Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Love At First Sight - Sehemu ya 64. - Naomi Simulizi

Love At First Sight - Sehemu ya 64.

“Ningefurahi Pius.” “Najua unahitaji mapumziko. Na Poliny nimemwambia umechoka, unahitaji kupumzika. Unatutumikia pale ndani bila kuchoka na ni kila siku! Nikamwambia ni lazima  atenge muda asaidie kukupa Off nyumbani. Ndio amekubali tuongozane. Kwamba atachukua vitabu vyake, twende na mwanao unayemdekeza. Anasema wakati anacheza game zake, yeye anasoma. Akianza fujo atatupigia chumbani kwetu, uje umtulize.” Raza alicheka sana.

“Hivi nyinyi mjue Polla ni mrahisi sana kuishi naye! Tatizo lenu wewe na Poliny hamjamjulia.” “Sasa yeye huwa anasoma saa ngapi? Mtoto asiyetaka kusoma hata kitabu cha hadithi jamani! Ukimwambia, ugomvi!” “Tatizo lenu nyinyi mnamuingilia katikati ya mambo yake. Polla hataki kuingiliwa. Wewe panga muda unaotaka asome, kisha ukimkuta katikati ya game yake, mwambia ile game kwa wakati huo ikifika mwisho, au hata kama haijafika mwisho, wenzie wakimtoa, ameshindwa hiyo game, afanye jambo unalomtaka afanye. Na unamwambia ukirudi kabla hajakufuata, unamzimia game nzima hata kama ndio ameanza au yupo katikati ya hiyo game nyingine. Sasa kwa kuwa hataki kuingiliwa katikati ya game zake, akifika tu mwisho tu kwenye game uliyomkuta nayo, anakufuata yeye mwenyewe mmalizane, ili aendelee na game zake.”

“Atafanya kila kitu tena kwa haraka na makini ili usimuweke. Na huwa ananijua, hawezi nidanganya maana namuuliza maswali kuhakikisha ameelewa. Basi atazingatia kwa makini ili kufupisha ule muda wako, awahi yake.”

“Tatizo lako wewe na mwanao Poliny, mnamuingilia. Halafu mnampa mambo asiyopenda. Wewe unajua kabisa hapendi kusoma vitabu vyenu hivyo ya historia za ulimwengu, halafu eti unaanza kumwambia aache game asome historia ya vita ya kwanza ya dunia! Polla!” Pius alicheka sana.

“Inamuhusu nini yeye vita ya kwanza ya dunia au uchumi wa ulimwengu?” “Ajue ulimwengu unavyoelekea!” “Hayo mambo ya mwanao Poliny. Sasa yeye akipewa vitabu na babu yake. Vikamsisimua yeye, anakuja mlazimisha mwanangu, kwa muda wake yeye, eti asome, kitabu ni kizuri. Polla akishakitizama na kile kichwa chake cha habari nzima ya hicho kitabu, anamuuliza kwa nini yeye asome!” Pius hana mbavu.

“Naye Poliny anaanza kumuelezea umuhimu wa kile kitabu, Polla hana muda wa kumsikiliza. Anataka amuache acheze game zake. Poliny anataka lazima asikilizwe, ndio ugomvi unapoanza, na kumsimanga mwanangu hapendi kusoma. Polla naye hataki kumsikiliza anamfukuza chumbani kwake. Ndipo ugomvi unapoanza.”

“Namuuliza Poliny, dada mkubwa vile kupigana na mtoto mdogo, haoni aibu? Anasema namtetea Polla kila wakati wakati yeye anamsaidia. Polla naye anasema yeye hataki msaada wake. Basi eti mwanangu yeye mkorofi!” Pius akazidi kucheka maana ndio kama anapata picha kamili ya ugomvi wa wanae. Maana yeye humuamini sana Poliny bila kumsikiliza Polla.

“Ila Polla ni kweli mkorofi bwana! Akitaka jambo lake anataka libakie hivyohivyo!” “Sasa wewe jiulize watoto hao wawili wenye aina hiyo ya tabia, wameipata wapi? Kushikilia jambo, hawataki mabadiliko?” “Raza!” “Taratibu tu. Fikiria wanao na jinsi wewe ulivyo Pius.” “Lakini bora Poliny bwana!” “Kwa kuwa misimamo yake inaendana na matakwa yako. Ndio maana unamuona yeye kama malaika.”

“Halafu Pius, Polla huwa hafeli. Hapati 100, ila mara nyingi anapata A, akifeli sana mwanangu ni B. Maana anajua akishuka tu hapo, basi namnyima game.” “Kweli?!” “Muulize mwenyewe. Akileta ripoti mbaya, anapumzika game kwa muda mrefu tu, ndipo utakapomuona amejaa jikoni na kukufuata wewe mpaka chumbani akitaka hili na lile, na maswali kwako hayaishi. Basi jua hapo nimempumzisha game zake. Mpaka arudie ule mtihani, aufaulu tena, ndio anarudia game.” “Basi mfundishe kusoma vitabu bwana!” “Sasa hapo unamtaka Mungu maneno.” Pius alicheka sana.

“Sasa kwa hiyo tunakwenda nao wote?” “Poliny anakwenda ili kunisaidia Polla. Kulala kwa wakati na kuoga usiku tukiwa chumbani kwetu. Ila muda wa kula tutakuwa nao. Hivi nimemwambia awahi kurudi nyumbani amsaidie kufungasha vitu vyake ili tukirudi tu na sisi ni kujiandaa, tunakuja kuchukuliwa saa moja usiku, tunaondoka.”

“Sasa ili kila mtu apumzike huko, mwambie Poliny asianze kumfungashia vitabu tu. Atajaa kwenye kila chumba na ratiba za watu atamiliki yeye, maana hatakuwa na chakufanya ila kutaka kila mtu amfuatishe anachokitaka yeye.” “Hata kitabu kimoja jamani!?” “Kama mnataka kweli tukapumzike huko, mwambie amfungashie game zake na nguo za kuogelea kama tunakokwenda kutakuwa na pool. Kitabu hatasoma, na ndipo watakapoanza kupigana, tuitwe chumbani kwao.” Pius akatingisha kichwa kwa masikitiko.

“Na umsisitize Poliny anayependa kumkazania mtoto.” “Basi nitampigia nimpe hayo maagizo.”  “Nashukuru Pius. Nimefurahi SANA.” Furaha aliyokuwa nayo Raza, hakuna jinsi angeweza eleza mtu akaelewa. Kuna ambayo anajibiwa hata hakuwa akijua jinsi ya kuomba.

“Tunakwenda wapi?” “Surprise.” Akazidi kucheka kwa furaha. “Sasa nibebe nini?” “Mama wewe, surprise. Mbona hivyo! Unataka kunidodosa mpaka niseme! Lakini jua hati zenu za kusafiria zimehusika.” Akatoa tabasamu akijua wanatoka nje ya nchi, ila ndani ya Africa kwa kuwa hawajahusika kwenda kuomba Visa popote ila hati zao kwenda kugongwa tu. Na kwa kuwa ni Pius, akajua ni sehemu ya maana.

“Na ungekuwa unaweza kuomba ruhusa kazini kwako jumatatu usiende, tungeondoka leo, tukarudi jumatatu. Poliny yeye amesema hana vipindi siku ya jumatatu.” “Na wewe kazini?” “Kwangu hili jambo ni la muhimu Raza. Naweza nikachukua Off hiyo siku ya jumatatu.” “Kweli Pius?!” “Kabisa. Sikumbuki kuwa na muda na wewe mtulivu wa namna hii ninaotaka upate. Nahisi hata mwanzo wetu haukuwa mzuri.” Raza akatulia akikumbuka fungate yao.

~~~~~~~~~~~~~~

Ni kweli haikuwa hata romantic. Kwa Pius ilikuwa ni bora liende. Ikawa kama anatimiza wajibu tu. Na hawakwenda mbali. Hapohapo jijini. Kitu alichokuwa akifanya huyo Pius huko fungate ilikuwa ni kusoma vitabu na kusikiliza taarifa za habari za kila pande ya ulimwengu mpaka mwisho wa fungate.

Hata walipokuwa wapo mezani wakila wanandoa hao wapya huko fungate, basi atakuwa na kitabu chake. Anakula huku akisoma bila hata ya kuzungumza na mkewe.

Basi Raza akajikuta mpweke mbele ya mume huyo wa ndoa mpya. Atakula na kuamua kurudi chumbani. Ataangalia movie mpaka achoke na kupitiwa na usingizi hapo kitandani. Baadaye ndipo Pius atafika kitandani. Kama hataomba penzi, basi ujue asubuhi ni lazima. Atamuamsha huyo Raza kwa kumpapasa. Raza ataamka. Atajituma hapo kitandani. Akimaliza Pius, anarudi kulala. Raza anaendelea na yake, kwenye hoteli hiyo nzuri ya kifahari mpaka fungate ilipoisha.

Miaka ikaenda. Pius anakuja kukubaliana na uhalisia kuwa Irena hatarudi tena kwenye maisha yake, ameshazaa kabisa na ana watoto zaidi ya wawili, maisha ya ndoa yake yalishachukua picha kongwe. Raza akawa ameshajitengenezea marafiki wa nje. Ratiba yake ikawa nyumbani, kazini kisha baa.

Hamjui Pius romantic wala hajawahi kukutana naye. Anaye mjua yeye ni Pius wa kutumikiwa. Apewe penzi. Chakula kizuri kwa wakati. Nyumba safi kila wakati na nguo zake ziwe safi kama mpya kila akitaka kuvaa. Na Raza akayamudu yote hayo akigawa kazi kwa wasaidizi wake nyumbani, maisha yake yakaendelea bila ndoa ya kufuatana nyuma.

Pius anarudi kutaka wa kumkumbatia, mkewe hata hajui kama Pius ni kiumbe wa malove dove. Anajua ni mtu wa kuingia, piga bao, toka. Na yeye kazi yake ikawa ni kuomba pesa kisha kwenda kufanya yake na wengine.

Na yeye Pius akaanza upweke mpaka alipompata Mina mpenda mikono, na yupo wakati wote. Basi ndio akawa anatulia nyumbani kwa mdogo wake.

Raza akirudi nyumbani anajua Pius hatakuwepo, akifanya yake ya umama, anasambaa baa, kwa wenzie. Pius naye alishajua mkewe hayupo nyumbani, basi akawa akiwekeza muda wake zaidi kwenye biashara zake, wazazi, na ndio mpaka akaishia kwa mke wa mdogo wake.

Wawili hao walikuwa wakikutana, Raza analojua ni kukata mauno. Mumewe anapiga bao. Kazi kwisha. Lakini kila mtu alikuwa akienda kuliwazwa kwengine na watu wengine. Maisha yakaendelea mpaka hayo majanga yakawapata. Wamejikuta wamerudi kuwa wao wawili. Ndoa kongwe takatifu na binti wawili.

~~~~~~~~~~~~~~

Raza alikuwa amepotelea kwenye mawazo yaliyomrudisha mbali ila wazi yalionekana ni mawazo yaliyoweza kumtoa furaha yote na kumpa huzuni. Alibadilika mpaka usoni akanyongea. Ikawa kama aliyekumbushwa fedheha. Akapoa kabisa mpaka Pius alipomshitua kwa swali. “Unafikiri wewe na mwanao mnaweza chukua off hiyo siku ya jumatatu?” Raza akagutuka na kujaribu kurudisha mawazo pale.

“Jumatatu wanaweza kukupa off ofisini kwako?” Ikabidi mumewe arudie swali na kuongeza. “Mbona umepotea tena?” “Sijategemea kama unaweza kuja taka muda na mimi, Pius!” “Naamini sijachelewa. Eti Raza? Si tumekubaliana safari hii tunaanza upya na vizuri?” “Nitashukuru. Na kuhusu ofisini hakuna tatizo.” Raza hakuwa na neno, alipokea vile Mungu alivyombariki bila kinyongo.

Katika Majivu ya Machungu, Upendo Wazaliwa Upya

Dereva alikuja kuwachukua mapema bila ya kuchelewa. Safari ya uwanja wa ndege ikaanza Raza na wanae hawajui wanakoelekea. Polla akawa anaimba njia nzima, dada yake anamkosoa. Wakaanza kubishana. “Umeanza Poliny!” “Sasa huyo mwanao asirekebishwe!?” Baba mtu naye akadakia. Polla akaanza kulia.

“Kwani nyinyi kila kitu ni lazima mumkosoe?” “Hata kama maneno anakosea mama jamani!?” “Kwa hiyo hivyo anavyolia ndio unaona raha?” “Mimi nilikuwa nikimsaidia.” “Niache mwenyewe, sitaki kusaidiwa na wewe.”

“Nyamaza mwaya Polla mtoto mzuri. Imba vile unavyotaka. Kwanza sauti yako nzuri.” Acha Pius na Poliny waangue kicheko, mbavu hawana. Polla akazidi kulia.

“Hivi kwa nini mnafanya hivyo!?” Dereva kimya, familia hiyo wakizozana. Raza akaanza kumbembeleza mwanae, Pius na yeye anacheka kimyakimya.

“Na kwenye ndege sikai na wewe, nakaa na mama!” Hapo Pius akashituka. “Mimi ndio nakaa na mama yako.” “Mimi nimeshawahi.” “Sasa unawahi vipi kwenye mipango yangu wewe Polla!? Nishapanga kila mtu anakaa wapi!” “Lakini hakuna aliyekusikia ukiwahi. Mimi nishawahi na kila mtu amenisikia. Usifanye uonezi kama Poliny.” Akaanza kubishana sasa Polla na baba yake, wote wanataka kukaa na Raza, yeye kimya.

Mwishoe Poliny akamtetea baba yake. “Kwanza hii safari ni ya dad, wewe umekaribishwa tu. Huwezi jichagulia.” Wawili hao wakaanza kumchangia Polla mpaka akaanza kulia tena. Baba yake muonezi kama Poliny.

Wakafika uwanja wa ndege wanabishana kwelikweli, Polla hataki kushindwa. Na anawamudu wote wawili kwa hoja. Anang’ang’ania yeye amewahi. Mwishoe akasema warushe moja ya kitufe chake. Kina pande mbili. Yeye akachagua upande wake. Baba yake akampa upande mwingine. Poliny akamuonya baba yake. “Usikubali dad. Huna game utamshinda Polla. Hapo anakutega tu, atakushinda.”

Wakabishana tena hapo nje ya uwanja wa ndege kila mmoja na mzigo wake mpaka Raza akamwambia Polla arushe. Ilipotua chini, Polla akashinda. Bwana alifurahi! Alishangilia hapo kila mtu akawageukia wao. “Raza, zungumza na mwanao. Mimi nishaweka mipango yangu.” “Kama sikai na mama, mimi siendi. Mwambie dereva arudi kunichukua, nitakaa mwenyewe nyumbani. Kwanza najua kupika kuliko Poliny, sina haja naye.” Polla akaweka ngumu hapo wanapita security point bado wanabishana.

Uzuri wote walikuwa wakikaa first class viti vinavyofuatana. Polla akaishia kukaa na mama yake mbele yao, Poliny na baba yake wamepoa. Vicheko vyote vimeisha. “Nilikwambia game yoyote anayokwambia mshindane Polla, usikubali.” “Halafu ananiita mimi muonezi wakati yeye anafanya maufilishi!” Raza hana mbavu amekaa na mwanae.

 ~~~~~~~~~~~~~~

Safari ya visiwa vya Mauritius ikaanza wote wamejawa hamasa ya kufika huko, maana ilikuwa mara yao ya kwanza. Kwa hakika waliandaliwa ipasavyo. Sekretari wa Pius aliandaa kana kwamba wawili hao wanakwenda fungate mpaka Raza akashangaa. Chumba chao kilitayarishwa kama wanaingia honeymoon!

“Au wametupa chumba sicho?” Raza akauliza akijaribu kutafuta pakukanyaga. Maana chumba kilijaa maua  ya roses nyekundu kila mahali mpaka kitandani!

 Honeymoon yetu ya pili. Ya kwanza haikuwa imekaa vizuri.” Raza akamwangalia kwa mshangao. “Kumbe unajua! Sasa kwa nini ulikuwa ukinifanyia vile!?” “Achana nayo.” “Hapana Pius, nataka kujua. Maana ilikuwa kama umelazimishwa au unanifanyia kusudi! Tena ni kama kikatili kabisa! Ni kwa nini?!” Akauliza kwa kuumia kabisa.

“Raza, tumefanikiwa kumlaza Polla, acha tutumie muda huu vizuri. Achana na mambo ya zamani.” “Wewe umesema tunaanza upya. Mwanzo huu unaweza kuwa bora kuliko wa mwanzoni. Sasa kwa nini tunaanza kwa kufichana? Niambie tu nijue kilichokuwa kikiendelea.” Pius akafikiria, akaona amwambie ukweli ila kwa ufupi.

~~~~~~~~~~~~~~

“Nisikilize Raza, wewe hukuwa tatizo kabisa, ila ulinikuta nikiwa na mambo mengi, na uchungu, ndio nahisi nikakumalizia wewe hasira kwa sababu ndiye uliyekuwa karibu yangu.” Akaanza Pius. Akamsimulia habari za Irena tokea mwanzo mpaka mwisho.

“Yaani wewe umekuja kwenye maisha yangu umekutana na moyo uliokuwa na maumivu na sijui chakufanya. Ila kuoa ilikuwa ni lazima na mama naye akawa ananilazimisha. Siku tunafunga ndoa ndio ilikuwa mbaya zaidi maana kwa mara ya kwanza ndio Irena alinijibu baada ya muda mrefu. Akaniambia ni kweli aliolewa na alishapata mtoto wa pili na hana mpango wa kuja kurudi tena Uingereza. Kwa kifupi ndio alikuwa akiniaga ramsi. Nilikuwa na hali mbaya, na ndio nilikuwa nikijitayarisha kuja kanisani.”

“Kumbuka matarajio niliyokuwa nayo ni angalau angemaliza muda wa kutumikia serikali yake na kuamua tukaishi Uingereza. Nilifika mahali nilikuwa tayari nirudi nikaishi naye nchini Uingereza. Kufupisha habari, ile harusi ilikuwa natamani ufupishwe, nitoke mbele ya uso wa watu, nikajifungie mahali. Ila nikawa sina jinsi, wewe upo. Ndio nikawa nazika hisia zangu kwenye vitabu. Lakini wewe hukuwa tatizo.”

“Ila ninachoshukuru, ulinijulia aisee! Ule ukimya na kuniacha, ndio kitu pekee nilikuwa nikihitaji. Ukawa umenisoma kwa haraka. Ukanijulia.” “Kwa hiyo ndio msichana unayempenda mpaka leo?” Akauliza kwa wivu.

“Sasa acha nikwambie ukweli. Akili ilikuja kukubaliana na matokeo tukiwa tumeshapotezana. Kumbuka baada ya pale ni kama sikuwa nikikaa sana nyumbani. Safari za nje ya nchi zikawa nyingi. Nakuja kutulia na kujirudi kwako, nikawa nimeshachelewa.”

“Nikakukuta na wewe ni kama unamaisha yako, na watu wako na utaratibu uliojiwekea. Haupo tena nyumbani na tukawa tushajiwekea msingi fulani hivi tunao usimamia ikawa  ngumu sasa kuanza upya wakati tushakomaa kwenye maisha fulani. Ndio ikawa tunaishi bora siku zinaenda. Halafu tukawa hata hatujaweka msingi mzuri wa ndoa. Mahusiano yetu yakawa kama tuliokubaliana kuishi kwa mtindo fulani hivi! Basi.”

“Swala la mimi kutamani nje likawa gumu kwa sababu ulikuwa mke sahihi tokea mwanzo. Yaani una VIGEZO vyote, ndio maana hata mama aliposema nikuoe wewe, nikajiambia kama si Irena, basi yeyote. Ila sasa ukawa WEWE. Unanijulia kila mahali. Halafu umesoma. Unauelewa wa mambo. Msafi. Unanijulia chakula. Nyumba ukawa umeimudu mpaka wafanyakazi wa nje unawajulia. Hilo nikajiambia swala la mwanamke, nimemaliza.”

“Hata swala la mtoto wa kiume lilipoanza, nakwambia ukweli kabisa Raza, swala la kuzaa nje hata halikuwepo. Kwanza nikajihisi usumbufu. Nikajiambia akija ongezeka mwanamke mwingine hapa katikati yetu, atatuvurugia utaratibu wetu. Wewe unanijua jinsi nisivyopenda mabadiliko.” Raza akacheka. Maana alimjua Pius. Hata kochi ndani ya nyumba yake mwenyewe anataka akalie hilohilo kila siku.

“Natakaga mambo yangu yasibadilike. Sasa nikasema naweza pata mwanamke akatupa mtoto wa kiume, lakini akaja na usumbufu na vurugu zake kwenye maisha yetu. Nikajiambia bora Raza amenipa watoto wawili, inatosha. Hakika sikuwa nakulaumu wewe hata kidogo. Na swala la kujaribu nje hata kabla wengine hawajanishauri, mimi nilishapingana nalo. Najijua mimi, siwezi kuanzana na mwanamke yeyote yule. Kwanza SITAKI.”

“Unaweza usiamini hili Raza, lakini wewe unanijulia aisee. Naweza nikawa nje ya nchi, kwenye mahoteli yao hayo wanayo yasifia, hata wanipe nini, nakumbuka nyumbani. Nahesabu siku nirudi nyumbani nikijua nitakukuta na kila kitu changu kitakuwa sawa. Kuanzia chakula changu mpaka mavazi yangu. Naweza nikawa nimefikia kwenye five star hotel, wananifulia nguo zangu, siridhiki najiambia ningekuwa nyumbani, Raza angehakikisha sitoki hivi.” Raza hakuwa akiamini kwa furaha.

“Na ndio maana tokea zamani walipokuwa wakisema unaniloga, sikujali. Kumbuka nilishajiambia kama si Irena, ni yeyote. Sasa yeyote ukawa ndio wewe, na wewe unaniwezea. Kwangu ukaonekana hujali vile nilivyo, na maisha tunayoishi. Ukawa ni kama ulikuwa umejitosheleza.”

“Sikuwa na jinsi Pius. Kumbuka nilishaondoka nyumbani, nikalaaniwa kwa laana zote kwa ajili yako. Sina wazazi, sina ndugu kwa kukimbilia ndoa ya kanisani. Leo narudi wapi! Nasema nini! Ilibidi nipambane kwa kadiri ya uwezo wangu kuonyesha kila mtu nilichokimbilia sikukosea. Lakini haikuwa rahisi Pius! Hata kidogo!”

“Lakini kwangu ulionyesha hujali, bora yako yanakuendea sawa! Na acha nikwambie ukweli Raza, ulianza kwangu kimaslahi sana. Tuwe wakweli. Mimi nikajua njia pekee ya kukufurahisha ni pesa ambazo unaomba kila wakati. Ndio maana kama utagundua linapofika swala la pesa huwa sikuzungushi hata mara moja. Kwa mara ya kwanza nimekukatalia hivi majuzi. Si kweli?” “Sasa haimaanishi eti kwamba ndio kitu pekee kilichonifanya niolewe na wewe!” “Raza!” Pius akawa kama anayemsuta.

“Basi niseme ni moja ya sababu zilizonivutia.” Akajisalimisha. “Kwa kuwa sina nia ya kurudisha mambo ya nyuma wala kukuumiza, nipo hapa kujenga na sitaki kukuingiza dhambini, acha nisikuulize hili swali.” “Swali gani?” “Acha tu Raza. Mimi nimekubali kwa upande wangu. Nimekubali yote.” “Wewe niulize tu.” “Raza, binafsi nimekubali yaishe. Tafadhali yaishe.” “Nataka kujua hilo swali.” Pius akamtizama mwishoe akaamua kumwambia kwa staha tu maana Raza mwenyewe alionekana kutaka kujua.

“Umesema pesa peke yake si kilichokuvutia kwangu. Mimi ambaye hata sikukuonyesha upendo! Usinijibu, lakini kuwa mkweli nafsini kwako na ujijibu, ni kipi kingine kilikuvuta kwangu mbali na pesa ulizogundua nilikuwa nazo tokea mwanzo?” Akamuona ametulia.

“Basi mimi nakuwa mkweli. Mimi nilikusoma, nikajua shida ni pesa, na mimi nikavutiwa na unayonifanyia, nikasema kwa upande wa mke utanifaa maana hukuonyesha kuhangaika na mambo ya moyoni. Nikajificha kwenye aina hiyo ya ndoa, sikujali. Nimekuwa mkweli. Ila wewe usinijibu.” Raza akapoa kabisa.

Akaamua kwenda kuoga. “Usinikasirikie, mimi nimekuwa mkweli.” “Mimi sijakasirika, naenda kuoga.” “Sasa aina hii ya chumba na yote humu ndani ni madhari ya fungate. Hata huko bafuni wametayarisha kwa muundo wa wawili wapendanao. Si tumekubaliana kuanza upya?” Ikabidi ajirudi kwa kuanza kutulia maana ni kweli moyoni alishaanza kusumbuka.

“Tuanze tu. Najua ni maisha mageni. Lakini naamini hatutakosea. Kwanza umri umekwenda. Tumebaki sisi wenyewe. Acha tuanze fungate nyingine.” “Sasa unataka tufanyaje?” “Tuanzie kwenye hilo jaccuz humo ndani. Wewe ushawahi fanya mapenzi kenye jaccuz?” Raza alicheka sana.

“Kwa uchekaji huo, ni hujawahi. Sasa twende nikakuonyeshe penzi la majini.” Raza hakuwa akiamini. “Kumbe mambo unayajua!?” “Nishakwambia nilikuwa nimeumizwa. Na wewe ndiye uliyekuwa karibu ukamaliziwa hasira. Nikaja kujirudi wewe haupo. Sasa tulia upend we. Na uache kujivua.” “Navuliwa?” Raza anauliza hana mbavu kwa cheko.

“Mpaka sidiria. Na hivyo unavyonijulia mpaka kitandani! Acha ulipwe fadhila. Kaa mkao wa kupokea tu.” “Sawa Pius.” Kwa hakika walikuwa na wakati mzuri sana. Waliendelea na huo mwanzo mpya wakiwa wanajuana vilivyo na msingi wa kimungu katikati yao.

Kila Undani Una Mlango Wa Kushangaza Usiotarajiwa

Yapo mambo yapo sirini kwa sababu. Mengine ni bora kuacha kuyachambua chambua. Unaweza dharau ukidhani ni jivu tupu kumbe limefunika makaa yenye moto.   Walirudi nchini wawili hao ungejua wapo ukurasa mmoja. Hata Poliny aliona tofauti kwa baba yake jinsi anavyomchukulia mama yao, na yeye heshima ikaongezeka kwa mama yake.

Ila bado Chezo alikuwa akimsumbua Pius akili. Kwa hakika alitaka kumuona mwizi wa mkewe. Akajikuta anampenda Raza, hataki kuja kumchangia tena na mtu. ‘Huyu Chezo aliyefanikiwa kumtuliza Raza kwa muda wote huo, yukoje na ana nini cha ziada!’  Maana mkewe mzuri haswa! Halafu ni mtoto wa mjini! Kweli aje ashie na dereva asiye na hela wakati alimjua Raza nimpenda pesa kama benki! Yakawa ni maswali yanayomnyima raha Pius, hawezi tulia nafsi mwake. Kwa Raza alijidai yameisha. Sasa anarudije tena kumuulizia Chezo na wakati wameshakubaliana wanaanza upya!

~~~~~~~~~~~~~~

Akaona aanzie kwa bosi wake Chezo. Mzee R uhinda. “Vipi Chezo?” Akauliza swali kimtego baada ya salamu. “Tena naona safari hii mmewahi vizuri sana! Nimesikia safari hii mkewe ameleta  samaki wa ziwani mpema kweli! Hivi nilikuwa nimtume Chezo awasiliane na Raza, kama atahitaji ili awapelekee nyumbani.” Moyo ukapasuka paa! ‘Mzee anataka kumtuma fisi buchani tena!’ Ila akajikaza na kufikiria kwa haraka.

“Pale nyumbani kwa sasa hatuna msichana wa kazi. Mida ya jioni Polla anakuwepo nyumbani peke yake, haturuhusu mtu afike pale mpaka sisi wenyewe tuwepo. Sasa kwa kuwa leo nitawahi kutoka, mwambie aniletee hapa ofisini kwenye mida ya saa sita, ila awafunge vizuri.” “Nitatoa hayo maagizo hayo.” Angalau hilo likakaa sawa.

 “Pius!” “Bado nipo baba.” “Mbona siku hizi nyumbani umepotea na jumapili kama mbili tatu sijakuona kanisani.” “Raza amepata kanisa fulani hivi, naona huko wamempokea vizuri. Polla amepapenda na ashatengeneza marafiki hapo. Ndio na mimi pamoja na Polliny tukaona tuwe tunaongozana nao huko!” Mzee Ruhinda kwa hakika si jibu alilolitegemea hata kidogo! Pius! Mromani damu! Halafu kukawa na jumbe kwenye hilo jibu lake, akajua amekusudiwa kufikishiwa. ‘Raza kupokelewa vizuri, na Polla kutengeneza marafiki!’

“Halafu weekend hii mimi na watoto tulimpeleka Mauritius kwenda kupumzika. Amepitia kipindi kigumu sana, nikaona akapumzike huko. Ndio tumerudi. Msalimie mama, nikipata nafsi nitapita.” “Uwe na siku njema.” “Asante baba, na wewe.” Wakaagana lakini wakaachana kila mmoja na lake.

Kwa Pius akiwaza. “Kumbe ndivyo jinsi walivyokutana hawa!” Akabaki akiwaza akimsubiria mwizi wake.

“Mama Pius atachanganyikiwa akisikia haya!” Mzee Ruhinda akawa kwenye butwaa. “Pius amehama dhehebu kumfuata Raza!” Akasahau yeye Raza alihama DINI kumfuata kijana wake. Sasa safari hii kijana wake anahama DHEHEBU kumfuata Raza! Mzee Ruhinda hajui mlango wa kanisa lolote isipokuwa la RC.

Polliny ni kopi ya babu yake na baba yake. Mitazamo yao wote inaendana. Huyo Polliny ni kipenzi cha mzee Ruhinda. Ukiwakuta wakizungumza utafikiri mzee Ruhinda anazungumza na mwanauchumi au mwanasiasa wa ulimwengu anayejua sheria. Lugha imenyooka. Akili safi kama baba yake. Mzee alimpenda sana kati ya wajukuu zake wote. Sasa leo na yeye haonekaniki kanisani wala nyumbani! Pius kipenzi cha mama ameacha kupita nyumbani! Mzee akajua shilingi ishapinduka.

Mwana Kulitafuta…

Kwenye mida ya saa sita kasoro hivi sekretari wa Pius akamtaarifu anamgeni getini anamzigo wake, kama aache getini! Pius alikuwa na shauku ya kumuona mwizi wake, akataka kumchunguza bata! Akasema akaribishwe mpaka ofisini kwake.

Akajiweka sawa akimsubiria. Baada ya muda sekretari akafungua mlango na kumtaarifu kuwa mgeni amefika. Akamwambia amkaribishe ndani. Chezo aliyeingia hapo, alimuacha Pius na mshangao.

Kwanza alikuwa msafi, amevaa shati jeupe linawaka kama na yeye anapeleka nguo zake dry cleaner. Halafu mrefu aliyejazia kama mwana ndondi anayefanya juhudi za makusudi kujazia misuli!  Nywele na ndevu vimechongwa kama mwanamtindo ambaye kazi yake ni kuonyesha uzuri wakiume. Rangi ya maji ya kunde kwenda mweupe. Mzuri wa sura, wakuvutia.  Chezo alikuwa si mchezo!

Aliendana na Raza haswa. Yaani ukiwasimamisha wao wawili ungesema ni zile couple zakufunga karne. Muonekano ‘A' mpaka akamvuruga kabisa Pius. Maana yeye alijua ni Chezo dereva, choka mbaya. Anakuja kukutana na Chezo aliyemfanya mpaka ajiulize ni kipi Raza kinambakisha kwake!

“Habari?” Chezo akasalimia kiuungwana akiwa na mzigo mkononi. Akamuita sekretari wake akamwambia ampokee mzigo na kuuweka kwenye friji. Hapo hata hakuwa amejibu salamu ya Chezo wala kumkaribisha kiti, alibaki amesimama vilevile kama alivyoingia.

Sekretari alipotoka akamwambia akae na wala si kwa kumkaribisha bali kama amri. “Kaa.” Chezo akaangalia jinsi kulivyopangiliwa pale. Pasafi, kila kiti kimekaa kwa mpangilio. Halafu na kuna makochi pembeni yamekaa kama sebule ya mtu! Yamezunguka meza nzuri sana katikati.

Akaangaza macho akaangalia kile chumba jinsi kilivyo kikubwa! Akababaika kidogo ila akavuta kiti ambacho kipo mbele ya Pius kwa pembeni kidogo. Akakaa na kubaki akimtizama Pius kwa utulivu wala hakuonyesha hofu kitu kilichomkera Pius na kumpandisha hasira.

“Kwahiyo mkeo akikutuma uuze samaki ndio unaiba na wake za watu?” Chezo akatoa tabasamu tu, hakumjibu kama aliyemdharau. “Nakuuliza wewe? Unatumia biashara ya mkeo ya samaki na kuiba au kulaghai wake za watu?” “Sijawahi iba.” Chezo akamjibu  kwa utulivu tu na kusimama. “Uwe na siku njema.” “Sijakuruhusu uondoke.” “Binafsi naona tumemaliza.” “Ukiondoka kabla sijakuruhusu, jua umejiingiza matatizoni mwenyewe.” Chezo akabaki amesimama kama ambaye anajishauri aondoke au la.

Pius naye akabaki akimtizama kwa jeuri, ila wivu tu. “Kama hakuna jingine tafadhali naomba mimi niondoke niendelee na majukumu yangu mengine.” “Ambayo yanahusiana na kuvunja ndoa za watu?” “Huwezi vunja kitu ambacho hakikuwahi kujengwa.” Pius hakutegemea. Kabla taarifa hazijafika kichwani, Chezo akaongeza.

Hukuwahi mpenda Raza, Pius. Nashangaa ni kwa nini sasahivi ndio unaanzisha fujo zisizo na sababu!” Hapo akamtibua Pius. “Unasemaje wewe?” “Mimi sitaki matatizo na wewe. Tafadhali naomba niondoke.” “Kitendo cha kuwa na mahusiano na mke wangu, ni kwamba tayari ulitafuta matatizo.” “Hayo umegundua lini Pius? Huyu Raza si alikuwepo miaka yote ukimdharau na kumpuuza tu!”

“Hivi unajua alipokuwa akiugua ni nani alikuwa akimuuguza? Unajua alipokuwa na matatizo nani alikuwa naye? Maana kwa hakika si wewe, japo ulikuwepo kwenye nyumba hiyohiyo ambayo Raza alikuwa akiteseka na maumivu makali sana ya tumbo kabla hajatolewa zile vimbe zilizokuwa sikimuandama kipindi cha hedhi zake! Leo unashindwa kujiangalia mwenyewe kwenye kioo na kujilaumu, unatafuta wakumtupia lawama!” Ya Andy yakamrudia yeye kama ilivyo! Asiamini.

“Na unachokifanya kwake sasahivi ni ubinafsi tu. Kumtenga na watu wanao simama naye kwenye upweke wake. Sasahivi unakumbuka shuka, na kumpa masharti Raza aliyekuwepo kwenye maisha yako karibia miaka 20! Ulikuwa wapi kipindi akidhalilika kwa kashfa yako ya kuzaa na mke wa mdogo wako? Sio wewe ulikuwa umejaa mitandaoni ukimpigania mke wa mdogo wako? Hukuwa umemkumbuka Raza? Hukujua kama na yeye ni binadamu na anayo nafsi kama binadamu wengine?” Kama alivyomjia juu Andy, ikawa kama Mungu amembananisha.

Pius alikuwa kwenye hali ngumu, gafla akakaukwa midomo. “Hivi unajua adha uliyompitisha lakini au ndio unatokea tu sasahivi na kuamua asitishe mawasiliano na kila mtu, ili umfungie ndani aendelee kukutumikia kama mtumwa wako, halafu wewe ukiendelea na maisha yako?” “Chezo…” Hakutaka kumsikiliza, akaendelea.

“Sasa kwa kuwa mimi simtumii Raza, na ninajali anachojisikia, nitaheshimu matakwa yake. Nitamuacha kabisa ili nisiendelee kumuumiza. Ila kuwa makini Pius. Takataka kwako, alumasi kwa wengine. Acheni kuchezea hisia za watu, mkiwafanya mateka sababu ya nafasi Mungu alizowapa. Uwe na siku njema.” Chezo akatoka kisha akarudi tena, kama aliyefunga mlango na kuufungua.

“Nina pesa ya Raza. Niliitumia kununulia baadhi ya vitu. Aliponipa maagizo yako, yakutowasiliana tena, nimerudisha kwa mwenye duka ambaye ni rafiki yangu. Kwa hiyo pesa yake ipo kama alivyonikabidhi mara ya mwisho. Naona kwa kuwa sasahivi wewe ndiye unayetoa muongozo wa nini kifanyike, ndio nauliza, pesa ya Raza itamfikia vipi?” “Lengo lako ni kumfikia tu mke wangu. Hatuna shida.” “Wewe ndio huna shida. Hili ni jasho lake. Anajinyima sana Raza kutafuta pesa. Kwa uzima na ugonjwa, huwa hakosi kazini. Wakati mwingine nilikuwa nikimpelekea dawa ofisini kwake ili kumsaidia kumaliza siku ya kazi, lakini si kulala nyumbani. Ni jasho lake, ni lazima limfikie. Acha kupuuza juhudi za Raza.” “Mpe mzee Ruhinda, atamfikishia.” Chezo akacheka kwa masikitiko na kutingisha kichwa.

“Wewe si unathamini sana jasho la mke wangu? Sasa mpe baba yake mkwe amfikishie. Na ole wako hata ukosee nije nikute simu yako au ujumbe kwenye simu ya Raza, ndipo utagundua aliyemfikisha Raza kanisani na kula naye kiapo ni mimi au wewe unayelilia mke wangu. Nitakuita mbele za mabosi zako, na kuhakikisha mkeo YUPO kwenye hicho kikao akusikie unavyomlilia mke wangu. Na nitahakikisha baada ya hapo, kila mwajiri hapa nchini anapata taarifa zako za kutokuwa mwaminifu.” Chezo alimtizama kwa sekunde kadhaa, bila hata ya kulipwa pesa yake au kuongeza neno jingine, akatoka.

Katikati ya Kungoja na Kutu.

Mill akashangaa Pam ametoka kitandani asubuhi na mapema. Akataka kuuliza ila akapitiwa na usingizi. Kuja kuamka akamkuta jikoni anakula ugali na kiporo cha nyama za jana yake, mboga za majani. Asubuhi! Akawa hajaelewa. “Leo tunaanzia ugali?!” “Wewe na mwanao mtakunywa chai. Ila acha nishibe kwanza. Nimeamka na njaa!” Akamuona anakazana kula, akahisi pengine ni mchezo mrefu wa usiku uliopita wakigeuzana kana kwamba hawajashikana miaka.

Akaangalia muda. “Huyu si atachelewa shule? Nisaidie nini?” “Kutengeneza kifungua kinywa chenu.” Akajibu na kuweka tonge zito tu na alionekana kweli ananjaa. Ikabidi sasa yeye asaidie mambo hapo, ndipo Shema akafanikiwa kutoka kwa wakati.

Mchana muda wa kula wakatoka. Akamuona anaagiza ugali wa muhogo, kuku wa makange na mtindi. Bwana Pam alikula! Akaomba afungiwe tena ugali mwingine na mboga kama vile. Mill kimya akishangaa nafsini mwake.

~~~~~~~~~~~~~~

Hayo maisha yakaendelea. Njaa ya Pam inatibiwa kwa ugali. Kila anachopika kikawa ugali mpaka Shema akaanza kulalamika kwamba amechoka ugali. Ndio Mill naye akaponea hapohapo lakini hakubadilika. Ugali kwenda mbele na halalamiki kama wao wanajinunulia kitu chao, basi ujue ndio amepata kifungua kinywa cha asubuhi. Chai, ugali na mboga walizokataa kula wao usiku, basi Pam atakula kwa furaha zote ndipo waende kazini.

~~~~~~~~~~~~~~

Mama yake alishaanza kazi hapo kwenye kitendo cha vipimo. Pam akipita mara kwa mara kuhakikisha yupo sawa na hakosei kazi ya watu.  Siku hiyo akatoka benki akaenda kwa mama yake na ugali alionunua, nyama choma na mtindi. Akaanza kula kama ametoka shamba na hajala siku nzima. Mama yake akamwangalia, akajua tayari.

“Njaa hiyo ni ya tokea lini?” Pam akacheka akiendelea kula kwa shangwe. Akala hapo huku akizungumza na mama yake. Simu ya Mill ikaingia. “Twende tukale.” “Hapa nakula. Ila nahisi wamenipunja. Kaugali kadogo!” “Kwamba ulishanunua ugali mapema hii!?” “Mbona kama swala la upunjwaji wangu huzungumzii?!” “Haya twende ukale ugali wa mtama, huwa unasema angalau huo unashika tumbo.” Akanyanyuka hapo haraka kama ambaye hakuwa akila.

~~~~~~~~~~~~~~

Aliporudi mama yake akamuita. “Mara ya mwisho kupata siku zako ilikuwa lini?” Pam akashituka na kubaki akipiga mahesabu, hayaji. Akatoka hapo bila ya kuaga wala kutoa jibu mpaka ofisini kwa Mill. Akamuuliza sekretari kama anamgeni, akaambiwa hana. Akaingia.

~~~~~~~~~~~~~~

Aliingia bila hodi mpaka Mill akashituka. “Twende.” “Wapi!?” Mill akauliza kwa kushangaa. “Mahakamani, tukafunge ndoa.” Kwa sekunde kadhaa Mill akawa kama hajaelewa. Pam akabaki amesimama, anamsubiria aamke kitini. Mill akaona aulize tu.

“Kwamba tunakwenda kufunga ndoa sasahivi?!” “Halafu ile mipango yako ambayo haikamiliki, itafuata baada ya sisi kufunga ndoa kisheria. LEO. Nikimaanisha hivi, hapa ninapozungumza, sasahivi, tunakwenda kufunga ndoa. Halafu mipango yako na watu wako itakapokamilika, tutaendelea. Lakini tusiendelee kuishi hivi bila ndoa.” Pam akaweka kituo, akimtizama machoni.

“Hatuwezi kufanya mambo kwa kukurupuka Pam! Na hatuwezi kwenda sisi wenyewe bila watu wetu wa karibu!” “Mimi nakutaka wewe uwepo. Basi. Wengine wote wanaweza kusubiria mipango yako. Huu ni wangu.” “Bado naona tufanye kwa utaratibu mzuri.” “Sawa.” Akajibu hivyo na kutoka.

Akamuacha Mill kama hajaelewa vizuri. ‘Sawa’ hii mbona imekubalika kirahisi hivi! Pam alivyombishi! Kengele ikagonga kichwani akajua hii sawa si sawasawa. Akasimama kwa haraka na kumfuata.

Alimkuta amesharudi mezani kwake amekaa. “Pam!” Akamgeukia. “Ila si umenielewa nilichomaanisha?” Akauliza kwa kujihami sana mbele ya wafanyakazi wengine. Hapo Mill mpole, mnyenyekevu, akimjua Pam, dakika 5 mbele.

“Ndiyo.” Pam akamjibu tena kwa ufupi ila kwa ufasaha haswa. Mill akasimama kwa sekunde kadhaa kama ambaye hajaridhika. Akabaki akimtizama, naye Pam akimtizama kama anayesubiria la nyongeza. Mill akameza mate kwa wasiwasi huku wakiangaliana kwa sekunde kadhaa, Pam alipoona hana la nyongeza, akarudisha macho kwenye kompyuta yake na kuendelea na kazi. Mill akasimama hapo kwa sekunde kadhaa mbele huku amepewa mgongo, wafanyakazi wengine wakiendelea na kazi, kimya, akaona aondoke pengine watazungumza vizuri baadaye.

~~~~~~~~~~~~~~

Pam amekuwa akisubiria hiyo ndoa, kama bahari isubirivyo mvua.
Miaka ikizidi kwenda kama mawimbi yanayogusa mwamba bila kuchoka.
Moyo ulijenga uvumilivu kama mti wa nyikani. Ukikua polepole, lakini ukiamini kesho itatoa maua. Ilikuwa kabla ya Shema. Akaja Shema, akapita Kisha na wanae, bado moyo wake ulikuwa na tumaini na yeye zamu yake itakujafika.

Mtoto wa pili anakuja, bado hamna ndoa! Akataka hata ya mahakamani, lakini Mill wa mipango. Sasa, safari hii mipango ya Mill imekutana na Sawa Ya Pam.

Ni nini kitaendelea?

Pius amechokonoa mpaka amekutana na Penzi la nje la mkewe Lililokuwa Limekomaa Mpaka Kuota Mizizi. Kumbe Kuna historia nzito katikati YAO. Ipo thamani kubwa iliyokwisha jengwa kwa mkewe. Yapo MAISHA ya undani kabisa yaliyokuwa yakiendelea, yeye hana habari! Hawa wawili walikuwa katika uzima na furaha, zaidi yake yeye na mkewe! Tena si kwa muda mfupi! Ni miaka!

Gafla yeye anaonekana muingiliaji na mvurugaji!

Chezo si Mchezo. Alichokitafuta, hatimaye amekipata. Amemchuguza bata yeye mwenyewe, ataendelea kumla? Chezo amemfanya ajione kama kipanzi!

Kama vile Raza si size yake!

Usipitwe.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment