N |
et ni kama alipoteza dira, hajui
chakufanya tena. “Naomba niondoke Net.”
“Kumbuka tumekuja na mama! Naomba nikamchukue mama ili tuondoke pamoja. Sawa?”
Tunda akatingisha kichwa kukubali. “Asante sana Tunda.” Net alikuwa amesha
changanyikiwa. “Twende basi ukasubiri kwenye gari.” Akarudi naye mpaka kwenye
gari, akawasha gari, akamuacha Tunda amekaa humo ndani ya gari.
Alikuta
Mchungaji akimsubiri, bado haelewi kilichotokea. “Kuna nini, Net?” “Naomba
tuwaulize hawa wazee, kwa nini Tunda amekimbia mara baada ya kuwaona.” Mmoja
wao akasema sijui. “Wewe hujui lakini Mzee Meto namwenzie wao wanafahamu.” Net
alikuwa amekasirika sana.
“Hivi unajua ni kwa muda gani nimekuwa
nikitaka huyu binti afikie haya maamuzi? Hivi mnajua ni jinsi gani
nilivyomuhubiria? Nimemwambia huku kanisani lipo tumaini. Ameteswa na shetani
kwa muda mrefu sana, nimemuahidi atapata pumziko. Halafu anakuja kukutana na
nyinyi watu wa kanisani mliokuwa wateja wake!” “Wateja?” Mama Cote alishtuka
sana. “Ndiyo. Tunda alikuwa akifanya biashara ya kikahaba.” Net alikuwa
amekasirika sana, hata hakuwa akifikiria alichokuwa akiongea. Aliendelea
kuropoka. Wote walikuwa kimya wakimsikiliza.
“Hivi
mnajua mlichofanya nyinyi? Mmechukua tumaini la pekee lililokuwa limebaki kwa
yule binti! Mtamfanya asiamini tena.” “Tulia Net. Kwa kuharibu kwa hawa wawili,
hakuchukui nafasi ya Mungu hata kidogo. Kama wao wameshindwa, bado tunayo
mifano mizuri ya watu wengi wanaoweza kuishi maisha maadilifu. Naomba ukamwite
Tunda.” Mchungaji akapiga simu kwa baadhi ya wazee aliojua wanaweza kufika pale
kwa haraka, wakaanzisha kikao.
Tunda akarudi
ndani, wakamuomba aelezee mahusiano aliyokuwa nayo na wale wazee. Tunda akakiri
kila kitu huku akilia na kusema ni kweli amechoka anatafuta njia ya kupumzika
nakuondoa ile hukumu moyoni mwake lakini si pale. “Hamuwezi
nyinyi kunisaidia. Hamtaweza hata kidogo.” Tunda akatoka. Net
alimkabidhi funguo mama yake na kumfuata Tunda.
Ilikuwa
ni aibu ya miaka kwa kanisa. Hakuna aliyeamini uchafu Tunda aliosema alikuwa
akiwafanyia wale wazee. Net ndiye aliyeishiwa maneno kabisa. Alishindwa aongee
nini na Tunda. Tunda alikataa kabisa kurudi kwa mama yake Net, akaishia kulala
hotelini. Aliomba Net akamchukulie mizigo yake nyumbani kwao, usiku uleule.
Kesho
yake asubuhi na mapema, bila hata kumuaga Net, Tunda aliondoka jijini Dar
kurudi Arusha kwa kutumia usafiri wa basi. Usiku ule ulikuwa mrefu sana kwa
wale viongozi wa kanisa lile. Wale wazee walikiri uchafu waliokuwa wakifanyiwa
na Tunda, na kesho siku ya jumapili kwenye ibada, walisimamishwa mbele ya
kanisa na Mchungaji akawatenga.
Ilikuwa
ni hali ya kusikitisha, kushtua na aibu kubwa. Kwani ni wazee walioheshimika
sana pale kanisani na wao ndio walikuwa wakitoa michango mikubwa ya kifedha
pale kanisani, wakisaidiana na Mama Cote. Mmoja alikuwa ana mke wake pale pale
kanisani. Watoto wao walishakuwa wakubwa tu. Na Meto yeye alifiwa na mkewe,
japo naye alikuwa Mzee wakuweza kumzaa hata Net. Alitambulishwa Tunda na huyo
Mzee mwenzake. Tunda akamridhisha kwenye gari kitu alichopenda. Hakuhitaji
kwenda naye popote. Kwa hiyo walimpenda Tunda, wakijua hawataweza kukamatwa.
Waliegesha magari yao sehemu tulivu mida ya usiku giza limeshaingia. Tunda
anafika hapo kwenye magari yao, anawahudumia, wanamlipa, maisha yanaendelea.
Mchungaji Amfuata Tunda.
Baada ya
ibada yule Mchungaji alipanda ndege kuelekea Arusha na Net, kumfuata Tunda.
Walimkuta amelala chumbani kwake. Mchungaji alimuomba waongee. Tunda alishtuka
sana. Hakutegemea kuja kufuatwa tena baada ya kugundulika uchafu wake. Yule
Mchungaji aliongea kwa muda mrefu na Tunda. Akimpa mifano hata ya watu
waliokuwepo kwenye bibilia walioaminiwa na Mungu, lakini walikuja kumkosea
Mungu, lakini baadaye walipotubu tena Mungu aliwasamehe. Alimpa mfano wa Petro
aliyemsaliti Yesu mara tatu, lakini baada ya kutubu alisamehewa, na akamueleza
jinsi Petro alivyokuja kuwa msaada mkubwa kwa kanisa mpaka sasa.
“Kama sio Petro kukubali kosa, kazi kubwa ya kanisa
iliyoifanya baada ya kutubu isingekuwepo leo. Kikubwa ni kukubali kuwa umekosa
na kuhitaji msaada wa Mungu. Halafu Tunda, wale wazee hawatakuwa mfano wako
wakuiga pindi utakapoamua kumpa Yesu maisha yako. Wote tunamwangalia mmoja tu,
ambaye aliishi hapa duniani bila kutenda dhambi, Yesu.”
“Wote tunamtizama yeye peke yake. Hata mimi huwa
najikwaa kwa namna nyingine, na ndio maana tupo kanisani. Kanisani ni kama
hospitalini, Tunda mwanangu. Wote tuliogundua tunahitaji msaada wa Mungu, ndio
tumekimbilia pale kama wagonjwa wanavyokimbilia hospitalini. Kanisani ndio
mahali pekee utakapopata msaada. Sisemi kama utakuwepo kanisani na uendelee
kutenda dhambi, hapana. Lakini ujue kuna madhaifu mengine yanachukua muda
kuondoka, lakini utakapotulia kwa Mungu, ukanyenyekea, ipo nguvu na uwezo wa
kushinda dhambi endapo utakusudia.” Yule mchungaji aliendelea.
“Mungu halazimishi mwanadamu kuacha kufanya dhambi.
Mimi na wewe ndio tunachagua. Kwa hiyo unaweza ukawepo kanisani, na ukachagua
kuendelea kutenda dhambi kama mtu wa nje kabisa, lakini haiondoi uweza na nguvu
za Mungu. Utende dhambi, usitende, bado Mungu atabaki kuwa Mungu ila wewe ndiye
utakayeteseka.” Net aliendelea kusikiliza na yeye kwa makini tu akiomba Mungu
huo ukweli umuingie Tunda.
“Hakuna pumziko kwa mwenye dhambi, si sasa au
baadaye. Bali ipo faraja, amani na utulivu kwa wale walioamua kweli kuishi
maisha yakumpendeza Mungu. Mpe Yesu nafasi kwenye maisha yako uone. Mruhusu Net
awe mwalimu wako, utajifunza mengi sana kupitia yeye. Nikijana aliyetulia sana
na anamjua Mungu. Anaishi maisha ya kikristo kweli kweli, najua wewe ni
shahidi.” Tunda akatingisha kichwa kukubali. Kidogo Mchungaji akapumua.
“Basi, na wewe unaweza kuwa kama yeye, kama
utakubali, ukatii na kutubu. Je upo tayari?” Tunda alishatulia kabisa.
Alimuelewa vizuri sana yule Mchungaji. Akakubali kuombewa. Aliongozwa sala ya
toba na Mchungaji akamuombea. Tunda alikuwa na mapepo mengi sana.
Alikuwa amefungwa na nguvu za giza, nyingine tokea
alipokuwa mtoto mdogo kwa baba Tom. Mashetani na majini mengine aliyapata akiwa
na Sadiki. Tunda akiwa amepagawa hayo mapepo, aliongea mengi sana. Basi ikawa
vurugu tupu hapo chumbani. Mchungaji na Net walimuombea, wakikemea yale mapepo
yamtoke. Kuna yaliyokuwa mabishi. Yakidai hiki na kile. Lakini yule mchungaji
alikazana akisaidiana na Net. Haikuwa kazi rahisi wala ya masaa machache.
Lilitoka pepo hili, na kuibuka jingine ndani yake.
Wakidhani wamemaliza, linaibuka jingine. Mara liseme ni jini lililomuoa Tunda.
Jingine lilisema ndilo linalomfanya awe na bahati na kuvutia wanaume kwake.
Ikawa fujo. Tunda alijawa nguvu za giza. Lakini Net hakushangaa. Tunda
alishamsimulia ibada za kipepo alizokuwa akifanya makaburini na huko Handeni
alipokuwa na Sadiki.
Maombi hayo yaliendelea, mpaka yote yakamtoka
Tunda. Akawekwa huru. Kuja kuangalia saa ni saa saba usiku. Ikabidi Mchungaji
achukuliwe chumba hapo hapo hotelini. Kesho yake asubuhi akaondoka kurudi Dar,
akiwa amefanikiwa kumpatia Mungu roho ya Tunda.
Maisha ya Tunda baada yakumpokea Yesu.
Net ndiye alikuwa na furaha
kuliko hata Tunda mwenyewe mpaka Tunda akashangaa. Alikabidhiwa rasmi kazi ya
kumtunza Tunda kiroho. Kitu cha kwanza alichomnunulia Tunda ni bibilia. Akaanza
kumfundisha Tunda jinsi ya kusoma bibilia. Kitu alichogundua Tunda kwa Net, ni
muombaji. Net alikuwa ni muombaji sana, kitu kilichokuwa kikimshangaza Tunda.
Kwa jinsi alivyo Net, na maisha anayoishi, ingekuwa ngumu kumdhania kama ni
mcha Mungu wa kiasi kile. Lakini Tunda alijua ndiyo siri yake kubwa ya hekima
na utulivu alio nao.
Kwa
harakaharaka wasichana wengi walikuwa wakichanganywa na Net, pindi wamuonapo.
Lakini baada ya kukaa naye kwa muda mfupi, wengi walimkimbia. Mara nyingi Net
alikuwa akimshukuru Mungu kwa kumuwahi. “Unamaanisha nini?” “Najijua hivi
nilivyo Tunda. Si watoto au watu wazima wanao nijaribu kunitongoza. Isingekuwa
Yesu kunificha, pengine sasa hivi ningeshakuwa nimekufa. Nashukuru Mungu kwa
kunipa baba na babu wenye msingi imara wa dini, zaidi babu. Walinikuza kwenye
maadili mazuri.”
“Yuko
wapi sasa hivi baba?” “Alishafariki.” “Pole sana.” “Asante, lakini ilimuathiri
zaidi Maya. Unajua yeye ndiye alilelewa sana na baba wakati mama yupo shuleni.
Kwa hiyo baba alipofariki, ndipo mama alipoamua kurudi huku Tanzania.” “Kwani
hamkuzaliwa hapa?” “Hapana. Tulizaliwa Canada. Mama alienda huko kimasomo,
ndipo akakutana huko na baba. Hata msingi wa shule niliyokuwa nayo ilikuwa ni
hukohuko, ndio maana ilinilazimu kurudi hukohuko kumaliza shahada yangu ya
pili.”
“Alitangulia kurudi huku mama peke yake. Akatuacha kule mimi na Maya tukilelewa na bibi na babu. Mama alipoweka mambo sawa, nikaanza kuja huku mimi ndipo tukamchukua Maya. Maya hana muda mrefu sana hapa nchini. Na hapapendi kabisa. Anataka sana kurudi kwa bibi na babu. Lakini mama hataki, anaona kule hana uangalizi mzuri. Pale alipo hataki kufanya kitu chochote hapa nchini, anataka kurudi kwa bibi na babu.” “Labda mngemruhusu ili akasome.” Tunda akajaribu kushauri.
“Mama
hawezi. Ni mtundu sana Maya. Na amedekezwa sana na kina bibi. Hana maadili
mazuri hata kidogo. Hata huko pia shule yenyewe hataki kwenda. Amemaliza high
school tu, anatapanya pesa ya bibi na babu. Ndio maana mama ameamua kumchukua.”
“Natamani kama mimi ndio ningepewa hiyo nafasi Net.” “Mungu amekupa nafasi
nyingine Tunda. Unaweza kuwa chochote utakacho.” Tunda akainama kama
anayefikiria kidogo.
“Lakini
sikurudi tena shule. Naanzia wapi?” “Sio lazima ukasomea elimu ya msingi au
sekondari. Kwa sasa unaweza kutafuta ujuzi wa kitu fulani unachopenda, kisha
ukaanza kukifanyia kazi.” “Ni kweli. Labda nianze kufikiria na mimi nikitu gani
napenda. Maisha hayakuwahi kunipa nafasi kama hii. Sasa hivi ninafuraha na
amani. Siamini kama na mimi Tunda, nipo kwenye nafasi yakuchagua.” Net akacheka.
“Nikwambie
ukweli Net, zile ndoto mbaya zimeisha. Halafu nilikuwa nina hofu fulani hivi.
Kama wasiwasi moyoni. Umeshawahi kulala usiku au hata kuwa umekaa tu hivi,
ukasikia moyo unashtuka?” Net akawa anafikiria. “Unaweza usijue, lakini
nilikuwa na hiyo hali. Hofu kila wakati kama moyo unashtuka kila wakati.” “Kwa
hiyo sasa hivi imeisha?” “Imeisha. Namshukuru Mungu. Najisikia huru.”
“Afadhali.”
Cheni ya Mguuni ya Tunda!
Ilikuwa jioni wametoka kazini.
“Nikuulize kitu Tunda?” “Niulize tu.” “Hiyo cheni ya mguuni ulipata wapi?”
Tunda akakunja mguu akaitizama na kuizungusha kidogo. “Alinivalisha Sadiki.
Nimeshindwa kuitoa Net.” “Kwa nini?” Tunda akafikiria. “Kuna jinsi Sadiki
alikuwa akinifanyia, sijui niseme kunidekeza au nini! Lakini kuna jinsi alikuwa
na mimi, alikuwa akinifanya kama yai! Alikuwa hapendi niwe na shida. Kabla
sijalia shida, ananipa pesa. Manguo haya yote, ni ya pesa nyingi sana Net.”
“Nakuona.” Net akaongeza.
“Basi ni
Sadiki. Nilikuwa nikiwa naye, japo nilimdanganya jina, lakini sikuwa
nikijitahidi kujifanya kuwa sivyo. Alinipenda yule kaka, karibu
kuchanganyikiwa. Wakati mwingine nilikuwa nikimgombesha sana, lakini
anavyojishusha, mpaka utamuhurumia. Sikuwa na shida na pesa nilipokuwa naye.
Sikuwa nikihangaika kwa yeyote na chochote. Alinilipia kila garama, tena bila
kuchoka au kulalamika.”
“Alikuwa
akiniona nimetulia tu hivi nawaza kitu, basi hata kama alikuwa anafanya kitu,
ataacha, anakuja japo aniguse. Nitakuwa mawazoni, naweza kushtuka kwa sababu
ananisugua mahali kwa upendo. Kiganja, bega, ilimradi tu kunionyesha yupo na
mimi.”
“Japokuwa
alikuwa anasema ananufaika na mimi, lakini Net, Sadiki alihakikisha nina furaha
wakati wote. Alinipenda sana. Nilipata miaka miwili ya aina yake na yule kaka. Hii
cheni nimeshindwa kuitoa kabisa. Wakati mwingine najiona ni kama nipo na ule
upendo wake. Sijui kama unanielewa?” Tunda akauliza na kuendelea bila kusubiri
jibu.
“Sijapata
mwanaume anayenipenda vile Net. Labda nikija kubahatika upendo kama ule tena.
Huyo mwanaume ndiye atakayekuja kuitoa hapa mguuni kwangu. Lakini mimi
nimeshindwa.” Tunda aliongea taratibu huku akiiangalia ile cheni na kuizungusha
pale mguuni mwake. Net akavuta pumzi kwa nguvu maana alikuwa akimsikiliza kwa
makini sana.
“Lakini
sasa hivi hauhitaji upendo wa Sadiki, Tunda. Unaye Mungu aliye hai. Upendo wake
unatosha. Usijifunge na upendo ambao haukuwa halisi. Nilivyokusikia juu yako na
Sadiki, mlifanya mengi na ya kutisha huku akikutumia wewe kama chambo yakuvuta
utajiri. Hudhani kama hiyo kitu inaweza ikawa imebeba mambo mengine?” Tunda
akashtuka kidogo.
“Nikuombe
kitu?” Tunda akamwangalia. “Naomba mimi niitoe, halafu nije niweke hapo
nyingine.” Tunda akajifuta machozi. “Hamna sababu
yakufanya hivyo Net. Acha tu. Lakini naomba nipe muda wakuja kuitoa. Isiwe sasa
hivi. Najiona sipo tayari Net. Mmeniombea, naamini hii cheni haiwezi kuwa na
madhara yeyote. Alininunulia cheni tatu. Shingoni, mkononi na mguuni.
Akaniletea na kuniambia ni ishara ya upendo wake kwangu. Najiona sipo tayari kuviachia.”
Net alibaki akimtizama.
“Ni sawa?” Tunda akauliza kwa upole. “Sio sawa Tunda.”
Tunda akaumia sana. “Tena kwa maelezo hayo, ndio sio sawa kabisa. Kwa nini
unataka kukumbatia upendo wa mtu aliyepita vibaya kwenye maisha yako?” Tunda
akanyamaza.
“Unakuwa
unang’ang’ania agano la mapenzi yaliyowekwa kwenye msingi mbaya na hatari sana
kwako! Tumekuombea, na tunaendelea kuomba. Lakini unakuwa uko kwa Mungu huku
umekumbatia maagano ya mtu mwingine kwenye ufamle mwingine! Hujui nia ya
kukuvalisha hiyo ki ukweli.” “Aliniambia ni ishara
ya mapenzi yake kwangu.” Tunda akatetea.
“Ndivyo
yeye alivyokwambia. Unajuaje kama ni kweli? Halafu Sadiki alikuwa mume wa mtu.
Unajifunga kwenye maagano ya ndoa ya mtu! Si sawa Tunda. Unatakiwa ubadilike
hata kifikira. Kuwa upande wa Mungu huku ukitetea mapenzi ya wizi,
unajifungulia milango mingine mibaya. Naomba ufikirie zaidi.” “Nimeelewa Net.
Nitatoa.” Tunda akaongea taratibu.
“Lini?”
Net akauliza bila kutaka kumpa nafasi Tunda. Tunda akanyamaza. “Tunda?” Net
akamwita. “Unataka kuishi kama Tunda au Ani wa Sadiki?” Tunda akashtuka kidogo
akamwangalia. “Ani alikufa na Sadiki, Net.” Tunda akajibu. “Haionyeshi hivyo.
Bado yupo na maagano yake yapo hai!” Akamuona anaizungusha ili aitoe.
Net
akasogea pale mguuni. Akapiga magoti. “Naomba mimi niitoe.” Tunda akamwangalia
kama ambaye hamuelewi vizuri. “Ni sawa?” Tunda akatingisha kichwa kukubali. Net
akaitoa. Nakubaki ameishika. “Utaifanyia nini?” Tunda akauliza. “Sijui.
Tumuombe Mungu. Kwanza akutoe kwenye haya maagano na akupe amani. Mengine Roho
wa Mungu atatusaidia.” “Basi acha nikupe vyote. Na cheni ya mkononi na
shingoni.” Tunda akaenda juu ya meza hapo hapo hotelini alipokuwa amening’iniza
mikufu yake.
Akarudi
na hizo cheni zote, akamuwekea Net mkononi. Ni kweli zilikuwa nzito. Net
akamwangalia. “Nipo sawa Net. Nimeridhia kutoa.” “Hilo ndilo la muhimu. Wewe
mwenyewe ukubali kutengana navyo kwanza. Ndio hata tukiomba na kuvunja hayo
maagano, itawezekana.” “Basi tuombe wote.” Tunda akapiga magoti pale alipokuwa
amepiga magoti Net akimvua. Net akacheka kwa furaha.
“Mungu
atakupa mtu anayekupenda kwa dhati.” Tunda akacheka kidogo huku akifikiria.
“Mmmh! Sidhani Net. Acha tu tuombe, niachane na Sadiki nitulie kwanza.
Nishahangaika na wanaume mpaka nimekinahiwa nafsi. Umenipa mapumziko ambayo,
hujui tu! Mungu atakuja kukulipa Net. Hujui kile umekifanya kwangu. Mungu
akuonekanie na wewe siku utakapomuhitaji. Kwa lolote lile. Akumbuke kile
ulichonifanyia mimi.” “Amina.” Wakatulia.
Net
akaweka vile vitu pale kwenye kochi akaanza kuomba. Ameanza tu, akashangaa
Tunda anaanguka tena na mapepo. Akajua ndio maana alikosa amani na ile cheni
pale mguuni. Yale mapepo yakasema yalikuwa hapo kutunza agano. Na lile agano
ilikuwa ni kama ndoa kati ya Tunda na Sadiki. Net alijua tu.
Kijana
huyo wa kizungu, alitumia mamlaka yote aliyopewa na Mungu. Akiwa peke yake pale
chumbani na Tunda akigaragara chini. Akaanza kutambaa kama nyoka na kutema mate
kama nyoka. Safari hii Net hakutumia muda mrefu, akayaamuru yale mapepo yamtoke
na yasirudi tena kwa kuwa Tunda ameshavunja yale maagano na amekiri kifo cha
Ani.
Akajinyonga
pale chini, yakatoka. Ndipo Tunda akazinduka sasa pale sakafuni. Net akamsaidia
kusimama. Alijawa mate. Akawa amejichafua sana. “Nini kimenipata Net!?”
“Ulikuwa na mapepo Tunda.” “Tena!?” Tunda hakuamini. Siku anaokoka alitolewa
mapepo kwa majini.
“Yalikuwa
yakilinda maagano yako na Sadiki. Mlikuwa mpo kwenye maagano yaliyoshikiliwa
kwa nguvu za giza Tunda. Hizi cheni zilikuwa ni ishara za hilo agano.” “Mungu
wangu!” “Usiogope. Umewekwa huru.” “Basi yeye Sadiki alijua anachokifanya. Mimi
nikijua ni zawadi tu, kumbe ni mambo yake. Tena aliniletea akiwa ametoka
safari. Ukute alizinunua ndio akaenda nazo kwa babu, wakazifanyia dawa. Sadiki
alitamani sana anioe nijulikane mimi ni mke wake kihalali. Nilipokataa
akaniomba angalau nimzalie hata mtoto mmoja! Napo nilikataa.” “Basi mshukuru
Mungu upo huru. Anza upya ukitumia uhuru wako vizuri. Nenda kaoge. Nakusubiri.”
“Acha nifute hapo chini sakafuni kwanza.” “Nenda ukaoge. Mimi nitaita mtu wa
hoteli apige deki.” Tunda akaingia bafuni akamuacha Net akiita muhudumu kwa
ajili ya kusafisha.
Tunda
alitoka bafuni na kumuomba Net waombe tena. “Acha woga Tunda.” “Tuombe tena ili
kuwa na uhakika yametoka yote.” Net akacheka. “Usinicheke bwana! Tena tupige
magoti. Ujue mwenzio nilijua nimewekwa huru kabisa na hayo mapepo!” “Yapo
maagano mtu unaingia. Kama si ya kimungu ni mpaka ukubali kuyavunja. Shetani
anakuwa na haki nayo, Mungu hawezi kuingilia. Ukikubali kuyavunja, hapo Mungu
anakuwa na uwezo wakukudai kwa shetani. Anakuwa na haki zote.” “Sasa hivi
sitaki tena Net.” “Na Mungu ameliheshimu hilo, sasa hivi wewe ni wake.”
“Kwani
wewe ulionyeshwa na Mungu juu ya hii sheni?” “Sio moja kwa moja. Ni kweli
inakupendeza sana. Huwa siachi kuitazama hapo mguuni. Lakini kila nilipokuwa
nikitazama sipati amani kama jinsi ilivyokukaa. Unajua kuna kitu kinavutia.
Ukikitazama kwa karibu, kinatakiwa kifurahishe sio kukukosesha amani! Ndivyo
sasa ilivyokuwa hiyo cheni kila nikiitazama kwa karibu, nilikuwa sipati amani.”
Tunda akatulia.
“Tutakuja
kurudisha nyingine hapo mguuni.” Tunda akacheka. “Sio lazima Net. Nakushukuru
kwa kusimama na mimi. Hujanikatia tamaa.” Net akacheka akijiambia ‘hujui hata nusu yake!’ Wakapiga
magoti, wakaomba, ndipo Net akaondoka pale na kumuacha Tunda amelala.
Maajabu ya zile Cheni!
Asubuhi Net alifika na kumpigia
simu ashuke chini waende kazini. Tunda akamwambia aende chumbani kwake. Net
akajua kuna jambo. Akatafuta sehemu ya kuegesha, akapandisha juu kwa haraka.
“Vipi?” “Nimeamka asubuhi, zile cheni hazipo. Au ulizitupa?” “Hapana. Niliweka
hapo juu ya meza. Zote tatu. Na niliziacha hapa wakati umelala.” “Basi
zimetoweka.” “Mwache shetani achukue mali zake.” “Nimeshtuka Net! Yaani
nilikuwa nimevaa na kujifunga mapepo!” “Lakini unachotakiwa kuwa nacho ni kuwa,
umebakiwa na uhuru.” Wakaomba tena na kwenda kazini.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Net
alitafuta kanisa pale pale jijini Arusha, wakawa wakienda na Tunda. Alipata naye muda mwingi wakumfundisha kila
baada ya kazi. Tunda alibadilika sana kimaisha hasa kimtazamo. Ile hukumu
aliyokuwa nayo zamani iliisha kabisa. Tunda alisahau shida zote akawa akiishi
kwa furaha. Net alijitahidi sana kumuelekeza kwenye neno la Mungu. Alimjengea
msingi wa kusoma bibilia. Kila alipomuuliza swali Net, Net alijitahidi
kumuelekeza kwakupitia bibilia.
Maya jijini Arusha, amtaka Tunda aishi nao.
Babu yao
aliugua huko nchini Canada, ikamlazimu mama yao aende kumtizama, ndipo ikabidi
Maya aende akaishi na Net jijini Arusha. Kwa kuwa Net ni kama alihamia Arusha,
na kushindwa kurudi tena Dar kwa kila sababu. Kazi anazofanya Net haikumlazimu
awepo Arusha na kushindwa kusafiri kwenda popote, lakini hakuacha kutoa sababu
zilizoonyesha ugumu wakuliacha hilo jiji.
Ofisi ya
Dar ambayo ilimuhitaji zaidi, kazi zake nzito ndio akawa akizifanya sasa kwa
simu na kompyuta, tena kwa juhudi ili kumnyima mama yake sababu. Tunda hakujua
anayopitia Net, ili kuwepo naye hapo Arusha. Alikuwepo hapo kwenye ofisi za
usafirishaji, lakini alifanya na kazi za mama yake pia huko Dar.
Tunda
alishangaa siku hiyo asubuhi Net anampigia simu kumtaka ashuke waelekee kazini,
akiwa na Maya. Alifika garini akamkuta Maya anamsubiria kwa hamu. Walikwenda
naye ofisini akiwa na Tunda wakati wote. Maya alionyesha kuvutiwa na Tunda kitu
kilichomshangaza hata Net.
Alikuwa
muongeaji sana tofauti na Net. Lakini binti mdogo tu na nadhifu. Baada ya kazi,
waliamua kwenda kula wote watatu kwenye mgahawa wa pale pale hotelini anapoishi
Tunda. Wakati wanakula wao watatu, akumuomba Tunda akaribie kuishi nao nyumbani
kwao. Tunda akashangaa kujua kuwa Net ananyumba kule Arusha. “Nilifikiri
unaishi hotelini Net!” “Hapana. Tulinunua nyumba.” Hata Maya akashangaa.
“Hujawahi
kufika!?” Akamuuliza Tunda kwa mshangao. Tunda akacheka. Maya akamgeukia kaka
yake. “You must be kidding me!” Akamwambia kaka yake. “Acha fujo Maya.” “Tatizo
la Net, yupo sooooo..” Akawa anafikiria Maya jinsi ya kumsimulia Tunda jinsi
alivyo Net. “Aaah! Sijui hata nikwambie nini! Lakini umenishangaza kushindwa
hata kumkaribisha sehemu unayo ishi!” “Ningemkaribisha bwana. Sema tumekuwa na
mambo mengi.” Tunda alishamjua Net ni mwadilifu sana na hana haraka.
Maya aliaga kuwa anakwenda kutumia choo. Net
akamgeukia Tunda. “Upo huru kuja kuishi naye kama unataka. Labda itamsaidia.
Hana rafiki hapa nchini na kila kitu mama anachomwambia anaona anaonewa. Labda
wewe unaweza kuwa karibu naye, ukamsaidia.”
Tunda akashangaa Net anazungumza nini!
“Net!
Namwambia nini mimi Maya!? Mwenzangu amezaliwa uzunguni, mimi mtoto wa mtaani.”
Wakacheka. “Inawezekana historia yako, ikawa msaada mkubwa sana kwake.
Usidharau.” “Mmmh!” Tunda akaguna na Maya akawa amerudi akawakuta wanacheka.
“Sasa Tunda umeamua nini? Nakuja kuishi hapa na wewe au wewe unakuja tuishi kule?”
“Upo kama kaka yako!” Wote wakacheka.
“Kweli.
Wote hamsahau jambo, na mking’ang’ania kitu, kinakuwa hichohicho na mpaka
mpate.” “Hiyo ipo kwenye damu. Sasa hujakutana na Nana. Nana ndio mbaya zaidi.
Hajui jibu la ‘hapana’ anapotaka jambo lake. Na hapendi mtu aombe kitu
ambacho hajakifikiria, au hana umuhimu nacho. Na anashangaa ukiwa unataka kitu
halafu ukakikosa, ukatulia. Anasema inamaana unataka kitu ambacho kwanza
kinakuwa hakina umuhimu. Na inamaana hujafikiria ndio maana ukikikosa inakuwa
rahisi kuridhika.” Tunda akapata hapo somo.
“Nana ni
nani?” Tunda akamgeukia Net. “Bibi ndio tunamwita Nana.” Net akajibu. “Oooh!
Anaonekana ni smart.” Tunda akasifia. “Hujawahi kuona mwanamke kama huyo hapa
duniani.” Tunda na Net wakacheka. “Lakini ni kweli. Nana yupo very smart.
Wakati wote huwa anajua anachokitaka. Na kama alivyosema Maya, huwa hajui jibu
la hapana, linapofika swala la kukamilisha jambo lake. Anaweza kuhamisha
milima, ili kukamilisha swala dogo ambalo kwako linaweza hata lisilete maana.”
Net akaweka msisitizo.
“Kwa
hiyo tunakwenda au tunabaki?” Maya akarudia swali. Wakacheka. “Eti Net?
Haitakuwa usumbufu?” “Hata kidogo. Ni sehemu kubwa. Utapata chumba chako na
utanisaidia kusikiliza kelele za Maya, ili niweze kufanya kazi.” “Heeee!” Maya
akalalamika nakukunja mikono kifuani kwake kama mtoto, akimtazama kaka yake.
Wakacheka. “Basi nitahamia kesho. Acha nifungashe usiku wa leo.” Tunda akubali
kwenda kuishi nao nyumba moja.
Tunda afanyika Msaada kwa Maya.
Nikweli
alibadili maisha ya Maya. Kwa kuwa na yeye alikuwa akiongea kingereza kizuri,
ilimrahisishia sana Maya kwenye mawasiliano, kwani mama yake ndiye aliyekuwa
akimlazimisha kujifunza kiswahili. Tunda alimweleza maisha ya shida aliyopitia,
bila kwenda kiundani zaidi, na kumwambia kama angepata nafasi kama yake,
angeitumia vizuri sana.
Ilikuwa
ni muujiza hata kwa Net. Maya alikuwa akimsikiliza sana Tunda kuliko mwanadamu
yeyote yule aliyekwisha kuwa naye karibu. Kwa asili Maya alikuwa mbishi sana.
Haambiliki na alilelewa maisha ya kudekezwa sana na bibi na babu yao. Hakuwa
akijua shida hata kidogo. Tunda aliongea na Maya mpaka akakubali kurudi shule.
Net alifurahi sana, akamshukuru Tunda. Alimpigia simu mama yake akiwa kule kule
nchini Canada, Maya akarudishwa Canada kwa ajili ya kuanza chuo.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Hali ya
babu yao ilizidi kuwa mbaya huko nchini Canada, ikamlazimu Net aende. Hawakuwa
ni babu tu na bibi. Waliwalea Net na Maya tokea wadogo sana tokea baba yao alipoanza kuugua mpaka akafariki. Na
hata mama yao alipoondoka nyumbani kwa wakwe na kurudi nchini Tanzania, wao
walibakia kwa bibi na babu yao. Walitunzwa wakachukua nafasi ya watoto kwa hao
wazee waliokuwa wamepata mtoto mmoja tu ambaye ndiye baba yake Net na Maya.
Net
alichukuwa jina la babu yake. Natheniel Cote. Ilibidi kuwa wakiandika sehemu
muhimu wawe wanaandika Jr au Seniour ili kujua ni yupi. Shule zote za mahela
yote hayo alizosoma Net, alikuwa akilipiwa na babu yao. Alipendwa sana, na
alimkuza Net kwenye maadili ya msingi. Ndio maana Net alikomaa mapema japo
alitoka kwenye familia ya kitajiri sana. Kila mtu alijua Net ndiye mrithi wa
mali nyingi za huyo mzee Cote.
Kwa kuwa
Maya alishaondoka nchini, wawili hawa walibaki wakiishi pamoja, kazini pamoja,
kwenye gari pamoja. Japo haikuwa kwa muda mrefu, lakini palishajengeka ukaribu
kati yao.
Net Arudi nchini Canada, Nakumlazimu kutengana na Tunda.
Tunda ndiye aliyemsindikiza Net
uwanja wa ndege. Alikuwa amepooza. “Utakuwa sawa Tunda. Na nitakuwa nikikupigia
simu kila siku. Kama ukiwa na maswali yeyote kazini, nikipiga simu nitakuwa
nakusaidia.” “Lakini haitakuwa sawa kama tulivyokuwa wote! Najiona kama bado
nakuhitaji sio tu ofisini, hata kwenye maisha ya kawaida. Naomba uniahidi kuwa
utarudi Net.” Net alimuhurumia Tunda akajua aliingiwa na hofu na ndio maana
hakumuaga mapema.
Tunda
hakujua huyo Net alikuwa akisubiriwa kwa muda mrefu sana, lakini akawa
akiahirisha safari kwa ajili yake. Kila alipojiambia ataondoka, alikuwa anaona
bado hili na lile. Akawa akimwambia bibi yake nitakuja hivi karibuni. Lakini
hakwenda mpaka alipoambiwa hali mbaya, anaweza asimkute babu yake, ndipo
ikamlazimu kuondoka.
Akamgeukia vizuri. “Niangalie Tunda.” Tunda akamwangalia vizuri. “Nikikwambia hata mimi natamani nisiondoke, utaamini?” Tunda akatingisha kichwa kukubali. “Basi ujue nitarudi haraka. Niombee mambo yaende vizuri.” Walitafuta sehemu wakakaa, wakati wakisubiria muda wa Net wakuondoka. Tunda alikuwa amejisogeza karibu yake, ameinama. Hakuondoka mpaka Net alipoingia kwenye ndege.
Maisha bila Net.
Tunda alitulia, akashika usukani. Ni kweli aliiendesha ile ofisi bila shida, huku akitumia gari ya Net na kuishi kwenye nyumba yao. Tunda hakuacha kuwasiliana na Net kumpa taarifa kwa kila kinachoendelea na kumtaka ushauri. Na kwakuwa na yeye alifanywa kuwa muweka saini benki, hata malipo mengine alifanya yeye mwenyewe, tena kwa uaminifu sana. Kila mwishoni mwa juma, alimtumia Net benki statement na ripoti ya matumizi yote. Walishauriana kwenye simu, na Net aliweza kuendesha mambo ya pale ofisini, akiwa mbali, kirahisi sana kwa msaada wa Tunda.
Mapambano Bado Yanaendelea.
Tokea
aachane na Mama Cote pale kanisani hakuwa amemsikia tena huyo mama. Hata
kupokea simu yake ya salamu hakupokea tena. Haikumsumbua Tunda kabisa, alijua
ni hali ya ubusy kwani yule mama alikuwa muhangaikaji sana kisha akawa
amekwenda nchini Canada kumuona huyo mgonjwa ambaye ni mkwewe.
Ilikuwa
siku ya jumamosi ambapo Tunda alishazoea kufanya nusu siku alipokuwa na Net,
lakini sababu ya kuwa peke yake aliitumia hiyo siku kukaa ofisini mpaka usiku.
Alifanya mambo mengi, na akatayarisha ofisi ile kwa siku ya jumatatu. Kijana wa
usafi hakuwa akija siku za jumamosi, kwa hiyo kila alipotumia ofisi siku za
jumamosi, alijitahidi kuacha safi ili asimsumbue kijana wa usafi anapokuja siku
ya jumtatu.
Alishaongea
na Net wakati Canada ilipokuwa usiku wakapeana maelekezo na miahadi yakupigiana
tena simu siku inayofuata, pale Tunda atakapo amka. Tunda akarudi nyumbani
akiwa amechoka sana. Mlinzi akamfungulia geti, akamsalimia kwa kumpungia mkono
akaingia ndani.
Alipoingia ndani, akakuta Mama
Cote amekaa na msichana mwingine pale sebuleni. “Net hakuniambia kama mnaishi
naye hapa!” “Sikuwa nikiishi na Net peke yake, mama. Maya ndiye alinikaribisha
hapa.” “Maya!?” “Ndiyo mama. Shikamoo.” “Mwanzoni ulikuwa ukiishi wapi?”
“Hotelini, mama.” “Kweli Net alikubali kukutoa kwenye nyumba za kulala wageni
akakuweka hapa na mtoto mdogo kama Maya!?” Tunda akanyamaza. Hakuwa ameelewa
kabisa, kwani Mama Cote aliyemfahamu yeye alijawa na hekima na mwingi wa
shukurani. Na alimkarimu sana nyumbani kwake, akampa hata chumba chakuweka
mizigo yake na kukitumia kama angelala.
“Kuna
nini mama!?” “Nimeshtuka sana kukukuta nyumbani kwangu!” “Samahani mama,
itakuwa Net amesahau kukwambia. Hata hivyo naweza kuondoka tu hata sasa hivi.”
“Kabla hujaondoka nataka kukutambulisha kwa bosi wako mpya, huyu hapa. Anaitwa
Safia. Safia amesoma na anauzoefu wa kazi, kwa hiyo atakusaidia sana.” “Karibu
sana Safia. Basi jumatatu nitakuonyesha pale ofisini.” “Sio kumuonyesha tu!
Nataka umkabidhi kila kitu, yeye ndiye atakuwa akikwambia kitu gani
chakufanya.” Tunda alishtuka kidogo, lakini hakujali. “Sawa mama.” Tunda
akaitika.
“Na
atakuwa akitumia hicho chumba ulichoweka mizigo yako.” “Hakuna shida mama
yangu. Nitaondoka na kila kitu.” Tunda akaingia ndani, akakusanya vitu vyake
vyote, akaweka kwenye begi lake akaanza kulivuta kulitoa nje pamoja na mizigo
yake mingine iliyokuwa na nguo, viatu pamoja pochi zake nyingi tu ambazo
alipenda kubadili kama viatu. Akakumbuka amesahau funguo za gari ndani.
Akarudi
wakati ameacha mizigo yake yote nje. Alipoingi tu, “Halafu binti!” Tunda
hakujua kama anaitwa yeye, aliendelea kuelekea kule alipokuwa ameacha pochi
yake aliyotumia siku hiyo. “Wewe Tunda, umeanza lini kiburi?” “Kwa nini mama?”
“Nakuita kwa nini unanyamaza!?” “Sikujua kama unaniita mimi. Samahani.” Tunda
aliendelea kujibu kwa heshima sana.
“Naomba
na funguo za gari. Atakuwa akitumia yeye hilo gari, kabla hatujamnunulia la
kwake.” Tunda alifikiria kidogo. “Sasa hivi ni usiku mama. Naomba niondoke na
gari, kisha nitarudisha gari asubuhi ili nisipate shida ya usafiri na mizigo
yangu.” “Naweza kukuitia taksii.” Tunda akatulia kidogo, kisha akamsogelea Mama
Cote.
“Kwani
kuna tatizo lolote mama yangu? Mbona kama..” “Hakuna tatizo lolote. Mimi ndiye
mmiliki wa kila kitu, au Net hakukwambia hilo?” “Nafahamu.” “Sasa unauliza nini
endapo mwenye mali anadai mali zake!?” Tunda akabaki ameduaa.
“Na
ninaomba funguo za ofisini kabisa, pamoja nafunguo za safe. Kwa kifupi naomba
funguo zote za ofisi na simu ya ofisi pia naomba.” “Unamaanisha simu yangu ya
mkononi!?” “Si ulinunuliwa kwa matumizi ya ofisini? Sasa unapunguziwa majukumu,
huhitaji tena simu ya mkononi.” Tunda alibaki ametoa macho kwa muda.
“Vipi?
Au uliahidiwa nini na Net? Isijekuwa navunja makubaliano fulani.” Tunda alivuta
pumzi kwa nguvu, kisha akanyanyua pochi yake, akatoa simu na funguo zote za
ofisi na gari kisha akamkabidhi. “Asante mama, usiku mwema.” Tunda akaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ulikuwa
ni mshtuko mkubwa sana kwa Tunda. Alijiuliza maswali mengi bila kupata jibu.
Alifikiri hili na lile bila kuhisi kosa lake. Alikuwa na wakati mgumu sana
akisubiria hiyo siku ya jumatatu, hata kanisani alishindwa kwenda.
Hakuwa
na simu ya kuwasiliana na Net, kwa kuwa simu alinyang’anywa. Simu yake ilipotea
kwenye mazingira ya kutatanisha. Hakujua kama aliiacha sehemu au aliibiwa
kwenye pochi. Alijikuta hana simu ndipo Net akampa iliyokuwepo tu pale ofisini
na kumtaka aitumie akisema ni muhimu kwa kazi kwa kuwa yeye alimwambia hana
shida tena na simu. Hana mtu wakuwasiliana naye. Lakini yule mama alimpokonya.
Ilikuwa simu nzuri sana.
Jumatatu
ya machungu na mapinduzi!
Siku
hiyo ya jumatatu aliamka mapema, na kuwahi ofisini. Alifika ofisini na kumkuta
Mama Cote yupo ofisini kwa Net, na Safia yupo kwenye meza yake. Tunda aliweka
pochi yake pembeni ya meza, akaingia kumsalimia Mama Cote. “Shikamoo mama.”
“Naona hapa mambo yamekuwa yakiendeshwa kienyeji enyeji kweli! Sioni faili lako
la kuajiriwa. Sioni vyeti vyako wala barua zako zakuomba kazi.” Tunda akabaki
kimya, lakini mwili mzima ukitetemeka.
“Naomba
ukaniletee vyeti vyako vyote vya shule,
ili tujue kama ni kazi ninakuajiri upande upi.” Tunda alibaki kama
amepigwa na butwa. Kimya. “Umenisikia?” “Sina vyeti mama.” “Kwa nini huna
vyeti?” “Sina vyeti kabisa.” “Kwani hukusoma!?” Yule mama akamuuliza kwa namna
yakumdhalilisha mbele ya Safia na yule kijana wa usafi, waliokuwa wakisikiliza
pale nje. Tunda akanyamaza.
“Hata
cheti cha kidato cha nne huna!?” “Sina mama.” Tunda alishaanza kupaniki. Hofu
yakufukuzwa kazi ikamjaa. “Wewe ulilemea upande mmoja tu, kutembea na wanaume
za watu! Ukapata ujuzi wa kuvutia wanaume, ukakosa ujuzi wa ofisini! Sasa hapa
Net wa kumrembulia macho ili aendelee kukuweka hapa ofisini, hayupo. Hii ni
ofisi yangu. Nimehangaika sana kufika hapa nilipo. Sikutafuta pesa kwa kuvulia
nguo waume za watu, nimehangaika mimi mwenyewe. Uzembe mdogomdogo sitaki.
Hamkawii kunirudisha chini kimaendeleo!” Yule mama alianza kupiga mahesabu,
kisha akanyanyuka.
Akafungua
safe akatoa pesa. “Huu ndio mshahara wako wa mpaka siku ya leo. Rudi shule
binti, acha kuruka ruka na wanaume. Ukishapata vyeti ndipo urudi tuzungumze.”
Bila kuongeza neno, Tunda akapokea pesa yake, na kuondoka pale.
T |
unda alirudi hotelini, akakaa
chini asiamini kinachomtokea. Aliumia sana kusikia anatukanwa na Mama Cote, kwa
kupitia maneno aliyosema kanisani, tena akiwa ameambiwa ni sehemu pekee ambapo
atakuwa salama! Tunda akalia sana, lakini alikumbuka jinsi alivyofundishwa na
Net kuomba.
Akapiga
magoti akamuomba Mungu kwa kulia sana. Tunda akamlilia Mungu kwa uchungu
akirudia rudia kumweleza maumivu aliyonayo. Hakuwa mjuaji sana wakuomba, lakini
alijua kumueleza Mungu kile alichokuwa akijisikia. “Naogopa
sana Mungu wangu. Nimeumia, nina maumivu makali sana. Sijasoma, sina kimbilio,
sijui naanzia wapi tena maisha. Katika yote naomba nisaidie nilinde mwili wangu
usiteswe tena. Sitaki kurudia yale maisha tena. Nisaidie kwa njia yeyote ile
ili niweze kuishi kwa uwezo au karama yeyote uliyoniumba nayo, ukaweka ndani
yangu kama alivyoniambia Net, kuwa kuna kipaji lazima umekiweka ndani yangu
ambacho kitanisaidia. Usiniache tena. Milango yote naiona imefungwa, lakini
najua Mungu wewe unaona kwa tofauti. Nisaidie.” Tunda akamaliza kuomba,
akapata faraja ya ajabu.
Wazo
la kurudi Dar likamjia. Hakutaka kupoteza muda tena pale hotelini, akabeba
mizigo yake yote, asubuhi hiyo hiyo akaenda kituo cha mabasi pale jijini
Arusha, akakata tiketi yake akapanda basi kurudi Dar. Alionelea ni heri kurudi
Dar, mji alioufahamu vizuri kuliko kuendelea kuishi Arusha. Hata hivyo vitu
vyake vyote aliviacha huko.
Tunda arudi jijini Dar na kupambana Njiani na Jaribu akumrudisha
kule Yesu alikomtoa kupitia Net.
Tunda alipata
siti ya upande wa watu wawili. Pembeni yake alikaa baba mmoja mtu mzima kidogo.
Walisha salimiana, lakini yule Mzee hakutosheka kumtizama Tunda. Na Tunda
alijua. Akaamua kutoa bibilia yake asome ili kumfanya yule baba amuogope. “Soma
kwa sauti basi na mimi nisikie neno.” Yule mzee alimtupia neno Tunda.
“Naweza
nikakupa tu, usome mwenyewe.” Tunda akataka kumkabidhi. “Unakwenda kanisa
gani?” Tunda hakuwa hata na kanisa analolifahamu huko Dar. “Ndio nahamia Dar,
bado sijajua nitapata wapi kanisa.” “Ooh! Karibu sana jijini. Kwa hiyo hata
sehemu yakuishi bado hujapata?” “Ndio naelekea huko. Naamini nikifika huko
nitapata.” “Basi mimi niwe mwenyeji wako. Nina nyumba yangu napangisha vyumba
huko Temeke. Naweza kukupangisha. Tena kuna mpangaji mmoja ametoka juma
lililopita tu, nilikuwa nakikarabati hicho chumba. Ni chumba kimoja na sebule
yake. Kwa kuwa ndio unahamia hata huna haja yakunilipa kodi kwa sasa,
tutakatana juu kwa juu.” Tunda alitabasamu kisha akageukia dirishani.
“Vipi?”
Akaendelea kutaka Tunda amsikilize. “Na kanisani nitakupeleka usiwe na
wasiwasi.” Tunda alimgeukia yule Mzee akamtizama kwa muda, asiamini. “Au hutaki
kuishi Temeke? Tunaweza tukashukia hotelini wakati tunatafuta nyumba nzuri ya
wewe kuishi.” Tunda alifunga bibilia yake akairudisha kwenye pochi yake, .......
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ni sura tu ya matukio ndio inabadilika, lakini
historia kujirudia kwa Tunda, inabaki palepale. Na hapo napo anafukuzwa baada
ya kutenda mema, yakusifika na kuvutia, lakini napo ikadumu kwa muda tu, bila
kujijua, akidhani ameokoka na dhoruba, kibao kimegeuzwa tena na Ulimwengu
umeshamfungulia tena mikono kumpokea. Ahadi ya matunzo ipo kiti cha pembeni
yake. Baba mtumzima kama wateja zake wa zamani. Amekwama, anahitaji msaada. Safari
hii hakuna Net wakumuokoa. Tunda atafanyaje?
Endelea
kufuatilia kujua ni nini atafanya na kwa
nini Mama Cote naye ambadilikie gafla!!!!
0 Comments:
Post a Comment