Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Nilipotea! - Sehemu ya 18. - Naomi Simulizi

Nilipotea! - Sehemu ya 18.

 

G

abriel alimuona vile Net alivyobadilika. “What Net? Nini?” Gabriel aliuliza kwa kujihami baada ya kumuona jinsi Netanavyomuangalia. “No man! Hamna neno.” Net alijibu na uso ulionekana kusikitishwa sana na rafiki yake. “No. Say it. Just say it Net. Kumbuka mimi nakufahamu wewe vizuri sana Net. Wewe ongea tu kile kilichopo mooni mwako. Maana ni wewe mwenyewe ndiye uliyeniambia niachane na huyu msichana. Tena kwa mikwara mingi sana! Nilikwambia jinsi ninavyompenda Nancy.” “Hujawahi kumpenda. Ulikuwa ukitumia tu mwili wake, lakini si kumpenda.” Net akamkatalia Gabriel na kumshangaza.

“Unajuaje!? Nilimpenda na….” “Please don’t. Just Don’t. Nyamaza  tu.” “What’s wrong with you Net? Unatatizo gani Net!? Mbona mimi sikuelewi?” Net aligeuka akataka kuondoka, kisha akamgeukia rafiki yake tena. “Na kwa taarifa yako tu Gabriel, jina lake ni Tunda, sio Nancy.” Gabriel alibaki ametoa macho asielewe, huku manyunyu ya mvua yakiongeza kasi kuashiria mvua kubwa inakaribia kumwagika. 

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Tunda alienda kuchukua mizigo yake aliyokuwa ameiacha pale mapokezi asijue anarudije Dar, na hata usiku huo anakwenda wapi. Alitoka pale hotelini taratibu huku akilia kwa uchungu sana. Mvua kubwa na radi iliyoanza gafla ilimfanya akimbilie kwenye moja ya jengo la hoteli hiyo. Alikimbia mwisho kabisa kwenye kona akajibanza huku akilia kwa hofu.

Kwa asili Tunda alikuwa muoga sana wa radi. Alianza kutetemeka baridi, kwani pale alipojificha pia mvua ilikuwa ikimfikia na hali ya hewa jijini Arusha ilikuwa baridi haswa. Tunda hakuwa hata amevaa sweta. Baridi na hofu vilimjaa, na kila aliposikia ngurumo za radi alizidi kutetemeka na kuzidi kulia. Pesa ya kuchukua taksii hakuwa nayo. Halafu akajiuliza, hata akichukua taksii, inampeleka wapi usiku ule! Akaendelea kulia. Mambo yamembadilikia gafla.

Aliona gari ikizunguka pale, ikienda na kurudi mara kadhaa. Tunda aliendelea kulia. Baada ya muda akamuona mtu akikimbia, kwenda na kurudi. Mvua kubwa bado ilikuwa ikinyesha. Kwa mbalii akasikia mtu akiita jina lake. “Tundaa! Tundaaaaaa!” Alihisi ni mawazo. Lakini kila alipojaribu kupuuzia ile sauti ndivyo alivyoisikia kwa karibu zaidi.

Akasimama kutaka kuthibitisha kama ni mawazo yake au la. Akajitokeza pale alipokuwa amejificha na kuchungulia nje huku radi ikipiga sana. “Tundaaa!” Ana kwa ana na Net, aliyekuwa amelowa chapachapa. Net alikuwa akimwita kama mwehu. Alipomtambua kuwa ni Net, Tunda alifunika uso wake nakuzidi kulia kwa aibu na uchungu. 

Net alimsogelea karibu kabisa, akasimama mbele yake asijue aseme nini tena. Alibaki akihema kama mbwa aliyekimbia mwendo mrefu sana. Akabaki akimtizama Tunda. Tunda akajua ni yeye ndiye aliyemuona akikimbia. Wakabaki wamesimama pale. Tunda akilia huku amejificha uso, akiwa amebeba mizigo yake, Net akihema.

“Twende kwenye gari.” Net alimpokea mabegi yake, akayabeba kwa mkono mmoja, kisha akamshika mkono Tunda kwa mkono wake mwingine, akamuongoza lilipokuwepo gari yake. Wote wawili walikuwa wamelowa haswa. Akamfungulia mlango wa gari, kiti cha mbele, Tunda akapanda na kujikunja kwenye kile kiti huku akitetemeka baridi. Net aliwasha heater ili kuleta joto mle ndani ya gari. Tunda aliendelea kulia mpaka alipopitiwa na usingizi. Hakujali anapopelekwa na Net, akalala.

Net aliendesha mpaka hoteli nyingine mbali kidogo na ile hoteli aliyokuwepo Gabriel na mkewe pamoja na mama yake Net, akaingia yeye mwenyewe kwanza akachukua chumba ndipo alipoenda kumuamsha Tunda. “Twende ukalale ndani.” Net alimbebea vitu vyake akaongoza mpaka chumbani. Kilikuwa ni chumba chenye kitanda kimoja tu, kochi na choo humo humo ndani.

Akamuwekea mizigo yake mle ndani nayo ilikuwa inachuruzika maji. “Pumzika nitakuona kesho.” Tunda alishindwa hata kumtizama Net usoni. Alibaki akilia sana, huku amefunika uso wake. Net alibaki kimya huku bado amesimama pale asijue aseme nini.

“Nenda kabadili nguo utaanza kukohoa. Nitawaambia hapo mapokezi wakuletee chakula. Utataka kula nini?” Tunda akatingisha kichwa kukataa bila hata kumtizama. “Basi nitakuoana kesho. Usiku mwema.” Net alisimama tena mlangoni kwa muda bila kusema kitu. Lakini ni kama maneno mengine yaligoma kutoka, gafla akajikuta hajui aseme nini tena. Akaona ni heri aondoke tu. Alipomuona Tunda anaelekea bafuni, akatoka na kufunga mlango.

Kesho yake asubuhi aliletewa kifungua kinywa na muhudumu wa ile hoteli, bila hata yakupiga simu kuagiza. Mchana akaletewa tena chakula cha mchana. Lakini ilipofika jioni aliamua kupiga simu mapokezi kuwaomba wasilete tena chakula kingine usiku.

Ilipofika saa mbili, akasikia mlango ukigongwa. Alisimama kwenda kufungua. Alikuwa Net. Mwili mzima wa Tunda ulikuwa ukitetemeka baada yakumuona Net. Alimpisha mlangoni, Net akaingia.

“Mbona wameniambia umekataa chakula cha usiku?” “Bado nimebakiza kile cha mchana. Sikula, nilikuwa bado nimeshiba” “Sasa sikitakuwa kimeharibika?” “Hapana. Bado kizuri tu.” Net alikaa kwenye kochi nakujiegemeza. Tunda akabaki amesimama pale pale mlangoni, Net akamgeukia. “Vipi! Mbona hukai?” Tunda alikwenda kukaa pembeni ya kitanda akainama.

“Tumefungua ofisi nyingine huku Arusha, nimekuwa huku kwa muda mrefu kidogo. Nipo kwenye kutafuta watu wakunisaidia kazi. Kama unataka kazi, unaweza kupata.” Tunda akatulia tu kama hakuwa akiongeleshwa yeye. Akabaki ameinama. “Tunda?” “Sijasoma Net. Sina kitu kichwani. Elimu niliyonayo ni kama ya darasa la pili tu.” Net alitulia akimwangalia mrembo mwenye elimu ya darasa la pili. Bado Tunda alikuwa ameinama nakushindwa kumwangalia kabisa Net.

“Kila kitu ni kujifunza Tunda. Ukiwa na nia hakuna kinachoshindikana. Hata hivyo sio kazi zote zinahitaji elimu.” “Nitaishi wapi huku Arusha?” “Sio lazima ukaendelea kuishi huku. Nahitaji msaada kwa sasa mpaka nitakapopata watu wa kudumu. Ukipenda kubaki sawa, ukitaka kuondoka baadaye pia siyo mbaya.” “Asante.” “Huwa unafanya kazi siku za jumamosi?” “Sina kitu chakufanya kwa sasa, naweza kufanya tu kazi.” “Basi nitakuja kukuchukua kesho twende wote kazini.” “Asante Net. Asante sana.” “Karibu. Nitakuona kesho.” Net akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Net alirudi pale hotelini asubuhi hiyo ya jumamosi akamkuta Tunda alishajiandaa. Alimtizama mara mbili mbili, Tunda alikuwa amependeza sana, lakini uso ulijaa majonzi. Net alimchukua mpaka ofisini. Ofisi ilikuwa nzuri na yenye vitu vya kisasa tupu, lakini havijapangiliwa. Tunda akaanza kubabaishwa na aina ile ya ofisi nakujiona hafai kuwepo kwenye meza nzuri za kiofisi, viti vyakuzunguka kama vile na makabati ya kioo! Ilikuwa rahisi kuigiza ni msomi na anakazi sehemu fulani. Lakini akakumbana na uhalisia, anatakiwa aishi kile alichokuwa akikiigiza kwa muda mrefu, hofu yakuishi vile ikamwingia.

“Ninae dada mmoja tu anayenisaidia. Naona kama analemewa kuwa peke yake. Jumatatu utakutana naye, atakuelekeza baadhi ya mambo ya kufanya.” “Sidhani kama nitaweza. Naona kama…..” Tunda akasita. “Sijui Net! Sina uwezo huo.” Net alibaki akimwangalia anavyojitetea kwa kubabaika. “Siwezi kukaa kwenye ofisi kama hii! Nitakuwa nikifanya nini?” “Mbona unashindwa kitu ambacho hata hujajaribu Tunda? Umeshajua kazi yenyewe? Au hutaki kuwa hapa? Kama hutaki upo huru kuondoka Tunda. Sitaki niwe nakulazimisha.” Tunda alianza kulia.

“Sina pakwenda Net. Ila nahofia kuharibu.” “Usigope. Utafundishwa taratibu mpaka utaweza. Kwani ulikuwa ukiishi wapi?” “Nilikodi nyumba. Lakini nimeshindwa kulipa kodi. Mwenye kampuni ya Ulinzi amenitumia ujumbe jana usiku kuwa, mlinzi aliyekuwepo pale nyumbani akinilindia vitu vyangu, amempigia simu usiku huo kumwambia mwenye nyumba ameenda pale na kuanza kunitolea vitu vyangu nje.” “Pole sana. Unataka kwenda kuvichukua?” “Nitaviweka wapi? Nipo kama nilivyo hivi.” “Hatuwezi kukosa pakuviweka. Tunaweza kuondoka kesho siku ya jumapili na ndege ya asubuhi nakurudi jioni.” Kwa kulia, Tunda hata hakusikia kauli sahihi ya ‘tuna’. Yaani Net akijiunganisha. Akaendelea kulia.

“Sina hata nauli ya basi, nitaweza wapi ya ndege!?” “Kwanza umekubaliana na wazo langu?” “Wazo ni zuri, lakini utekelezaji wake ndio mgumu. Nikifikiria pakuweka hivyo vitu ndio nachanganyikiwa kabisa. Sina ndugu wala rafiki kwenye ule mji.” “Kwanza naomba unyamaze. Acha kulia. Halafu nashauri twende wote kwanza tukaviangalie ndio tutajua pakuviweka.” “Asante Net.” “Basi usilie. Tufanye kile kinachowezekana sasa hivi kwanza. Hatua moja hadi nyingine. Sawa?” Hapo Tunda akawa ameelewa kuwa na yeye atasaidia. “Sawa?” Tunda akatingisha kichwa kukubali. Net akaingia ofisini kwake, akamwambia Tunda akae pale kwenye meza ya mapokezi amsubirie kidogo.

Walishinda siku nzima pale kazini. Net akionekana ana kazi nyingi zakufanya. Alibaki ofisini kwake bila kutoka. Tunda akahisi amemsahau. Akaangaza macho akijiuliza kitu chakufanya. Maana muda ulizidi kwenda, yeye amekaa tu. Mwishoe akaamua kusafisha na kupanga ile  ofisi iliyokuwa imejaa vitu vizuri, lakini hakuna mpangilio.

Akazunguka hapo ndani akakuta jiko na choo. Akapata vifaa vya usafi. Akaanza kusafisha. Net bado alikuwa ofisini kwake. Tunda hakujua kinachoendelea huko ndani. Ofisi yake ilikuwa ndani na mlango umerudishiwa. Pako kimyaa. Tunda akaanza kusafisha na kupanga ofisi nzima bila kusababisha kelele. Aliendelea kusafisha kwa haraka huku akimsubiria bosi wake atoke ampe kazi.

Baada ya muda ndipo Net akatoka nakubaki akishangaa. “Nimesafisha na kupanga. Sijui ni sawa?” Tunda alimuwahi huku akimalizia kuweka mafaili yaliyokuwa sakafuni, na kuyapanga kwenye kabati ambalo bado lilionekana jipya tu, zuri sana lenye milango ya kioo mbele, lakini lilikuwa tupu kabisa. “Ona kulivyopendeza! Angalau panaeleweka sasa hivi. Halafu unasema huwezi kufanya kitu chochote! Hapo si umefanya kitu kizuri kabisa? Pamependeza sana. Mama akija kurudi tena atashangaa sana.” Tunda alifurahi kuona amepongezwa.

“Nimewasiliana na watu wa ndege, tumepata tiketi ya asubuhi sana. Utaweza kusafiri asubuhi hiyo?” “Nitaweza. Asante.” “Twende basi tukale, uwahi kulala. Kesho nitakuja kukuchukua mapema sana.” Net alimpeleka sehemu ambayo alidhani Tunda hapafahamu kumbe vilikuwa ndio viwanja vyao yeye na Gabriel. Net alimwambia waende wenyewe jikoni wakachague nyama.

Wakaongozana mpaka kwenye dirisha la jikoni. Walikuta watu wengine wakisubiri. Na wao wakajiweka kwenye foleni yakusubiria. Mchoma nyama ndani alipomuona tu Tunda, akaanza kumchangamkia, kwani alimfahamu yeye na Gabriel jinsi walivyokuwa wakiwapa tip/pesa pale kila walipokuwa wakienda kula nyama choma.

“Mzee yuko wapi?” Yule kijana alimuuliza akiwa ameonyesha kumchangamkia kweli Tunda huku akiendelea kuchoma nyama. Tunda akaanza kubabaika, Net alibaki kimya pembeni. “Au leo uko peke yako?” “Sikuja naye.” Tunda akajibu kwa shida kidogo huku akijikanyaga kanyaga.

Walirudi mezani Tunda alishindwa kuongea kabisa. Wahudumu wote walimuulizia Gabriel, mwishowe Tunda akaamua kuondoka pale. “Naomba nikakusubirie kwenye gari, Net.” “Basi ngoja niwaambie watuletee chakula hukohuko kwenye gari, tutaenda kula hotelini.” Tunda alijisikia vibaya sana. Akatoka pale bila hata kusubiria zaidi.

Baada ya muda akamuona Net anarudi garini na chakula. “Naona tumefanyiwa upendeleo. Nilienda kuaga, naona wamenikabidhi chakula.” Tunda akakumbuka walikuwa wakifanyiwa hivyo hivyo kila walipokuwa wakienda pale na Gabriel kwa kuwa Gabriel alikuwa akiwapa tip nzuri.

Walirudi hotelini Tunda akiwa kimya kabisa na Net hakutaka kuuliza. Net aliwasha tv mara tu alipoingia chumbani kwa Tunda na kujitupa kwenye kochi. Alikula chakula chake huku akiangalia tv. Alibadilisha tv huku na kule ili kupata taarifa ya habari wakati akiendelea kula. Alipomaliza kula na kuangalia taarifa ya habari, akataka kuondoka. Tunda na yeye alikuwa ameshamaliza kula.

“Nitarudi kesho asubuhi na mapema, Tunda. Usichelewe kulala.” “Lakini Net.” Tunda alimuwahi Net akiwa anataka kutoka, akiwa amesimama, na yeye akasimama huku akibabaika sana. Alimuogopa sana Net, hata hakuwa akiweza kumwangalia vizuri. Net alibaki akimwangalia vile anavyotetemeka mbele yake. “Kuna nini?” Net akamuuliza taratibu. “Au usiku mwema.” Tunda alishindwa kuongea kwa hofu, akaamua kumuaga tu.

Net akarudi kukaa. Taratibu machozi yalianza kumtoka tena Tunda. “Vipi Tunda?” “Naona tuache tu.” “Nini?” Net akauliza. “Hiyo safari ya Dar. Nitakuja kwenda wakati mwingine.” “Kwa nini? Unajua nimeshakata tiketi?” “Samahani, lakini nadaiwa. Siwezi kurudi mikono mitupu, bila pesa za watu.” Net akatulia kidogo.

“Nani anakudai?” Net akauliza. Tunda akajifuta machozi na kujaribu kutulia. “Kodi ya miezi 3, kampuni ya ulinzi na kijana niliyemwajiri wa kazi.” “Kwa hiyo unataka kukimbia deni?” Net akamuuliza taratibu tu. “Sijui chakufanya Net. Sielewi nitafanya nini. Kwa mfano yule kijana wa kazi alikuwa akinipigia simu siku nzima ya leo akitaka nimpe pesa yake. Ndio jioni hii nimemtumia ujumbe, wakumtaarifu kuwa bado sijapata pesa, ila anaweza kwenda kuchukua kitu chochote kwenye vitu vyangu kama kujilipa. Hajanijibu. Haya, yule mmiliki wa kampuni ya ulinzi alinipigia simu siku ya jana akinitishia kunipeleka polisi kama sitampa pesa yake. Ameniambia jumatatu ndio mwisho. Nataka na yeye nimuombe kama anaweza kuchukua baadhi ya vitu vyangu, akae navyo mpaka nitakapo mlipa. Ila kodi ndio inanichanganya zaidi, sijui nitafanyaje!”

“Usiwe na wasiwasi, wewe twende tu. Watumie ujumbe sasa hivi, waambie ukutane nao wote hapo nyumbani kwako, siku ya kesho asubuhi ya saa nne. Na uwaambie wasichelewe, kwa kuwa tunarudi kesho hiyo hiyo huku Arusha. Hatutakuwa na muda wa kumsubiri mtu.” Tunda alifuta machozi kwa mikono yake, akafuata simu yake, akatuma ujumbe kwa wote kama alivyoambiwa na Net.

“Nimeshawatumia.” “Naomba uniambie kila mmoja anakudai kiasi gani. Nitawalipa kwa hundi. Unafikiri ni sawa? Maana sina pesa hapa mfukoni.” “Hawatakuwa na shida. Wanachotaka ni kulipwa.” Tunda akajibu na kumtajia kwa woga sana kiwango anachodaiwa na kila mmoja wao. “Lakini Net, naweza kuwaomba niwalipe kidogo kidogo. Sio lazima kuwalipa zote kwa pamoja.” Net akasimama. “Usiwe na wasiwasi. Wewe lala. Nitakufuata kesho.” “Asante sana Net. Nakushukuru.” “Karibu. Usiku mwema.” “Na wewe.” Net akatoka.

Alipofunga mlango tu, Tunda akaanza kulia kwa uchungu sana. Net alibaki nje ya mlango akimsikiliza jinsi anavyolia kwa kuugua. Alitamani arudi ndani, lakini aliona aache tu. Tunda aliendelea kulia kwa muda mrefu sana huku akigugumia kama mtu asimsikie. Alifika mwisho kabisa. Kama ni kuzama kisimani, basi alishazama na kunywa maji mengi sana, akabaki akielea kama mzoga.

Aibu ilikuwa imemuandama, hofu ndiyo ilizidi kumtesa. Net ndiye mtu wa mwisho kabisa kwenye Maisha yake angetamani kuwa naye karibu, kwa vile anavyomfahamu kwa uchafu wake. Alijua Net anamjua jinsi alivyo mchafu, yeye mwenyewe alijionea kinyaa. Net je? Alijiuliza huku akitamani asiwe Net anayemsaidia. Lakini hakuwa na namna nyingine. Alibanwa vyakutosha. Net aliposikia kimya, akajua amepitiwa na usingizi, ndipo alipoondoka.  

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

N

et alifika hotelini hapo asubuhi hiyo na mapema akamkuta Tunda alishajiandaa, anamsubiria akiwa mnyonge na macho mekundu. Alionekana aliamka na kuanza kulia tena. Net aliogopa kuuliza asije akaanzisha kilio kingine na kushindwa kuwahi ndege. Waliondoka mpaka uwanja wa ndege, akaacha gari lake uwanjani hapo, wakaenda kupanda ndege kuelekea Dar. Tunda alipofika tu kwenye ndege, alilala mpaka Net alipomuamsha kuwa wamefika. Alikuwa amechoka, zaidi akili.

Ndege ilitua jijini Dar, Net akamkuta Wanja, mtu anayemtumia kwa maswala ya usafiri hapo Dar. Alikuwa akimiliki magari makubwa na madogo anayofanyia biashara. Ndiye aliyemuomba afike hapo awasaidie usafiri wa kuwapeleka kwa Tunda akijua hata huko atakuwa msaada wakupata usafiri mwingine. “Nakushukuru sana Mkuu, na samahani kwa kukusumbua najua leo jumapili ni siku ya familia.” “Hamna shida kabisa. Nilipomwambia tu wife kuwa ni wewe, akaniambia nikimbie haraka sana.”  Wote wakacheka. Tunda alikuwa ameingia chooni mara tu walipotoka kwenye ndege. Kwa hiyo Net alikuwa na mwenyeji wake tu wamesimama wakiongea wakati wakimsubiria Tunda.

Alitoka chooni, na kuwasogelea pale walipokuwa wamesimama. Jicho kwa jicho na mteja wake huyo Wanja. “Judy!” Tunda aliinama. Net akabaki akiwatizama, kama aliyeshtuka. Hakutegemea hata Wanja! Alionekana mtu wa familia na mwadilifu. Wanja akajaribu kupotezea, lakini asijue Net anaelewa kila kitu. “Nafahamiana na huyu dada alinisaidia lifti kipindi gari langu lilipoharibika. Hata jina lake simfahamu vizuri.” Akajichanganya. Gafla akasahau kuwa alitoka kumwita Tunda, jina la Judy na wala Tunda hakuwahi kumiliki gari. Akajitetea kwa kubabaika sana huku akiongopa. “Ooh! Kumbe hamna haja ya utambulisho? Basi twendeni.” Net akajibu na kuwaacha wakitizamana nyuma yake. Kisha wakamfuata.

Tunda alipanda garini akabaki ameinama bila hata kuongea. Tunakutegemea wewe Tunda ili utuambie ni wapi unaishi na utuongoze njia. Nataka tuone vitu vyenyewe kwanza ndipo nijue ni aina gani ya gari itahitajika kuvibeba.” Tunda akanyanyua uso. Hakuwahi kutaja jina la mtaa anaoishi hata mara moja. Ni kama alilifuta hilo jina kichwani mwake kwa makusudi ili asije wahi hata kuropoka kwa mtu. Akabakia kujua njia tu.

“Nielekee wapi?” Wanja ambaye ni dereva akauliza wakati anatoa gari pale uwanja wa ndege. “La Dolce Vita.” Tunda akajibu taratibu. Mpaka Net akamgeukia. “Unamaanisha unaishi mitaa ya karibu ya ile hoteli ya La Dolce Vita ya Oyster bay!?” Net akauliza kwa mshangao. “Ndiyo. Twendeni mpaka kule baharini kabisa. Nyumba haipo mbali na ilipo hoteli.” Tunda alijibu kwa upole, Net akaelewa ni kwa nini anadaiwa kodi kubwa vile. Dereva akakanyaga mafuta, Tunda akarudisha uso wake kuangalia chini     .

Dereva alipofika mpaka baharini akataka kuelekea Coco Beach, Tunda akamwambia akate kona kulia. Akamuelekeza mpaka kwenye nyumba aliyokuwa akiishi.

“Hapa ndio kwako Tunda!?” Net akauliza kwa mshangao. “Ndiyo.” Nyumba ndogo lakini nzuri sana. Ilikuwa ya kisasa. Kuanzia getini mpaka ndani, ungependa. AC ilikuwa nyumba nzima. Pasafi. Kuja kuona hivyo vitu vyenyewe vya Tunda, ambavyo baadhi vilishaanza kutolewa nje, Net akamwangalia Tunda.

Vilikuwa vitu vizuri, vilivyotangaza utajiri mtupu kwa kuviangalia tu kwa macho. Marembo ya dhahabu nzuri iliyokatwa kwa ustadi yalizungushiwa kwenye kila kifaa cha Tunda. Kitanda, meza zake, makabati, vioo vyakujiangalia, meza yakujitengenezea na viti vyake, kila kitu kilikuwa na marembo mazuri sana na manyoya mazito meupe.

“Ulipata wapi haya makochi, meza…!? Kila kitu!” Wanja aliuliza kwa kushangaa sana. “Nilienda kununua Arabuni.” Tunda alijibu kiunyonge bila ujasiri.

“Daah! Ni vizuri sana. Sijawahi on ahata kwenye picha! Na vinaonekana ni vya thamani sana. Kwa ile lori yangu, Mkuu, itabidi kubeba hata mara tatu. Hivi vyombo ni vingi sana na vyote vinaonekana ni vya thamani sana. Tukivibebanisha, tutaharibu.” Net alibaki kimya akiwaza huku akiangalia vile vitu vyote, akifikiria pakuviweka. “Unapakuviweka lakini?”  Wanja akamuuliza Net. “Maadamu tupo hapa, lazima tutatafutia ufumbuzi. Hatutashindwa. ” Net akajibu na kuendelea. “Ili kuokoa muda, naomba ukatutafutie usafiri unaweza kubeba hivi vitu.” Wanja akaondoka na kuwaacha Tunda na Net.

Baada ya muda kidogo, akaingia mwenye nyumba na mwenye kampuni ya ulinzi. Ni kama waliongozana. Tunda akasalimia. “Ulituambia tuje leo.” Mwenye nyumba akavunja ukimya. Net akawasogelea. “Nashukuru kwa kuwa hapa. Niombe kama mtaridhia, mpokee hundi.” “Bila shida. Ilimradi tumalizane kwa amani.” Mwenye kampuni ya ulinzi akajibu.

Net alikuwa ameshawaandikia hundi zao kutokea Arusha. Alichofanya ni kumkabidhi Tunda anayewafahamu, ili awakabidhi bila kuchanganya. Tunda akazipokea huku akitetemeka. Hata mikono yake ilikuwa ikionyesha jinsi anavyo tetemeka. Akasoma kiasi kwenye kila hundi, akawakabidhi kila mmoja wao.

Net hakuwa ameandika majina yao, ila pembeni ya sahihi aliandika sababu. Ya kwanza, ‘Kodi ya Tunda.’ Hundi ya pili, ‘Ulinzi wa Tunda.’ Hundi ya tatu, ‘Mfanyakazi.’ Tunda mwenyewe akashangaa vile alivyoandika. Alimtajia tu walipokuwa hotelini, aliondoka pale Tunda akiwa hana uhakika kama atakumbuka. Lakini alikumbuka na akaandika kiasi kwa usahihi.

Aliwakabidhi hao wawili. Wakashukuru.  Wakamsikia mwenye nyumba akimwambia mwenye kampuni ya ulinzi angependa waendelee kulinda hapo mpaka mpangaji mpya atakapohamia hapo week inayokuja. Wakakubaliana, wakaondoka. “Nashukuru Net.” Net akamgeukia Tunda, akamuona anafuta machozi. “Karibu.” Net akajibu.

Baada ya muda wakati Tunda akikusanya vitu vyake vizuri, Net akifungua vitu kama kitanda, nakumsaidia Tunda kuweka vitu vyake pamoja na kirahisi ili viweze kuhamishika, kijana wake Tunda, wa usafi na yeye akafika hapo akiwa na usafiri wa baiskeli akiwa na maboksi mengii. Tunda akamtambulisha kwa Net. “Wewe naomba tumalizane ukishatusaidia kuhamisha hivi vitu hapa. Nitakulipa. Ni sawa, au kuna mahali unataka kuwahi?” Net akamuuliza. “Hamna shida Mkuu.” Akakubali kwa haraka bila shida.

Wakaungana kufungasha pale pale nje. Ni kweli vitu vyake karibu vyote vilikuwa nje. Nguo na viatu bado vilikuwa ndani, na vyombo vya jikoni. Wakasaidia kwa juhudi zote ili gari litakapofika iwe ni kupandisha tu.

Walifanya kazi kubwa. Mpaka lori linafika hapo, walikuwa wameshakusanya karibu kila kitu. Net alimwambia Tunda yeye asibebe vitu vizito. Wao watasaidiana kubeba. Kazi yakupandisha ikaanza, huku Tunda akipandisha nguo zake na viatu. Alikuwa ameweka kwenye masanduku na maboksi aliyoletewa na yule kijana wake wa usafi. Alimuagizia usiku uliopita. Alimwambia afike hapo kuchukua pesa zake, aje na maboksi makubwa na magumu. Na kweli yule kijana alifanya hivyo. Yakamsaidia sana Tunda.

Net na yule rafiki yake, Wanja pamoja na kijana wa Tunda na dereva wa lile lori walisaidiana kupandisha vitu vyote kwa tahadhari. Net akihakikisha hakiharibiki kitu hata kimoja. Akasimamia upangwaji wake, vitu vingine vikawekwa kwenye hiyo gari kubwa iliyokuwa imekuja kuwapokea uwanja wa ndege. Hasa viatu na nguo za Tunda. Walipohakikisha kila kitu kipo ndani ya magari, ndipo Net akamwambia rafiki yake apande kwenye lori, yeye ataendesha gari lake na Tunda. Wawafuate nyuma. Tunda akamuona akizungumza nao yeye akiwa anasubiri ndani ya hiyo gari ya Wanja, akamuona Net anarudi. “Tuondoke sasa.” Akawasha gari na kuondoka, Tunda hata hakuwa akijua wanaelekea wapi. Akaamua kunyamaza tu.

Akaona Net akiongoza njia mpaka Salasala. Tunda alikuwa ametulia kimya akimtizama na kumtafakari bila jibu. Kijana mtulivu. Alionekana kila kitu anakipigia mahesabu na kukifanya kwa makini sana kama asiyetaka kufanya kosa. Yupo makini, na kila walipopita na Tunda, alikuwa ameshaandaa mazingira. Kuanzia wanatoka Arusha, mpaka hapo walipo wanahamisha vitu vyake. Watu waliokutana nao pia aliwaandaa siku moja kabla. Anakwenda kwa muda na mpangilio. “Huyu kweli mzungu.” Alijisemea Tunda.

Waliendesha kimya kimya. Hakuna aliyemuongelesha mwenzake. Kutoka hapo Oysterbay mpaka Salasala. Tunda alikuwa amejiegemeza kimya, haamini kama Net anamtua mzigo mkubwa vile! Akaona wamefika. Net alipiga honi mara moja tu, geti likafunguliwa. “Hapa ni wapi?” Ikabidi Tunda aulize sasa. “Ni kwangu, lakini siishi hapa kwa sasa. Naishi na mama na mdogo wangu akiwa likizo. Kwa hiyo vinaweza kukaa tu hapa.” Tunda akajiweka sawa pale kitini ili kuangalia.

    Na yenyewe ilikuwa nyumba nzuri sana. Ilijengwa peke yake ndani ndani kidogo kwenye huo mtaa wa Salasala. Juu ya mlima. Ukisimama kwa nyuma, unaona bahari kwa kwa mbali na nyumba nyingine. Madhari yake na ramani, Tunda akabaki akishangaa. Ni kama kulipitishwa gari kubwa la greda ili kuchonga sehemu fulani fulani za bustanini. Kulizungushwa rembo za namna yake. Mbele ya hiyo nyumba kulikuwa na sanamu ya kipekee, inayotoa maji mdomoni, yaliyotengeneza bwawa la rangi ya bluu, humzunguka huyo sanamu. Na lile bwawa lilijengewa kisanifu. Tunda akabaki anakodoa macho.

    Net akavuta gari mpaka pembeni ili kupisha lori iliyokuwa imebeba vitu vya Tunda. Akawaonyeshea ishara wapite kama wazunguke nyuma kidogo. “Twende tukawaelekeze, halafu ndipo tutakuja kuchukua vitu vya humu ndani ya hili gari.” Net akashuka, Tunda naye akafuata. Net akamuelekeza dereva wa lori mpaka kwenye kinyumba cha nyuma. Tunda na yeye anafuata nyuma. Kumbe ilikuwa stoo. Walipoingia, palikuwa pakubwa. Humo ndani ni pasafi na kumepangiliwa pia.

    Akaingia kijana aliyemsalimia kwa heshima sana Net. Tunda akajua ni mfanyakazi wake. “Vipi Max?” Akamsikia akimuulizia yule kijana. “Nimetoka kumuogesha sasa hivi na kumpulizia dawa. Yupo sawa.” “Chakula chake bado kipo?” Net aliendelea kuuliza. “Bado kipo kingi tu. Week hii ndio ya chanjo. Nakumbuka. Nitampeleka.” Akajibu yule kijana. “Sawa sawa.” Net akajibu na kumgeukia Tunda.

“Huyu anaitwa Emma. Ndiye anayeishi hapa.” Akamtambulisha kwa Tunda. “Emma, huyu ni Tunda, ndiye mwenye hivi vitu vyote.” Wakasalimiana, Tunda akawa anajiuliza sasa Max ni nani!? Ila kama kawaida yake, akajua hayamuhusu. “Karibu dada.” Akampa mkono Tunda. “Asante.” Tunda akashukuru na kumgeukia Net. Macho yakagongana. “Asante Net.” “Karibu. Njaa inauma sana?” “Hapana. Sijisikii kula kabisa.” Tunda akaanza kutokwa na machozi. Dereva na rafiki wa Net wakaingia na wao.

Net akamshika mkono Tunda na kumsogeza pembeni mpaka sehemu iliyokuwepo makochi. “Naomba utulie. Tumeshapata hii sehemu. Tunaweza kuhifadhi hivi vitu kwa muda wote mpaka utakapokuwa tayari kuvichukua. Kaa hapa kwenye makochi, ni pasafi tu. Nisubiri tusaidiane kushusha vitu, tuondoke. Unataka soda?” “Hapana.” Tunda akakataa. “Basi nitamtuma Emma akuletee maji ya kunywa.” “Asante.” Ndilo neno ambalo Tunda lilikuwa likimtoka kila mara. “Naomba utulie. Naamini kila kitu kitakuwa sawa. Sawa?” Tunda akajifuta machozi, na kuvuta pumzi. “Nakushukuru Net.” “Karibu. Basi ngoja tuanze kazi.” Akamuacha amekaa hapo, akawasogelea wengine.

Akamuona anawaonyesha sehemu ya kuviweka vile vitu vya Tunda. Ukweli palikuwa pakubwa na pazuri. Ilikuwa ni bohari ndio, lakini sakafu yake ilionekana nzuri sana. Upande yaliopo hayo makochi, kulikuwa na kinanda cha kawaida tu. Tv kubwa imening’inizwa na meza yakuchezea tenesi. Kuliwekwa kapeti chini. Zuri sana.

Upande kulikuwa na vifaa vilivyofunikwa na mashuka makubwa. Tunda hakujua ni nini kilichofunikwa humo ndani ya hayo mashuka. Ila nakwenyewe kulikuwa kusafi. Kona ingine kulikuwa na chumba alichohisi ni choo. Ndio upande mwingine ulikuwa wazi kabisa. Ndipo alipoona akielekeza watu waweke vitu vya vyake.

 Alimuona Net akivipangilia vizuri. Walisaidiana wote wanne. Net, Emma, rafiki wa Net, Wanja, ambaye alishakuwa mteja wa Tunda na dereva wa lile lori. Walifanya kwa haraka mpaka wakamaliza. Net akamlipa yule kijana wa lori, akatoa lori yake pale.

Net alilisogeza ile gari ndogo karibu kabisa na mlango. Tunda alipomuona anashusha, akamsogelea. “Usibebe vitu vizito. Emma atatusaidia.” Net na Emma wakashusha mpaka wakamaliza. Vitu vyote vya Tunda viliweza kutoshea kwenye huo upande tena bila kubebanisha. Tunda alibaki na maswali lakini aliogopa kuuliza zaidi kwani alijua Net ndiye ana maswali mengi zaidi yake. “Asante sana Net. Nakushukuru.” “Karibu.” Akabaki amesimama kama anataka kuuliza swali, Net akaelewa. Akaomba Emma na rafiki yake wasubiri nje.

Wakabaki wao wawili. Akamgeukia Tunda. “Sijui nibebe nini kwa kuwa sijui nitakuwa kule kwa muda gani!” Tunda akaonge kinyenyekevu. “Inategemea na wewe. Unataka kuwepo Arusha?” “Sina uchaguzi Net. Kama unafikiri naweza kufundishika, nikaelewa, nitashukuru.” “Naamini utaweza tu. Ondoa hofu.” Tunda akajifuta machozi tena. “Basi naomba muda mfupi wa kuchukua baadhi ya nguo na vitu nitakavyovihitaji.” “Sawa.” Net akatoka nje kama kumpa nafasi.

Tunda alichukua begi kubwa. Akaanza kufungasha. Kila kitu alitamani kubeba. Kila kitu aliona kina umuhimu. Akaanza kulia kuacha vitu vyake. Alilia Tunda, asiamini kuwa ndio ni kama anaanza tena maisha. Alipenda kwake. Alifurahia kila kitu chake kwani alinunua si kwa bahati mbaya. Kila kitu alinunua kwa kusudi. Leo anaviacha stoo! Mpaka lini! Hilo ndilo lilimuogopesha Tunda.

Net akarudi. “Nikusaidie nini?” Akasimama kwa haraka kama aliyefumaniwa tena. “Unaweza kuchukua mabegi hata mawili au matatu. Beba vile utakavyo. Tutalipia kwenye ndege.” Net akaongeza. “Asante.” Tunda akainama kuendelea kufungasha mpaka akamaliza na kujifuta machozi vizuri. “Naona hivi vitatosha. Asante.” “Basi acha nikusaidie kubeba. Wewe beba huo mkoba mdogo. Tuondoke sasa hivi, tuwahi.” Net akachukua yale mabegi wakaondoka. 

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~


    Walirudishwa uwanja wa ndege, na Wanja tayari kwa safari ya kurudi jijini Arusha. Wakiwa kwenye ndege Tunda akiwa amekaa dirishani, Net alimuona akivuta pumzi mara kadhaa na kuzishusha huku akifuta machozi. Baadaye alimuona akijivuta karibu naye, akajiegemeza pembeni yake, akalala. Net alimuhurumia sana Tunda. Alionekana amechoka, zaidi mawazo. Akabaki akimtizama akiwa usingizini, akamfunika vizuri na mtandio wake, akabaki akimtizama huku akimtafakari. 

Walifika Arusha, Net akachukua gari yake sehemu alipokuwa ameegesha asubuhi, akamrudisha hotelini kwake. Wakaingia ndani, kama kawaida yake, alikaa kwenye kochi, kwa mara ya kwanza Tunda akakaa pembeni yake, kama anayetaka kuzungumza kitu lakini anasita. Net aliligundua hilo kwa hiyo hakutaka kuaga kwa haraka, akataka kumsikiliza. Akaamua kuagiza chakula kiwafuate palepale chumbani.

Baada ya muda kikaletwa. Net akiwa anaangalia luninga kama kawaida yake, huku amejiegemeza kwenye kochi, akimsubiri aongee. Kimya. Alimuona vile anavyotetemeka mpaka mikono iliyokuwa imeshikilia ile sahani ya chakula. Mwishoe akamuona amekiweka mapajani, napo sahani ikawa inacheza. Kwamba anatetemeka mpaka miguu. Net akaendelea kula na kubadili channels kama kumtoa kwenye mawazo.

Walimaliza kula bado Tunda alishindwa kuongea. Net naye akawa kama hana haraka. Akaendelea kuangalia tu luninga. Akibadili hiki na kile. “Huwa unapenda kuangalia nini kwenye tv?” Akamuuliza Tunda. Tunda akaanza kufikiria. Hakuwa hata akiangalia tv. Ilikuwepo kwake kama haipo. “Sio mpenzi sana wa tv.” Akajibu taratibu. Net akamwangalia. “Lakini huwa nawasha na kuangalia chochote kilichomo.” Akaendelea Tunda kama anayejitetea.

“Na movie?” Akamuuliza tena. “Napenda ila isiwe za vita au watu wasipigane.” Net akacheka. Nia yake ilikuwa kumtuliza tu ili aongee. Wakatulia kidogo. “Net!” “Vipi?” “Asante.” Net akatabasamu. Maana alishapokea hizo asante, kama nikuziweka kwenye gunia, zingekuwa zikifurika. “Asante kwa kila kitu. Namaanisha kila kitu. Angalau sasa hivi naweza kulala vizuri. Sidaiwi tena. Hiyo kodi ilikuwa inanifanya sipati usingizi. Nilijiingiza kwenye gharama ambazo sikuwa najua nitajitoaje.” “Pole.” Tunda akatulia kidogo.

Kisha akaendelea. “Sitaki kurudia yale maisha tena Net. Hapa hotelini ni gharama sana na kwa kuwa nitakuwa hapa Arusha kwa muda, labda nitafute chumba cha kupanga kwa muda.” “Wazo zuri. Lakini naomba tufikirie kazi kwanza. Tuna mambo mengi sana pale ofisini, hizi gharama za hapa hotelini unapoishi, ofisi italipa.” “Je nikishindwa hiyo kazi Net? Huoni mtakuwa mmepoteza pesa bure? Kwa nini usione kwanza utendaji kazi wangu, ukiridhika ndipo angalau utajua hata kama mnanilipa kiasi gani?” “Acha wasiwasi Tunda! Kila kitu kitakuwa sawa.” Akajibu hivyo tu, tena kirahisi tu. Akakaa tena kidogo, akamuaga kwa makubaliano yakumfuata hapo kesho yake kwenda kazini.

Nafasi Nyingine Tena.

I

lipofika saa mbili kamili, Net alikuwa akigonga mlangoni. Hakuingia hata ndani. “Kama upo tayari, twende.” Tunda akachukua pochi yake kwa haraka na kutoka. Walifika kazini siku hiyo ya jumatatu asubuhi, Net akapokea simu kutoka kwa dada aliyekuwa amemuajiri pale ofisini na kumwambia anauguliwa na mumewe hataweza kufika kazini mpaka atakapopona. Tunda aliingiwa na hofu sana. “Usiogope, nitakuelekeza utaelewa tu. Hata yeye mwenyewe mimi ndiye niliyemfundisha. Halafu mimi mwenyewe nitakuwepo, nitakusaidia.” Tunda akakubali lakini bado alikuwa na hofu sana.

Na hivi Net alionekana makini, hakurupuki! Ni kama hana mlango wa makosa kwenye maisha yake, wasiwasi ulizidi kumwingia Tunda. Hata wateja aliokuwa akiwahudumia kwa ngono, wote waliokuwa wakikutana na Net, au aliofumaniwa nao na Net, walianza kutoa sifa za Net hata kabla hawajakutana naye. Hata Tunda alipokuwa akiwaambia wamwambie Net wakutane club au baa, walikuwa wakisita na wengine kukataa kabisa. Kwamba yupo makini, anakwenda na muda, muadilifu, hataki hata kugusa pombe na kadhalika. Sasa leo umkutanishe na Tunda aliyekwisha kumfumania mara kadhaa, na kila wanayekutana naye, ameshamuhudumia!

Hofu iliyokuwa imemjaa Tunda, alitamani yeye ndio akakae na huyo mgonjwa, muhusika arudi pale kazini. Lakini akajikumbusha hayupo kwenye kuchagua. Amewekwa hotelini ili afanye kazi. Vitu vyake vipo kwenye stoo ya Net, juhudi zake ndio zitakazomfanya avirudishe chini ya himaya yake. Hana pakwenda, hapo alipo ndipo mwisho. Lazima atulize akili, aelewe.

Tunda akatulia kuelewa kwa makini. Na Net naye alimuelekeza taratibu bila haraka, kuhakikisha hapaniki na anaelewa ni nini wanafanya bila shida. Ilikuwa ni Kampuni mpya ya usafirishaji. Walihusika na watalii pamoja na kusafirisha bidhaa ndani na nje ya nchi. Net alimwambia ndio wanaanza tu. Kwa upande wawatalii wao walikuwa ni wakala tu. Wanafanya kazi na mahoteli mengi makubwa ya hapo nchini, walioingia nao ubia.

Wakipokea wao wateja, watatumia usafiri wao kina Net. Lakini watalala kwenye hoteli zao. Kisha hoteli kuwalipa wao asilimia fulani kwa kuwaletea watalii au wateja. Iwe mbugani au mijini na vijijini. Kina Net wao ndio walitumika kama wasafirishaji. Unahama kutoka sehemu moja kwenda nyingine, basi wanakuwa na malori makubwa na madogo, inategemea na ukubwa wa nyumba au ofisi unayotaka kuhamisha. Unayo bidhaa kubwa au ndogo, unataka usafirishe ndani ya nchi au nje, wao kina Net, watakusafirishia.

Kampuni yao ilikuwa ikiitwa African Cote transit. Jina la Net alikuja kugundua kuwa ni Nathaniel Cote. Kwa hiyo akahisi labda ile kampuni ni yake. Ila kama kawaida ya Tunda, haulizi kisichomuhusu, ila kufuata yake. Akaweka akili na kuendelea kumsikiliza Net. Kazi yake ikawa kupokea kazi zote kutoka kwa wateja. Kujua aina ya mzigo au watalii. Anaandika kwenye kompyuta kutokana na aina. Kwa urahisi tu, kompyuta yenyewe inamletea aina ya magari ambayo yapo.

Kama ni wateja wa kuzungushwa mjini, basi itampasa kumsomea mteja aina ya  magari ambayo yapo kwa wakati huo. Kama ni mbugani hivyohivyo. Kama mtu anayehama kutoka sehemu moja kwenda nyingine, Tunda alifundishwa aina ya maswali ya kuuliza. Ukumbwa wa vifaa vya hiyo nyumba anayohamisha. Umbali, na kadhalika.

Kama ni bidhaa, alimfundisha maswali yakuuliza pia. Ukubwa wa hiyo bidhaa, aina yake, umbali wakupelekwa na kadhalika. Kwa hiyo kazi kubwa ilikuwa ni kuelewa vizuri wateja, kuandika na kutoa lugha nzuri kwa kila mteja.

Hilo kwa Tunda likawa halina shida. Kwanza hana tatizo kubwa la lugha. Angalau lugha mbili muhimu alikuwa akizifahamu bila shida. Kingereza na Kiswahili. Pili, Tunda alijaliwa ulimi laini. Mtulivu na anayo lugha ya ushawishi. Akizungumza na wewe hata ukitaka kugairi, atakupanga mpaka ukubali.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kazi ikaanza. Tunda na Net wakisaidiana bega kwa bega. Kwa kuwa ilikuwa siku ya kwanza, Net alikuwepo kumsaidia. Walikuwa naye hapo mezani wakifanya pamoja. Alimsikia Net jinsi anavozungumza na wateja. Maswali gani anayajibu. Akawa anaandika yale maswali aliyoona wateja wengi wanauliza.

Tunda alijua ni kweli wanatengeneza pesa. Walikuwa busy kupita kiasi mpaka ile hali ya hofu kwa Net ikaanza kupungua kwa kuwa walikuwa wamekaa naye hapo mezani siku nzima. Wakizungumza wao wawili, wateja na Tunda ilimlazimu kuuliza maswali ili akija kuachiwa pale, asiharibu.

Hakuna aliyekumbuka kula. Mpaka inafika jioni ya saa kumi na mbili, ndio pakatulia. Simu zikaacha kupigwa. “Mambo yatabadilika Tunda. Utakuja kupata muda wakupumzika. Mwanzo mgumu.” “Hamna shida kabisa. Nimefurahi kuweza kuwa busy hivi. Imenisaidia sana.” Net akacheka kidogo.

“Hujuti kukubali?” “Hata kidogo. Angalau akili yangu imetulia kwa muda nakuacha kujifikiria. Lakini najua wewe njaa itakuwa ikikuuma.” “Na wewe?” “Mimi sio mlaji sana. Umeona kile kichupa nilichokunywa mchana?” Net akakumbuka kumuona akinywa kitu. “Ni meal replacement. Inachukua nafasi ya mlo mmoja. Imebeba virutubisho vingi tu. Kwa hiyo wakati mwingine ni kinywa ile, nikapata na matunda, inakuwa inanitosha.” Net akatabasamu. Maana kwa kumwangalia tu, utajua huo mwili unatunzwa vizuri.

“Mbona na mimi hukunipa sasa?” Tunda akababaika kidogo. Akataka kujitetea, Net akimtizama. “Unisamehe tu. Sikujua kama ungependa. Nimebakiza vingine hotelini. Nilikuja navyo kutoka Dar. Naweza kwenda kukupa.” “Nashukuru. Ila sasa hivi njaa inaniuma sana. Nataka kula chakula chakueleweka. Twende tukale chakula kabisa.” Wakaanza kufunga kazi kwa siku ile, na kutoka pale.

Walirudi hotelini na kuagiza chakula. Kililetwa chumbani. Wakaanza kula. “Nikuulize Net?” “Uliza tu.” Net akajibu huku wakila. “Nimeona ofisi ndio mpya. Lakini mnao wateja wengi. Mnafanyaje?” Net akameza chakula kilichokuwepo mdomoni ili aweze kuzungumza.

“Chakwanza, kujitangaza. Nimejitahidi kutangaza na nimehakikisha watu wengi wametusikia na kufahamu huduma yetu. Nilitangaza kwenye maredio, televisheni, na kugawa vipeperushi kwa wingi. Mjini, mitaani na maofisini. Ukiangalia hapa nchini, wengi wanatumia kupanga. Kama sio nyumba anayoishi, basi ofisi. Sasa ili kuwapata hao watu, basi, nimeweka uwanja mkubwa kwa watumiaji wote. Wenye pesa na wasio na pesa nyingi wanaweza kutumia huduma zetu. Ndio maana utakuta kuna aina tofauti tofauti za magari. Hiyo inategemeana na uwezo wa mtu. Sijui nimejibu?” Net akauliza.

“Hapo nimeelewa.” “Lakini umeonaje? Si ni kazi inayowezekana?” “Nafikiri. Si bado tutakuwa wote ili kuhakikisha siharibu?” Net akacheka. “Tunda wewe ni muoga sana. Acha kufikiria kuharibu kwanza. Naomba ufikirie ni jinsi gani utaboresha. Ni vipi pale patanufaika kwa Tunda tu kuwepo pale. Tunda huyohuyo unayemfahamu wewe, mfikirie ni kwa jinsi gani pale pamebahatika kupata uwepo wako. Ukifikiria kwa namna hiyo, utaona mambo yatakavyokuwa rahisi.” Tunda akatoa tabasamu kama anayefikiria.

“Niamini Tunda, kila mtu anahaiba yake na kitu kinachomfanya awe yeye. Wewe unajijua. Sasa jifikirie hivyo ulivyo unawezaje kupanufaisha pale! Jiweke kwenye nafasi ya kama ile kampuni ndiyo imebahatika kumpata Tunda. Jiambie kwanza hivyo. Hivyo tu. Weka mbali maswala yakukaa darasani na elimu. Wewe tu kama ulivyo. Jiambie kampuni ya Cote, imebahatika kumpata Tunda. Sasa utainufaisha vipi! Utaona jinsi itakavyokusaidia kukubadilisha mtazamo wako. Kwanza hofu itaondoka, na utashangaa utapata ujasiri wa umiliki.” Tunda akacheka kidogo.

“Kesho tutaanza kwa kukupa nafasi upokee simu.” Tunda akastuka. “Net!” “Si umenisikia leo jinsi nilivyokuwa nikipokea simu?” Tunda akakubali. “Basi fanya hivyohivyo na usiogope kuuliza mteja maswali kuhakikisha unamuelewa. Ukiona anaomba huduma ngumu kwako, au humuelewi, mwambie ili kumuhudumia vizuri, unamuunganisha na mtu atakayeweza kumsaidia vizuri zaidi. Basi, niunganishe naye kwenye simu yangu. Ila kwa kesho, pia tutakuwa wote. Usiogope.” Tunda akacheka kwa hofu.

“Sawa. Nitajitahidi Net.” “Hayo ndio maneno. Na ninakuhakikishia utaweza tu. Sio ngumu kabisa. Kwanza ile kompyuta ipo pale kukusaidia kukupa kila jibu. Si umeona?” “Nilikuona jinsi unavyofanya.” “Sawa sawa.” Wakazungumza kidogo, Net akaondoka.

 

Siku ya Pili, Tunda kazini.

Tunda alitegesha alamu ili imuamshe mapema kidogo. Akaoga na kujitayarisha. Kwa kuwa alirudi na baadhi ya vitu vyake kutoka Dar, Tunda alijitengeneza kawaida, kiofisi kama vile alivyokuwa akiwatengeneza kina Fina mwilini mwake anapokwenda kulaghai wanaume. Alivaa vizuri. Kiofisi. Kama msomi mwenye majukumu mazito. Ila kiheshima kwa kuwa alikuwa na Net.

Akaagiza kifungua kinywa. Chake akala. Cha Net, akaomba wamfungie maalumu kwa ajili ya kula ofisini. Alimuona akinywa kahawa, na walikuwa na microwave ofisini. Akaomba waweke kila kitu tayari na kuwaambia atapitia hapo mgahawani.

Net alifika hapo. Hakupanda juu kwenye chumba cha Tunda. Akampigia simu kuwa ashuke. Kwa haraka bila kuchelewa, akapitia mgahawani akachukua kifungua kinywa cha Net, akatoka nje. Alitoka kwenye mlango wa hoteli, Net akiwa kwenye gari akimtizama. Hakika Tunda alikuwa amependeza. Kigauni chakuchanua chini kama mwamvuli, juu kilimshika na kilikuwa kata mikono. Kilimfika chini kidogo tu ya magoti. Kiatu cha kufunika, cha juu. Hereni ndefu bila cheni shingoni ila hakuacha kuvaa ile  ya mguuni na mkononi. Pochi inayoendana na kiatu alibeba mkono wa kushoto, mkono wa kulia chakula cha Net.

“Waw!” Akajisemea Net mwenyewe wakati akimwangalia akimsogelea. Mwishoe akaamua kwenda kumpokea. “Hii ni kwa ajili yako.” Tunda aliwahi wakati Net amemsogelea na yeye akawa ameshafika karibu ya gari. “Asante. Sasa mbona ya kwako sioni?” “Uliniambia leo ni zamu yangu kupokea simu. Sasa wakati mimi nazungumza na wateja, wewe unakula.” Net akacheka. “Naona mudi wa kazi ameanza kukuingia.” Wakacheka. Net alikuwa ameshapokea kile chakula. Akamfungulia mlango, Tunda akapanda. Na yeye akaingia garini nakuanza kunywa kahawa yake. Kimya mpaka kazini.

Walipoingia tu, simu zikaanza. Net akakimbilia na kupokea. Tunda akaanza kuwasha kompyuta akijua wazi Net atahitaji. “Naomba nikupe mtu ambaye atakusaidia.” Tunda akashtuka na kumgeukia Net. Net akamkabidhi simu. Tunda akavuta pumzi. “Halow!” Tunda akaipokea. Net akavuta kiti nakuanza kula pale pale kwenye meza bila hata kumtizama Tunda.

Mteja alikuwa akisafirisha mzigo kutoka Arusha mpaka Moshi. “Ni mzigo wa aina gani na unaukubwa gani?” Alimsikia Tunda akiuliza taratibu tu. Akamuona anaandika huku akisikiliza kwa makini tu. “Kwa aina hiyo ya mzigo, tunaweza kusafirisha. Lakini naomba nishauri.” Mpaka Net mwenyewe ikabidi atulie asikilize huo ushauri. “Asante.” Akamsikia Tunda akishukuru na cheko kidogo. Akahisi amesifiwa huko kwenye simu. Sauti ya Tunda ni kweli ilikuwa nzuri.

“Nimesikia aina ya gari unayotaka. Na ukisisitiza unakwepa garama. Lakini naona mzigo wako unathamani kubwa. Isingekuwa vizuri kwanza tukufikishie pale ukiwa haupo kwenye hali nzuri. Lengo letu kama kampuni sio kukusafirishia tu. Tungependa kuhakikisha tunafikisha mzigo wako ukiwa salama pia.” Net mwenyewe akashangaa. Tunda akaendelea kusikiliza, akamuona anacheka.

“Hapana. Nitakupa kwa bei nzuri tu. Naomba nipe kama dakika moja au mbili, nikutajie aina ya magari yatakayofaa kwa bidhaa yako.” Tunda akabonyeza spika, akaweka simu chini, akaanza kuperuzi kwenye kompyuta. Net kimya. “Lakini hujanitajia jina lako.” Wakamsikia yule mteja. Tunda akaanza kuogopa. “Mrembo? Maana nataka kila nikipiga, niwe nasikia hiyo sauti nzuri. Au siruhusiwi?” Tunda na Net wote walikuwa wakisikiliza.

Tunda akanyanyua simu. “Naitwa Tunda na nimepata aina mbili ya magari ambayo nafikiri yatafaa kwa mzigo wako.” Tunda hakutaka kuendeleza maongezi juu yake. Akamtajia hayo magari na bei yake. Akampa nafasi achague. Akachagua moja na kutaka namba ya simu ya Tunda. “Naomba utumie hii ya ofisi kwa kikazi.” Net akajua anatongozwa na ameombwa namba yake binfsi ya simu. Yule mteja akaendelea kuongea, Net akamuona Tunda anakosa raha, akamuomba yeye hiyo simu.

Tunda akamkabidhi Net simu. “Malipo ni kama alivyokwisha kukwambia. Tutajitahidi kufika sehemu ya kuchukua mzigo kwa wakati na wewe tunaomba uwataarifu kuwa dereva wa kampuni ya Cote, atafika hapo akiwa na kitambulisho chetu. Asante.” Net alizungumza hivyo tu, na kukata simu. Tunda akasimama na kutaka kuondoka.

“Njoo kwanza Tunda.” Tunda akarudi. “Nisikilize. Kwanza umefanya vizuri sana. Hata mimi sikutegemea.” Tunda akatabasamu na kufuta machozi. “Kweli kabisa. Na ninataka uelewe hivi, kazi kubwa hapa au utakayofanya ni kuhudumia wateja wa aina tofauti tofauti. Usiogope kwangu au kwao. Fanya kazi vizuri, wakifika kwenye mambo yao binafsi, wajibu vile unavyotaka wewe. Usiogope. Sijui kama unanielewa?” Tunda akavuta pumzi.

“Lazima ufikie hatua uweze kutofautisha kazi na mambo binafsi. Na ile kauli ya ‘sina uwezo wa kuchagua’, ufike mahali ijifute. Wewe ndio ubakiwe kiongozi wa maisha yako. Yaani wewe ndio unajukumu lakuongeza nafasi kwenye maisha yako. Uchague chakufanya ukiwa unafikiria ili kuepuka majuto ya baadaye. Sijui kama umenielewa?” “Nimeelewa.” “Haya. Tuendelee na kazi.” Tunda akacheka na kurudi kukaa.

Kufika mchana, hofu ikawa imemuisha kabisa Tunda. Anapokea simu kwa ujasiri wote. Net alishangaa vile Tunda anavyozungumza kingereza kizuri. Akahisi Tunda alimdanganya. Alimwambia hajasoma. Na ni mtanzania! “Kingereza amekijulia wapi?” Akajiuliza Net kwa kadiri alivyokuwa akimsikiliza akikizungumza na wateja kwa ufasaha bila hofu na ujasiri usoni.

Hakuna aliyekumbuka chakula cha mchana. Kukawa busy mpaka jioni tena kama jana yake, ila siku hiyo walikaa hapo mpaka usiku wa saa moja. “Naona utajuta.” “Kwa nini?” “Si hivi unavyotumia muda mwingi hapa ofisini!” “Kwanza ndio nafurahia. Kwa mara ya kwanza maishani naona nafanya kitu cha kueleweka na mtu anakifurahia. Nashukuru kwa hii nafasi Net.” Tunda aliongea kwa upole. “Karibu. Na ninaona umeshakuwa mtaalamu.” Tunda akacheka taratibu wakati wanatoka.

“Ni hivyo hivyo tu, tena naona na umejaliwa lugha ya ushawishi. Hiyo pia itakusaidia zaidi.” Tunda akatabasamu. Walikuwa kwenye gari. “Hata nikiwa mbali na pale. Ukipata mteja ambaye unataka nizungumze naye, kama nilivyokufundisha jinsi ya kuunganisha. Kwa simu ya mezani na ya mkononi. Rahisi tu. Niunganishe na yule unayetaka nizungumze naye.” “Sawa.” Tunda akaitika          `.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Tunda na Net wakaendelea kufanya kazi kwa bidii zote. Wakisaidiana bega kwa bega. Wateja wao wengi walikuwa wafanyabiashara wakubwa hapo nchini na watalii. Walisafirisha bidhaa kubwa na za thamani huku wakipokea watalii nje na ndani ya nchi. Walikuwa wakipokea watalii kutoka nchi mbali mbali. Net alijitangaza kwenye website iliyokuwa ikivutia watalii kutoka nchi mbali mbali.

Tunda alimshangaa uwezo wake wakuzungumza lugha. Alikuwa akiongea lugha tano tena kifasaha. Kama sio kingereza au Kiswahili, Tunda alimuhamishia simu Net popote alipo azungumze na aina hiyo ya wateja. Na Net aliacha kusafiri. Akawepo Arusha kwa muda huo aliokuwa na Tunda hapo. Kwa hiyo, hiyo miezi ya mwanzoni ikawa rahisi kwa Tunda.

Wafanyabiashara wengine waliomsikia Tunda kwenye simu walipatwa tamaa. Baada yakushindwa kupata namba zake za simu, walikuwa wakiamua kufika kabisa hapo ofisini, ilimradi tu kumuona nakujaribu kumtongoza. Tunda akashangaa sana. “Kipindi nilipokuwa na shida nao, wote walijificha, sasa hivi ndio wanajitokeza!” Tunda akajiuliza. Net alikuwa akimtizama kwa karibu na alijua nia ya wengi wao.

Kila walipofika pale, Tunda alipowasukumia kwa Net, bado walitaka kuzungumza naye Tunda zaidi. Ghafla yeye akawa wamuhimu kuliko mwenye kampuni! Tunda akajua ni janja yakumpata tu         . Akawa akiwakwepa kiustarabu lakini akimaanisha kabisa. Alishatendwa na kuwatumikia hao wanaume, hakuwa na hamu tena. Alikinahiwa na swala la mapenzi, Gabriel akawa amegongelea msumari wa mwisho.

Hakuwa akijua kama anaweza kufanya kazi kama wasomi wengine kwenye ofisi kama ile. Tena alifanya vizuri sana, mpaka mama yake Net aliyekuwa akizungumza naye kwenye simu alikuwa akimfurahia sana. Tunda alifanya kazi kwa bidii sana bila kuchoka wala kulalamika na Net alimwambia atamlipa. Akajiambia hana sababu yakuuza mwili wake tena. Kwa mara ya kwanza akawa amepata nafasi ya kuchagua nini afanye kwenye maisha yake. Kuuza mwili au kufanya kazi ili kujipatia kipato. Sasa kwa kuwa wanaume walishamtenda na kutumia huo mwili vibaya, kwenye swala la biashara ya ngono, akaona aweke kikomo. Hakuna aliyemkubalia.

Hakuwa na jumamosi wala jumapili, pale alipokuwa na mambo yake yakufanya ofisini, hakuangalia muda hata kidogo. Aliongeza juhudi kazini. Hakujiangalia yeye tena. Akataka kumfurahisha Net na kulipa fadhila. Tunda alijua pesa inayomtoka Net kwa kuwekwa pale hotelini. Sasa ili kulipa fadhila, ni kuweka juhudi. Net mwenyewe alikuwa mchapa kazi. Wakaendelea kuchapa kazi kwa pamoja

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Siku moja ilikuwa jumamosi. Walifanya kazi hiyo week, kuanzia asubuhi mpaka usiku. Jumatatu mpaka siku hiyo jumamosi usiku. Net akamwambia Tunda wanastahili kwenda kula chakula kizuri sehemu kama kujipongeza. Tunda akacheka akijua wazi amefurahia. Waliingiza pesa hiyo week. Kuanzia dola mpaka pesa ya madafu.

“Unahamu ya kula nini?” Akamuuliza Tunda. “Mimi ikishafika usiku kama hivi, nilishakwambia, siwezi kula kitu kigumu. Sitaweza kulala.” Tunda akajibu na kumalizia kufunga kompyuta aliyokuwa akitumia.

“Lazima tujipongeze.” Tunda akacheka. Siku za jumapili ilikuwa wakionana jioni. Tena kwa muda mfupi. Net alikuwa akimpitia hapo hotelini kama kumsalimia tu. Wakati mwingine alikaa kidogo, wakati mwingine aliondoka. Tunda hakujua anaishi wapi. Kama ameoa au la. Anaye mwanamke hapo Arusha au la. Katika watu aliowaogopa hapa duniani ni Net. Alimuogopa huyo kaka kupita kiasi. Mbali na mambo ya kazi, hakuwa na ujasiri wakumuuliza chochote.

“Nishushe mimi hotelini. Wewe nenda tu Net.” “Hapana bwana. Hii ni tunajipongeza wafanyakazi wa Cote. Wewe vipi Tunda?” Tunda akacheka. “Twende basi ukale hata matunda wakati mimi nakula nyama choma. Njaa inaniuma.” Wakakubaliana.

Walitafuta hoteli nzuri. Ni kweli Net hakupenda sana kwenda baa, labda awe anakutana na rafiki zake au mambo ya biashara, ndipo itamlazimu kwenda. Waliingia sehemu ya chakula. Tunda akaagiza maji na fruits salad. Akiwa hana hata habari kama atamwingiza Net matatizoni siku hiyo. Alikuwa amependeza japo alikuwa ameshinda kazini siku nzima tena siku ya jumamosi.

Aibu ya Mwaka kwa Tunda Mbele ya Net.

Net aliagiza chakula chake na juisi ya embe. Hiyo hoteli juu ilikuwa na vyumba na kumbi ya mkutano. Hali ya Tunda ikabadilika ghafla hata kabla chakula hakijaletwa, Net asielewe ni kwa nini. Meza ya pembeni, mbele kidogo, akaona wamekaa wanaume wakila na kunywa huku wakiongea na kucheka. Watatu wa hao waliokuwa wamekaa hapo kwenye hiyo meza, Tunda alishawahudumia. Tena wakiwa kwenye baa.

Wote waliokuwa wamekaa pale walikuwa marafiki, walikuja mjini Arusha kwenye mkutano. Na wote walikuwa wakifanya kazi ofisi moja. Kwenye NGO ya kigeni. Vijana wenye pesa na wasomi tu. Sasa watatu wao pale ndio hao Tunda alishawahudumia zaidi ya mara moja. Mmoja alimpata kwa kuiba namba ya simu kwenye simu ya mteja mwingine.

Wawili aliwatongoza baada ya kukutana nao baa. Akafanya ule mtindo wake wakumchomoa mmoja baada ya mwingine. Siku ya kwanza akampata mmoja wao wakiwa wamekaa wote mezani wakinywa. Akatoka naye nje, akamalizana naye kwenye gari. Akamuomba namba yake Tunda. Wakaja kukutana tena kwenye nyumba za kulala wageni. Akampa kwa mapana na urefu. Wakati akiwa anaoga aondoke pale hotelini, kabla Tunda hajamfuata huko bafuni, akaiba ya watatu. Kwa kuwa aligundua hao wawili walikuwa karibu akajua lazima atakuwa na namba yake ya simu. Na kweli akafanikiwa.

Siku inayofuata, akampigia simu huyo wa tatu, akijidai anamuulizia yule wa kwanza kabisa ambaye alienda naye baa ndipo akakutana nao wote. Akamzungusha kwa maneno mazuri kwenye simu, mpaka akajikuta na  yeye anaomba penzi. Tunda akajidai kumkatalia kwa kumwambia wenzake watajua kwani alishaonekana na wote akiwa na yule rafiki yao. Akambembeleza akimwambia yeye ni mtu mzima, sio mropokaji. Basi, akachukua chumba mahali, Tunda akaenda kumpa kwa mapana na marefu. Na yeye huyu wa tatu akajua kuwa anamuibia rafiki yake. Ikawa siri yao wawili, ila nafuu zaidi kwa Tunda anayewazunguka wote. Marafiki hao watatu wasijue wanapewa uroda na mwanamke mmoja.    

Siku ingine aligonganisha magari wakiwa baa. Alijikuta na wote watatu meza moja, akiwa ameenda na yule yule wa kwanza, yule wa pili aliyemsaidia kumpata wa tatu akapewa penzi kwenye gari mpaka akatafuta chumba, akamtumia ujumbe wakiwa pale pale mezani kuwa watoke nje. Tunda alipopata ujumbe akiwa anacheza game yake pale kwenye meza ya wale marafiki walevi, akarudisha ujumbe akamwambia anatoka, ila asubiri baada ya dakika mbili kamili ndipo amfuate.

Basi wakafanya hivyo. Alipotoka tu, yule watatu naye akatuma ujumbe kuwa anamuhitaji. Akiwa anamsubiria yule wa pili, ndani ya zile dakika mbili akachat na watatu. ‘Ushawahi kuonja vya garini?’ Akamtumia ule ujumbe. Watatu akajibu kwa haraka. ‘Hapana mama. Ila nipo tayari kujifunza.’ ‘Basi nisubiri. Nikija kuomba funguo za gari hapo mezani. Unifuate baada ya dakika tatu tu.’ ‘Asante mama.’ Usiku huo akawapa dozi marafiki wote watatu bila wao kujijua.

Kwani alipomalizana na wa pili, akamwambia arudi ndani haraka na asiseme kitu. Baada ya muda, akarudi na kumwambia yule wa kwanza tumbo limejaa gesi. Anaomba funguo za gari yake aende akatafute dawa za gesi kwenye duka la madawa. Katikati ya pombe na vile anavyohudumiwa na Tunda, akatoa funguo za gari. Tunda akatoka, yule rafiki wa tatu akafuata nyuma. Alichofanya Tunda nikuhamisha upande lililokuwepo hilo gari. Akaenda kulificha mbali kidogo, hapo hapo baa. Dakika tano zikawa nyingi. Akamalizana na rafiki watatu. Akamshukuru sana na kufurahia ule wepesi. Akampa mahela, akamwambia arudi ndani kwa haraka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Sasa wote watatu wakawa wanajua uwezo wa Tunda wa mapenzi, na wale wawili walishapewa penzi la garini tena kwa muda mfupi sana na wote wakijua wanamwibia mwenzao. Na hawakuwahi kukamatwa hata mara moja. Yule mwizi wa halali, wa kwanza akawa amemuona Tunda pale kwenye meza. Akaamua kwenda kumsalimia Tunda pale pale mezani alipokuwa amekaa na Net.

“Habari Lina?” Akanyoosha mkono kwa Tunda. Net akamgeukia yule kijana na kumtizama Tunda. Tunda akakwepa ule mkono kwa kunyanyua glasi ya maji. “Nzuri tu.” Akajibu Tunda na kunywa maji. “Nikuombe msamaha. Majuzi ulipokuwa ukinitafuta, nilikuwa nimebanwa kweli ndio maana nikashindwa kabisa kupokea simu yako.” Yule kijana alijieleza kwa Tunda. “Hamna neno. Nilielewa.” Akajibu Tunda taratibu, Net akisikiliza.

“Vipi, umehamia Arusha nini?” Akamuuliza Tunda. “Nipo kikazi. Huyu ni bosi wangu.” “Oooh! Nimefurahi kukufahamu Kiongozi.” Akampa mkono Net, yeye Net akaupokea mkono na kujibu salamu. “Nipo hapa Arusha na wenzangu. Tumekuja kikazi. Nipo gorofa hii ya pili tu. Hapa hapa hotelini. Nakukaribisha.” Akamgeukia Tunda. “Asante, lakini hapana. Nipo busy na kazi.” Tunda alimjibu kwa msisitizo tena akimtizama machoni.

 “Kesho ni jumapili Lina. Najua hufanyi kazi. Na mimi kuanzia asubuhi nitakuwepo tu hapa hotelini. Kwa nini usije? Sitakuweka sana.” Tunda alitamani kama aondoke lakini ikamlazimu kujibu tu. “Nina mipango mingine. Tafadhali naomba uondoke ili nile. Unanisimamia hapa, tunashindwa kula. Nimeshakwambia hapana, inatosha.” Chakula kilikuwa kimeshaletwa.

“Au umekasirika sababu sikupokea simu yako?” Akaendelea kusisitiza. Mpaka Net akaweka kisu na uma chini. “Hapana sijakasirika ila sitaki kuonana na wewe tena. Naomba utupishe.” “Daah! Sawa Lina. Lakini…” Tunda akavuta kiti kwa nguvu na kusimama. Akamtizama machoni. “Samahani Lina, sikutaka kuwakwanza.” Tunda akaondoka kuelekea chooni, yule kijana naye akaondoka. Harufu ya pombe ndiyo ilikuwa ikitoka mdomoni kwake na kuenea pale kwenye meza ya Net na Tunda.

Wakati anarudi, ndio anatoka choo cha kike anaingia pale mgahawani alipomuacha Net, akakumbana na wale wengine wawili. “Samahani Lina, tunaweza kuzungumza kidogo hapo nje?” Mmoja wao akaanza na yule mwingine akabaki ameduaa. Kumbe wote waliaga pale mezani kwa rafiki zao kuwa wanakwenda msalani, kumbe walikuwa wakimfuata Tunda. Mmoja akawa amewahi.

Kabla Tunda hajajibu, mwenzie akadakia. “Mimi ndio nataka kuzungumza naye mara moja hapo nje. Hatutachukua muda mrefu, si ndio Lina?” Watatu akadakia, akijua Lina mwenyewe anaelewa. Huwa wanamalizana kwa muda mfupi sana, asijue na rafiki yake naye anachomtakia huyo Lina sio mazungumzo. Ni huduma kama anayoitaka yeye.

Wakiwa wote wamelewa, wakaanza kubishana. “Mimi sitachukua naye muda mrefu. Dakika tano tu.” “Aliyekwambia mimi ninamchukua kwa muda mrefu ni nani? Natoka naye mara moja tu, tunarudi.” Wakajibishana wale marafiki wawili, mmoja akiwa amemshika mkono Tunda. Tunda alitamani kukimbia lakini akajikuta wote wamemshika mkono. Mmoja huku mwingine kule. Ndipo ulipozuka ugomvi, wote wakimng’angania huyo Lina, hakuna anayetaka asubiri kwanza.

“Nakwambia mimi ni mara moja tu! Mbona unafanya mambo ya kitoto, Zimbe?” “Wewe ndio nakuona huelewi. Nimekwambia hata mimi sitamkawisha. Anarudi sasa hivi.” Watu wote mle ndani macho ya kawa kwao wote watatu. Tunda anatetemeka, anataka kubebwa juu juu ili watoke naye pale ndani. Uzuri wakaanza kurushiana wao ngumi, na kumuachia Tunda. Hakujua Net alipotokea, akamsogelea pale akiwa ameshika funguo za gari na pochi yake. Akamshika mkono kwa nguvu, akamvuta kumtoa pale.

Waliingia kwenye gari, Net akaondoa gari kwa haraka Tunda akitetemeka kama aliyetoka kwenye friza. Hata asante alishindwa kusema kwa aibu. Alipofika hotelini, alichukua pochi yake na kushuka kwa haraka kama anayekimbia. Net akaona amuache tu usiku huo. Hata yeye hakumfuta nyuma. Akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kuanzia siku hiyo Tunda alijiapia kutotembelea tena sehemu za starehe au kwenye mabaa. Na kwa kuwa Net alikuwa mstaarabu, hakuwahi kumuuliza tena juu ya ule mkasa. Ila alimuona ile hofu ya mwanzoni kabisa imerudi vile vile. Tunda aliacha hata kumuangalia machoni. Mara nyingi ilipomlazimu kumuongelesha alimuongelesha akiwa anaangalia pembeni. Kama yupo ofisini basi macho kwenye kompyuta au mafaili. Labda Net afanye juhudi za makusudi kumwita jina lake. Hapo atageuka na kukwepesha macho kwa haraka. Alikosa ujasiri kabisa, akapooza hata tabasamu likamwisha.

Wakajikuta muda mwingi wanakuwa pamoja ofisini, wakitoka hapo, anamrudisha hotelini. Week ya tatu Net alipata kijana wa usafi. Akamwambia Tunda atakuwa akifika hapo kusafisha na kutoka mchana. Na huyo ndio mara nyingi Net alianza kumtuma kwenda kuwanunulia chakula na kuwaletea hapo ofisini au wanapitia sehemu. Net anaingia ndani. Ananunua chakula, wanaenda kula hotelini huku Net akiangalia taarifa ya habari. Aliondoka muda alioona Tunda anataka kulala. Hakuna maongezi. Kimya kimya.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Karibu ya mwezi kuisha tangia aanze kazi, Net alimwambia inamlazimu kwenda Dar kwenye ofisi nyingine ambapo yupo mama yake. “Kuna mambo kadhaa yakuweka sawa. Ungependa tuongozane?” Akamuuliza Tunda. “Hapana. Wewe nenda tu. Niache mimi hapa. Nikikwama nitakujulisha.” “Hutaki kuona ofisi ya Dar?” “Halafu hapa tufunge!?” Tunda akauliza kwa mshangao kidogo.

“Hapana. Si unajua hiyo kazi unaweza kufanya popote tu?” Akamuuliza na kumuelekeza kuwa nikupokea simu ambazo wanaweza kuzihamishia hata kwenye simu ya Net au yake. Na kompyuta wanaweza kutumia laptop tu ambayo wanaweza kwenda nayo popote. Tunda akaelewa ila akanyamaza. “Hatutakaa muda mrefu.” “Kama sio lazima, naomba uniache hapa Net. Tafadhali.” Tunda akaongea kwa upole.

“Sio lazima Tunda. Ila sikutaka ubakie hapa peke yako kazi zikakulemea.” “Nitakuwa sawa. Nikishindwa jambo, nitakutafuta unisaidie. Ila nakuahidi kila kitu kitakuwa sawa.” Akasisitiza, Net akamwangalia. “Samahani lakini. Naomba usifikiri nakukaidi au nakataa kazi. Ndio maana nimeuliza kama kunakitu chakikazi natakiwa kufanya mimi huko. Uliponiambia hapana, ndio maana nimeomba nibaki tu.” Tunda aliongea kwa utaratibu na kujihami.

“Sasa hivi natamani maisha haya niliyonayo Net. Napenda hivi ninavyoweza kukufanyia kazi. Au kujiona nafanya kitu chamaana. Acha akili zangu zitulie kazini kwa muda. Nimepoteza muda mwingi sana kwenye lile jiji. Mbaya zaidi nimepoteza ‘kwangu’! Inaniuma sana kujiona nimegeuka kuwa mgeni kwenye nchi yangu mimi mwenyewe! Nyumbani kwangu ndio ilikuwa kimbilio langu. Nikishahangaika huko, nilikuwa nikijifariji ninalo kimbilio. Sasa hivi sina. Hii kazi ndio imegeuka kuwa kimbilio. Nikiamka asubuhi, najiambia ninakitu chakufanya. Inanipunguzia mawazo. Kuja kurudi Dar kama mgeni, nikijua sio kwangu tena, itaniumiza zaidi. Ndio maana nakuomba kama sio lazima, kwa sasa naomba nibaki tu hapa.”

“Nimeelewa. Hamna shida. Tutawasiliana basi. Ukikwama usisite kunipigia. Na bado zile simu unazotaka mimi nijibu, endelea kuwahamishia kwangu.” “Asante Net. Ungependa nikusindikize uwanja wa ndege?” Tunda akauliza kwa upole akionyesha kujali. “Ningeshukuru. Tena itakuwa vizuri nikuachie gari. Nitaondoka na ndege ya mchana. Utanipeleka na wakati wakurudi ningeomba uje kunipokea.” “Sawa. Lakini naomba usinielewe vibaya.” Bembeleza hiyo ya Tunda. Net mwenyewe alikuwa akilainika.

“Nimeelewa kabisa. Usiwe na wasiwasi.” Wakatulia kidogo. “Basi nitakuona kesho. Nitakuja kukuchukua asubuhi twende kazini, mchana ndio utanisindikiza.” “Sawa. Usiku mwema.” “Na wewe.” Net akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Net na Tunda walifika uwanja wa ndege, wakabaki kwenye gari upande wa kuegeshea magari. Hawakushuka. Kila mtu kimya kwa muda. Net macho kwenye simu yake, Tunda ametulia tu pale kwenye kiti kama hayupo garini. Hana simu mkononi. Ametulia kimya.

Baada ya muda akaita. “Net!” Akaita kwa upole. Net akamgeukia. “Unarudi lini?” “Nitajitahidi nisikae sana. Kuna kitu ulitaka kuniagiza? Hata kwenye vitu vyako. Nitakwenda kule Salasala kumuona Max.” “Max ni nani?” Ikabidi kwa mara ya kwanza Tunda kuuliza kitu mbali na kazi.

“Kumbe siku ile sikukuonyesha?” Tunda akatingisha kichwa kukataa. “Ni mbwa. Nilimnunua na akapatiwa mafunzo ya kiulinzi. Mzuri sana. Ananisaidia sana pale kwa ajili ya ulinzi. Yeye tu na Emma wanatosha.” Tunda akatabasamu. Net akacheka. “Ni mzuri sana. Nampenda.” “Mimi muoga wa mbwa.” “Max utampenda. Tutakuja kwenda wote siku moja, nikutambulishe. Kwa sasa ananijua mimi, Emma na daktari wake. Ni mkali au hatari kama akijua sio mtu salama.” Tunda akacheka na kutulia.

Wakatulia hapo kwa muda. Net alianza kuona uzito wa ile safari. Walishakuwa kwa karibu sana na Tunda karibia mwezi sasa. Kula na kuwa pamoja kila siku, tena kwa ukaribu! Tunda anautulivu fulani hivi, huchoki kuwa naye. Akaona uzito kumuacha. Akamwangalia, akamuona amegeukia dirishani kama anayewaza. Na yeye akatulia tu akimwangalia na kupotelea mawazoni.

Tunda akageuka, akamuona amejiegemeza kwenye kiti chake akimwangalia. “Huna haja yakunisindikiza mpaka kule.” Ikabidi amuwahi. “Sawa.” Tunda akakubali. “Kama hutataka lakini.” Akajihami Tunda asijefikiri anamkwepa. “Hamna neno.” Akajibu taratibu. “Au ungependa kufika mpaka kule ninapoingia kupanda ndege?” Akababaika tena kwani aliongea bila kufikiria baada ya Tunda kugeuka na kugundua anamwangalia. Akapaniki. “Ni sawa tu. Wakati wakuja kukupokea pia nikusubirie hapa hapa?” Tunda akauliza taratibu bila kuonyesha tatizo lolote. “Utakavyopenda. Ila tutawasiliana.” “Sawa. Uwe na safari njema.” “Asante na wewe ubaki salama. Unipigie ukikwama.” “Naamini kila kitu kitaenda sawa.” Tunda akajibu.

Inamaana hatutawasiliana mpaka nirudi?” Akajiuliza Net. Akaona amejifunga kwa maneno yake mwenyewe. “Unarudi hotelini au kazini?” “Sasa hivi nimapema sana. Acha nirudi ofisini tu. Nifanye fanye kazi upaka usiku, ndio nirudi kulala.” “Basi nikifika tu nitakujulisha.” Akachomekea Net na kujishtukia. “Na kujua umefikia wapi huko kazini.” “Sawa.” Tunda akajibu. Net akaona asije kuongea mengi na kuharibu zaidi, akashuka garini japo muda haukuwa umefika. Tunda akarudi kazini akitumia hiyo gari ya Net.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Net alitua jijini Dar, akili zikiwa Arusha. Mama Cote alikuwepo uwanja wa ndege kumpokea mwanae. Hawakuwa wameonana karibia mwezi. Kila weekend alipokuwa akimpigia simu nakumtaka arudi nyumbani, Net alisema yupo busy labda weekend ijayo. Siku zikazidi kwenda akahisi lipo jambo tu huko Arusha. Net sio mtu wa kung’angania Arusha na kushindwa kumuona mama yake zaidi ya majuma matatu tena akiwa hapo hapo nchini! Akajua lipo jambo kwa kijana wake. Na kwa kuwa alishazungumza na Tunda kwenye simu, akamsikia sauti yake, vile anavyoongea, akajua huyo Tunda pengine ndiye anayembakisha huko Arusha.

“Vipi Tunda?” Mama yake akauliza kiuchokozi tu na Net akajua. “Naona anaendelea vizuri. Kazi nyingi ameshazijua. Wateja wengi amewamudu.” “Lazima. Ana lugha nzuri. Namaanisha sauti.” Net akacheka. “Umeanza mama Cote.” “Jamani!”  Wote wakacheka. “Sasa kwa nini hukuja naye?” “Si yupo kazini mama jamani!” “Sawa, namaanisha weekend zile nyingine? Mkaribishe nyumbani. Hizo kazi mnaweza kufanyia hata huku Dar kama ulivyokuwa ukifanya.” Net akatingisha kichwa. “Sawa mama.” Wakacheka.

Net alikaa Dar siku mbili tu, tayari akawa anataka kurudi Arusha. Ghafla chakula cha Dar kikaanza kuwa hakiliki vizuri, masaa hayaendi. Ofisi ya Arusha ikawa inamuhitaji sana, basi ikawa vurugu. Akamuaga mama yake. “Nilijua week hii utamalizia huku urudi jumatatu! Maana leo ni ijumaa. Jumapili twende wote kanisani. Hata mchungaji amekuwa akikuulizia.” “Nitarudi weekend ijayo.” Mama yake akajichekea moyoni.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Jioni hiyo akampigia Tunda simu. “Nimepata tiketi ya asubuhi.” “Basi nitakuja kukupokea.” “Sawa. Ila kama utakuwa na mambo mengine naweza kuchukua taksii.” “Hamna neno. Nitatokea ofisini. Nitakuja kukupokea, halafu unirudishe ofisini kama umechoka unaweza kuniacha tu wewe ukapumzike.” “Sawa. Lakini nafikiri na mimi nitarudi ofisini.” “Sawa.” Tunda akajibu taratibu kama kawaida yake.

“Kuna kitu chochote unataka nikujie nacho kutoka huku?” Net akauliza. Tunda akafikiria kidogo. “Sidhani Net. Nipo tu sawa. Asante sana.” “Basi nitakuona kesho asubuhi.” “Uwe na safari njema.” Ikabidi kuagana tu. Hapakuwa na nyongeza.

Jumamosi Siku Isiyo ya Kazi, Net Arudi Arusha.

Kesho yake Net alitua uwanja wa ndege wa Arusha, Tunda akiwa anamsubiria hapo nje, wala si kule kwenye gari. Net akafurahi sana kumuona pale. “Pole na safari.” “Asante. Na asante kwa kuja kunipokea.” Tunda akatabasamu. “Nimefurahi umerudi.” Tunda akaongea kwa upendo kama aliyekuwa ameachwa hapo kwa muda mrefu. Net kijana wa kizungu akacheka. Na macho yake yale ya rangi ya bahari, Tunda akakwepesha huku akinyoosha mkono ampokee.

“Sio mzito!” Net akajihami kama asiyetaka kupokelewa, anaweza kubeba kila kitu yeye mwenyewe. “Lakini angalau nikupokee. Usibebe kila kitu peke yako.” Akampa mkoba wa laptop. “Nimekuletea movie za stori kama unazopenda.” Tunda akacheka. “Asante. Nitaangalia kesho jioni. Asubuhi nataka niende kazini kidogo.” Net akanyamaza. Ni siku ya jumapili. Yeye alikuwa lazima kwenda kanisani. Wakarudi ofisini mpaka jioni.

Jumamosi huwa kijana wa usafi hafiki hapo ofisini. Walikuwa wao tu wawili. Net alifikia kwenye meza ya Tunda. Tunda akashangaa haingii ofisini kwake. Yupo tu hapo mezani kwake akifanya kazi zake hapo hapo. Japokuwa alikuwa akimuogopa, lakini alifurahia uwepo wake hapo. Hawakuwa wameonana kwa ‘Siku mbili! Nzima’. Wakashinda wote hapo wakifanya kazi pamoja. Hapakuwa na maongezi mengi. Tunda anamuogopa Net. Zaidi ya kumjibu endapo atauliza, basi hatazungumza chochote. Net naye kimya akifanya kazi zake kwenye laptop yake, Tunda asijue ni nini kinachomfanya kijana huyo kuwa busy kwenye hiyo laptop kila wakati. Kazi zikaendelea kwa utulivu siku hiyo ya jumamosi.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakaendelea kufuatana. Kazini, hotelini kwa Tunda mpaka wakiagana kwenda kulala. Mwishowe Net akaonelea kutafuta vitu ambavyo angefanya pamoja na Tunda kila wawapo pamoja, baada ya kazi angalau wazoeane au kupata kitu chakuzungumza mbali ya kazi. Akaanzisha siku na muda wao wakuangalia movie pamoja.

Wakitoka kazini, badala ya kukimbilia rimoti na kuanza kuangalia taarifa ya habari peke yake, alimtaka Tunda wakae wote hapo waangalie movie pamoja, au wacheze karata. Basi watacheza hapo kisha anaondoka na kumuacha Tunda. Lakini hakuwahi kumuuliza Tunda swali hata mara moja juu ya mara zote alizowahi kumkuta na wanaume au hata kisa kile alichotaka kubembwa juu juu. Tunda alishindwa kumuelewa kabisa Net. Walicheza na kuzungumzia kile kilichopo mbele yao tu kana kwamba hakuwa akimfahamu.

Kitu alichokigundua kwa Tunda kila walipokuwa wakiangalia tv hapo kwenye kochi, chumbani kwa Tunda, Tunda alijivuta pembeni yake, alikunja miguu yake vizuri na kuweka mikono yake juu ya kochi kama mto na kulala usingizi mzito sana. Net alijaribu kubadili aina ya movie. Alileta za visa vya kusisimu, wakati mwingine historia za kusisimua lakini mara zote Tunda aliishia kulala kabla hata hazijafika hata nusu! Na ulalaji wake ulikuwa wa usingizi mzito sana, na mara nyingi Net aliishia kumfunika pale pale kwenye kochi na Tunda aliishia kulala hapo mpaka asubuhi, kwani alishamuomba wakati akiwa anaondoka asiwe  anamuamsha ili ahamie kitandani, alitaka aondoke kimya kimya amwache tu vile vile alivyolala.

Yeye Net alikuwa akifurahia sana kuwa na Tunda, lakini wawe wanazungumza. Macho na sauti ya Tunda ni kweli vilimsumbua Net. Alikuwa akipenda awe anamtizama sio vile anavyokwepesha macho au basi angalau azungumze ili tu asikie ile sauti yake akizungumza naye yeye. Na iwe kwa muda mrefu. Kila alivyojitahidi Net, Tunda hakuwahi kubadilika. Wakati mwingine anaweza akanyamaza hapo chumbani kana kwamba hayupo. Atatulia kimya, akijitahidi ni kutoa tabasamu.

Net alijua kwa hakika anamuogopa sana. Swala la afanye nini kuondoa ile hofu ndio ukawa mtihani mkubwa. Tunda kimya. Kila alipoanza maongezi alianza kwa kumwita jina lake, kumfanya angalau Tunda  amtizame ayaone hayo macho.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Uliniambia unapenda sana kuangalia movie za stori, Tunda. Kwa nini kila nikiweka movie unalala? Nataka tuwe tunaongea bwana! Tunakuwa ofisini busy week nzima, angalau jumamosi jioni au jumapili tuseme ndio tunapata muda wakupumzika na wewe unalala! Au hufurahii hizi movies ninazochagua mimi?” “Ni nzuri sana tu. Mbona mwenzako huwa naangalia tena kwa kuzirudia rudia? Kila nikitoka kazini, ukiondoka au nikishtuka usiku nakujikuta nimebaki peke yangu, naziangalia.” Net hakuelewa.

“Sasa kwa nini hutaki kuangalia na mimi?!” “Hata nikikwambia hutaelewa Net.” “Bila kunijaribu!?” Tunda akanyamaza. “Au nakukera nikiwepo hapa?” “Nisingelala Net.” Net akakunja uso kidogo kama ambaye hajaelewa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Net naye atafika wapi kwa Tunda anayemfahamu kwa mabaya matupu? Kwanza alisikia sifa zake kwa binamu zake kina Samantha. Akazithibitisha yeye mwenyewe kwa kumfumania. Net mwenyewe ni nani? Ana nia gani? Usikose muendelezo.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment