“Kwani na sisi si tumetoka
hukohuko! Umekua na Emelda siku nzima. Unataka nyumba nzima ikeshe! Wewe kuwa
na kiasi, kesho tena mtakutana. Dakika tano ya kiMungu. Haya nendeni
nasubiria.” Junior akasimama akitingisha kichwa kwa masikitiko. Wengine
wakicheka. “Acha mimi nitangulie. Usiku mwema.” Ezra yeye akaondoka.
Junior akamshika
mkono Emelda wakaelekea chumbani kwake. Akaingia na kusimama tu mlangoni.
Emelda akaweka vitu vyake vyote kitandani pamoja na alivyonunuliwa na Jelini.
“Jelini anaroho nzuri!” “Hayo ya kesho. Sasahivi nataka muda na wewe. Hizi
dakika tano, nikushike mpaka akili na moyo utulie. Leo nimekuwa na siku yenye habari
zisizo nzuri kasoro wewe tu. Acha nikushike, nitulie ndipo nikalale.”
Emelda akajichekesha na kumsogelea.
“Niambie ukweli jinsi
unavyojisikia. Jumlisha yote mpaka na ya Ester. Na usinifiche.” “Moyo wangu
umejaa amani na furaha Junior. Nimekupata wewe, halafu tunarudi wote nyumbani
kwetu! Sirudi tena peke yangu. Umemtoa mama yangu kwenye dhiki! Yote hayo
yananipa furaha. Na zaidi nina uhakika wanafikia kwenye mazingira ambayo
wanamsubiria kwa hamu si kama mzigo. Asante.”
Akamkumbatia vizuri
akiwa amepishanisha mikono nyuma yake. Akawa amemvuta karibu kabisa. Emelda
alipotulia, Junior na yeye akaanza kusikia kutulia mpaka akafunga macho kabisa,
kichwa akajiegemeza juu ya kichwa chake, wakatulia kimya. Emelda akamsikia
akivuta pumzi mfululizo kwa muda.
Akawa mwaminifu.
Baada ya dakika nne akamuachia. “Kesho nitakuja kukuchukua twende kanisani
pamoja.” Emelda akacheka kwa furaha. “Sasa sio uondoke na Noah. Unisubirie.”
Huwa mchungaji na mke wake wanawahi sana kanisani. Nusu saa kama wamechelewa
ila lisaa kabla ya ibada ya kwanza kuanza, wanakuwa walishawasili kanisani.
Kama Emelda akiwahi basi ataongozana na Noah ambaye huwahi na yeye kufunga
vyombo lakini sio lisaa. Mara nyingi hufika dakika 20 kabla ya ibada, ndipo
Emelda hujipatia usafiri hapo. Vinginevyo, daladala. Akapata kiss fupi
na kuondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~
Akamsikia akimwambia
baba yake huku akitoka. “Uaminifu na kiasi pia ni tunda ambalo na
mimi sikunyimwa.” “Sasa aliyekwambia umetumia dakika 5 tu ni nani?” “Utakuwa
umehsabia kutokea uliposema, na si tokea tumepata faragha na Emelda.
Sijazidisha muda. Nashukuru baba yangu na usiku mwema.” Akajichekea mwenyewe
chumbani. “Umakini huko barabarani tafadhali.” “Asante baba.” Kimya milango
ikaanza kufungwa. Akajua ameshaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~
Mara simu. Junior!
Akajawa furaha na kujitupa kitandani kabisa kisha akapokea. Wakaanza kuzungumza
kana kwamba hawajatoka kuagana. Cheko limemjaa Emelda kama sio yeye! Ndani ya
masaa machache tu ndani ya hiyo siku, historia yake imebadilishwa.
Alikuwa na furaha, yakupita maelezo. Hatimaye maombi yake yamejibiwa.
Jumapili.
Ikawa hivi. Emelda alifika
na Junior hapo kanisani. “Tafadhali kuwa makini na Edwin.” Emelda akajaribu
kufikiria. “Namaanisha sio tena unakuwa muda wa kubembelezana! Unamwambia tu
kwamba ulishampa jibu Ester, ila umekuja kugundua hakumfikishia majibu. Usianze
kusema juu ya vitu alivyokuwa akikupa. Halafu unamtaarifu. Sio kumuomba
ruhusa. Mtaarifu kuwa leo ni ibada ya kuchumbia Ezra, utakuwepo ibadani na
familia. Atafute mtu mwingine wa kushika darasa lako.” Emelda akashangaa sana,
ila akashindwa chakusema.
“Mbona kama
hujaridhika?!” “Watu wengi hawapendi kuhudumu kwa watoto Junior. Kila mtu anakuwa
na visingizio kama hiki unachosema! Wakati mwingine tunajikuta tukichanganya
madarasa sababu walimu ni wachache. Halafu hata hivyo hiyo sababu itakuwa si ya
kweli, kwa sababu mara nyingine tukiwa tuna walimu wachache, huwa tunafanya ibada
ya sifa pamoja na kanisa zima, kipindi tu cha neno ndipo tunaondoka na watoto.”
Junior akafikiria kwa haraka.
“Basi na leo mfanye
hivyohivyo, halafu wakati wa neno na mimi nakuja.” Emelda akazidi
kushangaa. “Kuja, unamaanisha na wewe kufundisha watoto!?” “Ndiyo. Au unaona
nitakuwa nikiwaingilia?” “Junior! Najua kwa hakika, mchungaji na mama
mchungaji, ibada huwa haindelei pale bila ya kukuona wewe na Ezra.”
“Nitawaambia na mimi nahamia kwa watoto.” Emelda akaona ugumu utakao kuwepo
lakini hajui amwambie nini!
“Mbona kama hutaki?!”
“Nataka Junior. Karibu.” Kisha akaanza kucheka. “Acha kunicheka Emelda!”
“Unajua wazi mambo hapa kanisani hayaendi bila wewe na Ezra. Hata umeme
ukisumbua katikati ya ibada, mchungaji ataita Junior au Ezra. Kipaza sauti
kikikwaruza tu, kila mtu anawatafuta nyinyi! Sasa leo mhamie kule kwenye madarasa
ya watoto, wewe na Ezra! Maana najua na yeye Ezra ibada haiendi bila kuwa
amekaa na wewe. Mtajaa nyinyi wawili kwenye darasa moja.”
“Itakuwa usumbufu
usio kifani. Kila mtu atakuwa anakuja kuwaita. Mwishoe na mama naye atakuja
mwenyewe. Jelini atafuata. Watoto watabaki wakitushangaa sisi. Itakuwa ni
vurugu ibada nzima!” “Nitahakikisha kila kitu kinakaa sawa ndio nakuja.”
“Saa ngapi na wewe
unakikao sasahivi, kisha unaongoza ibada nzima ya kusifu na kuabudu?” “Mbona
kama hunitaki kwenye huduma yenu!? Inakua kama unanitafutia sababu tu!” “Mimi
nakukumbusha majukumu yako hapa kanisani, Junior. Nilishatamani sana kukuona
ukihudumu na mimi. Lakini nikagundua nafasi yako hapa kanisani si moja, na
unahitajika sana.”
“Ili kila ibada
kuisha hapa kwa utulivu, ni lazima wewe na Ezra muwepo. Haya
ninayokuuliza, mwenzio nilishayafikiria hata miezi sita kabla ya leo.
Nikafikiria labda ufanye hili na lile ndio ungeweza hata kufika kule kwenye
madarasa ya watoto, nikaishia kujua kutofika kwako kule si kwa kupenda. Mmebanwa
sana. Sasa ukiweza, karibu. Nitafurahi kwa mara ya kwanza na mimi kupata
bahati ya kuhudumu na wewe.” Alipoiweka hivyo, akamtuliza. Akapoa
kabisa. Ndipo wakaweza kuagana.
Uchumba Si Ndoa.
Hope alipofika tu
kanisani, mchungaji akaomba afike ofisini kwake. Ukweli alikuwa amependeza tu.
Akakuta wote wakimsubiria. Ezra, Junior, mama mchungaji na mchungaji mwenyewe.
Kidogo akaingiwa na hofu, wasijue hofu yake ipo kwengine kabisa. Junior kubadili
mawazo. Mchungaji akamtaka akae.
“Mbona mnanitia
wasiwasi, kwema!?” “Hakuna tatizo Hope, binti yangu. Tulitaka tu tuwekane
sawa.” Akatulia akisikiliza. “Jana ulikuwa na kikao na Junior. Nimesikia upande
wake, ninataka kukusikia na wewe juu ya makubaliano yenu. Na kama umeridhia.
Una amani na makubaliano yenu au la?” Akaanza Hope.
“Makubaliano
ambayo Junior mwenyewe alikubali ni kwamba, pale alipoingia mkataba na
kunilipia kuishi, hatanifukuza. Ataniacha nikae pale. Ataniachia
gari. Tena kwa makubaliano ya kunipa kabisa funguo za gari na kadi
yake. Yeye mwenyewe Junior, kwa kukubali kwake yeye mwenyewe. Labda kama
anataka kunibadilikia. Lakini alisema yupo tayari hata kusaini kihalali kuwa
gari amenipa mimi.” Akawa ameshapaniki tayari.
“Sasa haya mambo ya kurudi
kinyumenyume na Ester kunitafuta eti kusema akili ya Junior sio yake,
kwangu ni usaliti. Tena usaliti mkubwa sana. Maana wakati yeye
Junior anaahidi kunipa lile gari na kuniacha niishi pale, hakuonekana na tatizo
lolote la akili.” Wote hoi! Mpaka mchungaji akabaki amepigwa na butwaa. Anachozungumzia
Hope sio kabisa walichofikiria angejibu. Wakabaki wote wamemkodolea macho.
Yeye Hope akaendelea.
Tena akisikika kabisa na jazba. “Tena yeye mwenyewe Junior. Wala si
mimi. Yeye mwenyewe, alisema hana shida ya kufanya kazi na mimi hapa
kanisani. Nirudi kwenye uongozi kwa sababu nawezea madaraka yangu. Na akasema
atazungumza na wewe mchungaji, pia niwe nalipwa. Kwa maneno yake mwenyewe,
alisema na mimi nastahili kulipwa kama wengine. Sasa hayo anayoanzisha
Ester akisema kaka yake hana akili vizuri au sio yeye, mimi hapo ndio
naona si sawa. Inakua kama kugeukana. Na si sawa. Mimi nimetumika
kwa uaminifu sana hapa….” “Hope! Hope!” Mchungaji akamuwahi.
“Tafadhali tulia, binti
yangu. Hakuna lililobadilika na ndio maana tupo hapa kuwekana sawa.” “Samahani
baba J.” Mpaka mama mchungaji akaishiwa uvumilivu. “Naomba niingilie kidogo.” Akaendelea
akimtizama Hope kwa mshangao mkubwa.
“Hope! Hivi unajua
kama uchumba wenu umevunjika! Na ndilo hilo mchungaji alikuwa akitaka…” “Najua.
Na Junior mbona amenieleza vizuri tu. Na mimi nakubaliana naye na naona yupo
sahihi. Sisi tunaweza kutumika pomoja lakini si kwenye maswala ya
familia. Yeye anamisimamo yake ya maisha ambayo kwakweli imeshindwa
kuendana na yangu na hapo ndipo tulipopishana. Lakini sio eti ni
kosa langu ndio ninyimwe haki yangu! Hapo mtakua mnanionea kwakweli na si sawa.”
“Maana kwa mtu yeyote
anayefuata haki bila upendeleo, akipima atagundua ni kama tumepunguziana
adha ya baadaye. Zaidi kwangu. Ukweli kwangu ingeniwia vigumu hapo baadaye, na
ingekuwa kama uonezi. Maana ukifikiria ni kama ningeingia kwenye ndoa
mbili kwa wakati mmoja! Hapa kanisani inaonekana nimeolewa na Junior, kumbe
kuna Ezra, halafu atakayekuwa mke wa Ezra! Hapo bado watoto watakao kuja kuzaa
huyo Ezra na mkewe. Pia eti waje kuwa jukumu letu!” Akashangaa kabisa Hope,
mbele ya wakweze na Ezra mwenyewe.
“Mwanzoni niligundua kajiudhaifu
kwa Junior. Nikadhani ni mzito kwenye kuamua mambo. Maana mkiwa kwenye mipango
ya muhimu kabisa, jibu analotakiwa kutoa hapohapo, anakwambia eti
anataka apate muda wa kufikiria. Nikaja kumgundua kumbe ni mpaka akamuulize
na Ezra! Yaani hakuna maamuzi ya kama familia! Lazima maamuzi yetu sisi wawili,
eti na Ezra naye ayapitishe!”
“Ikaja kuwa eti mpaka
na mwanamke wa Ezra hivyohivyo, aje aafiki maamuzi yetu sisi wawili!
Ikitokea Ezra hajakubaliana na maamuzi yangu na Junior, eti hapo kuna tatizo!
Kufanya chakula cha pamoja nyumbani kwa Junior eti pia, ni mpaka Ezra na
mwanamke wake wakubaliane na wazo langu!”
“Halafu eti mimi
natakiwa pia kumpenda na kumnyenyekea mpaka mwanamke wa Ezra
ambaye kwanza hatuendani. Jelini ni wale wasichana…” “Hapa
hatumzungumzii Jelini. Tafadhali, kwa upande wake naomba ishia hapohapo.
Zungumza juu yangu utakavyo. Lakini kumtaja Jelini, kwa namna yeyote ile, hapa,
ni kuniingilia vibaya sana, na sitakuruhusu.” Ezra akawa mkali
kabisa.
“Lakini yeye ndio
chanzo cha matatizo yote.” “Hapana Hope. Kwa jinsi nilivyakusikia hapa
leo, sidhani kama Jelini aliyekuja hivi karibuni ndio chanzo cha
kuvunjika kwa uchumba wenu.” Mama mchungaji akaingilia.
“Sio kwamba namlaumu
yeye!” Akajirudi kidogo. “Na pia nilikuwa nikimwambia..” Akasita kumtaja huyo
aliyekuwa akimwambia. Ila akaendelea. “Uchumba sio ndoa. Ni kipindi cha
kuchunguzana kabla ya ndoa. Junior mwenyewe, kwa kinywa chake, amesema hajaona
tatizo kwangu, ila tu mimi si mkewe. Akataja sifa zangu nzuri tu, na ni
kweli.” Hope akajikubali.
“Sasa kwa jinsi
nilivyo, na yeye alivyo pamoja na Ezra na zaidi mwanamke wake, ukweli hatuendani.
Ingekuwa ni shida tu. Hata hivyo na mimi nisingeweza kuwa kwenye ndoa ya
watu wanne. Nataka mtu ambaye tunapanga mambo yetu ya kifamilia, tunakubaliana
sisi wawili. Basi. Sio kila uamuzi eti lazima upitie kwa rafiki! Sasa hapo
kutakuwa na ndoa kweli!” “Ili tusikupotezee muda mwingi Hope, binti yangu, kama
nimekuelewa vizuri, ni kwamba mpo kwenye makubaliano ya kusitisha uchumba?”
Mchungaji akataka ukiri, wafupishe kikao kilichoonyesha dalili zote za kuvuta sana.
“Makubaliano yalikuwa
leo anikabidhi ….” “Usiwe na wasiwasi juu ya mali zake. Hizo..” “Lakini
ukiangalia kwa makini si mali zake peke yake, mchungaji.” Hapo akaongea
kwa heshima kidogo.
“Gari na mimi
nilichangia, hata kama ni kidogo, lakini..,” “Hope! Hope! Ninachotaka
kukuhakikishia ni kwamba, yote aliyokuahidi kukupa, utapewa. Kasoro swala
la uongozi hapa kanisani, juu ya ile nafasi uliyoachia ndio itabidi nipate muda
wa kuitathimini kwa upya na kumuomba Mungu zaidi. Maana kwa sasa
ni kama kuna utaratibu unaofanya kazi vizuri tu.” “Kwamba tayari mmeshamtafuta
mtu mwingine!?” “Juu ya hilo naomba kukutoa wasiwasi. Hilo niachie mimi.”
“Maana alisema pia nikirudi kwenye uongozi kwa sababu natumika sana,
tena vizuri, pia nitalipwa.” Ikawa mpaka imekera. Ila mchungaji
akajikaza.
“Tutawekana sawa,
tutakapofikia hapo. Tafadhali turudi kwenye ajenda ya UCHUMBA. Je, mmeafikiana
kusitisha uchumba? Kwamba na wewe umeafikiana na hilo bila manung’uniko?”
“Uchumba sio ndoa
mchungaji, kusema ilitakiwa iwe ya milele. Sisi tumechunguzana, ukweli hatuendani.
Na ndio maana tumeachana kwa amani kabisa. Na makubaliano yetu yapo palepale.
Hatuachani kwa ugomvi eti kufilisiana. Hapana. Au Junior amebadili
mawazo? Maana namuona yupo kimya tu muda wote!” “Hapana. Nilitaka kuwapa nafasi
na wao wakusikie vizuri na kukuelewa kwa uhalisia wako.”
Junior akaongea kama kuwafikishia ujumbe wazazi, yeye Hope asielewe anasemwa
yeye.
“Mimi naona
hatutafika popote mpaka Junior amkabidhi hilo gari. Haya Junior, mkabidhishe
ndipo mchungaji amuulize maswali yake, tutoke hapa. Ibada ikaanze.” Mama
mchungaji akaingilia akisikika amefika mwisho kabisa.
Junior akamkabidhi
bahasha kubwa. Akapokea. Akakuta kadi ya gari na karatasi zingine. “Mbona
hakuna funguo?! Maana funguo ya pil..” “Hope, kila kitu kipo ndani ya hiyo
bahasha. Tafadhali angalia kwa makini.” Akamwaga kila kitu hapo mezani kwa
mchungaji kama kuhakikishia wote maana alishapaniki tena. Funguo ilipodondoka
mezani wakamuona anatabasamu.
“Huyu Ester alitaka kunichanganya
bila sababu! Junior ni mtu wa kusimamia maneno yake tokea mwanzo. Akisema
atafanya jambo, anafanya. Na ndizo akili zake tokea namfahamu mimi. Hayo
mengine ni uzushi tu.” Wote hoi. “Sasa hapa tumehitimisha kwa amani. Hatudaiani
chochote. Na pete yako nilishakurudishia. Hunidai Junior.” Junior kimya. Wote
wakimtizama. Ni kweli alionekana kutulia kabisa.
“Kwa hiyo leo tutatangaza
kusitisha uchumba wenu, ili kama kuna mtu alikuwa akitaka kukuchumbia
akazuiliwa na Junior, basi ajue ni wakati wake.” Hope akacheka taratibu.
Mchungaji naye akacheka. “Au tayari Hope binti yangu?” Akacheka kwa wazi
kabisa. Tena akiwa amebadilika, mwema kama siye yeye!
“Habari njema
zinakuja, mchungaji. Na amekubali kuhamia hapahapa kanisani. Nimemwambia Junior
hana shida ya kuhudumu na mimi. Maana na yeye ni mtumishi. Acha tujipange,
nitamkaribisha.” Mama J, hoi! Akataka kuuliza swali, mumewe akajua swali lake
na akajua ameshakasirika.
“Mengine acha
tuendelee nayo tu baadaye mama J. Acha tuombe na kutamka baraka juu yao, tuwahi
ibadani.” Hakusubiri jibu. Maana hao watatu walibaki wamemkodolea macho kama
wanao muuliza ‘umeona sasa?’. Hope alishafunga macho. Bahasha yake kwapani
pembeni ya pochi yake. Mchungaji akawatizama vile wanavyomtizama, akafunga
macho na kupiga sala fupi. Hope akashukuru na kuondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Naona hili limekaa
sawa.” Mchungaji akawaambia maana walibaki wakimtizama. “Naamini hata kwa
Emelda huko kila kitu kitakuwa kilienda sawa.” Ndio akawa amemkumbusha
Junior. Akasimama kama mchale. “Nahamia kwenye huduma ya watoto.” Wazazi
wakapigwa na butwaa. Ezra naye akasimama. “Hiyo ni vurugu unayotaka
kuianzisha Junior. Na hapana.” “Kwa nini?!” Akamuuliza Ezra kwa ukali
kidogo.
“Wewe unajua ni kwa nini, Junior. Tafadhali twende
jukwaani. Noah ameshatuma ujumbe, anataka tukawekane sawa na waimbaji wengine,
tuanze ibada. Huwezi kurudi kinyumenyume sasahivi. Utamchanganya Noah ambaye ni
kiongozi wa sifa. Na najua kabisa sio lengo lako.” Wazazi kimywa
wakiwasikiliza.
“Tafadhali twende.”
“Sasa hata kama ni kwenda kwa watoto si ni baada ya ibada ya kusifu na kuabudu!
Sijasema kama nakwenda sasahivi! Kwanza watoto wenyewe watakuwa huku kwenye
ibada ya sifa. Wakiwa wanaondoka na mimi…” “Unarudi kwenye majukumu ya hapa
kanisani. Wewe unajua ibada hapa haziendi bila sisi. Hata kipaza
sauti kikisumbua ni sisi. Sasa unataka kwenda kumlinda Emelda
kule huku ibada ikwame?” Akawa ameongea kama Emelda. Hapo akapoa kidogo.
“Twende Junior,
tunazidi kumchelewesha Noah.” Ezra akatoka, akamfuata nyuma. “Na lengo si kuwa
nakwenda kumlinda Emelda! Nimejihisi nimekuwa kwenye kila huduma, kasoro
huko kwa watoto. Nataka kushiriki, na pia kumtia moyo.” Wakawasikia wakiongea
wakiondoka. “Lakini sio sasa na sio kwa gafla, Junior! Na wewe unajua.”
Wakabaki wakisikiliza mpaka wakapotea. Uzuri wenyewe wanawezana.
Angeingilia mchungaji hapo, Ezra angemtetea Junior, siku hiyo kweli wote
wangeishia hukudumu kwa watoto. Utabiri wa Emelda ungetimia.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Ndio maana wanawake
wanawaacha hawa!” Mama yao akaongea na kucheka kwa pamoja kama wanao
wasikitikia. “Ila katika hili, nilazima kumuomba radhi Junior. Huyu
binti angemsumbua sana kwenye ndoa.” Mchungaji akazungumza akimfikiria Hope.
“Hana habari na mwenzie kabisa, wala hajali swala la uchumba, yeye ni mali tu
jamani!” “Lakini mama, acha hivi ilivyoisha kwa amani.” “Halafu na huyo mchumba
atakuwa alimpata lini!?” “Nilitaka kujiuliza hilo lakini nikakumbuka na yeye
Junior mbona ana Emelda tayari!” Wakajisuta na kunyamaza.
~~~~~~~~~~~~~~~
Je, kwa upande wa Edwin yeye alichukuliaje taarifa za 'Hapana' akiwa ameshawekeza sana kwa Emelda?
Ester?
Jelini amechumbiwa kihalali, Colins?
Inaendelea.
0 Comments:
Post a Comment