangu kama yule mtoto.” Kisha akauliza swali. “Kwani huyu aliyetengeneza hili basi tulilopanda sasa hivi, si binadamu kama sisi tu? Alikubali kuacha vishawishi vyote, akajikana na kukaa chini, akaunganisha vyuma na mipira mpaka tukaliita basi.”

“Basi na mimi nitatafuta cha kwangu. Sitaki kulia tena wala kumchukia mtu. Nitajichelewesha kupata vyangu.” Tunda alishangaa kuona watu wote kwenye basi wakimpigia makofi. Alishtuka sana, kwani bado alikuwa amepiga magoti kwenye kiti chake akiongea kwa sauti na yule dada kwenye kiti cha mbele  kabisa aliyekuwa akitetea uchangu. Akawa kama ameshtuliwa, akarudi kukaa vizuri na aibu ya ghafla usoni.

“Unaakili binti. Nakupongeza.” Yule mzee aliyemtongoza na kumpa wazo hata lakumtafutia hoteli akajikuta akimpongeza tena Tunda. Lakini kwa sauti ya chini iliyojaa aibu kidogo na kujirudi. “Asante.” Tunda akacheka taratibu. “Na naomba nikuombe radhi.” “Wala usijali baba yangu. Ulikuwa mtihani wangu huo. Mungu alitaka kunipima, ajue nimeamua vipi kutorudi nyuma. Pale uliponiambia vile, ukaniona nimegeuka dirishani, nilikuwa nikimlilia Mungu aniepushe na watu kama wewe. Kwa kuwa ndivyo nilivyoanza kazi ya uchagudoa hivyohivyo.”

“Nilitoka hospitalini nikiwa sijui pakwenda. Wakati nimeenda kula mahali, nikakutana na mmiliki wa hilo eneo. Ndiye niliyeanza naye hiyo biashara. Akaniweka hotelini kama vile ulivyonishawishi mwanzo. Sasa na wewe ulivyonitongoza, na ahadi ya pakuishi, niliumia sana. Nikakumbuka niliingia kwenye ule uchafu mwanzoni kabisa sababu sikuwa na pakwenda. Sasa nikaona historia inataka kujirudia tena. Inakuwa vile vile na sababu ile ile. Ila nimekusudia baba yangu, sitarudi nyuma. Hata kama nitalala stendi ya mabasi, acha nihangaike tu mpaka nione mwisho ni nini.” Yule mzee alijisikia vibaya sana, na dhamira ikamsuta.

“Binti naomba unisamehe sana. Nimepitiwa na shetani tu.” Tunda akacheka. “Yameisha baba yangu.” “Ila kile chumba nilichokwambia ni kweli kilikuwepo, ila sijui kama dalali alishapata mteja! Kama upo tayari kuishi maeneo ya Temeke, naweza kumpigia simu yule dalali ili asikikodishe tena ili wewe ukaishi huko.” “Kodi ni kiasi gani?” “Yule mzee akamtajia.” Tunda akafikiria kidogo.

“Naomba nikulipe ya miezi mitatu wakati najipanga upya.” “Nitaongea na mke wangu tuone, maana ndio nyumba anategemea sana yeye.” “Unaweza kuwasiliana nao hao watu wawili ili mpaka tukifika Ubungo kituo cha mabasi, niwe najua kama nimepata au nihangaike kwingineko?” “Sawa.” Yule Mzee akakubali.

Alimpigia simu dalali, dalali akamwambia ndio ametoka kumpeleka mtu na mkewe hapo kwenye hicho chumba, wamepapenda na wamekubaliana kesho awapeleke kwa mke wa yule Mzee wakaandikishiane mkataba. “Basi hebu usubiri kidogo, usikikodishe kwanza niongee na mke wangu.” “Wanalipa kodi ya mwaka Mzee.” “Naelewa. Lakini hebu subiri.” Akakata simu.

“Vipi? Amesemaje?” Tunda akauliza kwa wasiwasi kidogo. “Anasema amepata mteja, tena mwenye kodi ya mwaka. Ngoja nimpigie simu mke wangu kwanza kabla hajawakodisha.” Tunda akakosa raha. Akabaki kimya.

“Mimi nitalipia hiyo kodi ya huyu binti.” Tunda akashtuka sana. Akamgeukia huyo aliyesema. Alikuwa ni kijana tu. Alikuwa amependeza, akaonekana nadhifu, kijana aliyefanikiwa. Shingoni alikuwa amevaa cheni aliyofanya juhudi za makusudi kuonekana. Ilikuwa dhahabu. Tunda muelewa vitu vya thamani, aliweza kutambua uhalisia wa ile cheni shingoni kwa yule kaka. Na saa nzuri sana tena ya thamani. Alikuwa amekaa kiti cha nyuma kabisa. Watu wote wakamgeukia.

“Kwamba?” Yule Mzee akauliza kutaka uhakika kabla hajazungumza na mkewe. “Nimesema mimi nitalipa hiyo kodi ya mwaka mzima ya huyo binti. Kama kumtia moyo kwa maamuzi magumu anayofanya.” Tunda aliogopa sana. Hakutaka kuja kudaiwa mapenzi baadaye. “Na wala hizo pesa hutazipata kwangu, utazikuta kanisani kwetu. Nitamkabidhi mama Mchungaji wetu. Utakapokuwa tayari, ukiipenda hiyo nyumba, wewe njoo kanisani kwetu utachukua pesa yako. Hata kama hutaipenda hiyo nyumba, tafuta nyingine, ila ujue pesa ya kodi ya mwaka mzima unayo tayari.” Tunda alianza kulia kwa furaha.

“Sikilizeni jamani.” Yule kaka akasimama. Akaanza kuongea mambo ya Mungu. Watu walikuwa wakimwangalia bila kupepesa macho. “Huyu Mungu yupo na wakovu ni halisi. Ukubali ukatae.” Yule kaka alianza kwa kusema hivyo.

“Wengine tumeua, tukauza madawa ya kulevya, tukavunja majumba ya watu, tumepita humo magerezani kama watu wanavyokwenda dukani kununua sukari, mpaka Mungu alipoingilia kati. Huyu dada anachoongea mimi namwelewa kabisa. Kuna mahali unapitishwa na maisha, msaada uliobaki pekee nikusalimisha maisha kwa Yesu. Ni uamuzi mgumu, lakini unalipa sana baadaye unapoamua kukubali nakubadilika.” Yule kijana akaendelea.

“Mimi nilipokubali kuokoka, nilipoteza kila kitu mpaka mke alinikimbia jinsi nilivyofilisika. Tena akaolewa na mwenzangu tuliyekuwa tukifanya naye biashara zetu za magendo. Nilirudishwa chini kabisa, nikawa masikini, omba omba. Nilikuwa na sababu zote zakurudi kufanya niliyokuwa nikifanya kwa kuwa nikweli nilikuwa nikitengeneza pesa ya haraka, lakini sikuwa na amani niliyokuwa nayo kama baada yakumpa Yesu maisha.”

“Wengi walinicheka na kuniambia nimepotea njia, lakini nilijua hawajui vile ninavyojisikia moyoni. Nilirudi kuosha magari Ubungo, mpaka nilipopata wazo lakurudi migodini kutafuta madini. Sikuwa na maandiko mengi kutoka kwenye bibilia, na nilikuwa mchanga sana Kiroho, lakini nilikuwa nikimkumbusha Mungu kuwa ‘fedha na dhahabu ni mali yake.’ Na mimi ni mali yake, nikawa nikimuomba Mungu anikutanishe navyo. Basi kila nilipokuwa nikizama kule machimboni nilikuwa nikimkumbusha Mungu hayo maneno. Ilinichukua miaka miwili migumu ya shida, nikiwa kule kwenye machimbo ya dhahabu, mpaka nikafanikiwa. Na mimi sasa hivi namiliki sehemu yangu huko.”

“Nilipochelewa ndege leo asubuhi, na kukosa gari ya kukodi kunipeleka Dar, nilipata amani sana yakupanda hili basi, kwani imekuwa muda mrefu, tokea nipande basi. Nimefurahi sana kukutana na huyu dada. Na inawezekana lilikuwa kusudi la Mungu ili nikutane na Tunda. Mungu akubariki sana dada yangu.” Akamtizama sasa Tunda, maana alikuwa ni kama anazungumza na basi zima.

“Hakuna sababu yeyote itakayokufanya kuishi kwenye dhambi na ikawa sawa. Hakuna. Hata ukijitetea vipi, hakuna. Dada Tunda nakuombea Mungu akutie nguvu, umeanza hii safari si rahisi, lakini Mungu hatakuacha, na kwa kuwa umefunguliwa ufahamu wako mapema, naona hutapata shida kama wengine.” Yule kaka akaendelea.

“Tatizo la wana wa Mungu wengi ni pale tunapoonywa na kukataa kubadilika. Au pale tunapoonyeshwa njia, tunakataa kufuata njia ya Mungu, na kutengeneza njia zetu. Tunachelewa na wakati mwingine hatufiki kabisa. Tunakubali faraja kama wewe ulivyosema. Faraja ya matunda, nakusahau vitu vikubwa tunavyotaka. Kama Mungu amekwambia akota boksi la biskuti utengeneze gari, okota na tengeneza. Acha ubishi, huwezi kujua katika kuinama huko, utaokota nini kingine!”

“Wengi wanapenda kuletewa wakiwa wanaomba Mungu. Haiwi hivyo kabisa. Muujiza wako uko pale unaponyanyuka na kuchukua hatua. Pengine yule mtoto asingekubali kutengeneza gari yake, ungekuta bado analia mpaka sasa, na asingegundua mbali ya vijiti, hata boksi pia linaweza kutengeneza gari. Tusibaki kung’ang’ania vya watu. Tutafute vya kwetu.” Yule kaka aliongea kwa mifano huku akisema maandiko kwa kichwa kitu kilichomshangaza sana Tunda.

‘Mwenzangu anaonekana amekaa kwenye wokovu muda mrefu! Anauwezo mkubwa wakusema maandiko ya bibilia bila kusoma!’ Tunda aliwaza. Alishangaa uweza wa kuchanganya kila analoongea na neno la Mungu. Ilimtia moyo sana Tunda. ‘Kweli huyu Mungu ana watu wengi! Wengine wanampenda na kuishi kwa dhati, wengine wanacheza. Ni uamuzi wako wa kuamua uishije naye.’ Tunda aliendelea kuwaza wakati yule kaka akizungumza mpaka akamaliza na kurudi kukaa nakuacha watu wote kimya kila mtu akitafakari lake.

Walipofika Ubungo, yule kijana akamsogelea Tunda, akampa kadi yenye mawasiliano ya Mchungaji wake. “Kuanzia kesho ukimpigia simu atakuwa na pesa yako. Mungu akubariki sana, na kamwe usirudi nyuma.” “Asante sana kaka yangu.” Yule kaka alikuja kufuatwa na gari nzuri ya kisasa, akaondoka. Tunda alibaki ametoa macho. Alipokea muujiza wake bila kutarajia.

Maisha yamrudisha Tunda Jijini Dar, Na bila kutarajia, katikati ya Jaribu kali, pakatokea mlango wake wakutokea.

Tunda hakutoka hata hapo kituoni Ubungo. Akaenda kwenye ile hoteli pale pale ndani ya Ubungo. Alishalala hapo na baba Tom, kwa hiyo alipafahamu. Akachukua chumba hapo. Kulikuwa kumejaa kumbukumbu ya mambo mengi aliyoyafanya humo ndani ya hiyo hoteli na baba Tom, lakini ikawa siku hiyo nayo amemuona Mungu. Akatulia kwa muda akiwa amekaa kitandani tu. Asiamini yupo hapo na hata siku hiyo, katikati ya jaribu gumu, lakini hana mtu anayetakiwa kumuhudumia kimapenzi ili kupata pesa.

Akajisiki machozi yakianza kumtoka. Akaamua kupiga magoti na kumshukuru Mungu huku akilia. Alikaa kwa muda mrefu magotini akilia mbele za Mungu wake, akaishia kujiambia hataweka kitu mdomoni mpaka mambo yake yakae sawa. Mpaka aushuhudie muujiza wake kwa macho. Ni kama aliamua kufunga.

Siku inayofuata, aliamua kutafuta sehemu ya kulipia ya kupiga simu. Akampigia simu huyo Mchungaji ili kujua kama kweli kuna pesa au la. Mchungaji akamwambia ni kweli mkewe alipewa pesa na kupewa maelekezo amkabidhi yeye. Tunda alifurahi sana. Kilichofuata ni kwenda kuona hicho chumba. Yule mzee wa kwenye basi mwenye nyumba alimpa namba yake ya simu na ya dalali. Alishazungumza na dalali, akamwambia atamsubiri Temeke hospitali ndio kituo atakachokitumia kufika kwenye hiyo nyumba.

Bila kupoteza muda, Tunda akiwa ameacha mizigo yake hapo hotelini, akapanda daladala mpaka Temeke kuona hicho chumba. Na kweli, aliweza kumtambua huyo dalali kwa nguo alizomwambia atamkuta nazo, kwa kuwa Tunda alimwambia hana simu, amwelekeze alivyo ili asimpotee. Akamchukua kutoka hapo kituoni mpaka kwenye hicho chumba. Tunda akaridhika nacho.

Akapapenda, akamuomba yule dalali atumie simu yake. Tunda akaongeza muda wa maongezi, akampigia tena simu yule Mchungaji, akampa namba ya simu ya mkewe. Tunda akampigia simu mke wa Mchungaji, yule mama akaamua amfuate.

Baada ya muda kama wa lisaa, alishangaa gari nzuri sana, SUV nyeupe, kubwa, imevimba vizuri, ikasimama mbele kidogo kituoni, pale pale Temeke hospitalini kama walivyokubaliana. Tunda na yule dalali wakamuona mwanamke akishuka kwenye hiyo gari. Alikuwa mtanashati, wakisasa. Akajitambulisha na kumwambia yeye ndiye waliyekuwa wakiongea naye kwenye simu, akamwambia wengi wamezoea kumwita mama Penny. Tunda akamsalimia na kujitambulisha na yeye.

Yule dalali akawapeleka kwa mwenye nyumba. Hakuwa akiishi mbali na hapo. Mama mchungaji akalipa ile kodi yote, Tunda akakabidhiwa funguo.

“Una kitanda?” Mama Penny akamuuliza wakati akimrudisha Tunda hotelini. “Ndiyo. Nina kila kitu, lakini nimefungia mahali. Itabidi kesho nitafute gari nihamie kwangu.” “Usiwe na wasiwasi, nitawatuma vijana wa pale kanisani na gari ya kanisa ikusaidie kuhama.” Tunda hakuwa akielewa kinachomtokea.

Akamgeukia mama Penny. “Nakushukuru sana dada yangu. Mungu akubariki. Asante kwa kila kitu.” “Karibu.” Alijibu kwa ufupi tu. Akamshusha hapo hotelini Ubungo, akaondoka na kumuacha Tunda na funguo za chumba chake na sebule.

Ile furaha ikageuka kilio kwa Tunda. Alilia Tunda, asiamini kama Mungu amemrudishia kwake. Kwa Tunda huo ulikuwa ni muujiza wa kama kumfufua maiti. Ilikuwa ni zaidi ya kuponywa. Historia yakufukuzwa kwenye majumba ya watu, kwa Tunda, haikuacha kujirudia.

Ametoka kufukuzwa kwenye nyumba ya watu Arusha. Mama Cote alimtoa nyumbani kwake usiku. Akampokonya chumba alichopewa na Net, funguo za gari na kazi. Anampa nini huyo Mungu kumfungulia mlango mkubwa kama huo! Tunda alilia, asijue nini chakusema mbele ya huyo Mungu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kesho yake asubuhi alipigiwa simu na mtu wamapokezi kuwa anamgeni pale mapokezi. Alipotoka alishangaa kukutana na mama Penny na vijana. “Uliamka salama?” “Ndiyo. Japo sijala.” “Sasa itabidi ujikaze. Nimewakamata hawa vijana wakusaidie kuhama kabla siku haijaanza, wakakimbilia kwenye majukumu yao. Wakishakuhamisha ndipo tutatafuta sehemu ya kula.” “Sawa. Nashukuru sana.” Tunda akachukua mizigo yake yote aliyokuwa nayo pale hotelini, wakaweka kwenye gari ya mama Penny. Akalipia kile chumba, wakaondoka pale.

Tunda alikuwa kwenye gari ya mama Penny, na wale vijana walikuwa wakiwafuata nyuma kwenye gari kubwa kidogo, aina ya Kenta. Walitoka hapo Ubungo kuelekea Salasala nyumbani kwa Net alipokuwa ameacha vitu vyake.

Walipofika pale, akawaambia wasubiri nje akagonge kwanza. Aliwaambia hiyo nyumba inalindwa na mbwa mwenye mafunzo ya kijeshi. Ndiye Max. Tunda alishapewa habari za Max. Net alikuwa akimsifia sana huyo mbwa. Alikuwa akisema kwa huyo mbwa mmoja tu kulinda hiyo nyumba yake, ni sawa na kulindwa na askari watatu wa kimarekani, tena waliokwisha kwenda kupigana vita huko Iraq. Huyo Max alikuwa akihudumiwa nakutunzwa kwa hali ya juu.

Tunda aligonga kengele nje ya geti, baada ya muda Emma akatoka. Wakasalimiana, akamwambia bado Net hajarudi nchini. Akamweleza kuwa amefika hapo na wale watu kuchukua baadhi ya vitu vyake. Emma alikwenda kumfungia Max, ndipo akarudi kufungua geti na ile sehemu alipohifadhiwa vitu vyake.

Kutokana na ile sehemu kuwa ndogo sana, ilimbidi Tunda kuchukua vitu baadhi, vingine akaacha pale pale. Emma alivifunika vile vilivyobaki kama mwanzoni ili visiingie vumbi, wao wakaondoka. Huku Tunda akiviambia vitu vyake vilivyobaki pale kwenye stoo ya Net, ‘ipo siku tutarudi kuwa pamoja. Nipeni tu muda.’ Roho ilikuwa ikimuuma sana Tunda. Ni kweli alikuwa na vitu vizuri. Hata wale vijana waliokuwa wakimsaidia kubeba, walisifia na kuongeza umakini kwenye kubeba.

Walimrudisha mpaka Temeke kwenye chumba chake, wakamsaidia kupanga vile vitu, kisha wale vijana wakaondoka. Tunda alikuwa akicheka sana jinsi wale vijana walivyokuwa wakitaniana na mama Penny. Walionekana wamezoeana vizuri. Yule mama alipohakikisha Tunda ameweka kila kitu chake vizuri, alimchukua mpaka nyumbani kwake Tabata.

Walimkuta dada wa kazi, akiwa anaandaa chakula cha mchana. Na yeye yule mama akaingia jikoni nakuanza kumsaidia yule dada huku akimuuliza maswali Tunda. Baada ya muda mfupi sana, Tunda akajisikia yupo nyumbani. Mama Penny alikuwa mcheshi wakupitiliza.

Mchungaji naye akaingia. “Wewe siulikuwa ukicheka kila ninaloongea? Sasa kaja mwenyewe, utapasuka mbavu.” Tunda alikuwa akicheka sana. Mchungaji na mkewe walikuwa kama ni mtu na rafiki yake. Walitaniana kwa kila kitu.

“Hivi kuna wakati huwa wanakuwa serious hawa?” Tunda alimuuliza msichana wa kazi.  “Mmh! Sikumbuki. Labda wakiwa kanisani kidogo, lakini watu wameshawazoea. Mtakaa mkicheka hapa, mpaka mnaenda kulala. Hawaishiwi maneno hao na vituko.” Tunda alikaa hapo mpaka usiku akarudishwa kwake na yule mama.

“Kesho unaratiba gani?” Yule mama akamuuliza Tunda kabla hajashuka. “Bado natafuta kitu chakufanya.” “Sasa mimi ninafanya kazi ya kupamba kumbi za sherehe. Kesho nina kwenda kupamba ukumbi mahali. Kuliko ukae tu nyumbani, ni heri twende wote. Mimi sipendi watu wanaokaa kaa kihasa hasara, mwishowe shetani anapata nafasi ya kukupa kazi zake.” Tunda akacheka.

“Unafikiri nakudanganya? Shetani anapenda mijitu isiyo na kazi. Iliyokaa kaa tu haina kazi zakufanya, ndiyo anaanza kuipa kazi zakijinga.” “Basi tutaenda wote dada yangu.” Yule mama akacheka kidogo kama aliyefurahia utayari wa Tunda.

“Sasa mimi mambo yangu ni asubuhi ili jioni niwe na familia yangu. Kwa hiyo asubuhi nakuja kukufuata. Au unasemaje?” “Sawa kabisa.” Yule mama akacheka, akafungua loki ya mlango pembeni ya mlango wake, ndipo Tunda akaweza kufungua  mlango wake, wakaagana na kushuka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alianza kulia tena mara baada yakufika chumbani kwake, akapiga magoti pembeni ya kitanda chake. Alishindwa hata kumwambia Mungu asante. Alibaki amepiga magoti akilia. Moyo wake ulijaa shukurani sana mbele za Mungu. Nyumba ilikuwa nawapamgaji wengine wanne, wote walikuwa na familia kasoro Tunda. Ilikuwa uswahilini tu, tena wala si uzunguni kama alikokuwa akiishi karibu na baharini.

Uswahilini hapo ni kelele mida yote tena kitanda chake kiliwekwa pembeni ya dirisha alilokuwa akisikia kila kitu wapita njia wakizungumza nje. Choo anatumia na watu zaidi ya 15. Alishaambiwa kuna zamu za kusafisha sijui choo, uwanja na mambo mengi. Ni maisha ambayo hakuwahi kuishi binti huyo. Lakini alijawa na furaha ya aina yake. Alikubali yote bila shida. Furaha aliyokuwa nayo moyoni, ni kama alipewa jumba la thamani sana.

Alipanda kitandani kwake, asiamini kama amerudi kukilalia kitanda hicho alichokipenda na kukithamini sana. Aligaragara kwenye hicho kitanda akinusa hayo mashuka yake kwa furaha sana. Akaanza kuongea na vitu vyake kama binadamu. Akakumbuka kazi aliyoambiwa atafuatwa asubuhi asubuhi. Ikabidi alale haraka ili aamke akiwa na nguvu.

Tunda aanza Safari ya Kupata chake. Bila kujijua, kwa kutii agundua kipaji chake.

Aliamka asubuhi na mapema kuwahi kuoga kabla wengine hawajaamka na watoto wao, akachelewa. Akaoga na kuvaa akabaki kwenye kiti akimsubiria mama Penny. Akasikia mlango wa bati, mdogo tu wakuingilia ndani ukigongwa, akajua ni mama Penny. Akatoka akiwa amebeba na pochi yake, ni kweli alikuwa mama Mchungaji. Wakasalimiana, wakarudi kwenye gari na kuondoka. Na hilo likamfurahisha mama Penny, hakutegemea kumkuta akiwa tayari kwa kiasi hicho.

Waliongea mambo mawili matatu mpaka walipofika kwenye ukumbi wenyewe. Ulikuwa ukumbi wa kawada sana huko Mbezi ya kimara. “Si unaona hili liukumbi lilivyo baya? Sasa utaona nitakavyo pabadilisha mpaka wenyewe watashangaa.” Akajisifia yule mama. Wale wale vijana waliomuhamisha Tunda jana yake, waliingia na ile ile gari iliyomuhamisha Tunda siku iliyopita, ila safari hii ilibeba viti vya maharusi na mapambo. Walianza kushusha huku wakiendelea kutaniana.

“Leo mama wametupa godauni.” “Hilihili leo, mpaka paeleweke hapa! Masaa matatu tu, tunaondoka humu ndani. Nataka nikampikie mume wangu ugali wa bada. Mnaujua lakini bada au mnanitolea mimacho tu?” “Umeanza mama Penny.” “Kumbe! Ndio muoe muache kula magengeni! Wakati wenzenu wanaoa nyinyi mmekazana mnaomba. Mtaomba mpaka Yesu anarudi anawakuta bado mnaomba. Hebu njooni tuombeni kwanza ndio tuanze kazi.” Wote walikuwa wakicheka.

Tunda alikuwa akiwashangaa furaha waliyonayo na yule mama. Wakashikana mikono, wakaanza kuomba kwa pamoja ndipo wakaanza kazi. Walianza kazi kwa nguvu zote. Wale vijana wakijua chakufanya. Na kweli baada ya masaa matatu na nusu ule ukumbi ulibadilika kabisa. Walianza kupongezana. Mama Penny akawalipa pesa yao pale       pale wakaagana.

“Na wewe hii ndiyo pesa yako.” “Wala sijafanya kazi kubwa sana!” Tunda alitaka kukataa. Yule mama akambadilikia. “Huwa sipendi watu wajinga. Unanisikia Tunda? Kila mtenda kazi anastahili ujira wake. Au husomi bibilia wewe?” “Nasoma.” “Sasa!? Au maandiko ya bibilia yalisema kila mtenda kazi sana ndiye anastahili ujira? Acha kuzubaa! Mjini hapa. Kusanya pesa, jenga nyumba, nunu magari ya maana, uache kuishi uswahilini. Unafikiri nitakuwa nakuja kukuchukua kila siku?” “Hapana.”

“Ndio unatakiwa uchangamke, unasikia? Umelipiwa kodi mara moja tu, ujue inayofuata ni juu yako. Huwezi jua. Mara nyingine Mungu anatokea mara moja tu, na akitokea usiachie hiyo bahati. Sasa hivi unakusanya kila kinachoingia. Hata kama kidogo. Halafu huwezi jua hii ndiyo inaweza kuwa ajira yako. Au unaonaje?” Yule mama akamuuliza.

“Nimeifurahia sana.” “Basi jipe muda. Omba Mungu hizi tenda ziwe nyingi, ujifunze kwa haraka, na wewe uwe na yako kama hii.” “Kama hii tena, sio uniajiri?” “Wewe mtoto wa wapi lakini!?” Tunda alitulia kidogo. “Mbona neno ‘changamka hapa mjini’ ni kama hulielewi!? Wewe Dar yote hii unafikiri harusi leo zinafungwa ngapi, au kuna sherehe ngapi zinazotaka wapambaji?” Tunda akacheka baada ya kufikiria kidogo.

“Muone kwanza! Ushapata jibu eeh? Sasa ndio uchangamke haraka, jifunze, pata ujuzi halafu unachanganya miguu. Sio ukae hapa unasubiri ajira. Nikikufukuza kama yule mama wa Arusha? Unahama tena kuajiriwa kwengine? Hapo Mungu alikuwa anakufungua macho anakwambia uwe na chako! Shule sio kila kitu. Mwenzio nimesoma, lakini napamba maukumbi. Naingiza pesa nyingi tena kwa muda mfupi. Umeona kuna sayansi niliyotumia hapa? Ujuzi tu na utundu.” Akawa ni kama anamfungua akili zaidi Tunda.

“Asante sana.” “Asante kavukavu tu?” Mama Penny akamuuliza Tunda, akaanza kucheka tena. “Sasa nifanyaje?” “Ukipata tenda ya kwanza unaninunulia pafyumu nzuri. Sio zile zakuita nyuki au kuleta mafua.” Tunda aliangua kicheko zaidi, wakaondoka pale.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Yule mama alikuwa akifahamika sana. Kwa juma moja hakuacha kupamba kumbi si chini ya tatu. Kuanzia kichen party, send off, harusi, na kila shughuli zilizokuwa zikihitaji wapambaji, aliweza kupata yeye hizo tenda, mpaka alikuwa akikataa. Alikuwa akiingiza pesa nyingi kwa juma.

Kwa kuwa alikuwa na watoto wadogo na huduma ya kanisani, mara nyingi alimtuma Tunda kwenye vikao vya harusi kwenda kuonyesha picha za kumbi walizokwisha kupamba na kuongelea gharama. Baada ya muda mfupi kweli Tunda akaanza kuwa mwenyeji na mjuzi wa ile biashara.

Akajiongeza. Akatengeneza albamu nyingine. Akapangilia picha na bei vizuri. Ikawa rahisi kila akitumwa na mama Penny, anaonyesha picha na bei. Kwa muda mfupi Tunda akaonekana amefikishwa kwenye uwanja wake anaomudu. Yeye ndio mtoa ushauri kwa mama Penny, kitu kilichomfurahisha sana mama Penny. Lugha nzuri ya biashara akawa anayo. Hakuna alikotumwa kwenye vikao viwe vya harusi au kiofisi, akarudi bila hiyo kazi.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

 “Sasa tunaanza kugawana. Wewe unapamba huku na mimi napamba kule.” Tunda akaingiwa hofu. “Yaani bila wewe? Sitaweza peke yangu.” “Wewe mtoto vipi!? Hata watoto wachanga huwa wanaacha kunyonya. Ulipokuwa ukikubali kupokea kazi za watu, tena nyingi kwa tamaa, ulifikiria nini? Unataka tuongozane kama makondoo mpaka lini!? Kwanza mimi huwa sipendi kufuatwa fuatwa nyuma.” “Nikiharibu sasa?” Tunda alijawa na wasiwasi.

“Shauri yako! Mimi hainihusu. Itakuwa ni juu yako wewe na hao waliokupa kazi. Mimi nachukua ukumbi mmoja tena wakaribia na kwangu, nikimaliza kazi yangu nitakupigia simu bosi wangu uje ukague, ukiridhika nataka pesa yangu uliyolipwa.” Tunda akazidi kuchanganyikiwa.

“Sasa na ule ukumbi wa tatu nani atapamba?” “Kwani wewe ulivyochukua kumbi tatu, kwa siku moja, ulitegemea nini? Mwenzio nina mume na watoto. Kazi yangu moja tu kwa siku na wewe unajua. Ulivyochukua kazi zote hizo, ulifikiri nini?” “Jamani mama Penny!? Basi tufanye wote hizi zote halafu siku nyingine nitajipanga vizuri.” Tunda akabembeleza akiwa na hofu.

“Akuu wewe mtoto usinivunjie ndoa yangu. Baba paroko unamsikia Tunda.” Yule mama alimwita mumewe. “Atalijua jiji! Na akikutana na walevi lazima wamshushie kipondo kama ukumbi haujaisha kwa wakati.” Mchungaji na mkewe wakaanza kumcheka Tunda, huku wakikumbushiana visa vya kazi hiyo ya upambaji kama wahusika wanakuwa hawajaridhika na kazi.

“Sasa nitafanyaje?” Tunda akauliza akilalamika. “Omba funguo za ukumbini ukalale nazo kwako. Amka hata saa kumi za usiku, nenda kaanze kupamba. Tena nakupa Josh na Julius wakusaidie. Wote wale wachapa kazi. Ukiamka mapema kwenye saa kumi jioni, utakuwa ushamaliza kupamba kumbi zote mbili.”  Hilo likamfurahisha Tunda.

“Sasa mapambo?” Tunda akauliza tena. “Mapambo!?” Mama Penny naye akauliza kama anayemshangaa. “Nauliza mapambo nitapata wapi?” “Piga magoti uanze kuyaomba kwa Mungu. Utakuta Mungu kakushushia huko huko ukumbini yanakusubiri. Kila ukumbi atakuwekea mapambo yake. Anza kuomba.” “Jamani mama Penny!” Kila mtu akaanza kucheka mpaka msichana wa kazi jikoni.

“Kumbe! Wewe hujui hii ni nyumba ya Mchungaji? Hapauzwi mapambo hapa. Ushauri utakaopewa ni kuomba. Ukiona hapa unabanwa, rudi kwako kule uswahilini, kwenye kelele, kajifungie anza kuomba kwa kulia.” “Au piga magoti nikuwekee mkono Tunda.” Mchungaji akaongeza. “Jamanii!” Tunda akazidi kulalamika.

“Changamka Tunda. Mjini hapa!” “Basi naenda kununua vitu vyangu.” “Kumbe unaakili?” “Usafiri sasa?” Tunda akauliza tena. “Piga magoti Mchungaji akuwekee mikono ili mkimaliza kuomba, ulikute gari hapo nje linakusubiri.” “Jamani mama Penny wewe!” “Kwani wewe huamini nguvu ya maombi? Au hujasikia kama kuna miujiza?” “Naamini lakini si kihivyo!” “Basi changamka. Una siku tatu za kukamilisha kila kitu uingie kazini.” Tunda akaondoka.

Tunda aanza biashara yake ya kupamba.

Usiku huo hakulala. Akaanza kuandika kila kitu alichokiona kwa yule mama, ambacho alijua atakihitaji na yeye. Kesho yake asubuhi akaanza kuzunguka madukani akiwa na Julius ambaye ni mpambaji wa mama Penny na ni dereva wa ile Kenta.

Akaanza kununua vitu kama vile alivyoviona kwa mama Penny. Anamwita Julius, anasogeza gari, wenye duka wanamsaidia kupandisha vitu kwenye gari, Julius anamsubiri, yeye anazunguka madukani peke yake.

Viti vya kukalia maharusi ndivyo vilimtoa jasho. Alitaka kama vya mama Penny, ila bei ilikuwa kubwa. Akaanza kujishauri akikumbuka akiba ya pesa aliyokuwa nayo. Inamaana kazi yote tangia aanze kazi kwa mama Penny na ile aliyolipwa Arusha, itaishia hapo kwenye manunuzi! Akajishauri Tunda. Lakini alitaka awe anafanya kazi nzuri kama mama Penny. Ikabidi ajikaze tu, anunue kila kitu vile vile na vizuri zaidi, mpaka akaishiwa kabisa.

Walirudi nyumbani kwa mama Penny na mchungaji  Tabata akiwa na mizigo yote aliyokuwa amenunua Tunda. Tunda mwenyewe alikuwa hoi. Amechoka na ule weusi ukaongezeka kwa kupigwa na jua pamoja na vumbi.

          “Naomba unikopeshe pesa nikaongeze kwenye mapambo.” Mama Penny akaanza kucheka. “Umeshaanza kupata akili eeh? Safi sana. Sasa hapa kwetu kukopa ni mara  moja tu, na unalipa ndani ya juma moja. Ukizidisha siku saba unaanza kulipa na riba.” “Mama Penny jamani!?” “Haya nenda kakope kwenye mabenki.” 

“Haya basi nitakulipa nikilipwa baada ya kupamba.” “Hiyo ndio akili. Sasa uchangamke na siku za alhamisi na ijumaa hapa mjini pia kunakuwa na sendoff na Kitchen party. Zote hizo siku hakikisha unapata kazi.” “Si nitachoka sana!” Tunda akashangaa. “Sawa. Nenda kalale. Kwanza hivi umepaona nyumbani kwake?” Mama Penny akamuuliza mumewe.

“Hapana.” “Kama chumba cha mbwa! Hapafai.” “Jamani mbona pazuri tu.” “Kama pazuri mbona mizigo yako ipo hapa? Si ungetoka Kariakoo na kuipeleka kwako?” “Mama Penny wewe? Pale padogo halafu nahofia wezi.” “Sasa unakataa nini na unaongea nini hapa? Dari lenyewe limeshuka mpaka mlangoni! Yaani kuingia inabidi uiname na unakuwa kama unatumbukia ndani hivi. Tena kama wewe baba Paroko na miguu mirefu hiyo! Lazima uiname ndio uweze kuingia mlangoni, na ukifika ndani itakulazimu kukaa tu. Lasivyo utagonga dari.” Tunda alianza kucheka huku anatingisha kichwa.

“Nitahama bwana.” “Utahama bila pesa? Nakwambia fanya kazi kwa bidii. Unasema utachoka! Tena kesho kuna kazi nimepewa ni kupamba ukumbi wa tamasha, pale Mlimani City, sitaweza kwenda namsindikiza mume wangu kwenye huduma Morogorooo. Sasa itabidi uwahi ukapambe na hao vijana.” Tunda akachoka kabisa.

“Utaniua mama Penny! Mlimani City? Nikiharibu?” “Ndio utakuwa umeniharibia biashara. Na tunakuomba ule uondoke Tunda. Nina mazungumzo ya faragha na mume wangu.” Msichana wa kazi alikuwa akicheka muda wote.

“Sawa bwana.” “Na tunakupa miezi miwili tu, hakuna tena kutumia gari yetu kubebea vifaa vyako vya kupambia. Tafuta gari yako, mrembo. Mjini hapa, watu tunaishi kwa mahesabu. Hakuna kuomba chumvi kwa jirani.” “Gari!?” “Na hivyo vifaa vyako hapo stoo, kuanzia mwezi wa kumi na mbili utaanza kulipia hicho chumba.” “Jamani mama Penny wewe!?”

“Sitaki hodi za asubuhi asubuhi wakati unakuja kuchukua vifaa vyako ukapambe. Ni usumbufu Tunda.” “Si kwa muda tu!” “Muda wenyewe ndio nakwambia mwisho ni mwezi wa kumi na mbili. Kwa hiyo wakati unapumzika huko kwako hutaki kufanya kazi kwa bidii, ujue unatakiwa gari na nyumba kubwa.”

“Patamu hapo. Na vyote hivyo si chini ya mamilioni ya pesa. Ukiiba tu, sisi tunakutenga. Ukihongwa tu, mimi Mchungaji nakupandisha madhabahuni nakutangaza kuwa wewe ni mzinzi, kisha nakutenga mbele ya watu.” Mchungaji akaongeza. Yule mama alisaidiana na mumewe kumshambulia Tunda.

“Hivi nyinyi mlikutana wapi?” Iliibidi Tunda kuuliza jinsi wanavyopokezana maneno kwa kupatana, kama wamepanga. “Maana mnafanana kila kitu!” Wote wakacheka. “Kanisani. Mimi nilikuwa kiongozi wa vijana, na bibie hapa alikuwa ndani ya kundi. Akanipenda ndio nikamuhurumia nikamuoa.” “Uringe. Alihangaika huyu, muone maneno mengi hivyo hivyo. Nilimtoa jasho!” Tunda alikuwa akicheka sana.

          “Kwa hiyo mlianzana tokea wadogo?” “Nimemfundisha hesabu za sekondari huyo, usimuone hivyo. Nilivyomuona anapenda pesa, nikaona nioe kabisa ili yeye awe anatafuta pesa mimi nahubiri injili. Ukimfatilisha huyu, ndani ya miaka miwili utakuwa mbali sana Tunda. Kazana, jiamini, utaweza tu.” “Umesahau kumwambia na awe anatoa fungu la kumi kanisani.” Mama Mchungaji, yaani mama Penny, akaongeza, nakumfanya Tunda aangue kicheko zaidi.

“Na sadaka kubwa kubwa. Umesikia Tunda? Sio zile sadaka unatumbukiza kwenye kapu la sadaka umekunja ngumi. Na baraka za Mungu zitakuwa ndogo ndogo hivyo hivyo”  “Nitatoa.” Tunda akakubali akicheka

Tunda aanza kupambana jijini.

Mwanzo wa Tunda haukuwa rahisi hata kidogo. Ilikuwa kazi tu. Hakuna masaji wala kutengeneza kucha na kubadili nywele kila week. Alianza kufanya kazi kwa bididii zote, akili ikiwa imetulia kazini asiharibu. Ndani ya juma moja alikuwa akipata kazi si chini ya nne. Zote hizo anasukumiwa na mama Penny. Kuna siku nyingine alikuwa akipamba kumbi mbili mpaka tatu.

Tunda akawa busy. Mchana na usiku yupo na kazi. Hakuna waxing tena kwenye huo mwili kutoa vinyweleo. Kazi tu. Anasaka pesa kwa juhudi zote. Na Mungu akawa akimfungulia milango kwa namna ya ajabu. Akawa ni kweli anapata kazi. Kila akijisikia kuchoka na kutaka kukataa kazi, alikuwa akijisuta na kukumbuka maisha yake. Basi anatoka kitandani bila hata alam.

Alianza kuingiza pesa na kufahamika mjini kwa kazi nzuri ya upambaji. Na akaongeza uaminifu kama mama Penny. Mkikubaliana aina fulani ya mapambo, basi ujue atakuwekea hayo hayo mapambo. Kama ni maua Rose, ujue hatachanganya wala kukuibia. Uwe na pesa usiwe, basi atakupambia kutokana na pesa yako na vile mlivyokubaliana.

Alipata familia kubwa pale kanisani kwa kina mama Penny. Tunda alijawa furaha, upweke wote ukaisha. Akawa mtu wa furaha wakati wote, na nyumbani kwa mama Penny ikawa ndio kituo chake kikubwa. Na mama Penny akafanyika dada kweli kweli. Ukimkosa Tunda kwenye simu, muulize mama Penny. Mchana na usiku wawili hao walikuwa wakiwasiliana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya mahangaiko mengi akichapa kazi mchana na usiku, akafanikiwa kuhama Temeke, akapata nyumba. Haikuwa nzuri kama ile aliyoishi La dolce Vita, lakini ilikuwa na ukubwa unaolingana na ile. Vyumba viwili kama ile, inajitegemea, maeneo ya Kimara, karibu sana na Ubungo. Akaenda kuchukua vitu vyake vyote kwa Net, akahamia kwake. Akaongeza bidii ili kupata usafiri pia. Kazi akafanya mchana na usiku bila kuchoka wala kulalamika. Hakuna tenda yeyote alipata akaacha.

Alipopata pesa, mama Penny akamsindikiza Tunda kununua gari. Kwa kuwa alikuwa na mambo mengi, alinunua gari nzuri lakini sio kama ile ya Mama Mchungaji iliyokuwa ya aghali sana. Tunda akapata usafiri wake wakumzungusha mjini.

Kila mama Penny alipopata kazi nyingi alimpa na yeye. Watu wakaanza kumfahamu yeye kama Tunda sasa. Akaanza kutafutwa yeye kama Tunda sio kwa kupitia tena mama Penny. Na kazi zake zilikuwa nzuri sana. Akaanza kuuzika kama Tunda, na watu wakaweza kutambua kazi zake.

Hakuwa amesoma, lakini kwa hakika kile kilikuwa kipaji chake bila kuuliza. Kilijionyesha kwenye kila kumbi aliyokuwa akipamba. Alijiongeza na ungeweza kutofautishi ukumbi aliopamba yeye au mama Penny, japo walitumia karibu kila kitu kinachofanana. Kipaji chake cha upambaji kilimkutanisha na watu waina mbali mbali. Wasomi na wenye pesa. Wake za mawaziri na mabalozi.

Alipoona kazi inakuwa kubwa, hana haja yakusaka kazi, zinamfuata tu, akatafuta ofisi na kuajiri watu wawili waliokuwa wakipokea kazi kutoka kwa watu. Alifungua website ambayo ilijaa picha zakuonyesha kazi zake. Kwa muda mfupi sana Tunda akawa mashuhuri pale jijini. Lakini katika yote hakuacha kuwa karibu na Mungu wake. Msingi wa kusoma bibilia na kuomba aliokuwa amefundishwa na Net, hakuacha hata kidogo. Kila akirudi nyumbani kwake, atapiga magoti na kuomba Mungu japo kwa ufupi. 

Kwa Mara ya Kwanza, Tunda amsaka  baba yake jela.

Alianza kuulizia kwenye magereza ya pale mjini, kutaka kujua alipofungwa baba yake, mpaka akajua kule baba yake alipokuwa amefungwa na siku ambazo wanaruhusiwa kutembelewa. Akaamua kwenda kumtembelea baba yake huko gerezani Segerea. Baba yake alifurahi sana kumuona Tunda. Lakini alikuwa amedhoofu na hakuwa na furaha hata kidogo.

“Wamenisingizia mwanangu. Kwa kuwa sina hela, nashindwa kutafuta mwanasheria mzuri wakunitetea.” “Mimi nitakutafutia baba.” Hilo likamfariji sana baba yake. Mtoto ambaye hakuwa hata anamtegemea, ndio anaahidi kuwa mkombozi! Akashukuru.  “Unafanya nini sasa hivi? Umependeza mama.” Ilibidi baba yake kuuliza. Maana ni kweli Tunda alionekana ametulia na pesa ipo.

Swali alilokuwa akilikwepa wakati ule akizunguka na wanaume, ndilo hilo baba yake anamuuliza. Lakini safari hii akamjibu baba yake kwa ujasiri wote. “Mungu ananilinda na kunitunza kwa namna ya ajabu baba! Mimi mwenyewe bado nipo kwenye mshangao baba yangu. Napamba kwenye kumbi za shuguli mbali mbali! Na wala sikurudi shule. Nilifundishwa tu.” Tunda akamuelezea juu ya wakovu aliopokea, familia ya mama Penny na mafanikio yake. Baba yake akafurahi sana, wakawa wanaongea mpaka muda ulipoisha, Tunda akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alianza kuzunguka kwenye ofisi za wanasheria pale mjini. Akiongea nao, kuona kama wataweza kumsaidia baba yake. Akiwa anajaribu kwenye ofisi nyingine, sekretari wake alimpigia simu kumwambia yupo mtu amesema anataka kuongea na yeye mwenyewe. Tunda alichukua ile namba akapiga.

Walimuomba huduma yake ya upambaji na kumtaka afike kwenye moja ya kikao chao cha ijumaa ili kuongea na wanakamati.  “Mlishaona kazi zangu lakini? Maana mnaweza kupitia kwenye website yangu, mkachagua muundo mnaoupenda, kisha unapiga simu ofisini onatoa oda yako. Sio lazima mimi nikawepo kwenye kikao.” “Tungependa kukuuliza maswali kabla ya kuchagua.” Tunda akakubaliana nao muda na eneo atakalokwenda siku hiyo ya ijumaa kukutana na wanakamati wengine.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ilikuwa siku hiyo ya ijumaa jioni, Tunda akiwa amejitayarisha vizuri kwenda kuonana na wanakamati hao. Alikuwa na kazi moja tu siku hiyo. Alishakamilisha tokea asubuhi. Akarudi nyumbani, akapumzika na kujiandaa tayari kwa kikao cha jioni. Kama kawaida yake, hakuwa akifanya makosa kwenye mwili wake. Alipendeza sana, akachukua picha zote alizojua angehitaji kuvutia wateja wake, akaelekea kwenye kikao.

Eneo tu walilokuwa wakikutania hao wanakamati, Tunda alijua watakuwa na pesa. Aliingia kwenye hoteli hiyo iliyokuwa Masaki, akasalimia pale mapokezi, kisha akampigia simu mtu aliyekuwa ameongea naye kwenye simu, akafika pale mapokezi kumchukua.

Tunda alimuona yule kaka jinsi alivyobabaika baada yakumuona. Akaongeza ujasiri. Wakaongozana mpaka upande wa chakula walipokuwepo wale wanakamati wenzake. Walikaa ndani, kwenye eneo kubwa kidogo. Waliunganishiwa meza mbili ili waweze kuonana. Tunda aliwasalimia bila kuwaangalia huku akijaribu kuvuta kiti alichoonyeshwa na mwenyeji wake.

Ana kwa Ana na Net tena!

“Tunda!” Tunda alishtuka kidogo baada yakusikia jina lake likitajwa pale mezani. Akanyanyua uso kutafuta aliyemwita na kukutana na Net. Tunda akatoa tabasamu kubwa sana la mshtuko. “Net! Habari za siku!?” Net alikuwa kwenye mshangao mkubwa sana, uliowafanya wanakamati wote wabaki wakiwakodolea wao macho. Tunda alikaa chini, na kumwangalia tena Net, pembeni ya Net, alikuwepo Gabriel. Tunda akashtuka sana, akaamua kutokuwaangalia tena. Akabaki akimtizama mwenyeji wake tu.

“Naona tumeshatambulishwa jina, tumeshajua unaitwa Tunda.” Yule mwenyeji akavunja ukimya. “Ndiyo. Ninaitwa Tunda, ndiye ninayehusika na mambo ya upambaji. Uliniambia mlishapitia kwenye website yangu. Si ndiyo?” Tunda akauliza huku akimtizama yule mwenyeji. “Ndiyo.” “Sio wote bwana.” Mwingine akakanusha. “Basi haina shida. Nimewaletea baadhi ya picha, ili muone baadhi ya kazi zangu kisha mchague.” Tunda akatoa zile picha alizokuwa amezipanga vizuri kwenye albamu.

          “Bei zako zikoje?” Mmoja wao akauliza wakati akiendelea kuangalia. “Inategemea na nini unataka ukumbini. Ukichagua moja ya picha hapo naweza kukutajia bei. Na pia kama hakuna muundo hata mmoja mtakao kuwa mmependa hapo, naweza kuwapambia kutokana na mtakavyo nyinyi. Mnaniambia nini mnataka, ukubwa wa ukumbi, meza na idadi ya wageni mnao tarajia, nitaandika na kwenda kuwapigia mahesabu kisha nitawajulisha. Mara nyingi najitahidi kwenda kutokana na bajeti ya mteja.” Tunda akajieleza vizuri sana na sauti yake tulivu bila pupa, nakubaki akiwasikiliza, ila macho yake yakiwa kwa mwenyeji wake tu.

Zile picha zilizunguka pale mezani watu wote wakiangalia kwa kurudia rudia. “Kazi yako nzuri dada Tunda.” Mmoja wa wanakamati akasifia. Tunda akatabasamu na kufanya azidi kuvutia kumtizama. “Asante.”

“Umeolewa?” Mwanakamati mwingine akauliza. “Acha hizo Tino, bwana! Wewe mtafute kwa wakati wako. Acha sisi tuongee mambo ya maana.” Wote walianza kucheka mpaka Tunda akatabasamu na kuinamia kwenye picha alizokuwa ameshika mkononi mwake. “Tatizo lako wewe Mgeekwa, unapenda kupania mambo sana. Si watu bado wanaangalia picha? Sasa kuna tatizo gani mimi nikaendelea  kuongea na Tunda?” “Utamchanganya bwana.” “Tunda mwenyewe haonekani kama ni mtu wakuchanganyikiwa hovyo. Halafu jibu lilikuwa fupi tu, ‘ndiyo au hapana’ ili nipate nguvu ya kuendelea kumtafuta baada ya hapa. Au hamtaki kikao kingine?” “Wewe si muoaji Tino. Acha fujo.” “Sasa ningemuoa nani wakati Tunda ndio amekuja leo? Eti jamani?” “Mgeekwa anakubania tu.”

“Mmeona eeh? Tuendelee Tunda. Sasa vipi?” Tino akaendelea kumchokoza Tunda. “Kwa kuwa wengi wenu hamkuwa mmeona kazi zangu, nashauri mtembelee website yangu ili muweze kuona kazi zangu nyingine ili mmfanye maamuzi sahihi. Kisha mnaweza kupiga simu ofisini ili kutoa maamuzi yenu na kujua gharama zinakuaje.” “Bwana Tunda yupo kikazi! Na mimi nimesoma Tunda. Nimeelewa kuwa hunitaki.” Kila mtu akacheka.

“Achana naye huyo Tunda. Tuendelee na kazi.” Mgeekwa ambaye alionekana ndio muongoza kikao, aliingilia.

“Jamani nyinyi mnamjua bibi harusi mwenyewe. Mimi naomba nikubaliane na Tunda. Nikamuonyeshe, achague. Kisha tutakuja kuongea na Tunda.” “Au kwa nini msitukutanishe naye, yeye mwenyewe huyo bibiharusi? Tuone kitu gani anataka. Na kama atataka ushauri pia tunaweza kumshauri.  Anaweza kufika ofisini kwetu, ninao wataalamu pale watamshauri vizuri au watamsikiliza anachotaka.” “Sisi tunakutaka wewe Tunda. Usitutupie kwa watu wengine.” Yule mwenyeji wake akamkatisha.

“Msiwe na wasiwasi kabisa. Hakuna kitakachoharibika. Naomba niwaache, tuwasiliane mtakapo kuwa tayari.” Tunda akasimama. Net hakuwa ameongea kitu chochote alibaki akimtizama tu Tunda. “Naomba nikusalimie pembeni kidogo, Net.” Tunda aliongea kwa sauti tulivu huku akimtizama Net. “Mimi hutaki kunisalimia pembeni kidogo?” “Acha Tino, nini lakini?” “Tatizo lako Mgeekwa, hutaki nioe kaka!” Tunda akacheka akiwa bado amesimama. “Tundaaa!” Tino akarudia. Net akavuta kiti na kuondoka pale. Tunda akamfuata nyuma. Net alikuwa akiongoza njia huku Tunda akimfuata nyuma.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Mbona huonekani kama una furaha, Net? Mzima?” Tunda akauliza mara baada ya Net kusimama nje ya ile hoteli na kumgeukia Tunda. “Kila kitu kipo sawa?” Tunda akarudia kwa upole akionyesha kujali. “Kwa nini hukunitafuta tena Tunda?” “Mama alichukua simu kwa ghafla, Net! Sikuweza kuchukua namba zako za simu. Nilishindwa jinsi ya kukupata. Hata nilipokwenda nyumbani kwako kufuata baadhi ya vitu vyangu, Emma hakuwa anajua lini unarudi nchini na hakuwa akijua njia ya kuwasiliana na wewe. Babu anaendeleaje?” “Alifariki. Unasema mama alikupokonya simu!?” Tunda akatulia kidogo.

“Tunda?” “Kwani yeye amekwambia nini?” Tunda akauliza. “Kwa nini unauliza swali juu ya swali Tunda? Nani anamjibu mwenzake?” “Samahani Net. Hakunipokonya, bali alichukua.” “Ilikuaje?” “Net please!” Tunda akamsihi kwa upole. Akimtaka ayaache tu. “What?” “Naomba tusiongelee mambo ya nyuma.” “Kwa kuwa wewe ushapita huko?” “Hapana Net. Kwa nini tusiongelee mambo ya sasa?” “Ya sasa yapi?” Tunda akanyamaza.

“Kama unashindwa kunijibu basi naona nikuache tu.” “Sishindwi Net. Lakini sijui ni nini mama alichokwambia juu yangu?” “Kwa kuwa wewe huna haja yakujua alichoniambia, mimi ninataka kujua nini kilitokea. Maana tuliagana vizuri siku ile ya jumamosi, ukaniambia tutawasiliana kesho yake. Ndio nakuona leo! Nakuuliza kulikoni, naona unashidwa kunijibu.” Tunda akaona ajieleze tu. Net alikuwa amekasirika.

“Siku ile tulipoagana, mimi niliendelea kukaa pale ofisini nikimalizia oda ya Nchawa. Si unakumbuka nilikwambia alipiga simu akitaka tumpelekee mzigo wake wote kwa pamoja siku ya jumanne?” “Ndiyo.” Net akajibu. “Sasa kumbuka nilikuwa sina lori kubwa. Yote mawili yalikuwa yamepeleka mizigo mikoani. Wazo lilinijia kuazima kwa kina Masai, ili nihakikishe napeleka mzigo wote siku ya jumanne ili kuhakikisha simpotezi Nchawa. Maana alisema nikimfanikishia, atakuwa anatupa kazi kila week hata kama mara mbili kwa week itategemea na sisi wenyewe na uwezo wetu. Sasa ikabidi kupambana ili nisiharibu, nimfurahishe.” Tunda akaendelea.

“Niliongea na Masai mwenyewe akasema lori analo lakini hana dereva anayemuamini. Dereva wake ambaye anatumia hilo lori amepatwa na matatizo, hayupo kazini. Akawa amenipa namba za simu za watu kadhaa, akaniambia huwa anawatumia mara moja moja. Nilikaa pale mpaka usiku nikijaribu kutafuta dereva wakupeleka mzigo wa Nchawa Moshi, siku hiyo ya jumanne asubuhi. Nilitaka kufikia jumatatu niwe nina uhakika na kila kitu. Dereva na usafiri wenyewe. Nilikuja kukamilisha kila kitu usiku kama kwenye saa mbili.” Net alikuwa akisikiliza tu.

“Niliporudi nyumbani baada ya kukamilisha kila kitu, nikamkuta mama na Safia.” Tunda akatulia kidogo. “Nini kilitokea?”  Kama kawaida ya Net, akataka amalizie. “Mama alionekana amenikasirikia sana na zaidi hakupenda kabisa kitendo cha mimi kuwa nikiishi pale bila yeye kuwa na taarifa. Alilaumu ni kwa nini uliweza kuruhusu mtu mwenye tabia kama zangu kuishi mle ndani na Maya, na mambo mengine mengi ambayo siwezi kurudia, itakuwa ni kama najitusi tena mwenyewe.”

“Lakini aliniambia Safia ndiye atakuwa bosi wangu, anahitaji nimkabidhi kila kitu ikiwemo simu ile ya mkononi na usiku uleule nimpishe Safia kwenye chumba kile nilichokuwa nikilala pale nyumbani kwake. Na usiku uleule niondoe mizigo yangu pale. Nilimkabidhi kila kitu, tena nilimuomba kwa kuwa ilikuwa usiku, na nilikuwa na mizigo, aniruhusu kuondoka na gari yako kisha niirudishe kesho yake, lakini mama alikataa. Nilijaribu kumuuliza kulikuwa na shida gani kwa nini amekuwa vile! Lakini mama alikuwa mkali sana, Net. Alinitaka niondoke pale usiku uleule. Ikabidi niondoke na mizigo yangu mpaka barabarani ndipo nikapata taksii.”

“Siku ya jumatatu asubuhi niliwakuta walishafika ofisini, Safia alikuwa kwenye meza yangu. Nikaamua kwenda kumsalimia mama ofisini kwako.” Tunda akanyamaza akageukia pembeni. Net akamuona Tunda akianza kufuta machozi. Alilia sana Tunda. Net akamshika mkono akamvuta nyuma ya gari.

“Nini kilitokea Tunda?” Tunda alishindwa kuongea kwa muda. Akajaribu kutulia ndipo akaendelea huku akilia. “Mama Cote alitumia maisha yangu ya nyuma kunidhalilisha Net. Alinitukana mbele ya Safia na yule kijana. Akinitaka nirudi kwanza shule niache umalaya, nikipata vyeti ndio nirudi pale kazini. Akanilipa na kunitaka niondoke.”

“Kweli sijui ni baya gani niliwatendea! Nilijitahidi kufanya ile kazi kwa kadiri ya uwezo wangu, na nilikusudia kuacha yale maisha machafu Net. Niliacha umalaya. Niliumia sana kuona mama Cote anatumia maneno niliyoongea kanisani tena mbele ya wazee, Mchungaji akinisihi niseme tu, pale ni sehemu salama, na wewe ukasema nisiwe na wasiwasi, lakini baadaye tena baada ya kutubu, na Mungu kunisamehe, bado nakumbushwa tena kwa kutukanwa! Bila kosa! Niliumia sana Net. Sana.” Tunda akajifuta machozi.

“Historia yangu yakufukuzwa ikajirudia, Net. Alinifukuza mama yako usiku nikiwa na mizigo, na pale ofisini akinitukana. Lakini nimesamehe. Sikutaka kurudia kuzungumzia na wewe yaliyotokea kwa kuwa yananikumbusha mambo ambayo hayanijengi bali kunibomoa. Isingekuwa Mungu, nisingeweza kurudi tena kanisani Net. Nisingeamini watu wa kanisani, na nisingekuwa kanisani mpaka sasa.”

“Lakini Mungu ameniponya Net. Amenipa familia ya kanisani. Nzuri sana. Nina mama na baba wa Kiroho wanao nifuatilia vizuri sana. Tena wao ndio wamenisaidia kufikia hapa. Na wala sikurudi tena shule. Kwa elimu ileile ndogo niliyonayo ninaweza kuishi.” Net alibaki kama amemwagiwa maji. “Pole Tunda na samahani sana.” “Yameshakwisha Net. Mungu amenisaidi ninaishi vizuri na nina amani.” 

Simu ya Tunda ikaanza kuita. Akasogea pembeni kidogo na kuanza kuongea. Alisikiliza kwa muda, akiwa kimya “Naomba subiri kidogo.”  Net akamsikia Tunda akiongea kwenye simu, akimwambia anayezungumza naye asubiri, kisha akamgeukia tena Net. “Net! Naomba nikuage, Mungu akipenda tutaonana tena.”  Tunda alikuwa bado ameshikilia simu yake kama kuna mtu anayemsubiri upande wa pili. Net alibaki akimwangalia. “Bye!” Tunda akamuaga, kisha akaondoka pale akilifuata gari lake. “Samahani kuna mtu nilikuwa nikizungumza naye hapa. Ehe! Kwa hiyo umesema inawezekana?” Net akamsikia Tunda akiongea huku akiishia.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Katikati ya mengi, Net arudi pichani. Nini kitaendelea?


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment