Love At First Sight - Sehemu ya 62.
“Ila ujue hii ni
hongo.” Raza akakunja uso akigeuka vizuri. “Hongo ya nini tena?”
“Nakuomba msamaha mke wangu. Najua sikulichukulia vizuri swala la kuzaa
na Mina.” Raza hakutegemea! Alilia Raza. Alilia sana kwa uchungu.
“Nimekukosea
Raza. Nikijifikiria, nahisi kama tokea mwanzo ninge handle hili swala la
PJ vizuri, usingefika ulipofika. Na mimi najua nimechangia.
Hilo ni la pili, ila kubwa ambalo si sawa, nikuzaa nje ya ndoa. Si sawa, naomba
unisamehe.” Hizo ni habari ambazo hakuwa hata na wazo kama atakuja
kuzisikia!
Pius anakiri
kosa la kuzaa nje! Tena mtoto wa KIUME! Akambembeleza mkewe mpaka akatulia.
Huku akimfuta machozi kabisa. “Lakini Naomba uelewe Raza. PJ ni mtoto wangu
kama Polla. Hilo siwezi kukwepa tena.” “Naelewa Pius.” “Basi naomba tujipange kwa pamoja. Taratibu, hatua kwa hatua, naamini
tutafika tu. Si safari hii unaniombea?” “Sana Pius. Na nimetubu hata swala la
mauaji.” Pius akatulia.
“Nisamehe Pius. Na natafuta jinsi
ya kumuomba Mina msamaha. Watu wananikimbia Pius!” “Wape muda Raza. Hawa watu umewatisha sana. Tafadhali wape muda.
Ila nakuahidi hutakuwa tena peke yako. Tutatembea wote. Mimi na wewe, kuonyesha
na sisi tumebadilika. Sisi na watoto wetu. Turudishe heshima
tuliyopoteza.” “Wanamkimbia Polla.” Akamsimulia yote
jinsi Paulina alivyomtenda binti yao, na yeye akajidai kama ndio anasikia hapo.
Akatulia akimsikiliza mkewe akisemelezea ndugu zake. Akalia wee, Pius
akimbembeleza.
“Watu wanashindwa kunisamehe Pius!” “Ni muda tu. Tulia kabisa. Waache. Inatosha. Ushaomba msamaha
kwa kila mtu uliyeweza kumfikia, wamesikia kama umeomba msamaha. Inatosha.
Tulia kabisa.” Hilo likamtuliza, alijawa furaha huyo! Machozi mengi
yalichanganyika na ya furaha. Amempata Pius bila MGANGA! Japokuwa ameomba muda
mrefu, lakini hatimaye amejibiwa.
Wakatulia kila
mtu akiwaza lake. Mwishoe Raza akagutuka. “Kesho ijumaa, siku ya kazi. Acha
nikuache na wewe upumzike. Ila ujue nimefurahi sana.” “Huna hata hamu na
mimi Raza!?” “Ungejua, ungenihurumia, ila hofu. Sijui kama utanipokea
tena baada ya kukuumiza!” “Si na wewe umenisamehe?” Raza akatulia.
Juu ya
Ayvin.
“Raza?” “Ndio
inakuaje Pius? Una mtoto na Mina. Mtoto WAKIUME!” “Wewe hiyo jinsia isikutishe. Huyo mtoto atafundishwa kukua na
kusaka pesa yeye mwenyewe sio akue akichungulia urithi wa dada zake!” Hapo
akampata Raza. “Mimi mwenyewe sijarithi mpaka leo na ni mtoto wa kiume wa
kwanza kwa mzee Ruhinda. Kama ningekuwa nikisubiria mali za mzee, sisi sote na
watoto wetu tusingekuwa na maisha haya. Maana nisingejibidisha,
ningebaki tunamsubiria mzee afe ndio turithi. Kwanza mzee mwenyewe hana hata
mpango wa kufa! Sasa kuja kupata mali zake si leo, mama.” “Lakini kweli!”
“Wewe unajipa pressure
ya bure! Sasahivi tujipange mimi na wewe jinsi ya kulea hao watoto watatu.” “Na mimi
Pius?” “Kumbe na nani? Tushaharibu.
Tushapoteza heshima huko nje. Tuanze kujipanga upya. Na najua Raza.
Najua mke wangu kuwa nimekudhalilisha sana. Lakini si tumekubali
kuanza?” “Ikiwa hivyo sawa Pius. Hapo umenituliza. Nilijua unanidharau
mimi kwa sababu nimezaa watoto wa kike tupu!”
“Unawezaje
kufikiria hivyo Raza!? Napenda binti zangu na najivunia haswa. Sina mtoto wa
bahati mbaya kati yao na siwaonei aibu hata kidogo. Ni wanangu! Wewe unafikiri
mapenzi ya Poliny yatachukuliwa na PJ?” “Hata sijui Pius! Nilibaki
nikidhania tu. Wewe hukuonyesha kama ni kosa mpaka leo! Angalau leo
umelizungumzia, umenituliza. Na nakushukuru.”
“Huyo PJ
anamajukumu huyo! Ungemuhurumia. Anatakiwa akue huku macho yapo kwa dada
zake. Asiwahi kutulia kama Polla wangu yupo matatizoni. Atakuwa
akifundishwa mafanikio yake ni pale dada zake wanapofanikiwa wala
sio kuwa mrithi wangu! Kwanza kwetu hatuna hata huo utaratibu wa kurishana!
Hapa nilipo hata sijui kama nina urithi kutoka kwa baba! Kwanza sitaki. Hata
hivyo mzee Ruhinda atanipa nini ambacho mimi sina, tena kwa kiwango cha juu
dhidi yake!? Halafu hata mimi nikirithi mali za mzee, yeye mama atakuwa wapi?”
Raza akatulia akifikiria.
“Halafu Raza,
hakuna anaye kudharau nyumbani kwetu eti sababu umezaa watoto wa kike!”
“Unajuaje?” “Kwa sababu mimi mwenyewe sikuwahi kuhisi kudharauliwa eti
kwa sababu nina mabinti tu, sina wakiume! Sijawahi poteza heshima kwa wazazi
kabla na baada ya Ayan. Alizaliwa wa kwanza wa kiume, tukampokea kama
mtoto wetu. Furaha iliongezeka kwa sababu alikuwa mjukuu wa kwanza wa kiume,
mtoto ambaye jinsia hiyo hatukuwa nayo, na tukajua jina letu halitapotea
hata kama kina Poliny watakuja kuolewa na kuchukua majina la waume zao, basi
Ayan atabakia kubeba jina letu, basi. Lakini si kwa kuwa yeye ni bora
kuliko wengine!” Akamuona ametulia akiwaza,
“Umeelewa na umenisamehe?”
Akamwangalia mumewe maana alishapotea hapo. “Juu ya kuzaa nje ya ndoa.” Pius
akaweka sawa. “Kwani mlikuwa na mahusiano ya kimapenzi na Mina?” Angalau
siku hiyo akapata ujasiri wa kumuuliza mumewe. “Nakwambia ukweli
na naomba uniamini.” Akamsimulia ile siku ilivyokuwa, tena kwa tahadhari sana.
“Kama unakumbuka
Mina alikuja pale kwa Paulina siku ile akitapika, hakuwa akijua kama ni mjamzito.
Unakumbuka?” “Ndio hapo mimi nilikuja changanyikiwa Pius!” “Kwa hakika yeye
hakuwa na hatia kabisa. Hakuwa akijua kabisa kwa kuwa ni kweli nilikuwa naye
karibu. Mina hakuwa na mwanaume mwingine. Aliamua kutulia na Andy. Ila
mimi nilijua kabisa, ila nilikuwa kwenye mshituko na sikuwa nikijua
nitafanya nini ndio maana nilinyamaza na kumuchia yeye abebe lawama
zote. Na hilo nilikuja kumuomba msamaha.”
“Kitu ambacho
unaweza usiamini Raza, Mina anakuheshimu sana. SANA. Na japokuwa ulikuwa
ukimtangaza vibaya kwa watu, lakini yeye alibaki akikutangaza vizuri hata siku
anarudi na watoto, mbele ya wazazi. Mina alibaki akikutambua kwa heshima
sana. Anavyosema ni kama wewe ndiye mwanzoni kabisa uliyempokea na kumkaribisha
kwenye familia, mbali ya Andy. Na anasema aliondoka kwa wazazi na kutoroka kwa
heshima yako WEWE, ili isiwe ni kama yeye ndiye amekutoa kwenye familia
wakati ulimkaribisha kwa upendo.” Akamsimulia kwa kifupi, akabaki ameinama
kwa majuto.
“Mina si mpinzani
wako kwangu na kwa wazazi.” “Una uhakika? Maana mwenzangu amekuzalia
mtoto wa kiume tuliyekuwa tukimtafuta, ikashindikana.” “Haimaanishi
yeye ni bora kuliko wewe ambaye ni mke wangu. Hapa tupo mimi na
wewe. Na mimi na wewe ndio katika shida, na raha mpaka kifo. Wewe ni
wangu Raza.” Hakika Raza hakuamini, akatulia akitafakari na kutamani hayo Pius
angemwambia muda mrefu sana wala hata asingehangaika kwa mateso yote
hayo aliyopitia. Kwa hakika alimtuliza nafsi. Akabaki mawazoni. Pius akabaki
akimwangalia.
Akamuona anavuta
pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu kama ambaye anayejaribu kutulia. Kisha
akamwangalia mumewe. “Nimeshindwa kumuomba msamaha kabisa.
Nashindwa hata pakuanzia!” “Kwa sababu mimi ndio nahusika.” Raza
akamwangalia kama asiyeelewa.
“Mimi nitamuomba
Mina msamaha kwa niaba yako. Kwanza. Kama njia ya kutengeneza mazingira mazuri
ya kukusikiliza wewe. Mimi ndio nilianza vibaya Raza. Ningeanza
vizuri na kukutuliza tokea mwanzo, nina uhakika usingepaniki na
kufanya yote hayo. Au si kweli?” “Niliingiwa na roho chafu Pius!
Kuna mambo nilikuwa nafanya, nikifikiria sasahivi mpaka najishangaa na naona
mama alikuwa sahihi. Alishanionya mno, na kunisihi niache lakini nilikuwa sina
jinsi nyingine ninayofikiria isipokuwa ushirikina. Na wala
usifikiri vilikuwa vinanipa furaha na amani!”
Pius akabaki
akimsikiliza. “Ni vurugu tupu. Havina raha! Mashariti mengi, ya wasiwasi!
Unaota mandoto mabaya, kila siku hulali vizuri. Bora sasahivi nikilala, nalala
hata sioti mandoto mabaya.” Akajifuta machozi na
kujaribu kutulia kisha akaendelea.
Juu ya
Familia.
“Nashukuru
kunisaidia kwa Mina. Na naomba nikiwa namuomba msamaha, na wewe uwepo Pius.
Watu wananiogopa!” “Sawa. Na acha
kuwafuata.” Raza akawa hajaelewa.
“Usilie.
Inatosha Raza. Nyamaza.” Akamsaidia kumfuta mkewe machozi. “Ila
sijaelewa! Kwamba nisiwafuate tena!?” “Wewe si
umeshawaomba msamaha?” “Wote, kasoro Mina tu. Mama yangu amenisamehe kabisa. Wala hana
neno, tena naona kama ameongeza ukaribu. Angalau anaweza piga hata kuulizia
maswala ya watoto na kunikumbusha niwe namwambia maswala ya Polla mapema, ili
na yeye awe anahudhuria kama bibi Ruhinda. Ila kwenu! Mmmh! Nimepoteza heshima
kabisa.”
“Basi inatosha.
Waache kabisa. Watarudi tu wenyewe.” “Kwa namna gani!?” “Wewe tulia kabisa. Na kuanzia sasa acha kulia. Tulia. Angalia ya hapa
nyumbani na ya wanao kuzunguka. Basi. Watarudi wenyewe. Mimi nitashugulika
nao. Na Polla akikulalamikia juu ya mtoto wa Paulina, tafuta hekima ya kumtuliza.
Atakuwa sawa tu.” Hapo akazidi kumtuliza zaidi.
Akamfuta machozi
kabisa kitu ambacho kwa wanandoa hao hakikuwa cha kawaida! Kwanza siku
hiyo ni kama Pius alitoa muda mwingi sana kwake kitu kilichokuwa kikimshangaza.
Alionekana kama hana haraka kabisa na kesho yake ilikuwa ni siku ya kazi!
Alimuonyesha yupo kumsikiliza tena bila haraka!
Juu Ya
Chezo.
“Nashukuru Pius.”
Kisha akacheka. “Nini?” “Umekuwa mwema kuliko nilivyokuwa nikikuloga!”
Mpaka Pius akacheka. “Kweli Pius! Sasahivi mpaka nasikia raha kuwa na wewe! Ulikuwa
unakuwa mkali kwangu, hunisikilizi kabisa kama mwanao Poliny. Nikawa namwambia
Katibu, mbona dawa unazonipa hazisaidii. Pius mkali sana kwangu.” “Usilie sasa. Si umesema sasahivi nakusikiliza?” Akamfuta tena machozi.
“Ila nilikuwa
natamani uwe na mimi kama hivi Pius. Ujue hata Chezo si kwamba tulikuwa
tukikutana tu kwa mapenzi!” Pius akaanza kubadilika. “Nakwambia ukweli Pius. Si
mapenzi. Chezo anauwezo wa kunisikiliza mno. Anaweza akakaa na mimi
zaidi ya lisaa, ananisikiliza tu nikilalamika. Ukumbuke
nilishakuwa fedheha pale ofisini. Wewe umezaa na Mina, na unampigania
mpaka mitandaoni. Watu wakawa wananicheka. Siwezi zungumza na watu
ofisini. Mashoga wakawa wananisanifu. Ndugu nao wakawa wananicheka. Nimebadili
dini kwa mtu ambaye hanitaki hata kwa tunguli.” Hapo akazidi kulia kwa uchungu. “Pole na samahani Raza.” Akazidi
kumbembeleza.
“Ndio nikawa nakaa na Chezo nakuwa
nazungumza naye. Ananitia moyo na kuniambia nitulie tu na watoto. Maadamu bado
hujanipa talaka, nitulie. Ndio nikamwambia mimi kwetu ni kama hata kaka zangu walinisusa,
hawanitafuti kwa la kheri wala la shari sababu nilikana imani ya wazazi.
Nikamwambia ukinifukuza leo, sina pakwenda. Ndio akanisaidia kutafuta
kiwanja.” Pius hakutegemea.
“Akanibembelezea
bei. Nikalipia na kunisaidia mpaka nikaweza pata hati yake. Hivi nilishaanza
kujenga, yeye ndio ananisaidia kusimamia na mafundi. Sema mkewe mkali sana. Sasa
wakati mwingine akiwa amegombana na mkewe ndio akawa anakwenda kukaa
huko site, na ndio ikawa msaada wangu maana anakuwa akiwasimamia mafundi.
Ila pesa ni zangu. Mshahara wote nikawa napeleka huko, ananisaidia. Na
nimwaminifu kwakweli. Hakuwa akiniibia. Halafu ishi yangu ndio ikawa wewe.”
“Umefikia wapi
ujenzi?” “Nakaribia kwenye paa.” “Raza!” “Sasa wewe unafikiri pesa zote
ninazolipwa mshahara napeleka wapi?” “Hata sijui! Maana unakazi ya kuomba pesa
mchana na usiku.” Raza akacheka sana.
“Najenga
mwenzio.” “Hapo nimekusifu. Ila Chezo iwe mwisho Raza. Sitaki.”
“Nishamwambia.” “Hata kukusaidia ujenzi, hapana.” “Mimi sina muda Pius. Yeye..”
Akasimama kabisa. “Hapana Raza. Hapana.” “Ni kwenye ujenzi tu! Hamna
mambo mengine. Kwanza nishamwambia nimebadili maisha yangu. Siku hizi nipo
karibu na Mungu. Sitaki tena kumkosea Mungu. Akaelewa kabisa na anaheshimu
hilo. Ila kwenye swala la ujenzi ndio atabaki akinisaidia, lasivyo mambo
ya hapa nyumbani nitapwaya, Pius! Kazini na kusimamia ujenzi! Hapa sitaonekana.”
“Raza, HAPANA.” Hapo akawa ashabadilika.
“Umenisikia
Raza?” “Basi nitamwambia asirudi tena kule. Nikuonyeshe hati yangu?” Akamfanyia
kusudi atulie. Akabaki amesimama. Raza na yeye akanyanyuka kuelekea upande
wa closet ambako kuna nguo zao na viatu. Akaenda upande wake ambako kuna
safe yake ndogo kama Pius tu, lakini safe ya Pius ilikuwa kubwa zaidi. Akafungua
na kuitoa. Aliporudi, akamkuta amerudi kukaa kitandani. Akampa. Akaisoma.
Juu ya
Urithi.
“Hongera sana.
Ila ujue hapa ni kwako Raza.” “Ila kama mama yako alivyosema, nilikukuta
na mali zako Pius! Hii nyumba ilikuwa inakaribia kuisha.” “Hata kama. Hata kama
kuna kurithi, ni mpaka na wewe ufe. Hakuna wa kukutoa hapa. Hata
Poliny hapa si kwake. Huyo unayemuhofia, PJ, ndio kabisa. Mungu anipe tu uhai. Urithi
wake ni SHULE nitakayomsomesha. Basi. Sio mali. Nilichofanyiwa mimi na
wazazi wangu, ndicho na mimi nitamfanyia PJ.” Pius alishindwa kabisa kumuita
mtoto wake Ayvin kama wengine.
“Niliye na
wasiwasi naye mimi ni Polla. Huyo nahisi ndio mrithi aisee! Amegoma kukua!
Michezo mingi! Sio kama dada yake.” Raza alicheka sana. “Usimkatie tamaa!”
“Aisee siwezi. Polla! Ukimuhimiza shule, analia! Ukimuhusia mambo ya
shule inakua kama unamkera, na ni kama hana mpango kabisaa!” “Anasema wewe
mkali kwake.” “Sasa kwa wewe mpole kwake mbona sasa hafaulu?” “Ila hafeli.”
Raza akaendelea kutetea.
“Lakini sio kwa
kiwango kizuri.” “Tatizo wewe unataka awe kama Poliny, Pius! Awe anapata zote
100. Nilishakwambia hawa watoto hawalingani. Poliny amechukua kichwa
chako.” “Siamini kabisa hilo. Huyo mwanao michezo imemzidi aisee! Akili ipo
kwenye games zake tu.” “Atakua tu. Tumpe muda.” Wakatulia.
Bado Chezo.
“Ila swala la
Chezo naomba tuhitimishe Raza.” “Sawa. Ila ujue na mafundi ni wake.”
“Mbona inakua kama hiyo nyumba mnajenga naye!?” “Ni pesa yangu, Pius.
Kwanza sio kwamba hata anahela ya kuwekeza hapo. Usiponisaidia wewe pesa ujue ndio nimekwama.” “Lazima ajue hatutaki
tena msaada wake. Na asikutafute TENA. Mimi SITAKI. Tutatafuta
mafundi wengine.” “Basi nikitoka kazini kesho nitakwenda tukakabidhiane
kabisa.” Hapo tena ikawa shida. Kitu kisicho cha kawaida gafla Pius akawa na wivu
na mkewe.
“Mimi hivyo pia sitaki.”
“Sasa tutafanyaje Pius!?” “Kwamba yeye ndio anajua kila kitu
kinachoendelea huko kama yake?!” “Ndiyo.” Akazidi kumvuruga. “Kwamba nyinyi
mlikuwa mpo kama mke na mume kabisa!?” “Umekasirika Pius. Na unaanza kutafuta
kujiudhi zaidi. Tafadhali nipe muda nihitimishe vizuri, nisipoteze
mahesabu, na pia nijue walipofikia mafundi. Naweza zungumza nao, nikaendelea
nao mimi.” “SITAKI. Simtaki yeye wala mafundi wake. SITAKI Raza.”
“Sawa.” “Sawa nini, sasa?” “Sichukui hao mafundi wake.” “Na kukabidhiana?” Raza
akakwama.
“Raza?” “Hata
sijui Pius! Basi nishauri wewe.” “Basi mwambie na mimi nitakuwepo.”
“Hawezi kukubali. Chezo anakuogopa sana.” Pius akakunja sura. “Kwa nini?
Akamuona anasita. “We Raza?” “Anahisi unaweza msababisha akafukuzwa
kazi.” Pius akabaki akimwangalia kama ambaye hajaelewa.
“Kwani wewe umemfahamu
Chezo kwa kiasi gani?” Kidogo Pius akatulia akifikiria. Hakutafuta kumfahamu
kwa undani huyo Chezo, ila kuishia hivyohivyo tu kama mwizi wa mkewe.
Akabaki akijaribu kutafakari. Kuna kina Chezo wangapi anao wafahamu! Kwa
ufikiriaji ule, Raza akashukuru Mungu kuwa hamfahamu Chezo kwa undani. Akaona
apotezee.
“Haina maana. Mimi nitamwambia aache
kwenda pale.” “Anafanya kazi wapi?” Hilo ndilo alilokuwa akificha sana Raza na
kufurahia kuwa hamfahamu kwa undani. Sasa anaanza kuchokonoa tena! Raza hakuwa
tayari.
“Naomba hayo
tuyaache Pius. Huko tushatoka. Nitamwa..” “Kwa nini sasa unamficha?” Akauliza
kwa ukali. “Simfichi, ila naona haina maana.” “Kwangu inamaana. NATAKA kumjua.”
Raza akanyamaza.
“Hivi si unajua nikitaka
kumfahamu kwa undani, nitamfahamu tu?” “Naomba nisikilize kwanza Pius. Huyu mtu
anategemewa sana. Na si na familia yake tu, kwamba mke na watoto!
Hapana. Ni mpaka nyumbani kwao, wazazi wanamtegemea YEYE. Kazi aliyonayo
inategemewa karibu na ukoo mzima. Hapo alipo anasema ameipata hiyo kazi kama
muu..” “Raza?” Akawa ameshakasirika. Akamuita mkewe kwa ukali.
“Anafanya kazi
chini ya mzee Ruhinda.” Pius akakunja uso kwa mshangao uliojaa mshituko.
“Kwamba na yeye ni miongoni mwa board of directors?!” Raza akanyamaza.
“Raza?” “Yupo kwenye maswala ya usafirishaji.” Alishituka Pius akahisi
hajamsikia mkewe vizuri .
“Raza, unataka
kuniambia huyu mtu ni miongoni mwa MADEREVA wa mzee Ruhinda pale ofisini!?”
Raza akashindwa hata kujibu, akabaki kimya. “Yaani wewe ulikuwa na
mahusiano na dereva wa baba yangu mzazi!?” Kimya ila wazi alisharudiwa na ile
hofu ya zamani aliyoitoa mumewe. “Kweli Raza?!”
Akashindwa kujibu akitetemeka. Mumewe alimtizama kwa muda, na kutoka
hapo chumbani kabisa.
Raza naye
alipoona hivyo akavua mkufu aliomvalisha. Akaurudisha kwenye mkoba wake
akamuwekea pembeni ya mto, akatoka hapo kimyakimya kurudi chumba alichokuwa
akilala.
Upepo Wa Usaliti
Unaponong’ona Kwa Uchungu
Kamila ndiye
aliyeandika kurasa mpya moyoni kwa Pam, tena bila kutegemea. Kamila mnyenyekevu
mwenye sauti tulivu alipokuwa akiwapokea alipokuwa na Mill, siye aliyemsikia
akimjibu mlinzi wake kikatili juu yake.
Alikuwa kama
nyoka aliyejivua magamba na kujionyesha uhalisia wake kwa Pam. Akawa kama
chui aliyekuwa amevaa ngozi ya kondooo mbele ya Mill na Mike alipokuwepo Pam. Kamila
mnyenyekevu! Aliyejitoa kuwahudumia kuanzia chakula cha asubuhi
akitangaza wema wake waziwazi, alimbadilikia Pam na kushindwa hata kumkarimu
maji ya kunywa! Aliandika kitu kipya na kigeni kilichoshindwa kutoka
moyoni kwa Pam.
Lakini jumapili
hiyo akaamua kujikaza na kumfuata Mill huko kwa kina Komba. Walijiandaa kwa
ibada, wakatoka hapo wao watatu, Mill, Pam na Shema kwenda kumfuata mama Eric
na binti aliyekuja naye mjini kumsaidia kazi.
Alijitahidi kwa
mama yake apendeze. Na kweli uzuri ni asili yake mama Eric alikosa tu matunzo. Wakatoka
watano hao mpaka kanisani baada ya ibada wakaongozana mpaka kwa kina Komba,
mapigo ya moyo ya Pam yakienda visivyo, analazimishia tu safari. Kimya garini,
anayezungumza ni Shema, baba yake na bibi yake.
Walifika kwa
kina Komba wakakuta wametayarishiwa kwelikweli na wanasubiriwa kwa hamu, maana
walienda kupokelewa nje kwenye gari kabisa. Pam kimya akijiangalizia, ila
Kamila hakutoka. Akatulia kuangalia kinachoendelea.
Wakakaribishwa ndani
ila akagundua kuna kujiwinda kwingi zaidi kwa maneno. Akatulia, wakakaribishwa
vinywaji, ilikuwa juisi iliyotengenezwa nyumbani. Nzuri sana. Wakiwa wanaendelea
kunywa, akatokea Kamila. Kitu kikaruka moyoni kwa Pam, ila akatulia. Akasalimia
kwa kuanza kuwashika mikono. Alipofika kwa mama Eric akakaa kabisa pembeni
yake, maana mama Eric mchangamfu. Msambaa asiye hila. Akaanza kumsifia
na kutaka kumtambua zaidis. Ikabidi Kamila akae sasa ajitambulishe huku
akijaribu kutulia kwa hofu mbele ya Pam akijua Mill anamtizama kwa makini sana.
Mwishoe mama
Colins akasaidia. “Huyo naye ni bibi harusi mtarajiwa, mchumba wa Colins.
Tukimaliza harusi ya Mill, inakuja ya Colins.” Mama Eric hanaga mengi, moyo
wake umejaa amani. Akampongeza hapo akimshika kabisa mkono kwa shangwe huku
akimbariki.
Kabla hajamsogelea
Pam sasa, baada ya shamrashamra na maneno ya pongezi ya mama yake kwa Kamila,
Pam akasimama na kuomba alekezwe chooni. Maana yeye Pam ndiye aliyekuwa
akifuata. Ile Mill amesimama ili ampeleke chooni, Shema naye akasimama.
“Subiri hapo na
kina bibi, na babu narudi sasahivi, namuonyesha mama yako chooni.” “Mimi naenda
na mama yangu.” Shema akamsogelea mama yake karibu kama anayekimbia hapo
sebuleni baada ya kuja Kamila. “Sasa utaingia naye chooni bwana Shema!?” “Basi
mimi ndio namuonyesha chooni, napafahamu. Wewe ndio ukae hapa. Twende mama.”
Pam akaondoka na mwanae Mill akabaki amesimama katikati ya sebule, mama Eric
hawaelewi. Akarudi kukaa, Kamila akapoa.
~~~~~~~~~~~~~~~~
“Vipi na wewe?”
Kamila akamtizama Mill kinyonge akitafuta pakukaa maana alikuwa akimsogelea Pam
na ndio Pam akanyanyuka. “Nifanyaje Mill?” “Huna chakufanya ila kumpa nafasi na
hili nilikwambia Kamila. Tafadhali tulia.” Mill akaongea kwa sauti ya chini
kama anaye mnong’oneza. “Hata hivyo kufika mpaka hapa, nahesabu ni hatua kubwa
sana. Na naona mama anafanya vizuri. Wewe tulia. Mwache kabisa.” Mill
akasisitiza kwa sauti ya chini, wengine wote kimya.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Pam akarudi na
mwanae akionekana ametulia tu, ila sebule nzima ilikuwa kimya. Akarudi kukaa
alipokuwa amekaa, na mwanae akamsogelea kukaa naye. “Ona saa yangu amenipa
anko.” Akamsogezea mkono mama yake, Pam akacheka akiiangalia. “Umemwambia anko asante
sanaaa?” “Sijasema sanaaaa,
ila nimesema asante. Maana hii saa nikitembea inahesabu steps zangu. Nikinywa
maji inakuwa inaweka kumbukumbu, na mapigo yangu ya moyo. Inakuwa inatunza
rekodi zangu vizuri. Nikikaa muda mrefu itaniambia nisimame nisikae sana niwe active.”
“Naona hapo haitakuwa na shida. Maana wewe huwezi kutulia.” Kila mtu akacheka.
“Mbona hapa
nimetulia!” “Ishakukumbusha kuwa active?” Mama yake akamuuliza. “Bado.” “Basi
haitakaa ikakukumbusha.” Akaanza kucheka mwenyewe kama wengine. “Mimi natulia
mama!” “Labda ukiwa unalala.” “Hapo inakuwa inajua natakiwa kulala.” “Basi
hicho kipengele hakitakuwa na kazi.” Pam akamjibu mwanae akiitizama saa ya
mwanae.
“Ni nzuri sana. Asante
Colins.” Pam akashukuru. “Karibu. Na wewe hiyo app unaweza kuwa nayo kwenye
simu yako, itasaidia kujua alipo kila wakati.” “Naona nitafanya hivyo. Tunashukuru.”
“Naomba unisikilize
na mimi, Pam. Nisamehe nilikuumiza. Ila tafadhali naomba uusikie upande wangu
na mimi. Na hapa nia yangu si kutaka kukuumiza zaidi wala kukuudhi japo
Mill amenikataza.” “Unataka kufanya nini Kamila?!” Mill akamuuliza kwa kushituka
kidogo. “Nataka anisikie Mill. Na baada ya hapa sitamsumbua tena.” Pam kimya
akimtizama.
“Kumbuka
ulinikuta katikati ya kina Mill.” Pam kimya akimtizama. “Na mimi nilikuwa katikati
yao kama mke wa Mike kwa miaka yote. Rafiki zake Mike wote walikuwa wakijua
tupo pamoja na Mike tokea shule ya sekondari lakini sijamzalia Mike mtoto hata
mmoja useme mtoto alikuja kufa baadaye. Hapana. Leo umekuja wewe, kwa muda
mfupi tu, na ujauzito wa kujifungua! Hakika nilipatwa wivu, nikatamani
watu wasijue nikaonekana mimi sifai zaidi.” Kamila akaanza kulia.
“Mwenzio
yatima Pam. Yatima nisiyejulikana hata ninakotokea. Hakuna anayejua hata ndugu
zangu useme nina kabila fulani! Kina Mike na rafiki zake ndio ilikuwa familia
yangu pekee. Mill na rafiki zake wengine waliokuwa wakituzunguka hawakuwa
na wanawake, ila mimi kwa Mike. Kila mtu alikuwa akitutizama mimi na Mike kama
mfano wa kuigwa na mimi nikawa mwanamke bora katikati yao. Wakinidekeza kama
dada yao wa pekee kwa kuwa waliijua historia yangu!”
“Gafla
ukaja wewe. Una kila kitu kizuri. Ile attention yote ikawa imehamishwa
kwako. Akili na mawazo pia ya Mike aliyekuwa hajui kugawa upendo wake kwa mwanamke
mwingine isipokuwa mimi tu, vikageuka ikawa na wewe! Kila wakati
anakuzungumzia wewe na jinsi ya kukusaidia umfikie Mill. Mill naye ikawa
hivyohivyo, hakuna mazungumzo kati yao isipokuwa wewe na mipango inayokuhusu wewe
tu, mimi tena nikajihisi kama nawekwa pembeni, sina umaana tena.” Pam akakunja uso kwa mshangao.
“Kamila,
ulijihisi tu!” “Kuwa mkweli Mill. Safari zote tulizokuwa tukija kwako na wewe
kuwepo hapa nchini baada ya Pam kuingia kwenye picha, hazikuwa tena zikinihusu
mimi kama zamani Mike akitaka nipumzike, lengo ilikuwa Pam, na mipango ya
kumleta karibu yenu. Tukiwa sisi wote aliyekuwa akizungumziwa ni nani kama si
Pam?” Mill akatulia akijaribu kuvuta kumbukumbu
ila kama hapati!
“Unakumbuka siku moja mpaka Sandra
akawaambia nyinyi wote watatu, kuwa akitokea mtu anatusikiliza pale, anaweza
asielewa huyo Pam ni mwanamke wa nani kati yenu. Anaweza fikiria ni mwanamke
wenu nyinyi wote watatu maana hakuna tunapokwenda wala hakuna mazungumzo
mengine nyinyi mnazungumzia ila Pam tu. Bisha Mill?”
“Sasa si kwa kuwa yeye
hakuwa katikati yetu tulikuwa tunatafuta jinsi ya kumuweka karibu!” “Zaidi ya vile ilivyokuwa! Maana pale tu alikuwa anakosekana
Pam mwenyewe, ila uwepo wake ulikuwa umejaa mpaka binafsi nikaona
nasahauliwa! Sasa eti anakuja Pam mjamzito! Hakika nilitishika
zaidi Pam. Wala sitaongopa.” Kamila akajifuta machozi.
“Mike ndio
sikutaka ajue kabisa, asije akazidi kupagawa na wewe. Kuona mwenzangu umekuja
tu na kushika mimba mimi sijaweza hata kubeba mtoto kwa miezi minne! Nikaingiwa
wivu na hofu na ndio maana nilitamani uondoke pale kwa haraka ili
hata Mike asije kukukuta pale getini au ndani. Ila sio kwamba nakuchukia
Pam. Sijawahi kukuchukia. Ni wivu tu.” Akajifuta tena machozi.
“Najua
una haki ya kunichukia lakini jua nia yangu ilikuwa mbaya kwa yeyote ambaye
angetokea bora kuliko mimi katikati ya kina Mike. Mwenzio nilikuwa nadekezwa
na kila mtu aliyekuwa rafiki yake Mike, na kuonekana wa maana sana.” Mpaka Pam
akacheka.
“Kweli
tena, muulize Mill. Hata Sandra aliyekuchukia wewe, ujue mimi mwenzio
alikuwa akinipenda.” “Sasa mimi Sandra alinichukia nini?” “Nakwambia
wewe ulikuwa tishio kwetu. Umekuja, umetukuta, ukachukua spot light
yote! Wanaume wote wanakuimba kama wimbo wa taifa sijui! Mimi na mwenzangu
Sandra tukawa hatuna maana tena!” Wakazidi kucheka, Mill akawa akitingisha kichwa
kwa masikitiko.
“Wewe
ulikuja ukawa tishio, bwana Pam! Mzuri. Halafu Mill akawa amechanganyikiwa
kabisa na wewe, akageuza marafiki wote wakawa wanakutukuza wewe
tu! Ulitutisha.” “Sasa mbona na wewe ulikuwa kila kitu lakini Sandra
hakukuchukia?” Ikabidi Pam amuulize ila akisikika ametulia.
“Sasa wewe hukuwa
umemjulia Sandra. Sandra hapendi kupitwa. Anataka uwe unamsifia. Usimuonyeshe
umemzidi. Halafu kitendo cha yeye kuwa na watoto mimi sina, tayari kwake
mimi nilikuwa chini yake na kwa kuwa mimi nilishamsoma, nikajua udhaifu
wake, basi nikawa siachi kusifia wanae, na kuwaletea zawadi yeye na wanae, kila
nikitoka nje ya nchi, ndio maana mwenzio alikuwa akinipenda.” Pam
alicheka sana.
“Kamila!”
“Mimi nakwambia kweli Pam. Sasa wewe ukaja kwanza ukawa mkimya. Hajui mambo
yako ya ndani ili akulinganishe na yeye ajione amekupita. Ukabakia
bora tu! Unaendesha gari jipya na ujauzito juu! Ndio maana mwenzio alikufunga
jela, japo mimi hilo sikulijua. Na hata Mike hakujua. Mike asingekubali
ukae jela. Kila mtu anamjua Mike.”
“Mbona aliniacha
na shida?” Pam akauliza kwa kuumia. “Mimi simsemelezei Mill. Ila jua
mwanaume wako huyu, Mill ndio ametuponza kwako.” “Kamila!” “Hakika tena
Mill. Acha na mimi nijitetee kwa Pam. Mike hapendi uonevu na angejua kama
unashida, kwa hakika angeenda hata kinyume na Mill akakusaidia. Muulize Mill,
anamjua.” “Kweli. Mike angejua unashida asingeacha kukusaidia.”
“Basi ndio Mike.
Ila huyu Mill alituambia hivi, wewe hapo mzuri sana. Utaulizia kidogo,
utaona anakubabaisha, utaachana naye, utaendelea na maisha yako. Tena Mike
akamwambia huyu Mike, mbona Pam haachi kukuulizia kwa Jerry! Tena akamwambia unamuulizia
sana. Mill huyu, hapo ujue ni wakati huo kesha haribu mipango, Kisha anampeleka
kama gari bovu, hawezi tena kukutafuta wala kurudi nchini. Akatuambia
tukupe tu muda, utaachana naye, na kumchukia yeye Mill na
kuendelea na maisha yako. Si ni kweli Mill?” Sebule nzima wanawasikiliza wao
wakiendesha kesi yao.
“Mimi ndivyo
nilivyojua. Lakini nishazungumza na mpenzi wangu, mimi amenielewa. Wewe usirudishe
dhambi zangu, zilishasamehewa zamani sana. Wewe pambana na hali yako Kamila.” “Sasa
wewe wakati ukiomba msamaha wako kwa nini usinitetee na mimi
kwamba wewe ndio uliniponza?” “Wewe ulimfanyia ubaya zaidi, bwana! Ulimnyima hadi maji ya kunywa! Wewe
pambana na hali yako Kamila.” Wakaanza kusemeana. Pam akiwatizama tu.
“Sasa na mimi
Pam ameshanielewa. Uongo Pam?” “Nyinyi wote mlinifanyia ukatili aisee! Ukatili
wa hali ya juu!” “Nisamehe Pam. Ila jua Mungu ashanilipiza kwa ubaya
wangu wala huna haja ya kunichukia. Nilipoteza kila mtu na kila kitu, nikawa
kama nimechanganyikiwa, mpaka huyu Colins alipo niokoa. Alinikuta
na hali mbaya kama kichaa kabisa. Marafiki niliokuwa nikiwalinda wenyewe waliondoka
kwenye maisha yangu, nikabaki kama peke yangu. Namangamanga, hata nyumba
niliyokukataza usiingie walinipokonya. Isingekuwa Colins ningekuwa nishakufa.
Nisamehe Pam.”
“Na usifikiri labda nakuomba
msamaha sasahivi sababu ya Mill yupo! Hapana. Sikuwa na huo uwezo kiakili wala
mali. Mike alikufa nikajua ndugu zake wamemficha, nikawa na kazi ya kumtafuta
mpaka kurukwa na akili.”
“Anapokwambia
kurukwa na akili si kidogo! Mimi nilikutana na Kamila aliyekuwa kama kichaa
kabisa. Hajitambui alipo wala siku au tarehe. Wazazi wangu na mimi ndio tulio msaidia
mpaka kuelewa majira na tarehe, na kuweka mazingira ya kumfanya aamini kama
kweli Mike alishaondoka hapa duniani muda mrefu sana. Na anaishi miaka ya mbele
sio siku aliyomwacha Mike hospitalini. Kwamba miaka ilishapita tokea siku hiyo.
Alipoteza miaka hapo katikati, yeye hana taarifa.”
“Tukafanya taratibu
za kuonyesha picha za msiba wa Mike na kumpeleka kaburini na kuona kaburi,
ndipo akaamini kama Mike hayupo duniani. Ndipo sasa akaweza kutulia hapa
nyumbani maana alikuwa hana hata pakuishi, anamangamanga kama ndege.” Yakawa
mageni kwa Pam.
Wakamsimulia
mwanzo mpaka mwisho, kidogo Pam akaingiwa na huruma. “Na ukumbuke kipindi hicho
hata Mill mwenyewe nilikuwa sijui alipo, maana mara ya mwisho nikiwa na akili
zangu, uhai wa Mike, huyu Mill alikuwa amefungwa jela la Kisha. Anakuja kurudi
Mill kwenye maisha yangu tena, ndio nimepokelewa hapa, yaani mimi na yeye ndio tunatafuta
kutulia, tunaanza upya maisha.”
“Halafu imekuwa
kama nina mkosi! Ndoa yangu na Colins nayo wale kituo cha yatima waliokuwa
wakinitunza tokea wameniokota, nao walimfungulia mashitaka
Colins, wakimtuhumu alinichukua nikiwa chini ya miaka 18, akanifungia kama mke.
Asiniendeleze.” Pam akashituka.
“Ilikuwa kesi kwelikweli mpaka Mill
alipokuja na kutoa ushahidi kuwa aliyekuwa na mimi si Colins, ila Mike. Baba hapa
amekubali kulipa faini kwenye kile kituo cha kulelea yatima na kulipa
mahari kabisa, ndio kama tupo kwenye makubaliano, wafute kesi na kutoa vipingamizi
kanisani, pengine ndoa ifungwe. Usinichukie Pam. Mill ndio amesababisha
yote. Ametuponza mimi na Mike, ila bora mwenzangu Mike hayupo. Ni Mill, usinichukie
mimi.” “Kamila!” Mill akashangaa sana hakutegemea
umaliziaji ule. Angalau wote wakacheka.
“Ila jua sikuwa
na nia ya kuingia katikati yenu na kuchukua nafasi ya hata mmoja wenu.” “Nakwambia
sio wewe Pam, Mill huyo! Alifanya ikawa kama tishio! Pam akageuka kuwa gumzo,
watu hatunywi maji! Yeye huyu ndiye aliyetuingizia hofu na wivu. Halafu baadaye
akaja kututuliza kuwa wewe mzuri sana. Kila mwanamme anakutaka wewe. Hutachukua
muda mrefu, utaachana na sisi wote. Na yeye msamehe. Mungu alimpa kiboko yake!”
“Kamila unanicheka?” Kamila akafanya wote wacheke maana na yeye mwenyewe alianza
kucheka mbavu hana.
“Bwana Kisha alimkomesha
Mill, mpaka mwili ukaisha! Kesi kwao haziishi! Mpo katikati ya usingizi, simu
kwa Mike. Wamegombana. Nakwambia kwao hata kukitaka kununuliwa chumvi, ni kesi
ya kuamuliwa na Mike. Alimnyoosha Mill, halafu kama haitoshi, akamuachia wale wanae.”
Pam akashangaa sebule nzima inacheka, Mill anatingisha kichwa.
“Wale watoto!” Kila
mtu akazidi kucheka. “Kuja kuletewa Shema, kila mtu akahema.” “Wewe tusamehe tu
Pam. Mungu wako ashatulipiza. Alikopita huyo Mill ni kama mimi tu, hatuna
tofauti.”
“Hii familia ya
kina Kombo, imekuwa kama kituo cha yatima!” Wote wakacheka. “Kweli tena. Wametukuta
mimi na Mill tuna tangatanga na dhambi zetu. Wakatupokea kama tulivyo, na
kutupa familia.” “Nimeona jinsi walivyo na upendo. Nawashukuru na kumpokea
Shema wangu. Ananiambia huwa mnakwenda mpaka shuleni kwao, wakihitajika bibi na
babu.” “Mwanao huyo anapendeka. Hana shida. Amejawa shukurani, nakwambia
Komba akiambiwa safari za Shema, anaihirisha kila kitu ilimradi awepo tu.” “Mtoto
mwenyewe anatia sifa kujulikana unahusika naye! Unafika shuleni unajazwa sifa,
sasa kwa nini usiende!” Akajibu mzee Komba kwa mkewe.
“Huyu mtoto
umelea vizuri Pam. Wewe na mama yako! Hakika mmeweka msingi mzuri sana.” Wakacheka
wakimwangalia huyo Shema. “Basi hilo ni deni la kwenda kucheza mpira
baadaye mpaka kuchwe. Utasikia hata bibi amenisifia mimi mtoto mzuri, niache tu
nikacheze mpira.” Mama yake akafanya wacheke.
“Mimi mtoto
mzuri mama. Na nikicheza mpira siku hizi sichezi kupitiliza.” “Si nilisema mimi?
Hilo lishakuwa deni.” Wote wakacheka. “Sisi furaha yetu ni mcheke kama hivi.”
Mama Komba akaongeza.
“Sikiliza Pam,
mwanangu. Nyinyi mlikutana ni kama kondoo bila mchungaji. Wote mkaishia
kufanya mambo vile mnavyoona inafaa. Ndio maana kukosea kukawa kwingi. Huku
kukutana tena ni neema ya pekee wanangu. Anzeni upya. Mkishikana nyinyi kama
hivi Mill anavyofanya na Colins, hakika mtafurahia. Wanafanya mambo yao kimyakimya
lakini mpaka yanashangaza! Wameinuana kiuchumi, kwa muda mfupi sana wapo
mbali sana kimaendeleo. Lakini ni kwa sababu wanania mamoja na kubebana. Umoja unanguvu.”
Akaendelea taratibu tu.
“Pole Pam
mwanangu. Naomba jitahidi kusamehe ili tupate muda wa kumuomba Mungu pamoja
pengine mambo ya kila mmoja wenu yatafunguka. Hawa nao waoane, watoke
humu ndani.” “Mama unanifukuza!!?” Colins akashangaa sana na kufanya wacheke.
“Umejaa sana
humu ndani Colins bwana! Mashariti mengi kwa msichana wangu! Nenda tu kwako. Kwanza
ni hapo mlango wa pili tu! Kwa nini hutulii kwako?” “Nipeni Kamila muone kama
sitaondoka humu ndani.” “Huyu hatoki hapa bila ndoa takatifu
kanisani.” Mzee Komba akadakia. “Basi naona na mimi hapa nipo sana tu.” Angalau
mazungumzo yakabadilika. Pam akaona jinsi walivyojawa umoja na upendo.
Kamila akaonekana
kama binti wa Komba kabisa. Mill kama kijana wao mkubwa. Wakawaongeza wao kama
wanafamilia kabisa. Mipango anayoweka mama Komba anamjumuisha mama Eric
kirahisi kabisa akimtaka ushauri. Mpaka wanaondoka hapo wote wapo ukurasa
mmoja.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Mwanzo mpya
umefika – wa amani, wa kujithamini, na wa kupenda
tena bila hofu. Ni safari ya kujijenga upya, kama
vile mto unaotafuta njia baada ya kuta kuvunjika. Huu ni
mwanzo si tu wa maisha mapya, bali ya nafsi iliyozaliwa upya.
Kwa Pius&Raza
je?